Baada ya kuutoa ushauri kwa
rafiki yangu, kukapita kipindi cha pilika pilika nyingi, mambo yakawa mengi ya
kupambana na maisha, kiasi kwamba hatukuwa na muda wa kukutana na rafiki yangu
, hata tukikutana ni ile ya haraka haraka kila mtu anakimbilia kwenye shughuli
zake, na mara rafiki yangu akanipa taarifa kuwa anahamishiwa Zanzibar kikazi,
‘Hamna shida kazi ni kasi, na popote uwapo tutazidi
kuwasiliana…’nikamwambia aliponipigia simu na wakati ananipigia yupo tayari
anaelekea kupanda express bot, kwani taarifa ilikuwa ya haraka, na alitakiwa
haraka akawasili kwenye hicho kituo kipya, na huko atapata maelekezo zaidi…basi,
tukawa tunawasiliana kwa simu tu, kuulizana hali na siku, na masiki yakapita.
Ikawa akija Dar, hakai
sana, na mimi nikawa na mishughuliko mingi ya shughuli zangu, wakati mwingine
anakuja mimi nipo mikoani, kazi ni kazi, hakuna kulala, ilimradi afya zipo,…na
kipindi chote hicho, tunapigiana simu au tunakutana kwa haraka, hutaamini
sikuwa na hata na akili ya kumuulizia lile zoezi letu lilikwendaje…
Miezi mingi ikapita, na siku moja akaja kunitembelea nyumbani
kwangu, alifika mara moja kikazi, basi tukaanza kuongea hili na lile, alikuwa
kavaa Madera yake mapana tu, mimi nilijuwa kwa vile kahamsihiwa huko Zanzibar,
basi kajifunza asili za huko, za kujisitiri mwili mnzima,….ila nilihisi kuna
mabadiliko, ukimuangalia usoni kazidi kuwa mweupe, na unene kidogo, sijui kwasababu
ya hizo nguo alizovaa, japokuwa nilikuwa na haraka kama alivyo yeye, nikamuuliza.
‘Vipi mwenzangu, toka lini ukavaa nguo hivyo, maana wewe ulikuwa
ni mdhungu, haahaha, naona sasa
ushakumwa mnzaibari tena, na nahisi huko ushampata shemeji au sio, kwa hilo
umbo na sura yako, sizani waname watakuacha upite hivi hivi tu, halafu hebu
niambie, nahisi mmh,…na nakuona kama mambo tayari au, ..?’ nikaanza kumtania.
‘Acha utani wako bwana, nimpate wapi mume mie, umri ushaenda,
..naona wengi wameamua kunikimbia, lakini sijali, ..na wala hilo haliniumizi
kichwa,… kabisa, kabisa,….mimi nimeamua
kula, kuishi kivyangu, yaani sitaki tena
usuhuba na hao watu, huwezi amini, nimeamua hivyo na imewezekana....’akasema.
Hapo ndio nikaumbuka kile nilichomshauri , ikabidi nimuulize
‘Vipi lile swala letu uliweza kulifanyia kazi?’ nikamuuliza.
‘Hahaha..unajua niliwazia sana hilo, nakumbuka tuliongea kuwa kama
…unajua iwe siri, na..aah, …’akasita kuongea
‘Aaah, mbona unasita kuongea, au ulizarau…?’ nikamuuliza
‘Mhh, hapana sikuzarau, ..sio maana hiyo ya kuzarau,..unajua
niliwaza sana huo ushauri,…, nikaona nisiende mbali…..lakini wewe ni rafiki yangu, na hili tulilijadili
pamoja, niliogopa ule usemi wako kuwa niwe makini maana wanawake wengine ni
vichaa….’akatulia , sikuwa nimemuelewa hadi hapo ana maana gani.
‘Kifupi ulifanya au hukufanikiwa…?’ nikamuuliza
‘Ndio maana nimekuja kwako hivi leo, sina muda, hapa unaona meseji
zimeshaanza kuingia natafutwa huko ...’akasema akitabasamu,…usoni ulionyesha
furaha ya kweli, japokuwa kuna kiwingu cha kuonyesha ana mawazo fulani.
‘Kwahiyo kifupi tuseme tayari…?’ nikamuuliza nikiwa na hamasa ya
kutaka kujua
'Mhh,…rafiki yangu, wewe na mimi ni marafiki, usingeliweza
kunishauri kitu nikipinge bure bure…. ushauri wako nimeufuata na sasa hivi
unavyoniona hapa nina uja uzito…hapa nilipo sitamani hata kula…kichefu
chefu..yaani taabu kweli kweli..hivi mimba ndivyo zilivyo hivyo…, hapana
nikizaa huyu mmoja, sizai tena, sitaki tena kuzaa.....’akaniambia.
'Mambo si hayo, ....umefanya jambo la maana sana, ....ulikuwa
unapoteza muda tu,.. na umri ndio huo, na kama ulivyosema waume wanakuona sasa
umeshakuwa mtu mzima, huna ujana tena, ..na ukiachia mwili
hivyo,…mmh,…’nikasema
‘Sijaachia mwili, nachoka tu, halafu …sijisiki vyema,…’akasema
‘Ni kawaida, hali kama hiyo ni kawaida, muhimu ni kufuata masharti
ya dakitari, hakikisha huharibu ulichokitaka, sawa….usije kujipilikisha na
kazi, mimba ikaja kuharibika…’nikasema.
‘Hutaamini, nafuatilia masharti yote, naingia kwenye
mitandao…nauliza madocta, sitaki kufanya makosa, na mungu anisaidie…’akasema
‘Hongera sana…’nikasogea na kumkumbatia rafiki yangu huyo…lakini
sijui kwanini kuna kitu nilihisi akilini mwangu,..hata siwezi kukielewa, hata
hivyo furaha iliweza kukimeza hicho kitu, ni kama mashaka,…’
‘Mhh,…hongera wakati hata sijafikia ….unipe nikishajifungua, au
sio…na kiukweli, nashukuru sana rafiki yangu, umenishauri, na najua utaendelea
kuwa name, hata siwezi kuelezea ninavyojisikia, japokuwa moyoni, kuna muda
nawaza sana…’akasema
‘Unawaza nini sasa, hayo yameshapita muhimu ganga hili lililope
mbele yako, jinsi ya kupambana na ujauzito maana nao sio mchezo, mengine
yasahau kabisa,…unanielewa, wala usifikirie kuwa umekosea, ..hayo muachie mungu
atakusamehe..’nikasema
‘Mhh…kweli wewe ni rafiki wa kweli..tatizo ndio hilo,… hapa
nilipo, najisikia vibaya, sitaki kuongea saaana, mate yanajaa mdomoni…’akasema
akitoa leso yake na kuweka mdomoni
‘Pole ndio uuke huo…’nikasema
‘Mungu anisamehe tu, na mnisamehe kwakweli….’akasema
‘Hamna shida wewe tema mate yako tu…ilimradi uteme sakafuni…’nikasema
‘Unajua haya yote ni
kutokana na ushauri wako, wakati mwingine najilaumu kwanini, niliamua kuvunja
nadhiri yangu, lakini sawa, kwa vile ni
wewe sina shaka....’akasema.
‘Usijali kabisa…..mimi nilikupatia ushauri huo nikiwa najua wewe
ni rafiki yangu, nikupe ushauri wenye tija,…usiwe na shaka na hilo..na sioni tatizo
lipo wapi, …muhimu kama ulifuata kama
nilivyokuambia, sizani kama itakuwa na tatizo,…kwani huyo mwanaume,
uliwahi kumwambia baada ya kuhisi kuwa una ujauzito unaotokana na yeye?’
nikamuuliza.
‘Mhh, …aah, …unajua wanaume walivyo, baada ya lile
tendo,…nisikufiche, ili kuwa na uhakika zaidi,…nilikutana nae mara mbili, mara
mbili tu….sasa ikawa ni taabu, unajua wanaume walivyo, na..na…nilipohamishiwa huko
Zanzibar, nikashukuru sana, maana huko mpaka aje sio kazi rahisi…na, nilimkanya
kabisa kuwa mimi, sitaki tena urafiki na yeye, ndio hivyo, na sitaki
kuyaongelea hayo tena tuyaache tu, ila nilitaka ni…niwe muwazi kwako…’akasema
‘Safi kabisa, lakini je baada ya kujihisi una mimba uliwahi
kumuambia…?’ nikamuuliza
‘Unajua.hapana sitaki tuliongelee zaidi…nataka kukuambia…hapana,
naogopa…’akasema
‘Unaogopa nini sasa, nimekuuliza hivi umemwambia…?’ nikamuuliza
‘Kama nilivyokuambia, wanaume hawana dogo, na hata siku ile, ya
kwanza nilimuambia nimfenya hivyo kwa vile nimeshindwa kuvumilia, ila naheshimu
ndoa yake, kwahiyo iwe ni mwanzo na mwisho…’akasema
‘Safi kabisa, inatosha ulivyomuambia…’nikasema
‘Lakini bado akawa ananifuatilia, japokuwa nilijitahdii sana
kumficha,...na nikajitahidi sana kuwa mbali naye, lakini sijui kwanini, imekuwa
kama nimemuonjesha asali , ….yaani nipo kwenye wakati mgumu sana, ndio maana
nakuambia nimekosea sana….sijui nifanye nini sasa…kwani hata nafsi inamtaka
najizuia napata shida sana….’akasema.
‘Lakini nilikuambia kuwa kama ni mume wa mtu, ukishahakikisha kuwa
keshakupachika mimba, achana naye kabisa, nilikushauri kuwa usimwambie hata
huyo mwanaume kuwa una mimba yake, utasumbuliwa sana…, unajua waume wengine walivyo,
hawatakubali damu yao ipotee hivi hivi, na hujui hatima yake itakuwa…na kumbuka
kama ni mume wa mtu , ….utakuja hatarisha ndoa ya watu, kuwa makini sana kwa
hilo…’nikasema
‘Hata sijiu nifanye nini, ndio maana nikaja kwako tena, nipata
ushauri, au sijui niitoe maana najuta, na inanipa wakati mgumu, namtaka aje awe
karibu nami, unaona ilivyo, hata sijui nifanye nini, ndio maana nafikia kujuta,
najiona kama nimebeba dhambi mwilini mwangu…?’ akasema sasa akikwepa kabisa
kuniangalia machoni
‘Kwani , hebu niambie ukweli huyo shemeji ni nani, maana sasa unanivutia
intake kumfahamu, inaonekana umempenda sana…., hebu niambie ni nani ili niweza
kukupa njia nyingine ya kumfanya asikusumbue tena..?’ nikamuuliza, nikiwa na shauku kubwa sana.
'Na wewe bwana, ina maana hapana…. sasa, itakuwa wewe ni wa kwanza kuvunja ushauri wako, mwenyewe
ulianiambia nikishatembea na huyo mwanaume, nisimwambia yoyote hata wewe
mwenyewe, sasa wewe unataka niseme, unajua hilo limekuwa likiniumiza kichwa,
nawaza nikuambie tu, au ..hapana mimi naona nifanye kama ulivyonishauri, au sio…maana
hakuna siri ya watu wawili..’akaniambia.
‘Lakini mimi ndiye niliyekushauri,…sasa , anyway,….fanya ilivyo
sahihi, ni kweli ni bora iwe siri yako, ..hata hivyo ukiona ni lazima kuniambia
ni nani, usisite kuniambia, kwangu usiwe na shaka kabisa, maana hatufichanai au..’nikamwambia
‘Lakini pia wewe ndiye uliyenishauri kuwa nikishahakikisha nina
mimba nisije kusema au kumtaja huyo mtu, kwa yoyote vile…, unakumbuka eeh, basi tufanye
hivyo, najua utanisamehe…. tusubiri nizae kwanza, ....’akasema
‘Usijali kabisa, kunificha ni sawa,….hiyo inanipa uhakika kuwa
hutasema lolotekwa yoyote, kama umeshindwa kuniambia mimi, nina uhakika
hutaweza kusema lolote kwa mwinginewe, au sio…’nikasema
‘Ni kweli, basi,…haina haja kukuambia, ..na hapa nilipo najisikia
vibaya,...ngoja niondoke, hapa nisije nikakutapikia bure, na na..nashindwa,
natamani niku—ooh, najisikia vibaya sasa...’akasema na haraka akimbilia nje.
‘Kama mambo yenyewe ni hivyo , hicho kinaweza kikawa ni kidume, na
ukija safari nyingine ni lazima uniambie
huyo shemeji ni nani, ...au nitakuja nyumbani kwako, upo mpaka lini...’nikamwambia
na yeye akawa ameshatoka nje, …nilipomfuata nilimkuta ameshaingia kwenye gari
lake na kuondoka.
*********
Miezi mingi ikapita, ...
kwasababu ya kikazi na mambo ya hapa na pale, na kwa vile sasa yeye yupo huko
Zanzibar, hatukuweza kuonana na rafiki yangu huyo, na siku moja nikapokea simu,
namba ilikuwa ngeni kwenye simu yangu, nikapokea nikijua yawezekana ni wateja
wangu.
‘Habari nani mwenzangu..?’ nikauliza
Sauti ya kinyongea kama mtu mgonjwa ikasikika,..kwanza sikujua ni
nani..hata kufikiri,…mambo mengi kichwani,…
‘Oh, …ni mimi, yaani …’akasema akitoa sauti ya kinyonge
‘Ni, ni …wewe ni nani maana namba hii ni ngeni kabisa…?’ nikauliza
nikjaribu kuwaza ni mteja gani huyo. Na kwanini anaonekana mgonjwa akilini
nikahisi inawezekana akawa mmoja wa wateja ninaye mdai.
‘Hii namba ni..simu ya rafiki yangu , ya kwangu imezima haina
chaji,…’akasema
‘Ok,….pole..nani mwenzangu, nikusaidie nini…’nikasema
‘Nilikutumia ujumbe nilipofika juzi, lakini ukawa kimia,…..’akasema
‘Ujumbe…ujumbe gani, kwani wewe ni nani…?’ nikauliza kikazi zaidi.
‘Ni mimi…nilikutumia ujumbe nikitokea Zanzabar,….nikajua utakuwa
wa kwanza kuja kuniona…nikaona kimia, nikakupigia , lakini kila nikipiga simu
yako ipo inatumika, na bahati mbaya nilikuwa natumia namba nyingine, ambayo
nilikuwa sijakupatia, ya Zantel…’akasema
‘Oh, ina maana ni wewe..mbona sauti ipo hivyo…?’ nikamuuliza baada
ya kugundua kuwa ni huyo rafiki yangu.
‘Ni mimi …sipo vizuri ..aaah , maumivu…’akasema na kabla hajaongea
zaidi ni kasema;
‘Ujumbe wako niliupata,nilipanga nije kwako nikiwa na uhakika kuwa
umeshafika…, ulisema umechoka…punguza kazi, pata muda wa kupumzika, ikibidi
chukua likiza usije kupata matatizo…’nikasema
‘Unajua nilitaka niende kijijini kwa wazazi…, ili kukwepa yale
uliyonishauri, lakini nikaogopa, unajua tena kijijini, nitaulizwa maswali
mengi, nikaona bora nipambane kivyangu….’akasema
‘Vizuri, usijali, mimi si nipo, kama utakuwa hapa Dar, usijali
kabisa, ..hata ikibidi unaweza kuja kukaa hapa mpaka muda wa kujifungua…’nikasema,
‘Kujifungua…hahaha…. nimekupigia kukufahamisha kuwa mimi nipo
hospitali…’akasema na kukawa na ukimia, na nikasikia kama sauti ya kichanga
kinalia.
‘Umelazwa,….ina maana…?’ nikauliza
‘Ndio nimeshajifungua mtoto wa kiume...’akasema na nikajikuta
nashikwa na mshituko, kama vile nimeambiwa jambo baya, badala ya kufurahi,
sijui kwanini…nikajikuta nimetulia kidogo.
Mara simu ikawa inataka kuingia, …na nakumbuka kulikuwa na mteja muhimu nilitakiwa
niongee naye, na hapa rafiki yangu kanipatia jambo muhimu sana…sijui ilikuwaje
nikajikuta nimekata simu ya rafiki yangu na simu nyingine ikaingia…alikuwa ni
mume wangu.
‘Oh, ni wewe…nilikuwa naongea na rafiki yangu, ….’nikasema na yeye
akasema, alinipigia kuniarifu kuwa atachelewa, kuna sehemu atapitia…
‘Wapi huko, maana hata mimi nataka kutoka, ….’nikasema
‘Napitia hospitalini…..’akasema
‘Unaumwa…?’ nikamuuliza
‘Hapana kuna mtu nakwenda kumuona…’akasema
‘Basi hata mimi nakwenda hospitalini, kuna mtu nataka kumuona…’nikasema
‘Hospitali gani…..?’ akaniuliza…na hapo nikashindwa kumjibu maana
nilikuwa sijamaliza kuongea na rafiki yangu, nikasema
‘Subiri kidogo nitakujibu, wewe unakwenda hospitalini gani…?’
nikamuuliza
NB: Haya mambo ndio hayo yameanza kujitokeza mkuki ulishafanya
kazi yake, sasa tuone matokea yake
WAZO LA LEO: Kwa
watu wengi, ulimi huwa ni mgumu sana kuuzia, mnaweza kupanga kuwa hilo
utakaloambiwa liwe siri, lakini kwa wepesi wa ulimi ulivyo, au kutokana na
tabia zetu zilivyo, hatuwezi kuhimili, twatamani kuongea sana, ukaja kuliongea hata
lile la siri, …siri ikavuja, na siri sio ya watu wawili. Tujifunze sana kutunza
kile tulichoahidiana na wenzetu, kama uliambiwa iwe siri, basi na iwe siri
kweli,..tukikumbuka kuwa ahadi ni dhamana.
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment