‘Docta ana mambo yake, ana shuku shuku
zake..mimi sijamuelewa, najua ni kwanini,…muhimu kwangu, wewe uifanye hiyo kazi
niliyokupa…sasa.., wewe ondoka ukaianze hiyo kazi mara moja, mengine niache
mimi na docta tutayamaliza…’
Tuendelee na kisa chetu….
***************
Docta alikuwa anakuja, akiwa kashikilia simu yake mkononi, kama
anaandika kitu kwenye simu yake, nahisi alikuwa akiongea na mtu fulani muhimu
kwake…kuna muda alikuwa akiongea huku anageuka kidogo kutuangalia, ikanipa
mashaka kuwa huyo anayeongea naye, anaweza akawa na jambo na sisi..lakini
sikuwa na shaka na hilo.
Niliona kamaliza kuongea na sasa alikuwa akija pale tulipokaa mimi
na rafiki yangu, lakini alikuwa
hatuangalii, anaangalia simu yake,.. na alipotukaribia tu ,simu yake ikaita
tena, ikabidi ageuka na kurudi pale alipokuwa awali, akaendelea kuongea na simu
yake, na kwa muda huo rafiki yangu alikuwa kasimama hajui afanye nini,…
‘Sasa wewe unasubiria nini, nenda kaifanye hiyo kazi, ukimsubiria
docta…akija hapa, ataanza kukudodosa, kwa maswali mengi ya ujanja ujanja…na
lengo lake jingine anataka kumuona mtoto, nahisi kuna jambo analifahamu, anataka
kulithibitisha,..au kuna jambo analifuatilia….’ nikasema hivyo.
‘Mhh,…ni kweli naondoka…ila mimi sijakuelewa hapo.., maana
unachotaka ni kama mtu kuchunguza kivuli chako, ni mambo ambayo hata wewe
mwenyewe unayafahamu,..’akasema
‘Nayafahamu kwa vipi, sijakuambia uchunguze mambo yetu, mimi
ninachotaka ni wewe kuchunguza hili tukio la mume wangu, chanzo chake, na ni
nini kipo nyuma ya haya yote, unajua…mimi sitaki mambo ya kusikia,..nataka
ukweli, nataka uhakika,..sawa hisia hizo zipo, watu wanasema hili na lile,
lakini mimi sio mtu wa kihivyo….nataka tuupate ukweli…’nikasema
‘Kwahiyo eeh, hili….’akasema na kabla hajamaliza, nikamkatiza kwa
kusema;
‘Sitaki nikufundishe kazi…. siku zote nikikuelekeza kazi unasema
nisikufundishe nimeshakupa kazi basi nikuachie wewe mwenyewe utajua jinsi gani
ya kuifanya,…iweje leo, kulikoni, unajua
naanza kukutilia mashaka,…’nikasema na yeye hapo akabakia kimia.
‘Katika jambo silitaki, ni kuwatilia mashaka watu wangu
ninaowaamini…wewe nakuamini sana, nilikupeleka shule usomee ujasiri, ujua jinsi
gani ya kujilinda, na uje kunisaidia na mimi, …unilinde kwa kila hali,
unakumbuka, uliapa mbele yangu, ndio, urafiki upo pale pale, lakini mengine ni
dhima, unanielewa hapo….’nikasema
‘Aaah,..ndio..naelewa…lakini kabla sijaifanya hii kazi, ni lazima
tukubaliane…eeh, kuna utata hapa…’akasema
‘Kukubaliana husu malipo au, kama ni malipo hakuna shida, toka
lini nikakupa kazi bila kukulipa, wewe angalia gharama zako nipatie ankara ya
deni,…au unataka kusema nini…?’
‘Kwahiyo, mmh, unataka nimchunguze shemeji….mmmh….’akasema
‘Ndio…umchunguze, …kwa masilahi yake, na masilahi ya familia,….fanya
ufanyalo, ila cha muhimu, nakuomba, na nasisitiza, mimi sitaki kashifa kwenye
familia yangu, ..na hili tumeshaonywa na wazazi wangu mara nyingi, hata wewe
uliwahi kusikia wakati baba akiongea, ..sasa kama kuna tatizo nataka tuliwahi
mapema kabla halijafika kwa wazazi wangu,...’nikasema
‘Nikuulize tu, samahani bosi… kabla sijaondoka, sasa kama ni
kweli mume wako kahusika na hicho unachokiita
kashfa,..itakuwaje…?’ akauliza na mimi nikamuangalia kwa macho makali, nikasema
‘Ninacho-kiita mimi kashfa..una maana gani, lugha gani hiyo…..ok,
sikiliza…mimi sitalivumilia kashfa yoyote kwenye familia yangu, hasa zile zenye
kuharibu biashara, zenye kuharibu ndoa, zenye kuleta jina baya kwenye familia
yangu, zote unazielewa..sitake nianza kuzitaja…’nikasema
‘Mhh…’akaguna hivyo.
‘Wazazi wangu unawafahamu walivyo, walinikataza nisioane na huyo
mume wangu kisa ni kuhusu familia yao, kuwa eti imegubikwa na mambo hayo…mimi
sikuamini hayo, najau tabia mtu anaijenga mwenyewe..mimi niliwahakikishia wazazi
wangu kuwa kashfa mbaya hataiweza kutokea kwenye familia yangu…’nikasema
‘Lakini kashfa yaweza kutafsiriwa vingine,..kama jambo limefanyika
kwa makubaliano linawezaje kuwa ni kashfa…muhimu tuliweke sawa,..kuna mambo
labda yalifanyika hivyo, sasa labda imekuwa kinyume kutokana na kutokuelewana…sasa
sizani ni kama ni kashfa, labda iwe ni kashafa kwa mtizamo wa watu wengine……’akasema
‘Kwa makubaliani!!! Weeeeh, makubaliano na nani..kuwa mimi
nitendewe ubaya, kwa vipi sasa, kuwa mume wangu, mbona haiji akilini… kuwa yeye
akazini nje ya ndoa au, tuchukulie kashfa hiyo ni ya ndoa, mimi sijui..yaani mimi,
nikae na mume wangu kuwa akafanye hivyo,…au nimwambie mume wangu akaibe
au..najua mume wangu hawezi kufanya hivyo, hata siku moja,..na mimi sio kichaa
wa kukubaliana na ujinga kama huo, hata dunia itanicheka au unataka kusema nini…’nikasema.
‘Sawa…lakini nikuulize kitu kingine kutokana na hali ya shemeji,
ukagundua kuwa kafanya hivyo, na hali kama hiyo, .. utachukua hatua gani, huoni
unaweza kumuua mume wako bure....?’ akaniuliza na mimi nikageuka kumuangalia
docta, alikuwa bado anaongea na simu, nikasema.
‘Kwanza tujue ukweli, unanielewa,, ....cha kufanya baada ya
ukweli.. , nitajua mimi mwenyewe, hiyo
sio kazi yako… ila kiukweli, kama ni kweli wanavyosema watu mimi bado siamini,…huyo
aliyemghilibu mume wangu, huyo shetani mtu…kama kweli kaghilibiwa, maana mume
wangu hakuwa na tabia hiyo,..huyo mtu, huyo shetani,,… nitahakikisha kuwa hanisahau maishani , na atajuta kuingilia ndoa
za watu kupoje…’nikasema kwa ukali, na uso wangu ukiwa sasa umebadilika kabisa,….
Mdada aliniangalia usoni, akionyesha wasiwasi mkubwa, mpaka, akawa
anarudi kinyume nyume..halafu akasimama ..rafiki yangu ni jasiri..alipitia mafunzo ya ujasiri,
kwahiyo anajua aweje kwa wakati gani…, lakini kwa hali aliyoniona nayo usoni nahisi
hakutarajia,…kabisa….
‘Ina maana utamuua au,…ha-ha- hata kama…?’ akaniuliza akionyesha
wasiwasi, akasita kumalizia.
‘Wewe subiria tu…utaona nitakachokifanya, unajua nimevumilia sana,
nimekuwa mtu wa watu, nawapenda sana watu wangu wa karibu, nawabeba kwa
mbereko....sasa ina maana kwa hali hiyo watu wanipande hadi kichwani, hapana,..hata
awe ni nani …’nikasema
‘Mhh, rafiki yangu siamini hili kabisa, lakini mume wako ni mtu
mwema sana, na kama kafikia kulifanya lolote baya, atakuwa na sababu…sizani
kama anaweza kufanya jambo ambalo analifahamu ni kinyume ..msamehe tu…’akasema
‘Nimsamehe nini sasa…kwanza, eeh, nisikilize, sio tukurupuke,
kwanza, tujue kosa lake ni lipi,…ili tujue jinsii ya kumsaidia,…unajua yapo makosa ya kusamehe, mimi ni binadamu,
nitayapima, …lakini sio kosa la kuingilia ndoa za watu…watu hao wanatakiwa
kuuwawa…unasikia, ku-uwawa, sasa mimi niwachekee, ndoa sio kitu cha mchezo
bibie…, ..’nikasema
‘Sikiliza…mimi naomba urejee yale mazungumzo yetu, mbona….’akasema
‘Mbona mbona nini…ile ni kitu kingine…najua unachotaka kukisema…ndio
maana nilikusihi iwe siri…sasa kama na wewe umelikoroga huko, acha mwenye mali
afanye kazi, yake utajua mwenyewe, na mimi natetea ndoa yangu…sasa nikuulize uUtaifanya
hiyo kazi au huwezi nimpatie mtu mwingine..’nikasema kikazi zaidi.
‘Mimi naona sitaiweza hiyo kazi, ..na ukizingatia nina mtoto, si
unajua tena….’akasema
‘Sikiliza, sitaki kusikia kauli hiyo…na nataka uifanye wewe….na
nataka iwe siri kubwa, unanielewa, siri kubwa, sitaki watu wengine waje kuligundua hilo kabla
yako, kuna watu wameshaanza kutaka kulifuatilia hilo tatizo la mume wangu, wanataka kujua kwanini mume wangu akawa hivyo,…hiyo
ajali sio ya kawaida,…wameshaanza kutunga hadithi…najua wakitaka jambo
watalipata tu…’nikasema
‘Akina nani hao…?’ akaniuliza akionyesha mashaka
‘Docta anataka na yeye kulichunguza kwa nia ya kumsaidia rafiki
yake, najua sio hivyo tu,…najua kabisa… wazazi wangu watakuwa wamemtuma kufanya
hivyo,…sasa sitaki aje kugundua kitu kabla ya yako, nataka wewe ukishagundua
tunahakikisha hakijulikani kitu tena…unanisikia, umeona jinsi gani jambo hilo
lilivyo nyeti,…umenielewa hapo…’nikasema
‘Mhh, mbona imekuwa ni tatizo, sikujua kuwa haya yote yanaweza
kutokea,…sasa huyu docta anataka kutafuta nini,…ina maana ndio maana umeniita
hapa, ili…na wazazi wako wanalifuatilia hili, mungu wangu …mimi sasa naanza
kuogopa, naona nijiondokee tu kwenda kusoma haraka iwezekanavyo, ….’akasema
sasa akirudi kinyume nyume
‘Sikiliza wewe ni rafiki yangu ninayekuamini, ndio maana kila kitu
tunaambizana, na huwa tunashauriana kwa kila jambo, sawa si sawa....wewe ndio
mimi, na wewe huwezi kufanya jambo la siri kinyume na makubaliano yetu, sizani
kama wewe unaweza kunigeuka mimi…nimekuwa nikikulinda kwa kila hali, mpaka
sasa.…’nikatulia
‘Ni kweli….’akasema sasa akiwa kainama chini kama mtoto mbele ya
wazazi wake akiwa kakosa au kuona aibu. Ni lazima awe hivyo kwangu mimi licha
ya urafiki lakini mimi nimekuwa kama mlezi, nilitumia gharama nyingi kumjenga
huyu binti kutoka kwenye hali ya kukata tamaa hadi akafikia sehemu ya
kujiamini..
***********
Rafiki yangu huyu, niliamua kumsaidia kutoka kwa wazazi
wake, hii ni kutokana na ule ukaribu wetu, sikutaka nimsaidie kipesa tu, lakini
pia kumjenga katika hali ambayo anaweza kufanya jambo lake kwa kujiamini.
Sisi kwenye familia yetu japokuwa tuna uwezo, lakini wazazi wetu
walifanya juhudi kubwa ya kutujenga kihali ambayo mtu anaweza kufanya jambo
bila kutegemea wazazi, walitujenga kujiajiri zaidi, pamoja na elimu yetu, na
mimi nikaona nimsaidie rafiki yangu awe hivyo hivyo...
Wazazi wake kuna kipindi walitaka binti yao aolewe na mtu
waliyeona kuwa atamfaa, na binti yao hakuwa tayari naye, kama alivyokuwa hayupo
tayari kwa wanaume wengi waliomtaka kumuoa kabla ya huyo ambaye wazazi wake, waliamua
kumshurutisha aolewe naye...ndio maana tatizo lake nikalichukulia sawa na la
kwangu..kuwa hata mimi nilikataa kuolewa na chagua la wazazi wangu
‘Hawa wazazi wangu siwaelewi, kama wamenichoka, na huenda wanaona
mimi ni mzigo kwao, waniambie, lakini sio kunitafutia mwanaume,....hivi
wananionaje mimi, eti niolewe na yule mzee, ..eti kwa vile ni tajiri,
....hapana, siwezi kuishi na yule mzee, hata siku moja....’akaniambia.
‘Lakini yule sio mzee,ukiangalai umri wako na yeye, huwezi kumuita
yule mzee, yule ni saizi yako kabisa, au unataka kuolewa na dogodogo,
usidanganyike, huko umeshakupita, sio kwako tena, huyo unayemuona ni mzee,
ndiye saizi yako...’nikamshauri.
‘Simpendi, na simtaki....’akasema na mimi nikamuelewa, nikaona
nimsaidie na nione vipi nitaweza kumfanya aishi maisha bila ya kutegemea wazazi
wake, , kwani kwa muda huo alikuwa ameshakosana na wazazi wake kabisa..na wazazi wake, walisema kuwa binti
yao huyo kazidi kwani kila mchumba anayemfuata yeye anamkataa,
‘Basi rafiki yangu mimi naona nikusaidie kwa hilo, unaonaje tukiwa
washirika, ....?’ nikamuuliza.
‘Washirika kwa vipi, sisi ni marafiki tangia zamani, hilo la
ushirika la kitu gani tena,…?’ akauliza.
Mimi namfahamu sana rafiki yangu huyo , hawezi kupata kazi ya
kuajiriwa akatulia, sizani kama anaweza kuhimili sheria na taratibu za kazi,
mara ngapi anaajiriwa na baada ya hata mwezi kuisha keshakosana na muajiri
wake,...nikataka nimbadili kabisa aondokane na hulika hiyo, japokuwa hiyo ya
kuchagua wanaume nilishindwa.
Nakumbuka wakati tunasoma rafiki yangu huyu alikuwa akipenda sana
kazi za upelelezi, kutokana na kusoma vitabu mbali mbali vya hadithi za
kipelelezi, na kuangalia sinema za namna hiyo,na hiyo ilikuwa ni ndoto yake
kuwa akimaliza shule atajiunga na kazi za upelelezi.
Kwa bahati mbaya, ndoto yake hiyo haikuweza kufanikiwa,
tulipomaliza shule, akajikuta akifanya kazi nyingine kutokana na matakwa ya
wazazi wake, ambazo hakuweza kuzifanya itakiwavyo, akaanza kutafuta sehemu
nyingine, na hata huko hakuweza kukaa muda mrefu,ikawa mtu wa kubadili kazi,
mara leo yupo hapa , kesho yupo kule.
Basi siku hiyo alipokuja kwangu na malalamiko hayo juu ya wazazi
wake, kutaka aolewe, mimi nikakumbuka ile ndoto yake hiyo, nikaona kwa vile
tumekuwa watu wakusaidiana, kupendana, toka utotoni, ngoja na mimi nijaribu
kumsaidia nionavyo mimi, na ndipo nikamapa wazo langu hilo nikamwambia;
‘Rafiki yangu mimi nataka kuifufua ile ndoyo yako ya shuleni, upo
tayari....?’nikamwambia na yeye akawa kama hakunisikia,kwani wakati huo alikuwa
anacheza na simu yake, nafikiri alikuwa akiandika ujumbe kwa watu wake, na
baadaye akasema;
‘Ndoto ipi...?’ akaniuliza kwa dharau, na huku akiendelea
kuangalia simu yake.
‘Kwanza rafiki yangu nakutaka unielewe, nikiongea na wewe
uhakikishe kweli unaongea na mimi, ....kama bado una tabia za utoto, hutafika
mbali, weka hiyo simu pembeni, nataka tuongee kikubwa....’nikasema kwa sauti ya
ukali, na yeye aliponiangalia usoni akakutana na uso wa kazi, uso unaoashiria
amri, akashangaa, kwanza, halafu akabetua mdomo, na kusema.
‘Ok. Bosi, maana kwa vile wewe ni bosi kwenye kampuni zako
unafikiria kila mtu utamsimamia hivyo hivyo..lakini kwa vile nimekwama,
nitakusikiliza bosi....’akasema huku akiiweka simu yake pembeni.
‘Nakumbuka wewe ulikuwa na ndoto ya kuwa askari mpelelezi...lakini
haikuwezekana, sasa nataka hilo liwezekane, hujachelewa, utakwenda kusomea
hilo, lakini sio askari mpelelezi wa kipolisi, nataka uwe mpelelezi wa watu
binafsi,...mpelelezi muhutasi, hiyo si inawezekana...?’ nikamuuliza. Na
yeye kwanza akawa kama haamini hilo kwani muda umeshapita, na huenda hakuwa na
wazo hilo tena.
‘Mhh, hilo nilishalitoa akilini, hayo yalikuwa ya kishule,
...sijui kama inawezekana, sina uhakika na hilo.na hiyo kazi inapatika kweli,
maana nahisi nitahitajika kwenda jeshini, na huu mwili sizani kama utakubali
shuruba, na amri.....’akasema.
‘Inawekana,....kwanini isiwezekane, kila kitu ni nia, kila kitu ni
utashi, na dhamira ya kweli, sasa hivi vipo vyuo vingi tu vya kutoa hayo
mafunzo, na hata kwenye mitandao kuna elimu kama hiyo, tuifanyie kazi, ...na na
kwa vile mimi nakuhitajia kwenye mambo yangu,...tushirikiane, tutaweza...upo
tayari....?’nikamuuliza.
‘Sijui...tuone ,..’akasema na mimi nikafahamu kuwa yupo tayari,
nikamwambia ili aonyeshe dhamira ya kweli, basi ahangaike mwenyewe kuvitafuta
hivyo vyuo, na mimi nitamsaidia kwa hali na mali. Na kweli baada ya siku kadhaa
akasema keshapata chuo cha namna hiyo, na yupo tayari kwa masomo, na mimi
nikamwambia nitawasiliana na wahusika wa hicho chuo.
‘Kwani ni mpaka wewe uwasiliane nao, cha muhimu ni maombi, na
maombi nimeshatuma na wao wameshanikubali, kilichobakia na malipo..hakuna
zaidi....’akasema.
‘Usijali..malipo nitalipa, lakini kama nilivyokuambia, mafunzo
hayo ni kwa ajili ya kazi zangu, kwahiyo nataka niongee nao, nione jinsi gani
wanaweza kukupika nitakavyo mimi....’nikasema na kweli nikaenda kuonana na
wahusika wa hicho chuo, na tutakakubaliana, kwani nilitaka kwanza wamjenge huyo
binti kikakamavu, na kuondoa ulegelege wa kutegemea wazazi,..na wao wakasema
hiyo kwao ni kazi ndogo tu.
Sikuamini, huenda ni kwa vile, alikuwa na ndoto hiyo, au ni
dhamira tu, ilimtuma ajitume hivyo, kwani, aliweza, na akafuzu vizuri sana, na
kuna muda aliombwa ajiunge na askari polisi, lakini yeye mwenyewe alikataa, na
akaja kwangu na kusema yupo tayari kwa kazi zangu, na tukaingia naye mkataba,
akawa ni mtu wangu nikimuhitajia, lakini hapo hapo akawa kaajiriwa kwenye kazi
fulani.
Nikawa kila nikipata kazi inayohitajia mambo hayo, nimampa
ananifanyia, namlipa vizuri tu, au wakati mwingine anapata kazi zake nyingine
binafsi akikutana na mawakili binafsi kuchunguza kesi fulani, basi ikawa ndio
kazi yake nje ya ajira yake.
Kwa hali kama hiyo tukawa ni kitu kimoja, na kikazi mimi ni bosi
wake, na haikutokea siku nikampa kazi,
akaikataa,...
Kwahiyo ni mtu nilishibana naye, na ananiheshimu mimi na familia
yangu, na alishaapa kuwa hataweza kunifanyia jambo baya,…je kwa hali kama hiyo
ninaweza kuamini mambo ya kusikia tu…hapana, ilihitajia mud asana kuyaamini
maneno ya watu
****************
‘Kwahiyo umenielewa, nikamuuliza , wakato docta naye anaongea na
simu
‘Nitafanyaje sasa..inabidi…’akasema
‘Unajua ni kwanini nataka hili, ni ili jamii isije kuniona mimi mjinga, kuwa nafuga
nyoka,…hilo linawezekana kweli, kuwa nilifanya yote hayo kwa mtu ambaye atakuja
kunizunguka, …’nikasema
‘Lakini…..’akataka kujitetea
‘Sikiliza…mimi sitakubaliana na mawazo yao hata mara moja kuwa
wewe rafiki yangu unaweza kunisaliti mimi, nitauweka wapi uso wangu…sasa ni
wewe kuilinda hiyo hali, sizani kama unaweza kufanya jambo kama hilo…sizani, …au
..niambie ukweli hapa hapa, je ni kweli…?’ nikamuuliza
‘Mim naondoka….’akasema sasa
akitikisa kichwa cha kuchanganyikiwa.
‘Sawa, mimi nakuamini, na..unasikia, …mimi nimeosha mikono yangu, nimechukua
dhamana yako mikononi mwangu.., na wewe usije kuniangusha kwa hilo,…umenielewa
lakini, na nataka hata wazazi wangu ikiwezekana wasijue kuwa mume wangu kapatwa
na ajali, nataka tufanye namna ambayo, sawa ni ajali, lakini kwa mazingira
yasiyo kuwa na kashfa, sawa..umenielewa hapo..?’ nikamuuliza
Nilimuona kama anataka kutoa machozi, lakini mimi sikujali,..najua
sio mtu wa kutoa machozi, labda kitu kimemuingia machoni,…na muda huo nilikuwa
kikazi zaidi, sikutaka kupoteza muda,
nilitaka yeye aifanye hiyo kazi, na nione ukweli wake kupitia kwake yeye
mwenyewe…., nilikuwa na maana yangu kubwa tu.
‘Ninataka wewe….uifanye hiyo kazi, sitaki utani, nataka tumfahamu
huyo mtu, ni nani anaweza kuingilia ndoa yangu, au kama kuna jingine, tulijue
mapema…, kwanini mume wangu awe hivyo…hapo kuna mawili, kashfa ya ndoa, au…kuna
tatizo kazini, mimi sijui, wewe ni mtaalamu wa mambo hayo, sasa mimi nahitaji msaada wako, hii ni kazi nimekupa…’nikasema
kwa hasira
‘Mimi naondoka….’akasema sasa akitaka kuondoka
‘Ondoka bwana,… mimi naondoka, mimi naondoka…ila kumbuka mimi…sitaki
utani, …unanielewa, sitaki utani kwenye ndoa yangu kwenye kazi yangu, kwenye
maisha yangu…ole wake huyo mtu, sitajali ni nani…hili nakuambia wewe kama
rafiki yangu, ukisikia mimi nimefanya jambo, hutaamini….’nikasema kwa jaziba.
‘Sawa bosi....naondoka…’akageuka na nikahisi kuna mtu nyuma yangu nikageuka
kwa haraka, nikiwa sasa naangalina uso kwa uso na baba yangu mzazi.
‘Baba…….’nikasema kwa mshangao mkubwa, wenye wasiwasi,
‘Kuna nini kimetokea…?’ ilikuwa sauti ya baba ya kiaskari
WAO LA LEO: Mara
nyingi tunapokuwa na shida, tunasahau kuwa wenzetu pia na wao wana shida kama
hizo za kwetu au huenda shida zao ni zaidi ya shida zetu, wakati huo wa shida,
hatujali shida za wenzetuo,cha muhimu kwa wakati huo ni shida zetu,
tunachotamani ni jinsi gani ya kusaidiwa, ni jinsi gani, shida zetu
zitachukuliwa kipaumbele, na hapo utaanza kuwachuja marafiki zako, na rafiki
utakayemuona ni wa kweli kwako ni yule atakayesimama kwenye shida zako, na
kutetea hoja zako.
Tukumbuke kuwa,sisi sote ni wanadamu, na shida zimeumbiwa
kwetu, na kwahiyo sote ni wahitajia,kama ni hivyo basi, ili tuwe sawa,
tujaribu kuona shida za wenzetu zina umhimu sawa sawa na shida zetu.
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment