Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Thursday, November 9, 2017

MKUKI KWA NGURUWE-22


‘Baba umerudi lini…?’ nikasema, nikiwa nimenywea, maana ili sura ya kutisha ilipotea ghafla, na uso ukawa wa aibu,…uso wa kujipendekeza. Kwa muda huo, baba alikuwa kanikazia macho tu, akimaanisha anasubiria jibu la swali aliloniuliza. Nilipoligundua hilo, nikasema ;

‘Ni ajali tu baba,….mume wangu kapatwa na ajali….’nikasema

‘Nimeshaonana naye na nimeshapata taarifa zote kutoka kwa dakitari, na bado nasubiria taarifa nyingine, maana ajali hiyo sio ya kawaida,…kuna kitu ndani yake. Ni lazima kujiuliza ni kwanini, akaendesha gari kwa mwendo kasi kiasi hicho, alikuwa kalewa..’ akawa kama ananiuliza

‘Hapana….’nikasema

‘Una uhakika….?’ Sasa akaniuliza

‘Mhh…ndio baba, maana hata Docta wamesema hakuwa kalewa, na hakuwa amekunywa kabisa siku hiyo….’nikamtetea mume wangu.

‘Lakini kulewa sasa imekuwa kawaida yake au sio…? Ni kwanini anafanya hivyo…?’ akaniuliza

‘Ni starehe zake tu baba, lakini litamalizika hilo…’nikasema

‘Una uhakika…?’ akauliza akiniangalia kwa makini

‘Baba….’nikasema hivyo na kutulia.

‘Nauliza swali langu tena….kuna nini kati yako wewe na mume wako, nilishakuuliza hilo swali awali ukasema ni mambo ya kawaida tu…, nilikuambia, nikusaidie ukasema hapana,..mtayamaliza wenyewe,  sasa kwa hili, sitaweza kusubiria , nataka kujua kila kitu, au uniambie mwenyewe kuna nini…?’ akauliza

‘Baba …ni mambo ya kawaida tu ya ndoa, sizani kama wewe na mama mpo na furaha wakati wote, ..kuna muda kunatokea hili na lile, na sizani yote ya ndani ya ndoa nahitajika kuyasema kwako, tutayamaliza tu kwa amani baba, hii ni ajali tu…’nikasema

‘Bint, mimi sio mtoto mdogo wa kukuuliza haya, nimesoma, nina uzoefu wa maisha zaidi yako,…unanielewa,..sitaki nikukumbushe kila kitu…kuwa tulikuambia, tulikuambia,.. hukutusikia…, na asiyesikia la mkuu hufanya nini…’akasema

‘Lakini baba, nilishawaambia, mimi nitaweza, na ninaweza…, haya ni maisha yangu na mume wangu, tuachieni wenyewe…, maana tumeshaoana sasa…, sizani kama ni busara tukarudia yale yale malumbano ya zamani, sasa hivi tuna watoto, tuna familia..baba maji nimeshayafulia nguo nitafanyaje sasa, hebu niambie baba…’nikasema

‘Nafahamu hilo..utasema hivyo, utajitetea tena na tena…., si umekuwa bwana, unajiweza au sio…..haina shida,… ila lile linalogusa familia yangu…, lile linakuja kunigusa na mimi mwenyewe.., sitaliacha lipite hivi hivi, hebu nikuulize ikitokea tatizo, la kikashifa kwako, utaambiwa wewe ni binti wa nani..?’ akaniuliza

‘Kuna kashfa gani baba imetokea, mbona baba mnataka kuyakuza mambo, a kuna nini umesikia kibaya,…baba hakuna kashafa yoyote,…kama umesikia hivyo, ni ….watu tu, kama ujuavyo wanadamu hatuna wema, …mimi nakuhakikishia baba haya mambo nitayamaliza mwenyewe,…niamini baba…’nikasema

‘Una uhakika …..?’ akaniuliza, baba akikuuliza hivyo ujue hilo jambo analifahamu , anakupima tu.

‘Baba…’nikasema na yeye akageuka kuangalia nyuma, ..nahisi alikuwa akimuangalia docta, nikaangalia kule anapoangalia, lakini docta hakuwepo..sijui alikuwa kaenda wapi…lakini badala yake nilimuona  jamaa mmoja kasimama, akiwa anatuangalia..alipoona baba anamuangalia, kwa haraka akaja alikuwa kashikilia  bahasha kubwa mkononi

‘Binti yangu..nilikuwa safarini, lakini hata nikiwa huko nimekuwa nikiiwazia familia yangu, na familia yangu ni pamoja na wewe…mimi nina hisa kwenye kampuni zenu, nilifanya hivyo makusudi,  maana siwezi kutoa pesa zangu ziwekezwe tu, bila ya mimi kujua kinachoendelea,....hii hapa ni taarifa ya kibishara ya kampuni yako na mumeo ..umeshawahi kuipitia vyema…?’ akauliza

‘Ndi-ndio baba lakini….eeh, kuna matukio mengi yamepita hapa karibu, sijapata muda wa kuipitia vyema, ila naifanyia kazi, kwangu, kwa mume wangu sijawahi kukaa naye, sijui kinachoendelea, nitakaa naye nione tatizo lipo wapi…’nikasema

‘Kwanini biashara imeshuka kiasi hiki, hasa ya mumeo…?’ akauliza

‘Baba ni hali halisi, sio sisi tu,…na ngoja nitakuja kuipitia, mimi nina nakala zangu, au hii ni nyingine zaidi..?’nikasema

‘Na hizo pesa nyingi alizochukua mumeo, ni za nini, ni kwa ajili ya nini, umeshawahi kumuulizia mumeo pesa hizo kazifanyia nini…?’ akauliza

‘Pesa gani baba…?’ nikauliza maana sijui kama mume wangu alichukua pesa nyingi kwenye kampuni yake, mimi siingilii kampuni ya mume wangu.

Anyway..hilo sio tatizo kwa sasa…, lakini ndani ya bahasha hiyo kuna kitu kingine, kuna taarifa ya biashata ya mumeo pia, na mengine utakuja kuyaangalia humo ndani, halafu tutaongea…utaniambia hayo yote yana maana gani..’akasema
‘Sawa baba, nita-ipitia..’nikasema

‘Na kingine je wewe unakubaliana na hali hiyo ya mumeo …au ni maisha gani mnaishi hivyo…, nataka majibu kutoka kwako, sio leo, tukikutana unanielewa, maana hujalelewa hivyo, sitaki aibu kabisa....’akasema

Alinikabidhi ile bahasha, na kwa mashaka nikaipokea, na kabla sijataka kufanya chochote, akasema;

‘Ile hali ya mumeo itachukua muda kupona….na ina maana shughuli nyingi alizokuwa akizisimamia yeye, zitasimama, na..zaidi hatujui mapesa yote aliyochota aliyachukua kufanyia nini…sasa, kazi ni kwako, kabla mumeo hajazindukana, ulifanyie hilo kazi, fuatilia kinachoendelea , baada ya hapo, mimi mwenyewe, nitajua la kufanya, sikutoa mataji wangu upotee bure, umenielewa…’akaangalia saa yake.

‘Baba hapa sio mahali pa kuulizana maswala ya biashara baba…mume wangu yupo hali mbaya, nina mawazo kuhusu afya yake, nipe muda kidogo kwa haya…, naomba hayo tuyaache kwanza…’nikasema

‘Haya, ninayokuuliza....ni moja ya sababu ya kuchanganyikiwa kwa mumeo, kuna mengine kati yako na yeye, usipoziba ufa utajenga ukuta, akipona akirudia tena, itakuwaje,..ni bora ujua cha kufanya kuanzia sasa..’akasema

‘Sawa baba nimekuelewa…’nikasema

‘Kuna maelezo muhimu humo, ila mengine..eeh yanafanyiwa kazi, ikithibitishwa kuwa ni kweli…unajua ni nini kitafuta,…maana tulishakubaliana hilo, na sitarudi nyuma tena, unanielewa…?’ akauliza nakabla sijamjibu akasema

‘Nilikuambia na narudia tena,…kunguru hafugiki, sasa yanaanza kujitokeza, usizarau maneno ya wazee wako, ukataka kushindana nao, sasa ni lako hili, ila lisiharibu familia yangu kwa ujumla, sitarudia tena hili…’akasema

Hapo nikabakia kimia tu…nikiwa nimeishikilia ile bahasha kubwa mkononi.

‘Mume wako, ….kabla niliwahi kuongea naye, nikamwambia nikirudi nahitajia majibu na maelezo…. sasa sijui ni sababu hiyo au kuna jambo jingine, nahisi pia kuna jambo jingine limejitokeza…ila ninachotaka isije ikawa ni kashfa kwenye familia…sitavumilia hilo kabisa…’akasema.

‘Sawa baba, nina imani hiyo, kuwa hakuna kashfa mbaya….’nikasema

‘Na iwe hivyo, na iwe-hivyo,….’akasema akiangalia saa

‘Sawa baba, niamini mimi…hakuna jambo baya …’nikasema

‘Na huyo rafiki yako, unamuamini sana eeh…’akaniuliza

‘Yupi baba…?’ nikauliza

‘Huyo mzazi….’akasema na mimi hapo moyo ukalipuka paah.

‘Baba huyo ana nini tena…’nikasema

‘Najua unamtetea sana,…, niliwahi kukuambia, unachokifanya wewe, ni kama kufuga nyoka mwenye sumu chumbani kwako, ipo siku atakuuma wewe mwenyewe, sikiliza binti,  huwezi kumbadili mtu aliyeshindikana na wazazi wake, hu-we-zi, umepanda mbegu juu ya jiwe…’akasema

Hapo nikakaa kimia,… nilikawa nawaza mbali kuwa huenda  docta ndiye anafanya kazi na baba, anachukua kwangu anayapeleka kwa baba, na hili la rafiki yangu inaokena limekwenda mbali, litanisumbua sana, sasa nitafanya nini…lakini moyoni, nikajipa imani kuwa nitalimaliza mimi na huyo rafiki yangu..sizani kama kuna jambo kubwa kiasi hicho.

‘Huyo rafiki yako, ndiye atakayekuangamiza,..unajua kuwa yeye anashirikiana na mume wako…?’akasema kama ananiuliza, na mimi hapo nikamwangalia baba yangu kwa macho ya mshangao, ila sikuwa nimemuelewa ana maana gani hapo…

‘Anashirikiana na mume wangu, kwenye nini baba, hapana, ni kawaida tu….!!’nikasema kwa mshangao.

‘Una uhakika…’akauliza na mimi nikakaa kimia

‘Ndio maana nakuambia…kuna tatizo, na tatizo hilo linaweza kuleta taswira mbaya kwenye familia, na …narudia tena sitaki kashfa mbaya kwenye familia yangu, muuguze mume wako apone,…na apone kweli, maana sitarudia tena. ….’akasema na kuondoka.


************

Huyo-huyo rafiki yako, ndiye atakayekuangamiza, akishirikiana na mume wako…’ ilikuwa sauti iliyokuwa imebakia akilini mwangu, na kunifanya niduwae kwa muda, hadi pale nilipohisi mtu kunikaribia.

Nikainua kichwa kuangalia ni nani huyo, …alikuwa ni docta.

‘Vipi, mwenzako ndio keshaondoka….?’ Akaniuliza docta

‘Wewe ulikuwa wapi..?’ nikamuuliza swali kabla sijajibu swali

‘Unajua nilimuona docta kwa mbali, akitoka, nikaamua kumkimbilia kumuwahi kabla hajaondoka, kwahiyo sikuweza kuwaambia,…na kweli alikuwa akitoka, ,…na  nimeweza kuongea naye na kwenda kumuangalia mume wako, bado amelala, ila yupo sawa, hana tatizo….’akasema

‘Kwahiyo mimi siwezi kwenda kumuona…?’ nikauliza

‘Kwa mujibu wa dakitari, ndio huwezi kwenda kumuona, kwa vile anatakiwa kulala ili dawa zifanye kazi....ila unaweza kwenda kumuona tu, kwa mbali, kama unataka, muhimu usije kumghasi, mpaka hapo atakapozindukana kutoka usingizini yeye mwenyewe, …’akasema

‘Oh….hata hivyo, ni bora nikamuone tu…’nikasema

‘Sawa twende….’akaanza kutembea kuelekea huko alipolazwa mume wangu, na mimi nikawa namfuatilia kwa nyuma hadi chumba alicholazwa mume wangu, alikuwa kweli kalala, ..nilimuangalia kwa muda, na kuhis machozi yakinilenga lenga, akilini sikuwa na wazo jingine zaidi ya kumuombea apone haraka iwezekanavyo.

‘Haya umemuona, …twende maana tumejiiba tu, haitakiwi mtu kuja kumghasi, mpaka wakija kuhakikisha kuwa sasa hana maumivu tena….’akasema, lakini nilikuwa kama simsikii, hadi pale aliponishika mkono na kunivuta tuondoke humo ndani.

‘Mume wangu jamani…’nikasema

‘Atapona ….’akasema docta

*********

 Tulipokuwa nje, docta akaniuliza;

‘Kwanini rafiki yako kaondoka kwa haraka hivyo, tuiliongea nini na wewe umafanya nini, ..kuna kitu gani mnataka kukificha, mimi, eeh...nilikuwa nataka kuongea naye maswala mengine….’akasema.

‘Ulitaka kumuona mtoto ili utake kuthibitisha uvumi na hisia zako, au…ndio keshaondoka hivyo, ..’nikasema.

‘Haya sawa, hamna shida, unaonaje sasa twende nyumbani,…maana kwa hivi sasa utakaa tu, na kwa mahesabu yao, mgonjwa ataamuka baada ya kama masaa manne hivi,…chini au juu ya hapo… na akiamuka watamchunguza kwanza..ili kuhakikisha kama yupo sawa kabla hawajawaruhusu watu kuongea naye, ….’akasema

‘Sawa…’nikasema hivyo tu, na tukatoka hadi tulipoweka magari yetu, kila mmoja akaingia kwenye gari lake na ikawa ni safari ya kurudi nyumbani. Na sikutaka kabisa kusimama kwa docta, moja kwa moja nikaelekea nyumbani kwangu. Nilipofika kwangu,  kwa haraka nikampigia simu rafiki yangu.

Kwanza simu iliita kwa muda bila kupokelewa, …nikatulia dakika moja hivi nikapiga tena, ikawa hivyo hivyo,…lakini wakati inataka kukatika, ndio ikapokelewa, na mimi nikamuuliza mdada, kwa haraka ni kwanini hapokei simu anajua namuitia nini.., yeye akajibu kwa haraka tu;

‘Nilikuwa naanika nguo za mtoto nje, sikuweza kusikia simu ikiita, na wakati naingia ndio nikasikia ikiita, nikaiwahi, habari za mgonjwa, kuna lolote jipya tangia tuachane….?’akasema na kuniuliza.

‘Vipi umefikia wapi, au umeamuaje..?’ nikamuuliza , bila kujibu swali lake

‘Mhh…nimeongea na watu wa usalama barabarani kujua kinachoendelea kwanza, wamenipa picha halisi ya ajali yenyewe,…nilikuwa sijaipata hiyo, zaidi ya kusikia kwa watu, sasa nimeweza kujua ajali ilivyotokea…zaidi ni mwendo kasi na wakati anakata kona kuingie ile bara bara nyingine ndio wakakutana na lori, …kiukweli ni ajali mbaya…’akasema

‘Ndio hivyo, …kwahiyo umeshaianza hiyo kazi…au..?’nikamuuliza

‘Ndio nimeianza hivyo…bo-si’akasema na kumalizia neno la mwisho kwa kukata

‘Najua umetoka kujifungua na ulihitajia muda wa kupumzika, hilo nalifahamu sana, na sikuona kama kazi hii ina uzito wa kukufanya ushindwe kuifanya kutokana na hiyo hali,…’nikasema, na nilisikia mlio wa simu kuingia, sijui ni ya kwake au ni yangu

‘Nitaangalia….’akasema, nahisi alitaka kukata simu.

‘Mimi nionavyo, ni kazi unayoweza kuifanya hata bila ya kutumia nguvu, kwani wewe una vyanzo vyako vingi vya kukusaidia bila ya hata ya wewe kutoka hapo nyumbani kwako..'nikasema

'Sawa...'akasema

'Cha..., muhimu ni kuhakikisha kabla hawajafanikiwa watu wengine kujenga hoja za fitina, uwe umeshajua ni nini kinachoendelea, na je umeshaweka mikakati yako tayari...?’ nikamuuliza, nikasikia mlio wa kuingia ujumbe nahisi ni simu yake.

 ‘Sawa nimekuelewa …’akatulia kwa muda, halafu akasema

‘Bosi…, nafahamu nipo kwenye mkataba na wewe, na niwajibu wangu kutimiza kila utakachoniambia, lakini nilitaka nikuweke wazi, kabla ya kazi yenyewe ndio maana uliniona nasita sita...’akasema sasa kwa sauti ya kujiamini kidogo.

‘Kwahiyo umeshaelewa, au bado unasita sita, …’nikasema

‘Nitafanya kama utakavyo, hamna shida…na nilimuona baba yako, hapo hospitalini,....mliongea nini na yeye au…?’ akaniuliza.

‘Ni mambo ya baba na binti yake, ..ni yale yale…yeye hawezi kunizuia mimi nisifanye kazi yangu, ila kuna jambo..ndio maana nataka ulifanyie kazi, kabla mambo hayajawa mabaya ....’nikasema

‘Sawa..nitaifanya tu, hamna shida… ila nami unielewe, ndio nimetoka kujifungua, kitoto changu bado kichanga, hali yangu bado haijawa safi, nahitajia muda wa kutulia kwanza, nahitaji muda wa kukaa na mwanangu na pia nipo kwenye maandalizi ya ile safari ya kwenda nje kusoma, kwahiyo huenda nisiifanye hiyo kazi kwa muda unaotaka wewe,.....’akasema rafiki yangu huyo.


‘Hamna shida, mimi naelewa hilo….ila fanya uwezevyo, kabla wengine hawajagundua lolote, kama kuna kashfa ya mume wangu nataka niifahamu mapema ni kashafa gani, na …mengine nitayafanyia kazi mimi mwenyewe …’nikasema

‘Hamna shida, nitafanya hivyo…bosi…’akasema kwa kujiamini.

Ndio hapo nikakumbuka ile bahasha,..

‘Haya badae nitakupigia…’nikasema na kukata simu.

 Nikakumbuka kuwa sikuichukua ile bahasha kwenye gari, haraka haraka hizi bwana, na mawazo mengi kichwani,….nikatoka hadi kwenye gari, ..nakumbuka niliiweka kwenye kiti cha mbele, kwanza nikawasha kiwambo cha gari ile niweze kufungua mlango,..kwa haraka nikafungua mlango,

Hakuna kitu…! Bahasha haipo….!

‘Haiwezekani…’nikasema nikikagua kila mahali, na kujaribu kuvuta hisia za kumbukumbu yangu kuwa labda niliondoka nayo, …hakuna kitu….

‘Nina uhakika sikuondoka nayo!..ilikuwa hapa..’nikasema mwenyewe.

Mara simu yangu ikaita,…nikaangalia, alikuwa ni docta

‘Unasemaje , una mzigo wangu…?’ nikajikuta namuuliza hivyo kwa haraka.

‘Mzigo gani…?! ‘akauliza kwa mshangao, halafu akaendelea kusema

‘Nataka kukuambia hivi, wakati tunakuja,…nikiwa nyumba yako, ..niliona kama kuna mtu alikuwa akikufuatilia kwa pikipiki,…hukumuona…?’ akauliza

‘Hapana…sikuwa makini kukagua nje. Mbona zilikuwa pikipiki nyingi tu, una uhakika ….ni nani…?’ nikasema na kuuliza

‘Lakini sizani kama alikuwa na nia mbaya, mimi nilipoona kapitiliza ulipokuwa unaingia kwako, nikajua labda ni hisia zangu tu, kuna lolote limetokea…?’ akaniuliza

‘Huyo mtu aliishia wapi, hakuingia kwangu…?’ nikamuuliza

‘Alipitiliza, hakusimama, sikumuona akisimama,..kwani kuna tatizo…?’ akauliza

‘Hakuna tatizo,..ila…lakini sina uhakika, kuna kitu wamechukua kwenye gari langu…’nikasema

‘Haiwezekani, muda gani sasa huo..! Ina maana labda,… alirudi akaingia kwako, maana mimi nilipoona kapitiliza, niliingia kwangu, siwezi kujua kama alirudi au laa..hakuna mtu hapo nje kwako unaweza kumuulizia…?’ akasema

‘Hamna shida, sio kitu muhimu sana…’nikasema

‘Kama wamehangaika kukichukua, kitakuwa muhimu kwao..jaribu kufanya uchunguzi…na kama unahitajia msaada wangu niambi..’akasema, na mimi nikakata simu,

Nilipokata simu kuongea na docta,nikatoka nje na kukagua..sikuona dalili ya mtu, hata gari,…sikuona dalili kuwa mtu alilifungua, kwa vipi lakini…nikataka kumpigia rafiki yangu simu, yeye ndiye msaada wangu wa vitu kama hivi, lakini kabla sijaanza kupiga simu, simu ikaanza kuita, ….alikuwa ni baba!

NB: mambo ni mengi lakini tutafika tu


WAZO LA LEO:  Wahenga walisema hata mbuyu ilianza kama mchicha au mche wa harage ukichipua..Na hata matatizo, yana chanzo chake, kidogo kidogo huja kuwa tatizo kubwa, …nibora kuchukua tahadhari kabla tatizo halijawa kubwa, tusizarau matatizo, na kuyasubirisha , kama lawezekana kushughulikiwa lifanyie kazi haraka iwezekanavyo, ya leo yaweza yasiwe ya kesho.
Ni mimi: emu-three

No comments :