‘Shemeji samahani nilikuwa nataka kukuuliza maswali kama
hutojali...’ sauti hiyo ilinishitua kutoka kwenye dimbwi la mawazo ya maisha
yangu yaliyopita.
‘Unaonekana upo kwenye mawazo mazito, pole sana, najua
unavyojisikia lakini usijali mumeo atapona tu….lakini baada ya hili, nawashauri kwa nia njema tu mkae muone tatizo lipo wapi ….’Alikuwa ni docta ambaye alizoea kuniita
shemeji.
Docta mara nyingi amekuwa mshauri wangu, hakujali yaliyopita kuwa tuliwahi kuwa wapenzi, hakujali, kuwa huyo
mume wangu ndiye aliyefanya akanikosa mimi..ndio hapo unapoweza kumuona docta
mtu alivyokuwa mtu wa peke yake.
Nikamwangalia machoni kabla ya kumjibu, na yeye kwanza
akatabasamu, pili akaonyesha uso wa kushangaa, na kabla hajasema lolote zaidi
nikasema.
‘Naomba usiniulize maswali ya kuzidi kuniumiza kichwa changu,
maana leo imekuwa siku ya mikasa kwangu, hapa nilipo nina mawazo emngi sana....’nikasema.
‘Lakini, …mmh, naweza kusema haya yote umejitakia mwenyewe,
usimlaumu mtu yoyote, wazazi walikuambia kuchia mimi mwenyewe, ..anyway, ...sitaki kurudi nyuma, lakini
wewe mwenyewe unalitambua hilo...’akasema .
‘Ndio hayo siyataki kuyasiki, maana hayatanisaidia kitu,..nafahamu
sana unamaanisha nini, lakini nikuambie ukweli, haya yanayotokea hayana msingi
kabisa na mambo yetu ya nyuma, na unafahamu kabisa kwanini nilichukua uamuzi
huo, na sitajutii kwa hilo...’nikasema.
‘Kulipa fadhila...eeh, haya endelea kulipa fadhila, kiukweli, mimi
nimekuvulia kofia, upo tayari kuyaweka maisha yako, rehani…kwa sababu ya kulipa
fadhila, na nini unakipata sasa, eeh, mimi nitaendelea kukusaidia tu, hilo
nakuahidi …’akasema
‘Najua wewe na wazazi wangu mtasema hivyo sana, ..lakini hamjui ni
nini kilicho moyoni mwangu, mume wangu nampenda na nilimpenda toka siku ile ya
kwanza, nilipomuoana akiwa na hali yake hiyo hiyo ya umasikini..’nikasema
‘Sio kweli…uwadanganye wengine, lakini sio mimi…’akasema
‘Lakini kwanini unasema hivyo, mimi nimefanya kosa gani, kuwa eti
kwa vile nimeolewa, mnayemuita wa daraja la chini au masikini,…hahaha, hebu niambie sasa hivi ana umasikini gani,
mbona mpo sambamba kimaisha, ni hali ya kusaidiana na kuinuana,....’nikasema
kama namuuliza.
‘Mimi sijakulaumu kwa uamuzi wako huo, lakini tabia za watu
hazijifichi, zingine ni za kihistoria, hata ufanyaje ni kama vile wanavyosema, …mmh,
kuwa kunguru hafugiki,.. na ndivyo
maisha yetu yalivyo, misingi ya kizalia ni vigumu sana kuigeuza...unajaribu
lakini ipo siku itatokea na tabia itajionyesha na kukuathiri...’akasema.
‘Tatizo lako wewe ni dakitari lakini ukifikia kwenye maswala haya
unaacha udakitari wako pembeni, hutaki kuutumia hata katika mambo kama haya,
kizalia kina nini na maswala ya mapenzi, ..kuacha kuolewa na wewe imekua ni nongwa, kwani huyo mkeo uliyempata
humpendani...mbona mimi sijaingilia maisha yenu..?’ nikamuuliza.
‘Tuyaache hayo nataka kukuuliza mambo ya msingi, maana pamoja na
yaliyotokea nyuma, bado nakuona wewe ni rafiki yangu, na mumeo ni rafiki yangu pia,
ndio maana nilipogundua kuwa ndio yeye unayemtaka, sikutaka kupambana kwa
vyovyote vile, niliona nikuachie tu, kwa vile ulinitamkia mwenyewe kuwa
unampenda,..na ukaja kunitamkia kuwa mimi hunipendi tena…, nikaona kwanini
ning’ang’anie mtu asiyekupenda,.....’akasema.
‘Uliza maswali yako bwana, sijasema kamwe sikupendi, nilikuambia
sababu za uamuzi wangu, na unazifahamu sana ...’nikasema na yeye akaniangalia
kwa muda, halafu akasema;
‘Nataka nikuulize maswali ya ndoa yenu,...’akasema
‘Kama ni maswali kuhusu ndoa yangu, ningelifurahi kama ungeyaacha
kama yalivyo, kwani akili yangu haijatulia, siku ya leo imekuwa ni ya mitihani,
tangia asubuhi, ni matatizo, ofisi matatizo..nyumbani matatizo, huko kwa rafiki
yangu matatizo..’nikasema
‘Kwa rafiki yako kuna matatizo gani…?’ akaniuliza
‘Haya hebu niulize, tuyaache hayo, unataka kuniuliza kuhusu nini?’
nikasema nikijua ni yale yale ambayo mara kwa mara ananilaumu eti kwanini nilimkataa
yeye nikaamua kuolewa na huyo rafiki yake.
‘Shemeji ...rafiki yangu…mpendwa…hahaha, wakati mwingine naogopa
kuongeza maneni hapo..nikuambie kitu, iIli kuondokana na huko kuchanganyikiwa
kwako ni bora ukajaribu kuyaongea hayo matatizo uliyo nayo kwa mtu anayeweza
kukusaidia,..’akasema.
‘Hapana, mimi nakufahamu bwana, ...wewe na wazazi wangu siku zote
mnaombea ndoa yangu ivunjike, hebu nikuulize, kwa mfano ndoa yangu ikivunjika
utapata faida gani, maana wewe sasa una mke, utamuacha mkeo ili uje unioe mimi,
au ndio mnataka kunikomoa...?’ nikamuuliza.
‘Hahaha..hivi wewe unafikiri mimi nachukia ndoa yenu, kuwa
natamani ivunjike eti kwa vile ulinikataa, acha hiyo, mimi mumeo ni rafiki
yangu,...unalifahamu hilo fika, na kama asingelikuwa ni rafiki yangu
ningelipambana hadi nihakikishe nimekuoa, lakini niliona hakuna haja, kwanza umepata
muda wa kumsaidi rafiki yangu ambaye katokea kwenye shida,....sitaki hata
kumuongelea kuhusu maisha yake ya huko nyuma, na kwa kupitia kwako, nimeweza kulipa
fadhila zangu pia...’akatulia.
‘Najua hilo mtalirudia kila siku...na hamtafanikiwa, maana sasa
mnaishia kumuonea wivu, ana kampuni, ana maisha mazuri,..nini tena cha kumsuta
, hakuna, iliyobakia sasa ni majungu, nashukuru kwa ushauri wako wa mara kwa
mara sikatai, ila nisingelipenda unilaumu kwa uamuzi wangu huo...’nikasema.
‘Haya bwana, ngoja nikuulize hayo niliyotaka kukuuliza ili uone
kuwa mimi najali sana ndoa yenu,...’akasema
‘Uliza, na nitakujibu,....lakini kama ni mambo ndani ya familia
yangu,sitaki...’nikasema
‘Hebu niambie ukweli, mume wako alikuwa wapi, kwani watu walioona
hiyo ajali wanasema mume wako alikuwa akiendesha gari kwa mwendo wa kasi
sana...kama vile alikuwa akikimbizwa,au akikimbia jambo?’akaniuliza na mimi
hapo nikashituka, nikikumbuka kuwa hata mimi nilifanya hivyo hivyo.
