Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Saturday, October 14, 2017

MKUKI KWA NGURUWE-7



Mume wangu aliponiambia yupo barabarani, nikakumbuka kitu, wakati tunatoka pale hospitalini, ..japokuwa sina uhakika sana, niliona kama gari la mume wangu likitoka,..unajua gari langu niliegesha sehemu ya nyuma ya jengo la hospitali…

Hapo nikawaza jambo, huenda mume wangu alikwenda kumuona mzazi hapo hapo hospitalini, ..sikuweza kukumbuka kumuuliza huyo mzazi alilazwa hospitalini gani, kama ningelijua kumbe ingelikuwa ni rahisi tu, ningelimuita aje tumuone rafiki yangu.

Lakini haikuwa na umuhimu kwa muda huo…

Tuendelee na kisa chetu…

**********

‘Mhh, aisee, mtoto wako anafanana sana na watoto wangu, sasa nimemwangalia kwa makini, mwanzoni nilijua ni kwa vile watoto wachanga huwa wanafanana sana wanapozaliwa…, lakini kwa huyu, nimehakikisha, anafanana sana na watoto wangu, isingelikuwa wewe ni rafiki yangu,… ndugu yengu, ningelifikiria vibaya, lakini sizani kama wewe unaweza kufanya hivyo hahaha, sina mawazo hayo mabaya, samahani…’nikasema

‘Kufanyaje…?’ akauliza akikwepa kuniangalia

‘Hebu tuyaache hayo, haya niambie ilikuwaje, ni nani huyo shemeji , maana umekuwa ukisema tu shemeji, shemeji, unajia nikuambie kitu, kila hatua navutika kufahamu ukweli, niambie nisibakie hewani, maana kiukweli umeweza…, hujafanya makosa, na umekipata kile ulichokitaka, mimi nakuaminia, sikufanya makosa kukushauri…’nikasema

‘Nikuambie nini tena rafiki yangu nimeshakuambia,… kosa la awali sitaki kulirudia tena, kuna kauli zako zimenitisha amani…, naona hata ushauri wako, haukuwa na usawa kivile…, ulinishauri tu, kwa kunifurahisha…’akasema akinikwepa kuniangalia machoni.

‘Mhh, sijakuelewa, hapo una maana gani, ina maana mimi nilifanya makosa kukushauri hivyo au….rafiki yangu hapo sasa wanifanya nitake uniambie ukweli,…sasa niambie ukweli, tusije kuudhiana bure…unanifahamu nilivyo, subira yangu ni kubwa lakini ikifikia mahali …inakuwa siwezi tena,.., unanifanya nianze kuvuta hisia ambazo hazipo na mimi sio mtu wa namna hiyo , hasa kwako..’nikasema

Rafiki yangu akabakia kimia, halafu akamuangalia mtoto wake, kwa muda huo nilikuwa naye mimi, ….akasogea na kumchukua, na mimi nikajiweka sawa, kusubiria maelezo,, namfahamu rafiki yangu huyo, akiamua jambo lake , kaamua, lakini pia ananifahamumimi nilivyo, nikisisitiza kitu ujue kweli ninakitaka, sio kawaida yangu kusisitiza kitu, kama hakina umuhimu,

Alitulia kidogo huku akimuangalia mtoto wake,…ilikuwa kama yupo kwenye wakatimgumu sana, nilitaka kumuambia basi, asiumize kichwa, lakini mimi nitakuwa sina amani, sio amani ya kutokumuamini, mimi namuamini sana rafiki yangu huyo,..ila hali ile ilinifanya intake nimfahamu tu huyo mwanaume aliyempa mimba sijui kwanini,

Baadae rafiki yangu akainua uso na kuniangalia,….uso ulikuwa kwenye hisia, ni kama mtu anayehisi maumivu, na kiukweli sikutaka mjadala huo uendelee, naona namtesa, lakini yeye baadae akasema;

‘Kwanini unataka niendelee kuharibu, si wewe ulishaanza kunilaumu kuwa nimeharibu, sasa kwanini tuendelee kufany ahivyo tena…?’ akaniuliza

‘Hapana…hata mimi sikulitaka hilo, ila hizo kauli zako, kauli zako zenyewe zinakusuta, zinavuta hisia nyingine kabisa,....nahisi kuna jambo unanificha, … isije ukawa kweli umetembea na mdogo wa mume wangu, hapana kama ulifnaya hivyo, sio vizuri, sijui lakini...!'nikasema na yeye hapo akacheka kidogo, na kilikuwa sio kicheko kile cha furaha ni kama kulazimisha hivi, yeye baadaye akasema;

'Hapana sijatembea naye, na kwanini…hahaha, hapana…bwana, na wewe mawazo yako ….katika wote, …huyo sikuwa na mpango naye kabisa, unajua aliwahi kunitongoza kipindi fulani, unakumbuka nilikuambia…na tulivyokosana naye pale, ikawa basi tena tatizo lake…, hajui kubembeleza, analazimisha, alihisi mimi ni muhuni, tokea kipindi kile sijawahi kuwa na uhusiano naye wa karibu, nikusalimiana tu kama tukikutana,…kiukweli, siwezi kuficha, awali nilitamani sana awe rafiki yangu, sasa alipokuja kuoa ndio ikawa basi, nikamtoa kabisa akilini mwangu...’akasema sasa kwa kujiamini.

‘Ulimtoa sasa ukamtafuta …hahaha, wewe bwana, nakufahamu ulivyo, ukitaka jambo lako hushindwi…au uniambie ukweli, ulimpata wapi mwanaume anayefanana na mume wangu,…na ni nani huyo, hapo ….sikuachii,… kama sio huyo basi ni nani mwingine,…niambie ukweli rafiki yangu..usiniache njia panda…’nikasema


‘Unajua …hadi hapa nakuona kama huna amani na mimi, na ndio maana najiuliza ule ushauri wako ulikuwa wa nini hasa, kweli ulitoka moyoni,….sasa nafikia kuogopa,..ni kweli, wewe ni rafiki yangu mkubwa sana, na mara nyingi tumekuwa tukishauriana mambo mengi, na mara nyingi wazo lako huwa nalichukulia kwa uzito mkubwa sana, …sikutaka nikufiche kwa hili, kabisa, nilipanga nikuambie kila kitu, lakini naona bora tuyaache tu, kwa usawa wa urafiki wetu..’akaniambia na mimi hapo nikasimama.

‘Hapana wewe niambie tu, ….usiponiambia moyo wangu utakuwa hauna amani….kiukweli ndio hivyo, sio kwamba nakudhania vibaya, katu wewe siwezi kukuweka huko huwezi na hutaweza, ila nataka kumfahamu huyo mtu tu..basi, ili niweze kukusaidia….’nikasema

‘Unakumbuka, niliwahi kukuambia kuwa  nawapenda sana watoto wako, na ningelifurahia kupata watoto kama wako…hilo lilitoka ndani ya nafsi yangu, ni kweli nawapenda sana watoto wako, na mimi nilitamani nipate watoto wanaofanana na watoto wako…’akamuangalia mtoto wake.

‘Na…, na uliponishauri hivyo, ..mimi nikaona nifanye juhudi za kumpata mtu atakayenizalia mtoto kama wako, na muda huo nilikuwa natamani nipate mapacha, kama wa kwako, ....’akasema na mimi nikamuitikia kwa kichwa na yeye akaendelea kuongea kwa kusema;

‘Nililiwazia sana hilo,…sasa nifanyeje,…ndio nikaanza kuwachuja watu ninao watamani, maana sio kupenda…siwezi kusema nilimtafuta nimpendaye, …hivi utampandaje mume wa mtu,nikaona nisicheze mbali,…kiukweli,  sisi ni marafiki wa kweli na tunaweza kufichiana siri...au sio rafiki yangu…?’ akaniuliza na mimi nikatikisa kichwa, .

‘Wewe na mimi ni kama pete na kidole….au sio…na umkuwa ukinipa kila ulicho nacho, na mimi halikadhalika, ilimradi tuchangiane kwa …urafiki wetu, hilo lipo wazi, wapo waliowahi kusema urafiki wa namna hiyo hawautaki…eti haufai, lakini mimi sioni kama kuna ubaya, au sio …?'akasema huku akisimama na kumlaza huyo mtoto kwenye kitanda chake chenye chandarua,

Unajua kiukweli, wengi watashangaa kwa hili, lakini kwangu mimi akili ilifungwa kabisa kumdhania  vibaya rafiki yangu..kabisa kabisa, rafiki yangu nilimchukulia kama mdogo wangu, kwahiyo nisingeliweza kumfikiria chochote kile,…, hata alipotoa kauli hiyo sikuwa na mawazo yoyote mabaya, mimi akili yangu ilifikiria kwingine kabisa,…nikasema

‘Sasa kwanini inanificha, unanificha hata mimi rafiki yako, nilijua tu..’nikasema hivyo, na yeye akanitupia jicho kidogo, na kusema;

‘Unajua sikutaka kukuambia moja kwa moja, kutokana na kauli yako uliyoitoa awali, nikaona bora nisiseme ukweli, hata hivyo….’akasema hivyo na kukatisha, huko kukatisha katisha maneno kwake, ndio kulikuwa kunanipa hamasa ambayo haikuwepo kichwani kwangu kabisa. Hata hivyo sio hamsa ya kumdhania ubaya, hivi ndugi yako anaweza kutembea na mume wako,..kiuhalisia…hasa awe ni ndugu unayemuamini….huwezi kufikiria hilo kabisa.

‘Lakini yule ni mdogo wa mume wangu huoni italeta picha mbaya…’nikasema , na yeye akanitupia jicho kwa sura ya kushangaa, akasema;

‘Hahaha… rafiki yangu, mbona hivi…mimi siwezi kukuficha, na …hebu tuyaache hayo jamani,…’akasema akionyesha ile ishara ya mikono ya kuupia jambo.

'Ni kweli kabisa sisi ni marafiki wa kweli...na hatuwezi kuangushana, lako ni langu na langu ni lako..nakubaliana na wewe, na wala usiwe na shaka na mimi, …mimi naona ajabu wewe kuogopa kuniambia ukweli, ….sasa nimeshaujua, hata kama, japokuwa bado nahitajia uhakiki wako,…mimi kama mimi  nakuahidi kabisa, hilo litaishia moyoni, na hakuna mwingine anayeweza kufalifahamu hilo zaidi yako na mimi,..na huyu uliyemuambia ukaharibu, hilo nakuthibitishia...'nikasema huku nikiweka kidole mdomo kama ishara ya kuahidi

‘Hahaha kweli rafiki yangu, mmh, mbona nitashukuru, ila sio huyo jamani, unayemfikiria wewe, haaah, mimi hapo siwezi kuelewa, nilijua una..umeshafahamu, maana ..aah, sasa hata sijui nisemeji,…kwanini huelewi….’akasema

‘Nimeshaelewa, nakushangaa leo ulimi wako unakuwa mnzito tu…imeshapita hiyo na maji yakimwagika hayazoleki labda yamwagike kwenye udogo wa mfinyazi uliokauka…hahaha…uliposema tu kuwa hukutaka kucheza mbali, basi hapo imejieleza kila kitu, usiwe shaka kabisa, mimi nimelipokea kwa moyo mmoja..., na wewe bwana kwa  kupenda stori ndefu, kwanini usiningeliniambia tu moja kwa moja kwa shemeji ndiye kayafanya hayo, basi, limekwisha, au….’nikasema

‘Tafadhali mimi nakuomba, tuyaache….’akasema

‘Tuyaache mbona unasema hivyo tena, au, …?’ nikauliza kwa kushangaa maana mpaka hapo nilishaamini kuwa ni mdogo wa mume wangu, ..yeye akabakia kimia, akiwa kainamisha kichwa chini.

‘Ina maana sio yeye, au…unaogopa nini kuniambia…?’ nikamuuliza

‘Tuyaache jamani…’akasema akitikisa kichwa.

‘Mimi nauliza tu, kama sio mdogo wa mume wangu ni nani mwingine anayefanana na mume wangu…, maana sasa unaanza kuniweka roho juu, kama tumechangia kuna ubaya gani, limetokea limetokea, eeh,....kwanini unaogopa kusema huo ukweli kuwa tumechangia, siwezi kukulaumu zaidi, ..najua wewe ni rafiki yangu, kuchangia, tunachangia sana, au sio,…sasa itakuwa …, mimi mkubwa na wewe mdogo mtu au…?’ nikasema na kuuliza.

‘Kama wewe ni rafiki wa kweli sizani kama hili jambo litakukwaza, ndivyo nilivyokuwa nimefikiria hivyo,…na…na…, na kama kweli ulikuwa na nia njema na wazo lako natumai hutaniona kuwa mimi  ni mtu mbaya, kwani yote niliyafanya kwa kufuata ushauri wako…. Zaidi ya hayo kuna kukosea, nimekubali nimekosea kuliweka hili bayana mapema…na kiukweli , hata mimi sikupenda iwe hivyo kwa hali hiyo, ila ningefanyaje basi, mmh,  …’akasema

‘Sijasema, au kukulaumu kwa hili kuwa umekosea kumchagua huyo…sawa  lakini picha kwa jamii, ndio maana nilisisitiza sana usiri..jamii itatuelewaje au sio…, ninachojiuliza ni kwanini unifiche kitu kama hiki ambacho watu baadae watakuja kujiuliza na wengine watapa mwanya wa kusema la kusema…sasa ni vyema ningelijua mapema ili tuweze kuweka, kinga…’nikasema

‘Mimi nilikuamini sana rafiki yangu kwa ushauri wako, nikaona ngoja nifanye kama ulivyonishauri...sizani kama nimekosea jambo, ni ushauri wako ndio umefanikisha hili, na...na nitafurahia sana na wewe ukilipokea hili kwa moyo mkunjufu...ndio maana sitaki nikufiche kitu...’akasema

‘Kiukweli umefanya jambo la maana sana, kwani hivi ndivyo nilivyotaka,…. Uzae uapate mtoto na wewe…, maana mtoto ana raha zake, wewe mwenyewe utaona, utakuja kuniambia…sitawezi kukulaumu kwa vyovoye vile, maana ndivyo nilivyotaka mimi iwe hivyo, na kwanini nikwazike kwa hili ilihali wewe ni rafiki yangu kipenzi na pia hilo wazo nilikupa mimi. Nikuambie ukweli wazo hilo nililiwazia sana kabla sijakushauri,na lilitoka ndani ya moyo wangu, nipo tayari kukusaidia kwa vyovyote vile….’nikasema kwa kujiamini.

‘Basi kwa vile umenihakikishia hilo na wewe ni rafiki yangu mpenzi, nitakuambia kila kitu bila kukificha, ila nakuomba uwe mkweli wa kauli yako hiyo,..kuwa utalipokea kwa moyo mkunjufua…na nanomba iendelee kuwa ni siri kati yangu mimi na wewe, ama kuhusu shemeji, basi, tutaona jinsi ya kufanya au sio …’akasema

‘Hapo sasa umenena, na …unajua yule haivani sana na kaka yake, kwahiyo sina mazoea naye sana, usiwe na shaka na hilo, na tutajua jinsi gani ya kumbana kiasi kwamba hatafunua mdomo wake, anamuogopa sana mke wake yule, unasikia…’nikasema

‘Tatizo, ….moyo unaniuma, na naingiwa na uwoga, sipendi kabisa urafiki wetu uje kuharibika kwa hili, nakuomba sana, maana sijui nitauweka wapi uso wangu kama wewe ukiamua kunisaliti, ukanitangaza vibaya kwa watu, nitavunjika moyo wangu sana tena san,… kama …oh, kama…wewe utafanya hivyo, lakini zaidi ya hayo nitaumia sana kama hili litakukwaza na kukuumiza…nakuomba sana, tena sana….for the sake of this baby…uwe mkweli kwa akuli yako hiyo’akasema akimwangalia mtoto wake.

‘Kwanini unasema hivyo rafiki yangu kama vile huniamini au mimi siakuelewa hapo,..kwa hili nakuhakikishia kuwa tupo pamoja…hili nimekushauri mimi na nitakuwa mtu wa ajabu kama nitakulamu kwa lolote lile…wewe niambie tu,na nimeshajua ila ni uhakika wako…mimi nakuhakikishia kuwa tutakuwa pamoja kwa lolote lile, si ndio hivyo…mmh, sasa moyo umetulia...’nikatulia kidogo

Yeye akatulia na mara alipoinu akichwa na kuniangalia nikaona machozi yanamtoka,…hapo nikashikwa na mshangao kidogo, sio rahisi kwa rafiki yangu kutoa machozi, akitoa machozi ujue limemfika kweli, kama mwanamke inatokea…hapo mimi kwa huruma  nikamsogelea, na kumshika, tukawa kama tumekumbatiaana kiupande upande…alitulia kwa muda, halafu akasema;

‘Rafiki yangu,.oooh, naumia, ….mimi ...nakuomba tuliache hili tu, nakuomba tena na tena, tuliache kama lilivyo, …sitaki,..na … nitaumia sana ikija kutokea kinyume na …..ulivyosema, ulivyoahidi, naogopa sana, kumbuka rafiki yangu ahadi ni deni, ulinishauri wewe, kumbuka hilo….’akasema

‘Hili ninakuthibitishia kutoka moyoni mwangu…, sizani kama huyo mke wa shemeji atalijua hili..zipo namna nyingi ya kulificha…tutashauriana muda ukifika…huyo hatajua kabisa …maana akijua vumbi lake naye sio mchezo…’nikasema

‘Hapo ndio waanza kuniogopesha…’akasema

‘Hatajua bwana…usiogope kabisa..nani atamuambia…mimi nakuahidi kama rafiki yako , mimi nipo tayari kupitisha rupia,… ikibidi…japokuwa ni mkali, lakini namfahamu  madhaifu yake,…yule mwanamke anapenda sana pesa,...usiogope kabisa...mimi na wewe hakitaharibiki kitu,..na kwanini ulie, hebu nikuulize, niambie ukweli ni nani mwingine analijua hili….ni mimi na wewe tu au sio, usije kuwaambia hata wazazi wako unasikia, ukiharibu tena huko shauri lako..’nikasema.

‘Oh, basi …mimi naona unipe muda,… niliwazie hili zaidi, nitakuambia kila kitu, usijali, sasa hivi akili yangu haipo sawa....nashukuru sana rafiki yangu…ningeomba nikapumzika, au…sio nakufukuza..jamani…ila kumbuka tu ahadi ni deni..’akasema

‘Mimi nimeshakuambia hakuna kitu kitaharibika niamini mimi rafiki yako, kwanini nikuahidi kitu halafu nije kukusaliti, haitatokea kabisa, nakupenda sana..wewe ni sawa na mdogo wangu kabisa….hata mume wangu namuambiaga hivyo,  na kila nikitaja majina ya wadogo zangu na wewe nakutaja, uone ninavyokuthamini, najua wewe huwezi kufanya jambo la kuniumiza mimi au mimi kufanya jambo la kukuumiza wewe….’nikasema

‘Mhh…hapo sasa….’akasema

‘Ndio hivyo…kwahiyo mimi  siwezi kuja kukasirika eti kwa vile umefanya hivyo kwa shemeji…, hapana na kama wazo nilitoa mimi eeh,  kwanini nije kuumia,…hapana nikifanya hivyo, itakuwa  ni ujinga, …siwezi na sitaweza kukusaliti, unasikia, sawa…kama wahitajia kupumzika basi wewe pumzika, sijui nikufanyie nini kwa hivi sasa…’nikasema

Na mara simu yake ikaingia ujumbe, akaichukua na kuusoma, halafu akanitupia jicho, na mimi nikajifanya kama sikumuona, akawa anaandika kitu kwenye simu yake, nahisi alikuwa akijibu huo ujumbe wa simu, halafu akasema;

‘Mimi naona wewe uende tu, usiwe na shaka na mimi, ndugu yangu anakuja, na nikikuhitajia nitakuambia, usiache shughuli zako, mimi nafahamu sana shughuli zako zilivyo, kazi kwanza au sio, hata mimi sizani kama nitajilaza tu kwa vile nimejifngua, mwili wangu ni kuhangaika sio wa kulala lala…’akasema

‘Sawa mimi naondoka naona hata mume wangu ananisisitiza kwa ujumbe wa maneno kuwa niwahi nyumbani …na nikichelewa sitamkuta, sijui ana jambo gani muhimu kihivyo..ngoja niondoke ..haya ..ooh, baby kalala, hivi jina bado eeh, ..’nikasema

‘Adamu….’akasema

‘Safi kabisa, …ooh,babu Adam…bakia kwa amani eeh, …’nikasema nikipitisha mkono na kumshika kwa mbali kichwani, na taswira ile ile ya watoto wangu wakiwa wachanga ikanijia, ..sijui kwanini….na simu ya rafiki yangu ikawa inaita, ..aliangalia mpigaji, halafu akaniangalia,

Mimi nikasema

‘Haya mimi naondoka, wewe endelea, nitarudi…’nikasema na akawa kama anataka kunizuia, nisiondoke, nilijua anataka kuniaga huku anataka kuongea na simu, nikasema

‘Wewe endelea usijali na wala usinisindikize…, nikatoka kwa haraka, nikiwahi kwenye gari langu, na..kuanza kutoka, na wakati natoka, gari kama la mume wangu likawa linakuja, …ikanifanya nisimame, nihakikishe kuwa ndio lenyewe, na linakwenda wapi…




WAZO LA LEO: Ni rahisi sana kutamka neno, hasa la kuahidi, na hata kuapa kuwa nitaweza kutimiza malengo au kutimiza jambo fulani vyovyote iwavyo. Ni vyema, tukawa na uhakika na kauli zetu hizo, na kama hujalifahamu jambo sio vyema kuahidi kuwa ni lazima ufanya hivyo, `lazima’ sio kauli nzuri. Tukumbuke kuwa Ahadi ni deni, na ukiahidi jambo ujue unahitajika kulitekeleza, na ukikiuka ujue umehini ahadi yako, ni hiyo ni tabia ya mnafiki.
Ni mimi: emu-three

No comments :