Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Monday, October 16, 2017

MKUKI KWA NGURUWE-8



Ikapita wiki, kutokana na shughuli za kazi nyingi, nikawa kama nimeshamsahau rafiki yangu huyo, na nikawa na migongano ya hapa na pale ya kifamilia, ni kawaida, lakini safari hi ilizidi, maana mume wangu ratiba zake zikawa hazieleweki sio kama ilivyokuwa awali, tukawa tunabishana, lakini kwangu nilichukulia ni mambo na kawaida tu.

Basi  siku moja nikapokea simu kutoka kwa huyo rafiki yangu, akaniambia kuwa anajiandaa kuondoka kwenda Zanzibar, kuna mambo muhimu anatakiwa kuyafuatilia

‘Mambo gani mbona mapema hivyo…?’ nikamuuliza

‘Kuna jambo natakiwa kwenda kulifanya, natakiwa kukabidhi kabidhi ofisi, kwani  inawezekana nikasafiri kwenda kusoma nje ya nchi…niliwahi kukuambia kipindi fulani kuwa niliomba kwenda kusoma, sasa imetokea kipindi hiki na mimi siwezi kuachia hiyo nafasi,…’akasema nilitaka kumuuliza na mtoto vipi, nikasita yeye akasema

‘Na uzuri..haitakuwa muda wote, nitaweza kulea na kusoma, mfadhili wangu kasema hilo halina shida..kwahiyo  sitakuwa na muda wa kukabidhi, nikimaliza likizo yangu ya maternity, yawezekana nikaondokea huku….’akasema

Ilinisthua kidogo, ikizingatiwa kuwa mtoto bado mdogo, sikumuulizia sana kuhus mtoto,…. kwasababu hapa kati kati tulifikia sehemu hatuelewani na yeye kabisa, alichoka na maswali yangu na  hata kufikia kusema niache kumfuta fuata masiha yake na mtoto wake.., kauli hiyo ikaniudhi sana, ikabidi kweli nimuache na maisha yake. Hata hivyo kiukweli, sio kwasababu hiyo, ila sikuwa na muda wa kukutana naye mara kwa mara, majukumu yalizidi sana.

Tuliongea kidogo kwenye simu …tukamaliza hivyo tu, na sikuweza kumpigia tena , na siku mbili baadae akapiga yeye, nahisi ni pale aliponiona nipo kimia, akasema;

‘Rafiki yangu vipi, nilijua utakuja, kabla sijaondoka, si nilikupigia simu jamani, sawa najua labda, bado umenikasirikia,… lakini utakuja kuelewa tu, baadae, …ila nilikuwa na ombi moja kwako, kwa vile wewe nyumba yako ina nafasi naomba baadhi ya vitu vyangu nije kuviweka kwako maana hizi nyumba za kupanga nikiondoka, vitakuwa havina usalama kabisa....’akasema

Kiukweli mimi sikuwa na hasira kihivyo, hasira zangu ni za hapo kwa hapo..na ukiniudhi naweza kufanya jambo kubwa hapo hapo…baada ya hapo, mambo yamekwisha, ila …kiukweli naweza kufany ajambo baya huwezi amini,..mimi kwa hilo nilishaliondoa nafsini kwangu sikuwa na kinyongo na yeye,..nikasema hakuna shida, nyumbani kwangu ni kwake, nikazidi kumsisitizia kwa kusema;

‘Wewe ni rafiki yangu bwana, hakuna haja ya kuniomba, hapa ni nyumbani kwako pia, watoto wanakuulizia kila siku, wewe lete vitu vyako na wewe kama mkataba umekwisha kwenye hiyo nyumba haina haja ya kulipia tena, njoo ukae hapa, mapak siku ukiondoka, ...’nikamwambia.

‘Hapana, sina maana hiyo, na sitaweza kufanya hivyo, urafiki wangu usiwe mzigo kwako, umeshanisaidia mengi sana, kiasi kwamba najihisi vibaya, na ..hata sijui nitawezaje kulipia hayo,…. ninachokuomba kwa sasa ni hilo tu....’akasema.

‘Sawa hamna shida, wewe vilete wakati wowote utakapopata nafasi, au nikipta nafasi, hata kama wewe haupo ninaweza kuja au kutuma gari likaja kuvichukua haina haja ya kusumbuka sana, ila nitajitahidi nije kabla hujaondoka..’nikasema, nikiwa na mambo yangu mengi shughuli zangu, na sikutaka kuongea naye zaidi, hasa kuhusu maisha yake alishasema hataki nikikutana naye tuyaongelee maisha yake, hasa kuhusu mtoto na aliyezaa naye.

Kesho yake nikapata nafsi nikaona nimpitie kidogom, nijua kinachoendelea, na kama vitu hivyo sio vingi, na kaviandaa, basi ninaweza kuondoka navyo, kwa kukodi gari, sikutaka kumpigia simu, mimi mwenyewe nikaenda nyumbani kwake…kwa mbali niliona gari kama ya mume wangu, lakini sikuwa na uhakika kama ilitokea kwake, au ilikuwa inapita tu, na mume wangu alikuwa kwenye mkutano.

‘Hivi mkutano ulishamalizika,..au kuna mtu kamtuma na gari lake…?’ nikajiuliza, nikataka kupiga simu kwake, lakini ikaingia simu ya mteja wangu muhimu, nikajikuta naipokea kwanza, na nilipomaliza kuongea naye , nikiwa nimesimamisha gari nyumbani kwa rafiki yangu,..nikawa nimeshaua kumpigia simu mume wangu

Rafiki yangu alikuwa kasimama mlangoni kwake kunikaribisha, nikamsogelea tukasalimiana kama ada yetu, nikaingia ndani na swali la kwanza likawa hili.

‘Mtoto kalala…?’ nikamuuliza

‘Ndio….’ Akasema ile ya kulazimishwa, sio sauti kama ile niliyo-izoea, halafu akauliza

‘Hujakutana na….’akasita,kwani simu yake iliita, akaisikiliza kwanza kwa muda, akasema

‘Nimekuelewa hamna shida, lakini niache kwanza, sitaki, sikiliza, nilikuelezea, msimamo wangu basi…’akasema na kukata simu.

Alionekana kama ana hasira na hataki kuongea, akawa kama anataka kuniambia jambo lakini anasita, nilihisi hivyo, ila na mimi nikasimamia kwenye msimamo wangu kuwa sitamuuliza tena kuhusu maisha yake na mtoto, …kwa jinsi alivyo  nilijua ana tatizo.

Baadae mtoto akawa analia, kwahiyo akaenda kumchukua, na kumnyonyesha alipomaliza, akanipa nimpakate ili aniandalie kinywaji, ndivyo tulivyozoeana , nilitaka kujiandalia mimi mwenyewe, maana anajua mimi ni mpenzi wa sharubati ya baridi,… lakini akasema hapana

‘Wewe mpakate mtoto ..hujamshika tokea siku ile….’akasema na mimi sikukataa nikamchukua mtoto.

Unajua mtoto wa mwenzako hakawii, sasa anageuza macho, anangalia, na sura halisi inaanza kuonekana, sura haikujificha alikuwa akifanana kila kitu na watoto wangu, maana watoto wangu wanafanana, ni wale mapacha wanaofanana kwa kila kitu, mimi akilini nikaweza hitimisho kuwa rafiki yangu atakuwa atakuwa katembea na mdogo wa mume wangu. Hata hivyo sikuweza kuvumilia nikamwambia;

‘Hapa sasa haijifichi kitu, lakini tuyaache hayo, lini unaleta hiyo mizigo, au nitafute mtu tupakie, kukurahisishia kazi…’nikasema

‘Haijifichi nini, usianze yale mazungumzo tena, nimefikiria kwa makini nimeona, ni bora iwe hivyo, libakie kama tulivyokuliana basi… sasa ibakie utakavyofikiria wewe inatosha,..’akasema.

‘Hamna shida, isiwe taabu, sasa unasemaje…?’ nikamuuliza

‘Nilitamtafuta ,mtu, kuna mambo sijayaweka sawa, kuna mtu ananisumbua akili yangu, sipo sawa, ila nimeshukuru kuwa umafika….’akasema

‘Ok, sawa mimi naondoka…’nikasema

‘Kuna kitu nilitaka kukuambia, lakini bado sijawa na uhakika, nataka nipate ushahidi halafu tutaongea….’akasema

‘Kuhusu nini….?’ Nikauliza

‘Nataka uwe na amani na hili jambo tulimaliza kabisa….’akasema

‘Jambo gani…?’ nikamuuliza

‘Kuhusu huyo mtu niliyezaa naye….’akasema

‘Sijakuelewa bado…na usiumize kichwa chako kabisa,..kama hutaki nijue haina shida, ..mimi nakujali sana, sitaki uumie, uwe na wakati mgumu kwa ajili yangu,…mimi nina amani kabisa, sina kinyongo na wewe, naahamu una sababu yako muhimu tu y akufany ahivyo….’nikasema

‘Unajua mimi linanisumbua sana, nimejaribu kuliwazia tukio zima la siku ile sijaweza kulithibitisha,…sijawa na uhakika ilikuwaje…’akasema

‘Tukio gani…?’ nikamuuliza

‘La kuipata hiyo mimba….’akasema

‘Mhh..sikuelewi, ...usinidanganye rafiki yangu..wewe sio mtu wa kubakwa, wewe sio mtu wa kufanyiwa tendo bila rizaa yako, nakufahamu sana, kwa hilo usinidanganya....’nikamwambia, ni kweli rafiki yangu ni mbabe, mjasiri na anajiamini, anaweza kupambana na midume, hata kama ni kwa kupigana ngumi.

‘Kwakweli siku ile, nilizidiwa, na sijui kwa vile nilitaka iwe hivyo, ndio maana sikujali, hata hivyo nikuambie ukweli, sikuwa nimepanga itokee hivyo, sio siku ambayo nilisema leo nataka nikafanye hivyo, hapana, ...ilitokea tu , na huenda ilipangwa iwe hivyo, kwa kifupi siwezi kukumbuka siku ile nililewa...’akasema.

‘Ulilewa, ulianza lini kunywa…?’ nikamuuliza

‘Siku hiyo hiyo…na nilijuta …na mara pili, nikarudia tena, ..na kilichotokea ndio nikasema sitakunywa tena,…najuta…’akasema

‘Wewe mtu…..ina maana ukinywa pombe…na wewe uliwahi kuapa kuwa katika vitu ambavyo hutaweza kuvitumia kimojawapo ni pombe…?’ nikamuuliza

‘Nimevunja miiko mingi sana ya kwangu, na kila nilichokifanya kwa kuvunja miiko yangu nimekuja kupata matatizo makubwa..hadi sasa sina amani…’akasema

‘Ilikuwaje maana wewe mwenyewe ndio umenichokoza, nilipanga nisikuulize tena, lakini umelianzisha wewe mwenyewe, utanieleza au niondoke, na nikiondoka sitaki tena kuniambia kuhusu maswala yak ohayo…’nikasema

 ‘Sawa kama umeamua hivyo, mimi nitakuambia ilivyokuwa siku ile, na wewe mwenyewe utajaza,…na naomba usije ukanilaumu,....maana wewe mwenyewe ndiye uliyenishauri...’akasema na mimi nikafurahi tukakaa na kuanza kuongea, na yeye alianza kusema hivi;

Siku uliponipa ushauri wako, moyo wangu ulianza kuwa na shauku, …nikawa na hamu sana ya mtoto kuliko siku zote,….nikawa nawaza sana kupitiliza mpaka watu wakanifahamu kuwa nina mawazo…niliwazia nikiwa nimempakata mtoto wangu, na hasa wawe mapacha….nilipata shida sana....’akatulia kidogo.

‘Unakumbuka ulivyoniashauri, nimtafute yoyote hata awe mume wa mtu nifanye naye tendo kwa minajili ya kupata mtoto, na nilijiuliza nitamuendeaje mwanaume bila..unajua mume ndiye anakutongoza, au sio..sasa nitakuwaje na uso usio na aibu….haraka nikasema kwanza labda nitafuta kitu cha kuniondoa aibu,…’akasema.

‘Ndio ukaenda kulewa…kwenye mabar, au ilikuwaje…nashindwa hata kukuelewa, kwanini usingeliniomba ushauri nikakuelekeza jinsi gani ya kufanya…’nikasema

‘Unajua rafiki yangu, kinachonishinda kwa hivi sasa ni kuhusu shemeji…’akasema

‘Nani, huyo bwana mliyezaa naye…?’ nikamuuliza

‘Ndio.....’akasema.

‘Kasemaje…? Nikamuuliza.

‘Ndio, kaniomba sana, tena sana hata kulia, hata kunipiga magoti, kuwa nisimwambie yoyote kwa sasa iwe siri kubwa kwani kuna mambo kayagundua yanaweza kumleta matatizo kwenye familia yake….’akasema

‘Ni sawa,…hata mimi nilikushauri hivyo, je labda mkewe keshamuhisi vibaya au….?’ Nikamuuliza

‘Anasema…kuna mambo yake ya kifamilia, ambayo hataki yaharibike, na ikigundulikana kuwa ana …mtoto nje, atayaharibu..ok, mimi nilion  ni jambo la maana, kama na yeye kakubali iwe hivyo itakuwa ni heri kwangu…ila kwa masharti kuwa anataka mtoto atambulikane kuwa ni kwake kwa siri..hapo ndio tukaanza kukorofishana,...’akasema.

‘Unakubali nini na unakataa nini, kosa umelifanya wewe mwenyewe, kwanini toka mwanza usingelimdanganya kuwa mimba sio yake,..hii inaonyesha kuwa ulitaka afahamu, na huenda ulifanya hivyo kwa dhamira fulani ambayo unaogopa kuniambia...’nikasema na yeye akainama chini kuashiria kuwa kauli yangu umemgusa moyoni.

‘Kwa hali kama hiyo nimeona nisimwambae yoyote ....shemeji kaniomba na mimi nikamuahidi iwe hivyo, kwa masharti kuwa na yeye asinifuate fuate tena..lakini naona yeye kaanza kuvunja ahadi, kila siku hodi, na mbaya zaidi ananunua vifaa vya mtoto..sipendi, na ndio maana ilipotokea nafasi hiyo ya kusoma mimi nikaikubali kwa haraka sana, na sijamwambia kuwa mimi nakwenda kusoma nje....’akasema.

‘Kwahiyo eeh, unajua mimi unaniweka kubaya, …mimi naona nikuache na mambo yako, kwani kila hatua unanitamanisha intake kumfahamu huyo shemeji, na hutaki kuniambia ni nani…tuyaache kama ulivyosema au…?’ nikamuuliza nikiwa nimekunja uso kwa hasira.

‘Mimi nitakuambia jinsi ilivyotokea siku ile...au niache maana wewe unakimbilia kumjua huyo shemeji lakini hutaki kujua ilitokea vipi, nataka ufahamu ilivyotokea, ili uone kuwa sikuwa nimekusudia siku ile,…japokuwa tulipanga iwe hivyo, lakini sio kwa huyo na …hata sijui, nisemeje ndio maana nataka nikuelezee ilivyo kuwa na sio alzima nikutajie kwua ni nani...’akasema

‘Sawa hebu elezea, uonavyo wewe… maana na wewe sasa unajifanya mtunga tamithiliya, wengine hawapendi vitu virefu, sawa mimi sijali ila unipe kitu cha ukweli, sio hadithi za kubuni...’nikasema kutoka moyoni hadi hapo sikuwa na dhamira yoyote mbaya dhidi yake, sikua na wazo kuw ahuyu mtu anaweza kunifanya chochote kibaya, yaani sijui kwanini ilitokea hivyo, maana pamoja ya kuwa ni rafiki kwangu mimi nilishamweka kuwa ni ndugu yangu…moyo wangu umejengwa hivyo kuamini watu.

‘Baada ya ule ushauri wako, nikajikuta nakutana na wanaume wale ambao wana watoto ninaowapenda, nilijipangia kama karatiba fulani, ..ni ngumu lakini…kwahiyo ikawa inatokea awali, kwa huyo na yule lakini ghafla ikaja kubakia kwa huyo mtu mmoja, bila hata kukusudia,…

Cha ajabu sio kama awali wengi wakinialika kwenye chakuala cha jioni, inaishia kula na kunywa kidogo basi, tunaagana imekwisha, nahisi walishanisoma, na wengi hawakutaka kuniomba tufanye lolote zaidi ya hapo, ni ile raha ya kukaa na mimi kula kuongea, inaishia hapo tu,…na mimi  sikuweza kushinikiza ili lifanyike hilo tendo, siwezi, ningalianzaje..na hata  kwenye akili yangu bado nilikuwa na shaka...’akatulia.

‘Kwahiyo baadae ndio akabakia huyo mmoja ambaye hutaki kumsema, japokuwa mimi nimeshamfahamu kuwa ni nani, au sio… shemeji yangu wa ukweli.. au sio..?’ nikamuuliza huku nikicheka.

‘Ndio, sijui ilitokeaje, …ilikuwa kila nikienda kupoteza mawazo, shemeji yumo..ni kama ananifuatilia nyuma, utafikiri alikuwa ananilinda, au hata sijua ni kwanini alikwua akifanya hivyo, na ndiye niliyekuwa nikijaribu kumkwepa kuliko wengine, lakini haikuwa rahisi, kila nikitaka kutoka shemeji yupo nyuma, akiona sina mtu, anakuja kunipa pambaja,…nikaanza hata kuogopa, nikifahamu ukaribu wangu na mkewe, na familia kwa ujumla....’akasema.

‘Ok,…tuendelee..’nikasema.

‘Lakini mimi naona tuache tu kuyaongelea haya,…’akasema

‘Umeshaanza, siwezi kuondoka mpaka uelezee, hapo utaniuzi, hatutaelewana…’nikasema

‘Sawa, ngoja niendelee,  maana hata mimi sijawa na uhakika, ni  kwanini litokea hivyo na je ni yeye kweli,..nachanganyikwia ndio maana sina raha na kwanini ilitokea siku zote mbili, ilikuwa kama….haa, hata sijui nisemeje,....’akasema.

‘Sawa endelea ilikuwaje, ...kwani naiona hiyo sasa ni tamithilya fulani , kuna kitu unanificha na nitakigundua tu,...’nikasema.

‘Ofisini kwangu kupo karibu sana na ofisi za shemeji..’akasema.

 ‘Ok…ni sawa, ...ndio maana ilikuwa ni rahisi sana, kwako wewe ..mmh najaribu kujiuliza ni nani pale anafanana na mume wangu, mbona wengi wanaofanya kazi pale nawafahamu hata huyo mdogo wa mume wangu yupo karibu sana…ok..na upande huo wa pili yupo mume wangu,…, sasa naanza kuelewa, tuendelee..’nikasema na yeye akaniangalia huku akijaribu kutabasamu lakini uso ulikuwa umejaa huzuni.

‘Ndio ni kweli ndio maana ilikuwa ni rahisi sana kwake.., kuniona nikitoka, na niliona kama kadhamiria kufanya hivyo, na mimi hata nilivyojaribu kumkwepa ikawa haisadii, nikaona isiwe shida, kwanza ni mtu ninayemwamini hawezi kunifanyia lolote baya na anafahamu kabisa kuwa mkewe ni mtu tunayefahamiana sana naye...’akasema.

‘Mhh, ndio nafahamu si mlikuwa mashoga kipindi fulani na mkewe.., nikafikia kukukanya kuwa huyo mwanamke haaminiki, anajaribu tu kuficha ule ubaya wake , ili uone ni kawaida tu…maana kama angelikuwa rafiki wa ukweli, asingelikuibia mchumba wako, …mara nyingi marafiki wanaweza kuwa hivyo, unatakiwa rafiki awe kweli rafiki mnayeaminiana, ambaye huwezi hata kumdhania ubaya, au sio..?’ nikamuuliza na yeye akatikisa kichwa kukubali, hakusema neno

‘Ni kama mimi na wewe, mtu hawezi kuniambia kitu kibaya kuhusu wewe, najua huwezi kamwe kunifanyia mabaya, kama mimi nisivyoweza kukufanyia mabaya, mtu kama humfanyii mwenzako ubaya, huwezi kufanyiwa ubaya, au sio..itakuwa ni ajabu sana wewe ukinifanyia ubaya, au sio…....’nikasema na yeye akatabsamu na kusema.

‘Mhh, mabaya kama yepi tena rafiki yangu, wakati mengi tunafanyiana baada ya kushauriana…?’ akaniuliza

‘Kama aliyokufanyia yule rafiki yako, mtu unamuamini, halafu anakuja kukuibia mchumba wako…kiukweli inauma, kuibiwa mume au mke, unajua inatokea kama nilivyokushauri,au sio, na huwezi kumfanyia rafiki yako, mpendwa,, ni lazima utafanya mbali kabisa,…maana kama ni rafiki yako, mtaumizana sana…’nikasema

‘Mhh…hapo sasa…’akasema, akijikuna kichwa, halafu akajaribu kutabasamu na kusema;

‘Nimewaza sana hili…..naona bora ….nikuambie tu, ilivyotokea…’akasema

‘Ikawaje hebu endelea bwana, acha kusua sua, usinipe ugonjwa wa moyo….’nikasema

‘Basi kutokana na hali hiyo, kuwa mke wake namfahamu, ni mtu tunaheshimiana, nikaona nisimzalilishe, maana kama unavyonifahamu,  huwa simkopeshi mtu, huwa siogopi mtu, kama sitaki sitaki...naweza nikamtolea nje mbele za watu akabakia kuzalilika na nisingeliweza kufanya hivyo kwa shemeji....’akasema.

‘Ni kweli mimi nakuaminia,ndio maana hilo lililotokea siwezi kuamini kuwa lilitokea bila ya ridhaa yako, wewe utakuwa ulikubaliana nalo, vinginevyo kuna kitu unanificha, na sipendi unifiche kitu, maana nikigundua, haaa..weee, si unanijua nilivyo, mume wangu mwenyewe ananiheshimu kwa hilo, ananiogopa, ndio maana anajitahidi kuwa mkweli kwangu, kama nilivyo kwake...’nikasema.

Hapo akatulia kidogo kama anawaza jambo, baadae akaendelea kunihadithia…

‘Ikawa kila nikitoka kwenda kula jamaa huyu hapa, nikitoka kwenda kazini, jamaa huyu hapa, ikawa kila siku nakutana naye, nikajikuta sina raha, na hata yeye akaliona hilo,…lakini akaniambia niwe na amani, atajitahidi kuhakikisha hatuvunji heshima yetu, …kiukweli hata lile wazo likafutika, sikutaka tena,… lakini moyoni...nilikuwa unanijia ule ushauri wako,na nikawa natamani ufanye kazi, lakini sio kwa huyo mtu, mume wa mtu, siku zinasogea...’akatulia kidogo.

‘Endelea…nina muda kidogo…ila najiuliza kwanini ulipoteze muda kwa huyo mtu, maana hapo ulikuwa unajichora kwa watu, walikuona, wanakuona au sio, kwahiyo hadi hapo wana ushahidi bayana  ….hapo eeh, uliharibu…’nikasema

‘Kwa vile ni jamaa, ambaye…ni..ni .. shemeji yangu, sikuona tatizo, na ..unajua nisingeli…mkatalia hata chakula, japokuwa awali nilikuwa nafanya hivyo….’akasema

‘Ok nimekuelewa, sasa nikuulize katika wanaume wote wewe uliona huyo ndiye anakufaa au kwa vile ulihisi atakuzaliwa watoto sawa na wakwangu au…?’nikauliza

‘Kiukweli ndio hivyo, kama ungelianiambia nichague ni nani wa kunipa mimba, kama hakuna kikwazi, mimi kutoka moyoni, ningelimchagua yeye....lakini kutokana na ukaribu  ulivyo hapana,  sikupenda litokee kwake, lakini ndio hivyo, watu husema litokee ili liwe fundisho,...kwakweli hadi sasa siwezi kuamini, sikujua kabisa kuwa nitakuja kuzidiwa kiasi hicho…ni pombe, sitarudia tena…’akasema.

‘Hebu kwanza nikuulize yule jamaa anakunywa, unajua mimi simpafahamu vyema maisha yake, na unijuavyo huwa sifuatilii maisha ya watu wengine hata mke wake hatupo karibu kihivyo, japokuwa ni mke wa shemeji yangu…?’ nikamuuliza


‘Anakunywa lakini sio kihivyo….’akasema

‘Mhh, hawa wanaume jameni…. unajua nilikuambia hata mume wangu anakunywa, lakini akiwa na wazee, watu wa heshima wa dini, anajifanya mtu wa dini sana, na kupinga ulevi,....mimi nafahamu siri yake, uzuri wake hata akinywa huwezi kufahamu, anajitahidi sana kujificha…, nimemkanya sana tabia hiyo ya kunywa pombe…, yeye anasema anakunywa kwa dharura, na kidogo sana…’nikasema

‘Wanaume wengi wapo hivyo….sioni ajabu kwake,…’akasema.

‘Ilikuwa sio sana kama ilivyotokea baada ya kunipa huo ushauri, mwanzoni nilikuwa nakutana naye, anaiomba tukale chakula pamoja, tunaongea,…ananishauri kuhusu maisha, ni nani angelipenda awe mume wangu,…nikawa nimezoeana naye sana, nikiwa sina raha, yeye anipa ushauri , lakini sikuwa na wazo jingine lolote dhidi yake, na yeye alilitambua hilo...’akasema.

‘Mambo ya shemeji hayo , nafahamu sana ulichompendea, ni kw vile kwanza ni mtanashati,…. mrembo kama mume wangu, wanafanana sana, na mume wangu, kwahiyo nahisi ndio sababu ulimpendea hivyo au sio..?’ nikamuuliza..

Kwanza akaniangalia kwa makini, halafu akawa kama anasita kunijibu baadae kwa shingo upande, akiwa kainamisha kichwa akasema…..

Nb….naona inazidi kuwa ndefu na muda umekwisha, ngoja niishie hapa kwa leo


WAZO LA LEO: Urafiki wa kweli ni ule wa kuangalia athari za kila jambo kuwa unalolifanya halitamkwanza mwenzako,... ni hilo litafanikiwa pale utakapojiuliza je, kama nitafanyiwa  mimi jambo kama hilo nitafurahia au nitachukia. Tukiwa na tabia hiyo ya kuchuja matendo yetu kwa wenzetu nina imani kuwa hatutachukiana, tukumbuke kuwa ubaya kwe wenzetu unauma kama vile tungelifanyiwa sisis, kwani mkuki sio nguruwe tu, na kwa binadamu mchungu.
Ni mimi: emu-three

No comments :