Mwenyekiti, akauliza tena;
‘Huyu mtu ameenda wapi, mnakumbuka nyie ndio mliotaka awepo hapa
kwenye hiki kikao mkifahamu kuwa anatafutwa na polisi kwa uhalifu, na mimi
nikamthibitishia ofisa wa polisi kuwa, huyo kijana atakuwepo hapa hadi mwisho
wa kikao…?’ akauliza mwenyekiti na watu wote wakawa kimia.
‘Hakuna wa kujibu .. mnataka mimi nieleweke vipi kwa hao watu wa
usalama, kuwa nilikuwa namuhadaa, au sio,…sasa niambieni huyu mtu kaenda
wapi...?’ akauliza mwenyekiti kwa ukali, lakini wote walibakia kimia kuashiria
kuwa hakuna aliyemuona akitoka.
‘Mwenyekiti, inawezekana huyu mtu alitoka kipindi tunaangalia hiyo
lap-top yako, na kwa kipindi hicho hakuna aliyefikiria kuwa huyu mtu ataondoka…’akasema
docta, na wakili naye akasema hivyo hivyo.
‘Haiwezekani mtu atoke humu ndani bila ya mtu yoyote humu,
kumuona, docta , wewe na mke wako mlikuwa huku nyuma, karibu na yeye,
nakumbuka hata wakati tunaendelea na hilo zoezi, hususani mke wako ambaye kwa
muda mwingi alikuwa amekaa huku nyuma, alikuwa wa mwisho kuja kuangalia
tunachokifanya, kwahiyo nina uhakika, yeye atakuwa kamuona huyo kijana akitoka,
kwanini tusiwe wakweli, ...’akasema mwenyekiti.
‘Hapana mimi sijamuona akitoka, kiukweli mimi muda mwingi nilikuwa
nimegubikwa na mawazo yangu, sikuwa nikimtizama mtu, na hata ningelimuona
akitoka ningelijuaje kuwa anatoroka, sikumuona kabisa...sikuwa na haja ya
kumuangalia yeye, nina mambo yangu mengi kichwani ya kuangalia, kwanini
nihangaike kumchunga yeye, ....akili yangu haipo hapa jamani’akasema huyo mke
wa rafiki ya mume wangu, na mwenyekiti akamwangalia kwa mashaka, na kumuuliza
‘Unavyozungumza hivyo hueleweki, ina maana haupo pamoja na sisi
hapa kwenye kikao, sasa umefuata nini, ni kweli unaonekana kabisa kama vile
haupo ndani ya kikao, upo kimwili lakini kiakili unaonekana haupo kabisa, kuna
tatizo gani linalokukabili?’ akauliza mwenyekiti.
‘Haya ni ya kwangu, niachieni mimi mwenyewe, kama ikibidi Itafika
muda wake, mtayafahamu, ....mimi naona tuendelee na kikao, huyo muachieni
polisi hao ndio kazi yao....’akasema huyo mke, na mimi nikaona niingilie kati
nikasema;
‘Baba , hilo la kutoroka kwa shemeji yangu, tuwaachie polisi
wakiuliza tutawaambia ukweli, sisi sio walinzi wa huyo mtu na sisi
hatutawaficha ukweli,ni kuwa huyu mtu alikuja kwenye hiki kikao na
baadaye akatoroka,sisi tungelifanyaje...’nikasema
‘Hilo unalitamka tu kirahisi bila kujali kuwa mimi ndiye
niliyemdhamini, hivi kweli kuna mtu
atakuamini ukisema hivyo, hivi nyie taifa la leo mna nini akilini mwenu,
msipende kuchukulia mambo kirahisi tu, kitendo kama hiki kinatutia dosari,
uamanifu wetu unapungua,..'akafoka mzee.
‘Ni kweli baba, lakini imeshatokea swala ni tufanye nini…’nikasema
'Kiukweli mimi sipendi kabisa tabia ya namna hiyo...unapoahidi
kitu, unatakiwa ukitimize, ...mimi sio tabia yangu ya kukubali dhamana halafu
ninakuja kuihini,mnaniharibia mwenendo na tabia yangu..’akasema mwenyekiti na
kuanza kupigia simu, alikuwa akiwapigia watu wa usalama, akaongea na huyo mtu
wa usalama, na kumuelezea ilivyokuwa na alipomaliza kuongea naye akasema
‘Sawa tuendelee, wanamfuatilia wao wenyewe kwasasa, ila imewakwaza
sana, kwani hatukutimiza wajibu wetu,…sasa wewe kaka mtu, mdogo wako
keshaharibu, hata kama tulitaka kumsaidia, sasa haitawezekana tena,..,
keshajiharibia yeye mwenyewe kabisa, ...’akasema
*********
‘Kwanini mnamfanyia hivyo mdogo wangu,kwani ungekaa kimiya
unafikiri hao polisi wangekuja kukuuliza, nyie mnajipendekeza tu kwa hao watu,
lakini hawatawasaidia lolote, siku yako ikifika wanakusweka ndani kama hawakujui…’
akasema mume wangu, na hapo nikakumbuka jinsi alivyomnong'oneza kitu muda
uliopita
‘Hiyo ndio tabia ambayo siitaki, na hilo nimekuwa nikiwakanya,
....kama umezoea tabia hiyo ya uwongo, mimi kwangu haipo, na kwanini unasema
tumemfanya nini mdogo wako, hakuna aliyemfanya kitu mdogo wako, unajua mimi
nilipanga nini akilini mwangu…’akasema mwenyekiti
‘Nilishakuwa na malengo ya kumsaidia, nilitaka tukitoka hapa mimi na
yeye mguu kwa mguu hadi kwa hao watu kuona yeye ana hatia gani,....sasa sisi
tushatimiza wajibu wetu kama raia wema, ....’akasema mwenyekiti.
‘Mdogo wangu hana hatia yoyote…,yeye sio mhalafu...polisi
wanamshuku bure,wameshindwa kazi yao sasa wanapapatika...na huenda kaondoka
hapa kutokana na vitisho vyenu, sasa mimi nasema hivi, kama litamkuta baya nyie
ndio mtawajibika...’akasema mume wangu.
‘Tuendelee na kikao chetu, atawajibika yeye mwenyewe. Na wewe mkwe…,
nakuonya, sasa sitaki utani,tuambie, imekuwaje, ukawa na mkataba tofauti na ule
mliokubaliana na mke wako, na ukijua kuwa huo ni ukiukwaji wa sheria,umekiuka
kiapo chako ulichokiweka kisheria wewe na mke wako, ndivyo unavyoishi
hivyo,...?’ akauliza mwenyekiti.
‘Mimi sijui kama huo mkataba ni tofauti na ule tuliokubalina na
mke wangu, kwangu mimi nauona ni ule ule,na kama nilivyowataka, japokuwa
msajili kasema hivyo, nahisi na yeye kaongea tu bila ya kuuangalia mkataba huu
nilio nao…’akasema akiwa sasa kaushika huko mkataba.
‘Mkataba huo ni ushahidi tosha kuonyesha jinsi ulivyo…’akasema
mwenyekiti.
‘Ni ushahid wa nini, mimi sijui kama upo tofauti na huo wanaosema
ni halali, kama wlaiona kuna tofauto hiyo kwanini hawakuniita mimi, mimi ndiye
mume, niye ninayefahamu ukweli wa huo mkataba, sasa kama kuna tofauti mimi
kiukweli sijui...na hiyo tofauti imetoka
wapi?’ akauliza mume wangu.
‘Unamuuliza nani hilo swali, hilo swali tunakuuliza wewe, kama sio
wewe, na kama hujui wakati wewe umekiri hapa kuwa wewe ni mume na wewe ndiye
unayebeba dhamana za familia, haya tuambie ni nani aliyeugushi huo mkataba,
kwanini kunapatikana mikataba miwili, huu mkataba ulio nao unatoka wapi, hayo
ni maswali yako ya kujibu...’akasema mwenyekiti.
‘Hayo nimeshawajibu, sijui...ninachojua ni kuwa huu mkataba ndio
halali.....na kama sio halali mimi sijui, kwangu mimi hadi sasa bado sijaamini
kuwa kuna mikataba miwili, mimi sijui..’akasema na watu wakamwangalia kwa
mashaka, na alipoona watu wanamwangalia yeye, akasema;
‘Kama ni hivyo, hebu tuuone huo mkataba mnaosema ni halali?’
akauliza
‘Umeshaonyeshwa na msajili wataka upi tena, eeh, usitusumbue
.....’akasema mwenyekiti
‘Mke wangu kasema anao mkataba anayo nakala halali ya huo mkataba,
kama anavyodai yeye,…nataka anionyeshe tofauti iliyopo kati ya mkataba huo na
nakala hii niliyo nayo hapa....’akasema
‘Mimi naona lengo lako ni kutupotezea muda, hebu mke wa familia
mtolee huo mkataba, anaoutaka yeye, na kwa amri ya kikao hiki, halali, tunataka
ujibue maswali yetu, kwani kila ulichokitaka umekipata, kwahiyo timiza wajibu
wako, sisi tumeshatimiza wajibu wetu....’akasema mwenyekiti.
Mume wangu akanigeukia, huku akionyesha kushangaa, pale aliponiona
nikitoa mkataba kwenye mkoba wangu, nikauinua juu, na kusema;
‘Mkataba halali ndio huu hapa, mkataba ambao umeuulizia ndio huu
hapa, hii ni nakala yangu...’nikasema na yeye akabakia mdomo wazi, akiwa katoa
macho ya kutokuamini.
‘U-ulipatia wapi …haiwezekani…’akasema kwa kigugumizi
‘Mpe wakili wenu wa familia authibitishe kuwa ndio
wenyewe,..’akasema mwenyekiti, na mimi nikainuka na kwenda kumkabidhi wakili wa
familia ambaye aliufunua akaanza kuukagua na kufanya kama alivyofanya kwenye
mkataba aliokuwa na mume wangu, halafu akatabasamu na kuuliza;
‘Umeipatia wapi hi nakala, ndio wenyewe kabisa, sasa mambo
yamekwisha, tumemaliza kazi...’akasema kwa furaha.
‘Siamini ina maana mke wangu umeamua kunifanyia hivyo, ...ina
maana ..haiwezekani, kumbe,..hapana,....umaupata wapi huo mkataba,
uli...uli...oh, huyu mdogo wangu yupo wapi’akasema huku akiwa kashika kichwa.
‘Haya mume wa familia, sasa kazi inaanza, natumai sasa upo tayari,
kuwajibika kama ulivyoahidi wewe mwenyewe,…hatuna muda wa kupoteza tena..,kama
wenzako wamekusaliti, utakwenda kuwauliza baadaye, sasa hivi ni kazi ...jibu
swali letu, kama ningelikuwa mimi ndio wewe ningekiri makosa na kukubali
yaishe, maana mwisho wa hadaa ni fedheha, kwanini unataka ufedheheke’akasema
mwenyekiti.
‘Swali gani,...sikumbuki kama uliniuliza swali...’akasema
‘Nilikuuliza kuwa kwanini huo mkataba uliokuwa nao ni tofauti na
mkataba halali, tunahitaji kulitambua hilo, kama wanafamilia, kama wajumbe wa
kikao hiki, na ikibidi pia sheria inatakuhitajia uilezee kwani wao bado
wanatafuta kiini cha hilo tatizo, ilikuwaje kuwepo na mikataba
miwili,..’akasema mwenyekiti.
‘Ndugu mwenyekiti, mimi muda mwingi nilikuwa naumwa, na siwezi
kujua jinsi gani huo mkataba ulivyobadilika, mimi hadi sasa sioni tofauti yake,
sijaona hayo mabadiliko ni yapi...’akajitetea hivyo.
‘Kwahiyo bado hutaki kukiri kuwa kuna hujuma mlipanga, kuwa
mlifanya kosa, kwahiyo kama wanafamilia, kama kikao tukufikirieje, unaonekana
unatujaribu, unatuona sisi hatuna akili?’ akauliza mwenyekiti.
‘Sijasema hamna akili, lakini siwezi kusema mimi nimefanya hujuma,
nikiri kosa ambalo sijalifanya, hilo halipo,kwani kama ni hujuma
iliyofanywa mimi siijui, huenda kuna watu walifanya hivyo, bila ya mimi kufahamu….’akasema
Ni nani zaidi yako wewe ambaaye ni muhusika, na wewe ulianza
kutimiza yaliyoandikwa kwenye hiyo katiba tofauti na ile ya kwanza, unafikiri
sisi ni watoto wadogo au…’akaambiwa
‘Ninachoongea hapa ndio ukweli, kuwa kipindi hicho nilikuwa
mgonjwa, yote haya yamefanyika, nilipopata ajali, ndio maana nimekuwa
niking’ang’ania kuwa hiyo katiba ndiyo ile katiba niliyo kuwa awali na ndiyo
iliyokuwa sahihi, mimi sikumbuki kuwa na katiba nyingine tofauti..mnakumbuka
kuwa ajali hiyo ilinifanya niwe nasahau...’akajitetea.
Kukawa na ukimia kidogo
***********
‘Lakini kama sikosei, katiba hiyo inavyoonyesha ilibalidilishwa
kipindi wewe hujapata ajali, ina maana mipango hiyo mliipanga mapema, na
mlikuwa mkiifanyia kazi hatua kwa hatua,, na ajali hiyo ilipotokea mkapata
sababu nyingine, na hiyo ajali ilitokea mkiwa kwenye michakato yenu ya
kukamilisha hiyo hujuma....’akasema mwenyekiti.
‘Ulikuwa unawahi kufanya jambo, bahati mbaya ajali ikakukuta
njiani…’akaambiwa
‘Mimi hayo siyajui, nayasikia kutoka kwenu, na kwa jinsi
inavyokwenda hapa sasa, mimi naona nimuite wakili wangu, kwasababu mnataka
kunitia hatiani, na mimi sitaweza kujitetea kwa hali kama hii, ni lazima
mwanasheria wangu awepo...’akasema
‘Hatujafika huko, ikifika huko ikibid tutakupa nafasi hiyo, lakini
bado tunakuhitajia wewe uwe mkweli kwetu, unasikia,…’akaambiwa
‘Hata nikisema ukweli ni nani ananiamini kwasasa..hakuna nyote
mumeshaniona mimi ni mkosaji..nimekosa nini,…eeh, sasa ili na mimi niwe na
amani, nataka hili swala liende kisheria, awepo hakimu wangu hapa…’akasema
‘Kwahiyo wewe, sasa unarudi kule kule, kuwa hili swala kwa vile ni
la kisheria zaidi, na linaonekana ni kuvunjwa kwa sheria, kama alivyopendekeza
awali wakili, tulipeleke kisheria zaidi, ikibid twende ngazi za juu, tulipeleke
hili swala mahakamani, si ndivyo unavyotaka wewe..’akaulizwa
‘Sijasema twende mahakamani, ...sio lazima twende mhakamani, hapa
tuna mawakili wenu, lakini hatupo mahakamani, hawa mawakili hawanitetei mimi, wanatetea
nafsi zenu , matakwa yenu, mkinisakama mimi wao wataangalia jinsi gani y
akunibana mimi kisheria wajuavyo wao,.. basi ngoja ni mimi nimuite wakili wangu
ili naye aangalie upande wangu.....’akasema.
‘Hakuna anayekusakama wewe, wewe ndiye uneyeweka kwenye mazingira
ya kuonekana hivyo, kama ungelikubali kusema ukweli, haya yote yasingelitokea,
kwanini usikubali kuwa kuna shetani aliwapitia, mkaamua kupanga hayo
mliyoyafanya, lakini kwa vile dhamira mbaya haijengi, basi imefika
kikomo,kubali, tuangalie jinsi gani tutalimaliza hili tatizo...’nikasema.
‘Wewe mke wangu hujui tu, mimi nayafanya haya kwa masilahi ya
familia yetu, hapa nafanya kila iwezavyo kuulinda ndoa yangu, wenzako wanataka
ivunjike, hili lipo siku nyingi, kama kweli unanipenda, ulitakiwa uwe pamoja na
mimi....huoni kuwa wamenitega,...lakini nawaambia hivi hata kama mke wangu
haupo na mimi bado wewe ni mke wangu,...’akasema.
‘Sikuelewei ukitaja neno kupenda,....’nikasema.
‘Unaona, nilijua kabisa mnanitega, wewe na familai yenu,
mumelipanga hili makusudi,na kwa vile umeshaona mumefanikiwa mipango yako, sasa
unatafuta njia za kuniharibu kabisa maisha yangu, mimi sikubali....na kwa hilo
la kukubali kuwa nimefanya kosa, mimi hadi hapo sioni kosa langu kabisa, mimi
kauli yangu ni hiyo kuwa sijui kama hiyo katiba iligushiwa, na hiyo mipango
mnayosema nyie mimi siifahamu, ni nani walifanya hayo nyie ndio mnaofahamu, sio
mimi, kwanini mnanilazimisha niseme uwongo.’akasema.
‘Kwahiyo unataka tulitolee ushahidi kama hilo la hiyo katiba kuwa
sio katiba halali, ujue kila tutakavyofanya hivyo ndivyo na sisi tunashindwa
kukuamini tena, na hapo ina maana kuwa wewe haupo nasi..unajiweka mbali na
sisi, unaikimbia ndoa yako kiujanja, huku unajifanya upo nayo’akasema
mwenyekiti.
‘Tangu hapo naona mumeshaniweka pembeni, sizani kwenye nafsini
mwenu mpo na mimi tena, mumeshaniweka kwenye kundi la wahalaifu, unaona mdogo
wangu ambaye hana kosa mumeshamuitia polisi, na nahisi hata mimi mtanifanyia
hivyo hivyo,niwaulize kama angelikuwa ndugu yenu wa damu awe anatafutwa na
polisi, mngelimfanyia hivyo mnavyomfanyia ndugu yangu,au kwa vile sio ndugu
yenu?’ akauliza
‘Huo ni unyonge unaojitakia, nimeshakuambia, wewe kama mume wa
familia unatakiwa upambane kiume, lakini katika misingi ya ukweli na haki, hiyo
kauli yako uliyoongea sasa hivi kuwa tunakuonea wewe na ndugu yako, ni kauli ya
kujizalilisha, kujishusha, ni unyonge wako mwenyewe, ...ongea ukweli, toa hoja zenye mshiko, tuoni
ukweli upo wapi,...’akasema mwenyekiti.
‘Ukwelii gani nitakaouongea sasa hivi mniamini, mimi
sijajizalilisha, ndio maana ninaendelea kukataa hayo mnayonishinikiza nayo,
haya nipeni huo ushahidi kuwa mimi nilikuwepo kwenye huo mpango wa kufanya hayo
yaliyotokea...maana ndivyo mnavyotaka nyie, mimi nimeshawambia ukweli wangu,
hamunikubalii, sasa kwa vile mnaona nasema uwongo, nikosoeni kwa kulibainisha
hilo...’akasema kwa kujiamini.
‘Kwa hali hiyo ni kuwa hutaki kusema ukweli, unataka sisi
tuutafute kwa nguvu za ushahidi, ..kama unataka iwe hivyo, sisi tutafanya,
lakini kwa mtaji huo ni kuwa wewe hutaki kushirikiana nasi, hutaki kuwa
mwenzetu, ukatusaidia tukalimaliza hili tatizo kama wanandugu....na kwa hali
hiyo ikibainika na ndivyo ilivyo, tukatoa ushahidi, basi hatuna jinsi nyingine,
hukumu itafuatia kitanzi chenu wenyewe kitakuhukumu.’akasema mwenyekiti.
‘Kwahiyo nyie mnataka mimi niseme nini?’ akauliza
‘Sema yote yaliyotokea, jinsi gani mlivyoibadili hiyo katiba, na
kwanini ,lifanya hivyo. Na mlikuwa na nani na nani, halafu unaomba msamaha
yamekwisha,...sisi kama kikao tutakaa na kuangalia jinsi gani ya kulimaliza...
huo ndio uadilifu na utawala bora, kwanini mnataka msutane kwanza, mshikane
mashati, hata ifikie damu kumwagika, ...hiyo ni tabia ya watu wasio
waungwana’akasema mwenyekiti.
‘Mimi sio mtoto mdogo, wa kudanganywa kihivyo, nawafahamu sana,
hapo mnataka kunitega tena, kama mlivyonitega hapo mwanzo, ...ukweli
niliouongea ni huo huo, kama kuna ukweli mwingine niambieni nyie, na
mnithibitishie na mimi kama nitaona kuna ukwel ambao niliusahau ,au nilikuwa
siujui, maana mengi yametokea nikiwa mgonjwa, sikumbuki, nikumbusheni
nyie,....’akasema
‘Na ikiwa ni hivyo, tukakuthibitishia kuwa ni mpango ilipangwa na
wewe ukiwemo ukiwa na akili zako timamu, ukishirikiana na wenzako, kwa ajili ya
masilahi fulani, .. upo tayari kuwajibika?’ akaulizwa
‘Hiyo ni juu yenu...lakini mimi sijui kama kulikuwa na mipango
huyo, mimi sikumbuki....’akasema.
‘Unakumbuka sana, unalifahmu sana, ndugu mwenyekiti naona
tunapoteza muda, huyo mtu nimeshamuelewa, ...anachotaka ni kuona je tunafaamu
hiyo mipango yao, je tunafahamu hayo aliyoyafanya yanajulikana,...hataweza
kukubali na kusema ukweli...mimi naona tuendelee na kikao, na hatima ijulikane,
mkataba upo utafanya kazi yake...’nikasema.
‘Kutokana na uchungzi uliofanyika, inabainisha wazi kuwa mipango
hiyo ilikuwepo kabla ya wewe hujapata ajali, ...watu wanaohifadhi hiyo
mikataba, wamelibainisha hilo, na hata huyo mtu mliyeingia naye kwenye hilo
kosa, baada ya kubanwa, na baada ya uchunguzi alikuja kusema kila kitu. Hata kama
kulikuwa na shinikizo lakini ndani yake kulikuwa na mbinu zenu....’akasema
mwenyekiti.
‘Mimi hayo sijui....sikumbuki, kama nilivyowaambia ninachojua mimi
, hii ndio katiba, niliwahi kuwekeana na mke wangu,kama kulitokea kubadilishwa,
basi labda kuna mtu alifanya hivyo, akanitumia mimi kama chambo, kwa vile
anafahamu kuwa kumbukumbu zangu hazikiwa sawa...’akasema
‘Alikutumia kwa msilahi ya nani, yake au ya kwako, hebu tuangalie
hiyo katiba, tutakuja kuiangali vipengele mlivyobadilisha, vilikuwa vinamgusa nani,
na kwa masilahi ya nani, na hapo mengi yatagundilikana, kwahiyo ndugu yangu,...usitudanganye hapa, na
kama unahisi hivyo kuwa labda kulikuwa na mtu kafanya hivyo kukutumia wewe,
basi tuambie ni nani huyo mtu...’nikasema.
‘Ni kwa masilahi ya familia yangu, mimi na wewe na watoto wetu…,
ukiangalia hiyo katiba eeh , nilivyoisoma mimi, inatuhusu mimi na wewe mkwe wangu, na ya
kwamba hakuna mtu mwingine wa kuingilia masilahi yetu, zaidi ni mimi na wewe,
kuilinda ndoa yetu , watoto wetu na familia yetu kwa ujumla....’akasema
‘Ni ile ya mwanzoni ilikuwa haifanyi hivyo?’ nikamuuliza
‘Mimi sijui hiyo katiba ya mwanzoni ilikuwa inasemaje, sikumbuki,
kwani ninachofahamu mimi ni jinsi nilivyosoma kwenye katiba hii, labda nyie
mnikumbushe ..’akasema.
Mwenyekiti akamtizama binti yake, na kutikisa kichwa, kama
kusikitika, na wajumbe wengine kwenye kikao wakaonekana kuchoka, na hapo
mwenyekiti akasema;
‘Naona tupate mapumziko kidogo, tukirudi tunaingia ajenda
nyingine, sasa tukitumia katiba halali, mliyojiwekea nyie wenyewe, si ndivyo
uliahidi mjumbe, mume wa familia, hakuna kurudi nyuma kwa hilo…’akasema
mwenyekiti
Mume wa familia akabakia kimia
‘Tulishajua mbinu zenu, na huu ujanja wenu sijui mlifikiri
hamtapatikana, na hapakwenye kikao, limeshafahamika, kuwa baada ya ajali, kuna
muendelezo wa mambo mengi, ajali hiyo ilitumiwa kufanikisha mambo mengi, ni
kama ilipangwa…’akasema mwenyekiti
‘Ilipangwa…!!’ akasema mume wangu kwa kushangaa.
‘Ni kweli baada ya hiyo ajali, wewe ulipoteza kumbukumbu, na mengi
yalifanyika kipindi hicho, ...huenda ilichukuliwa hivyo kama mwanya wa
kukamlisha huo mpango, mpango ulikuwa umepangwa kabla ya hiyo ajali, ...’akasema
mwenyekiti
‘Kwahiyo unamaanisha kuwa kwenye huo mpango tulipanga mimi nipate
ajali, ili baadaye nisingizie kupotewa na fahamu,yafanyike kama yalivyotokea
...hivi kweli kuna mtu mwenye akili zake anaweza kufanya jambo kama hilo
la hatari, ina maana hata hawo madakitari walionihudumia wanahusika na
huo mnao-uita mpango, maana wao wanajua fika kuwa nilipotewa na fahamu , na
kupoteza kumbukumbu kwasababu ya hiyo ajali.....?’akasema mume wangu.
‘Hatukatai kuwa kutokana na hiyo ajali ulipoteza kumbukumbu na hali
hiyo akasababisha wewe kutokukumbuka mambo ya nyuma, lakini hiyo kwa mtizamo
wenu,na uchunguzi wetu hali hiyo ilikuwa imetokea kwa muda fulani tu,
ambao kitalamu inajulikana, ...wewe ukauendeelza ule muda, na kuendelea
kujifanya kuwa bado unaumwa, ili kutimiliza malengo yenu....’nikasema.
‘Hivi kweli mke wangu unaweza kusema maneno kama hayo, naona kweli
umenichoka, sikujua kama utafiki hatua hiyo, ....kuna nini kibaya
nilichokufanyia ambacho kimeweza kukugeuza na kunichukia kiasi hicho…?’
akauliza mume mtu.
‘Hakuna aliyekuchukia ni matendo yako yanatufanye tuwe hivyo, na
kwanini hutaki kukiri kosa…’nikasema
‘Nikiri kosa , kosa lipi,..huo ni mtego wenu,..mtego ambao wazazi
wako wanausubiria,…kwanini mimi
nisingizie ugonjwa, mke wangu, kuwa naumwa na uzidi kuteseka, ili iweje,
hapana, siwezi kukufanyia hivyo, hizo ni hisia umepandikiziwa, usiwasikilize
watu wasioitakia mema ndoa yetu....’akasema.
