Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Thursday, October 12, 2017

MKUKI KWA NGURUWE-5



Ikabidi nimpigie simu tena rafiki yangu ili kuhakikisha kuwa hajatoka, maana hospitali nyingine ukijifungua kama huna tatizo, unaruhusiwa mapema tu, na mazungumzo yetu yakawa hivi;

‘Samahani rafiki yangu, simu ilikatika, mzee aliingilia kati, unajua tena, mume ni mumw inabidi umpe kipaumbele au sio, nisamehe tu kwa hilo, …hebu niambie kwanza unaendeleaje?’ nikamuuliza

‘Kiukweli, ni maumivu tu…hapa yananitesa kweli, wamenipa dawa za maumivu lakini bado,…oh, ….ila sikupata taabu kujifungua, sio ile kama ninavyohadithiwa, namshukuru sana mungu….ooooh, , nimejifungua salama, iliyobakia ni jinsi…lakini nitajitahidi kama ulivyonishauri …’akasema

‘Yaani siamini ina maana miezi tisa tayari… hivi urafiki wetu umekuwaje, ndio ..lakini ndio maisha au sio…kweli, kweli siku zinakwenda na maisha yanabadilika, umesema ..upo hospitali gani vile maana mimi nimebahatisha tu?’ nikamuuliza.

‘Hilo swali gani tena rafiki yangu…, mimi siendi kwenye hospitali tofauti na ile hospitali yangu niliyozoea kutibiwa na ndipo nilipojifungulia, wewe kama upo bize, haina haja…utanikuta nyumbani,..nilikuwa nakufahamisha tu...’akasema rafiki yangu huyo na mimi huwa naifahamu hiyo hospitali yake anayopenda kwenda mara kwa mara akiumwa.., sikutaka kumuuliza zaidi, nikasema;

‘Eti kama nipo bize, hilo usithubutu kusema, mimi na wewe tena, ninakuja hivi sasa nipo njiani,…maana taarifa hiyo kwanza ilinishtua, na furaha ikawa kama mshtuko fulani, sijui kwanini…’nikasema

‘Oh, unakuja….mbona unasumbuka hivyo, kuna mtu ….’akasema akiwa kama anauma uma maneno

‘Ninakuja usiwe na shaka, kama ni kukuchukua nitakuchukua mimi,…oh, nimefurahi kweli, ....nakuja sasa hivi, nataka niwe wa kwanza baada ya manesi kumshika huyo mtoto na kumpa huduma stahiki, mimi ndiye wa kuendelea kutokea hapo, sijali kazi hilo ni muhimu kwangu kwa sasa...’nikasema na kukata simu.

Kiukweli nilikuwa na mambo muhimu sana lakini niliamua kuyasitisha kwa kuona umuhimu wa jambo hilo, nilimthamini sana rafiki yangu na, haraka  nikaingia kwenye gari kuelekea huko hospitalini. Sikukumbuka kumpigia tena mume wangu kumuarifu mimi ninakwenda hospitali gani!

Tuendelee na kisa chetu

****************


'Rafiki yangu nimejifungua, mtoto wa kiume...bado nipo hospitalini...' nilijikuta maneno hayo yakijirudia rudia kichwani, hasa nikikazia hilo la ‘mtoto wa kiume…’

‘Mtoto wa kiume…mmh,….ana bahati kweli…’nikasema nikakumbuka mume wangu jana alivyokuwa akiongelea kuhusu watoto na alitamka neno kuwa hivi sasa anatamani kumpata mtoto wa kiume, akishampata huyo hasumbuki tena, nikamwambia

‘Kupata mtoto wa kiume ni majaliwa ya mungu, ..’nilisema hivyo, tukaishia kuongea maneno mengine.

Nikiwa kati kati ya bara bara ndio nikakumbuka kuwa mume wangu alitaka nimuambie naelekea hospitali gani, nikampigia simu , lakini kila nilipojaribu namba yake  inasema inatumika, sikujali sana, nikijua mwenzangu katingwa na majukumu, yake ya kikazi.

Mimi nikaongeza mwendo, na kuelekea hospitalini hapo alipolazwa huyo rafiki yangu, na wakati naendesha nikaona nimpigie tena huyo rafiki yangu, nia ni kujua kinachoendelea kama nahitajika kumchukulia chochote cha kula. Lakini badala ya kuliongelea hilo kwanza tukajikuta tunaongea mambo mengine.

'Oh, hongera sana mambo si hayo, ..wewe ulikuwa unapoteza muda bure, uzee ndio huo. Ulikuwa unasubiri mtoto aje akuite bibi,..’nikaanza kwa utani na akawa anacheka, na kusema.

‘Usinitanie mbona sijazeeka kiasi hicho cha kuitwa bibi…ni kweli ukiangalia wenzangu wenye umri kama wangu, unaweza kuwasalamia lakini mimi bado naonekana kijana tu…sasa naogopa nisije kuelekea huko’akaniambia na mimi nikasema;

‘Ni kwasababu ulikwepa majukumu ya kuolewa na kuogopa kuzaa mapema, ndio maana bado unaonekana bado kijana, ngoja upate mtoto wa pili, na upate shemeji anayejua mfumo dume, kama hutabadilika sasa hivi na kuitwa bibi...’nikaendelea kumtania.

‘Nani azae tena, …mimi...subutu yake..na kwa vile sina mume, …hilo limepita.., hii kasheshe niliyoipata siwezi tena kubeba mimba, kwanza uone ilivyo, nimezaa nikiwa mzazi peke yangu, nawaza huko mbele, mtoto akikuwa, anaweza kuanza kudai baba yake ni nani….na ole wake akiniuliza , nitampa jibu hatakumbuka kuniuliza tena….’akasema.

‘Oh, kwanini useme hivyo mpendwa, siumesema huyo shemeji anajua una mimba, na kwahiyo nahisi utakuwa umeshamwambia kuwa umeshajifungua, japokuwa kiukweli hayo uliyoyafanya hayanihusu , umekwenda kinyume na makubaliano yetu, ni hatari, nahofia ndoa za watu, ….’nikasema.

‘Ukifika tutaongea bwana, ….pamoja na mengine niliwazia sana ushauri wako, kuwa nimtafute mwanaume ambaye sitakuja kupatishwa taabu na mkewe, na..laki ni stutakuja kuyaongea, nataka nije kuyaweka wazi mapema tu….’akasema

‘Kwahiyo unataka kusema nini, kuwa utamuhusisha na huyo mzazi mwenzako je mke wake itakuwaje…?’ nikamuuliza

‘Nitajitahidi sana …unajua, sizani kama ni tatizo, hata hivyo, ifike muda tuongee, tuone tutafanyaje, na huyo mwanaume …sihitajii sana kumueleza, japokuwa ananiganda sana, unajua awali kabla sijajifungua nilikuwa natamani sana awepo, kuna hali ilikuwa inanivuta awepo,..mpaka nakereka,…lakini sasa nimeshajifungua, sitaki hata kumuona, sijui kwanini ....’akasema

‘Haya tutakuja kuongea tu, na kuhakikisha kila kitu tunakiweka sawa, mtoto wako ni wangu, hilo halina shida, usijali kabisa....’nikasema huku nikimuwazia huyo rafiki yangu na mtoto wake, nikikumbuka ushauri nilio mpa, na kujisifia moyoni kuwa nimefanya jambo moja kubwa kwa rafiki yangu, nikasema.


‘Ninakuja na zawadi kibao kuonyesha jinsi gani nilivyofurahi, na shemeji nilimuambia kuwa ninakwenda hospitalini kumuona mzazi, unajua alichoniambia,….eti na yeye kuna hospitali anakwenda kumuona mzazi pia…’nikasema

‘Oh, ndivyo kasema hivyo, …..’akasema hivyo.

‘Nahisi ni mfanyakazi wao ….sijamuulizia sana, lakini anaweza akaja kukuona, ingelikuwa ni bora tungelifika sote,…wanaume hawajui zawadi gani kwa mtoto ningemshauri zawadi gani tuje nayo,…’nikasema

‘Ok….sawa, nimekuelewa, …ukija tutaongea….’akasema na mimi nikaendelea kuongea;

‘Unajua hizi kazi zetu tena,  mimi na yeye siku hizi tumekuwa kila mtu bize-bize, yeye na shunguli zake, na kazi zake za kuajiriwa, na bado anahitajika kusimamia, kwenye ofisi yake aliyoifungua, kwahiyo kazi zinamuendesha mbio mbio, kama ilivyo mimi,…mimi tu,  nina ofisi yangu mwenyewe bado nasumbuka hivyo, na wafanyakazi, je yeye mwenye majukumu mawili itakuwaje…kwenye ajira ya kuajiriwa na kwenye ofisi yake ya kujiajiri, sio mchezo. …’nikasema

‘Hongera zenu mlioweza kujiajiri na sasa mnaajiri wafanyakazi, hata mimi natamani niwe hivyo, natamani sana maisha yenu, yaani sijui kwanini, nataka niwe kama nyie…’akasema

‘Unajua …nilitaka nimwambieje shemeji yako, aje tukutane mahali ili tukakununulie kila kitu sitaki ugharimie chochote, cha mtoto hadi wewe mwenyewe…mimi ninataka kila kitu nitoe mimi, unasikia, wewe ni rafki yangu, hilo halina mjadala…’nikasema.

‘Mhh, rafiki yangu, utanifanya nilemae bure…hapana… mimi nataka niwajibike kama mzazi, kuanzia mwanzo hadi mwisho, nataka nifaidi kile nilichokikosa miaka yote hiyo, nataka niwe mzazi,… sio mlezi,….’akasema

‘Hili usiniambie, bado utaendelea kuwa mzazi,…najua tutanyaje….Hivi nikuulize maana tumeongea sana, vipi kuhusu chakula ….ngoja kwanza nikakununulie supu ya nguvu, napitia kwenye hoteli, .. nitakuja nayo hiyo supu sijapika mwenyewe, nitakuwa nakupikia …lakini kwa leo, kwa dharura, ngoja tununue hotelini…, sitaki mtu mwingine alete unasikia….najua ndio chakula chako kwa hivi sasa…’nikasema


‘Haya usichelewe maana huenda wakaturuhusu leo hii…, kwa hivi sasa docta hajapita bado, …..na mimi sipendi kuendelea kukaa hapa ndani, madawa na harufu za kihospitali sizipendi ....we acha tu..hata hiyo supu sizani kama nitaweza kuinywa,…mimi naona ususumbuke kuinunua,..labda kama utainywa wewe…’akasema

‘Ina bidi uanze kuzizoea hali za namna hiyo, maana kuna kiliniki ya mtoto, laaima ufike hospitalini, na huwezi jua, ...akiumwa unatakiwa kuja kumuona docta, tena docta wa watoto…’nikasema

‘Najua najua..hayo baadae…’akasema

‘Sio unajua sikiliza, hayo ni muhimu sana, mtoto mchanga akiumwa uhakikishe unampeleka kwa docta bingwa wa watoto,..sio unaitisha madocta mitaani, au nyumbani,..na usimpeleke  mtoto kwa docta wa kawaida, unaweza ukamkomaza mtoto kwa madawa yasiyomsaidia.....’nikamwambia.

‘Haya bwana, wajifanya wewe ni mzoefu sana nakusikiliza, kwani upo wapi, maana nakusubiria, mshauri wangu, na…hebu kwanza,…ok, … nakata simu, maana naona kama docta anakuja....’akasema na mimi nikakata simu.

************

Nilifika kwenye hiyo hospitali mapema, maana kulikuwa hakuna foleni kama nilivyotarajia, nikampigia simu katibu muhutasi wangu abadilishe ratiba zangu za siku, ofisi yangu ya kujiajiri ni kubwa, ina kila kitu kinachohitajika kama kampuni inayojitegemea.

Nilipofika hospitalini, nikapitia njia tofauti ya kuingilia, nilipitia njia wanayotumia wafanyakazi wa hapo maana wao wanasehemu yao, nikaenda kulisimamisha gari langu sehemu wanayosimamisha magari yao, kama mfanyakazi wa hapo, nikaongea na mlinzi alilalamika, lakini nikampa pesa ya soda, akanyamaza.

Nikaenda moja kwa moja kwenye wodi ya wazazi, nikamuona rafiki yangu, akiwa amekaa kwenye kitanda, huku akiwa na mkoba wake pembeni, nikashangaa, na kumuuliza.

‘Vipi tena, mbona umekaa mkao wakuondoka…?’ nikamuuliza nikimkagua akiwa kambeba kichanga chake na mimi nikasogea na kumpokea.

‘Yaani ulipomaliza kuongea na mimi kwenye simu , akaja docta, na akaniambia sina haja ya kuendelea kukaa zaidi hospitalini, nilishukuru kitu, alisema kwa vile mimi sina tatizo lolote, ninaweza kuondoka tu…, basi, nikaona nifungashe-fungashe vitu vyangu, nimempigia simu ndugu yangu aje kunichukua, japokuwa....’akatulia kidogo akimwangalia mtoto.

Wakati anaongea akili yangu ilishazama kwenye mtoto, nikawa namkagua,unajue tena sisi akina mama, macho yetu yameumbwa hivyo kudadisi, sura, umevaa nini upoje…kwahiyo kwa muda mfupi nilikuwa nimeshamkagua mtoto , usoni, ..na sikutaka kumuuliza kwanini kakatisha kuendelea kuongea, nikasema;

'Mhh, mtoto mnzuri kweli, halafu,ana kila ngapi, mnzito…….umegundua kitu,  kwanini watoto wachanga wote huwa wanafanana, maana namuona mtoto wako anafanana sana na watoto wangu, walipokuwa wachanga...’nikasema na  yeye akaniangalia kwa haraka, halafu akageuka kumwangalia mtoto wake, huku akitabasamu, hakusema kitu akawa anamweka vizuri.

‘Naona kweli ndoto yako imetimia, maana ule usemi wako wa kuwa unatamani mtoto wako afanane na watoto wangu, umekamilika…’nikasema

‘Mhh, nashukuru kwa hilo,ahsante sana rafiki yangu, bila wema wako sijui ingelikuwaje, .….’akasema akitabasamu.

‘Ni kweli, unajua rafiki yangu…ni kweli sasa kile tulichokitaka kimetimia, kweli mungu kasikia kilio chako…yaani nikimuangalia huyu mtoto wako, nakumbuka watoto wangu walivyokuwa wachanga,…’nikasema nikiendelea kumkagua mtoto.

‘Kwanza  angalia vimdomo vyake, na…na, macho yake japokuwa kalala.....yaani kama ungelimuweka na watoto wangu enzi hizo wakiwa wachanga, ungelisema ni mapacha na watoto wangu….’nikasema huku nikiendelea kumchunguza yule kachanga.

'Kweli,...japokuwa nilitaka wasichana kama wa kwako, na wawe mapacha kama wakwako, …unajua nilitakamani kuzaa mapacha kama wewe…lakini mungu kanipa mvulana, na kweli eeh,…kumbe … wanafanana na watoto wako, oh…’akasema

‘Unajua watoto wangu wanafanana zaidi na baba yao kisura , na kirangi wanafanana na mimi, watu wengi wanasema hivyo, hata wewe uliwahi kuniambia hivyo…’nikasema

‘Hivi eeeh, ni kweli, …anafanana shemeji…unajua nilikuwa sijaligundua hilo…akili yote ni kwenye furaha kuwa nimempata mtoto…'akasema na akawa kama anaonyesha uso wa haya, hata kuniangalia machoni inakuwa ni ngumu mimi sikuwa na mwazo yoyote zaidi ya kujua ni kufanana tu;

‘Mhh, nina hamu sana ya kumuona huyo shemeji, maana sipati picha, kama umeamua kumuhusisha basi hata mimi nastahiki kumuona, au sio,..kwani nikuulize huyo  shemeji yangu ni nani, nahisi kama anafanana sana na watoto wangu, je ameshafika kukuona?’ nikamuuliza

‘Bwanaeeh, hayo tuyaache kwanza, tutaongea vizuri tukifika nyumbani, najua una hamu kujua mambo mengi kwa wakati mmoja,…kila kitu nitakuambia,.. lakini kila kitu na wakati wake au sio, tukianza kuongea hapa, huoni watu watatusikia,a au….’akasema

‘Mhh, leo twaanza kufichana, haya bwana, lakini kama umeamua kumuhusisha huyo shemeji,…kiukweli sikupendezewa na hilo, halikuwa kwenye makubaliano yetu,  mimi ni mwanamke…, nipo kwenye ndoa, nafahamu ndoa ilivyo…hili lilitakiwa liwe siri yako mimi na wewe, sasa umeshaanza kuharibu mapema, sijui una lengo gani, sijapendezewa na hilo, kwanini ukamwambia huyo mwanaume…’nikasema

‘Lakini …sikupenda iwe hivyo,…nilijitahidi sana rafiki yangu… hata hivyo…sizani kama itakuwa na matatizo, sizani..’akasema

‘Najua haitakuwa na matatizo,…nitajitahidi kukusaidia, na kukushauri inavyotakiwa, ila nakuonyesha hatari yake,…ndoa ni kitu kingine,…na kwa hili, mimi nataka nionane na huyo shemeji nimsomeshe mwenyewe, ili aelewe…, sitaki uje kupata matatizo, sitaki nikuone unakuja kuishi maisha ya kujihami, maana hujui wanawake wa ndoa walivyo…’nikasema

 Nikamuuliza huku akilini nikimuwazia huyo shemeji, ambaye nahisi atakuwa akifanana na mume wangu, kwani kiukweli watoto wangu wanafanana na baba yao, na kiukweli, ukimuangalia huyu kichanga,  anafanana sana na watoto wangu.
‘Mwambie kuanzia sasa hatakiwi kabisa…na wala asije hapa kukuona…’nikasema

‘Mbona keshafika, alikuwa  wa kwanza kufika hapa, na ,na hukumuona huko nje, au aliniambia anasubiria nikiruhusiwa mapema, kama ndugu yangu hajafika atanichukua yeye,… yupo huko nje, ila mimi nimemkatalia kama ulivyonishauri,nimemuambia aondoke, sasa kama bado yupo huko nje shauri lake…’akasema

‘Ina maana alishafika…tatizo sikuingilia mlango wa kawaida, nimeingialia mlango wa mastafu…unajua rafiki yangu unafanya visivyo kabisa…’nikasema

‘Sikutaka kabisa yeye aje nilimuelezea yote hayo, kuwa kuanzia sasa sitaki anifuate fuate, lakini akasema na yeye atachukua tahadhari, hata hivyo hawezi kuniacha, …ndio maana alikuja mapema ili anichukue , halafu arudi nyumbani kwake…hata yeye hapendi…lakini unajua tena…hata hivyo nilimuambia huu ni ushauri wako …’akasema

‘Masikini…mmh, unajua naanza kuwazia mbali, huyo mke wa huyo mwanaume, unajua inauma sana....lakini tutaona la kufanya, ila nataka nionane naye huyo mwanaume kwanza ni muhimu nikutane naye nimsomeshe mimi mwenyewe.., kama ni lazima vitu vyote vipitie kwangu, na mimi nitajua jinsi gani ya kufanya…’nikasema

‘Usijali rafiki yangu, …mimi nataka hili jambo niliweke wazi kwako, ndio maana nataka tukaliongelee huko nyumbani, wewe ni rafiki yangu, najua hutanilamu kwa lolote lile, nilifuata ushauri wako tu…’akasema

‘Siwezi kukulaumu kabisa, kwanini nikulaumu..ushauri nimeutoa mimi mwenyewe, sasa itakuwa ni ajabu nianze kukulaumu, ila ni lazima tuchukua tahadhari, maana utu, ubinadamu,…kuna kuumia hapo, mwenye mume, akijua ni lazima ataumia, ndio hilo silitaki kabisa…’nikasema na rafiki yangu akawa kama ananywea fulani hivi.

‘Umefanya makosa sana…’nikasema

‘Usinilaumu rafiki yangu, maana nilifanya juhudi zote,….lakini ikashindikana…hata sijui alijuaje kuwa nimejifungua, sikutaka kabisa kumfahamisha hilo maana nilikuja kutoka Zanzibari kwa siri, na sikuwahi kumpigia simu, …’akasema

‘Sasa alijuaje…?’ nikauliza

‘Hata sijui, kaniambia … kumbe alikuwa akinifuatilia kila siku alipogundua kuwa nimefikia muda wa kujifungua, akawa anafuatulia nitakwenda hospitali gani, sijui kwanini …nashangaa nimejifungua, sina hili wala lile huyu hapa , akawa yeye ndiye  wa kwanza kuja kunipa hongera, na alipogundua kuwa nimejifungua mtoto wa kiume, amefurahi kweli kweli, nikampa onyo, kuwa huyo sio mtoto wake...’akasema

‘Kwahiyo kumbe mlikuwa mnaelewana sana na huyo shemeji, mlikuwa karibu sana kihivyo usinidanganye rafiki yangu, umefanya makosa ambayo utakuja kujijutia, nakueleza ukweli ulivyo…, inatakiwa tuwe makini kuanzia hivi sasa, utakuja kupata lawama kubwa sana.

‘Kuelewana kwa vipi, si tuliliongea hili kuwa nimetafute yule ambaye namuelewa sana,….na unajua,… nikuambie kitu, shemeji alinibana sana...mwanzoni nilimficha, lakini wanaume bwana, akawa akinidadisi mara kwa mara hasa alipoona mabadiliko, najuta kwanini nilishindwa kumdanganya, ...na tatizo kama nilivyokuambia awali , nilikuwa natamani sana awepo karibu yangu mara kwa mara..na…kila mara nataka angalau nisikie sauti yake, angalau, …mimba ina matatizo jamani….’akasema

‘Nayafahamu sana, ukiwa na mimba unaweza ukampenda sana mume wako au ukamchukia sana, inatokea hivyo, lakini mimi naangalia kote kote, kwa vile mimi ni mzazi, mimi nipo kwenye ndoa, nayafahamu hayo zaidi, jinsi gani mtu unavyoumia ukiibiwa mume wako…’nikasema

‘Usitake kunitia kwenye lawama tena, ushauri wako ndio umeifanya hii kazi, na najua wewe hutaweza kunilaumu kwa hili…’akasema kidogo akionyesha hasira.

‘Sio kwamba nakualaumu, ..unasikia kwa vile ni mimi nimeutoa ushauri, nataka ushauri uende ilivyo, isje ukapata matatizo, tunahitajika kuchukua tahadhari zote, unielewe hapo…’nikasema

‘Sawa basi tuondoke, maana dawa ndio hizo hap anazileta nesi, kila kitu sasa kipo sawa sawa….’akasema

‘Kwahiyo mimi nashauri ni bora twende nyumbani kwangu ili niweze kukusaidia vizuri, sitaweza kujigawa, mimi nilikuja na wazo hilo japokuwa sijaongea na mume wangu, lakini hili sio lazima nimuambie anakufahamu wewe kama ndugu yangu…’nikasema.

NB: Ngoja tuishie hapa kwa leo


WAZO LA LEO: Urafiki wa kweli hujengwa na kuaminiana,..kama mtakuwa manafichana mambo yenu, ujue urafiki huo una walakini. Lakini pamoja na hayo, tusiwe tunafanya mambo kama kufurahishana tu, unamshauri rafiki yako, ili tu afurahi, bila kujali athari zake mbeleni.

Ni mimi: emu-three

No comments :