Nilipohakikisha kuwa kweli ule mkataba haupo kwenye sehemu yake,
nikamuita mmoja wa wafanyazi wangu wanaofanya usafi na kujaribu kumdadisi kama
aliwahi kumuona mtu mwingine akiingia ofisini kwangu wakati nipo mapumzikoni.
‘Hakuna bosi aliyewahi kuingia bila ya ridhaa yangu…’akasema
‘Lakini kuna mtu aliwahi kuingia, ukiwemo
‘Hakuna bosi…mtu akija namuekeleza kwa msaidizi wako…’akasema,
‘Kwani kuna kitu kimepotea
bosi?’ akauliza kwa mashaka.
‘Bado sijahakikisha, kama kuna kitu kimepotea, ila kama kipo
nitakuambia, na uwe na uhakika ..jaribu kukumbuka vyema kama kuna mtu ulimuona
akiingia humo, au alikuomba ufunguo, ...ndicho ninachotaka kusikia kutoka
kwako, nakuamini sana...? ‘nikauliza
‘Hakuna kabisa mtu aliyeingia humo,,...hilo nina uhakika
nalo...’akasema na kwa vile mimi namwamini sana huyu mfanyakazi wangu sikutaka
kumshinikiza zaidi.
‘Hamna shida,....’nikasema
Niliona hakuna haja ya kuendelea kuuliza uliza watu wengine, na
sikuwa na hamu tena ya kuendelea kufanya kazi kwa siku hiyo, haraka nikaondoka
zangu kurudi nyumbani maana bado nilikuwa likizo.
Wakati nikiwa ndani ya gari, nilijaribu kuwaza, nifanye
nini,...na sikutaka mambo haya ya ndani ya familia yangu yatoke, nje, na mtu
pekee angeweza kunisaidia kwa hili ni rafiki yangu, ambaye hayupo.
‘Lakini nasikia anarudi…’nikajikuta nikisema hivyo
‘Hata hivyo maswala ya mkataba wangu na mume wangu hastahiki
kuhusika kabisazaidi ya wakili wangu..’nikasema.
Hata hivyo sikuwa na shaka sana, maana ipo nakala nyingine
nyumbani , nikifika nitaisoma, ila kiukweli kupotea na nakala hiyo kulipa ni
shida sana, ni nani kaichukua na kwa nini. Akili yangu ilivyo, sikuwa na dalili
yoyote ya kumshuku mtu yoyote, na kila niliyemuwazia, nilijikuta nikimuondoa
kwenye ushukiwa.
Nafasi kubwa ilikuwa kwa mume wangu, lakini alikuwa mgonjwa,...na
kabla hajaumwa, nakumbuka ipo siku niliwahi kuuchukua huo mkataba na kuusoma,
na kuurejesha nilikuwa natafuta mkataba wa kampuni ya mume wangu, nilikuwa na
nakala , na siku mbili baadae ndio akapatwa na hiyo ajali.
‘Haiwezekani akawa ni mume wangu,, yeye ana nakala yake,
Nilijaribu kumuwazia mtu mwingine, lakini sikuweza kumpata, kwani
sikuona umuhimu wake na huo mkataba wetu.
‘Sasa atakuwa ni nani?’ nikajiuliza bila kupata jibu.
Nilifika nyumbani, nikaliendesha gari langu mbele kidogo, kuna
duka langu la vipodozi, na vifaa vingine vya namna hiyo,, nikamwambia mlinzi wa
pale, aniangalizie hilo gari, nitalipitia baadae, nikarudi nyumbani kwa miguu, ni hatua chache, kwani ukuta wa
sehemu hizo za duka zimeshikana na ukuta wa nyumbani kwangu.
Kwa haraka nikaingia ndani, na moja kwa moja nikakimbilia chumbani
kwangu, nikafungua mlango taratibu maana sikutaka kumsumbua mume wangu kwani akiwa
amelala haitakiwi kusumbuliwa.
‘Kwa vile kalala nitafungua kabati na kuchukua huo mkataba,
nikasome huko mbele kwa mbele..’nikasema na huku nikihakikisha kama kweli mume
wangu kalala. Alikuwa kalala, dawa zilikuwa bado zinafanya kazi,...nikageuka na
kuelekea chumba chetu cha maktaba, humo ndipo kwenye kabati, sehemu hiyo
ni kama ofisi yetu ndogo.
Nikajifungua, kuhakikisha kuwa hakuna mtu atakayekuja kunisumbua,
haraka nikaliendea kabati tunapoweka nyaraka za kifamilia, huwa kila mmoja ana
ufungua wa hilo kabati, lakini mimi nilikuwa na sehemu yangu nyingine, ambayo
mume wangu hana ufunguo nalo, ninaweka vitu vyangu vya kike, lakini
nilitengeneza sehemu ya kuhifadhia kumbukumbu zangu binafsi ambavyo .
Nikafungua ile kabati, ...niliona kila kitu kipo kama nilivyokuwa
nimeacha, hapo huwa napatumia mara kwa mara, nikihitajia vitu vyangu ,
nikasogeza vitu vingine na kuinua sehemu ambapo niliweka huo mkataba, ..sikuamini
macho yangu
Kweupe...hakuna kitu...nikashikwa na butwaa, haiwezekani ,
haiwezekani, sasa hili ni tatizo, ...
‘Kwa hali ilivyo, sasa naanza kumuhisi mume wangu, hakuna mwingine
anayeweza kuhangaika na huu mkataba,..huyu atakuwa ni mume wangu tu..’hapo
nikasema kwa sauti
‘Hata hivyo kaupatia wapi ufungua wa hapa, uungua bado ninao
mwenyewe na akiba yake....’nikawaza mwa kwa sauti, nikafunga kama ilivyokuwa na
sikutaka kuchukulia pupa…nilipohakikisha nimefunga kama kawaida nikageuka
kuondoka.
Ni wakati nataka kutoka nikakumbuka kitu, sijui kwanini niliwazia
hivyo, nikarudi sehemu ile tena, nikafungua, upande wa pili yake.., na
kuangalai hicho nilichotaka kukiangalia...nikakuta kipo pale pale...sijui
kwanini nilitaka kufanya hivyo, lakini moyo ulitaka kuhakiki, kuwa silaha yangu
binafsi bado ipo, ..huwa nina kibali cha kumiliki bastola, na tangu niinunue,
ni muda sasa sijawahi kuigusa.
Mwanzoni nilikuwa na tabia ya kwenda kulenga shabaha hata kuwindia,
lakini kutokana na majukumu, nikawa sina muda huo tena. Kwahiyo ni muda
sasa sijaitumia hiyo silaha
‘Hata hivyo silaha ya nini....?’ nikajiuliza, niliikagua na
kuhakikisha ipo salama, baada ya kumaliza kuikagua nikafuta alama za vidole,
kama kawaida yangu,..na kurudisha sehemu yake.nikahakikisha nimefunga kabati
vyema, nikafungua mlango wa hicho chumbani , na kutoka, hapo akili ilikuwa kama
sio yangu, hasira..lakini
Nikaingia chumbani, nikajikuta nashikwa na butwaa, kitanda
kilikuwa kitupu, mume wangu alikuwa hayupo kitandani,…kaamuka muda gani na
kaenda wapi…nikajiuliza kwa haraka nikajua katoka nje.
‘Huyu mume wangu kaamuka saa ngapi?’ nikajiuliza maana
nilihakikisha kuwa alikuwa kalala, kabla sijaenda huko maktaba yetu, na kuamuka
huko ni kama vile huyu mtu alikuwa macho, maana sikukaa muda mrefu pale ndani.
Na mimi kwa haraka nikatoka kule chumbani na kwenda sebuleni,
sehemu ya mapumziko, …lakini kwa kunyata kimia kimia…na pale sebuleni..,
nikamkuta mume wangu kakaa kwenye sofa.Alikuwa hajaniona, na mkononi kashika
kitu.
Taratibu nikamsogelea, hadi nikamkaribia,….nahisi alihisi kuna mtu
nyuma yake, kwani aligeuka,… akaniona, alishituka, mpaka nikaogopa, maana kwa
hali yake, hakutakiwa kushituka kiasi hicho,....