‘Mjumbe, usitusingizie sisi wazazi, hilo ni lenu wawili,…mimi
huwezi kunidanganya kitu,nakufahamu sana, usijifanye kuwa hayo yaliyotokea
huyafahamu, nakufahamu na washirika wako wote nawafahamu…,mimi nilitaka kuona
kuwa kweli labda umebadilika kama alivyokuwa akidai mke wako, lakini kwa haya
uliyoyaonyesha leo, sioni ajabu ....lakini haya bado tuendelee kukupatia nafasi
nyingine ya mwisho..ila kwangu mimi nataka kusikia ulivyofanya hayo, na kwanini…ukiyaeleza
kiunaga ubaga, nitajua kweli umekiri kosa na hukumu itabakia kwa wajumbe….’akasema
mwenyekiti.
‘Mimi sielewi hapo…ina maana baba mimi nijifanyize ajali,
nijifanyize ugonjwa, hapana , hiyo sio kauli nzuri kutoka kwa wazazi…’akasema
‘Ajali iliyokupata, ilichukuliwa kama nafasi nzuri ya kufanikisha
malengo yenu, na huenda kulikuwa na hujuma kwenye gari lako, hicho kitu utakuja
kupambana nacho kwenye taarifa ya polisi ambayo haijawekwa wazi,..ajali hiyo...ilipangwa
makusudi, ili itokee, ....’akasema mwenyekiti na mume wangu akamuangalia
mwenyekiti kwa jicho la kushangaa…
‘Lakini hilo halikuweza kuthibitishwa,…kuna kitu kilitakiwa
kifanyike, muulize mke wako aseme ukweli…atakuja kuyaelezea hayo yote kama
kweli anataka kuelezea ilivyokuwa, hatujasikia alichopanga kuelezea,..wewe ndio
umevuruga utaratibu…’akasema mwenyekiti
‘Unasema nilipanga ajali, baba ni kweli uanongea jambo kama hilo…na
mke wangu unabakia kimia, ndivyo mlivyoongea hivyo..’akauliza
‘Inavyoonekana ndivyo..hata polis waliliona hilo, japokuwa halina
nguvu, na mimi nikawaoba wasiliongelee maana ni hisia labda ..labda..na
vielelezo, inavyoonekana ilitakiwa mimi ndio nije kupata ajali na hiyo gari,…
nia ni mimi nife , kwani siku hiyo kama unakumbuka vyema nilikuomba gari lako,
nilitumie mimi,....lakini kwa bahati , ukalichukua wewe mwenyewe, sijui ni kwa
kusahahu au ilikuwaje, mimi hapo ndio sijui, ndio maana nikawaomba polis
waliache hilo kama lilivyo....’nikasema
‘Huo ni uwongo wa hali ya juu, mimi nipange kukua wewe halafu
unakubali huo uzushi, kwanini nifanye hivyo...’akasema mume wangu.
‘Hiyo ajali ilipotokea, ikawa imefanikisha baaadhi ya mambo
yenu,hata kama utakataa kuwa hiyo ajali ilipangwa, kwa nia ya kumuua binti
yangu, na iliposhindikana lengo lake hilo, ikageuzwa, ikachukuliwa kuwezesha
mambo mengi,mengi yalifanyofanyika yalifanyika baada ya hiyo ajali, ili
usiwepo nyumbani, ili isionekane kuwa wewe unahusika, ...’akasema mwenyekiti na
mume wangu akatikisa kichwa kukataa.
‘Kiukweli hii ni kashfa ..mnanikashfu..na sitaweza kuvumilia hili..hiyo
kauli yenu inanisikitisha sana…kiukweli siwafichi, imeniuma..na sijui kama
nitaweza kuwaamini tena, sawa…ila nitataka hili mlithibitishe,la sivyo..hata
sijui..’akasema
‘Kwa vile tumeongea sana na huu ni muda wa kupumzika, ...hiki
kikao kinakupa nafasi ya mwisho, ya kufikiria kwa makini..., tukirudi uje na
ukweli, kama utaendelea kutuficha huo ukweli ambao sisi tumeshaujua, kikao,
kitakuchukulia wewe kama mhalifu ambaye kafanya kosa, lakini hataki kukiri
kosa, na hivyo, unatuweka katika nafasi ya kutengeneza kesi, na yote mengine
yatabainishwa, na hapo hatutakuwa na kurudi nyuma tena…’akaambiwa
‘Kesi ya nani,..ni nani mhalafu hapa..kuwa nilipanga kumuua mke
wangu au…?’ akauliza
‘Ni kesi dhidi yako ndio…kudanganya , kugushi…na mengineo,
yatakuja kujitokeza kama hutakubali kusema ukweli tukamaliza na mengine
yakamezwa, sisi ni wanadamu, tutaangalia utu,…sasa kaam wewe hutujali,
tufanyeje, kama hujijali familia yako, tufanyeje....’akasema mwenyekiti.
‘Hata siwaelezi…mimi nimeshasema yote haya,…ni kwa ajili ya
familia, yangu, ndoa yangu, na watoto wangu, hata hiyo katiba imenipa mamlaka
hayo,…sasa jaman kichwa kinauma…’akasema mume wangu, akishika mkataba wake
mkononi, kama anataka kuondoka.
‘Sasa tukapumzike kidogo, nafahamu bado kuna ajenda nyingi, zenye
maswali mengi yanayohitajai majibu mengi, wajumbe hapa wana yao mengi tu…, na
yote ni dhidi yako wewe…au nyie wanandoa wawili.., na moja wapo jingine ni
kuhusu kifo cha makabrasha,..hili linaanzia ni kwanini ulimuacha wakili wenu wa
kawaida ukaamua kumtumia Makabrasha, kifo chake kimeanzia hapo, sasa jipange na
hilo…’akaambiwa
‘Hahaha mnataka kusema mimi ndiye nilipanga hili pia, ili auwawe,
hapo sasa mumevuka mpaka, hilo, nipo tayari, hata makamani…’akasema
‘Ni katika kuweka haya mambo sawa, kabla hatujaenda kumpumzika, hebu
kwanza niambie ulikosa mawakili wa maana, mpaka uamue kumchukua Marehemu, eeh,
kila mtu anajiuliza hilo…’akasema mwenyekiti
‘Yeye ni wakili mbona anatambulikana kisheria, mimi sijui kosa
lake…’akasema
‘Nasikia , sio nasikia , ndivyo ilivyokuwa, kumbe marehemu ndiye
alikuwa kichwa chenu akisemacho ni lazima mkifuate..na uliamua kumchukua kabisa
sasa awe wakili wako ili kubadilisha hiyo katiba, lakini baada ya hilo, yeye
naye akakugeuka, na ndipo kifo chake kikatengenezwa,…hahaha, mjumbe hili unalo,
sisi tutamalizana na wewe lakini una kesi ya kujibu, haya hilo tutakuja
kuliongea badae!’ Akasema mwenyekiti na kumfanya mume wangu amuangalie
mwenyekiti kwa uso uliokunjamana kwa hasira
‘Sio kweli mwenyekiti, ninapinga hizo shutuma zote…’akasema mume
wangu kwa sauti kubwa.
‘Tumeshachunguza na kuligundua hilo, …baada ya kugundua wewe
umefanya makosa makubwa ya kukufanya uvunje ndoa ukose kila kitu, maana dhamira yako ni mali, hakuna zaidi…vingine
ni visingizio…ukaona njia ya kulikwepa hilo ni katiba…mikakati ikapangwa jinsi
gani ya kubadili katiba, marehemu akakuambia hiyo ni kazi rahisi kwake...’akasema
mwenyekiti na mume wangu akawa kainama chini.
‘Marehemu anatambulikana kwa uhalifu wake wa milungula, wenzetu
huko majuu, wanaita blackmail. Yeye kwasababu alisoma soma huko nje,
akaona kwa wabongo, hawana ufahamu sana na mambo hayo, basi anaweza kuutumia
njia hiyo kujitajirisha, hapa kwetu...’akasema mwenyekiti
‘Kosa kubwa linalobainsiha mipango yako, ni huko kumtumia
Makabrasha, ni kwanini umchukue yeye,… lakini hukujua kuwa unamfuga nyoka, ili
akulinde, wakati yeye ana sumu,, sasakwanini usituambie ukweli,ili tuweze
kuliweka hili jambo sawa,...tutahitajai majibu yako, ili tukusaidie, kama
hutaki, haya tutaona mbio za sakafuni huishia wapi..hilo...tukirudi,...usikimbie
kama mdogo wako..’akasema mwenyekiti, na mume wangu akasema;
‘Makabrasha ni rafiki yangu wa siku nyingi, kumtumia yeye, kwangu sio
jambo la ajabu sana, hilo naweza kulithibitisha popote pale, waulizeni hata
familia yake,.. na mengi anasingiziwa tu, mimi sipendi kumuongelea marehemu,
lakini nitajitetea kwa nafasi yangu, na kumtetea yeye ikibidi,lakini mimi
sitapenda kumuongelea yeye sana, maana hayupo duniani,…’akasema
‘Sawa tutaliongea hilo baadae…kila kitu kipo tayari, ushahidi wote
upo, ukikana huo ushahidi tunauwakilisha polisi, wao watajua jinsi gani ya
kukufanya, hapo hatutakuwa na lawama tena ..’akasema mwenyekiti
‘Vyovyote iwavyo, mimi sikubali kuivunja ndoa yangu…’akasema
‘Tutaona hilo tukirudi, kama nikuivunja ndoa yako utakuwa
umeivunja ndoa yako wewe mwenyewe,…muda umekwenda jamani…mnasemaje, tukapumzike
kidogo halafu tutarejea, au vipi docta… ’akasema mwenyekiti,..na watu wakasimama
na kunza kutoka nje
************.
Mume wangu badala ya kutoka
nje akanizonga,
‘Wewe mke wangu haya umeyasababisha wewe, sasa nakuambia hivi hata
ufanye nini, ndoa haivunjiki…si ndioengo lenu hilo…sasa ndoa itabakia hivyo
hivyo, ili tuone mwisho wake…’akasema
‘Kwanini hutaki kusema ukweli tukayamaliza haya mambo..?’
nikamuuliza
‘Tungeyamaliza tukiwa sisi wawili kulikuwa na kosa gani, kulikuwa
na haja gani ya kuita watu hapam kuanza kuumbuana na kunitwika makosa ambayo
sio ya kweli..?’ akauliza
‘Hilo la kuita watu bado kabisa, sijaliongelea,…huo ni mwanzo tu…maana
umesaidia kuweka mambo mengine sawa, kushinikiza kwako kwanza tuongelee mkataba
umenisaidia sana, sasa tutaingia kwenye kadhia yenye, ni kwanini nikaitisha
hiki kikao, jiandae kwa hilo, mume wangu nimekupa muda wa kutosha umeshindwa
kuutumia, nimeshajua lengo lako, sasa kabla hujaniwahi, naona kila mtu
alifahamu hilo…’nikasema
‘Hahaha, mke wangu, unafikiri mimi naogopa, utaona..hata kama hilo
mumepanga wewe na baba yako, au sio mimi halinitishi kwani wewe unajua mangapi
yako ninayafahamu tu,...wewe na rafiki yako mlijadili nini..hilo hutaki
lisikiwe na watu, eeh,…na na hapo nakupa angalizo tu,…na jingine nikuambia
ukweli, hakuna mwenye uwezo wa kuvunja ndoa yangu, hakuna..…wanasahau kuwa
ndona inavunjwa na mume…’akasema.
‘Kwanini unatetea kitu ambacho hakipo, au hulijui hilo..kiimani,
kisheria..wewe kwa vitendo vyako ulivyovifanya, ulishaivunja ndoa yako wewe
mwenyewe, bado unashikilia kuwa ndoa ipo ndoa ipo, hebu niambie, ina maana gani kung’ang’ania kuwa ndoa ipo na wakati
matendo yako yanaikana, una watoto wangapi nje,..eh, kauli zako za kuikana
ndoa, umeziongea mara ngapo kwa hao mahawara wako, eeh,....’nikasema
‘Haya ongea tu..utaongea mengi,lakini na mimi utanipa nafasi ya
kuongea mengi, nasubiria hio nafasi,…na kuvunja ndoa ni kutoa talaka, ni nani
alitoa talaka …wapi nilikutolea tamko kuwa nimekupa talaka,..wapi kwa maandishi
gani, acha wewe…huo mkataba uliubuni wewe, haya kama uliubuni wewe ndio mimi
nimetoa talaka, humpati mtu hapa…ndoa haivunjiki …hata wafanye nini..’akasema
kwa kujiamini kabisa.
‘Ndio ni mkataba…ulishatamka kama ukifanya hili na lile basi ndoa
haipo, hukutamka kwenye kile kikao, mbele ya wakili, au hilo umelisahau,…hujazaa
nje,…au hilo utalikana, utamkana mtoto wako, huo sio ushahidi yote haya
yameandikwa waziwazi, hata ukisema ni mimi nimeubuni huo mkataba, lakini kauli
zako je…mume wangu tuliza kichwa, kuwa mkweli, ongea ukweli tuyamalize haya…’nikasema
‘Hahaha..mke wangu, tatizo wewe hujui kuwa mimi nina mambo yako
mengi tu, mimi sitaki kusema sana maana wewe ni mkwe wangu nitakulinda wewe na
familia yangu…hilo nimeahidi…’akasema
Mara baba akaingia, yeye alishatonga nje akiwa anaongea na simu,
na alipotuona tunazozana na mume wangu akasema;
‘Jamani kuna tatizo lolote...?’ akauliza mwenyekiti
‘Hakuna tatizo tunaongea tu na mke wangu...’akasema mume wangu
huku akijaribu kukunjua uso wake.
‘Mimi, nimesema huu ni muda wa mapumziko, tutakutana baada ya nusu
saa, mimi natoka, nimeitwa na ofisa upelelezi kituoni , nitarudi, kabla ya muda
huo wa kikao, nikirudi nataka tuyamalize haya yote leo, nataka haki itendeke,
na kashfa iliyotuama kwenye familia yangu isafishike, kwa amani, na vinginevyo,
mimi sitakuwa na lawama tena....’akasema mwenyekiti
Na pale muume wangu akamwangalia baba mkwe wake kwa mashaka, na
kusema;
‘Unaona, baba yako anakwenda wapi,....ndio zenu hizo, anakwenda
kuwaweka sawa hao watu wake, ..kama mlivyowaweka sawa watu wa kusajili
mikataba, lakini hayo hayanitishi mimi…’akasema kwa sauti ndoto ili baba
asisikie.
‘Eti baba unasema unakwenda kituoni ni kuhusu shemeji, au kuna
nini huko kuonana na mtu wa usalama ..?’ nikauliza
‘Ni kuhusu kesi ya mauaji ya Makabrasha kuna mambo wameyagundulikana
zaidi na ni muhimu nifike nionane nao mimi mwenyewe kuhusu pia kutoroka kwa
huyu mtu, maana mimi ndiye nilimdhamini, ..ni muhimu..’akasema mwenyekiti
‘Ina maana mdogo wa mume wangu wamempata..?’ nikauliza
‘Sijui, nitalifahamu huko mbele, ila walitaka kuja kumkamata na
mume wako, wanahisi anahusika na kutoroka kwake..’akasema
‘Kwanini mimi nihusike…?’ akauliza mume wangu.
‘Kuna kitu umemtuma akakifanye, au …?’akasema mwenyekiti na mume
wangu akabakia kimia, na mwenyekiti akaondoka zake.
Haya tutaona tukirudi
mapumziko kama kikao kitaendelea.
WAZO LA LEO: Kuna
matendo tunayotenda kila siku hasa kwa wanandoa, matendo ambayo kiimani,
kimila, na kiutaratibu yanakuwa moja kwa moja yameshavunja miiko ya ndoa,…tunavunja
mikataba ya yale tuliyokubalina siku ya kufunga harusi,, hata kabla hautajoa
kauli zetu.
Kila kitu kina makubaliano na masharti yake, ndoa ina masharti na
makubaliano yake, ndio maana ikaitwa ndoa. Je tunafahamu nini maana ya ndoa! Je
kama ndoa ni kuhalalisha mahusiano mema kati ya wawili hao, iweje mtu amsaliti
mwenzake kwa siri. Mtu anayeisaliti ndoa yake ni sawa na yule mtu
anayeacha nyama yake safi nyumbani na kwenda kula nyuma iliyooza
maporini, huyo keshavunja ndoa yake kivitendo,...Tuweni makini na ndoa
zetu.
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment