Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Monday, January 29, 2018

MKUKI KWA NGURUWE-69


 Niifuata maelekezo kama walivyotaka wao, walichokuwa wakifanya ni kuniamuru, kwa kunielekeza kuwa nielekee wapi, nikate kushoto au kulia, hadi tukafika maeneo yasiyokuwa na umeme, eneo hilo ilikuwa na majengo mapya mapya, na nikaambiwa nisimamisha gari.

‘Simamisha gari..’nikaamriwa

Nikafanya kama walivyoniamurisha na nilipotaka kugeuka kuwaangalia ni akina nani, maana nilishahisi kuwa wapo wawili, kiyoo cha kuangalia nyuma walikuwa wameshakigeuza kwa juu ili nisiweze kuwaona kwa nyuma.

Wakati nataka kugeuza kichwa, mkono wenye kitambaa ukapitishwa puani kwangu na aliyefanya hivyo, akanishika shingoni kama mtu anayenikaba, na mwenzake akasema;

‘Mbona unamkaba, hukusikia bosi alivyosema, bosi alisema tusimdhuru sehemu yoyote, atajua mwenyewe ni nini cha kufanya tukimfikisha..’akasema mwenzake

Niliposikia hivyo mawazo yakanipeleka mbali kuwa huenda ni yale yale niliyotaka kumfanyia rafiki yangu, ndio yamenigeukia mimi, sikuweza kujitetea maana kile kitambaa walichoniwekea puani, kilinivunja nguvu zote, viungo vyote vikalegea, japokuwa kwa mbali  niliweza kusikia wanachokiongea.

‘Sasa ningewezeje kumweka hii dawa...kwanza haijaingia vyema huoni bado yupo macho...’akasema na wakanishikisha kile kitambaa puani, na nilipoivuta pumzi, nikahisi nikizama kwenye giza, sikujitambua tena.

Sijui ilipita muda gani, lakini nahisi ni karibu ya saa moja au nyuma kidogo, ..nilihisi kitu kikipita puani, na hapo nikapiga chafya mfulululizo, hadi nikashikwa na kikohozi, na hapo hapo nikawa kama mtu aliyekuwa kwenye ndoto ya majinamizi, napaigana kushindana na hiyo hali, lakini viungo havina nguvu, nikawa kwenye hiyo na hali na baadae nikaanza kurejewa na fahamu.

Ikapita muda, na taratibu akili yangu ikaanza kunirejea kama mtu anayetoka usingizini, bado wakati huo mwili mzima ulikuwa umelegea, nikajaribu kuinua mkono, mkono ulikuwa kama haupo kwenye mwili wangu mara nikasikia sauti kwa mbali;

‘Bosi anasema kila kipo tayari,..ngoja azindukane tu…’sauti ikasema

Nikajitikisa kidogo, kujaribu mkono kama unaweza kuinuka…

‘Naona kama keshaanza kuzindukana....mnaweza kumrejesha kwenye gari lake, lakini hakikisheni, anazindukana kabisa ndio muondoke, mlindeni asije akaumizwa na watu wengine, tukaja kupata lawama, kazi tuliyomuhitajia imekamilika, kila kitu chake kirudisheni kama kilivyokuwa....’sauti ikasema

‘Bosi ina maana tumuache hivi hivi tu....’nikasikia sauti ikisema

‘Wewe ulitaka kumfanya nini, acha na tama mbaya, hapa ni kazi tu, kama tulivyoagizwa, kazi yetu ni kufuata maagizo, tunachohitajia sisi ni pesa si vinginevyo, hatutafuti mengine, hayo unayoyataka wewe sio utaratibu wetu, na ole wenu mumuguse, huyo ni hatari kuliko ,mnavyofikiria, ...’sauti ikasema

‘Kama ni hatari huko mbele akizindukana itakuwaje...?’ akauliza mmojawapo

‘Ndio maana nawataka mumurudishe kwenye gari lake, na hakikisha mnamkalisha kwenye kiti chake aonekane kalala kwenye gari lake, akizindukana, atajijua mwenyewe, sisi kazi tumeshamaliza, tunakwenda kuchukua mshiko wetu, ...’ sauti ikasema

‘Sawa bosi…’sauti nyingine ikasema

‘Na muhimu hakikisheni kuwa yupo salama, na mkiona kuwa kazindukana, poteeni mbali kabisa, ukibakia hapo yatakayokupata sisi hatupo, na hakuna kutajana hapa, kila mtu afe kivyake,…nawaambia tena, ukishikwa ukafunua mdomo wako, utakuwa mgeni wa mchwa..’sauti ikasema

‘Sawa bosi tumekuelewa...’nikahisi mmoja akisema wakanibeba, na mmoja akawa anasema kichichini.

‘Huu mwili, laini, laini hivi, tutaishia kuubeba tu...hawa watu hawana akili kweli, ...’akasema

‘Unajua wewe utakufa kwa ukimwi, wewe unapenda mambo hayo sana, kama umelaaniwa nayo, mwili tu unakusumbua,..tunachokitafuta hapa  ni pesa, tufanye kazi yetu tulipwe, ..ukishapata pesa, watu kama hawa utawapata wengi, ....’sauti nyingine ikasema.

‘Sawa bwana,...pesa yenyewe , shilingi ngapi kwanza, ...aheri ile ya wenzetu, wabakaji, wanaopewa kazi ya kudhalilisha wanawake,..wanaifanya hivyo na bado wanalipwa...’akasema.

‘Kubaka nako kazi, ..ile sio kazi ya kufanya, ni hatari tupu, na umewasikia wenzako, kilichowatokea,...sasa hivi wanatafutwa na polisi, safari hii wameshindwa, nasikia wamepewa kazi, kabla hawajaifanya wakafumwa, ngoja wafukuzwe na polisi,karibu wakamatwe..nilikutana na yule jirani yako, akikimbia utafikiri yupo kwenye mbio za dunia, na akaniomba nauli, anataka kupotea hapa jijini.’mmoja akasema

‘Kwani na nani na kwanani?’ mmoja akauliza

‘Nasikia ni kwa binti mmoja , aliyetoka ulaya hivi karibuni…’akasema

‘Sasa huyo ana kosa gani , maana nasikiwa wakijiita kundi la kurekebisha tabia..’akasema

‘Anajua huyo aliyewatuma kuwa ana kosa gani…’akasema

‘Ikawaje sasa
‘Basi bwana,..walifanya kama kawaida yao, na hizi dawa za kupoteza fahamu, kwanza walipambana, maana huyo binti sio mchezo, kilichowasaidia ni hiyo dawa ya nusu kaputi, walifanikiwa kumnusisha, hapo ndio wakamuweza, wakambeba, sasa walisahau kuwa nyumba hiyo kuna mtu mwingine,alikuwa chumba cha pili, huyo ndiye aliyewaharibia, akawapigia simu polisi..

‘Ehe, ikawaje..?’ akauliza na wakati huo, wameshanifikisha kwenye gari langu , wakawa kwenye harakati za kuniweka kwenye kiti, nilikuwa bado nimelegea lakini akili ilishaanza kufanya kazi,sikutaka kuwashitua ili nisikie ni nini wanakiongea, nikaendelea kufumba macho.

‘Basi bwana kama kawaida yao, maana wanapofanya hiyo shughuli, huku wakirekodi tukio nzima, kwahiyo walipomfikisha huyo binti kwenye kichochoro, walichoona kina usalama, wakaanza kuweka vyombo vyao vya kuchukua hilo tukio, ili wakamuonyeshe tajiri wao, wakati wanajiandaa, wapo tayari, kufanya mambo yao, mara king’ora cha polisi kikasikika, na hawo polisi walifanya hivyo makusudi, maana hawakujua hawa jamaa  wamejificha wapi...’akasema

‘Oh, kwahiyo kazi ikavurugika...wakakamatwa...?’ akauliza mwenzake

‘Wakamatwe wapi, ...tatizo lao waliposikia king’ora cha polisi hakuna aliyemwangalia mwenzake kila mmoja akajua njia yake, wakaacha kila kitu hapo, polisi wakafika na kumuokoa huyo mwanadada...na vitu vyote vikachukuliwa kama ushahidi, na mijamaa hiyo inatafutwa kama alimasi...kwasababu wanajulikana, na huyo dada anawafahamu, ...’akasema

‘Mhh, hapo kazi ipo....’akasema

‘Nafahamu kukamatwa sio rahisi, watakuwa wameshavuka milima na mabonde, hawataonekana hapa hadi mwaka upite, tatizo, hawana pesa, maana kazi hawakufanya, watalipwaje sasa...je wataweza kuvumilia kuishi bila pesa, ...huko walipokwenda labda wakavunje nyumba za watu na kuiba, na hiyo sio fani yao....’sauti ikasema.

‘Mhh, imenitisha, kwahiyo polisi wamecharuka kwa hivi sasa, mmh, hapo sasa mimi naanza kuogopa, tuondoke zetu, kama ni hivyo polisi watakuwa kwenye patroo zao, hebu mwangalie, nimemuona kama anajitingisha, keshaamuka yule, funga mlango wa gari tuondoke zetu bwana...’sauti ikasema

‘Una uhakika..?.’akauliza mwenzake.

‘Nenda wewe ukahakikishe, unasikia ulivyo ambiwa, huyo dada sio mchezo, kwa vyote, ana pesa na pia anazijua ngumi,,...mimi sitaki jela, naondoka zangu...’sauti ikasema na mara baadae  kukawa kimiya

Hapo nilipo nikahisi wameshaondoka, na mimi nikajaribu kuinua mkono, na huku nikijikagua, sikuhisi maumivu sehemu yoyote, nikajinyosha na kukaa vyema, nikafungua viyoo kupata hewa, nikataka kutoka nje ya gari, mara nikaona gari likija mbele yangu.

Mimi nikawasha gari langu, lakini kabla sijaanza kuendesha, gari hilo likiwa limeshafika, walikuwa ni polisi, wakasimamisha gari lao karibu na gari langu, na silaha zao mikononi, mmoja akasogea kwenye gari langu na kugonga kwenye kiyoo, mimi nikashusha kiyoo, akaniangalia kwa makini akaniomba kitambulisho, nikamuonyesha leseni yangu, akaikagua halafu akasema;

‘Madamu huku umefuata nini, kuna tatizo lolote..?’ akauliza

‘Nahisi hakuna tatizo, gari lilinizimikia , lakini naona lipo sawa...’nikasema, na sauti kavu ya kulazimisha ikanitoka, ilikuwa kama sio ya kwangu, nilihitajika kupata kitu cha kulainisha koo, na yule askari aliposikia hiyo sauti akaniangalia na kusema;

‘Unahis ulikuwa kwenye tatizo,…nyie zunguka kila mahali…’akatoa amri.

‘Madam tuambie ukweli maana hizi  sehemu hizi sio nzuri, kuna watu wabaya huku, kuna kesi nyingi za wahuni, wavuta bangi na wabakaji, kama kuna tatizo lolote, tuambie, vinginevyo, ni bora uondoke kabisa eneo hili..’akasema na mimi sikutaka kumsikiliza tena zaidi, nikaondoa gari langu na sasa nikawa na kazi ya kutafuta njia ya kurudi nyumbani.

*************

Ilikuwa ni kama saa sita na nusu hivi za usiku nilipofika nyumbani, na mlinzi wangu alikuwa keshaanza kuingiwa na wasiwasi, aliponiona akanijia na kuanza kuongea kwa haraka haraka;

‘Bosi, nilishaingiwa na wasiwasi, hapa tu nilitaka kuwapigia simu polisi, lakini kwanza nilitaka kuwasiliana na wakubwa zangu wa kazi, sio kawaida yako kutoka usiku, na kuchelewa kurudi kama leo, kuna tatizo lolote bosi?’ akaniuliza

‘Hakuna tatizo..’nikasema na sikutaka kuongea na mtu nikakimbilia ndani, na cha kwanza ni kunywa dawa , ni dawa maalumu za kuvunja nguvu za madawa kama hayo waliyonunusisha puani.

Ninafahamu jinsi gani ya kuyavunja nguvu, na nafahamu ni aina gani ya dawa hizo, nilifanya juhudi ya kuyaondoa hayo madawa kabla sijala kitu, ilikuwa usiku sana kwakweli, na baadaye nikaoga, huku nikijikagua kuhakikisha kuwa nipo salama, na kilichofuata hapo ni kutafuta usingizi, nililala hadi saa tatu, asubuhi.

Niliamushwa na kelele za mlangoni, nikatoka na kukutana na msaidizi wangu wa kazini amfika nyumbani, akasema kapiga simu yangu haipatikani ndio maana akaamua kuja nyumbani…, nikamwambia sijisikii vyema, na akanikumbusha kuwa leo nina kikao cha kukutana na familia yangu, saa nne, nikamwambia kitafanyika kama kilivyopangwa.....

‘Na pia kutoka msajili wa mikataba, alikuwa anataka kuongea na wewe..’akasema

‘Kwanini aongee na mimi , anatakiwa kuongea na wakili wangu au sio…’nikasema

‘Hata mimi nimemwambia hivyo hivyo, lakini akasema ni muhimu angeongea na wewe …kasema atakupigia tena…’akasema

‘Ok akipiga niunganishie kwenye namba yangu nitakayokuwa hewani, kuna jingine …?’ nikauliza
‘Hakuna bosi mengine ni ya kawaida,…matumizi ya ofisi…kanipatia muhasibu, na hundi ya kuweka sahihi..’akasema

‘Ok, nipatie….’akanipa nikapitia kwa haraka, nikaweka sahihi, na mambo ya kiofisi yakaishia hivyo.

*********

Nilijiandaa kutoka, na nilipokuwa tayari nikaenda kuchukua laptop yangu, sehemu nilipoiweka, nikaumbuka sikuirudisha kabatini, ikawa ni kosa, haikuwepo...sikuamini, maana hapo nilipokuwa nimeiweka sio rahisi mtu kuigundua, lakini imeshachukuliwa

‘Ni nani huyu…?’ nikajiuliza na kwa haraka ,...nikajua huenda waliochukua ni hawo watu walionikamata jana...nikatoka na kwenda maktaba,huko niliona kila kitu kipo kama kilivyokuwa japokuwa kuna dalili za kutaka kuvunjwa...

Hawa watakuwa hawo watu wa jana, na kwanini wachukue laptop yangu tu...?’ nikajiuliza, na mara nikakumbuka,.

‘Ina wezekana ni shemeji yangu, huenda alitaka kuhakikisha kuwa sina zile kumbukumbu zake za diary yake, amejidanganya...’nikasema kimoyomoyo

Wakati nataka kuondoka, nilipotoka nje, niliona boksi limewekwa mlangoni, sikulishika kwanza, nikamuita mlinzi, kwani msaidizi wangu wa mambo ya ndani, alikuwa kaelekea sokoni kununua mahitaji ya nyumbani, Mume wangu alishatoka hospitalini, lakini tulikuwa hatukai naye hapo nyumbani, alikuwa akikaa kwenye nyumba yetu nyingine, tulikubaliana iwe hivyo.

‘Hili boksi kaweka nani hapa?’ nikamuuliza mlinzi, akasema yeye hafahamu

‘Hufahamu ina maana huu mzigo umeingia wenyewe humu, kuna mtu kaingiza, wewe hukuwepo getini?’ nikauliza kwa ukali, kiukweli hata mlinzi akiliniangalia kwa mashaka, sina kawaida ya kuongea na wafanyakazi wangu kwa ukali hivyo.

‘Bosi nilikimbia kidogo kujisaidia, nilipokuja , sikuangalia huko , hata hivyo, ...mmh, ndio, niliona mtu akitoka wakati wakati natoka chooni, nikajua ni wafanyakazi wako, ....kwani sio boksi lako bosi,..?’akasema

‘Haya lifungue mwenyewe, kama ni bomu utajua  mwenyewe jinsi gani ya kulitegua...’nikasema na huyo mlinzi akiwa na wasiwasi akalifungua, ...

‘Oh, ni laptop yangu...’nikasema huku nikiitoa, nikaikagua, ilikuwa haina tatizo lolote, nikaingia nayo ndani cha kwanza ilikuwa kuangalia ni ile diary ya shemeji,...kila nilipojaribu kuiifungua inasema haifunguki, haifanyi kazi, na mwisho ikasema haipo kabisa...nikajua kuwa ni huyo shemeji yangu

Kabla sijaifunga hiyo laptop yangu, nikaona ujumbe kwenye komputa ulikuwa umeandikwa kama barua pepe, nikaufungua na kuusoma

Ujumbe;

‘Samahani sana shemeji imenibidi nitumie njia hii, ili kuzipata kumbukumbu zangu, ambazo nyingi ni mambo yangu binafsi, na si vyema watu wengine wakayafahamu, natumai ulifika salama, hakuna lolote lililotokea dhidi yako, na kila kitu chako kipo salama, japokuwa kuna vitu nilishindwa kuvichukua kwenye kabati la kaka, kaka aliniagiza, lakini hakijaharibika kitu, mtamalizana na yeye, ninachokuomba ni kumsaidia kaka, na mimi unisamehe sana kwa kutokukukutimizia yale uliyoyataka....

‘Huna adabu kabisa,unafikiri hilo ulilolifanya litasaidia kitu, tatizo huyu kijana hanielewi mimi, yeye hujui kuwa mimi ni mjanja zaidi yako...’nikasema, nikachukua kidude cha mtandao (moderm), nikaweka mawasiliano, nikaingia kwenye mtandao, nikatafuta kumbukumbu zangu, nikaona ninachokitafuta, nikafungua, nikaiona kumbukumbu  iliyoandikiwa diary ya shemeji, ipo kama ilivyokuwa...nikatabasamu, nikainakili tena kwenye laptop yangu.

Nilipohakikisha kuwa kila kitu kipo sawa, nikampigia simu, rafiki ya mume wangu, ili kuhakikisha kuwa na yeye atakuwepo kwenye kikao, kwani bado alikuwa akihangaika na mke wake,...

‘Vipi upo, maana siku hizi wewe hukai nyumbani kwako, sijui bado unatafuta mtoto wa kiume au..?’nikamuuliza

‘Ni kawaida tu, ...nipo kwenye kikao, na ikao cha familia nitafika pia, na mke wangu keshafika, alifika jana usiku, na amekubali kuwepo kwenye hicho kikao, anasema ana yake ya kuongea, baada ya hapo anarudi huko kijijini alipokuwa, sijamuelewa huyu mwanamke mpaka sasa, nimechoka...’akasema.

‘Vyema kabisa, nimefurahi kusikia hivyo, je uliwahi kuongea naye lolote na akaweza kukuambia chochote.... ?’ nikamuuliza

‘Hataki kuongea lolote, anasema yote atayaweka wazi hapo kwenye kikao, alikuwa anatafuta nafasi kama hiyo, ...nahisi kuna jambo kubwa linamkera, maana hata wazazi wake, wanasema kawa kama mtu aliyepagawa, hana raha,...sijui ana tatizo gani...’akasema

‘Pole zake, ndivyo ilivyo, majuto mara nyingi huja baada ya kitendo, tunapofanya mambo bila kuangalia mbele,mwisho wake unakuwa mgumu, ...natumai atakuwa mkweli, na ukweli wake ndio utakaoweza kumsaidia, sio vinginevyo...’nikasema.

‘Mhh,..kwanini unasema hivyo nahisi wewe kuna jambo unalifahamu kumuhusu yeye, na ameamua kuwa msiri sana, na hilo ndilo litakalomuangamiza, ni jambo gani hilo jamani..?’akasema na kuuliza

‘Kila jambo lina mwisho wake, nina uhakika yote yatajulikana kwenye kikao, ujiandae kwa lolote lile, na mimi siwezi kukuambia chochote, yote yataanikwa kwenye hicho kikao...’nikasema.

‘Kwanini lakini, hamjui mnavyonitesa?’ akaniuliza

‘Wewe ulijifanya unafahamu yangu mengi tiu…, mbona hukuniambia, hukujua jinsi gani nilivyokuwa nateseka,..sasa ni zamu yako, lakini usijali, yote yatajulikana kikaoni, natumai wote watafika, wasiwasi wangu ni kuwa shemeji yangu anaweza asifike, na yeye ni mtu muhimu sana....’nikasema

‘Kwani kaenda wapi, maana hata mimi namtafuta kwenye simu hapatikani..?’akaniuliza

‘Unamtafuta wa nini..au ndio kupanga njama za kuharibu ushahidi, safari hakiharibiki kitu,…’nikasema

‘Kijana amekuwa mtoto wa mjini, anayoyafanya anayafahamu yeye mwenyewe, na hata mke wake analalamika sana,..na zaidi hata kaka yake ananipigia simu mimi kuniuliza wapi alipo mdogo wake…’akasema

‘Waongo hao…jana tu walikuwa pamoja, walichokifanya mungu mwenyewe anajua, lakini ama zao, ama zangu…’nikasema

‘Mhh, haya bwana, lakini namlaumu sana mume wako, yeye ndio anamuharibu mdogo wake, ...nasikitika sana, kwani juhudi zangu zote zimekuwa hazina manufaa, kwa huyo mdogo wetu...’akasema.

‘Je mie niliyemgharamia masomo na kila kitu, hadi kuoa, nitasemaje…ni kweli shutuma zote ni kwa kaka yake, mimi sizani kama nitakuja kumsamehe…’nikasema.

‘Unajua sema ni kwa vile mambo yangu yamekuwa mengi nimeshindwa kuyafuatilia maisha yao, na yenu kwa ujumla,mnisamehe sana, hata wazazi wako nimewaambia hivyo, mambo yemeniwia mengi sana, ila kwenye kikao nitajitahidi niwepo tu, japokuwa …sijui..nitakuwepo, ngoja niweke mambo yangu sawa....’akasema.

‘Ni muhimu sana uwepo, kama mkeo yupo, basi hatima ya yote haya itajulikana kwenye hicho kikao, na wasiwasi wangu ni kuwa baada ya hicho kikao huenda kusiwe na urafiki tena, lakini sio kitu, bora nusu shari kuliko shari kamili ....’nikasema

‘Kwanini kusiwepo na urafiki, mimi nilijua ni kikao cha usuluhishi?’ akauliza

‘Kwasababu ukweli ni mzuri sana, lakini unauma, na utahukumu yanayostahiki kuhukumiwa, ili haki itendeke,...’nikasema.

‘Sawa hamna shida, mimi sina tatizo,...kama kuna ukweli ninaoufahamu nitausema, kama utasaidia, ...’akasema.

‘Na hasa uwe wa kumsaidia mke wako, ...’nikasema.

‘Yah, mke wangu na wewe pia,....nikuambe ukweli, hapa nilipo nakuwaza wewe, namuomba sana mungu, itokee miujuza, ile hali ya zamani irejee,sina raha kabisa, najuta kwanini haya yametokea, inafikia hatua natamani ndoa yangu ifike mwisho tu, ili nijue moja...’akasema.

‘Nini…ndivyo unavyoombea ili iweje sasa, muhimu ni wewe na mwenzako, ...kila mtu ana shida zake, hilo nilowahi kukuambia kuwa usione mimi napata taabu na mume wangu, wapo watu wanapata shida sana na ndoa zao, sio mchezo, lakini mwisho wa yote ni nyie wenyewe, kila mmoja anatakiwa kuwa na maamuzi yake, unasikia, kila mtu aubebe mzigo wake yeye mwenyewe..’nikasema.

‘Haya nakuja , ngoja nimpitie mke wangu, ,....’akasema

‘Sawa na mimi ndio naondoka nyumbani hivyo, uwe makini na mkeo..’nikasema

‘Na wewe pia…’akasema

Nikaanza safari ya kuelekea kikaoni na wakati nipo njiani nikahisi kuna pikipiki, ilionekana ikinifuata kwa karibu sana, sikusimamisha gari hadi ninafika, na yule mtu mwenye pikipiki, akanipita, na kunipungia mkono, sikujua ni nani, kwani alikuwa kavaa helimeti ...mimi nikafika kwenye eneo tulilopangia kufanya kikao.

Wazazi wangu na mawakili walikuwa wameshafika…,



WAZO LA LEO: Migogoro mingi huishia pabaya, wengine husihia hata kupigana, au kukosana kabisa, ni kwanini tukimbilie vita, kukosana, na hata kutalikiana, kwanini kwanza tusikae tukaongea tukatafuta chanzo cha tatizo ni nini, huenda ni shetani, tu, huenda ni wenzenu wanataka muharibikiwe tu…mzungumzo ya heri, ya kujadili tatizo yana tija zaidi ya uhasama wenyewe.
Ni mimi: emu-three

No comments :