Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Monday, February 8, 2010

Ni mali asili yetu tu!

‘Eee jamani angalieni bonde hili lilivyo na rutuba, inaonyesha mahali hapa hapajalimwa miaka mingi, jamani nchi yetu hii imebarikiwa..’ ilikuwa kauli ya mmoja wa abiria katika basi tulilokuwa tukisafiri kutoka Kilimanjaro kurudi Dar. Nilikuwa nimeenda kumzika kaka yangu aliyefariki hivi karibuni. Wakati tunarudi usafiri ulikuwa sio shida kama ilivyokuwa mwezi wa kumi na mbili. Na nauli zilikuwa zimerejea mahala pake.


Njiani tulishuhudia mahindi yaliyositawi vizuri kuashiria kuwa huenda neema baada ya kipindi cha ukame inakaribia. Pia tulishuhudia maeneo mengi yaliyojaa rutuba, lakini hayajawahi kulimwa, na hapo ndipo mjadala ukazuka, wengi wakiuliza kwanini maeneo kama hayo yapo wazi muda mrefu, ina maana hayana watu wa kulima, au ni maeneo yaliyotengwa na serikali kuwa yasilimwe!

‘Mimi sikubaliani na hilo kuwa haya ni maeneo ya serikali ambayo hayaruhusiwi kulimwa, haya yapo miaka nenda rudi, ila nani atakuja kupambana na hizi mbuga, si hatari tupu, wanyama na huduma za kimsingi hazipo maeneo kama haya..’ alisema mmojawapo.

‘Mimi naona ipo siku serikali itamkabidhi muwekezaji mmoja toka nje, na itakuwa mwanzo wa migogoro kama ya akina Mgabe..’ akasema mmoja wa abiria.

`Lakini ina maana hata kilimo kinahitaji muwekezaji, kina utaalamu gani zaidi wa kumuita Mzungu, hili naona lipo ndani ya uwezo wetu, labda tuseme zana za kilimo kama matrekita, na pembejeo, na haya yanaweza kununuliwa’ akasema mwanamama mmoja.

‘Mimi inanishangaza kweli kila kitu muwekezaji toka nje, ina maana vyuo vyetu haviwezi kutoa wataalamu wakuweza kuyamudu haya, hawa mabwana shamba hawa wataalamu wa viwanda, mashine wanaomaliza wanakwenda wapi?’ Mmoja akauliza, akisubiri apatiwe jibu.

‘Mimi nauliza swali moja, kuna kitu gani ambacho tumekifanya kama waafrika, au tuseme kama Watanzania ambacho wazungu watakuja au wanatamani kuja kukiiga, kweli kipo kitu kama hicho?’

Swali hili ndilo lilozaa mjadala na kila mmoja alijaribu kutoa hoja zake, wengine waliishia uchekesha watu kuwa kitu pekee ambacho mzungu angependa kuja kuiga kwetu ni uchawi na utamaduni wa asili kama wa kimasai. Huyu alitoa mfan, kuwa maeneo mengi tunayopita ambayo wanaishi watu, lakini maendeleo yao ni duni, vijumba vya majani , mashamba madogo yote hayo yanasababishwa na ushirikina, watu wanaogopa kulogwa na hili wazungu hawana na huenda wanatamani walijue’ watu wakaangua kicheko,.

‘Mimi naona kitu pekee ambacho mzungu anakitamani kutoka kwetu ni maliasili yetu tu, hakuna kingine. Malisili iliyopo hapa nchini ni utajiri mkubwa na wazungu wakipita hewani wanautamani, na hili ndilo jambo ambalo wao kwao ni adimu na wanatamani waje , na ipo siku watakuja tu!’ akasema mzee mmoja. Ilibidi nigeuke nimwangalie mara mbili, kwani hoja yake ina maana kubwa kwa wenye kutafakari.

Ukiangalia maeneo yaliyopo wazi ni mengi lakini asilimia kubwa ya kila Mtanzania inauangalia mji wa Dar, au miji mingine, hata mambo muhimu na huduma za kibinadamu zote zinalenga mijini, na hapo sera zetu ni kilimo kwanza. Hivi hiki kilimo kwanza kitakujaje, kama vitu muhimu kama matrekita na huduma za jamii zitakuwa hazikupelekwa vijijini.

Mimi ningeonelea ile sera ya Mwalimu ya vijiji vya ujamaa, ingerejeshwa kitaalamu zaidi. Wakusanywe vijana, mashababi, wenye nia safi wakabidhiwe vifaa vya uzalishaji na huduma muhimu wapewe mapori, na huko vitu kama jeshi la kujenga taifa likapewa dhamana ya kusimamia. Kama ingefanyika hivi nahisi miji ingehamia vijijini muda si mrefu, na tusingekuwa na haja yawawekezaji wenye uchu wa uchumi wetu.

Na jambo jingine kwanini hawa wawekezaji wakija wanapewa viwanda vyetu ambavyo tulishaumia navyo, kwanii wasiunde vyao vipya ili vije vishindane na hivi vyetu? Kwa mfano wangekuja waanzishe Tanesco yao, Tazara yao , TRC, yao, na waanzishie vijijini…akaongezea Yule mzee.

Jamani mna chakuongezea, kwani mjadala huu ulitufikisha kwenye foleni za Dar, tulijikuta tumeshafika Ubungo, na kukaribishwa na adha ya foleni.

From miram3

No comments :