‘Unataka kusema nini hapo, kuwa mume wangu…ni mhalifu au…?’
nikamuuliza.
‘Nataka kujua kama unafahamu wapi mume wako alikuwepo leo hii,
kabla ya hiyo ajali…kuna maswali mengi yanaulizwa, na yataulizwa na polisi pia,
…?’ nikamuuliza
‘Kwani hawo watu wanasema alikuwa akitokea wapi...!?’ nikamuuliza
huku nikiashiria kushangaa na sijui kwanini niliuliza swali hilo badala ya
kujibu swali.
‘Shemeji mimi nakuuliza swali na wewe unaniuliza swali, kwani siku
ya leo toka asubuhi, ...mliagana vipi, na mchana kutwa, hamkuwahi
kuwasilina, hamkuonana, au kuambizana mnakwenda wapi, mnafanya nini....nafahamu
unafahamu wapi alipokuwa akitokea au hufahamu?’ akaniuliza.
‘Sikiliza nikuambie, mimi na mume wangu tuna mishughuliko tofauti,
kila mmoja akiamuka asubuhi anakwenda kwenye shughuli zake kivyake vyake,
hakuna kufuatana..hayo ndio maisha yetu na sitaki uniulize kwanini maana hata
mimi sijakuulizia kuhusu maisha yako wewe na mkeo, au sio…’nikasema.
‘Sio hivyo, ninachotaka hapa ni kuwasaidia, na wala sio kubomoa,
na hata kama wewe ungeliona kwenye nyumba yangu kuna matatizo na kwa vile tunafahamiana,
ungeliniuliza, ili uone kama unaweza kunisaidia au sio...’akasema.
‘Sijaomba msaada kwako, mimi na mume wangu tuna utaratibu wetu wa
maisha na hatuna shida na hilo,, na haikuwa na umuhimu kuliulizia hilo, ni kama
simuamini mume wangu..’nikasema.
‘Lakini mwenyewe kwa kauli yako hapa, umesema siku ya leo imekuwa na
mitihani mingi,ukasema matatizo nyumba, matatizo kwa rafiki yako....hii
inaashiria nini, kama sio mna matatizo wewe na mume wako, kwanini hutaki kusema
ukweli nikaweza kusaidia, hata kiushauri tu...?’ akaniuliza.
‘Hatuna matatizo, na kama yapo ni ya kawaida tu , ya mume na
mke..hayakuhusu, na kama yangelikuwa makubwa, ningekuuliza, mbona mara nyingi
nakuuliza, au kuna jingine...’nikasema.
‘Sawa, bado hujanijibu swali langu, ....’akasema.
‘Swali lipi zilipendwa....?’ nikamuuliza na kucheka, yeye
hakucheka, akasema;
‘Hebu niambie utaratibu wenu wa leo ulikuwaje, ..?’ akaniuliza na
mimi nikamwangalia kwa makini, nikaona nisibishane naye sana nikamwambia;
‘Sisi utaratibu wetu ni kuwa, kwa vile kila mmoja ana kampuni
yake, na ana mambo yake, tukiamuka kila mmoja ana hamsini zake, hatuaingiliani
kabisa, wakati mwingine kama ni lazima ndio tunapeana taarifa, ...’nikasema.
‘Hiyo ni kwa ujumla je kwa leo ilikuwaje, ...?’ akaniuliza, na
sikumuelewa ana maana gani, kwani maswali yake niliyaona kama ya polisi
nikasema.
‘Ama kwa leo, nakumbuka aliniambia kuwa akitoka kazini anaweza
kupitia kumona mke wa rafiki yake ambaye kajifungua, ...nakumbuka aliniambia
kitu kama hicho, na sikuwa makini sana kumsikiliza maana nilikuwa na mambo
mengine ya kikazi yalikuwa yamenitinga...’nikasema.
‘Mke gani wa rafiki yake, aliyejifungua…?..., alikwenda kumuona
mzazi, au mume wa huyo mzazi, maana mimi nijuavyo mara nyingi mke akijifungua
wanaokuwa karibu na huyo mzazi ni wanawake, kwahiyo ilitakiwa wewe uende
naye....au nimekosea?’ akauliza
‘Kwahiyo unataka kusema nini hapo..?’ nikamuuliza
‘Sitaki kusema kitu, ninachotaka ni ukweli ili niweze
kusaidia,...kama ningelikuwa nataka kusema kitu, kwanini nikuzunguke, wakati
wewe ni rafiki yangu, na mume ni rafiki yangu pia....’akasema.
‘Nakuuliza hivi kwa maelezo yako una maanisha nini kuhusu rafiki
yako?’ nikamuuliza
‘Inawezekana hakuwa katokea kazini,....maana mimi nilimpitia
na nikaambiwa kuwa ametoka mapema tu, kikao chao kilivunjika mapema, kuna mambo
yalikuwa hayajakamilika, kwahiyo alitoka mapema ofisini kwake,...’akasema
docta.
‘Mimi siwezi kujua mipangilio yake, na siwezi kutabiri kuwa
alikuwa wapi, ...kama hakuwepo kazini, basi alikuwa kwenye shughuli nyingine
nje ya kazini kwake, hilo linawezekana na hilo la kusema mzazi ni lazima
muandamane na mke wako, halina mantiki yoyote kwangu…, wewe unachotaka hapa ni
kujenga sababu ya kumuona mume wangu ana tabia mbaya....’nikamwambia.
`Shemeji lakini nakumbuka tulishaliongelea hili kabla, nilishawahi
kuwakanya haya maisha yenu mnayokwenda nayo, ...sio mazuri kwa mke na mume,
kiukweli kwa wanafamilia hilo sio jambo jema, hata kama mnaona kuwa huo ni
usasa, au wengine wanasema ni uzungu...mimi siupendi. Mimi nawajali sana,
kuliko unavyofikiria wewe....’akasema.
‘Nashukuru kama unatujali, na ningelishukuru kama unalosema linatoka
moyoni na lina ukweli, kwani hata wazazi wangu wanasema hivyo hivyo, wakati
walishatamka kuwa,....nikiendelea na mume wangu watahakikisha maisha ya mume
wangu yanakuwa ni mashaka, na huenda akaishia jela...nikakumbuka kauli ya
wazazi wangu wakisema;
‘Wazazi ni wajibu wao kumlinda mtoto wao, hata wewe ukifikia
mahali pako, utasema hivyo hivyo kwa binti zako, hutapenda aende kuishi na mtu
ambaye humuamini..’akasema.
‘Haya unatushauri nini Docta...’nikasema kwa dharau.
‘Mimi nasema hivi maisha hayo mnayoishi yana madhara yake hasa
katika maisha yetu haya ya kiafrika,...miundo mbinu ni mibaya, hali za
barabarani tunazijua wenyewe, usalama hauna uhakika, kwahiyo ni vyema kuwa na
mawasiliano ya mara kwa mara na kila mmoja kumjua mwenzake yupo wapi na
anafanya nini, kwani simu zina kazi gani?’ akaniuliza.
‘Unanichekesha kweli, ...yaani umefikia hatua ya kutudharau kiasi
hicho...’nikasema
‘Lakini mwenyewe umesema kuwa kila mmoja ana mambo yake, na leo
hukujua kabisa kuwa mume wako alikuwa na taratibu gani, za nje ya
kiofisi....sasa utajuaje mwenzako yupo wapi, kama likitokea tatizo....’akasema
huyo docta na mimi sikuwa nimemuelewa sana, nikamsikiliza tu aendelee kuongea.
‘Endelea doct-aah’ nikasema kwa dharau
‘Mimi siwapingi kwa utaratibu wenu huo wa maisha, lakini ni vyema
mkajenga tabia ya kuambizana wapi mmoja anakwenda, sio kila mtu akirudi
nyumbani yupo kwenye laptop yake
...kila mtu yupo bize, na kazi zake, mnasahau majukumu yenu ya
ndoa...’akasema kama mzazi anayemuelezea mtoto wake aliyekosana na mkewe.
‘Umekuwa kungwi siku hizi au mwanandoa mzoefu, ...nyie mnajipa
moyo kuwa ndoa yenu ipo safi eehe, haina matatizo au sio, unaiona ndoa
yangu ndiyo yenye matatizo au sio....?’ nikamuuliza.
‘Mimi siwezi kujigamba kuwa ndoa yangu haina matatizo, yapo na
kila ndoa ina matatizo yake, lakini yakizidi ni lazima tuambizane, ni mimi
nawaasa, kama wewe ungeliniasha mimi ukiona utaratibu fulani sio mnzuri kwenye
ndoa, hasa huo mnakwenda nao.’akasema na mimi nikahisi kukerwa na hayo maneno
yake, niliona kama ananiingilia maisha yangu ya ndoa, japokuwa sikutaka
kumkatiza, nikatulia tu.
‘Mimi kiukweli sifurahishwi na tabia hiyo, halafu rafiki yangu
huyu, siku hizi anaonekana kunywa sana pombe, bila mpangilio, naufahamu unywaji
wake, huu wa sasa ni ulevi, sio unywaji...’akasema na mimi hapo nikaa kimia tu.
‘Mimi nionavyo, ana tatizo, ana msongo wa mawazo, ...mimi kwasababu ya
safari zangu za hapa na pale, sijaweza kukaa naye tukaliongelea hili kwa kina,
ila kila muda nilipopata nafasi kidogo ya kuwa naye, nimemuona sio yule rafiki yule
ninayemfahamu..hana raha, anaonekana anakerwa na jambo fulani..nahisi kuna
tatizo ndani ya ndoa yenu..’akasema.
‘Wewe unahisi kuna tatizo kwenye ndoa yetu....kwani hiyo kuhisi
imeanza leo?’ nikawa kama namuuliza
‘Ndio maana nataka tusaidiane kwa hilo,...kama kuna tatizo lolote
niambie shemeji, hiyo dalili aliyo nayo rafiki yangu inatokana na msongo wa
mawazo, shemeji jaribuni kukaa na kuliongelea hili nahisi kuna tatizo..ongeeni
ambizaneni, ili muwewe kuishi kama wana ndoa, na sio wabia...’akaniambia huyo
dakitari nikacheka kwa dharau aliposema `wabia...’
‘Eti eti unasema nini, ndio umefikia huko kuwa tunaishi kama wabia...dharau
ya ajabu kabisa...’nikasema na kutulia
Nilitulia kwa muda bila kusema neno..hayo maneno ya mwisho
yalinichefua,, hasira zikanikaba, maana sikuona tatizo lipo wapi, na sikupenda
mtu aniingilie maisha yangu, hasa huyu, ambye alikuwa ni mpinzani mkubwa, kwa
vile alitaka anioe yeye.
Mara akaja docta kutokea
maabara, akapita na kuelekea kwa docta anayemuhudumia mume wangu, hakusema
kitu.
‘Rafiki zilipendwa mimi sijui kama kuna tatizo kubwa kihivyo, kama
yapo ni mambo ya kawaida ya mume na mke. …’nikasema
‘Una uhakika kweli na hilo unalolisema…?’ akaniuliza
‘Nikuambie kitu, yule ni rafiki yako, kama umeona kuna tatizo
nenda ukamuulize yeye mwenyewe, umesikia sana...’nikasema huku nikionyesha
kukerwa.
‘Shemeji ni sawa...sio kwamba nataka kuingilia maswala yenu ya
ndani, hapana, ...na nafahamu kila tukiliongelea hili wewe unayaunganisha maswala
haya na mambo yaliyopita, mimi nakuhakikishia kabisa sipo huko, nipo kwenye
kuijali ndoa yenu,...’akasema.
‘Sawa, nimekuelewa…’nikasema, na aliona sitaki kuliongelea hilo,
tukaa kimia kidogo baadae akasema;
‘Shemeji samahani nikuulize swali muhimu sana, nililokuwa nataka
kukuulizia...usinielewe vibaya, na wala usilipeleke kwenye urafiki wetu wa
zamani, ninachotaka kufanya hapa ni kujaribu kuangalia kama kuna tatizo maana
nyie mnaweza msilione, lakini mimi kama docta ninaweza kuliona hata kama hujanielezea
kwangu, nakuomba nikuulize maswali ya ndani ya ndoa yako, kama hutojali,
...’akasema.
‘Wewe uliza tu, sioni ajabu na maswali yako,..nitakujibu kama
ninavyojua, ..lakini mimi siwezi kumjibia rafiki yako, yeye huenda anaweza
akawa matatizo yake binafsi, lakini kama hajaniambai siwezi kuyajua,..kweli
mimi ni mke wake, lakini kama mmoja atakuwa sio mkweli kwa mwenzake, basi hilo
ni tatizo lake, na huwezi kukimbilia kumlaumu mke au mume, bila kujua undani
wa maisha yao....’nikasema.
‘Shemeji sasa mimi nataka nijue undani wa maisha yenu,..niamini
mimi, nina nia njema kwenu, kama mlivyoniamini siku ya ndoa yenu, kama rafiki
mkubwa wa mume wako, kama rafiki yako mpenzi wa zamani, nataka niingie ndani ya
ndoa yenu, nijaribu kuangalia undani wa ndoa yenu, kama kuna
tatizo....tusaidiane’akasema.
‘Haya ....Unakaribishwa....ingia maana nimeshachoka kukuambia kuwa
hakuna tatizo...sijui nikueleze vipi,..haya uliza hayo maswali ya ndani ya
ndoa...’nikasema
‘Shemeji, je katika mambo ya unyumba mnashirkiana kama kawaida?’
akaniuliza swali lililonifanya nishituke na kugeuka kumwangalia usoni…huku uso
umeonyesha kutahayari…
Na kabla sijamjibu, akaniuliza swali jingine,…
‘Na huko kwa rafiki yako kuna tatizo gani, je tatizo la huko kwa
rafiki yako haliwezi likawa linaingiliana na matatizo mlio nayo nyie wawili,…?’
akaniuliza na mimi hapo nikabakia kimia, nikiendelea kumuangalia kwa uso
uliotahayari….
‘Ukinijibu kwa uhakika…tunaweza kulitatua hili tatizo lenu, nina uhakika kuna tatizo, na...usipoangalia, utakuja kuniambia, je upo tayari kunijibu hayo maswali, tukasaidiana au..utaendelea kunificha,...?' akaniuliza
Nikainua uso na kumuangalia, ...na kabla sijamjibu, docta yule anayemuhudumia mume wangu akatokea....
NB: haya, mambo ndio hayo
WAZO LA LEO: Wakati mwingine unaweza ukawa na
matatizo, lakini usijue kuwa una matatizo, wakati mwingine ndoa zinaweza zikawa
na matatizo, lakini wanandoa wakajifanya hawana matatizo,…kila mtu akimtegea
mwenzake, na kuona mwenzake ndiye anayestahiki kusema, au kulalamika…tukumbuke
ndoa ni ya watu wawili, na wote wana dhima sawa ya kuona ndoa yao inasimama
imara, tusijenge tabia ya kutegeana, kwani kukiharibika jambo, athari zitakuwa
kwa wote, na familia yenu.
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment