Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Friday, November 10, 2017

MKUKI KWA NGURUWE-23


 Nilipomaliza kuongea na baba, nilihisi mwili mnzima ukinicheza cheza kwa hasira, lakini sikujua namkasirikia nani, au naogopa nini, lakini anayoongea ni kama ana uhakika nayo,..awali nilijua ni ile chuki kuwa nimeolewa na mtu wasiyemtaka, lakini haya anayoongea sasa yananifanya nianza kuingiwa na mashaka

Wakati anaongea akili yangu ilikuwa mbali, ikijaribu kuunganisha matukio yaliyofuatana, kujifungua kwa rafiki yangu mtoto anayefanana na watoto wangu, ajali ya mume wangu, ambayo ina utata, na inaonekana alitokea upande anapoishi rafiki yangu.

Sasa kuna mtu kaiba bahasha , bahasha ambayo nahisi ilikuwa na ushahidi,…sikupata hata nafasi ya kuifungua,..kwa hali hiyo akili ikaanza kunionya kuwa kuna kitu...kuna mtu, ananichezea, ..ni nani huyo

Mume wangu, ...hapana, mume wangu anaumwa, hajiwezi,

Rafiki yangu....…


‘Unasikiliza wewe bint...'baba akaongea kwa ukali kwenye simu

'Nakusikiliza baba...'nikasema

'Nimekupigia simu, kuwa kampuni ya mume wako, ipo karibu kufilisika, na kuna madeni mengi sana…una hiyo taarifa…?’ baba akauliza

‘Baba ndio nimerudi nyumbani, sijapata hata muda wa kuipitia ile taarifa uliyonipa, mimi sijui lolote kuhusu kampuni yake, alikuwa akiendesha mambo yake na mimi yangu…’nikasema

‘Unaona sasa, hiyo ndio ndoa mnayoitaka nyie uhuru wa kufanya mtu apendavyo, hata kwa mke na mume, aah…kila mtu kivyake, ..nikuulize hivyo ndivyo tulivyokufunza…’akasema baba na mimi nikabakia kimia.

‘Sasa sikiliza mimi sitaweza kutoa chochote tena kwenye kampuni ya mume wako, au hata yako, maana nyie sasa mnajiweza, au sio…na hayo madeni ya mume wako mtajua jinsi gani ya kuyalipa, kama ni kufilisi mali za kampuni mtajua wenyewe, ila mjua kuwa mnahitajika kurejesha mtaji wangu…’akasema

‘Baba, hatuwezi kufanya hivyo wakati mtu yupo mahututi hospitalini…’nikasema

‘Na huyo rafiki yako alizaa na nani…?’ akanishtukiza na swali ambalo lilikuwa kama mtu kazabwa kibao usoni.

‘Mi-mi…baba, sijui…’nikaweza kusema hivyo

‘Una uhakika…?’ akauliza

‘Mi-mi..sijui baba, kama mwenyewe hajawaweza kunieleza, nitajuaje, nahisi hataki watu walifahamu hilo…’nikasema

‘Mtoto wake anafanana na watoto wako au sio…’akasema kama kuuliza

‘Mhh, baba umeyajuaje hayo ina maana  umeweza kumuona huyo mtoto…?’ nikauliza na mara kwenye simu yangu kukaingia ujumbe , sikutaka kukatiza simu ya baba, ila yeye akasema.

‘Tazama hiyo picha niliyokutumia kwenye simu yako…’akasema ikabidi niache kuongea naye nitazame hiyo picha.

‘Huyo ni nani…?’ akuliza

‘Hawa ni mapacha wangu, watoto wangu wakiwa wadogo…’nikasema

Baadae ukaingia ujumbe mwingine akionekana mtoto mchanga, .alikuwa mtoto wa rafiki yangu, na pembeni wamewekwa watoto wangu kama kuwafananisha na huyo mtoto, kiukweli wanafanana sana, hana tofauti na watoto wangu kwa sura, isipokuwa yeye hana nyusi nyingi…sura ya kiume ilionekana usoni mwake.

‘Hata usemeje,….mtoto wa rafiki yako anafanana sana na watoto wako…sasa niambie ukweli kuna nini hapo, je sio kweli  kuwa mume wako anashirikiana na rafiki yako au kuna nini kinachoendelea kati yenu, mimi nisichokifahamu…’akasema baba

‘Una maana gani baba…!!, kuwa rafiki yangu anaweza kutembea na mume wangu…?’ nikauliza

‘Nikuulize wewe sasa…’akasema

‘Haiwezekani baba, unataka kusema nini kuwa mimi nimeshirikiana na rafiki yangu kulifanikisha hilo, au…’nikasema

‘Sasa hilo utajua wewe mwenyewe na mume wako na huyo unayemuita rafiki yako kipenzi…ndugu yako…, lakini kama ikatokea kuwa ni hivyo, sitaweza kuvumilia upuuzi huo, kwanini ukaruhusu hilo, au ulitaka rafiki yako awe mke mwenza wako…au?’akasema baba kwa ukali

‘Baba unanijua nilivyo, mimi siwezi kuruhusu kitu kama hicho, na sio kweli baba, kufanana kwa watoto sio ushahidi wa kulithibitisha hilo, ndio hata mimi niliingiwa na mashaka hayo, lakini rafiki yangu hawezi kunifanyia hivyo baba, sio kweli…’nikasema

‘Sasa ilikuwaje…jiulize hilo kwa makini,…je ni mume wako kakuzunguka au unataka kusema nini, jitetee sasa….?’ Akauliza

‘Baba huyo anaweza akawa mdogo wake mume wangu, anaweza akawa ndiye baba wa huyo mtoto, niliongea na huyo rafiki yangu, na kasema hivyo, hanificho kitu, kiukweli siwezi kuamini hayo, baba haiwezekani, …’nikasema hivyo japokuwa sina uhakika

‘Na iwe hivyo…..vinginevyo, utaniambia,  mimi kama mzazi nimeshajua ukweli, lakini siwezi kwanza kuliingilia hilo, …isome hiyo taarifa niliyokupa, halafu na hayo yaliyogundulikana , kila kitu kipo wazi, ukiunganisha hiyo taarifa, matukio na picha, utakuja kuniambia….umesikia, …’akasema na kukata simu

‘Bahasha haipo, sasa itakuwaje..siwezi kumuambia baba ukweli kuwa imeibiwa, ataniona mimi ni mzembe..sasa nifanyeje…’nikawa naongea peke yangu

  Akilini nikajua kuwa baba atakuwa aliandaa taarifa inayohusiana na mume wangu, huenda na ….ingenisaidia sana, sasa nifanyeje, na ni nani kaiba hiyo bahasha?

‘Sasa hiki ni kitendawili kwangu….’ Nikasema nikikaa kwenye sofa, nikashika kichwa nikiwaza…nifanyeje

Kwa haraka nikachukua simu yangu.

***********

‘Umefikia wapi…?’ nikamuuliza

‘Kuhusu hiyo kazi eeh… bado sijapata lolote la muhimu, ila kuna jambo nalifuatilia bado halijawa sawa, nikiwa na uhakika nalo nitakuambia…’akasema

‘Wewe na mume wangu mumeanza lini mashirikiano ..?’ nikamuuliza na nilihsi hali ya kupumua kwa nguvu kutoka kwa rafiki yangu huyo

‘Una maana gani sijakuelewa hapo…?’ akauliza

‘Yoyote yale…najua unaelewa ninachokuuliza..?’ nikauliza

Kukapita ukimia fulani, halafu nikauliza tena

`Umenisikaa nilichokuuliza....?’ nikauliza .

‘Nimekusikia lakini sijakuelewa bosi, una maana ganu kuuliza hivyo, sijui unachokiongea bosi...’akasema

‘Kwanini unakuwa tofauti hivyo, sio kawaida yako unanipa mashaka , mara nyingi nikikuuliza swali unakuwa mwepesi kulitafsiri na majibu yako yanakuwa ya haraka…na mara nyingi yanakuwa ya ukweli, tunageukana siku hizi…’nikasema kwa ukali

‘Rafiki yangu,  mimi sijakuelewa,o-bosi, sina mashirikiano yoyote zaidi ya yale tuliyokubaliana, ukiniagiza nifenye ndivyo nafanya, na zaidi subiria taarifa ya kazi uliyonipatia, kwani kuna nini bosi…’akauliza, kiukweli tukiwa kwenye maswala ya kikazi hupenda kutumia neno hilo bosi.

‘Ukweli utadhiri,…endelea na kazi niliyokupatia, ila ujue mimi sio mjinga, kukuamini kiasi hicho sio kwamba nimefumba macho na kuziba masikio, akili yangu inafanya kazi vizuri tu, …unanielewa…’nikasema

‘Nakuelewa bosi….’akasema

‘Watu wanasema , na sio mmoja sasa, na hili kama limefika kwa baba ni hatari sana, kama kaamua mwenyewe kulifuatilia, sijui itakuwaje, mimi nilipomuona mtoto wako kufanana na watoto wangu niliingiwa na mashaka, hayo kama binadamu, lakini najua wewe kama rafiki yangu huwezi kunisaliti…’nikasema

‘Ni kweli…siwezi kufanya hivyo….’akasema



‘Je kuna kitu unanificha…?’ nikauliza

 ‘Bosi  unakumbuka ni wewe uliyenishauri kuwa nikatembee nje ili nipate mimba, na ukanishauri nitafute hata mume wa mtu…’akasema

‘Ndio ukaamua kutembea na mume wangu…?’ nikamuuliza

‘Hapana bosi, mimi najiuliza ni kwanini wewe unapaniki kiasi hicho…’akasema

‘Kwasababu lisemwalo lipo…na wewe hutaki kuniambia ukweli, haya basi niambie baba wa huyo mtoto ni nani…kama hayo yanayosemwa sio ukweli…?’ nikauliza

‘Yanasemwa mengi bosi na sio yote yana ukweli, …niamini bosi mimi sifanyi kitu kinyume na ulivyoniagiza….na..hebu kwanza subiria nimalize kazi uliyonipa ili tukiongea tuwe na ushahidi….wewe si ndio unataka huo, sasa subiria….’akasema

 ‘Mume wangu ana kitu kinamsumbua, mdocta wananiuliza kuna jambo gani kalifanya ambalo halimpi amani, nataka kulifahamu, sasa kama ni hilo, ..na wee unamjali shemeji yako, niambie, sema ukweli tuone jinsi gani ya kumsaidia…’nikasema

‘Sizani kama …’akatulia

‘Huzani nini, ..?’ nikauliza

‘Kuwa yeye kuna jambo linalohusiana na mimi au mtoto linamsumbua, sizani, nahisi ni mambo yenu wewe na yeye, au mambo ya kazini kwake…’akasema

‘Aliwahi kukuambia hivyo…?’ nikauliza

‘Nasema tu..na yote utakuja kuyaona, si umenipa kazi, sasa subiria…’akasema

‘Kwahiyo katika ugunduzi wako, umeliona hilo..sawa…?’ nikauliza

‘Ndio nahakiki ukweli, siwezi kukujibu kwa sasa unajua nifanyavyo kazi yangu, niamini bosi…’akasema

‘Lakini baba anahitajia majibu nitamjibuje mfano akinipigi asimu sasa hivi…?’ nikauliza
‘Mwambia tunalifanyia kazi bosi…’akasema


‘Sasa nisikilize sana, acha maneno hayo, ya kunizunguka, naona unapima hasira zangu, acha kauli za kufanya niondoe uaminifu wangu kwako, nimeongea na baba, na nimemthibitishia kuwa huenda mtoto wako anafanana na watoto wangu kwa vile ulitembea labda na ndugu za mume wangu, sasa tafuta ushahidi wa kulithibitisha hilo, kama ni kweli, vinginevyo, hutaamini nitakachokifanya…’nikasema

‘Kwani kamuonea wapi mtoto wangu, mbona hajawahi kuonana na mimi…?’ akauliza

‘Mimi sijui yeye kanitumia picha ya mtoto wako, na mimi nilipoichunguza kiukweli mtoto wako anafanana sana na watoto wangu, kwa mtu yoyote atafikiria hivyo, kuwa wewe umetembea na mume wangu…’nikasema


‘Rafiki yangu, ...najua itafika muda ukweli utadhihiri, wa-ache watu wasema, lakini ukweli utabakia pale pale, na ukweli mwingine kama sitaki ujulikane hakuna wa kunilizimisha, hata awe nani…’akasema

‘Kwahiyo unataka kusema nini…?’ nikauliza

‘Kuwa subiria taarifa ya kazi yako, halafu utakuja kuamua mwenyewe…’akasema

‘Kwahiyo ni kweli…?’ nikauliza

‘Kuhusu nini sasa…?’ akauliza

‘Usitake kunifanya mimi kama mtoto mdogo, unajua nimekuuliza nini…’nikasema kwa ukali

‘Hapana, sio kweli, kama ni hivyo unavyofikiria wewe, japokuwa sijui ina maana gani hapo, ukweli wote nitakuambia mimi ambao ni lazima uujue,  ngoja nimalize hii kazi uliyonipatia kwanza…’akasema

‘Narudie tena, mimi nimeongea na baba yangu nikamthibitishia hilo, kuwa mume wangu hawezi kufanya upuuzi huo, kwani kama ni kweli, itakuwa kashfa kubwa sana kwenye familia yangu, unalifahamu hilo…’nikasema

‘Mhh…nakuomba kitu kimoja,kwanini usisubirie kwanza nimalize hii kazii uliyonipatia, kila kitu kitakuwa wazi, na hata baba yako, ataamini tu, usiwe na wasiwasi kabisa, …’akasema

‘Nakuuliza tena, je kuna ukweli wowote wa hizi shutuma kuwa huenda wewe na mume wangu mna mashirikiano fulani, ambayo yamekwenda zaidi hadi kuingilia ndoa yangu…?’ nikamuuliza

‘Sio kweli….’akasema

‘Nataka ushahidi…wa kumthibitishia baba yangu,,unanielewa, kesho niupate, nakupa muda huo hadi kesho, unanielewa…’nikasema na kumuuliza

‘Sawa bosi….’akasema.

‘Kama ni kweli, umenithibitishia hilo, basi mimi nataka ukweli wote kuhusu mume wangu, nataka kujua ni kwanini hayo yakatokea, nataka kufahamu  huyo mwanamke mwingine aliye na mashirikiano naye, nilikuambia utafute huyo mzazi ni nani, nimeambiwa, hakuna mzazi mwingine sasa ni nani zaidi yako…’nikasema

‘Utamfahamu bosi, kila kitu nimekifuatilia …’akasema.

‘Sawa, kwa ajili ya urafiki wetu, kwa ajili ya kupona kwa mume wangu nakusubiria wewe, natumai haitafikia muda tukawa maadui,...’nikasema

‘Ni kweli, haitatokea hivyo, niamini, …’akasema

‘Una uhakika..?’ nikauliza kama anavyopenda kuuliza baba yangu.

‘Siwezi kukuangusha bosi, ndio maana nataka kila kitu kiwe wazi, ili nikikuletea hiyo taarifa, kusiwe na kigugumizi tena, unanielewa nifanyavyo kazi zangu, najua baada ya taarifa hiyo hata baba yako, hatakuwa na tatizo tena, itabakia wewe kuchukua hatua zako...’akasema.

‘Sawa ……na nitaichukua hatua ambayo hutaweza kuamini…’nikasema

‘Oh,  hatua gani…?’ akauliza

‘Nimeliwazia sana hilo,…limeniumiza sana kichwa changu, huyo shetani nikimpata, kuna watu nimewapanga, kuna wale mabaunza, niliwahi kukuambia walishaifanya hiyo kazi kwa rafiki yangu mmoja, unakumbuka yule binti aliyejiua, nataka iwe hivyo kwa huyo shetani, harabiwe kiasi kwamba hatatamani kuishi tena....’nikasema.

‘Mungu wangu....’akasema.


‘Lakini kwanini kufanya unyama wa aina hiyo …?’ akauliza.

‘Wewe  kafanye hiyo kazi…kuna jambo jingine nilitaka wewe ulifanyie kazi, lakini naona nitalifanya peke yangu,  kuna watu wanataka kunichezea…wameingia hadi kwenye anga zangu…sitaki baba anione mimi sijui kazi,…baadae nakwenda hospitalini kwanza...’nikasema na kukata simu.

                                         **********
Nilifika hospitalini, na kabla sijaenda wodini, akaja docta rafiki yangu, kumbe yeye alihawahi hapo hospitalini, …nilipotoka kwenye gari langu tu, akajitokeza na kuniwahi, akanisalimia kwa haraka halafu akasema;

‘Niliongea na docta anayemshughulikia mume wako, hali yake ipo salama kuna mambo kidogo yapo kwenye uchunguzi,  na docta wamesema unaweza kwenda kuongea na yeye, japokuwa anaongea kwa shida, kumbukumbu zake bado hazijawa sawa, ni kawaida tu…zitakuwa sawa taratibu, nab ado hajaweza kujiinua mwenyewe kitandani…’akasema

‘Mhh..kwahiyo unataka kusema nini… kuwa hakumbuki kilichotokea au hakumbuki watu….?’ akauliza.

‘Yah, kwa hivi sasa hata ukimuuliza atakuwa kama anatafakari, kujiuliza, sasa kwa hivi sasa haitakiwi kumuuliza uliza maswali kama hayo, ..ndio maana walizuia watu kuonana naye, kwa hivi sasa wanaruhsu watu wachache wanaomfahamu..lakini kwa tahadhari hizo…’akasema.

 ‘Sawa nimekuelewa, ..lakini huenda kukatokea athari gani nyingine, hata kama ni huenda, nataka kujua tu..’nikasema.

‘Mhh…athari nyingi ni za muda tu, Inawezekana ikatokea , asiwezi kuzaa tena, inawezekana sio lazima,  athari nyingine ndio hizo kama hiyo kushindwa kutembea kwa muda, kukosa kumbukumbu nk, lakini mengi ni ya muda tu,...’akasema.

‘Unaposema kuwa anaweza kushindwa kuzaa, ina maana gani, kuwa hataweza kabisa ku-ku....’nikasema kwa kigugumizi.

‘Kufanya kazi ya uanaume..sio hivyo…atafanyakazi kama kawaida, ila..kuzaa, hata hivyo, sio lazima kuwa hivyo…’akasema

Mara akaja, docta aliyekuwa akimshughulikia mume wangu, alikuwa anataka kuongea jambo, na huyo rafiki wa mume wangu akamuwahi kabla hajasema lolote, na kitendo hiki sikukipenda, niliona kama anazuia nisisikie jambo fulani, nikawasogelea na yule docta akasema kwa haraka;.

‘Mnaweza kwenda kumuona mgonjwa, yupo katika hali nzuri tu, ila kwa tahadhari, msimuongeleshe sana, au kumuuliza maswali ya kumfanya afikirie sana, na mengine bado tunayafanyia kazi, bado yupo kwenye uchunguzi, ....kwa ujumla hali yake inaendelea vyema...’akasema, na mimi nikataka kumuuliza swali, docta  rafiki wa mume wangu akadakia na kusema,..

‘Hakuna shida docta, mimi nitahakikisha mgonjwa hapati shida, ...na tunashukuru sana, nitakuja tuongee vizuri....’akasema na yule docta akaondoka, na mimi nikageuka kumwangalia docta na kumuuliza.

‘Hivi kwanini unakuwa hivyo, inakuwa kama kuna jambo hutaki mimi nilisikie kutoka kwa huyo docta, mimi ni mke wake, nina haki ya kufahamu kila kitu...kwanini mnataka kuniweka roho juu...?’ nikauliza.

‘Sikiliza mimi ni docta, na pili mimi niliwahi kuwa mpenzi wako, nakufahamu ulivyo, ndio maana nataka habari zote kwako ziwe kwa maslahi yako, zisije zikakufanya ukawa na mshituko, na pia usije ukafanya kitu kikaja kumuathiri mgonjwa..’akasema

‘Kwahiyo kuna kitu unanificha…?’ nikauliza

‘Hakuna…ni tahadhari tu,…niamini mimi, nayafanya haya kwa nia jema kabisa..nilikupenda na nitaendelea kukupenda…na namjali rafiki yangu…sitaki aje kudhurika wakati nafahamu …’akasema na mimi nikamtupia jicho na kuangalia pembeni.

‘Wasiwasi wangu ni kuwa inavyoonekana kuna tatizo la kiafya kwa mume wangu, na nyie hamtaki kuniambia, ndio wasiwasi wangu huo...’nikasema.

‘Ninachotaka hapa ni hekima, mara nyingi docta akisema mgonjwa wako anahisiwa kuwa tatizo, watu hulichukulia kama ndio tatizo, uvumi husambaa, na hata kumfikia mgonjwa, kwa hivi sasa hatutaki mgonjwa apate kitu cha kumuumiza kichwa, ....inaonekena ana mfadhaiko fulani unaomkera,, unampa shida sana, sasa hilo ndilo ninalotaka baadae tuongee....’akasema.

‘Mfadhaiko....?’ nikauiliza kwa mshangao.

‘Ndio kunaonekana kuna  jambo lina mkera, linampa shida,na kwa minajili hiyo, anajikuta hana amani...au nafsini mwake, anaogopa kuwa kuna kitu kitatokea kibaya, lakini yupo kwenye hali ambayo hawezi kufanya kitu..naweza kusema hivyo...’akasema.

‘Mhh, hapo mimi sijuii....’nikasema.

‘Ndio maana nataka utumie hekima kubwa katika kuliongelea hili , tumia hekima sana kuongea na mum e wako, na kwepa sana kumshinikiza kwa maswali magumu na shutuma, ndio maana nilitaka wakati unaongea na yeye na mimi niwepo, kipindi kama hiki kwake ni kigumu sana, ... na hebu nikuulize, je mwenzako hana tatizo jingine kubwa unalohisi kuwa kalifanya....’akaniuliza.

‘Kiukweli sijui, labda mambo ya kazini kwake, lakini nitajitahidi kutafuta kama kula lolote zaidi…kuna watu wanalifanyia kazi………’nikasema

‘Rafiki yako..au sio?’ akaniuliza

‘Yawezekana…’nikasema

‘Una uhakika hakuna kitu kingine kinamsumbua mume wako ambacho wewe unakifahamu na unaweza kukifanya kumsaidia ….ili awe na amani…?’ akauliza na mimi sikutaka kumuambia hayo aliyoniambia baba, kuwa huenda ni madeni, …

‘Sina uhakika, ndio maana nasema , labda maswala ya kikazi, huko ofisini kwake, na mimi sina ushirika na yeye huko….’nikasema

‘Ya kikazi hayo mhh, ni ya kawaida, watu wanadaiwa wengi tu…nahisi kuna jingine kubwa ya hilo,…wewe ndiye mtu wake wa karibu wa kulisaidia hili’akasema. Na kabla sijasema kitu simu ya docta ikawa inaita na yeye akaangalia mpigaji na kusema;

‘Tutaongea baadaye hii simu ni muhimu sana...wewe tangulia huko kwa mgonjwa, nakuja, ila kumbuka,....usimuulize maswali mengi ya kumuumiza kichwa’akasema docta  huku akianza kuongea na hiyo simu yake.

Nikawa natembea kuelekea huko kwa mgonjwa, nafsini nina wasiwasi, …nitaongea nini na yeye, na nashindwa kuvumilie mengina yanayotokea, nimesikia mengi, nay eye ndio mwenye kauli ya kukubali au kukataaa..je nitaweza kujizuia..



Nikashika kichwa nikiwaza,;

‘Lakini kwanini niteseke kwa mawazo wakati muhusika yupo...kwanini nisimuulize tu, hapana nitasubiria, lakini nikisubiria baba anahitajia majibu, je kama ni kweli, kuwa mtoto wa rafiki yangu ni wake, nitajuaje, hapana sio wa kwake..mmh, sijui nifanyaje....’nikajisemea mwenyewe kwa sauti ya chini chini.

 ‘Nitamuuliza tu, kinamna ambayo sitamuumiza…’nikasema, na nikageuka nyumba, kumuangalia docta, alikuwa bado anaongea na simu, sasa akawa ananionyeshea ishara kuwa nisubirie kwanza...mimi sikumsubiri nikaingia ndani kukabiliana na mume wangu...

‘Nitamuuliza tu….’nikasema na nilipoingia nilishangaa, mume wangu alikuwa kakaa kwenye kitanda, miguu chini, nikashikwa na butwaa, walisema hawezi kujiinua mwenyewe, mbona…na kwa mdua huo alikuwa …anaangalia mlangoni kama anasubiria mtu, akiwa na tabasamu mdomoni,  na aliponiona mimi, tabasamu lililokuwa mdomoni likatoweka, akakunja sura…

                                                             **********

WAZO LA LEO: Mwili wa binadamu ni mdhaifu sana, na kosa dogo linaweza likaharibu utaratibu mzima wa mwili wa binadamu, mfano angalia wengi waliofikiwa na matatizo ya kupatwa na kiharusi, kupooza kwa viungo, ...ukichunguza sana utaona kuwa tatizo hilo lilitokea baada ya jambo dogo tu, kwako wewe mzima, uliona ni jambo dogo tu, lakini kwa mwenzako mwenye tatizo, alishindwa kuhimili, hasira kidogo, au  mshituko kidogo tu, na vitu kama hivyo, vimeharibu utaratibu mzima wa mwili wake, na kupelekea kupooza sehemu za viungo vyake.



Ni muhimu, tunapokabiliana na watu wenye matatizo kama hayo iwe ni matatizo ya moyo, shinikizo la damu, sukari, au vidonda vya tumbo, tuwe na hekima ya kuongea nao,  tujaribu kufuata masharti ya dakitari, na tusipuuze, maana tunaweza kuja kujuta wakati tumeshaharibu.
Ni mimi: emu-three

No comments :