Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Wednesday, February 7, 2018

MKUKI KWA NGURUWE-76


‘Mimi naomba aje Binti yangu wa kufikia, ..aje yeye kwanza maana anahitajika kwenda kujiandaa kesho anasafiri....’akasema mama

Na mwenyeketi akageuka kumuangalia mwenyeji wa kikao ambaye ndiye alikuwa muongeaji , na yeye ndiye alistahiki kuita mashahidi wake,…

‘Unajuaje kuwa huyo ni shahidi wake, usiharibu utaratibu, au..’akasema mwenyekiti

‘Sawa ila…’nikasema nikiwa sijui lolote kuhusu huyo bint

‘Mimi nina uhakika ni shahidi wake..’akasema mama.

‘Haya, kama muhusika umemkubali kuwa ni mmoja wa shahidi zako, aitwe, au unasemaje mwenyeji wa kikao..?’ mwenyekiti akauliza na mume wangu akawa kabakia kimia, akiwa kashika kichwa…

Tuendelee na kisa chetu

**************

Kila mmoja alikuwa na hamu ya kumuona huyo shahidi, na wengine walipumua, kwani hakuna aliyejua ni nani ataitwa kama shahidi, na hadi pale mlango unagongwa, wengi bado walikuwa kwenye kutafakari, na kuwazia ni nani huyo binti wa kufikia wa huyo mama, ambaye hajulikani, ni nani huyo binti ambaye anaweza kutoa uahshidi na alifanyiwa nini...

Mlango ukafunguliwa, na akaingia binti, akiwa kavalia kiheshima na mkononi alikuwa kashika bahasha, na  , hakuwa na kitu kingine, kwanza kwa aibu alipoingia pale mlangoni, hakujua afanye nini, alishikwa na butwaa hasa alipoona watu wote wamegeuza kichwa kumuangalia yeye,...

‘Sogea huku mbele...’ilikuwa sauti ya mwenyekiti, ndiyo iliyompa nguvu huyo binti, na taratibu akawa anasogea kuja upande ule watu walipokaa, kulikuwa na kiti kipo wazi.

 ‘Wewe umefuata nini huku...’

Sauti iliyowafanya watu wageuka, na kuangalia muongeaji ni nani,

 Kumbe mume wangu wakati watu wanahamasa ya kumuona huyo shahidi yeye bado alikuwa kainamisha kichwa, na hata sauti ya mwenyekiti, ya kumkaribisha huyo shahidi ilikuwa bado haijamshtua vyema, akawa kama katokea usingizi, akainua kichwa na kumuona huyo shahidi.

Hakuamini macho yake,, macho yakamtoka pima, mdomo ukabakia wazi, na alichosema ndio hicho…

‘Wewe umfuata nini huku……….’.

Binti yule kusikia hivyo, akawa anaonyesha hali ya kuogopa, …akawa kashikwa na butwaa, akawa sasa hajui afanye nini..

Kwa wakati huo watu wote sasa wamemtupia macho mume wangu, ambaye kwa muda huo  alikuwa kasimama nusu, na mwenyekiti akawa anaangalia hili tukio kwa hamasa ya aina yeka, huku tabasamu tele mdomoni, alikuwa akisubiria hiyo hali kwa hamu kubwa sana,..

Na mimi nilipogundua kuwa ni huyo binti, moyoni nikasema, ‘huyu ni shahid wa kweli,..hata hivyo mimi sikuamini, maana sikuwa nimelifahamu hilo, kwahiyo kwangu moyoni nilitamani kusikia atakachokizungumza huyo binti…nilimuangalia yule binti wa watu kwa moyo wa huruma….

‘Haya huyo hapo shahidi wako wa kwaza, unataka uendelee naye mwenyewe, au nishike usukani mimi, maana wewe ndiye mzungumzaji..?’ akauliza mwenyekiti, lakini mimi niliishiwa nguvu, nilibakia kimia, nikiwa nimwangalia yule binti, sijui ilikuwa ni huruma, hasira, au nini sikuweza kuongea, kilichotokea ni mimi kuangusha chozi..chozi la nguvu, nikikumbuka huyo binti alikuwa kwenye dhamana yangu, nikikumbuka kuwa huyo ni sawa na watoto wangu, mtoto wa mwenzio ni sawa na mtoto wako, umtendeayo mtoto wako ukumbuke na wewe utakuja kutendewa.

Mwenyekiti akaiona ile hali, akaamua kuendelea mwenyewe, akasema;

‘Kweli inauma, hii isikie kwa mwenzako tu, lakini ukitendewa wewe utaona uchungu wake, na hasa utendewe na mtu unayemwamini, huwezi kuamini …huwezi kuamini mpaka likufike, tujiulize hivi sisi hatuwezi kuwa na watoto…’akasema mwenyekiti.

