Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Wednesday, October 25, 2017

MKUKI KWA NGURUWE-14


 Docta amekuwa mfariji wangu mkubwa, tokea enzi hizo, ananifanya nikumbuke mbali sana, maana mara kwa mara nikiwa sina furaha, basi naweza kumpigia simu,tukaongea akaniliwaza, na hata kunipa ushauri, na sijui kwa vile ni docta, lakini hata hivyo tumetoka naye mbali sana, na sehemu katika maisha yangu ndio maana sitaacha kumsimulia kwenye kisa cha maisha yangu….

Kutokana na huyu docta ndio nilijenga na kuiendeleza tabia yangu ya kuamini watu, sio kwa kila mtu lakini wale unaoona wanaaminika, wale marafiki zako wa karibu, waamini, maana na wao watakuamini, yeye ndiye aliyenifundisha jambo moja, kuwa nisipende kuwadhania watu vibaya, maana ukifanya hivyo unajijengea hisia mbaya moyoni mwako, na kujitwika mzigo ambao haujatua kichwani mwako.

Basi wakati nipo hapo hospitalini, docta huyu akawa karibu nami kunipa faraja ili nisahau maumivu ya kumuwaza mume wangu …na kiukweli nilikuwa kwenye hali ngumu sana…mawazo, na yote yaliyotokea siku nzima, yangeliweza kunifanya niathirike kisaikolojia, docta akanipa pambaja, nikahisi sasa nipo na watu wenye kutumania.

Huyu docta  ndiye aliyewahi kuwa mchumba wangu, sasa kwanini ilitokea nikamuacha na kuolewa na huyu mume wangu,..ni kisa fulani chenye mazingatio kwa wenye hekima…

Tuendee na kisa hiki

***********


Docta alikuwa pia ni rafiki ya mume wangu, wengi walitarajia angelikuwa nai adui yake mkubwa, baada ya kunyang’anywa tonge mdomoni, lakini haikuwa hivyo,…docta amekuwa seehmu ya kuijenga ndoa yangui kila inapolega lega..

Naweza kusema pia docta ndiye aliyeniingiza kwenye dunia ya mapenzi, alinitoa kwenye ujana na kuniingiza kwenye usichana, nikafahamu ni nini maana ya mapenzi, enzi hizo, nikiwa kwa baba na mama yangu…hutaamini, kinyumbe na walivyotaka wazazi, sikuweza kuolewa naye….

Huyu docta ni nilianza kujuana naye zaidi tukiwa chuoni, huku nyuma, miaka ya utoto, shuleni, … nilikuwa namuona tu, ..kwa vile walikuwa majirani zetu, na ni familia yao ni miongoni mwa familia zilizokuwa na uwezo wa mali, wasomi waliobobea, kwani hata mtoto wao huyu aliweza kusomeshwa nje, kabla hajarudi hapa nchini,

Pamoja na mengine mengi sitaweza kumsahau kabisa katika maisha yangu

Ilivyotokea tunaweza kusema ni mipango ya mungu, maana kipindi nipo na huyu docta , ndio amerudi kutoka ulaya, wakati huo hajawa docta kamili, ndio alikuwa anachipukia, na kwa vile familia zetu zilishibana, aliporudi tu, akawa anakuja kwetu, na akija anakaribishwa vizuri, mtoto wa watu, basi tunakutana naye na kuongea mambo mbali mbali,  akanizoea mpaka tukafikia hatua ya kukubalina kuwa wapenzi.

Basi ikawa ni jambo la furaha kwenye familia zetu, maana tupo kwenye daraja moja,…ni maisha yalivyo, kila mti na ndege wake. Familia zetu ikawa imeliidhinisha tamko la kuwa mimi ni mchumba wa docta, kwahiyo yeye aliweza kuja kwetu kunichukua, …unajua tena wao waliishi kizungu zaidi,..basi akija, ndio hivyo tena, ila hali ya wazazi kukuchunga kwake inapungua,  ananiombea ruhusa tunatoka kutembea sehemu mbali mbali,…kiukweli mimi sikupenda sana maisha hayo y akujichanganya kwenye majumba ya starehe nk..lakini utafanyaje

Na kitu ambacho kilinifanya nisipende maisha hayo, ni ile hali ya kutizamana, nani kavaa nini, na zaidi pombe, tangia utoto nilitokea kukichukia kinywaji kinachoitwa pombe ya aina yoyote…namshukuru mungu kwa hilo.

Na hata nikiandamana naye kama  mpenzi wangu, alifahamu kabisa mimi nipo mbali na ulevi, yeye kunywa kwake, ilikuwa kama kunywa soda, lakini hakuwa anakunywa kuelewa, alikuwa na kipimo chake, sijui kwa vile ni docta.

Ikafikia muda akaanza kunishawishi ili nami niwe nakunywa kama yeye, hapo ndio hisia zetu zilianza kusigishana, na hilo ndilo lilofanya tukaja kukosana kabisa nay eye, lakini haikutokea hivyo tu kwa vile, hapana mimi naweza kukiri kuwa ni mipango ya mungu ilipangwa iwe hivyo.

Kiukweli ilibidi afanye juhudi sana kunishawishi kwa kitu ambacho sikipendi, na sijui kwanini siku hiyo ilitokea nikakubali. Ilitokea siku hiyo, kulikuwa na shughuli za jirani, mmoja wa watu wenye uwezo, waliandaa tafrija kwenye hoteli moja kubwa tu, tukawa tumealikuwa…baada ya mambo mbalimbali, ikawa watu wanakula na kunywa, na hapo mpenzi wangu huyu akaanza kunishawishi, ninywe

Kwa vile niliona ni siku ya furaha, na sikutaka kumuuzi mpenzi wangu, siku hiyo nikasema ngoja nijaribu, nione ina ladha gani, ngoja nijaribu nione hiyo raha wanayoifaidi wenzangu,…ilikuwa ni aibu kwangu na ndio siku niliapa kuwa sitakunywa tena.

Nilikuwa nimekunywa kidogo, kumrizisha mpenzi wangu ambaye kipindi hicho alikuwa ni huyu docta, nilikunywa gilasi moja tu tena kwa kujilazimisha, ilikuwa haipiti kooni, nahisi ni harufu mbaya, nilipomaliza hiyo gilasi moja tena haikumalizika,..,…

Hapo hapo nikaanza kujisikia vibaya, tofauti na ninavyoona wenzangu wakichangamka, mimi nilihisi vibaya kupindukia, niliona kama dunia inageuzwa, inazungushwa, roho imechafuka, tumbo linapanda na kushuka, nataka kutapika lakini hakitoki kitu

Yaani siku hiyo nilijuta ni kwanini nilikunywa,..nilimuona mpenzi wangu kama alitaka kuniua, na muda huo huo, nikamwambia mimi naondoka, siwezi kukaa hapo tena, akanisihi, na kunishawishi, kiukweli anajua kubembeleza, na unajua tena ni mpenzi wangu ikabidi nikae tu…kumrizisha.., na hata aliponishawishi ninywe tena sikukubali, nilimuambia kabisa ukiendelea kunishawishi kunywa hii sumu tutakosana kabisa.

 Kwa muda ile nikajitahidi, lakini hali haikuwa nzuri, bado nilikuwa najisikia vibaya,..ikafika muda, siwezi kuvumilia tena, kwani roho ilishachafuka kupitiliza, nikakimbilia chooni, (washing-room), nikamuacha docta na watu wengine wakiendelea kuongea na kunywa, wanajisikia raha zao.., ambazo kwangu mimi ilikuwa ni kero tu.

Nilipokuwa kule hali ikatulia, kidogo cha ajabu sikutapika, kama nilivyodhania nitafanya hivyo,..nikaona labda, hali imetulia, ndio wakati nataka kutoka sasa,natoka chumba hicho cha usafi, nipo mlangoni, nikahisi kizungu zungu,na kama asingelikuwa huyo jamaa kunidaka ningelidondoka vibaya kwenye sakafu….

‘Pole sana dada, ....’akanidaka huyo jamaa na kunisaidia kusimama vyema, lakini sikuweza, mwili ulikuwa hauna nguvu, tumbo linapanda na kushuka, na sikuweza kuvumilia zaidi nikaanza kutapika, na matapishi ya mwanzo yakaenda moja kwa moja kwenye nguo za huyo jamaa.

‘Oooh...pole pole, inaonekana umelewa, wewe..oh, ..tulia kidogo,....’akasema bila kujali kuwa nimemchafua. Na kunisaidia ….

Na hutaamini hakujali kuchafuka kwake, yeye alichojali kwangu  ni kunisaidia mimi akanishika vyema, akichelea nisichafuke na yale matapishi niliyomlowesha nayo mimi, ambayo yalikuwa kwenye nguo zake,....na akaweza kunisaidia hadi chooni, ilibidi aingie choo cha wanawake ili niweze kujisafisha,..alipohakikisha nipo sawa, yeye akakimbilia choo cha wanaume kujisafisha, nilijiskia vibaya sana siku hiyo.


Hali ilipotulia nikatoka, kumbe huyu jamaa alikuwa hapo nje akinisubiria, alikuwa keshamaliza kujisafisha, na kukausha nguo zake usingeliweza kujua kuwa nilimchafua, na aliponiona nikitoka akanifuata pale mlangoni, na kuniuliza.

‘Upo sawa sasa,…?’ akaniuliza

‘Ndio nipo sawa, hamna shida, samahani sana, na nashukuru sana…’nikasema

‘Usijali, inatokea tu…na samahani nikuulize ,upo na nani maana naona hiyo hali unahitajia msaada...?’akaniuliza huku akinisogelea, na sikutaka kuongea na mtu, nilichotaka ni kuondoka, na kwenda nyumbani kulala.

‘Nipo na na...’nikasita kusema

‘Na mume wako, au mpenzi wako, off course....’akamalizia na mimi nikakubali kwa kutikisa kichwa, ili nitimize ule usemi wa kubali yaishe, ili aondoke zake, na mimi niende kumuaga docta kuwa narejea nyumbani.

Kiukweli kwa muda ule nilidhamiria kuondoka, sikujali tena kuendelea kukaa kumrizisha mpenzi wangu, wakati hajui kinachonisumbua, yeye aliona ni kwa vile ni mara ya kwanza, basi nitazoea,…hapana sikuzoea na sitaweza kuzoea maishani mwangu.

Nikawa natembea kulekea kule walipo docta na marafiki zake, lakini nlikuwa nayumba, kizunguzungu, yaonekana kichwani bado nilikuwa sipo vyema,na kumbe jamaa yupo nyuma akiwa na mashaka kuwa naweza kudondoka tena,…na alipoona sipo sawa akanijia kwa nyuma na kusema;

‘Basi ni bora nikusaidia hadi kwa huyo mume wako,maana unavyoonekana hujawa sawa, kwanini unakunywa pombe, wakati unaona hazikupendi,.....achana na pombe,pombe zinawenyewe bwana, mimi mwenyewe sinywagi kihivyo, ni kwa dharura tu....’akasema.

‘Sinywi tena...hapana nitaweza mwenyewe…..’nikasema na nikamtupia jicho huyo mtu, na ilikuwa kama ndio namuona kwa mara ya kwanza, nikahisi hali fulani, kama mshituko , ni kama kuna kitu nilikihisi, lakini niliona ni sababu ya pombe, maana mtu mwenyewe simfahamu, lakini nikajiuliza ni kwanini nihisi kitu kama hicho, nikapotezea, na sikutaka kumwangalia tena machoni.

‘Samahani nikuulize,… inakuwaje mume wako asijitokeze, kwani naona kama umekaa huku muda mrefu hajashtuka tu…kama ulikuwa na hali hiyo alitakiwa akujalia, au sio,,? Samahani lakini kama nawaingilia maisha yenu, au....?’akasema kama kuniuliza, hata mimi nililiona hilo , lakini sikujali, na sikutaka huyo docta afahamu kilichotokea.

‘Wenyewe wameshalewa, sizani kama hata wanatambua kuwa nimechelewa huku....na nisingelipenda wanione kuwa nimetapika kwa ajili ya pombe, wala usije ukawaambia hata hivyo nipo safi, haina haja ya wewe kunisaidia nashukuru kwa wema wako huo..na sitakunywa tena hiyo mipombe yao, ....’nikasema.

‘Pole sana....mimi kama ningelikuwa na mpenzi  kama wewe, ningeshtuka haraka sana, ulivyochelewa hivyo…sio kwamba namsema vibaya huyo mpenzi wako, lakini kwa hali hiyo alitakiwa awe karibu yako,…mimi hapa naogopa usije kudondoka tena.. sawa, basi tembea mimi nitakufuatilia kwa mbali kuhakikisha umefika salama kwa mume wako, ...’akasema, na kunifanya nifurahie sana wema wake.

‘Hongera ...kama upo hivyo, na mpenzi wako atakuwa na bahati sana…hata hivyo, ni leo tu, mbina mpenzi wangu ananijali sana, sina shaka naye….’nikasema na nikatamani kumwangalia tena huyo jamaa usoni, na nilipomuangalia, akili yangu ikakumbuka kama niliwahi kuiona hiyo sura mahali, lakini sikuweza kukumbuka vyema ni wapi, na lini, sikutaka kuwaza zaidi , nikapotezea.

‘Ina maana hunikumbuki mimi kabisa...?’ akaniuliza na kunifanya nisimame wakati huo nilishaanza kuondoka kuelekea kule walipokuwa docta.

‘Kwani wewe ni nani…?’ nikamuuliza , na hapo ndio nikapa ujasiri wa kumchunguza vyema usoni baada ya kugeuka kumuangalia vyema…hata hivyo sikuweza kumkumbuka kuwa ni nani, akili ilikuwa haitaki kufikiria sana, na sikutaka kufanya hivyo nikasema;

‘Samahani kwakweli sikukumbuki kabisa,..zaidi ya kukufahamu hapa kuwa wewe ni mtu mwema, ...tuliwahi kukutana wapi mimi na wewe, shuleni, au chuoni, au wapi?’ nikamuuliza ili tu kumuonyesha kuwa namjali kwa fadhila zake hizo, lakini sikuwa nataka kuongea...

‘Kweli ukiwa mtu wa chini, ..watu hawakukumbuki kabisa, wewe sio wa kwanza kusema kuwa hunikumbuki, lakini nafahamu ni kwanini...’akasema hivyo.

‘Hapana sio kwa vile wewe ni mtu wa chini, kwanini unasema hivyo, wewe ni mtu wa kawaida mbona, mimi sipendi watu kujishusha, hakuna mtu wa juu na chini, hizo ni hisia potofu, na kiukweli sipendi watu kujifanya hivyo…’nikasema, na nikamwangalia tena kwa makini,japokuwa akili iliona kuwa nilishawahi kukutana na mtu kama huyo, na sio kukutana tu, lakini moyoni nilikuwa kama nimeguswa na hamasa, lakini sikuweza kukumbuka kabisa kuwa huyu mtu ni nani.

Muda ulikuwa umekwenda, sikumuona docta akija ..na sikupenda kumuacha huyu msamaria mwema hivi hivi, nilitaka niondoke akiwa amerizika, sio niondoke aone nimemdharau..hisia za wema wake ziliuteka ubongo wangu, ule ukaribu wake , kunijali, nilimuona kama mtu niliyemzoea….sijui kwanini, yaani kumbe kitu kidogo tu kinaweza kubadili hisia za mtu.

‘Samahani sana, labda kwa vile nipo katika hii hali, ndio maana akili haifanyi kazi vyema, na nisingelipenda kufikiria zaidi, maana kichwa kinaniuma, labda unikumbushe tu, kama hutojali...’nikasema na huku nikikwepa kumwangalia tena moja kwa moja usoni na yeye akaniangalia na kusema;

‘Mimi ni mtoto wa mzee Mchapakazi…’akasema

‘Mchapakazi…?’ nikauliza, sikuweza kukumbuka ni nani anamuongelea kwa wakati huo..

‘Humkumbuki yule mzee, aliyekuwa  mlinzi wa pale nyumbani kweny, na pia alikuwa akiwalimia mashamba yenu na mimi nilikuwa nafika kumletea baba chakula, na siku moja ukanisadia pesa za ada ya shule, kipindi mzee anaomba mkopo kwa baba yako, na baba yako akakataa kumpa hizo pesa..umeshanisahau ehe...’akasema

‘Mungu wangu ndio wewe..mbo-mbona..hapana sio wewe…’nikasema huku  nikainua kichwa kumwangalia na mdomo wangu ukabakia wazi kuonyesha mshangao.

‘Ndio mimi …huamini eeh…mlifikiri tumejifia au sio…’akasema

‘Oh, …sio…ila kiukwe umebadilika sana..ooh, nimeshakukumbuka, ..oh jamani , mimi nilikuwa kasichana kadogo kipindi kile,…unajua baada y alile tukio, nilitokea kuwachukia sana wanaume, na nailijiskia vibaya sana kwa yale yaliyotokea, hata hivyo nilitamani nikuone tena, lakini hukuja, nilishaahidi kukusaidia ..kukulipa fadhila ulizonitendea...’nikasema.

‘Kunilipia fadhila , si zilishalipwa na baba yako, au umesahau yaliyotokea..’akasema

‘Usiseme hivyo, wazazi wangu na wao walipokea taarifa tu,..nakubali hawakutaka kuzichunguza,..’akasema

‘Unaweza kuwatetea hivyo, sawa, ni wazazi wako ni lazima useme hivyo…ila kiukweli iliniuma sana kumuona baba yangu anazalilishwa, na sikutaka kurejea tena kwenu, na nikawa nafanya vibarua  tu pale waliponiachia jela, na sijui ilitokeaje kesi ikafutwa na kuachiliwa, nilihangaika sana...hadi nikapata pesa za kujisomesha, unakumbuka nilifaulu, na kwasababu ya kufungwa sikuweza kwenda sekondari,…’akasema

‘Pole jamani…nilisikia, lakini aah, mimi sikuweza kufuatilia, maana sikuwepo tena yaliyotokea nyuma nilifanya kuhadithiwa, nilijua yameisha, kumbe..ndio hivyo tusamehe tu, na wazazi wangu…’nikasema

‘Nilipata msamaha, sikufungwa muda mrefu,.. na nilipotoka nilimuomba baba tuhame hapo kijiji kabisa, tukaenda kuishi kijiji cha mbali, huko nikaweza kujisomesha kwa kufanya vibarua...Baba yangu aliumwa sana, naweza kusema ni  kutokana na hilo tukio, na kuumwa huko ndio ikawa sababu ya kufariki kwake...’akasema kwa uchungu.

 ‘Oh, pole sana, ina maana yule mzee alishafariki...?’nilimuuliza nikishikwa na huruma, na fadhaa, na nilitamani nimkaribie ni mkumbatie kumuonyesha jinsi gani nilivyojisikia….kiukweli niliona nina deni kubwa la kumlipa huyu mtu, maana hii ni mara nyingine ananiokoa na kunifanyia huruma…moyoni niliahidi kuja kumlipa kwa kadri nitakavyoweza.

‘Alifariki......ndio mapenzi ya mungu, na mapenzi ya mungu ndivyo yalivyo, na moyoni hatukosi kuwa na sababu..ila kiukweli, baba alinipenda sana, na hali yake hiyo ya kuumwa, na ilianzia pale mama alipofariki , mama yeye alifariki mapema tu, tulipohamia huko,…na,… na hutaamini, baba alikuwa haishi kumkumbuka mama, na hicho ndicho kilichomfanya hali yake izidi kuwa mbayae....na hakupenda mimi niteseke, aliona ni bora yeye akafungwe, aliwaomba sana wahusika afungwe badili yangu...’akasema.

‘Oh, jamani, poleni sana, sizani kama wazazi wangu walifahamu hilo, na ukweli wote wa hayo yaliyotokea…na kwa vile alikuwa mfanyakazi wao kwa muda mrefu wasingelifikia kumfanyia ubaya huo wote…na hata kufariki huko, sizani kama walikuwa na taarifa,..wangeliniambia, na hata wao kufika kwenye msiba, sizani kama wangeshindwa kufanya hivyo, sizani...’nikasema.

‘Baba alikataa kabisa, mama alipofariki, hakutaka kutoa taarifa kwa watu wa mbali, na hata yeye alisema ikitokea akifariki..sisi tufanye hivyo hivyo..maana alishaona dunia haina wema..aliniusia kabisa,.., nisije kuja kuwaambia...na ndivyo ilivyotokea, alizikwa na watu wachache tu…, na wengi hawakufahamu zaidi ya ndugu na jamaa wa karibu tu .....ndio hivyo, lakini mimi sikukata tamaa ya maisha, nikasonge mbele, ....’akasema.

‘Sasa hivi unafanya kazi wapi?’ nikamuuliza.

‘Nipo hapa kwenye hii hoteli nabangaizabangaiza, nilipata tenda ndogo hapa, ndio naifukuzia, ikiisha nakwenda sehemu nyingine, maisha yanakwenda kidogo ninachokipata kinanisaidia, sitaki ile ya kuajiriwa maoja kwa moja, mpaka nikamilishe malengo yangu…’akasema

‘Mungu wangu, imeniuma sana…sikutarajia hili , kweli milima haikutani, ila wanadamu..mmh…sijui nitakulipa nini, sijui nifanye nini ili hayo machungu yaliyokupata yaishe,..sijui, tusamehe tu, mimi na wazazi wangu..’nikasema

‘Ndio maisha sisi watu wa chini kupata  kazi inakuwa shida, na sipendi kwenda kuwapigia watu magoti kuwa wanipe kazi, sitaki nizalilike kama alivyozalilika baba yangu, mimi nimeona njia iliyorahisi ni kujiajiri kwa njia hii...hapa leo, keshi kwingine maisha yanakwenda,…..’akasema na hapo nikamwangalia na kumbukumbu za nyuma zikanirejea...

‘Maua unafanya nini huku….?’ Ilikuwa sauti ya docta, na nikageuka haraka na kuanza kutembea kumfuata, nilipomfikia, akaniuliza

‘Ulikuwa na nani muda wote huo…?’ akaniuliza

‘Nilikuwa najisikia vibaya, …sana…’nikasema

‘Utazoea tu,…pombe kidogo tu ndio imekufanya hivyo, ajabu kabisa… tatizo lako hutaki kujifunza, starehe hiyo unaikosa bure, dunia hii kuna starehe gani kama oh, upo ok, lakini samahani, sikuja kukuangalia, kuliko na maongezi nyeti kidogo, nisamahe mpenzi…’akasema akinishika kiunoni kunifanya nisipepesuke.

‘Nipo sawa, haina haja kunishika hivyo, mimi sipendi…’nikasema

‘Ok, ok…samahani nimesahau…haya twende, na yule aliyekuwa karibu yako ni nani..?’ akaniuliza

‘Ni mfanyakazi wa hii hoteli, kanisaidia, sana, maana nilizidiwa kidogo…’nikasema

‘Mhh, ok, sijamshukuru, naona simuoni tena....haya, twende tukaendelee ..wenzangu ndio kumekucha..’akasema, na docta alikuwa hivyo hana hisia mbaya na watu, ndio nilimpendea hivyo, ukimuambia kitu atakuamini, na inaishia hapo.

‘Hapana mimi naondoka…siwezi kurudi tena kule, nahisi harufu za pombe zitaniua,wewe nenda kaendelee tu na wenzako…’nikasema

‘Oooh,..hapana usifanye hivyo,…utaharibu, nitawaambiaje rafiki zangu, kuna mambo muhimu tunaongea pale unajua kazi zangu ni watu, na watu ndio wananiongezea michongo ya maisha..unajua, ...na wale pale ni watu muhimu sana, ni madocta, wamenitangulia, nikiwa nao, najua nitafika sehemu ninayoitaka sana, elimu yangu nataka inifikishe mbali kabisa..’akasema

‘Basi ..ndio maana nasema, wewe nenda kaendelee nao, wala sijali kuhusu mimi,   mimi nitarudi nyumbani peke yangu, maana hapa na nyumbani sio mbali, nitafika bila wasiwasi..’nikasema

‘Siwezi kukuacha uende peke yako, na hii ni shughuli muhimu ya majirani zetu haitaonekana vyema tukiondoka, hata wazazi wako hawatafurahi, wakisikia hivyo, hebu lifikirie vyema hili, nikuombe kitu.., vuta vuta muda, tutaondoka pamoja ..’akasema, niliwaza sana baadae nikasema sawa, basi nikarudi pale mezani, lakini baadae nikamuomba mpenzi wangu kuwa nataka nikakae kwenye hewa, nipate upepo,..sijisikii vizuri.

‘Wapi sasa, unaona mambo tunayoyaongea hapa ni muhimu sana, yanaweza kukusaidia hata wewe , kwenye maswala ya ajira, kujiajiri, kuwekeza, unaona, ni mambo muhimu kwenye maisha, leo wazazi, kesho ni sisi, tunahitajika kuchukua hatamu, au sio..umesikia mwenyewe, mimi  hatima ya haya ni kuwa ni hospitali yangu kubwa, ndio ndoto yangu…’akasema

‘Usijali, mimi nitakuwa kule sehemu ya kutokea, ..palee , unaona, wamekaa akina mama , na wasichana wasiopenda kujichanga huku,…utakuwa unaniona au sio…’nikasema akakubali, kwa shingo upande, ..kiukweli kwa muda huo, sikutaka kukaa pale na akili yangu ilishaondoka, yaani kuna kitu kilinibadili ghafla, na ..hata sijui ni kwanini.

Nikaenda ile sehemu na kukaa , kulikuwa na watu wengine wasiokunywa wamekaa hapo wanakunywa vinywaji vya kawaida, nikatafuta sehemu nikaa, na nikanyosha mkono kumuashiria docta, kuwa nipo sehemu hiyo, na akanipungia mkono kuwa kaniona..

Sasa ni wakati nimetulia, mara akaja mtu pembeni na kukaa, …sikutaka kugeuka kwa haraka, kumuangalia ni nani, nilikuwa akili yangu imetekwa na tukio kwenye Tv, kuna tamithiliya nzuri inaonyeshwa, na mara sauti ikasema;

‘Kumbe yule ndio mume wako, najua hata yeye keshanisahau, …yupo na akina kaka zetu wa enzi hizo,…mnaoana watu wenye hadhi zenu…’nikashtuka, kumbe alikuwa yule msamaria mwema, nikahisi moyo ukinienda mbio, maana sasa kakaa karibu yangu, nikageuka kuangalia kule alipokaa docta, nikawaona wanaongea na kucheka tu. Hana habari kabisa na mimi…

‘Mhh…sio mume wangu…’nikasema

‘Kwahiyo, kumbe hujaolewa bado…’akauliza

‘Bado ndio tupo mbioni…’nikasema

‘Oh, mungu wangu kwanini hivi lakini…’akasema

‘Kwanini unasema hivyo…?’ nikamuuliza

‘Unakumbuka ahadi yetu lakini…?’ akaniuliza

‘Ahadi, mmmh…na..ndio na…nakumbuka,  lakini…hayo yalishapita au sio ni mud asana, na mambo yamebadilika,…na nishamuahidi docta kuwa ndiye mume wangu mtarajiwa, samahani sana..’nikasema

‘Najua,hamna shida , nilitaka ukumbuke tu hilo, najua huwezi kuolewa na mtu kama mimi,….ila nakuuliza tu…je moyo wako bado upo kwangu, au uliniambia tu  kunifurahisha, utoto..lakini hatukuwa watoto kivile, au sio…samahani sana kukuuliza haya, najua umeshampata mtu wa hadhi yako…sizani kama nina maana tena kwako…’akasema

‘Usiseme hivyo, wewe hujui tu….niliteseka sana,…sijui kwanini, na hadi naamua kumkubalia docta, ilikuwa ni baada ya kusikia kuwa wewe haupo hai, walisema ulifia jela au baada ya kutoka kitu kama hicho….’akasema

‘Eti nini…nilikufa…hahaha.., hayo labda waliyatunga wazazi wako,..ili….lakini haina haja, najua, hutaweza kuolewa na mtu kama mimi, nafahamu hivyo,… lakini niliapa kuwa bila wewe sitaweza kuoa tena, ndio maana nikawa napambana ili niwze kufiki hadhi yenu, na nilitaka siku tukikutana unione tofauti, lakini ya mungu mengi tuakutana leo bila kutarajia…’akasema

‘Jamani…..’nikasema hivyo nikigeuka kumuangalia kwa macho yaliyojaa huruma

Na wakati namuangalia, ndio kumbukumbu za nyuma zikaanza kunirejea, na ikawa ndio sababu ya kunibadili kabisa mawazo yangu, hasa kutokana na yaliyotokea siku za nyuma kweli kumbukumbu hubadili maisha…na kutokana na kumbukumbu hizo zikanifanya nimuache docta…haikuwa kazi rahisi, lakini…

NB: Tutaendelea sehemu ijayo. Ilikuwaje, na ina umuhimu gani kwenye hiki kisa, tuzidi kuwepo…


WAZO LA LEO: Tofauti za maisha, tofauti za kipato, tofauti na utawala na wasio kuwa watawala, isiwe ndio sababau ya kuzarauliana, maana huwezi kujua, ni yupi ni muhimu kwenye maisha yetu. Unaweza ukawa na kipato lakini ukawa na mapugufu fulani ambayo yanaweza kujaziliwa na yule unayemuona ni hadhi ya chini, au akaja kukusaidia yule ambaye hukutarajia kabisa. Mola ni mwingie wa hekima anajua ni kwanini maisha yapo hivyo,..

Ni mimi: emu-three

No comments :