Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Tuesday, January 30, 2018

MKUKI KWA NGURUWE-70


Nilifika sehemu ambayo huwa tunafanyia vikao vyetu, ni kazini kwangu , lakini kuna sehemu maalumu imejengwa kwa ajili ya vikao, na siku hiyo sehemu hiyo ilipangwa mahsusi, kwa ajili ya hicho kikao cha familia yangu.

Nilipofika kwenye chumba cha mkutano nilimkuta baba keshafika, yeye alifika mapema tu baadae akafika mama,  baba ni mtu anayejali sana muda.

Nilipofika tu nilimkuta akipitia makabrasha yake, na lapotop yake ikiwa pembeni, akionyesha kuwa anakwenda na wakati,  na mar simu yake ikawa inaita, hapo akawa na wakati huo alikuwa anataka kuongea na mimi.

‘Tafadhali bint, karibu, ngoja niongee na hii simu…’akasema na mimi nikawa nimekaa kwenye kiti nikisubiria amalize kuongea na simu,…alipomaliza tu, akaanza kunilaumu akisema;

‘Nilitarajia watu watafika kwa muda, lakini naona dakika tano zimepita, siwaoni watu, ..’akaanza kulalamika

‘Foleni na hulka zetu baba, lakini nina uhakika wote watafika, ambao ni muhimu kwa kikao hiki,....’nikasema

‘Sawa  hebu kaa kwenye kiti tuanze kuongea yetu, ya baba na binti yake, wewe mama unaweza kukaa kimia kwanza, usiingilie….’akasema

‘Sawa mimi siunaniona sina maana kwako…’akalalamika mama

‘Hapana unakaribishwa nilikuwa natania tu…’akasema baba

‘Umafanikiwa ulichokwenda kununua…?’ baba akamuuliza mama kwanza

‘Ndio…japokuwa sio vyote,…’akasema mama

Mama alisema alipitia kumfanyia manunuzi binti yake, nguo na vifaa, vya safari ya huyo bint.

‘Ni binti  gani huyo?’ nikamuuliza.

‘Utamuona tu , na yeye atakuwepo kwenye kikao, ....’akasema na sikutaka kumuuliza zaidi, kuhusu huyo bint.

Nilipotulia kwenye kiti, baba akaniangalia kwa makini kama ananisoma kwenye ubongo wangu, halafu akasema;

‘Nilitaka kufahamu maamuzi yako, nataka nijue ni nini msimamo wako baada ya haya yote, nataka nikushauri kama baba yako, kama mzazi wako, japokuwa mimi na mama yako tumeshaongea na kufikia uamuzi wetu, ambao sio tofauti na ule wa awali, kwa nia njema tu lakini yote inategemea nyie wenyewe,....’akasema

‘Baba maamuzi yangu yatatolewa mbele ya wahusika, ninawahitajia wenyewe waje wathibitishe waliyoyafanya, ninataka kusikia kauli zao kwanza, je wamesimamia wapi, kwenye ukweli au kuficha ukweli..’nikasema

‘Sio rahisi mtu kukubali kosa kwanza, hasa akijua madhara yake..’akasema baba

‘Sasa kwa vile watakuwepo, ngoja tuwasikie kwanza , yote yaliyotokea tutayamaliza kwa amani na salama, kutegemeana na wao wenyewe,  vinginevyo, kama ndivyo walivyo, na watang’ang’ania kuwa waongo, basi baba mimi nitanawa mikono..’nikasema

‘Hebu niambie wewe ulishafikia wapi, maana uliniambia kuwa unafanya uchunguzi, na utakuja kutoa maamuzi yako mbele ya kikao, ..nataka kuona mtoto wangu anaongea kama mimi, au zaidi ya mimi, unanielewa, nataka niione kazi yangu kwako, kama huwezi uniambie, nitajua ni nini cha kufanya...’akasema

‘Hivi baba hujaniamini, baada ya yote hayo niliyoyafanya, baba mimi sio mtoto tena, ni mtu mzima nafahamu ni nini ninachokifanya, nimeweza kuisimamia kampuni yangu bia kutetereka, na ikawa kubwa, kama unavvyoiona, nimetulia kidogo baada ya matatizo na mume wangu, lakini kuna msaidizi wangu ambaye anaifanya hiyo kazi vizuri tu, japokuwa sasa naona mume wangu kaamua kuingilia kati, lakini ni kwa muda tu, baada ya hiki kikao nitarejea tena kwenye ulingo wangu..’nikasema

‘Binti yangu, sio kwamba nakushusha chini katika utendaji wako wa kazi, hapana, kiukweli unajitahidi sana, hata mimi najisifia mbele ya wenzangu, lakini hili lililotokea, ....mmh, limekushusa, haya yaliyotokea kati yako na mumeo wako, imeharibu kila kitu. Unafahamu kupanda juu, kunachukua muda, akini kushuka, ni mara moja tu...’akarudisha kichwa na kuegemea kiti, haafu akasema;


‘Baba mimi sijashindwa kabisa kuiongoza familia yangu, na unapozungumza hivyo, unasahahu kuwa mimi ni mke wa mtu, ambaye nina mipaka yangu, ...lakini hata hivyo, sio kwamba nimeshindwa kuiongoza familia yangu kama mke...nimejitahidi kufanya yale ya mpaka wangu, kwa kadri ya uwezo wangu, yaliyotokea yamekuwa changamoto kwangu..na sizani kwamba nitafanya hayo makosa tena,..kamwe, baba niamini, ....’nikasema

‘Binti yangu, Usije ukaharibu, .mimi hilo sitakubali, kwasababu tabia ya kizalia haina dawa, hayo waliyokufanyia ni mwanzo tu, ujue chini kwa chini kuna dhambi za damu ya mtu, unafikiri hiyo damu itafukiwa kwa mchanga tu hivi hivi, hata kama tutayamaliza kienyeji, lakini sio sahihi, kuna mtu kauwawa, hakuna haki iliyotendeka, hata kama alikuwa na madhambi yake, watu wanasema aheri kafa, lakini ni wapi sheria ilisema auliwe hivyo,hilo uliangalie kwa makini..’akasema

‘Baba mimi naomba unipe nafasi hiyo, kama nitakuwa nimekosea mtanisahihisha, lakini nina imani kila mmoja atajihukumu mwenyewe muda ukifika, uwongo na hadaa una mwisho wake, ...wewe subiria, tu, tusichukue maamuzi kabla wenyewe hawajajitetea tukaona ukweli upo wapi..’nikasema.

‘Na muda mfupi uliopita nilikuwa nawasiliana na mkuu wa upelelezi wa kituo chenu, na yule aliyefuatilia kesi ya mauaji ya Makabrasha, wameniambia mengi ambayo wameyagundua wao kama wao,…’akasema na kabla hajaendelea watu wakaanza kuingie, ikabidi tukatize mazungumzo;




**********

‘Hivi mama huyo bint yupo wapi…?’ nikamuuliza mama

‘Ataingia tu usiwe na wasiwasi, hatutaki watu wamuone sana, na iwe ni maswali mengi, ataingia kwa muda muafaka akihitajika, baba yako kasema kuna muda atamuita, lakini sio kwasasa ..’akasema mama

‘Ni muhimu kulifahamu hilo, maana hayupo kwenye orodha ya wajumbe wanaohitajika kuwepo, kikao hiki kipo kisheria…’nikasema

‘Usijali, mimi nimemuita kama mwenyekiti…nitamlinda, na kumdhamini,…’akasema baba.

Muda wote tuliokuwa tukiongea mawakili walikuwa upande mwingine wakiongea yao , hawakutaka kuingia mambo ya kifamilia hasa pale tulipokuwa tunaongea na baba, lakini kwa hivi sasa wakasogea karibu, kwenye meza kubwa

‘Nyie mawakili wetu mtakaa kimia, ila mkihitajika kuongea au kuelezea jambo, tutawafahamisha, au sio, haya ni mazungumzo ya kifamilia zaidi, lakini kuna muda mtahitajika…’akasema baba, na mimi nikakubaliana na hilo.


Tulitaka kuanza kikao, lakini kuna wajumbe muhimu walikuwa bado hawajafika na wao ni muhimu sana, kikao kisingeliweza kuendeshwa bila kuwepo kwao, nikataka kupiga simu , lakin kabla sijafanya hivyo mara wakaanza kuingia wajumbe wengine.

Aliyefika sasa hivi alikuwa rafiki wa mume wangu akiwa na mkewe, na baadaye akaingia mume wangu, alipofika kwanza akajibaragua kidogo, kama ujuavyo, waliokuwepo hapo ni wazazi wangu tu, ni wakwe zake, kwahiyo alionyesha ile adabu ya ukwe, akawasalimia na baadaye akaja kukaa karibu yangu,

‘Samahani sana nimechelewa najua mimi ndiye mwenyeji, lakini kuna mambo yalinitinga,…’akasema

‘Hamna shida…’akasema mzee

‘Ni lazime niwajibike, hata mkataba wetu unasema hivyo…’akasema akijitutumua, na mimi nikamuelewa anaelekea wapi.

‘Mkataba upi unaouzungumzia hayo, wa zamani au mpya?’ nikamuuliza kumchokoza huku nikitabasamu, hapo akasita na baadaye akasema;

‘Hakuna mkataba mpya na wa zamani, hiyo kauli yako tu mke wangu usiwachanganye wajumbe...’akasema na hapo nikajua hajafahamu kuwa nimeshaupata ule mkataba wetu wa asili.

‘Tutaona..muda ukifika hilo litasahihishwa, ...fungua kikao, au nifungue mimi maana ndiye niliyekiitisha,…?’nikasema na kuuliza

‘Hapana, tunafuata mkataba wetu, nataka kikao hiki kitambue kuwa kuna mkataba wetu wa kifamilia…’akasema

Mume wangu kwanza akamuangalia baba, akainama kiheshima na kufungua kikao kwa kumkaribisha mwenyekiti wa kikao, ambaye ni baba, kikawaida kwenye familia yetu, kukiwepo kikao kama hicho mwenyekiti ni baba.

Baba kwanza alianza kufungua makabrasha yake, na kabla hajasema neno, mlango ukagongwa, na kwa vile wote tulijua kuwa tumekamilika, hatukutarajia mtu mwingine mpya, kujitokeza tena, kwahiyo hiyo hali ikatufanya, sote tugeuke na kuangalia mlangoni, kuona ni nani huyo anayetaka kuingia

***********,

Mara akatokea mtu akiwa kavaa kofia la waendesha pikipiki, akasimama pale mlangoni akisita kuingia…

Huyu mtu, alikuwa kavalia jaketi la kuzuia upepo mwilini, na kumfanya aonekane bonge, alisimama pale mlangoni kofia likiwa bado kichwani, inaonekana hakutaka kulivua huko nje, labda kwa vile aliona keshachelewa, kama ni mjumbe wa kikao hiki, ambaye mimi sikuwa na habari na yeye,au alifanya hivyo kwasababu zake nyingine.

Kila mmoja ndani ya kikao alimwangalia yeye, na yeye alipoona watu wote wanamtizama, akafanya mambo mawili kwa haraka,  kwanza akainama, kama vile anasalimia au kutoa heshima na pili, akageuka kuangalia mlangoni, kuhakikisha kuwa amefunga mlango,  akalivua lile kofia lake na kuvua koti , halafu taratibu akageukia watu, na kusema;

‘Samahani sana wakubwa zangu, na baba na mama pale..mimi nimechelewa, nilikuwa naweka mambo yangu sawa, maana kiukweli...jamaa wananifuatilia kila kona...’ akasema huku akiangalia pale alipokaa mwenyekiti, lakini alikuwa hamuangalii moja kwa moja usoni, na mwenyekiti akasema;

‘Huyu mtu amefuata nini kwenye hiki kikao...?’ mwenyekiti akaniuliza mimi na kabla sijamjibu akamgeukia huyo mtu na kusema;

‘Kikao hiki hakikuhusu, hiki ni kikao cha watu maalumu, sizani kama wewe ni mmoja wa waalikwa…sina uhakika na hilo, ‘ akasema sasa akikagua majina ya wajumbe..,

‘Mhh, sioni jina lako hapa…kama unavyoona hawa ni wanafamilia, na watu maalumu...walioalikwa..’akasema mwenyekiti.

‘Lakini mimi nimealikwa pia....’akajitetea huyo mtu akigeuka kuniangalia mimi.

‘Ni nani aliyekualika, majina yote ninayo hapa, sijaona jina lako,..., kwanza wewe unatafutwa na polisi, kweli si kweli…?’ akauliza

‘Ni kweli…lakini…’akasema lakini kabla hajajitetea, mwenyekiti akaendelea kuongea

‘Na kwhiyo ukionakena hapa tutaambiwa kuwa tunamficha muhalifu,  tafadhali, ondoka, usituharibie mipangilio yetu, sisi sio wavunja sheria, kumficha muhalifu ni kuvunja sheria za nchi, unalifahamu hilo...’akasema baba, na mimi nikaona niingilie kati nakusema;

‘Baba , oh mwenyekiti, mimi ndiye niliyemualika huyu mtu, nilimualika wakati nimeshakupa hayo majina ya wajumbe, kwani sikuwa na uhakika naye, kwa vile alikuwa haonekani, lakini ni mmoja wa watu muhimu kwenye hiki kikao..’nikasema

‘Binti, hilo haliwezekani, huyu ni mshukiwa wa uhalifu, anatafutwa na polis, mbona unafanya mambo yasikubalika…’akasema mwenyewekiti

‘Baba uwepo wake ni muhimu sana kwenye hiki kikao, ili aweze kutoa ushahidi, kutokana na mambo tutakayoyaongelea leo hii hapa, hatuwezi kumkosa mtu kama huyu, na nilikuwa naombea sana awepo...’nikasema na mume wangu akadakia na kusema;

‘Unasema anakuja kutoa ushahidi…!!’ akasema sasa akimuangalia mdogo wake kwa mashaka

‘Ndio…’nikasema

‘Ushahidi gani atautoa mdogo wangu, kwanza niulize kwa kauli yako hiyo , kwani hapa kuna kesi ya nani, sijaelewa hapo mke wangu, ninani kashitakiwa, eeh..anyway, vyovyote iwavyo, lakini kitu kinachomuhusu mdogo wangu nilitakiwa mimi nikifahamu kwanza..’akasema akikunja uso, kuonyesha kukerekwa.

‘Utayafahamu yote hayo baadaye, kikao hiki nimekiitisha mimi, kuna mambo mengi ambayo yatajitokeza ndani y afamilia, ambayo yanaweza kuvunja usalama na umoja wa kifamilia,.., na yeye anayafahamu zaidi yako, kwa vile wewe ulikuwa mgonjwa,....’nikasema

‘Sio kweli,… mdogo wangu hawezi kufahamu jambo, mimi nisiwe nalifahamu, mimi na yeye muda wote nikiwa mgonjwa tulikuwa tunawasiliana, je kuna kitu gani anakifahamu mimi nisikijue…?’ akauliza
‘Subiria sasa kikao kipo kwa ajili ya hili na mengine..’nikasema

‘Hapana…wewe una nia mbaya na mdogo wangu, mdogo wangu kwanini, wewe hujui umejileta kwenye mtego,…’akasema akimuangalia mdogo wake, halafu akaniangalia mimi na kusema

‘Hivi kwanini mke wangu unataka kumuingiza mdogo wangu kwenye matatizo, ni kwa vile sio damu yako, au sio.. huyu ni mdogo wangu, mimi ndiye mwenye dhamana naye, ...kama alivyosema mwenyekiti ni bora mdogo wangu uondoke hapa hahusiki kwenye hiki kikao..’akasema

‘Kwanini aondoke unaogopa nini wewe, una mashaka gani…?’ nikauliza

‘Sio swala la kuogopa, ni swala la usalama wake, mimi nafahamu, polis wakimuona hapa watakimbilia kumkamata, kabla hatujaweka mambo sawa, wao hawajafahamu ukweli ulivyo..’akasema ndugu mtu akionyesha wasiwasi.

‘Hilo nimelifanyia kazi, wewe subiria kwanza…’nikasema

‘Hakuna swala la kusubiria haoa,..nafahamu lengo lako, ni ili mdogo wangu ajitokeze polis wamkamate, ndio hivyo tu…mimi naomba aondoke tu, nitaongea naye baada ya kikao, kwanini kila mara unapenda kumuingiza mdogo wangu kwenye matatizo......’akasema mume wangu.

Muda wote huo mwenyekiti alikaa kimia, akiandika mambo yake ni kama vile hajali hayo yanayoendelea.

‘Asiondoke, hiki kikao nimekiitisha mimi, na huyu ni mmoja wapo wa shahid wyangu muhimu sana na ajenda zote za kikao ninazo hapa kama katibu, na kwa bahati mbaya sikuwawagaia ajenda za kikao hiki mapema, kwasababu maalumu..’nikasema

‘Najua wewe hujali hilo…’akasema

‘Sio kweli …, mimi sijawahi kumuingiza mdogo wako kwenye matatizo, ni wewe ndiye uliyemuingiza ndugu yako kwenye matatizo, kama tutakavyokuja kuona huko mbele… hayo yote tutayabainisha kwenye hiki kikao, na ndipo itajulikana wazi ni nani anayemjali mdogo wako..mimi au wewe…’nikasema

‘Unasema nini, mimi ndiye niliyemuingiza mdogo wangu kwenye matatizo gani, usilete hoja za kuharibu hiki kikao, kama hakinifai mimi nitaondoka zangu…’akasema sasa akiniangali a kwa mashaka

‘Huyu ni mmoja wa wajumbe muhimu kwenye hiki kikao, na kuwepo kwake hapa ni kwa ajili ya kusema ukweli, ulitokana na wewe, yeye hawezi kuondoka mpaka huo ukweli uthibitishe, na ukweli ukiwa bayana, kama ni mtu wa kwenda polisi atakwenda tu...’nikasema

‘Hapana hawezi kwenda polisi, labda mimi niende huko kama lengo lako ndio hilo, hilo halitaweza kutokea nikiwemo hapa, na kwa hili nitachukua jukumu la kumuondoa, kwani mimi ndiye mwenye mamlaka ya familia na ndugu zangu, hata mkataba wetu,wa kifamilia, unaliongelea hilo ....’akasema na kuushika mkataba mkononi, utafikiri ndio mtetezi wake.

 Hapo sasa mwenyekiti akaingilia kati na kusema;  ‘Hebu tusikilizane kwanza… mimi ndiye mwenye mamlaka ya hiki kikao, au sio..kwahiyo mimi ndiye nitasikilizwa…’akasema na sisi tukatulia,

‘Kwanza , mimi kama mwenyekiti sijakubaliana na kuwepo kwa huyu mtu hapa, kwani anatafutwa na polisi, mnafahamu kuwepo kwake hapa ni kuvunja sheria za nchi, na mimi ni mmojawapo wa watu wanaosimamia hilo bungeni…,na mimi sio mvunjaji wa sheria, kama mwenyekiti ninaamuru huyu mtu atoke kwenye hiki kikao...’akasema mwenyekiti.

‘Hata mimi nakuunga mkono mwenyekiti, sawa kabisa...’akasema mume wangu.

‘Mwenyekiti, naomba huyu mtu awepo, na kama ni swala la uvunjifu wa sheria, hilo tutakuja kuliona hapa, kuwepo kwake, hapa kutasaidia kuyaweka haya mambo yote sawa, na huenda tukaisaidia hata hiyo polisi kwa hayo wanayoyatafuta..’nikasema na baba akaniangalia kwa makini, na akageuka kumwangalia huyo mtu,

‘Mimi bado sijaafiki kwasababu muda uliopita niliongea na mkuu wa upelelezi wa eneo lenu nikamkatalia kabisa kuwa huyu mtu sijawahi kumuona, na nikimuona moja kwa moja nitamfikisha kwao, au nitawaita waje wamchukue, na sasa hivi napiga simu waje wamchukue...’akasema

‘Usifanye hivyo baba tafadhali, huyu ni mdogo wangu, na mimi ndiye nabeba dhamana naye, kama polisi wanamuhitaji kwanza waje kuonana na mimi,...mdogo wangu hana hatia, kama wanavyodai wao, wanamuhisi tu..mimi ndiye niliyesababisha aonekane hivyo...’akasema.

‘Umekumbuka hayo eeh…’nikasema na hapo akatikisa kichwa kama kuchanganyikiwa halafu akasema, akiniangalia mimi kwa hasira

‘Wewe ndiye uliyesababisha yote haya hdi mdogo wangu kushukiwa uhalafu ambao hajawahi kuufanya,..basi polisi wakija utawaambai hivyo, lakini kuwepo kwake hapa ni ukiukwaji wa sheria....’akasema baba.

‘Baba usijali tuendelee na kikao, mwenyewe utakuja kuona umuhimu wake, kama nilivyokuambia, niamini, nisingemuita hapa kama asingelikuwa ni mtu muhimu sana kwenye hiki kikao, je hutaki kujua jinsi gani vitu vyangu vilipotea, hutaki huo ushahidi uwe bayana ...’nikasema na baba akasema;

‘Sawa mimi naendelea na kikao, lakini msimamo wangu ni huo huo, huyu mtu atoke nje, mimi kama mwenyekiti wa kikao sikumruhusu awemo kwenye hiki kikao...na kwa vile nimemuona, nitawapigia polisi waje wamchukue..siwezi kwenda kinyume na sheria...’akasema

Mdogo mtu akawa bado kasimama akishindwa kuondoka, na mwenyekiti akasema;

‘Kwanza mume wako kasema kuwa nyie katika familia yenu mna katiba, na Katiba hiyo ndiyo inayowaongoza,..naona katika ajenda zako katibu, hilo swala la katiba umeliweka kuwa la kwanza, na mume wako keshalianza, naona tuanze na hicho kipengele, tusipoteze muda…’akasema sasa akindika kitu kwenye simu yake.

‘Sawa lakini….’akasema mume wangu na kabla hajamaliza mwenyekiti akaendelea kuongea kwa kusema;

‘Hebu niambieni kwanini mliamua kuanzisha katiba kama hiyo, hata mimi mwenyewe sina kitu kama hicho, labda itatusaidia na sisi …? Akauliza mwenyekiti, na mume wangu akasema;

‘Nafahamu kuwa swali hilo limemlenga mke wangu,kwa vile ndiye mwenye hiki kikao, na ndiye alitakiwa ataje ajenda zake, na bahati mbaya , kikao kimeanza juu kwa juu, kutokana na hili lilitokea, ...ni kweli ndugu mwenyekiti, katika familia yangu, nikiwa na maana mimi na mke wangu na watoto, tuna katiba yetu inayotuongoza....’akatulia kidogo akiishika ile katiba.

‘Kwanini tuliamau kuwa na katiba, ….kiukweli ni wazo la mke wangu , hata mimi nikalipenda sana….kwanza tulitaka familia yetu iongozwe kitaalamu zaidi, ...’ akageuka kuniangalia mimi

‘Lakini sababu kubwa ya kimsingi ni kuwa tulijiona kuwa tuna mambo mengi, mimi nikiwa nashughulika kwenye kampuni yangu, na mke wangu kwenye kampuni yake,lakini vyote hivyo ni vyetu, japokuwa kitaalamu kutokana na hisa kila mmoja alikuwa na mamlaka na kampuni yake...’akatulia

‘Kwa vyovyote iwavyo, mnapo-oana, hata kama mke alikuwa na vitu vyake, kampuni yake, mali yake, lakini akishakuwa mke wa mtu, basi kila kitu chake kinakuwa kwenye mikono ya mume kama kiongozi wa familia au sio....na hili tumelibainisha kwenye katiba yetu, ili kuondoa migongano, tukaona jambo nzuri ni kuwa na katiba....’akasema akitaka kufungua hiyo katiba.

Mwenyekiti akasema;

‘Mhh, usifungue hiyo katiba kwanza, nilichotaka mimi ni kufahamu ni kwanini mliamua kuanzisha hiyo katiba, na kwa ufupi tumeelewa hilo...swali langu la pili, je katiba hiyo imesajiliwa kisheria au ni katiba yenu tu kwa ajili ya mambo yenu ya ndani?’ akauliza

‘Sisi baba, eeh,  ndugu mwenyekiti, kila kitu tumekipeleka kitaalamu, katiba yetu hii imesajiliwa, na aliyeiandika ni mwanasheria, kwahiyo katiba yetu ni kisheria, imetimiza matwakwa yote ya kisheria, ..hatuna matatizo na hilo....’akasema

‘Kwahiyo unataka kusema kila kitu chenu, taratibu zenu za kila siku mlidhamiria ikiwezekana, kifuate taratibu kama mlivyoanisha kwenye katiba yenu hiyo…, na likitokea tatizo, mnahukumiana kutokana na katiba yenu hiyo au sio?’ akaulizwa

‘Ndio mwenyekiti, ndio maana nashangaa kikao hiki, kuitishwa na mke wangu, nilitakiwa mimi ndiye nikiitishe, lakini kuna dharura kama hizo, siwezi kuktaa, au sio mke wangu…’akasema akinigeukia na mimi nikabakia kimia tu

‘Kama ikitokea dharura,basi mmojawapo anaweza kuitisha kikao, lakini ilitakiwa mimi niambiwe kila kitu kwanza…, kwanini kikao kiwepo, lakini mmh, kwa bahati mbaya kwa hili, silaumu, lakini halikufuata utaratibu...nimeshitukiziwa tu, kuwa kuna kikao, cha nini na kwanini, sijaambiwa, huo ni ukiukwaji wa katiba, ila tuliache tu hivyo, tupo pamoja...’akasema

‘Sawa kama imeshtukizwa tu ni makosa, na katibu wako atawajibika kuelezea ni kwanini…’akasema akiniangalia mimi, na mimi nikatikisa kichwa kukubaliana na hilo,…Na mume wangu akadakia kwa kusema;

‘Ndugu mwenyekiti naomba niongee kidogo kuhusu hii katiba, samahani sana, kwani mimi ndio mwenye mamlaka, na kiongozi wa familia yangu, na kwahiyo nina mamlaka ya kuona kila kitu kinaenda sawa...na hilo lipo kwenye katiba…’akasema na mwenyekiti akageuka kuniangalia, mimi nikamuashiria amuache mume wangu aendelee

 ‘Watu wanapofunga ndoa, wanakuwa na taratibu zao, kama mke na mume, na wanakuwa wameshajitoa kwenye mamlaka ya baba na mama zao, hawalindwi au kuchungwa tena na familia za baba na mama zao, kikeni au kiumeni, wao ni watu huru, na wanakuwa na utaratibu wao kama familia inayojitegemea,  au sio …’akasema kama anauliza

‘Na  ndivyo tulivyofanya sisi, na kwa ajili ya kurahisisha mambo yetu tukaona tuwe na katiba, ni wachache sana wanakuwa na utaratibu kama huo, ni tendo la ajabu lakini sis imetusaidia sana, ningeshauri kila familia iwe nayo....’akasema mume wangu.

‘Hii katiba imesajiliwa kisheria, kwasababu imeandikwa na mwanasheri a wa familia, yetu, na sote tukaweka sahihi zetu, mimi na mke wangu, na wakili wetu. Sio katiba ya mitaani , ni Katiba iliyokubalika kisheria, ukiangalia hapa ina kila sifa zote za kisheria, ...mimi kama kiongozi wa familia kwa kupitia hii katiba ninaweza kumshitaki yoyote atakayeingilia au kuingilia mambo yetu ya ndani....’akasema.

Aliposema hivyo akamuangalia mwenyekiti na mwenyekiti akawa naye kamkazia macho, halafu akageuka kuniangalia mimi….

‘Kwahiyo itakuwa ni ajabu kama mtu atakuja na kuingilia familia yangu,wakati yeye ana familia yake, ni ajabu kabisa, labda kuwe na jambo, na jambo hilo liwe wazi kwa kiongozi wa familia ambaye ni mume wa familia, au sio, huo ndio utaratibu, na ndivyo ilivyo kwenye hii katiba .....’akasema na mwenyekiti kwanza akatabasamu, maana aliona hizo shutuma zinaelekezwa kwake, akauliza

‘Hiyo Katiba yenu iliandikwa lini?’ akauliza mwenyekiti

‘Muda mrefu sana, kipindi wakati watoto wetu ni wachanga tu…, imeshafanya  kazi zaidi ya miaka tisa, au sio mke wangu, kwahiyo sio kitu kigeni ndani ya familia yangu...’akasema

‘Naomba niione hiyo katiba..’akasema mwenyekiti, na mume wangu akasimama huku akiwa kashika ile katiba na kwa madaha, akaelekea pale alipokaa mwenyekiti kumkabidhi hiyo katiba, na wakati huo shemeji yangu alikuwa bado kasimama, alikuwa hajafahamu kuwa akae au aondoke, na mimi nikamuonyeshea ishara kuwa akae kwenye kiti. Na mwenyekiti akamuona , na haraka mwenyekiti akasema;

‘Mimi sijakuruhusu ukae, mimi bado sijakukubalia na uwepo wako kwenye hiki kikao, kama mwenyekiti siwezi kukaa kwenye kikao kinachovunja sheria, nimeshasema huyu mtu anatafutwa na polisi, kuwepo kwake hapa ni uvunjifu wa sheria....’akasema mwenyekiti sasa akiangalia kitu kwenye simu yake, na mimi nikasema;

‘Mwenyekiti nakuomba uniamini, huyu mtu ni mtu muhimu sana kwenye hiki kikao nakuomba umruhusu awepo, na kama ni uvunjifu wa sheria mimi nitalijibu hilo, ...’nikasema.

‘Mimi nakubaliana na mwenyekiti, ndugu yangu huyu atoke nje, kwanini  mke wangu unamkaidi mwenyekiti, unaona ilivyo vigumu kwenye familia yangu, silaumu lakini hili halikubaliki, kiongozi ni kiongozi lazima aheshimiwe bila kujali ni nani, sasa na mimi ni kaka yake nipo hapa, nitawakilisha mawazo yake, kwanini ung’an’ganie awepo apa, au unataka polisi waje wamkamate...’akasema na kuongeza kusema;

‘Nina maana muhimu sana, …na ni muhimu sana kuwepo hapa, najua ni kwanini hutaki awepo hapa…’nikasema

‘Mke wangu umekuwa ukimuandama sana mdogo wangu, sijui kwanini,kama kuna lolote dhidi yangu niambie mimi mwenyewe…, na sio kumtumia mdogo wangu kinyemela,mimi sipendi, kama kaka yake ninaamuru atoke kwenye hiki kikao, mimi nitawakilisha mawazo yake kama kuna umuhimu huo, ni kwa usalama wake kwa sasa, mengine aniachie mimi ...’akasema mume wangu.

‘Hata mimi sioni umuhimu wake hapa, maana anatafutwa na polisi akionekana hapa itaonekana kuwa tunamficha sisi, au ngoja tulimalize hili, ngoja ofiswa wa upelelezi aje amchukue,...’baba akasema huku akinua simu yake kumpigia huyo mtu wa usalama

‘Baba tafadhali utaharibu kila kitu, nilishakuomba kuwa unipe nafasi nifanye nionavyo mimi ni sawa… , kama utamuita huyo ofisa wa polisi utaharibu kila kitu, naomba tafadhali endelea na kikao chako, muda utafika , utaona ni kwanini nimeamua awepo hapa kwenye kikao hiki...’nikasema,

‘Wewe unataka tufanye kikao kisicho fuata taratibu, unanielewa sheria za nchi zilivyo, unaelewa mamlaka niliyo nayo..unataka wapinzani wangu wapate cha kuongea..’mwenyekiti akasema;

Mdogo wa mume wangu, alipoona malumbano dhidi yake yanapamba moto, akaona aingilie kati  mwenyewe, akasema;

 ‘Tafadhali mzee wetu, na wajumbe wote wa kikao hiki,mimi naomba mnipe muda, niongee kilichonileta hapa, na baadaye kama unaona nimevunja sheria, basi utampigia huyo mtu wa usalama, aje anichukue, mimi siogopi kukamatwa kwa hivi sasa, ..kwa vile nimeshathibitisha kile nilichokuwa nikikichunguza, na kumgundua muuaji wa Makabrasha,...

‘Nini…wewe unasema nini, acha kuongea haya hapa,…utaharibu!!’ ayetamka hivyo na hata kusimama alikuwa mume wangu.

‘Mimi kuja kwangu hapa,ni kusema ukweli…’akasema na kiukweli hapo kila mtu akabakia kimia, kumsikiliza yeye hasa hapo aliposema keshampata muuaji wa Makabrasha.

‘Pamoja na mengine, nafahamu kuwa askari polis wananitafuta mimi kuthibitisha kuwa kweli kaka ndiye muuaji,..’akasema

‘Hapana sio kweli…kaka yangu sio muuaji..’akasema

‘Mimi sijaua…ni uwongo wao tu..’akasema mume wangu

‘Ndio hivyo kaka,..ndio maana mimi nataka nilithibitishe hilo mbele ya hiki kikao, kuwa wewe hujamuua Makabrasha…’aliposema hivyo, kaka mtu akakaa kwenye kiti sasa akipumua kidogo.

‘Lengo langu hadi kufika hii leo hapa, ni kumtetea kaka yangu, kwani kuna mipango ilipangwa dhidi yake, yeye hafahamu tu…, kuwa kuna watu walioshirikiana kumuua Makabrasha, na kwa vile wanataka wasikamatwe, wameona kosa hilo wambambikie yeye, kaka yangu, bila ya hata yeye kufahamu, ...’akasema na kaka yake akabakia kuduwaa,

‘Mimi nina ushaidi kuwa kaka hajamuua Makabrasha, na wala hajui ni kitu gani kilitokea siku ile, yeye kwanza alikuwa mgonjwa, na pili, aliyemuua, alikuja bila ya kaka kufahamu kinachoendelea,  alitokea kwa nyuma wakati yeye kaka akiongea na marehemu na huyo mtu alikimbia..kwahiyo kaka hafahamu lolote kuhus huyo mtu, na kwanini  ilitokea hivyo..’akasema na kaka mtu akataka kumzuia mdogo wake asiendelee kuongea.

‘Inatosha, usiseme kilakitu,…’akasema kaka mtu

‘Kaka nakuomba utulie , nataka kuongea haya kwa masilahi yako, na masilahi ya wote waliohusika, kwasababu nimeona huk o tunapokwenda ni kubaya kuliko mnavyofikiria nyie…, na hayo yaliyopangwa dhidi yako, au yenu, yatakutia matatani kaka, yataharibu familia yako, na kashfa itasambazwa kila mahali..’akasema na kaka yake akamsogelea na kumshika mkono na kusema;

‘Mdogo wangu hayo sio ya kuongea hapa, tutakuja kuyaongea tukiwa wawili, wewe toka nje ya kikao,...’akasema huku akimshika mdogo wake mkono, ili watoke naye nje...mwenyekiti alipooa hivyo akasema;

‘Naomba mtulie mimi ndiye mwenyekiti wa kikao, nimeshamfahamisha mkuu wa upelelezi, amesema tuendelee na kikao, lakini kikao kikisha, huyu mtu tunatakiwa tumkabidhi kwake, kwahiyo kuanzia sasa upo mikononi mwa polisi mimi siwezi kuvunja sheria kwa ajili ya kumfurahisha mtu yoyote, hata akiwa mwanangu,mimi nafuata sheria na taratibu zilikubalika ....’akasema

‘Kwahiyo mimi sihitajiki tena kusema ukweli ambao nilitarajia kuusema?’ akauliza shemeji yangu.

‘Ukitaka kuusema sawa, sasa hivi upo huru kusema, maana wenyewe wameshatambua kuwa upo hapa, na ukweli gani ulio nao ambao ni tofauti na ukweli ninaoufahamu mimi, hayo unayotaka kuyasema , na jinsi ulivyoelezea hapo, ni mbinu tu ya kuficha ukweli halisi…ni jinsi nyingine ya kumtetea kaka yako kiujanja unjana, na mimi sikubaliani na hilo....maana ushahidi wote ninao hapa...’akasema baba.

 ‘Baba labda tufuate utaratibu wa kikao chetu, wewe endelea na kikao, ukifika muda wake wa kuongea ataongea, na ukweli utajionyesha, labda tuanze na ajenda zetu kama zilivyojipanga, kama tulivyoanza awali, tulikuwa tukiongelea kuhusu katiba,,...au sio mwenyekiti…’nikasema.

‘Utaratibu kama huu siutaki, mnasikia, … sawa tuendelee  na kikao, na kijana upo chini ya ulinzi, kuanzia sasa, ...’akasema mwenyekiti kwa hasira.

Kikao kikaendelea kwa namna hiyo…Karibuni kikaoni..

WAZO LA LEO: Taratibu na sheria zilizowekwa zina umuhimu wake kwenye jamii husika,  na jamii hiyo inatakiwa kuzifuata hizi sheria na taratibu zilikubalika, ili kuzuia uvunjufu wa amani. Watu wakianza kutafuta uchochoro wa kuzikweka sheria hizo kwa visingizio mbali mbali, malengo na dhamira ya kweli hupotea, na matokea yake ni fujo … Sheria au taratibu zinatakiwe ziwe kwa masilahi ya jamii, na sio kwa ajili ya kuwakandamiza wanyonge.


Ni mimi: emu-three

No comments :