Hatukupenda aibu kam hizi ziwekwe hadharani hivi, ila naamini kuwa nyie ni wanafamilia, na hili kwa hivi sasa libakia humu humu, hadi hapo, tutakapoona sasa ni wakati muafaka wa jamii kufahamu…’akasema mwenyekiti.

‘Nawausia ndugu zanguni, mimi hapa ni mzazi, na ni mkubwa wenu wote hapa,  tuweni makini sana, ..tena sana na wafanyakzi wenu wa ndani, msipende kuwaacha na waume zenu kwa muda mrefu, au kuwapa kazi ambazo sio stahiki zao, kila kitu mfanyakazi wa ndani, hata kutandika kitanda chenu..jamani, ..’akasema na watu kidogo wakacheka.

‘Binti wengine ni mtihani…yeye aje kukutandikia kitanda, afagie, ainame wewe dume upo humo..mnawatia majaribu waume zenu..’hapo watu wakacheka,

‘Lakini sahamanini,..lakini ..hahaha, msicheke jamani, sio kwamba nasema wanaume wote wana tabia hiyoo chafu, ..hapana, wapo wanaume wanajikubali, wanahulka ya utu wema, ..muulizeni mke wangu...mimi aah, maana na umri huu nao…’akasema mwenyekiti na watu wakacheka.

 Ilibidi watu waachwe kwanza watulie maana baada ya kicheko, ilifuatia watu kuteta, kwa kunong’ona na mnong’ono wa wengi ni ngurumo, mwenyekiti akaacha hali hiyo ipite kidogo.

‘Huyu hapa mbele yenu ni shahidi,…kama mjumbe alivyotaka upatikane ushahid wa madhambi yake,..hajataka kukubali mpaka ushahidi, haya ushahidi ndio huo hapa, ambao, utadhihirisha urijali wa mume wa familia…’aliposema hivyo watu wakacheka.

‘Tusicheke jamani, hebu muangalieni huyu binti, afadhali sasa kakua, ..anaonekana mdada, kumbuka umri aliokuwa nao, kipindi hicho wanaishi nah ii familia, ndio ni kweli umbo lake lilikuwa kubwa la kuvutia, lakini kumbuka kiumri…na kumbuka huyu ni binti sawa na binti yako wa umri huo…napenda kurudia sana haya maneno ili nyote muwe ni mashahid kuwa nililisema hili…’akasema mwenyekiti.

‘Huyo ni sawa na binti yako mume wa familia, japokuwa binti zako hawajafikia umri wake, lakini watafikia umri huo, huyo ni sawa na dada yako, kama una madada…wewe ukaamua kula kuku na mayai yake..bado hutaki kukiri kume umekosa, una makosa, utubu mbele ya jamii…haya ngoja tuanze na huyu shahidi wetu...’akasema mwenyekiti.

‘Binti usiwe na hofu, wala usimuogope huyo mtu, kauli yake ya kukutisha haina maana mbele ya jamii…kama kakosa kakosa, ..na wewe uliyekosewa ni haki yako kusema ulichotendewa, sisi hapa tutakulinda, …’akasema mwenyekiti

‘Hebu tuambie jina lako,....?’ akaulizwa na akabakia kimia, halafu akainama, halafu akaanza kulia

‘Binti, ..ule ushujaa umekwenda wapi, kwanini unalia, sikia binti usiogope, hata tunachotafuta hapa ni haki yako,ukiogopa haki yako yote itapotea, na waliokuharibia maisha yako wataendelea kuyafanya haya kwa watu wengine, ...’akasema mwenyekitu

‘Sisi hapa tunataka ukitoka hapa, uondoke na tumaini, na haya yaliyotokea kwako,  yakomeshwe, na ili hili lifanikiwe tunatakiwa tuanzie huku  majumbani kwetu, kama hivi,..likitokea jambo, mkosaji aitwe, aadhibiwe, ikishindikana, apelekwe kunakostahiki,...’aksema mwenyekiti.

‘Haya jitambulishe mpendwa,...’akasema mwenyekiti.

‘Mimi naitwa Tabia...’akasema kwa sauti ya kinyonge

‘Tabia,..tabia yako ni ya upole, au sio, mchapakazi, au sio, ...sasa nasikia kuna kitu kilitokea, wakati unafanya kazi kwenye nyumba moja, kilipotokea ukakimbia jiji, ni kwanini ulikimbia jiji, wakati wenzako wanasema tutabanana hapa hapa...?’ akamuuliza mwenyekiti.

‘Sikukimbia jiji, niliambiwa niondoke, la sivyo yatanikuta makubwa, na...na...’akasita kuongea

‘Hebu sasa tuanze, maana nilikuwa nakuweka sawa, hebu niambie, wewe ulikuwa ukifanya kazi wapi , na kwa nani…?’ akaulizwa

‘Mimi nilikuwa mfanyakazi wa ndani wa nyumba, ya ya...’akageuka kuniangalia mimi

‘Ya mke na mume wa familia hao hapo au sio, hapa tunawatambua kama mke na mume wa familia, ambayo ndio tunayoiongelea hapa hii leo ..ngoja nimsaidie...’akasema mwenyekiti.

‘Ulifanya kwenye hiyo nyumba kwa muda gani?’ akaulizwa

‘Kwa zaidi ya mwaka mmoja...’akasema

‘Hebu niambie, wakati upo hapo, kulitokea nini, kilichokufanya uondoke, uliamua kuacha kazi , kwa vile umepata mume huko kwenu au ilikuwaje?’ akauliza mwenyekiti.

‘Niliondoka baada ya kugundua kuwa nina uja uzito...’akasema na watu wakaguna

‘Wakili wa mume wa familia, unalisikia hilo…sitaki uweke pingamizi najua ndio zenu kuwalinda wahalifu..’akasema mwenyekiti alipoona huyo wakili wakitaka kunyosha mkono.

‘Jamani msigune, ndio hali halisi, na tunapoongea hapa watu wanafikiria tunamuonea mlalamikiwa, yeye anafikia kusema mimi nataka kuvunja ndoa yake tu , kwa vile… ngojeni sasa myasikie na nyie kwa masikio yenu…’akasema mweneykiti.

‘Haya tuambie, unasema ulipata uja uzito, kumbe wewe badala ya kufanya kazi za ndani ulikuwa ukifanya uhuni na wavulana wa mitaani eehe...’ aksema mwenyekiti kwa sauti ya nzito, kama kumtisha huyo binti.

‘Hapana mimi sio muhuni, sijawahi kufanya uhuni na mvulana yoyote, tangia nifike hapa mjini , kazi yangu ilikuwa …...’akasema na hapo akaanza kulia

‘Unasema hujawahi kufanya uhuni na mvulana yoyote, sasa hiyo mimba uliipata kutoka mbinguni, hebu sema ukweli, ...’akasema mwenyekiti

‘Mimi nilikuwa simjui mwanaume yoyote, nilikuwa nafanya kazi zangu na sikupenda haya yanitokee, ..niliapa kwa mama yangu kuwa sitakuwa muhuni, na nilipochukuliwa na ....wazazi wangu hawo, nilijua kuwa nimefika mahali salama....sikutarajia kuwa hayo yangelitokea,....’akawa analia

‘Usilie, …ongea yaliyokukuta sasa, ilikuwaje tuanataka kusikia kuhusu maisha yako…wapi ulipotokea wazazi wako, ulifikaje hapa kwa hiyo familia ili muone ni dhambi gani huyo mtu aliibeba, na kama bado anakataa kutubu basi huyu sio mwanadamu..hebu tuambie kisa cha maisha yako;

***********

Mama yangu ni mjane, baada ya kufariki baba, kwa ghfla,sisi tulibakia na mama kwenye kibanda kibovu tu,tukiwa watoto watano, na alituacha tukiwa masikini sana, mama akawa anaangaika sana kututafutia riziki, na sisi japokuwa tulikuwa wadogo, lakini tulijijua kuwa hatuna mtu atakayetusaidia, kwani baada ya msiba, vitu vilivyokuwepo vichache viligawanywa, na wanandugu wakachukua kile walichoona kinawafaa, tukabakia mikono mitupu.

Mimi nilikuwa mkubwa ukilinganisha na wadogo zangu,kwani mimi nilikuwa mtoto wa kwanza nna kwa vile ni mwanamke , nilionekana mkubwa kidogo, basi ikawa kazi kubwa ni kumsaidia, kila tukitoka shule tunajipanga, huyu afanye hiki na yule afanye kile, ili tu tuweze kumpunmguzia mama kazi za nyumbani..

‘Kazi kubwa ya mama ilikuwa kutengeneza vyungu, kwa kutumia udongo wa mfinyazi, alikuwa akienda huko mlimani kuutafuta udongo wa mfinyanzi, na akileta anatengeneza vyungu vya kupikia, …

‘Kiukweli mama alikuwa mtaalamu sana wa kazi hiyo, lakini hata hivyo kazi hiyo ilikuwa hailipi, kwani akijitahidi sana anakuwa katengeneza vyungu, hata kumi havifiki, na bei za kijijini ni ndogo, ni kazi nzito, lakini tungefanyeje...kuna kipindi tunakuwa hatuna hata senti moja, nyumbani, inabidi mama aende kwa majirani kuomba hata kazi ya kulima, au kuosha vyombo ili angalau tupate pesa ya kula, ndio maisha niliyokulia hayo.

Wingi wetu, ulikuwa mzigo sana kwa mama, na ukumbuke baba alifariki akatuacha tukiwa tunasoma shule ya msingi, mimi nilikuwa darasa la saba, na wenzangu, la sita, la tano la nne, na la tatu, na wamiwsho alikuwa darasa la pili,tulipishana mwaka mmoja mmoja wa shule, japo kimuri tulipishana kidogo. Ilibidi tusome kwa shida, hata nguo za shule, zilichakaa, ikawa tunaweka viraka, na wengi walianza hata kututania, kuwa sisi ni viraka.....’akasema

Darasa la saba nilimaliza kwa shida sana, kwa vile mimi ndiye mkubwa, basi ilikuwa kama mimi ndiye msaidizi mkubwa wa mama, nilitakiwa kuamuka asubuhi sana, kumsaidia mama, ili aweze kukusanya, vile vyungu vilivyokuwa tayari, maana tulikuwa tukivichoma usiku,na asubuhi, tunavitoa ili vipoe, vingine vinavunjika, ndio hivyo tena...’akatulia.

Nilipomaliza darasa la saba tu, watu wengi wakaja kunitaka, niende nikafanye kazi kwao, kama mfanyakazi wa ndani, kutokana na jinsi walivyoniona, kuwa ni mchapakazi, sikupena kabisa niondoke nimuache mama yangu, lakini pia tulihitajia pesa kwa ajili ya kuwasomesha wadogo zangu, basi mtihani ukaanzia hapo, niende kwa nani..

Kabla hatujaamua ndio siku moja likaja gari, na wakaja hawa wazazi wangu , ambao mama alikubali niondoke nao,mama alisema anawafahamu vyema, na aliona kuwa watatusaidia kujikwamua kimaisha, angalau wadogo zangu waweze kusoma na kufika mbali sio kama mimi niliyeishia darasa la saba ...’akatulia.

‘Wageni hawo, waliongea na mama wakakubaliana, na kesho yake nikachukuliwa na kuja huku Dar, na kama ujuavyo, kila mmoja kule kijijini anatamani sana kuja huku, kwahiyo hata mimi nilifurahi sana, na nilishukuru kuwa nimapata kazi kwa watu wenye uwezo. Nikawaga wanafamilia, yaani mama na wadogo zangu. Mama alizidi kuniusia kuwa nifanye kazi kwa bidii nisije nikandanganyika na kuingiwa na tamaa, na kujiunga na wahuni, mimi nikamuahidi mama sitafanya lolote baya.

Mshahara wangu wa kwanza wote niliutuma kijiji kwa mama, na mama yangu mpya, yaani bosi wangu, alikuwa akinijali sana, alinisaidia mambo mengi, na kuanza kunisomesha msomo ya jioni, nikaanza kuelewa maisha na jinsi gani ya kuishi kisasa, sio kama nilivyokuwa huko kijijini, na alikuwa akinisaidia kunipa peza za kuwasomesha wadogo zangu kila nilipomweleza matatizo ya nyumbani kwetu...’akatulia kidogo.

Kwakweli mimi darasani sielewi, ninachojua ni kufanya kazi, nikamwambia mama asipoteze pesa zake bure, kunisomesha,  kwania yeye alitaka kunisomesha sekondari, kiujumla kichwa changu ni kizito sana darasani, akaniuliza kitu gani rahisi ninaweza kukisomea au kukifanya, nikamwambai ufundi, na nikachagua ufundi wa kushona, na kweli huo nikauwezea sana...akaninunulia cherehani, nikawa nashona nguo hapo nyumbani, na alikuwa na mpango wa kunifungulia duka langu...lakini oh bahati haikuwa yangu....’akaanza kulia.

‘Aaah, tulishakuambia, ujikaze, mambo ya kulia hapa hatuyataki...yote ni mitihani ya maisha, unachotakiwa ni kumkabidhi mungu, ..usilie mwanangu ongea...’mama yangu akamwambia na kumpa moyo.

‘Ndoto zangu za kuwa mtu maarufu zikazimwa kama taa ya kibatili,maana nilikuwa na ndoto za kuwa mwanamitindo, nishone nguo za kila aina,lakini ndio hivyo tena yakanikuta makubwa ambayo sikuyatarajia...kwasababu ya ...ya...’akasita kusema huku akigeuka kumwangalia mume wangu ambaye kwa muda huo alikuwa kainamisha kichwa chini.

‘Hebu tuambie ndoto yako hiyo ilizimikaje, kwa maana ulikuwa unaishi na watu wenye uwezo wangeliweza kukusaidia sana tu, na nakumbuka  mwanzoni nilipowatembelea ulionekana mwenye furaha,ukasema kuwa umewapata wazazi wazuri wanaokujali...?’ mwenyekiti akauliza

‘Ndio mwanzoni mambo yalikuwa mazuri sana, sikuwa na shida, na niliwaona wazazi wangu ninaoishi nao ni kama baba na mama yangu, na kwa ujumla wao walikuwa wachapakazi kweli, hawakutaka mchezo, na wakanikuta na mimi ni mchapakazi kama wao, japokuwa ni za nyumbani, kwahiyo kila mmoja alikuwa akiamuka asubuhi anakimbilia kwenye kazi yake…

‘Na mimi nikawa naendana nao,.. hakuna muda wa kuongea, na mimi nilikuwa nafanya kazi yangu vyema, bila ya kusimamiwa,...ghafla nikahisi mabadiliko, maabdiliko hayo niliyaona kwa baba, akawa analewa sana....’akasita kidogo pale mume wangua lipoinua uso kumwangalia.

‘Usimwangalie, wewe ongea ,hana lolote kwa sasa, hawezi kukufanya lolote....’akamwambia mama, ambaye alionekana kama muongozaji wake.

‘Kabla hata ya hapo, nilipokuwa nimekaa hapo kwa mwezi mmoja tu, nilikuwa nimeshabadilika sana, mwili wangu ukawa mkubwa, nikawa naonekana msichana,mkubwa kuliko umri wangu, mmmh....’akatulia na mwenyekiti akasema;

‘Msichana mrembo...eeh’akamalizia mwenyekiti, na watu wakacheka kidogo

‘Ndio ndivyo walivyokuwa wakiniambia watu, lakini mimi sikujali, maana nilikuwa nafahamu ni kitu gani kimenileta hapa Dar, nikawa nawajibika ipasavyo, sikuwa na muda na watu wa mitaani hasa wanaume…, ambao walikuwa wakinisumbua kila nilipokuwa nikitoka, kwenda dukani au sokoni, ...huko nje niliweza kabisa kuwashinda, sikuwapa muda wa kuongea nami, lakini tatizo likawa ndani,....’akatulia kidogo.

‘Ulikuwa unanyanyaswa, au hayo mabadiliko yalikuwa yapi, mpaka nyumbani kuwe ni mtihani kwako?’ akauliza mwenyekiti.

‘Baba….a-a-ah…, nilimuona  baba akinitizama kwa macho yaliyonitisha..sivyo kama ilivyokuwa mwanzoni’akasema

‘Kwa vipi hebu fafanua..na ulihisje hivyo, kwani mama yeye alikuwa hakuangalii, kama anavyofanya baba ?’ akaulizwa na mwenyekiti.

‘Ni kama ..ya tamaa, maana anakutizama mpaka unaona aibu, kuna siku nilimuuliza mama mbona baba ananitizama hivyo,mama akasema hajawahi kumuona baba akifanya hivyo, akaniambia nifanye kazi zangu, nisiwe namwangalia baba, kwani utajuaje kuwa mtu anakutizama, kama wewe hujamuangalia, nikaona aibu kwanini nilimwambia mama hivyo

‘Siku moja nikashindwa kuvumilia, nilipomuona baba ananitizama nikaona ngoja nimuulize kama baba yangu, yeye, akasema siku hizi  nimekuwa mrembo sana...’akasema.

‘Unaona eeh…haya endelea…’akasema mwenyekiti

‘Kauli hiyo ikanikwanza, nikaona nimwambia mama tena, kesho yake, nilimuona baba kanikasirikia, na hakutaka hata kuitikia salamu yangu, nikahisi huenda waliongea na mama kuhusu hayo niliyomwambia, na hali ikatulia kidogo, lakini baadaye, nikaona ile hali inarudi tena, baba akawa ananifuata hata sehemu ninyofanya kazi na kuanza kunitania, mimi kwa vile niliona ni baba yangu, nafurahi,naongea naye tu, ila kwa tahadhari, kwani mama alishaniambia kuwa nisipoteze muda kwa kuongea ongea...’akasema.

`Ikazidi, kwani nilishawahi kumfuma baba akinichungulia,....’akasema na watu wakaguna

‘Akikuchungulia kwa vipi?’ akaulizwa

‘Kama nimetoka kuoga, nikiingia chumbani kwangu,kama mama hayupo, baba anaweza kuingia chumbani kwangu ghafla na kujifanya kauliza kitu, na wakati huo huenda nilikuwa nipo uchi, kwani .....’akatulia

‘Tunaelewa endelea..’akasema mama.

‘Kuna kipindi alikuwa akija usiku nimelala, na kuanza kunifunua nguo...nikishituka, anasema alikuwa akinifunika vizuri,....’akasema

‘Oh, muongo mkubwa wewe, unawadanganya watu , mimi niliwahi kukufanyia hivyo, nitakukomesha kwa uwongo wako...’mume wangu akasema kwa hasira na wakili wake akamtuliza.

‘Je alikuwa akifanya hivyo, akiwa amelewa?’ akaulizwa

‘Hapana hiyo ilikuwa mwanzoni kabla hajaanza kulewa, na alipooanza kulewa, ndio akaanza visa vyake...’akasema.

‘Haya tuambie hivyo visa vyake vilikuwaje...’ akasema mwenyekiti

‘Alianza kunitongoza...’akasema na watu wakaguna

‘Hahaha, anamtongoza binti yake,…jamani…’akasema mama

‘Eehe, alikuambiaje, na ulijuaje kuwa anakutongoza, na wewe ulimjibuje vipi?’akaulizwa

‘Aliniambia kuwa ananipenda sana, na anataka...anataka tuwe wapenzi wa siri...’akatulia kidogo.

‘Akasema atanifundisha jinsi ya kupata raha ya mapenzi,...’akatulia kiogo.

‘Mungu wangu…’mimi nikasema hivyo nitaka kumwambia huyo binti asiendelee maana nilikuwa naumia ndani kwa ndani, kila hatu ilikuwa ni mateso kwangu.

‘Kwa kipindi kile mimi sikuwa namuelewa ana maana gani, ila akilini mwangu ikanituma kuwa huyu anataka nifanye naye kitendo kibaya, ..’.akasema.

Basi aliponitongoza tena, mimi nikamwambia;.

‘Wewe nakuheshimu kama baba yangu, kwanini unaniambia mambo kama hayo, yeye akasema hajanizaa, na mimi ninaweza kuwa hata mke wake, na yupo tayari kuninunulia chochote hata kunijengea nyumba ya kifahari huko kijijini,...’akasema

‘Mwongo sana huyo binti msimsikilize ni mfitinashaji huyo ndio maana nilimfukuza..’akasema mume wangu lakini hakuna aliyemsikiliza

‘Wewe endelea, cahana na huyo…’akasema mama

‘Mimi nikamwambia mimi nawaheshimu wao kama wazazi wangu siwezi kufanya jambo kama hilo, na mama yangu alinikataza kabisa kufanya huo uchafu, kwani mimi bado mdogo, na natakiwa kufanya hayo mambo nikiolewa...’akasema

‘Ulimwambia hivyo huyo baba yako, na ulijuaje kuwa anataka mfanye mambo machafu, ?’ akaulizwa

‘Ndio nilimwambia hivyo, yeye aliniambia kuwa anataka tufanye mapenzi, ...’akasema

‘Wewe mapenzi uliyajuaje..?’ akaulizwa

‘Mimi nilifahamu mapenzi ni kitu kichafu, lakini ni kizuri kwa wandoa, ..shuleni tuliwahi kufundishwa vitu kama hivyo…kwahiyo mimi hapo nilifahamu kuwa ananitaka kwa mambo machafu , mama alishaniambia hayo kuwa mwanaume akisema anataka kufanya mapenzi na wewe ujue anataka kufanya mambo mabaya ya kukuharibu usichana wako, ....’akasema.

‘Baba hakuchoka  kunibembeleza na aliniambia nikumwambia mama hayo anayoniomba, atahakikisha narudi kijijini na kuwa masikini wa kutupwa,...nikaaogopa sana, kwani kule kijijini kweli baba yangu huyo wanamuogopa sana....’akasema

‘Kwanini wanamuogopa?’ akaulizwa

‘Wanasema baba huyu ni tajiri na anaweza kukufanya lolote asifungwe, kwa vile ana kampuni yake kubwa, na anajuana sana na polisi...na pia anajuana sana na yule mwanasheria aliyekufa, ...’akasema

‘Kwanini huyo mwanasheria aliogopewa…samahani kidogo japokuwa tunamteta marehemu lakini hapo kuna ushahid pia tunauhitajia,…’akasema mwenyekiti

‘Huyo mwanasheria aliyekufa naye alikuwa akiogopewa sana, kuliko hata baba, kwasababu wanasema anafahamu  uchawi wa kisasa, anaweza akakuangalia hivi akakuambia yoye unayofikiria kichwani mwako,anaweza kujua kitu gani ulikuwa ukifanya nyumbani kwako, wanamsema kwa mambo mengi tu,...anaogopewa sana kule kijijini, na huyo alikuwa rafiki mkubwa wa baba yangu huyu ...’akasema

‘Kwahiyo alipokutongoza alikuambia kuwa usipomkubalia atakuloga au atakufanya nini?’ akaulizwa

‘Hakusema kuwa ataniloga,yeye  alisema atahakikisha mimi na familia yangu tunasota, tutakikimbia kijiji,na kuwa omba omba...na mama yangu atakufa kwa kihoro...mimi niliogopa sana alipofikia kusema mama yangu atakufa kwa kihoro..hata hivyo sikumkubalia alivyotaka yeye...’akasema

‘Siku moja alikuja nyumbani, huwa ana kawaida ya kuja akifahamu kuwa mama hayupo, na ananiambia niache kazi zote tongee, na siku hiyo akanituma pombe, akanywa na kunilazimisha mimi ninywe, nilikataa kabisa,...kuna muda akanituma maji ya kunywa nikaenda kumletea, akanywa, na mimi nikaondoka kufanya kazi zangu , baadaye akaniita, nikashangaa ananimiminia maji ya kunywa na kuniambia ninywe, kweli nilikuwa na kiu, lakini niliingiwa na wasiwasi nikijua huenda kaweka kitu.

Akanishika kwa nguvu mpaka nikayanywa yale maji..yalikuwa hayana ladha nzuri, sijui ilikuwaje, maana niliona macho yote mazito, ...nikawa sina nguvu tena, akanibeba, hadi chumba cha akiba, akanilaza kitandani...hapo akaanza kulia ...’ hapo hakuweza kuendelea akaangua kilio..

Kulitulia kwa muda..mimi niligeuka kumuangalia mume wangu…unajua chuki, uso uliomwangalia ulikuwa sio wangu…lakini niliwastahi wazazi wangu nikabakia kutikisa kichwa tu

‘Niliumia sana siku hiyo, aliniumiza..alinishika kwa nguvu, na sikuwa an nguvu za kujitetea mwili wangu wote ulikuwa umelegea, lakini niliweka kuhangaika, na.....akaniumiza....sikuamini yaani baba yangu niliyemuamini kama baba yangu mzazi, alifikia hatua ya kunifanyia hivyo,mungu ndiye anayejua, ...’akatulia akilia

‘Hapo nikamkumbuka mama alivyoniusia, nikajitahidi kutimiza wajibu, nikawa namuogopa mungu, lakini baba akayaharibu yote hayo,..ningefanya nini hapo jamani, ..ina maana sisi kwa vile ni masikini wetu ndio watufanyie wanavyotaka, niliumia sana siku hiyo...nililia sana mpaka macho yakavimba…’akawa anaongea huku akiwa analia.

‘Endelea, usilie, ongea ili watu wasikie, unyama wa mtu anayejiona mwema usoni kwa watu kumbe kavaa ngozi ya kondoo..’akasema mama.

‘Alipomaliza shughuli zake, akaondoka, huku akisema nikimwambia mtu ataniua, atamuua na mama yangu...sikuweza kumwambia mama, wiki nzima nikawa kama mgonjwa, nikawa nalia,hadi mama akaja kunifuma nikilia, sikuweza kumwambia, kwa vile niliogopa kuvunja ndoa ya watu, na pia kwa vile baba alinitishia kuwa nikimwambia mama atamuua mama yangu. Nilimwambia kuwa nimemkumbuka marehemu baba yangu alivyokuwa akinipenda.

‘Tatizo mama kipindi hicho alikuwa na kazi nyingi, na kila unachomuambia anakuamini, hakupenda kunidadisi sana, akanipa pole, na kunishauri kuwa nisikumbuke sana kwani hayo ni mapenzi ya mungu, halafu akaniuliza kuwa baba ananisumbau tena,...kwa kuogopa nikamwambia hanisumbui...

‘Ikapita hiyo siku, na wiki nikijua hilo limekwisha, siku moja akiwa amelewa akanijia chumbani, ilikuwa usiku akanishika kwa nguvu,....na karibu aniue, alinikaba nikafikiria kuwa huenda alikuwa anataka kuniua, nilipigana naye sana, lakini akanizidi nguvu, baadaye akaanza kunizalilisha tena, ...’akasema

‘Kwahiyo kumbe ilikuja kwua ni tabia yake…?’ akauliza mama

‘Ndio…yaani karibu nimtapikie akwa jinsi nilivyo kuwa najisikia, harufu ya pombe na matendo yake, ...nilijua nafanyia yote hayo kwa vile mimi ni masikini, nitasema nini nieleweke kwa jamii, akafanya alichotaka akaondoka...kesho yake nikataka kumwambia mama, lakini ikashindikana, kila nilipotaka kumwambia mama, baba anakuwa karibu, na siku ikapita., Siku ikipita unajikuta umesahahu, ukikumbuka inaishia kulia.

Basi nikaona niache tu iwe kama iwavyo, akawa akifika, usiku anajifanya halali na mama, anakuja kulala chumba cha akiba, akiona kupo kimiya anakuja kwangu..nikawa najitahidi hivyo hivyo, ila sikuwa na raha, nikawa nalia sana, na kuanza kukonda, na baadaye ndio nikagundua kuwa nina miimba..sikujua kuwa ni mimba, siku hiyo nilikwenda kupima malaria, nilikuwa najisikia vibaya sana, mama akaniambia nikapime malaria, ndio docta akaniambia nina mimba...

Nilipotoka pale nikapitia duka la dawa za mifugo nikanunua sumu ya kuulia wadudu, baada ya kuuliza na kuambiwa hiyo dawa binadamu akinywa anakufa mara moja,..akilini , nilishazamiria kujiua tu, sikujiona binadamu mwenye thamani kwenye hii dunia, kwani sikuweza kuvumilia tena,nilishaona kuwa nimefanya makosa makubwa, kwanini sikumwambia mama yangu huyo wa kufikia mapema...nilijiona mzembe, ...mkosaji asiye na maana .

Akilini mwangu, nilijua hata nikimwambia mama kwa sasa hataweza kuniamini tena, ataona mimi nilikubali kirahisi , na atanichukulia mimi ni mzinzi, Malaya. Na pia sitaweza kumwambia mama, yangu mzazi, nitamuumiza sana, mama ambaye siku zote alikuwa akinionya,nisije kujiingiza kwenye uchafu wa zinaa, je nitmwambieje mama yangu,  nikaona bora nikajiue tu....niondoke kwenye hii dunia, wabakie wenye pesa zao.

Nilipofika nyumbani nikaikoroga ile sumu kwenye kikombe cha plastiki, ilikuwa haiwezi kuonekana maji hayakubadilika rangi, nikaweka kwenye meza karibu na kitanda changu, nikachukua karatasi na kuandika ujumbe nikielezea kila kitu ilivyotokea...

Nilipomaliza hiyo kazi ya kuandika,... sikutaka nife kabla sijatimiza wajibu wangu, kwahiyo nikahakikisha nimefanya kazi zangu zote za nyumbani,...nilipomaliza nikaoga, nikamuomba mungu, nikaingia chumbani kwangu,nikaichukua kile kikombe, ambacho kilikuwa na maji niliyochanganya  na ile sumu ....

Wazo likanijia, kuwa nisifie chumbani kwangu, nikaona sehemu nzuri ya kufia ni kule kule nilipozalilishwa , nikavua nguo zangu za kawaida, nikachukua gauni kubwa jeupe, refu, lenye mikono mirefu, nikalivaa, halafu moja kwa moja nikaenda chumba ambacho baba alianzia kunizalilisha

‘Pale nikamuomba mungu tena, na kulia, nikisononeka, na kila uchungu ulivyonizidi, ndivyo tamaa ya kujimaliza ilivyozidi kunijia, kuna muda nilikuwa nasita kufanya hivyo, nikimkumbuka mama yangu, lakini baadaye nikaona jambo jema, ni kuondoka hapa duniani, bila kupoteza muda nikanywa yale maji niliyokuwa nimechanganya na sumu...

NB: Tuendelee na huyo binti, au ..tukutane sehemu ijayo.


WAZO LA SIKU: Tuweni na ubinadamu kwa wafanyakazi wetu wa ndani, visa vingi vinaelezewa jinsi gani wafanyakazi hawa majumbani wanavyonyanyaswa au kuzalilishwa, lakini wengi wanaofanyiwa hivyo wanashindwa kuongea ukweli kwa wazazi wao kwa kuogopa , na wengi wanaofanyiwa hivyo ni watoto wa kike,wasichana….je wewe uliwahi kumuuliza mfanyakazi wako wa ndani kuhusu shida zake, je yupo salama na baba….tuwaulize kama mabinti zetu wa kuzaa.
Ni mimi: emu-three

No comments :