Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Saturday, November 11, 2017

MKUKI KWA NGURUWE-24



 ‘Mnaweza kwenda kumuona mgonjwa, yupo katika hali nzuri tu, ila kwa tahadhari, msimuongeleshe sana, au kumuuliza maswali ya kumfanya afikirie sana, na mengine bado tunayafanyia kazi, bado yupo kwenye uchunguzi, ....kwa ujumla hali yake inaendelea vyema...’

Tuendelee na kisa chetu…..

**************


Nilisimama nikiwa siamini,…au docta alikuwa ananidanganya,….nikatulia, nikawa namuangalia mume wangu, ambaye kwasasa uso niliouona awali ukitabasamu sasa umekuwa hauna nuru tena, uso ukawa kwenye kukunjamana kwa maumivu au hasira.

Unajua wakati nafungua mlango nilikuwa nimepanga kumuuliza maswali yaliyokuwa yakiniumiza akilini, na nilipomkuta kakaa kitandani, nikafurahia kuwa sasa nitaweza kupata majibu ya hayo maswali, ...

‘Swali la kwanza nilitaka nimuulize, je ni kweli kuwa ana mahusiano yoyote na mwanamke mwingine zaidi yangu mimi mke wake, jibu liwe  ndio au hapana, hakuna maelezo, sitaki nimchoshe..

‘Swali la pili je ana mtoto nje ya ndoa ...jibu ni ndio au hapana.....’ na kama majibu ya maswali hayo mawili yatakuwa ni ndio....basi hakuna jinsi, akipona tu, ndoa imekwisha, kila mtu ashike mipango yake, mkataba wangu na yeye basi, ...niliwazia hilo nikiwa na dhamira ya dhati.

Lakini nilijipa moyo kuwa majibu yake yatakuwa hapana, kwani mume wangu hana tabia mbaya, hawezi kunisaliti,….

Lakini kabla ya maamuzi ya kuvunja ndoa,  kwanza awe amepona kabisa, pili, ni lazima nimfahamu huyo mwanamke shetai ni nani,…ni lazima nimfahamu huyo mwanamke ili abebe dhamana yake, ni lazima nimfunze adabu, mbele ya.....’

Na nilipofika hapo nikawa nimeshafungua mlango, na ndio hapo nikajijuta namuangalia mume wangu akiwa kakaa kitandani.

******************

‘Mume wangu umepona…’nikasema nikiwa bado nimesimama siamini. Mume wangu alikuwa kakaa, lakini mikono miwili huku na huku imeshikilia kitanda, alikuwa kama anajilazimisha kukaa sawa…nilihisi mikono yake ikitetemeka.

Ghafla , nilipotoa kauli hiyo mume wangu akadondokea kitandani, na kilichofuata hapo ikawa heka heka, maana yule mtu aliyekuwa kakaa, kwa shida, maana ilijionyesha kuwa alikaa vile kwa kujilazimisha, kwa jinsi nilivyomuona,.. sasa anatikiswa na bora alidondokea kitandani miguu imening’inia , akawa sasa anatikisika, anatikiswa mwili mnzima.

Hapo sasa nikachanganyikiwa kwa haraka nikaanza kuita madocta, kuomba msaada, na haikupita muda, madocta wakaja, na nikaambiwa nitoke humo ndani haraka…nikawa siwezi hata kuinua mguu, na kwa muda huo docta rafiki alishakuja, akanishika mkono, akawa sasa ananikokota, kunitoa nje ya kile chumba.

‘Umefanya nini sasa…?’ akaniuliza docta kwa ukali

‘Mimi sijui, sijafanya kitu…’nikasema
‘Uliongea nini na yeye, si nilikuambia…usimsemeshe kitu cha kumpa mawazo..’akasema

‘Sikuwahi kuongea naye, nimeingia, akiwa kakaa kitandani, miguu chini..anatizama mlangoni akiwa na tabasamu, cha ajabu aliponiona tu, akakunja uso…’nikasema

‘Unasema ulimkuta kakaa kitandan, haiwezeani,…?’ akaniuliza sasa akishangaa

‘Ndivyo nilivyomkuta hivyo…’nikasema

‘Mhh…matokeo mazuri hayo,…kama ulimkuta kakaa kitandani, basi tuna matumaini sasa….una uhakika…alikuwa kakaa kukaa..?’ akauliza

‘Ndio docta…..kwani wewe ulimuachaje..?’ nikauliza

‘Nilimuacha kalala, baada ya kumpatia mazoezi, kiukweli  mwili wake ulikuwa bado haujawa tayari kukaa wenyewe bila msaada, basi nilipomaliza kumfanyia usafi, nikamuacha akiwa amelala..’akasema

‘Sasaa, mhh…najiuliza ni kwanini …’nikasema

‘Unajiuliza nini…hiyo ni iashara nzuri, kama hukuongea naye, na ulimkuta amekaa peke yake bila ya msaada wa mtu, ujue ni kumbukumbu zinarejea na pia mwili umeshaanza kukubaliana, …’akasema

‘Ninachojiuliza mimi ni kwanini alikuwa na furaha kama alitarajia kitu na nilipotokea mimi furaha hiyo ikatoweka…..na hali hiyo ikaja ?’ nikauliza.

‘Hapo ina maana kuwa kumbukumbu zinaanza kurejea, huenda katika kumbukumbu zake, alitarajia kuona kitu alichokuwa akikiwazia…lakini ikatokea tofauti na matarajio yake…, inaweza ikawa hivyo, au alipokuona alikumbuka jambo, ..linalomsumbua, akashtuka…vyote au jingine yaweza kuwa hivyo…’akasema

‘Sasa mbona naanza kuogopa….’nikasema

‘Usiogope, hiyo kwetu ni ishara nzuri..kama kaweza kuinua ule mgongo, na miguu peke yake, basi matajio ni mazuri sasa, ni swala la muda tu…’akasema.

‘Sasa alitarajia nini, au kuna kitu gani ananiogopea mimi, au ndio keshajenga chuki na mimi kabisa, au nikuulize wewe ulisema uliwahi kuongea na yeye,, si ulisema mliwahi kuongea naye..?’nikauliza.
‘Sikiliza, …usipende kujitwika mzigo kabla haujatua kichwani mwako, utachoka kabla huo mzigo haujatua kichwani, umenielewa, …mume wako hapo alipo anapambana na mitihani mingi, hatujui kilichosababisha hayo yote ni nini..’akasema

‘Sasa tutamsaidiaje..?’ nikauliza

‘Cha kumsaidia ni kuhakikisha ukija una hali ya kumpa moyo,..usiongee lolote la kumuumiza kichwa, na nahisi kuna kitu anakitegemea au mtu anapenda aje aonane naye, nahisi ndio maana ulipotokea wewe tabasamu likapotea…’akasema

‘Ni nani sasa huyo anayetaka kuonana naye…?’ nikauliza

‘Hapo mimi na wewe hatujui..tunawazia hivyo tu, lakin wewe ni mke wake, unahitajika kufika, kwasababu kutokufika kwako, kunaweza kumfanya afikirie vibaya zaidi, cha muhimu nikugundua ni kitu gani anakihitajia kwa sasa…’akasema

‘Nani ataligundua hilo…?’ nikauliza

‘Mimi nitagundua anahitajia nini, usijali…’akasema

**********
 Basi siku ile ilipita, nikawa nafika, namkuta kalala, haongei,..nikimsemesha ahasemi neno, ikawa sasa mimi sina raha…hata rafiki yake, yaani docta akaniambia hali ya mume wangu imekuwa tofauti na matarajiao yao.

Siku moja, nikafika hospitalini, nilimkuta mume wangu kalala tu, kaangalia juu, kama kawaida yake, nikamsaidia kumgeuza geuza japokuwa alishafanyiwa mazoezi

Sasa nikamgeuza aniangalia, nilitaka kujua kama ananifahamu mimi, akawa ananiangalia tu, kama mtu mgeni kwake kabisa, moyoni nikaanza kuingiwa na wasiwasi, nikihisi vibaya, mbona huyu mtu kawa hivi, ni kama mwili mtu....

 Ghafla sasa nikaona hisia za uhai kwenye macho yake,  nilimuona akigeuza mboni za macho yake,  na mara machoni niliona machozi yakimtoka...nikasogeza mono na kuyafuta machozi yake..nikawa najiuliza ni kwanini machozi hayo yanamtoka, anahisi maumivu au kuna nini, .nikatulia, na hapo huruma, woga, wasiwasi na kukata tamaa, vikanitawala, ...

‘Mume wangu mbona upo hivyo, niambie kinakusumbua nini jamani..?’ nikauliza

Nilichoona ni machozi yakiendelea kumtoka kwenye macho yote mawili na mimi nikawa nakazana kumfuta hayo machozi;

‘Mume wangu unalia nini, niambie anagalau na mimi nijue, ..mimi ni mke wako, unavyokuwa hivyo mimi naumia sana, niambie kitu ili niwe na amani moyoni, unalia nini, nimekukosea nini…?’ nikauliza

Mara mume wangu akawa anahangaika kupanua mdomo, unakuwa kama unatetemeka, kuashiria anataka kuongea jambo;

‘Kama huwezi basi usijilazimishe, ila ujue mimi mke wako nakupenda sana…’nikasema na hapo macho yakameta meta, kuashiria uhai, na hali ya kutikisika tikisika kichwa, nikaogopa kuwa huenda ile hali iliyowahi kutokea inaweza kutokea tena, lakini haikuwa hivyo, mara akasema;

‘Mke -wangu,…m-ke..w-w-wwngu..’akasema

‘Mimi hapa mume wangu, ..’nikasema

‘Ni-ni-samehe…na-na- na-kuomba ni-ni-s-s-samehe…’akasema

‘Mume wangu hujanitendea ubaya, hata hivyo usiwe na wasiwasi, sina tatizo na wewe…’nikasema

‘Ni-ni-ni…..me-me-ku-ku-kosea….’akasema

‘Nimekusamahe mume wangu japokuwa sijui …’nikasema

‘Yah---ohhhhh……’hapo akavuta pumzi halafu akatulia kwa muda, macho yapo wazi nayaona, na…machozi hayatoki tena…’halafu nikaona kichwa inatikisika, ilichukua dakika chache kikatulia, ikaanza kwikwi….hapo ikabidi niwaite madocta…

Nikaambiwa nitoke, nikatoke pale na mimi machozi yakaanza kunitoka, nahisi huzuni, namuonea huruma mume wangu anavyopambana na hiyo hali na siwezi kumsaidia ..

Nilikaa nje kwa muda, mara docta akaniita,…nikaingia, na docta akasema

‘Haya mwambie mke wako unachotaka kumuambia…’akasema docta

‘Mke wangu, so-so-sogea….’akasema na mimi nikasogea na kukaa kitandani karibu yake.

‘Ni-ni-sa-mehe..m-m-mke wangu…ha-ha-ya yo-yo-te ya-ya-na-na-natokea ku-ku-ku-toka-ka-kana na dh-dh-dhambi zangu, ni-n-nisamehe sa-ss-sana...’akasema

‘Dhambi gani mume wangu...’nikasema na safari hii nikawa nimeshusha sauti na kuongea kiupole

‘Wewe kubali kuwa umeshamsamehe, na itoke moyoni…’akasema docta

‘Nimekusamehe mume wangu uwe na amani, upone, nakuhitajia sana nyumbani..’nikasema, na nilijikuta pale siwezi kujizuia, machozi yakaanza kunitoka, na nilibakia vile mpaka nikahisi mtu akinishika begani sikutaka kugeuka kumwangala ni nani nikasema;

‘Mume wangu ana tatizo gani..mbona kawa hivi tena jamani...?’nikauliza huku nimeshika kichwa.

‘Ni tatizo la muda mfupi, litakwisha na ataweza kutembea cha muhimu ni kufuata masharti ya dakitari, dakitari bingwa wa mambo hayo keshamwangalia , kasema hilo litakwisha, hali iankwenda vyema kabisa, kuna kitu anakihitajia, labda ilikuwa ni hiyo kukuomba msamaha,lakini bado, kuna kitu anakihitajia....’akasema.

Niligeuka kumwangalia huyo aliyeongea haya, alikuwa docta  rafiki wa mume wangu, na kwa muda huo nilitamani nimkumbatie, ili nisianguke, maana miguu ilikuwa haina nguvu, nilihitajia mtu wa kunifariji na kusema mume wangu atapona tu, hakuna tatizo.....

Nikageuka kumwangalia mume wangu, na nilimuona akiwa sasa akiwa kaangalia juu, hatikisiki , alikuwa kama gogo tu, alikuwa kama mwili wa marehemu, lakini unachojua kuwa yupo hai ni machoni, akiyapepesa na kuyageza huku na kule, na sasa machozi yanamtiririka.

Pale...moyoni nikaingiwa na huruma, woga ukachukua nafasi nikiwazia mbali zaidi, kuwa sasa mume sina tena, kauli hizi ni za kuniaga, ....na ile hali ya hasira chuki ..vikayeyuka...sasa namkabili mungu anisamehe, kama nina kinyongo na mume wangu mimi sina tena amponye mume wangu tu.

‘Ndio maana nilikuwa nakuzuia sana, usiingie bila ya mimi….’akasema docta.

‘Hali kama hii hata ingelikuwa ni wewe…’nikasema na mara sauti ya mume wangu ikasema

‘Mke wa-wa-ngu, ...usiondoke kabla hujanisamehe, na-na-na taka nikifa niwe huru, na-jua ni-meku-kosea sana, nisa-mehe mke wangu...na baba-ya-ko, ani-sa-sa-mehe..na-na deni…na..na..mto-ooooh..’hapo hakuweza kumalizia, akawa kimia

Milio ya mashine ya hatari ikaanza kulia, hapo ikawa heka heka kwa madocta na mimi nikatolewa nje kwa haraka…hapo ndio nikajua sina mume tena,…..nililia, na kulia….

Sitaweza kuisahau siku hiyo…

NB: naishia hapa kwa leo


WAZO LA LEO: Katika maisha yetu, katika kuhangaika kwetu, maana yabidi tuhangaike, tutafute riziki za halali,..yabidi tupambane na mitihani ya maisha magumu, kuna wenye maradhi ,madeni nk..yote ndiyo maisha yetu, vyovyote iwavyo, hata kama tupo kwenye raha, hatuna shida, tunakula na kusaza…bado sisi ni waja wa mola, hatuna jinsi, tupo kwa rehema zake,…tuyakumbuke mauti, kuwa ipo siku yatatukuta, hata tukiwa nani,…muhimu kwetu, ni kujiuliza je tumejiandaaje na siku hiyo, siku ambayo roho itauwacha mwili,…
Ni mimi: emu-three

No comments :