‘Oh, mke wangu umerudi saa ngapi..si ulisema hutarudi mapema?’
akaniuliza huku akiwa ananishangaa, na mkononi alikuwa kashika mkataba.
Ule mkataba wa kifamilia…!!
Kwanza nilijifanya kama hakuna kitu, lakini yeye aligundua kuwa
macho yangu yalikuwa yameangalia ule mkataba aliokuwa nao mkononi, na
nilivyomshitukizia, hakuweza hata kuuficha, akawa kaushika vile vile mkononi,
na mimi nikawa namsogelea kuhakikisha kuwa ni huo mkataba wetu, yeye ana nakala
yake, na mimi ya kwangu, ila mimi kuna alama niliweka kwenye nakala zangu.
‘Nilikuona umelala, wakati naingia na sikutaka kukusumbua, kuna
kitu nimekifuatilia huku nyumbani, na huenda nikarudi tena ofisini, ila na mimi
nashangaa maana muda huu ulitakiwa ulale, kwani hujanywa dawa zako sawa sawa
nini?’ nikamuuliza.
‘Dawa nimekunywa, lakini sasa hivi hata nikinywa, sipati usingizi
kama ule wa mwanzo...’akajitetea.
‘Sawa mimi naona nisikusumbue,,..’nikasema kama vile nataka
kuondoka, lakini nikamsogeela na kuangalia kile alichokuwa kashika mkononi
nikasema;
‘Naona unasoma mkataba vipi tena, unajikumbushia zile enzi zetu za
kuishi kwa kufuata mkataba, hahaha mume wangu bwana, au unaangalia nini, na
peni, kama unasahihisha jambo, kuna nini kimekukwanza mume wangu ...?’
nikamuuliza na yeye akajibaragua kama vile anataka kuuweka chini, kama vile sio
kitu muhumi sana kwake, akasema;
‘Aaah unajua tena ukikosa la kufanya, niliona nisome some tu
kupoteza muda.....lakini ....’akasita.
‘Hakuna wasiwasi mume wangu, ...hiyo naona kama ni nakala yangu au
, niliiweka wapi, sijui, uliipatia wapi...?’ nikamuuliza nilipoona ile alama
yangu, nakutambua kuwa ilikuwa ni nakala yangu.
‘Hapana hii ni nakala yangu, sio ya kwa-kwako…kwani nakala yako
haipo?’ akaniuliza akionyesha ishara ya kushangaa.
‘Unavyouliza ni kama vile unafahamu kuwa nakala yangu haipo, au?’
nikamuuliza huku nikitabasamu, nilikuwa nimejisahau sasa, maswali kama hayo
sikutakiwa kumuuliza.
‘Ndio maana nakuuliza, maana kila mmoja ana nakala yake, au sio,...mmh,
halafu mke wangu nilataka tuongee kitu muhimu, nilikuwa najaribu kupitia baadhi
ya vipengele mbali mbali kwenye huu mkataba eeh, na sijui utakuwa na nafasi
tukae tuongee, kwasababu mengi yamepita, na hatujawahi kuongea haya yaliyotokea...’akaanza
kusema.
‘Mume wangu achana kabisa na mambo hayo, wewe hujafikia muda wa
kuongelea hayo mambo, hujaruhusiwa na docta kabisa…subiria kwanza upone, na
hata hivyo, sioni kwanini ukimbilie kusoma katiba kwa sasa, huoni utajitakia
matatizo, unakumbuka tulivyokubaliana, hata kwenye mkataba hilo lipo kuwa mtu
akiumwa, mambo ya mkataba yanawekwa pembeni kwanza,mengine yote yanasahaulika
mpaka anayeumwa apone..sioni umuhimu wa mkataba ukiwa kwenye hiyo
hali.’nikasema.
‘Swali linalonisumbua ni kuwa nikipona, itakuwaje…inanipa shida
sana hiyo, na akili yangu haiwezi kutulia kama tusipolitatuia hilo, unanielewa
hapo..itakuwaje sasa…?’ akauliza huku akifungua fungua ukurasa kwenye ule
mkataba.
‘Kwani una wasiwasi gani mume wangu,...mimi sioni tatizo, kwani
ulishaniomba msamaha, nikakukubalia kuwa nimekusamehe, hayo yanatoka wapi
tena?’ nikamuuliza .
‘Kusamehe kwa maneno ni kitu kingine, lakini yapo mambo ya
kisheria…na haya ni kati yangu mimi na wewe…sasa….’kabla hajamaliza mlango
ukagongwa, nikageuka kuangalia mlangoni, na mara ukafunguliwa akaingia docta, rafiki
wa mume wangu, ambaye aliponiona kwanza alijifanya kama vile hajashituka.
Lakini nilimuona na dalili ya kushtuka, hakutarajia kunikuta hapo
‘Nilisikia umekwenda kazini au…mbona umerudi mapema hivi,.....?’
akaniuliza docta
‘Kwani tuliongea na wewe leo, kuwa nimeenda kazini na sitarudi
mapema, mbona unaingilia mambo yasiyokuhusu, unakuwa kama unafahamu ratiba
yangu kuwa nitarudi nyumbani kwangu saa ngapi, kwanza ukumbuke kuwa nipo
likizo, kwa ajili ya kumuuguza mume wangu!’ nikasema nikimwangalia kwa makini
machoni.
‘Nilipiga simu kwa mumeo akasema haupo, ....nikajua upo kazini, na
kama upo kazini, sizani ungelifika tu na kuondoka…’akasema na akawa sasa
anamuangalia mume wangu kwa makini, nahisi kuna ishara aliona kutoka kwa mume
wangu ndio akakatiza maneno, sikutaka kuongea sana au kufanya lolote litakalo wakwanza,
nikasema;
‘Mume wangu naazima hii nakala …mara moja…’nikasema nikiwa
nimeinama kuichukua hiyo nakala, ni kitendo cha haraka, maana nilipotamka
hivyo, nay eye alikuwa keshafikisha mkono kama kuishika hiyo nakala ya mkataba,
lakini mimi nilihsiwahi
‘Hapana nina kazi nayo…si una ya kwako…’akasema
‘Ni kitu kitu kidogo, nakurudishia sasa hivi, nyie si mnaongea
wewe na rafiki yako, au sio…’nikasema nikimuangalia docta, na docta akawa
anaonyesha uso wa tahadhari, akimuangalia sana mume wangu
‘Mhh, hapana hiyo nakala yangu ...ina mambo yangu binafsi
nimeandika,....unaonaje ukaenda kuchukua nakala yako, kama hutojali mke
wangu...’akasema akionyesha wasiwasi fulani.
‘Usijali mume wangu, nitakurudishia tu, ....endeleeni
kuongea...’nikasema huku nikiwa nimeshauchukua na kuanza kufungua sehemu za
ndani za mkataba ule, niliona mistari imechorwa chorwa, kama kukata kata kata
sehemu, na maneno mengine yameandikwa kwa mkono, kama vile ni rafu.
Kiukweli hii ilikuwa nakala yangu , pamoja na sahihi, kuna sehemu
niliandika mambo yangu, na sahihi,
lakini kwa hivi sasa naona mume wangu naye kaandika mambo yake..akifuta
yale yangu…, nikageuza kuangalia juu, nikaona sahihi yangu na sehemu niliyokuwa
alama ipo, kuashiria sijakosea hiyo ilikuwa ni nakala yangu...’
‘Mke wangu, ...nauomba huo mkataba, tafadhali....’akasema huku
akisimama kuja kuuchukua mkononi mwangu, na mimi nikasogea pembeni nikiendelea
kufungua fungua, na yeye akawa hana jinsi, akatulia huku kanikazia, macho
akionyesha wasiwasi,
Mimi kwa muda huo sikujali tena kuwa nitamkwaza, nikawa sasa
natembea kutoka nje nikiwa bado nimeushikilia huo mkataba huku nikiendelea
kufungua sehemu nyingine, na hakukua na maandishi ya kuhakikiwa kwenye sehemu
nyingine zaidi ni kwenye vipengele vya ndoa.
Nikafika mlangoni bila kugeuka nyuma, na huyo nikatoka nje bila ya
kugeuka nyuma, nikawa sasa naelekea kule kwenye bustani, ili nikae, nitulie
nipate muda wa kuangalia ile sehemu,…kwa haraka nikachukua simu yangu na kutaka
kupiga picha ili niwe na kumbukumbu, lakini kabla sijafanya hivyo nikasikia
sauti toka ndani;
`Shemeji,...njoo haraka...’ ilikuwa sauti ya hatari kutoka kwa docta,
rafiki wa mume wangu. Simu ililia mlioa wa kuchukua picha, lakini sizani kama
itakuwa imelenga sawa sawa maana nilisthuka…
Kwa haraka nikajizoa zoa na
ule mkataba haukubanduka mkononi, nikakimbilia ndani, nilipofika nikakuta mume
wangu kalala sakafuni..na docta kamuinamia akimfungua shati, na mimi
nikamsogelea na kuuliza;
‘Kuna nini tena jamani..?’ nikauliza, na docta akaniangalia kwa
macho, yaliyoonyesha kukerwa, na kusema;
‘Umefanya nini sasa...nilishakukanya, unaona sasa....’akaanza
kunilaumu mimi na sikujau ananilaumu kwa lipi….
**************
Hali ya mume wangu ilibadilika na kuwa mbaya,na juhudi za docta
hazikufua dafu, alimpa huduma ya kwanza lakini haikusaidia, ikabidi akimbizwe
hospitalini na docta huyo huyu na alipofika docta wake akamkagua, na kusema
haraka aingizwe kwenye chumba cha wagonjwa mahututi.
‘Kuna jambo gani limemshitua?’ akauliza huyo docta baada ya
kumhudumia na kurudi pale nilipokuwepo, na hadi muda huo tulikuwa hatujaongea
lolote na docta rafiki.
‘Kwakweli mimi siwezi kujua, labda tumuulize rafiki yake, maana
mimi nilimuacha wakiwa naye, akiwa mzima kabisa, na niliwaacha hata dakika
mbili hazikupita, nikasikia sauti ya huyo rafiki wa mume wangu akiniita kuwa
mume wangu hali yake sio nzuri...’nikasema.
‘Mhh, inaonyesha kuwa kuna kitu kimemshutua, na wewe unakifahamu
ni kitu gani,...hukutakiwa kulazimisha kufanya kitu ambacho hakitaki, au
alipata mshtuko fulani, mshituko kwake ni tatizo…lakini….’akasema huyo docta,
na docta rafiki akamkatiza na kusema;
‘Nahisi ni ule mkataba…’akasema
‘Lakini mbona ni mkataba wetu mimi na yeye, na anaufahamu siku
zote kuwa tunao , na haikuwa na ubaya mimi kuuchukua, na hata hivyo wewe
unajuje kuwa ni kuhusu huo mkataba…?’ nikauuliza kwa mshangao.
‘Kwasababu nilimuona na dalili mbaya, wakati huo mnaongea na
uliuchukua mkataba akawa hataki, ile hali ikawa inazidi kumsukuma kwenye hatari…’akasema
‘Usinitupie lawama kabisa…’nikasema.
‘Kwani ni mkataba gani huo, inawezekena kuna kitu hakipendi kwenye
huo mkataba…?’ akauliza docta anayemtibia
‘Hakuna cha maana vitu vilivyopo humo ni kati yangu na mume wangu
hakuna la zaidi, na sioni ni kwanini liwe ni tatizo hilo…..’nikasema.
‘Una uhakika kuwa hakuna jambo linalomkwanza mume wako kwenye huo
mkataba, nahisi inawezekana kuna kitu ambacho anakihofia..?’ akaniuliza huyo
docta, na mimi nikasema;
‘Lakini sizani hata kama kuna kitu…kipo kipo…nahisi ana lake
jingine, hata sielewi, kwanini iwe hivyo, unajua nimejitahidi sana, sasa
nachoka jamani…aah, basi nifanyeje jamani?’ nikasema huku nikuliza kwa
mshangao.
‘Muhimu, ni kumuhakikishia kuwa kama kuna lolote humo, halitafanya
kazi, au kama hataki wewe uwe nao, mrejeshee, haraka iwezekanavyo…’akasema
docta rafiki.
‘Hivi kwanini unaongea hivyo, unajua lolote kuhusu huo mkataba
maana, maana moja ya makubaliano yetu mimi na yeye ni kuwa mkataba huo ni baina
yangu mimi na yeye tu, wewe umayefahamu
vipi hayo…?’ nikamuuliza docta rafiki kwa ukali, mpaka docta anayemtibia mume
wangu akatuangalia kwa mshangao
‘Off course, …mimi sijui lolote zaidi ya kuwakuta pale mkiwa
kwenye kubiashana..eeeh, nahisi , mimi nahisi huenda mwenzako kinachompa shida
kwa sasa ni kuhusu mliyoandika kwenye huo mkataba…sasa sisi hatujui ni nini
kilichomo humo ndani,...je huna uhakika kuwa huenda kafanya kitu kinyume na huo
mkataba wenu..?’ akaniuliza docta rafiki.
‘Mimi sijui, na hakuna kitu kama hicho, huo ni mkataba wetu tu wa
kikazi, hakuna tatizo, …’nikasema kuvunga ili isije kuleta maana kamili ya
kilichomo kwenye huo mkataba.
‘Haya, kama unaona hivyo, sawa,...ila jitahidi sana, kuwa
mvumilivu, huko mnapokwenda, ni kubaya, na mwenzako yupo mahali pabaya,
hajijui...na usije ukafanya mambo kwa pupa, ukaanza kujijutia, ....itakuathiri
sana kwenye maisha yako...’akasema.
‘Hamna shida, hilo niachie mimi,..., cha muhimu ni kutafuta njia
za kumponyesha huyo mtu, na sijui nifanye nini, maana kila ninachotaka
kukifanya, kwa masilahi yetu, kinakuwa na utata, nitawezaje kuishi maisha ya
nama hii, ina maana mimi nakuwa kama mfungwa...’nikalalamika.
‘Ni swala la muda tu...vumilia, hadi mume wako apone, na mengine
yatakuja baadaye, usije ukafanya mambo, ambayo yatakuharibia, na hata ukienda
kisheria ukaonekana wewe huna haki...’akasema huyo rafiki wa mume wangu na
wakati huo docta alikuwa akitusikiliza tu baadae yeye akaondoka zake na
kutuachia nafasi ya kuongea.
Aliposema hivyo, nikaingiwa na shaka, kwani anavyoongea ni kama
vile anafahamu kitu kwenye huo mkataba wetu, kuna kipengele, kuwa kama mmoja
akiumwa, mambo mengine yote yasimame, hadi hadi huyo anayeumwa apone....na
isitokee shinikizo la mmoja kuchukua nafasi hiyo kwa masilahi yake binafsi...
‘Kwahiyo wewe unasemaje...unataka mimi nifanye nini?’ nikamuuliza,
kwanza alitabasamu, kama kunidhihaki kuwa sasa naanza kumtegemea yeye, lakini
hakufahamu mantiki ya swali langu.
‘Kwa taarifa yako, tu, licha ya kuwa ni hatari, lakini docta
kasema tukio hilo limesaidia kitu fulani, limashitua ile mishipa iliyokuwa
haijashituka, na sasa hivi kila sehemu ya mwili imerejea kwenye hali yake ya
kawaida, lakini kuna angalizo kubwa, tena hilo ni hatari zaidi, kuwa kama hali
hiyo ikiendelea inaweza kuleta matatizo mengine makubwa zaidi...’akasema
‘Kama yapi?’ nikauliza kwa hamaki
‘Stroke....anaweza akapata na kiharusi,ni hiyo ikamfanya
apooze kabisa...’akasema
‘Mungu wangu....’nikasema
‘Lakini yote yanategemea nyie wawili, kama kuna kitu unaona
kinaweza kumkwanza mume wako, ni vyema ujaribu kukiwepa, jaribu
kujizuia,....kwanini usiwe na subira…achana na mambo mengine yote..’akasema na
mara docta akafika, na mimi nikawa na shauku ya kusikia mume wangu
anaendeleaje. Na kabla hajaongea kitu rafiki wa mume wangu akasema;
‘Docta mimi nilikuwa na wazo, je huyo mgonjwa hatuwezi kumpeleka
mahali ambapo atakuwa hakutani na mkewe...maana naona wakiwa pamoja matatizo
kama haya yataendelea kutokea na kama ulivyosema kuwa ni hatari kama akipatwa
na stroke? Akauliza rafiki yangu.
‘Hiyo ni mbaya zaidi, maana mume wake, hataki kuwa mbali na mkewe,
niliwahi kumwambia hilo kabla, lakini alipinga kabisa,.., na kufanya kitu
ambacho hakipendi kitamfanya ajisikie vibaya, cha muhimu ni mke wake, kukwepa
yale yote yanayoweza kumfanya mume wake ashituke,au ahisi vibaya, ndio
hivyo....’akasema docta.
‘Unasikia, ....nilikuambia, uwe makini, mimi nakushangaa una
haraka gani, kuna kitu gani unakihitajia kwasasa, sasa uchague mwenyewe, mume
au hayo unayoyataka wewe....’akaanza kunilaumu rafiki wa mume wangu
‘Wewe hujui kinachoendelea ina maana nikae kimiya wakati naona
kuna mambo yanaharibika, kuna vitu muhimu vinapotea, kwanini vipotee, kuna nani
yupo nyuma ya hayo yote, unataka mimi nikae kimiya, hivi kweli mimi unaniona
kuwa sina uchungu na mume wangu....’hapo nikawa nasema kwa ukali.
‘Hujanielewa …’akasema docta
‘Nimekuelewa sana,…nikuulize kama kuna vitu vinapotea, ambavyo
vitakuja kuitahiri familia, akiwemo huyo mume wangu… , nikae kimiya
tu..nisifuatilie, na hata huko kufuatilia, sijamuhusisha yeye, ila yeye
anajiingiza kwenye mambo yasiyomuhusu kwasasa…ni lazima nifanye yote,
nimhudumie mume wangu na wakati huo huo nilinde masilahi ya familia..’nikasema.
Na mara kukatokea suti ndani ikumuita huyo docta, na docta
akakimbilia ndani, na sisi tukabakia tukiwa na wasiwasi, lakini baadaye huyo
docta akarudi na kusema;
‘Mgonjwa anaendelea vizuri, lakini anamuhitaji mke wake..’akasema
docta
‘Itabidi nifuatane naye maana mimi nawajulia hawa watu…’akasema
docta rafiki
‘Hapana, mgonjwa kasema anataka kuongea yeye na mke wake tu...’ aliposema
hivyo docta, mimi sikupoteza muda nikakimbilia huko ndani alipolazwa mume wangu…,
na nilipofika ndani nilimuona mume wangu akiwa kalala huku kaweka mikono yote
miwili kichwani kama vile hakuna mto, huku kaangalia juu.
‘Oh, mume wangu umepona...’nikasema na yeye akajitahidi kucheka
huku bado akiwa kaangalia juu, kama hataki kuniangalia machoni,na kwa sauti ya
huzini, akasema;
‘Yah, nimepona, lakini sasa naogopa kupona, ...’akasema
‘Kwanini unasema hivyo mume wangu?’ nikauliza
NB: HAYA KWA LEO NIISHIA HAPA
WAZO LA LEO:
Dunia nzima, inaingia kwenye matatizo kwasababu kubwa ya mali na masilahi,.
Watu wanakosana, kunakuwa na vita, migongano makazini, familia hazipatani,
ukichunguza sana ni kwasababu ya mali na masilahi.Ubinadamu, utu, udugu,
unasaba, ndoa vyote hivyo vinaharibika, na kuingia kwenye matatizo kwasababu ya
mali, na masilahi.
Tukumbuke kuwa vyote hivyo, mali na masilahi ni vitu vya kupita
tu...vilikuwepo, na vitaendelea kuwepo, wewe kama binadamu mali na masilahi
yako ni matendo yako mema.Matendo yako mema ndio mali na masilahi yako,
itakayoweza kukusaidia hata baada ya kufa..
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment