Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Tuesday, October 10, 2017

MKUKU KWA NGURUWE-3



Kama nilivyokwisha kusema awali, rafiki yangu tulishibana sana, na tulijaliana sana, na hakuna angelipenda kufanya jambo kwa mwenzake ila liwe la heri na lisiwe la kumkwanza mwingine, tulichunga sana hilo, tokea tulipokuwa na akili…kwa hali hiyo tulichunga mipaka yetu kuhakikisha hatukwazani.

Na kwa upande wa mume wangu alikuwa mpole sana, hakupenda makuu, hakuwa na tabia mbaya , hakuwa mlevi, kuvuta sigara, au tabia za uhuni-uhuni, na alinijali sana na kuijali ndoa yake.  Sikuwa na wasiwasi kabisa na mume wangu, na usingeliweza kunidanganya kitu kuhusu mume wangu…na yeye hakupenda kufanya jambo linaloweza kunikera mimi au familia yake, alichunga sana hilo, ni mume wa pekee..ndio maana hata rafiki yangu alimuheshimu sana

‘Mume wako namuheshimu kama mkwe,  nampenda sana kwa tabia yake, yaonyesha kabisa hana tamaa, au tabia mbaya, na wanaume wa namna hii ni wachache saa,..unajua nikimuona mahali natamani asinione, sipendi, hali ya kuwa naye faragha, japokuwa ananisalimia vyema tu…na kuna kipindi ananialika chakula cha mchana, namkatalia

‘Kwanini unafanya hivyo, huoni atakufikiria vibaya, huyo ni shemeji yako, si zani kama mnaweza kufanya lolote baya…?’ nikamuliza rafiki yangu siku moja kipindi hicho nina uja uzito.

‘Hapana sitaki watu waje kusema lolote dhidi yetu, najua watu wanaweza kujenga fitina na urafiki wetu ukaja kuleta madoa, nachunga sana hilo…sisi tumetoka mbali,..na kama tulivyowahi kuambizana,  muhimu ni kuchunga  yale yote yanayoweza kuvuruga urafiki wetu, sitakufanyia chochote kibaya, nikijua kitakuja kukuumiza, ni bora nikafanye kwa wengine na sio kwako…’akasema

‘Usijali, mimi na wewe..sina shaka kwa hilo….mimi nafahamu hata kama itatokea mkalala chumba kimoja na mume wangu bado nina imani kuwa hutawezi kunisaliti, hahaha.’nikasema tukacheka.

‘Ni kweli…hahaha eti tulale chumba kimoja ina maana vyumba vya wageni havipo, tusifikie huko ..pa kujaribiana…’akasema

Mimi na rafiki yangu ilikuwa hivyo…

Nayaweka haya  bayana kwanza, ili uone tulivyokuwa tumeshibana na huyo rafiki yangu, kwahiyo kwa kutoa kwangu ushauri kama ule.., sikuwa nina mashaka yoyote na yeye, maana wengine watasema kwanini, ukamshauri mwenzako hivyo, wakati una mume, kwanini sikumshuku vibaya…na najua itakuwa hivyo…. aah,  nilimshauri rafiki yangu nikijua atafanya kile ambacho hakiwezi kuniumiza na atafanikiwa na hatimaye na yeye atakuwa na furaha,…

‘Sasa nilimshauri nini, hebu sikia ushauri wangu….

Tuendelee na kisa chetu…

*************

‘Kama ni hivyo, mimi sioni kwamba kuna tatizo, kwanza wewe tayari ni mzoefu wa wanaume,…mimi sijawahi kuwa na mahusiano yoyote zaidi ya huyo mume wangu, kwahiyo kwako, sioni kama ni tatizo, au…?’ nikamuuliza, baada ya mume wangu kuondoka,…

Mume wangu alipofika tulikatisha mazungumzo, hakukaa sana, alisema alikuja mara moja, kuna sehemu anakwenda mara moja…


‘Ugumu unakujaje …nataka mtoto ambaye ana sura ninayoitamani mimi, ..yaani ninachowazia, sio ilimradi tu kupata mtoto, ukichagua nyama, chagua iliyonona, au sio, ….unajua sitaki kukufuru, ila kwa vile nimeamua hivyo, basi kiwe kile kitakachonisuuza moyo wangu….’akasema.


‘Wewe cha muhimu si ni kupata mtoto, hujali tena cha ndoa, au sio..hapo uwe na uhakika,..usije kusema aaha rafiki yangu, kanichuuza…kama ni hivyo, …, basi zaa kwanza na mwanaume yoyote…ningependa kukushauri hivyo…’nikasema na kumkagua usoni.


‘Hapana ….sio hivyo…’akasema.


‘Sio hivyo kwa vipi tena, kwani unataka akuoe,….au wewe watakaje…mimi nilionea hivyo, wewe uzae kwanza na yoyote yule… , huku ukiendelea kusubiria kama utapata mwanaume chagua lako ambaye ataweza kukuoa, lakini huku ushapata mtoto wako ili kutokuingia kwenye umri hatari hujazaa..…unaona hapo, hata akiolewa umeshafikia huo umri,  huna haja ya kuzaa tena maana unaye mtoto tayari unaona hilo wazo langu lilivyokaa...’nikamwambia na yeye akaniangalia sasa kwa uso uliojaa hamasa.


‘Hapo sasa nimekuelewa, hivi kweli hilo inawezekana kirahisi  hivyo…?’ akauliza


‘Kwanini isiwezekane, hahaha, wewe ni mjanja bwana, usitake kunifanya kwua mimi sikufahamu, …’nikasema.


‘Mhh, kunifahamu unanifahamu lakini sivyo kama nitakavyo mimi….’akasema

‘Unatakaje…?’ nikamuuliza

‘Kwanza niambie, kwa vipi hapo, maana nilitaka nizae ndani ya ndoa,..huo ndio ukweli wangu, sasa ndoa imegoma, hivi sasa tunashauriana kuwa  ni zae tu hata nje ya ndoa…si hivyo…?’ akaniuliza

‘Hilo ni jibu lipigie mstari, au…?’ nikasema na kumuuliza

‘Mmhh, hapo kwangu bado pagumu kweli kweli,…isingelikuwa hoja hiyo ya kuchelewa kwa umri, nsingelijali sana, isingelikuwa ….aah, hapana mimi nataka mtoto, kwa vyovyote vile…lakini sipendi maana   hapo nitakuwa nimekiuka kiapo changu,…nitakuwa msaliti wa ahadi yengu mwenyewe..unajua , niliapa mimi sitazaa nje ya ndoa, sasa nifanyeje mungu wangu,..?’ akaniuliza.

‘Hili si unalifanya kwasababu, hii tuichukue kama dharura, maana …. umri umekwenda, au sio, unaogopa utafikia kikomo kabla hujapata mtoto, hiyo si dharura, au sio…. basi wewe cha kufanya ni kutembea na mwanaume yoyote, …mimi hapo nasema ‘yo-yo-te’  sijui kwako wewe….maana mtoto ni mtoto au sio, kwa mzazi kama mimi…’nikasema

‘Ha-pa-na sio kwa yoyote, hilo hapo natofautiana na wewe kidogo, tuliweke sawa hilo, ..maana yoyote atanizalia mtoto yoyote, hapana, mimi nataka yule atakayenipatia nikitakacho, moyo unapenda, unaona hapo, tuliangalia kihivyo, mimi naona hapo turekebishe kidogo....’akasema.

‘Mpaka hapo tunakwenda sawa, siwezi kukukatilia hivyo uakavyo, ila wasiwasi ni kuwa ukianza kumtafuta umtakaye inaweza ikachukua muda tena,…na hujui ya kesho au sio….’nikasema

'Mhhh…hapo sasa, unaleta ugumu , mimi kama nimeamua kula haramu, basi acaha nile haramu haswaa…unielewe hapo, sitaki nile haramu halafu nisikie kichefu chefu, hapama, nataka mume anipatie mtoto ninayempenda….’akasema

‘Wewe ndio unaleta ugumu, unarudi kule pa kuchagua chagua..mwishowe siku zinakwenda, …’nikasema

‘Hapana si ndio tunawekana sawa, tukishakubaliana hilo, kuwa nataka mume atakaye nizalia mtoto ni nimpendaye,…hapo tutaingia kuangalia ni nani…unajua pamoja na yote mimi najali sana mtoto wangu aweje, naanza kuangalia sasa…nisije kujitia baadaye…mtoto awe na sura , tabia, maumbile…ninayoyatamani mimi, eeh, hapo hapo tufanyeje ..’akawa kama anaota au kujenga taswira fulani akilini

‘Aaah, unajua kwangu mimi kama mzazi mtoto ni mtoto tu…hayo ya sura, sijui nini, hayo ni wewe ambaye hujabahatika kuzaa, …mmh, na wewe kwa kuchagua, unachagua mpaka maumbile ya mwenyezimungu, usikufuru kihivyo,….’nikasema

‘We-we..unasema mtoto ni mtoto tu, ina maana mimi kuchukua dhima hiyo basi nijizalie tu,… hapana..ni lazima nifanye jambo nije kulifurahia mwenyewe, sitaki nije kujutia baadae,.. najua nimetenda dhambi, tena ya kudhamiria,…sasa nije kupata adhabu hivi hivi tu, mungu anisamehe tu, sipendi hili jamani,…sasa mimi nitakavyo nikipate nikitakacho,..nizae mtoto nikimuangalia  hivi eeh , moyo unasuuzika na wala nisije kujijutia…’akasema

‘Oh, mungu wangu , hapo sio dharura tena,..ni dhamira mbaya,..hebu niambie kwahiyo wewe unatakaje…?’ nikamuuliza

‘Ninataka huyu mwanaume akinipa mimba, nizae mtoto mwenye sura nzuri, umbo nzuri, maana na mtoto anarithi tabia, basi awe na tabia nzuri kutoka kwa baba yake,…na hata mimi nikimuona huyo mtoto ninafurahi  mwenyewe…’akasema akitabasamu sio kama alivyokuwa awali, sasa uso umeshaanza kunawiri na urembo wake ukawa bayana, kiukweli rafki yangu ni mrembo, sijui kwanini kapata bahati hiyo mbaya ya kutokuelewa.

‘Mhh, ….haya, kama utakavyo ni hivyo, basi twende hivyo hivyo, nikubaliane na wewe, na lile wazo langu la mwanaume yoyoete tuliondoe, sawa, twende sasa,…kwahiyo inabidi hapo uchague mwanaume sasa kama ni hivyo mbona ulikosa wa kukuoa, maana usione ni rahisi kumpata atakayekidhi viwango vyote, ndoa inajengwa na wawili na ndiyo inazaa chema..’nikasema

‘Ndio hapo unisaidie, wewe ushaingia kwenye ndoa, ..na najua vyovyote iwavyo, mtoto huwa anatokana na damu ya wazazi wake, hata tabia, uziri, umbile ndio basi tena…nisaidie kwa hapo…’akasema

‘Unajua wewe unanitwika mzigo ambao mimi sina tabia nao…mimi sijui kuchagua chagua kihivyo, najua chema ukimuomba mungu atakupatia, sio mpaka nianza kuchagua tu..kama nguo,..hapa hatuzungumizii nguo, tunazungumzia mtu, na mtu huletwa na utashi, wa muumbaji, ..sio kweli kuwa unaweza kumpata mume akakupatia hichoukitakacho…’nikasema

‘Rafiki yangu tuangalia uhalisia, hili ulilonishauri, la kuzaa eeh, hata nje ndoa, ni uhalisia, pia linaendana na maumbile, ..tusikwepe ukweli hapa…’akasema

‘Ok, sawa nimekuelewa…..’nikasema

‘Sasa tuseme tumeshakubaliana huyo mwanaume aweje, ..eeh,awe nitakavyo mimi, kazi inakuja , nitamuanzaje, kuwa nataka unipe mimba, au nataka…inakuwa kama nauza mwili wangu..huoni hapo najizalilisha…’akasema


‘Hilo rafiki yangu utaanzaje, mimi siwezi kujua, najua wanaume wakiona ishara fulani wanajua huyo mwanamke anataka kitu..kapenda, tatizo ni huyo mwanaume uliyemchagua je…ana tabia hiyo,…’nikasema

‘Unajua kuna kitu nikuambia ukweli rafiki yangu, pamoja na ya kuwa hawataki kunioa,..lakini nimegundua kitu,  wanaume wengi wananiangalia kwa matamanio,..wengine wananitongoza, tatizo ni hilo wengi wao, wanachotaka ni mwili wangu, na wengi wao sijawapenda…sasa hapo, nifanyeje….?' akasema.

‘Unajua pamoja nakushauri hivyo, bado mimi silipendi hilo wazo,…lakini pia nakuona kweli umri umekwenda, na wanaume ndio hao, …mikosi, sijui tuite hivyo, au ndio huko kuchagua kwako kumefikia…’nikasema

‘Tusirudi huko, tutashindwa kufikia muafaka,…najua mungu anakuadhibu, kwa kasumba yangu hiyo, sawa….’akasema

‘Hapana usifikirie hivyo….mimi bado nilikuwa na imani kuwa muda bado upo,…lakini mtoto kweli ana umuhimu wake, cha kufanya mtafaute huyo unayempenda, mengine utajua mwenyewe cha kufanya, usitake mimi nikutanue kila kitu...’ nikasema na hapo akanikazia macho kwa kushangaa.

‘Nimtafute yoyote ninaye mpenda, bila kujali,…aah ina maana unanishauri hivyo, yoyote ninayempenda, …mmh, hapo sasa ndio naanza kuogopa, maana,….sijui sijui..nifanyeje rafiki yangu…?’ akaniuliza

' Wewe wazo lako si kuzaa tu na mwanaume yeyote unayeona atakuwezesha kupata mtoto mwenye sura unayoipenda wewe, si ndio hivyo naona hata `wadhungu’ wanafanya hivyo, wanaingia kwenye mitandao, wanaandika wakitakacho kuna mawakala wanakutafutia, sasa huku hakuna, ila wewe unaweza kutafuta mwenyewe,....na kwako wewe sizani kama itakuwa ni ngumu kihivyo, wewe mwenyewe unajifanya u mzungu, unaishi kizungu-zungu, matawi ya juu, kwanini kitu kidogo kama hicho kikushinde, haikuwa na haja ya kuja kuniuliza hayo yote.., au sio, mtafute unayempenda uzae naye...kwa siri…unielewe hapo…'hatimaye nikamshauri hivyo rafiki yangu.

‘Sasa nikufuchulia ukweli,..sikuwa na wazo hilo kabisa, maana naogopa sana, ila uliponishauri hivyo wewe rafiki yangu kuwa naweza ..sas anikuambie ukweli, wengi ninaowapenda, kama mungu angenijalia, …wengi ninao ona wanaweza kunipatia mtoto nimtakaje ni waume za watu, ndio hapo naogopa sana.…’nikasema

‘Oh waume za watu ina maana hakuna mwanaume mwingine ambaye hajaoa, hapo uanishangaza, waume wapo wengi, wana umbile, sura nzuri, kwanini ushindwe kuwapata, mimi hapo sioni kuwa ni tatizo …’nikasema

‘Ni tatizo,..maana ni waume za watu, ndio sana nawapenda, ndio sana nikiangalia watoto wao nasema hata mimi nataka mtoto kama yule, nina ushahidi wa kizazi chao, hawa ambao hawajazaa, sina ushahidi nao, ndio maana naingiwa na mashaka nao, uone wazo langu lilivyo, hao, nawa-penda, sio kuwa….unielewe, sio kwamba nina nia mbaya nao, lakini ndio najua wataweza kunizalia kile nikitakacho na nina uhakika nacho..…’akasema

‘Mhh, rafiki yangu utavuruga ndoa za watu, ….’nikasema

‘Sasa mbona unaharibu, unanitisha, basi tuache….’akasema

‘Sio nakutisha, nawazia mbali unajua…’nikasema

‘Kiukweli  mimi sipendi kuvuruga ndoa za watu…yaani sijui kwanini, sijawahi kumuona wa kumpenda ninayevutika naye, ambaye nahisi nikizaa naye nitapata mtoto mwenye sura na umbile nilipendalo ambaye hajaoa,…huo ndio ukweli..nakuambia ukweli kwa vile wewe ni rafiki yangu,… sijawahi kumuona, nimezunguka nimeangaza huku na kule hakuna,....ninao waona na kuwapenda  wengi ni waume za watu...sijui kwanini inanitokea hivyo,…’akaniambia.

‘Sawa mimi nimekuelewa sana, mimi sioni tatizo, kwa vile hutarajii kuishi na huyo mwanaume, ..nikuuliza hapo, kwani wewe najali nini sasa maana sasa unataka nikufundishe kila kitu, kwanza ninataka unihakikishie kuwa lengo lako sio kuvunja ndoa ya watu, ni kuzaa tu, na kuzaa huko kuwe ni siri yako…usije kuniingiza kwenye lawama ya kuvunja ndoa za watu, mimi sipo….’ nikasema

‘Ndio hivyo….’akasema

‘Na pili wewe unataka mwanaume salama asiye kuwa na tatizo, nahisi nimekuelewa hivyo…na unahisi kuwa wao watakuwa na tabia nzuri, sasa kama anakubali kutembea nje ya ndoa, mimi naingiwa na walakini na tabia hiyo, lakini wewe utakua jinsi gani ya kumshawishi , maana wanaume hata aweje, ukimfikisha mahali sizani kama anaweza kurudi nyuma….’ nikamwambia.

‘Mhh, hapo kuna mawili, nimuambia lengo langu au nimfiche lengo langu, mimi sitaki iwe hivyo, unaona hapo, nataka iwe siri ili sije kuvuruga ndoa au sio, nionavyo mimi,…haaah…. unajua umenitia hamasa kwa wazo lako, nimelipenda, japokuwa sipendi kutembea na mume wa mtu,…kwani nitakuwa nimevunja ahadi yangu nyingine kubwa , tena kubwa sana…’akasema

‘Ahadi gani…?’ nikamuuliza

‘Ahadi ya kuwa sitatembea na mume wa mtu, vinginevyo aje kunioa…’akasema

‘Nimeshakuambia uichukulie hiyo kama dharura tu, ikipita basi isahau kabisa, msahau huyo mwanaume na usahau kile kitu, usije kunogewa ikawa ndio basi tena…’nikasema

‘Mhh, hapo nipagumu,  kutembea na waume za watu na huenda awe ni mume wa rafiki yangu,  hapana mimi nawaheshimu sana marafiki zangu....hilo mimi naliona tuliache tu,  sio wazo zuri, na kumpata ...ambaye atanipatia mtoto nimtakaye inakuwa ngumu, ninaowapenda zaidi ni waume za marafiki zangu, mmh, mimi naona mungu kapanga iwe hivyo, tuliache …..’akasema.

‘Wewe usijali, ukimpata huyo mwanaume, hata kama ni mume wa mtu, tembea naye bila kumwambia kitu, hakikisha umelenga zile tarehe…., nia na lengo ni akupe uja uzito, mkishamalizana, unaachana naye kabisa…., na fanya hivyo ukiona kweli mimba imeingia,…maana yawezekana ukajaribu mara ya kwanza isiingie…’nikasema

‘Hapo sasa si ndio nitaanza kujenga mazoea…’akasema

‘Hapana, akili yako iswe kumchukua mume wa mtu,…mimi nina imani hiyo mara ya kwanza inaweza kuleta matunda,..ukishamalizana naye, achana naye,  usiwe na mawasiliano naye tena, achana naye kabisa mpige marufuku kukufuata fuata tena….mimi naona iwe hivyo.,…’nikamsahauri hivyo.

‘Hiyo ni kazi kubwa, maana hapo natakiwa nitongoze mwanaume wa matu, wakati  siku zote natongozwa mimi, nitamuanzaje huyo mwanaume, tena mwanaume wa mtu tena labda awe ni mume wa marafiki zangu,…’akaangalia juu akiwanza.

‘Mwanaume ukimuonyeshea ishara tu wao wanajua, na wewe bado mrembo unavutia, sizani kama hilo litakuwa tatizo kwako, mimi sioni kama ni tatizo, ndio inauma, na sijui, jitahidi umalizane na hilo usahau, mimi naona ufanye hivyo. Maana sasa unaniingiza kwenye kuchagua chagua……’nikasema

‘ Sio hivyo, ..hapa tunapanga kitu chenye uhakika,….maana  hapo unazungumzia mume wa mtu ninayemfahamu ,maana ili niwe na uhakika inabidi awe ni mwanaume ninayemfahamu, si ndio hivyo,..ambaye natamani anizalie watoto kama ….unaona inakuwa ngumu, nitakuja kumuangaliaje huyo rafiki yangu, ndio maana nikasema hili wazo sio zuri, naona tuliache tu...’akatulia kidogo.

‘Wewe unajali nini kwani unaondoka na huyo bwana..hahaha, naona unanifanya na mimi niwazie mambo niliyokuwa sinayo kichwani mwangu, wewe kama lengo lako ni mtoto na ni kweli umri ndio huo,… fanya hivyo, na iwe siri yetu wawili tu..,usije kumuambia mtu kuwa mimi nilikushauri hivyo….sitaki..’nikasema huku nikicheka.

‘Mhh, unajua ni rahisi kusema, lakini kwenye kutenda ni kugumu,  maana ni kweli watoto  wa marafiki zangu nawapenda sana, na natamani niwapate kama hao hao....hapo ndipo naona ugumu, kuwasaliti marafiki zangu, wewe huoni hapo inaweza kuleta shida baadaye, wanaweza wakaja kugundua, urafiki utageuka kuwa ni uadui, sipendi kukosana na marafiki zangu....mmh, ngoja nifikirie huo ushauri wako…’akaniambia.

‘Sio swala la kufikiria sasa rafiki yangu, …hapo ni swala la kulifanyia kazi, sizani kama itakuwa ni ngumu kwako,  wewe ni mrembo bwana, nashangaa kwanini hujaolewa, kila mtu anakushangaa mrembo kama wewe huna mume...’nikamwambia.

‘Kila mtu ananishangaa, basi anipatie mume wake,, waache wafikiria watakavyo, mimi hilo sijali kabisa..maisha yangu hayawahusu....kwangu mimi hilo la watu kiukweli ninachohofia kwasasa, nisije nikafikia umri ambao hautakiwi kuzaa tena,  sijapata mtoto, yaani hilo ndilo tatizo kwangu si vinginevyo....’akaniambia.

‘Kama ni hivyo , basi fuata ushauri wangu, na wala usipoteze muda, kama waume za watu ndio unaowatamani, ndio watakao kupatia mtoto unayemtamani, basi hao wapo wengi, ila chunga sana, ....’nikamwambia

‘Nichunge nini tena, unanikatisha tamaa…?’ akauliza akiniangalia kwa mshangao.

‘Kuna waume wana wake zao ni wakorofi, wakija kugundua wanaweza kukuharibu hiyo sura yako, tafuta waume ambao wake zao ni wastaarabu, ...na iwe siri yako, usimwambia yoyote...haya,usipoteze muda tena kalifanyie kazii hilo…’nikamshauri.

‘Sawa rafiki yangu, maana umenipa wazo ambalo sikuwa nalo kichwani kabisa...kiukweli naogopa sana, waume za watu...bado naogopa....kutembea na mume wa mtu, na mbaya zaidi awe ni mume wa rafiki ninamyemuheshimu sana ..naogopa sana... hapana hiyo sio tabia yangu, itakuwa ni mara ya kwanza kutembea na mume wa mtu...’akasema.

 Rafiki yangu alitulia kwa muda, nadhani alikuwa akiwaza jinsi gani atakavyotembea na huyo mume wa mtu,  na wakishamaliza, jinsi gani atakavyojisikia vibaya, na kama kweli huyo mwanaume ni muungwana na yeye atabakia akiwa anajutia....nikamtoa kwenye mawazo hayo na kusema;

‘Shauri lako kama na hilo nalo ni mpaka uchague chague kama nazi endelea kufanya hivyo, hilo halina kuchagua tena hapo, maana mwenyewe umeshasema kuwa waume za watu wapo wengi unaowapenda, na umeshaona watoto wao au sio, sasa watakaje, nikuchagulie mimi au..?’ nikamuuliza

‘Hapana, umeshanipa njia inatosha…na kiukweli marafiki zangu wote nawafahamu watoto wao, nafahamu yupi ni yupi anafaa, nitachagua mmojawapo, au sio..?’ akaniuliza

‘Ndio hivyo,  chagua yoyote atakayekukidhi matakwa yako, sizani kama hilo ni tatizo kwako, au…?’ nikamuuliza

‘Sijui kama ni tatizo, maana sio kawaida yangu, lakini nitajaribu, maana wengi, nawaoana wakinitizama kwa jicho la kunitamani, kwahiyo..sawa, natumai sitaharibu kitu, ngoja nione itakavyokuwa, nashukuru sana rafiki yangu, kwa kunijali,..wewe ndiye rafiki wa kweli, hilo wazo limekaa vyema japokuwa ..mmh…’akasema

‘Usijali,..sasa kazi ni kwako wewe ushawajua ni nani anakuvutia zaidi,  mweka kwenye anga zako, tembea naye,hakuna atakayejua...wewe mjanja bwana, hilo lifanyie kazi, haraka iwezekanavyo, kabla mambo hayajabanika..’nikamwambia na yeye akataka kuondoka

‘Mbona huwaagi watoto , …naona wazo hilo limekuhamasisha sana…’nikasema
‘Oh, yaani we acha tu,….’akasema na kuwafuata watoto kule wanapojisomea, na kuwa-aga…wakamsindikiza hadi mlangoni… , na alipofika mbele kidogo,  akageuka na kuwaangalia , akatabasamu na kuwapungia mkono na huyoo, akaondoka zake….

‘Mlikuwa mnajadili nini….?’ Ilikuwa sauti ya mume wangu ilinishtua kwakweli… sikujua bado yupo, maana aliaga kuwa anaondoka!


Nb, mkuki ukachongwa, tayari kwa kumchoma nguruwe......


WAZO LA LEO: Wengi twachukulia rahisi tu kuongea, kutamka neno, vyovyote akili zetu zitakavyotutuma, tukumbuke kuwa kila neno lina thamani yake inaweza kuwa mbaya au nzuri... Neno dogo tu laweza kuzua sintofahamu, likajenga chuki, likaumiza, na hata kubomoa kile ulichoanza kujenga…rafiki wa leo anaweza kuwa adui mkubwa wa kesho, sababu tu ya kauli.. , kauli zaweza hata kuua.
 Wachamungu wa kweli wametuasa kuwa ni bora kufunga mdomo wako, ukauzuia ulimi wako, ili kujiepusha na mtihani wa ulimi.

Najiusia mimi mwenyewe na kuwausia wenzangu, tuweni makini sana na kauli zetu, tuchunge sana ndimi zetu.
Ni mimi: emu-three

No comments :