Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Tuesday, December 5, 2017

MKUKI KWA NGURUWE-34


‘Hayo sasa tutakuja kuyaongea  akifika muhusika, ambaye ataweka kila kitu sawa….unajua mke wangu nataka kila kitu sasa kiwe kwa namna ambayo, hakuna mtu ataumia,..nafanya haya kama mume wa familia….

‘….Je ni kweli una mtoto nje…na ni nani huyo…?’ ,

  Wakati anataka kujibu swali hilo mara…wakaingia madocta na nyuma yao, akaingia mtu, mtu ambaye alinifanya nipandwe na hasira, ..

Ni nani huyu…

Tuendelee na kisa chetu…

**************
Ungeliniona nilivyokuwa nimeshikwa na butwaa ndio ungelifahamu haya ninayokuambia hivi sasa…, maana akili yangu ilishahamanika, niliposikia mume wangu kama vile anataka kukubali au kukataa kuwa ana mtoto nje ya ndoa, na huo ndio ungelikuwa ni shahidi wangu mkubwa, ama kwa heri au kwa shari..

Kiukweli hadi muda huo nilishaamua moja, kama ni kweli hayo wanayoyazungumza watu basi mkataba ungelifanya kazi yake,..ama kama ni uwongo, kuna mambo mengi yangelinifanya nianza kukosana na marafiki zangu kuwa wao wanataka kuivunja ndoa yangui…ila nilichohitajia kwangu kikubwa ni ‘ushahidi..’

Kauli ya mume wangu ingelikuwa ni ushahidi tosha, wa kumaliza matatizo haya yote kichwani mwangu,angekuwa mkweli, huenda ningeliumia, lakini mwisho yangelifikia muafaka, lakini kwanini hataki kuniambia ukweli, hapa nabakia na swali kubwa kichwani,  je ni kweli mume wangu kafanya hivyo, ina maana alisahau huo mkataba, na sikuwezi kupata jibu hilo, maana mbele yangu kulitokea tatizo jingine…

Mawazo yangu yalikatishwa na huyo jamaa, aliyeingia, kumuona yeye tu, nilijua kuna tatizo, na tatizo hilo sio dogo,…hapo akili ilishtuka, na kuharibu mawazo yote niliyokuwa nayo kichwani…!

Cha ajabu hata baada ya wale wengine kuingia ndani, wao waliingia na moja kwa moja wakaja pale tulipo kwa mgonjwa, ambapo mimi nilikuwa nimesimama karibu naye, lakini huyo jamaa yeye baada ya kuingia alipiga hatua moja , mbili, halafu akasimama karibu na mlango, na mbali kabisa kutoka pale tulipokuwepo sisi, hakusogea ..


Nilibakia nimeduwaa, nikimkodolea macho huyo jamaa, kiukweli sikutatarajia kumuona huyu mtu tena katika maisha yangu…baada ya tukio lililotokea huko nyuma baina yangu mimi na yeye,..na nakumbuka kwa mara ya mwisho nilipokutana naye, hatukuachana vizuri kabisa, nikakumbuka kauli yangu kwake;

‘Sitaki kuja kuonana na wewe tena, …sikutaki kabisa na ukumbuke hili, siku nikija kukutana na wewe tena, nitahakikisha nakufungulia mashitaka ya utapeli, na uwongo, na nitahakikisha, unakwenda ndani, na ukitoka jela, hutajishughulisha tena na utapeli wako huo….’nikamuambia hivyo kwa hasira.

‘Na pia nakutahadharisha,..mimi nitakuwa nakufuatilia, hatua kwa hatua,…mimi nakuonya uwe mbali kabisa na mume wangu..unanisikia wewe tapeli…’nilizidi kumpa onyo na kwa muda huo hakuwa na cha kusema, bali ni kukaa kimia tu.

‘Kama nikikuona upo karibu na mume wangu, nitahakikisha ninakumaliza kwa mikono yangu mimi mwenyewe…na nitaanika mabaya yako yote hadharani….’nilimwambia…kiukweli nilikuwa nimeshamfahamu alivyo na jinsi anavyofanya kazi zake, na ushahidi wote nilikuwa nao…

‘Samahani sana..ni makosa yalitokea, sitarudia tena….’alijitetea hivyo

‘Sina haja ya samahani yako, ondoka mbele yangu…’nilimuambia hivyo tukiwa ofisini kwangu na alitoka haraka na sikuweza kuonana naye tena, mpaka siku hii ya leo.

Jamaa aliendelea kusimama pale, hakusogea hata hatua moja kuingia ndani, sasa sikufahamu ni sababu ya kuniogopa, au alikuja kwa malengo yake binafsi.

Kama kawaida yake, alikuwa kavalia mawani meusi machoni, akificha unafiki wake, mkononi akiwa kashikilia mkoba wake mweusi, mkoba ambao umekuwa kama sehemu ya mkono wake, maana popote utakapokutana naye, huo mkoba upo mkononi, sijui ndani yake kuna nini!


Kwa muda ule mimi nilikuwa nimeshikwa na butwaa, mwili ukinicheza cheza kwa hasira, mdomoni nikitaka kutamka jambo au kupiga ukelele wa hasira…, lakini sikuweza kufanya hivyo , nikiheshimu mamlaka ya hapo, kuwa hapo ni hospitalini.

Lakini pia sikuweza kufanya jambo, nikichelea matatizo ya mume wangu…kiukweli isingelikuwa hayo mambo mawili, ungelisikia mengine, nahisi ningelipiga ukele, au kwenda kumvaa huyo jamaa kwa hasira,  lakini kwa muda huo na sehemu kaam hiyo, ilibidi ninywee tu, na kuumia na hasira zangu moyoni

Baadaye  nikageuka kumwangalia mume wangu nisikie anasema nini,...kwani kwa muda huo alishamalizana kusalimiana na walioingia humo ndani kasoro huyo jamaa.

Mume wangu aliponitupia jicho, akaiona hiyo hali usoni mwangu, nilishabadilika, hasira zote zilikuwa usoni mwangu, alitarajia kuwa ningelifanya jambo, la kumvaa huyo jamaa au kuongea kwa hasira, lakini hilo halikutokea, alishangaa kuniona nimesimama tu, siongei neno, ila uso wangu ulionyesha kila kitu…

Mume wangu akasema;

‘Mke wangu samahani sana, nafahamu hupendi kabisa kumuona huyo mtu..na nafahamu ni kutokana na yale yaliyotokea kipindi kile..na hayo yaliharibu sifa zake..lakini hukutaka kuyafuatilia zaidi kuwa yeye hakuwa na kosa, kama ni kosa basi labda ungelinilaumu mimi, unanielewa hapo, lakini hukutaka hata kunisikiliza…’akasema kumtetea huyo jamaa.

‘Mimi namfahamu sana rafiki yangu huyu,…ndio kuna wakati mwingine anafanya mambo-mambo, lakini sio kwa kupenda yeye, wakati mwingine ni kutokana na mteja wake anavyotaka yeye…anajulia namna za kuweza kumsaidia mteja wake,…’akatulia

‘kwa hali kama hiyo, yeye yupo tayari kuingia kwenye hatari, ili kukidhi matakwa ya mteja wake…na wakati mwingine anahatarisha taaluma yake, lengi ni kusaidiana, anatufahamu maisha yetu sisi watu wa kawaida, na anafahamu maisha ya watu wliopo kwenye dhiki..au kukwama kwa namna hii au ile, maana sisi wanadamu tuna madhaifu yetu…’akaendelea kuongea lakini mimi hayakuniingia akilini.

‘Kwa namna hiyo na nyingine wale maadui zake, na wasipomtakia mema, wamefikia kumharibia jina lake…, lakini afanyeje kama mteja wake anataka hivyo, na kama mtu kaja kumlilia hali, mtu kama huyu anatusaidia sana sisi watu tuliokwama, ni vyema tukamfahamu hivyo, japokuwa upande wa pili watamsakama sana…’akatulia

‘Sisemi haya kuwa wewe ulitaka kufanya mabaya, kwa kupitia kwake, hapana, ila kwa taarifa alizozipata,…’akataka kuendelea mimi nikaonyesha mkono wa kukataa hayo maelezo yake nikasema

‘Please,..bsi basi inatosha,…mimi sitaki tena kusikia  hayo maelezo ya huyo mtu, mimi namfahamu vilivyo,..hakuna mtu anayeweza kunidanganya lolote, sijafanya makosa …namafahamu..kwahiyo sijui kaja hapa kufanya nini..’nikasema

‘Mke wangu ..najua wewe hurudi nyuma, unamuamini sana rafiki yako, au sio…lakini nikuambie kitu,….lakini hayo tuyaache kwanza, maana hayo yalishapita au sio..’akasema na kutulia kidogo

‘Hata hivyo kutokana na hayo yaliyotokea…eeh, yanaweza kuwa ni sababu, kwani huko yanapoendea, kunaweza kukazuka sintofahamu eeh..nashindwa kuelezea kiuwazi zaidi..kisheria, si unajua membo mengine yapo kwenye mkataba, yanahitajia sheria, na..na..ndio maana, nimeona huyu mtu aje kunisaidia, …, yeye, ni rafiki yangu wa siku nyingi, namuamini sana kuwa atanisaidia kwa hilo…’akatulia

‘Kukusaidia, kwani una kosa gani mume wangu…..?’ nikamuuliza sasa kwa hasira , na hapo mume wangu akaonekana kunywea, lakini kwa haraka akajirekebisha kuonyesha nafasi yake akasema;

‘Ndio hivyo, makosa yap ndio maana nikakuomba msamaha,..au sio, lakini haya yatasemwa baadae kwa muda muafaka, ngoja nimalizane na huyo mtu…yeye nimemuita ili aweze kulisaidia hili…’akamuangalia jamaa

‘Huyu jamaa namuaminia…, yeye anajulia sana mambo ya mikataba hasa ya kifamilia kama hii ya kwetu ya kienyeji enyeji, iliyotengenezwa kimtego mtego…na pia ya kikazi, na anaweza kufahamu madhaifu ya mikataba hiyo na lipi lifanyike ili kuirekebisha, bila kuleta matatizo makubwa, anajua njia zote kwa jins tunavyotaka sisi umenielewa hapo…’akasema

‘Kwanini unataka kufanya hivyo..?’ nikamuuliza

‘Kama nlivyoanza kukuambia awali, mke wangu..nielewe..sitaki tuongee sana kabla sijaweka haya mambo vizuri, lakini ni hivi.., huo mkataba wa kimtego,…una mapungufu mengi, na ..ukifika kwa baba yako, kashapata panga la kukata mti..na huo mti ni nani, sio mimi kweli..ndio hivyo, sasa nikimalizana na huyu jamaa, nitakuja kuakuambia kila kitu,... ila kwa hali ilivyo inabidi kujihami, sipendi kazi zetu zote zionekane hazina maana, …na mume nipo, ni aibu jamani...ni lazima sasa nishike hatamu…’akasema akitikisa kichwa kama kukubali.

‘Mume wangu unajua unajizalilisha wewe mwenyewe, mambo ya ndani unamtafuta wakili wa kazi gani, umeua..umafanya kosa gani kubwa kihivyo…’nikasema

‘Hapana, ..sijaua..lakini aheri uneliua, ikajulikana moja,…nafahamu kabisa mbele ya baba yako, naweza kuonekana kama muuaji tu….nitazalilika, …na, nitakimbilia kujiua…si umeona hapo…ila mke wangu haya ni mambo ya kawaida tu,..utakuja kunielewa, wala usipate shida, niachie mimi, nitayaweka sawa, mwenyewe utakuja kuona…’akasema

‘Sitakuelewa kamwe,…na kwanini unafanya hivyo, kwa hali uliyo nayo, kwanini hujionei huruma, na kama wewe hujijali, kwanini usiwajali wanaokuhangaikia, eeh, hili …mume wangu…hapana, hapa kiukweli umevuka mipaka…’akasema

‘Mke wangu, niamini, …si unaniamini,..sasa endelea kufanya hivyo, utaona manufaa yake, mengine nitakuja kukuambia nyumbani,..huyu mtu sivyo kama unavyomfikiria wewe, na kutokana na hali zetu kuwa sio nzuri kibiashara, yeye kajitolea kwa gharama ndogo tu, na haya tutayayamaliza haya mambo kwa haraka iwezekanavyo...’akasema mume wangu.

‘Mimi, sikuelewi na sitakuelewa, na sipo kabisa na mambo yako, samahani kama nitakukwaza, ila kwa huyu mtu, sipo tayari kushirikiana naye kwa lolote lile,…’nikasema huku nikimuangalia docta rafiki ambaye kwa muda huo naye alikuwa kama kachanganyikiwa.

 Wakati huo docta yule aliyekuwa akimshughulia mgonjwa alishaondoka, na alisema atarudi baadae kutuambia cha kufanya kama nikuondoka na mgonjwa, au bado anahitajika kuendelea na matatibabu.

‘Mke wangu…usiwe na wasiwasi kabisa…haya nitayamaliza tu, ngoja docta aje kama ni kuniruhusu haya, kama ni kuendelea kubakia hapa , sawa , lakini kabla ya mimi kuondoka hapa, ni lazima mambo fulani yafanyike ili huyu mtu aondoke ..na kuanza kazi yake…’akasema

Mimi pale nikakaa kimia,…baadae nikageuka kumwangalia docta. Docta rafiki, alikuwa bado kakaa kimia, na sasa akimuangalia rafiki yake kwa makini…, na baadae akaniangalia mimi,..na muda huo ndio na mimi nageuka kumuangalia yeye nikitaka asaidie kwa hili. Macho yakakutana…

***************

 Docta rafiki alipoingoa mara ya kwanza, alichofanya yeye, baada ya kusalimiana na rafiki yake, alijitenga pembeni, ..lakini pembeni mwa kitanda kama kutupatia nafasi, na muda mwingi alikuwa katulia huku kainama chini, kama vile hataki kuingilia mambo yetu, lakini akiwa tayari kutoa msaada ..na kila alipoona napandisha hasira, alikuwa akinitupia jicho,  la kunipa tahadhari…lakini kwa muda huo mimi sikujali tena,.., nikamgeukia mume wangu.


‘Mume wangu huko unapokwenda ni kubaya, nakuomba tena tuyaache haya mambo mpaka upone, tafadhali, usije ukafanya mimi nikaja kuonekana mbaya…’nikasema

‘Wala usijali mke wangu hakuna baya litatokea,…uwe huru tu..lakini hili lazima lifanyike…’akasema

‘Hili lipi….weka wazi….na sijui kwanini mume wangu unayafanya haya yote..ina maana una kosa gani kubwa mpaka unadhamiria kuyafanya haya yote, wakili, wakili wa nini…sijakuelewa bado…?’ nikamuuliza

‘Wakili ndio…ila kwa sasa usiwe na papara, utakuja kujua kila kitu…nimeshakuambia dhamira yangu kuwa ni lazima apatikane mtu wa kuyaweka haya mambo sawa, ya ndoa, mali na kadhalika, kuna mkataba au sio, je upo sawa..sasa nilazima nimpate mtu sahihi wa kunishauri…na nimeonelea mtu wa ngu sahihi huyo jamaa…’akasema

Nilitaka kugeuka kumuangalia huyo jamaa, lakini hata kichwa kikasita kufanya hivyo…nikasema;

‘Mume wangu kwani wewe una wasiwasi gani, mimi nipo kwa ajili yako, na kama unahisi kuna tatizo, mimi nitasaidiana na wewe kulimaliza hili au sio,....mimi sioni umuhimu wa kumleta mtu mwingine kwenye mambo yetu ya nyumbani, tulishasema haya ni yetu wawili, sasa huyu mtu ni wa nini…, jaribu kujionea huruma wewe mwenyewe kwanza, ....!’nikasema.

‘Mke wangu usione nayafanya haya kwa kuwa labda nimependa, …hapana nimejikuta sina jinsi, na nikiyaachia, nitakuja kudhalilila…hapana, hapa ilipofikia ni lazima na mimi nifanye jambo…’akasema

‘Ufanye jambo gani,…weka wazi,…na kama kweli kuna tatizio kubwa kihivyo, na mpaka haya yote yanatokea, utuambie ili na sisi tuweze kusaidia,..uliua, hapana, ulifanya nini basi…haya kama ni hivyo, kwanini haya yafanyike hapa hsopitalini,… basi subiria tutoke hapa, tukifika nyumbani tutakuja kuayaongea haya vizuri…’nikasema nikijaribu kujishusha

‘Hapana mke wangu tulishaongea yote na huyu mtu, sasa hivi kaja ili kumalizia hili jambo kwa ujumla wake, …ukitaka unaweza kubakia, kusikiliza kila tutakachoongea, lakini kama hutapendelea, basi, nitakuja kukuambia tulichokubaliana,..lakini vyema na wewe ungelikuwepo,  maana mim nimekuwa mtu wa kuumwa, umwa,..sasa lini litafanyika hili,naona sku zinakwenda, na baba yako anazidi kuwa juu..hulioni hilo, ..ngoja tulimalize hili kabisa leo hii hii,..’akasema


‘Mimi sikubaliani na hilo kabisa, unasikia, wewe kwa vile umeamua kwa masilahi yako, wewe endelea na huyo mu wako, na mimi usinihusishe kwenye makubaliano mtakayofanya na huyo…na nasema hivi kama una nia njema na hayo unayotaka kuyafanya, basi subiria tufike nyumbani kwanza...’nikasema.

‘Mke wangu kwa hatua ilipofikia hatuna jinsi, inabidi tukubaliane na huyu mtu, vinginevyo, mambo yataharibika, nielewe hivyo, na niamini hivyo,mwenyewe utakuja kuona....’akasema

‘Tukubaliane na yeye, una maana gani hapo na ni mambo gani hayo yataharibika…?’ nikamuuliza

‘Ndio nasema utakuja kujua lakini kwa hivi sasa siwezi kukuambia lolote uniamini tu..’akasema

‘Nakuuliza hivi, kwani huyu mtu ndiye anakulazimisha kufanya hivyo, au ni kwa utashi wako wewe mwenyewe, niambie kama kuna kitu nyuma ya pazia, nifanye kazi yangu, huyu mtu mimi hanibabaishi kwa lolote lile, ninamfahamu sana ni mbabaishaji tu, ni tapeli huyo, utakuja kujutia, umeshachelewa…’nikasema
  
‘Mke wangu mimi nakupenda sana, na sitaweza kuachana na wewe, hilo nimeahidi , sio bab yako wala kitu gani kitavunja ndoa yetu,.. nafahamu hata wewe unanipenda pia, au sio…?’ akasema kama kuniuliza, sikumjibi kitu

‘Sasa. kwa ajili ya ndoa yetu, kwa ajili ya maisha yetu na familia yetu, na watoto wetu,...mimi siwezi kukubali mambo mengine yaje kutuingilia,...nafahamu kabisa nikikaa kimiya hilo litatokea, na....sijui itakuwaje kama likitokea...ni nani wa kualaumiwa kama sio mimi,...hapana mimi siwezi kukaa kimia,  ni bora nijitetee mapema,...’akasema na akawa anakunja uso kama anahisi maumivu fulani.

Nikageuka kumuangalia docta, na docta akawa naye anamuangalia mume wangu kwa mashaka...akageuka kuangalia kule wanapokaa madocta, kulikuwa hakuna mtu, halafu akaniangalia mimi...

‘Mke wangu wewe niamini mimi..na sifanyi hili eti kwa shinikizo la mtu, kuwa eti labda huyo jamaa kafanya jambo kunirubuni, hapana hakuna kitu kama hicho, huyo ni rafiki yangu hawezi hata siku moja kunifanyia hivyo, haya yote nayafanya kwa masilahi ya familia, kwa utashi wangu  mimi mwenyewe…’akasema mume wangu.

‘Sizani kama nitakuelewa, na aah, hata sina hamu tena ya kuendelea kukaa hapa, mimi nataka kuondoka, kama ..oh, docta alisema tumsubirie, ok, au..?’ nikasema nikiwa nataka kuondoka, nikamuangalia docta rafiki, naye akawa ananiangalia kwa uso wa kunionya kuwa niwe makini.

‘Mke wangu usiondoke kwanza tafadhali…, maana sizani kama nitaendelea kulazwa hapa, kiukweli hata mimi mwenyewe nataka kuondoka hapa...,ikibidi leo hii….docta kaniambia hali yangu imeshatengamaa, sasa nikae hapa kufanya nini..mambp yangu yanalala,..na ndio maana nimemuita huyu mtu, aanze kunisaidia yale mambo yanayoweza kuleta madhara kwenye familia...’akasema.

 Alipoongea hivyo, nikageuka kumwangalia docta rafiki. Nilimona kainama vile vile, nikamsogelea pale aliposimama, na yeye akainua kichwa taratibu na kuniangalia machoni, huku akiwa nusu kutabasamu na nusu kuonyesha mashaka fulani, lakini bado nilikuwa sijamuelewa, kuwa yupo na mume wangu au yupo na mimi,mimi nikamwambia kwa sauti ya chini chini ili mume wangu asisikie;

‘Hivi huyo mtu mumemchukulia wapi,…?’ nikamuuliza

Docta rafiki akamtupia jicho yule jamaa , huku mimi naendelea kuongea

‘Hivi si nyie mlionionya kuwa hali ya mume wangu haihitajii mambo ya kugandamizwa kimawazo, sasa hamuoni kuwa kwa hali kama hii tunaweza kumuathiri mgonjwa, au kuna jambo jingine mumelipanga mimi silifahamu...?’ nikamuuliza

Docta rafiki,..akatulia kama anawaza jambo, halafu, akageuka kumuangalia mume wangu,…mume wangu alikuwa kainamisha kichwa chini, hatuangalii, ni kama ananiacha niongee na docta, na hakuwa na wasiwasi na hilo

Docta rafiki, akageuka kumwangalia yule jamaa tena pale aliposimama karibu na mlango, alikuwa kasimama pale pale, hajasogea hata hatua moja, na vile vile alivyokuwa kasimama awali ni hivyo hivyo.. docta akawa anauangalia kwa makini, tatizo yule jamaa alikuwa kavalia mawani meusi, kwahiyo huwezi kufahamu ana hisia gani machoni…

Baadae docta akanigeukia na kunitizama machoni, na kwa sauti ndogo akasema;

‘Mimi sijui kabisa ni kitu gani kinachoendelea hata mimi nimebakia kuduwaa, mpaka sasa nawaza kuna kitu gani kinachoendelea...sijui kuna tatizo gani kubwa limetokea kwa rafiki yako mpaka kufikia hatua ya kumuita huyo mtu, kiukweli bado nipo gizani…’akasema

‘Siwezi kuamini hilo…kuwa wewe hujui, rafiki yako hawezi kukuficha, ninajua wewe unalifahamu hili,  mumelipanaga hili, kwa dhumuni fulani, basi niambieni na mimi, ili niufahamu huo ukweli…’nikasema

‘Ina maana huniamini mimi, ..mimi sijui kitu, muulize mume wako, hili ni lake yeye mwenyewe, na …kiukweli, limenishtua na mimi…’akasema docta, na mgonjwa aakinua uso kutuangalia, na docta akasema

‘Tunateta kidogo na mke wako,…samahani lakini…’akasema docta

‘Ongeeni tu , tena ni vizuri,..mshauri afahamu kuwa mimi ni mume wake,..na haya nayafanya kwa ajili ya familia yangu..unajua mimi nataka haya mambo tuyamalize yote leo hii hii, hebu mshauri ili tulimalize hili tatizo..., najua wewe ni rafiki mwema kwetu..’akasema mume wangu.

'Ukisema hivyo unanifanya kama vile nafahamu unachotaka kukifanya....'akasema docta

'Hapana,...simaanishi hivyo, nataka wewe umshauri aakubale yale ninayotaka kuyafanya, kiukweli wewe hujui lolote kuhusu hili, ni mambo ya kifamilia, lakini wewe unaweza kumshauri, akakubaliana na mimi...'akasema

Docta akaniangalia mimi...na mimi nikasema;

‘Nakuapia kama unajua lolote kuhusu hili, mtapambana na mimi….nikitoka hapa naenda kuongea na baba, tuone hatima ya haya mambo itafikia wapi, maana kiukweli nimechoka, nimevumilia na kila hatua inakuwa aheri ya jana, na mimi ni binadamu jamani ….’nikasema

‘Usifanye vitu kwa pupa, najua ukilifikisha kwa baba yako hivi kama lilivyo, utakuwa umeharibu kila kitu,...tafuta ni nini kinachoendelea kwanza, ili uwe na uhakika, je kama mume wako ana kusudia jambo jema,...huwezi jua, na  mwache baba yako afanye kivyake, ipo siku mtakaa meza moja mtayamaliza, nina uhakika na hilo….’akanishauri docta.

‘Kwanini kwanza mkamruhusu huyu mtu kuingia ndani..hapo ndio nasema hata wewe unalifahamu hili, sio vizuri mlivyofanya…’nikasema

‘Nikuambie,…huyu mtu alipofika alisema kaitwa na mume wako…nasikia mapema tu,alimwambia docta kuwa kuna mgeni wake atafika, kwahiyo, akifika aruhusiwe kuingia, kwani yeye ana mazungumzo muhimu na huyo mtu, ambayo yanamsumbua kichwa chake...’akasema rafiki wa mume wangu.

‘Na wewe ukakubali kirahisi hivyo..ulitakiwa kwanza uje uongee na mume wangu, au uniambie mimi ili nikupe ushauri, maana huyo mtu namfahamu sana mimi…hebu niambie tukianza kuzozana hapa, huoni lolote laweza kutokea, maana mimi kiukweli sitakubaliana na haya mambo...’mimi nikasema.

‘Mimi nakushauri uvute subira ufahamu wanachotaka kukifanya,…na mimi nisingeliweza kumzuia huyo mtu, nilijua bado ile hali tete ya mume wako bado ipo na ukizuia jambo analolitaka yeye,..inaweza ikamuathiri mume wako...’akasema

‘Mhh…siamini, …kuna nini lakini…’nikasema

‘Hata huyo jamaa sisi tulimtahadharisha, kuwa hali ya mume wako haitaki mawazo mengi kama kaja na mambo yenye utata, ni bora yasubirie, lakini  alichotuambia sisi wenyewe tulibakia hatuna jinsi…’akasema

‘Kasema nini…?’ nikauliza

‘Kasema hiyo hali aliyo nayo mume wako,  yeye pekee ndiye anayefahamu jinsi gani ya kuimaliza, keshaongea na mume wako na keshajua tatizo lipo wapi, kwahiyo yeye, kaja kumalizia makubaliano, na ana uhakika atayamaliza matatizo yanayomsumbua mume wako, hebu tuambie sisi hapo tungelifanya nini..’akasema rafiki wa mume wangu.

‘Huyo ni tapeli mkubwa, anajua kucheza na hisia za watu, ni kama mchawi fulani hivi..namfahamu sana…nahisi kuna kitu..lakini ngoja tu, nitakigundua, kwa vyovyote vile, na ataishia kubaya..’nikasema

‘’Usichukulie jaziba…’akasema docta,

‘Wewe subiria uone…nitafanya jambo, ananitambua nilivyo, wewe subiria uone…’nikasema na sasa nikasogea pale nilipokuwa awali, na kumuinamia mume wangu…nilimuangalia moja kwa moja usoni, lakini yeye akawa ananikwepa tusiangaliane machoni…kama ananionea aibu, …sikujali, nikamuuliza;

‘Mume wangu nakuomba tena, huyu mtu aondoke hadi hapo hali yako itapokuwa salama, kama kuna lolote niachie mimi, nitaongea naye, nahisi kuna kitu kakufanyia, au kakutisha nacho, huyu mtu ni tapeli, na mimi namjulia, unaisikia.....’nikamwambia kwa sauti ya chini chini, na yeye akasema;

‘Mke wangu, usiwe na wasiwasi,....mimi nimeshaongea na huyu jamaa, na sivyo kama unavyofikiria wewe, nahisi uliyoyasikia kwa watu ndiyo yamekufanya ufikirie hivyo,…sikiliza  yeye kufika kwake hapa ni kwa vile mimi ndiye nimemuita. Na nilishawahi naye kabla…, na leo, kaja tumalizane…yeye kaja kwa nia njema tu, ya kunisaidia..ya kutusaidia ili haya mambo yaishe kwa amani. ..na hatakuwa na muda mrefu,…nakuomba uondoe wasiwasi dhidi yake…’akasema.

Nilikaa kwa muda, nikiyawazia haya, nikainua kichwa kugeuka, kwangalia docta rafiki wa mume wangu, ambaye alikuwa akituangalia tunavyoongea na mume wangu, na aliponiona nipo kimiya,akataka kunisogelea nahisi alitaka kunisihi jambo.

Mimi niliona nisipoteze muda, kwa haraka nikatoka pale na kutembea hadi pale alipokuwa kasimama jamaa…jamaa alikuwa kasimama vile vila hakujali kuwa nakuja mbele yake, hadi nilipofika pale aliposimama. Na niliona kama anataka kusogea nyuma, lakini hakufanya hivyo, akatulia, akisubiria nitafanya nini….

NB: Sehemu nyingine inakuja soon


WAZO LA LEO: Ukiwa na hasira usifanye jambo kwa pupa, hakikisha umetuliza hasira yako kwanza kabla ya kuchukua maamuzi, mara nyingi ndani ya hasira ibilisi hachezi mbali, na hasira inaweza kuwa ni hasara. 
Ni mimi: emu-three

No comments :