‘Kakupigia nani,…rafiki yangu…?’ nikamuuliza
Na docta akaikata ile simu,
…haikuipokea ikanifanya niwe na mashaka, ni kwanini docta hakutaka kuipokea
nikiwemo.
‘Ni kwanini unaikata hiyo simu…ni kwanini hutaki kuongea na
yeye,labda anahitajia huduma yako ya kidakitari..?’nikauliza.
‘Hapana , tokea jana anataka kuongea na mimi, ..siwezi kuongea na
yeye mpaka nimalizane na wewe…’akasema.
‘Sijakuelewa hapo,…kuna nini kinachoendelea kati yako na rafiki
yangu, ..?’ nikamuuliza.
‘Kiukweli,…sijui…alinipigia simu, akasema nikipata muda, anataka
tuongee mimi na yeye, nikamuuliza kuhusu nini, akasema ni maswali ambayo hataki
kuyaongelea kwenye simu,…nikamuuliza je yanahusu mtoto, au yeye, akasema
mtoto….nikamwambia mimi nipo likizo, akasema hahitaji kuongea kiofisi…’akasema
‘Unahisi anakuhitajia nini…?’nikamuuliza.
‘Yeye anafahamu wewe ni rafiki yangu, nahisi ..yale yale
ninayotakakujua kutoka kwako, huenda anataka kuyafunika, kinamna.. au…..’akasema
‘Mimi siwezi kukuelewa kabisa, wewe una hisia zako mbaya dhidi ya rafiki
yangu au hebu nikuulize kwanini unawazia hivyo…?’ akaniuliza
‘Kuwazia hivyo kuhusu nini…?’ akaniuliza
‘Kuwa huenda huyo mtu aliyekuja wakati nipo kwa rafiki yangu
anaweza akawa ni mume wangu, kwanini, rafiki yako unamuhisi vibaya, kwanini
lakini..?’ nikamuuliza
‘Kwanza tukubaliane, upo tayari tusaidiane kwa hili, la kumtafuta
huyo mtu ni nani, au kumtafuta mwanaume aliyezaa na rafiki yako ni nani, na
tuyafanye hayo kwa nia njema kabisa, sio kwa ubaya…?’ akaniuliza
‘Halafu ukishamfahamu,…?’ nikamuuliza
‘Tutakuwa tumemaliza tatizo, sasa itabakia kuona jinsi gani ya
maisha yaendelee..nina imani wewe utakuwa huru,..hutahangaika tena, na mume
wako atapona haraka….’akasema
*****************
‘Kwahiyo unatakaje hivi…?’ nikamuuliza
‘Ninachotaka mimi, ni wewe kuwa muwazi, uwe mkweli, ….’akasema
‘Kama hayo yatamsaidia mume wangu sawa, nitafurahi sana, lakini
kunisaidia mimi, sijui unataka kunisaidia nini hapo, sijakuambia kuwa nina
tatizo…?’ nikauliza
‘Nina imani yote yanaendana…kwanza tuanze hivi,..kwanini mume wako
akawa mlevi hivyo wakati awali hakuwa hivyo, naomba unijibu kwa uwazi, ili
tufike kunakotakiwa…?’ akaniuliza
‘Kiukweli, labda nijenge hisia tu…mume wangu kuna kipindi
tulijadili kuwa tuzae, tupate watoto, na wazo lake kubwa ni kupata mtoto wa
kiume, sijui kwanini analihitajia hilo sana…’nikasema
‘Ikawaje…mjadala huo uliishia wapi…au wewe ulisemaje..?’
akaniuliza
‘Nilimshauri kuwa hilo lisiwe kipaumbele chetu kwanza, kwasababu tupo
kwenye harakati za kujiimarisha kiuchumi, lisubirie, akadai kuwa yeye
anahitajia watoto mapema iwezekanavyo, ..hataki kuja kuzaa uzeeni…’nikasema
‘Huoni kuwa ana ukweli fulani
hapo, kama wewe ulivyomshauri rafiki yako kuwa azae mapema, mbona wewe
hukujiangalia au kuna tofauti kati yako na rafiki yako, unajiamini vipi hapo
..?’ akuliza
‘Tofauti yangu na rafiki yangu ni kuwa mimi nina mume na muda
wowote nikihitajia kuzaa, kabla sijafikia ukomo, nitazaa kwa majaliwa ya mungu offcourse , lakini yeye mpaka ahangaike
kumpata mwanaume na zaidi anayemtaka yeye, pili awe na uhakika wa ..…na huenda
katika kulifanya hilo ikachukua muda, na jinsi gani ya maelewano a huyo
mwanaume…’akasema
‘Kwahiyo ukamshauri akazae vipi hapo…?’ akauliza docta
‘Hilo la kuzaa vipi au na nani, nilimuachia yeye mwenyewe,
sikutaka kumuingilia hayo…., si unajua alivyo, kwahiyo kama alizaa na nani, sio
muhimu sana kwangu, kama hakuna tatizo…’nikasema.
‘Kama hakuna tatizo, nahisi sasa kuna tatizo….ok, ..Je hukuwahi
kuongea kuwa azae na kundi gani, walio-oa, au wasio, oa…au azae baada ya
kufunga ndoa..najua hilo la kufunga ndoa lilikuwa ni gumu kwake, au sio, kwa
jinsi alivyojiwekea misimamo yake,…ya kuchagua chagua sana..sasa ulimshaurije
hapo?’ akaniuliza, kiukweli sikutaka kumwambia ukweli wa hicho tulichokubaliana
na rafiki yangu.
‘Nimeshakuambia hilo la kuzaa na nani, nilimuachia yeye mwenyewe, …’nikasema
na kukaa kimia.
‘Una uhakika?…anyway,
sasa hebu nikuulize, baada ya wazo hilo, ni kwanini asitafute wanaume ambao
hawajaoa…?’ akaniuliza
‘Aaah, mbona maswali yako ya kujirudia rudia, jibu nimeshakupatia,
na sijui alitafuta nani, sijui…’nikasema
‘Nasema hivyo nikiwa na maana. kiukweli mara nyingi huko nyumba alikuwa mbali
sana na wanaume za watu, lakini ghafla nikaja kumuona akiwa karibu na wanaume
wali-oa….au…mmm mlipanga iwe hivyo…?’akasema
‘Docta, mimi sina tabia ya kufuatilia maisha yake, kama wewe una
muda huo, mimi sina muda huo kabisa, ..kwahiyo sikujua ni nani na nani alikuwa
karibu naye…kama ni wewe au mwanaume mwingine yoyote…’nikasema
‘Au shemeji yake…’akasema docta na kunifanya nimtupie jicho
‘Shemeji yake..!!? Nani, mume wangu au…na wanini unamtaja yeye,
nilishakuambia yeye ni shemeji yake, na hata wakiwa naye, hakuna shida, ..na na…au
wewe unamshuku kuwa huenda ana
mahusianio ya siri na mume wangu…mbona unantia mashaka ambayo sikuwa nayo
kabisa..?’ nikamuuliza, nikimuangalia moja kwa moja usoni, na yeye akatabasamu
na kusema;
‘Sijamshuku,… ila nataka kuwa na uhakika, ili tuweze kumsaidia
mume wako…, nahisi mume wako ana tatizo kubwa, sasa ni tatizo gani, hilo mimi
kama rafiki yake linanisumbua kichwa sana, ....’akasema.
Na hapo tukakaa kimiya kwa muda, mimi akilini nikawa nawazia hiyo
kauli ya docta, kwanini ni kama anamshuku mume wangu, na nafahamu kuna muda
mwingi baada ya kazi wanakuwa naye..japokuwa sio sana
Nilimuangalia docta, …huku nikiendelea kuwaza,..labda, inawezekana kukawa na lolote kati ya rafiki
yangu na mume wangu, ..hapana hilo siwezi kabisa kuliamini, ...yule ni rafiki
yangu mpenzi nimemuweka kwenye kundi la ndugu, siwezi hata siku moja kumfikiria
vibaya, lakini huyu ni docta, na hana tabia mbaya, ni kwanini aliwazie hili, hapa
nikaingiwa na mashaka....
‘Shemeji huenda utaniona, kuwa naingilia ndoa yenu, huenda ukahisi
kwa vile nilikukosa wewe ndio maana najaribu kuona kila mlitendalo sio
jema,..au kama unavyodai wewe…, kuwa wazazi wako wamenituma, kufanya lolote ili
kuiharibu ndoa yenu, ..lakini kwanini tufanye hivyo..
‘Nikuulize wewe…’nikasema
‘Sio kweli, mimi nina nia njema kabisa na ndoa yenu, ndio maana
nilikuomba sana mapema tu, nilipoona rafiki yangu anabadilika, anakunwya
kupitiliza, nikakuomba sana ukae uongee
naye, wewe ukapuuzia, mimi nahisi mume wako ana kitu kinamsumbua...’akasema
‘Mimi bado hapo sijakuelewa, tuongee nini hasa kuhusu
starehe yake ya kulewa,..., mimi huko sina muda huo, kama kaona ni starehe yake
muache endelee..au wewe unahisi kuna tatizo gani jingine...,mimi ninaanza kuingiwa
na wasiwasi, kuna nini kutoka kwa rafiki yako ulichokiona kingine…,
niambie, mimi si rafiki yako unaogopa nini sasa…’nikasema
‘Hapana, mimi sijui kitu,..ningekuwa na uhakika ningelikuambia
mapema kabisa, ila ninachotaka mimi ni kujua ukweli…, nataka kuwa na uhakika,
na uhakika huo nitaupata zaidi kutokwa kwako, na akili yangu inanituma, kuwa
kuna kitu ambacho huenda kimesababishwa na mahusiano yenu wawili, wewe na mume
wako, na kikaenda hadi kwa rafiki yako, sasa ni kitu gani hicho…’akasema
‘Una maana mimi nimemfanya mume wangu atembee nje ya ndoa, …labda
kwa vile..si ndio hivyo…na aliyekwenda kutembea naye, au anayetembea naye ni
rafiki yangu, kisa kwa vile umewaona wakiwa naye karibu, au sio, na matokeo
yake ni huyo mtoto, au sio..niambie ukweli….’nikasema
‘Unaweza ukawa , haupo mbali na hisia zangu,…unanifahamu nilivyo,
mimi ni docta, au sio, siwezi kutibu ugonjwa bila kujua vipimo, ndio maana
natadadavua kuupta huo ukweli, na wewe hutaki kutoa ushirikiano…’akasema
‘Kwahiyo…unataka kunipima nini…niambie…’nikasema
‘Ukweli…nataka ukweli kutoka kwako…’akasema
‘Hebu niambie kuna nini kinachoendelea kati yako wewe na rafiki
yako, naanza kuhisi vibaya, kuwa huenda kuna jambo kalifanya, au kuna jambo
unalifahamu dhidi ya rafiki yako, labda mlishirikiana wewe na yeye, sasa wewe
unatafuta namna ya kujikosha kwangu, ili usionekane kuwa na wewe unahusika,
sasa ...niambie rafiki yako kafanya nini?’ nikamuuliza kwa ukali.
‘Shemeji siwezi kujua zaidi , ...yule ni rafiki yangu, lakini tuna
mipaka yetu, sio rafiki wa kujua kila kitu, kuna yake anayafanya mimi siwezi
kuyafahamu,..lakini naomba unielewe , mimi nilichokiona ni hiyo tabia yake ya
kunywa kupita kiasi, ilianza tu…nikamuuliza akasema kaamua tu, na unielewe sio kila siku ni kitoka jioni ninakuwa naye,
hapana. Hebu nikuulize je hajawahi kulala nje...?’
‘Kulala nje!!!..., hapana, hawezi kulala nje, kwanini alale nje,
wakati ana nyumbani yake, labda kuwe na sherehe ya kukesha huko kazini kwao,
hilo linatokea…, na hilo kwa siku hizi halijawahi kutokea, ...kuchelewa hilo
nalikubaliana au kurudi akiwa kalewa sana huwa inatokea, na yah, …kuna siku
alichelewa sana mpaka nikawa na mashaka, kama mara mbili tatu hivi…karudi
alifajiri....lakini yeye ni mtu mzima, ulitaka hapo nifanye nini mimi,
nijiumize kichwa na starehe za mtu, kaamua, tumuache, dunia itamfunza...’nikasema.
‘Na akiwa kalewa sana ni nani anamleta nyumbani kama mimi sipo
naye…, maana akilewa sana nikiwa naye, huwa mimi namleta mwenyewe, je kama
sipo, ni nani mwingine anapenda kumleta
nyumbani, maana hapo huwezi kunificha kuwa halewi kiasi cha kutokujitambua?’
akaniuliza.
‘Wewe unafahamu bwana, kuwa mara nyingi ni mdogo wake anayemleta,
huwa akiona kalewa kupitiliza kiasi cha
kutokujitambua, sijui kwanini mtu mzina kama huyo anafanya hivyo…mimi nijuavyo
kama haupo, anamuita mdogo wake, na mdogo wake, anafika hapo alipo anamchukua...’nikasema.
‘Kwahiyo …eeh, mdogo wake atakuwa anafahamu mengi kuhusu kaka yake
ambayo mimi siyafahamu, …sawa hapo eeh,.. umenipa wazo, jinsi ya kulifuatilia hili jambo, huyo ni mtu
mwingine anaweza kutusaidia, umeliona hilo hata wewe.....?’ akawa kama ananiuliza
‘Mmhh,…kuliona …!!Lakini nikuulize kwanza, ni kwanini unamshuku
rafiki yako, kaua, kafanya jambo gani baya sana, maana unavyouliza ni kama vile kuna kesi ya
mauaji,..., au hahaha, kufamaniwa, …hapana huyo sio mume wangu, …ka-kafanya
nini kikubwa hivyo, mbona hutaki kuniweka wazi?’ nikamuuliza.
‘Sijasema kuwa kafanya lolote baya, hilo uliweke akilini,
ninachotaka kukifanya hapa ni kutafuta kama kuna tatizo, ta-ti-zo ...je
huko kuendesha gari kwake kwa kasi huoni kuwa kuna kitu kilitokea akawa
anakimbia, au kuna jambo alikuwa akilifuatilia nyumbani kwa haraka, huenda
alikuwa anakuja kuku....’akakatisha
‘Unataka kusema alikuwa anakuja kutaka kunifumania au....acha hayo
mawazo hayo docta, wewe ni msomi bwana…na familia yangu ni ya watu wastaarabu,
hakuna mwenye tabia chafu kama hiyo...kama unayo wewe usifikirie kila mtu ana
tabia kama hiyo.’nikasema kwa hasira.
‘Hahaha…lakini, unanifahamu sana, nilivyo, lakini vyovyote iwavyo,
sote sisi ni wanadamu inaweza kutokea mtu akateleza, jua ibilisi mkubwa
wa mwanadamu ni mwanadamu .., huwezi jua,...hata wewe unaweza kughilibiwa
ukajikuta umefanya jambo ambalo baadaye linakuja kukuleta matatizo, ukawa
unatafuta njia ya kujisafisha, lakini wenzako wameshaliona na huenda wamekuweka
kati, dunia hii ina watu wabaya.....’akasema
‘Mpaka sasa sijakuelewa msingi wa maswali yako...unachokitafuta
hasa ni nini, kuwa mimi nina matatizo au mwenzangu ana matatizo?’ nikamuuliza.
‘Sijawa na uhakika na hilo ndio maana nakuuliza ...maana kama wewe
ungeliweka wazi, kuwa kuna tatizo, kwako au kwa mwenzako, ningejua jinsi gani
ya kufanya, na nini nifanye ili niweze kusaidia, lakini naona nyote
mnanificha, ndio maana najaribu kuwa mpelelezi, kwa nia njema kabisa
....’akasema.
‘Yatakushinda....siku hizi umeacha kazi yako ya udakitari unaanza
kufuatilia ndoa za watu, haya na ili upate faida gani...’nikasema na yeye
akaangalia saa yake, halafu akasema;
‘Kuna watu wawili wanaweza kutusaidia kwa hil tatizo , ...ili
kugundua kuwa huenda mwenzetu ana tatizo gani, hadi sasa kwa uoni wangu nimeona
kuwa kuna tatizo, sasa ni tatizo gani, ni muhimu sana tusaidiane kulitafuta
haraka iwezekanavyo kabla hali haijawa mbaya zaidi, ...’akasema.
‘Umeona kuwa kuna tatizo, umeona kuna tatizo gani,..kuwa huenda
ajali hiyo ilikuwa na msukumo fulani, si ndio maana yake hiyo, au..?’nikasema
kwa upole, kwani hapo niliona kuna hoja ya msingi.
‘Ndio ...hebu angalai hili bila kujali kuwa mimi ndiye
nalifuatilia, angalia kwa nia ya kumsaidia mwenzako, na hatimaye kuisaidia ndoa
yako, na urafiki wenu na huyo rafiki yako, huenda tatizo limeanzia kwako bila
kufahamu ...’akasema.
‘Nani na nani wanaweza kutusaidia sasa, maana hili naona
umelivalia njuga, na ukianzisha jambo lako mpaka upate majibu, haya ili
tuyamalize haya, ni nani anaweza kutusaidia, nataka uwe huru, kuwa unavyohisi
sio kweli, ni nani atatusaidia....?’ nikauliza na yeye akasogea karibu yangu,
na kusema kwa upole.
‘Wa kwanza ni mdogo wa mume wako, ....japokuwa kwenye ajali hiyo
hakuwepo , lakini nahisi anafahamu mengi kuhusu mienendo ya kaka yake....huyo
naweza kuongea naye mimi, naona uniachie mimi huyo mtu,..nitambana mpaka
atanieleza...’akasema
‘Sawa nakuachia wewe hilo…na mwingine au huyo anatosha…?’
nikamuuliza, hapo nilianza kuingiwa na mawazo , nikijiulia kweli ni kwanini
mume wangu aliendesha gari kwa mwendo huo, na ni kinyume na tabia yake, ...basi
kulikuwa na jambo, lakini mbona hata mimi niliendesha kwa mwendo
kasi,nilipopewa ujumbe huo kuja nyumbani haraka,kumbe inawezekana
ikatokea hivyo ..
‘Kama ni kujua kwanini alikuwa akiendesha kwa mwendo kasi, mimi
naona hakuna cha muhimu hapo, mbona hata mimi , leo nilijikuta nikiendesha kwa
mwendo kasi uliponipigia simu kuwa nije nyumbani kwa haraka, kwasababu
kuna tatizo huku nyumbani...na sikujua kabisa kuwa nilikuwa naendesha kwa
mwendo kasi.....’nikasema.
‘Unaonaeeh,wewe ulifanya hivyo kuja nyumbani kwasababu hiyo ya
msingi, je mume alifanya hivyo kwasababu gani ya msingi.., nikuulize swali ili
uone kuwa kuna tatizo, je mume wako ana tabia ya kuendesha gari kwa fujo,
hapana au sio namafahamu sana?’ akaniuliza.
‘Hana kabisa tabia hiyo, ndio maana nashindwa
kuelewa,.....’nikasema.
‘Unaonaeeh, sasa tunaanza kuwa pamoja..?’ akawa kama ananiuliza.
‘Ninaona nini hapo, kuwa pamoja kwa vipi, mimi nataka nifane
unavyotaka wewe, sawa, hisia zipo, na kiukweli sio kwamba sina hisia kama zako,
lakini nazipotezea, maana hao ni watu nawaamini, sasa kama kuna walakini, haya
ngoja tuutafute, sawa?’ nikamuuliza.
‘Ndio maana yake mimi nina imani kuwa mume wako alikuwa akikimbia tatizo,....maana
kama wewe huna tabia anayoihisi mume wako,...na alifahamu kuwa haupo nyumbani,
basi huenda alikuwa akikimbia jambo, sasa alikuwa akikimbia jambo gani, au
alikuwa akifuatilia jambo gani, ataulizwa hilo na watu wengi wakiwemo watu wa
usalama, bima nk......’akasema, na mimi hapo nikatulia kidogo nikiwaza.
‘Yawezekana ndio,…ndio maana hata hakutaka kwenda hospitalini...’nikasema.
‘Kwahiyo huyo mmoja, anatosha kutusaidia….?’ nikauliza
‘Mtu wa pili ambaye anaweza kutusaidia ni rafiki yako,
....’akasema.
‘Kwani vipi shemeji ....rafiki yangu anahusikanaje na mambo yangu
ya kifamilia..au ajali ya mume wangu, hapo ….ok, ok, ….lakini kama na yeye ni
muhusika, atanisaidiaje,, hebu niambie hapo,?’ nikamuuliza .
‘Akusaidie kujua kama anafahamu lolote, kuhusiana na mume wako, kama
kuna tatizo linalomsumbua, maana inawezekana mume wako yupo kwenye mtego wa
watu wanaomtishia amani, labda kama asipofanya hivi au vile anaweza akaingizwa
kwenye matatizo, ....nasema tu, kama mfano, ....'akasema
'Mhh, huko umekwenda mbali, rafiki yangu amrubuni mume wangu, na amwambie kuwa asipofanya hivyo, atafanya vile..kwanini..hapana, kwa maana hilo alilofanya rafiki yangu, tulishauriana mimi na yeye, sasa kwanini ...'nikasema
'Mlishauriana, ndio, lakini umesema, hkumshauri amtafute mume gani, au sio..je kama alimtafuta mume wako,...?' akaniuliza na kunifanya nishtuke
'Acha hayo maneno kabisa, usinichafue...hivi nikuulize kuna mtu anaweza kutembea na shemeji yake mwenye akili timamu, unazungumzia hapo rafiki yangu, unamfahamu kabisa alivyo, hapendii kabisa kutembea na wanaume za watu, ...usimzushie rafiki yangu uwongo....'nikasema
'Kuna kitu nataka tukihakiki...je wewe unaweza kufanya hivyo, kuongea na rafiki yako, au, nina wazo, hebu fanya hivi, unaweza
ukamuita rafiki yako , akaja hapa hospitalini, na ikiwezekana aje na mtoto wake, anaweza kuja, au sio..?’ akaniuliza.
‘Aje na mtoto, ...mhh, kwanini lakini, yupe bado ni mzazi, kwanini tumsumbue, atoke ahuko na mtoto kwanini lakini...na huyo mtoto wake unamuhitajia nini...hahaha nimeshakuelewa, unataka kufanya nini...hapana siwezo...’ akasema.
'Sikiliza...ni muhimu sana...fanya hivyo, kuna kitu nimekiona , fanya hivyo, muite rafiki yako aje hapa hospitalini,..na mtoto, ....unaweza kufanya hivyo...?' akasema
'Mhh.....' nikaishia kuguna, na sikuelewa kabisa docta anataka nini, lakini, ....
NB: Docta anataka nini hapa, …mtoto…mtoto wa nini…?
WAZO LA LEO: Urafiki wa kweli ni wa kujaliana,
mwenzako akipatwa na tatizo, iwe ni kama wewe umepetwa na tatizo hilo. Ni
faraja sana ukiwa na tatizo rafiki yako akawa anatafuta njia ya kukusaidia.
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment