Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Thursday, July 26, 2018

YOTE NI KWA MAPENZI YA MUNGU-25


Shemeji alibakia kimia, na Dalali, akasema;

‘Shemeji mimi nimekuwa nikiishi nawewe...unanifahamu sana tabia yangu ilivyo, hata kaka aliniamini sana, mimi siwezi kuwa kinyume na hii familia, siwezi kufanya kitu kimachoweza kuiumiza hii familia, na wasiwasi wa huyu mtu tu..’akasema

‘Kwahiyo sasa unataka mimi niseme nini…maana ulishanionya nisiongee baadhi ya mambo…naogopa nisije kuongea hapa yakaja kutokea mengine..?’ akauliza na kusema mama mjane kwa sauti iliyojaa huzuni.

‘Nataka niwe na uhakika shemeji, nijue nipo peke yangu au na familia yangu...'akasema na kuonyesha uso wa hasira hivi.

'Kwani...'akataka kuongea shemeji yake lakini akamkatiza kwa kusema

'Ninachotaka kufahamu ni...., je wewe, ulimtafuta huyu wakili, maana …mwanzoni alijifanya yeye ni ndugu yako, kumbe mlikuwa mnanichezea shere, eeeh, shemeji, ndio tumefikia hapo…sasa naona sio ndugu tena , bali ni …niambie ukweli shemeji..’akasema akimuangalia mama mjane.

Mama mjane  akawa kainamisha kichwa chini tu, na alipoona  shemeji yake yupo kimia anasubiria jibu, akainua uso kidogo na kusema;

‘Kwa hali ilipofikia, sikuwa na jinsi, yoyote mwenye kutaka kunisaidia, nisingelikataa, …na wewe mwenyewe unaona hali ilivyo... wote waliofika kabla hakuna aliyetusaidia kwa jinsi hii,..huyu angalau naona kuna matumaini, …lakini..’kabla hajamaliza Dalali akasema.

‘Kuna matumaini gani shemeji, huko kuongea tu, kama kuongea, hata mahakamani tuliongea sana, lakini mwisho wa siku tuliulizwa nini..ushahidi....hatukuwa nao...shemeji tunapoteza muda bure...'akasema Dalali.

'Mimi naona tumpe nafasi tu, atusaidie, yeye anaweza kuwa msaada mkubwa kwetu....'akasema mama mjane.

'Kwahiyo mimi sikukusaidia kitu..hayo niliyoyafanya hayana maana..., na kwa hatua hii ina maana gani,...shemeji kwa tafsiri ya haraka ni kuwa huniamini tena..au sio shemeji?’ akauliza.

‘Sio swala la kutokukuamini hapa shemeji,..hivi wewe huoni kuwa kwa hali ilipofikia tunahitajia msaada, na sijui kwanini unaukataa msaada shemeji…?’ akauliza

'Msaada !! Shemeji unaamini hilo, kuwa huyu mtu anafanya hili jambo kama msaada tu, hatahitajia malipo..?' akauliza akinigeukia mimi.

'Hajasema anahitajia malipo...'akasema mama mjane.

‘Hakukuwa na haja ya msaada shemeji,... mimi mwenyewe nilishafikia hatua ya kulimaliza hili jambo kwa manufaa yetu sote na marehemu, ina maana wewe humjali tena marejemu…’akasema Dalali.

'Simjali kwa vipi...?' akauliza mama mjane.

'Wewe huoni hilo...na kwa jinsi hiyo hili tatizo halitaisha kamwe...mimi nilishafikia nafasi nzuri tu ya kulimaliza kabisa, deni lilipwe, tuwe huru, na bro huko alipo awe huru...'akasema

‘Kulimaliza kwa kuachia nyumba ipigwe mnada, nyumba ambayo kaka yako aliapa hataiuza, na alitamani idumu hadi vitukuu, kulimaliza kwa kukubali kuwa kaka yako alikopa,..hivi kweli hapo ulipo unaamini hilo, kuwa hilo deni ni la kaka yako,?…hapana sio mimi, niliogopa tu....?’ akauliza Mjane.

‘Ina maana ulivyokubali kule mahakamani ilikuwa ni geresha…na hata ushahidi wote ule waliouleta benki hujauamini, si uliambiwa uukague, ukathibitisha kuwa ni ...…shemeji…?’ akauliza na hakumalizia hapo.

‘Lakini mimi nilikuambia…kuwa mimi sitakubaliana na lolote lile, maana mimi ninamfahamu sana mume wangu..na hadi kuja kukubaliana na hayo ni baada ya kuona familia yangu inateseka, ningelifanya nini sasa…’akasema mama mjane.

'Lakini ukweli si ulionekana, na mizimu ikathibitisha, kuteseka kwa familia tuliambiwa ni kwasababu gani...si hata ndugu yako alikuambia, alivyoambiwa huko, ..shemeji, mimi nilijua tumeshaafikiana...'akasema

'Sasa...kwanini tusimuachie huyu mtu akajaribu....tumuache tu shemeji..kuna ubaya gani...'akasema mama Dalali

‘Haya sawa, lakini nikuulize tu shemeji yangu,..hilo deni si lipo..?' akauliza

'Ndio lipo..lakini siamini kuwa ni la mume wangu...'akasema mama mjane.

'Kimaandishi na kwa ushahid i inaonyesha hivyo,...swali la kujiuliza hapo ambalo ndilo la muhimu, hilo deni litalipwaje..hilo ndilo la muhimu,..sasa nikuuliza shemeji yangu, maana tunatwanga maji kwenye kinu,...niambie wewe, tutalipaje hilo deni..?' akauliza

Hapo mama mjane akabakia kimia

'Shemeji, nijuavyo mimi, kesi ikifika mahakamani,…tutashindwa tu,..Sasa Shemeji yangu pesa ya kulipia hilo deni na gharama ya hiyo kesi itapatikana wapi, umelifikiria hilo…?’ akauliza, na shemeji akabakia kimia

'Mbona hapo unabakia kimia...mambo mengine msikurupuke tu,...hilo ni swala langu, na nilishajua nifanye nini...tatizo, shemeji...umesahau kuwa mimi ni nani kwako, hata wanafamilia wameniamini, wewe unafiki hadi kunidharau, sawa wewe ni mkubwa kwangu kwa vile umeolewa na kaka,lakini...ilibidi uniombe ushauri kwanza...sio vizuri shemeji..'akasema

'Sasa niambie...maana hapo ulipo huna mbele wala nyumba, kula , maisha yenu yote yananitegemea mimi,...au nasema uwongo,..haya tumeenda huko mahakamani kesi tumeshindwa tena, unahisi ni nani atabeba huo mzigo...mbona unataka kuniua, maana nimechoka shemeji...'akasema

‘Yote mimi namuachia mungu, …maana yote ni kwa mapenzi yake…’aliposema hivyo  mama mjane akaanza kulia.

‘Shemeji, nimekuuliza tu, ndio inakuliza, …'akasema

'Maneno yako yanaitesa, yananisimanga...'akasem

'Hapana huo ndio ukweli,..inavyoonekana wewe humjali tena marehemu , kwa vile keshafariki,hushukuru kuwa katuma mjumbe kutufunulia huo ukweli...sasa wewe bado huamini..au kwa vile hayupo tena duniani tumuache tu ateseka, asiyekuwepo na lake halipo au sio...'akasema.

Mama mjane akabakia kimia 

'Shemeji nioneeni na mimi huruma..., maana sasa nashindwa,..., tuache hata hawa watoto wateseke tu, na hatujui hatima yake itakuwaje hao mizimu wakicharuka tena, itakuwaje, mimi sijui….’akasema.

‘Una uhakika gani kuwa hilo deni lilikuwa la mume wangu,.....mimi ninachopigania ni hicho...akasema mama mjane.

‘Shemeji mbona tunarudia kule kule…uliuliza hayo…. hadi tukafika mahakamani, wakathibitisha kisheria, wewe si umesoma, eeh, unafahamu sheria, eeh…sasa wewe ulitaka mimi nifanye nini, eeh..vielelezo vyote vipo..'akasema

'Lakini bado kuna mashaka kwangu...'akasema mama mjane.

'Haya sawa una mshaka na huo ushahidi au sio...na usione hivyo, kuwa kwanini mimi nakubali tu yaishe,… mimi nakubali kweli, kuwa kaka hakuwa na tabia hiyo, lakini tutaithibitishaje hilo mbele ya mahakama, na uzuri, eeh, mambo ya asili yametusaidia, tumeonyeshwa kwa kupitia mizimu, wewe huiamini hiyo…?’ akauliza

‘Ina maana hadi hapo tumeshashindwa, au sio shemeji….sasa kama tumeshindwa na katokea mtu wa kutaka kutusaidia,  kwanini tusitoe ushirikiano kwake eeh,…mimi sioni kama hapo kuna tatizo, au wewe ulikuwa na maamuzi gani..?’ akauliza mjane.

‘Maamuzi gani…! ungeliniuliza hilo kabla hujatafuta mtu..unajua madhara yake, huyu atataka malipo yake, na tukishindwa kesi tutahitajika kulipia gharama zake,za usumbufu,....bado hutajasahau, hayo yanayotokea kwa mtoto,…una maana huumii mtoto akiteseka,  na je itakuwaje huko baadae,..hawa wakiondoka,..na  tatizo jingine hata huyo mtaalamu hapatikani tena…’akasema

‘Labda kaona haina maana tena, kuwatesa watu wasio na hatia..’akasema mjane

‘Nini!!….shemeji, unasema nini,?  una maana gani,?.... ina maana umeshamuamini huyo mtu..huyo sijui ni wakili, shemeji, uwe na huruma na watoto..usipende mali kupitiliza, hii tabia sio nzuri, hata bro alikuwa akikukanya sana kuhusu hilo, na kwa vile umeona mimi sina mali unanidharau au.....’akasema

Mama mjane sasa akainua uso na kumuangalia Dalali moja kwa moja usoni, na niliona keshabadilika,…

‘Shemeji,..mimi napenda mali,khaa! ..kweli unasema hivyo, nimeishi na nyie nikajinyima ili mfanikiwe,…leo hii unasema hivyo, hivi kama ningelipenda mali nyie mngefikia hapo mlipo…sijapenda hiyo kauli yako shemeji, kabisa kabisa…’akasema mama mjane.

‘Nimesema hilo, kwasababu kwa hali ilivyo, hatujali utu wa marehemu, hatujali haya yanayotokea kwa watoto, na ili haya yote yaishe ni deni lilipwe, na deni hilo limethibitishwa kuwa ni la kaka…mimi sijaona ushahidi mwingine wa kulitengua hilo, kama ushahidi mwingine upo nionyesheni mie,ukiwepo kwanini ning’ang’ania hilo, itasaidia sana..ndio maana naona kama wewe unachopigania ni mali zaidi…’akasema.

Hapo mimi nikaona niingilie kati, na kusema;

‘Dalali ulichotaka shemeji yako umeshakipata..haina haja ya kumueleleza shemeji yako, yeye hapo alipo, anachopigania ni haki,..haki ya mume wake. aliyemfahamu vyema tu, na haki ya familia yake, kuhakikisha kile alichokiacha mumewe kinabakia salama…’nikasema

‘Naomba tafadhali, msiingilie kati, …hili ni swala langu na shemeji yangu, mimi ndiye mwenye mamlaka ya hii familia, nyie baada ya hili mtaondoka, ni nani atawatunza hawa watu, nataka niwe na uhakika kuwa kweli shemeji kakuchukua kwa dhamira ya kweli au ni hadaa zako…’akasema Dalali.

‘Mimi nitajitunza mwenyewe shemeji, kama unafikia kuniona kuwa mimi nina tamaa ya mali, ..sitaki tena msaada wako, nashukuru sana kwa huduma zako zote, nashukuru sana…’akasema mama mjane.

‘Shemeji…sasa hivi hutaki huduma zangu au sio…wakati umelala huwezi hata kujiinua ..ni nani alikusaidia,..shemeji mimi sio kwamba naongea haya kwa nia mbaya,…au kutaka fadhila baada ya hayo yote niliyojitolea, .. kiutaratibu eeh..wewe ulitakiwa uongee na mimi kwanza, hapo mimi nina makosa gani shemeji…?’ akauliza

‘Huna makosa, kwa vile..wewe huna tamaa ya mali, mimi nina tamaa ya mali, lakini bado nasema siwezi kukubaliana na hilo deni, moyoni mwangu nahisi hilo deni sio la kaka yako, je sitakiwi kuwa mkweli..najua hukutaka niyasema hayo, kwa saabu ya mizimu, lakini nataka mizimu ijue kuwa mimi sina kosa, …’akasema mama mjane.

‘Sawa shemeji mimi nimekuelewa,...ngoja tuone, si tupo,...na... na kama nimekosea kwa kauli yangu hiyo naomba unisamahe tu shemeji yangu…nitakuwa mkosaji sana, wewe kwangu ni kaka yangu ambaye hayupo duniani…nisamahe tu shemeji, nimeshachanganyikiwa,..mimi naogopa sana yakitokea tena...’akasema.

‘Hamna shinda, nimekuelewe na mimi nimeshakusamehe…’akasema shemeji yake.

‘Lakini  kwa hali inavyokwenda inabidi nimuite wakili wangu …maana sasa najiona nipo peke yangu, nayasema haya kwa nia njema tu, ili kila jambo liende kisheria, najua huko mbele tutakwama, sasa isije kuja kutupiwa mimi lawama, ningelipenda haya yote yaende kisheria..’akasema.

‘Shemeji mbona mimi sijafikia huko..kwanini tusimuache huyo mtu akatusaidia, huenda akafanikiwa, kwanini hilo likuumiza kichwa, mpatie ushirikiano huyu msamaria mwema,…tuone kama tufanikiwa, ikishindikana basi..’akasema mama mjane.

‘Tatizo sio hilo, tatizo, kwanza nikuzarauliwa, pili ni kukiuka sheria, hukumu ilishapitishwa,sasa tunakiuka je ikienda na kuonekana ni sahihi, nii nani atalipa hizo gharama wewe hulioni hilo, jingine ni hayo mambo ya mizimu, wewe huyaogopi, lakini inaniumiza nikiona mtoto anateseka, je wewe hata hilo hulioni ..?’ akauliza.

‘Huyu aliyejitolea analifahamu hilo…na sizani kama atafanya hivyo kwa nia ya kutukomoa sisi, ..kaona kama kuna namna ya kushinda, tumuache tu aifanye hii kazi, na sisi tumpa ushirikiano, na hayo mambo ya mizimu nakuachia wewe, ufanye uwezavyo, ili tuone tumefikia wapi…’akasema mama mjane

‘Kwahiyo kwa kauli hiyo, wewe umerizika naye, sio...sawa,  na kama umekubali kuwa ulimtafuta wewe kwa lengo hilo, hata bila kunishirikisha, sawa pia...'akatulia kidogo.

'Haya… sawa shemeji..ngoja tuone, mimi sina shaka kwa upande wangu....ila bado msimamo wangu wa wakili upo pale pale,maana huyo wakili nilishamtafuta nilishaingia naye mkataba kuhusu hili tatizo, ngoja awepo kutusaidia zaidi, wapambane wakili kwa wakili …’akasema akinitupia jicho mimi

‘Lakini huyu hapa sio wakili…’akasema mama mjane akinionyeshea mimi, lakini ni kama hakuwa na uhakika na kauli yake hiyo.

‘Ni nani sasa..mbona unanitia mashaka…!?’akasema kwa mshangao na kuuliza

‘Ni msamaria mwema tu..kaliona hili tatizo na ni mwerevu wa kulitafutia majawabu…na yeye anawatumia mawakili…au…?’ mama mjane akasema na kuniangalia mimi.

‘Naruhusiwa kuingilia kati..?’ nikauliza

‘Haijalishi,… ila bado mimi nitamuita wakili wangu aje hapa…’akasema

‘Wa nini, unawasiwasi gani.?’ Aliyeuliza sasa ni mpelelezi

********

Dalali akageuka kumuangalia mpelelezi, huku akitabasamu kuonyesha hana wasiwasi na akasema;

‘Wasiwasi wangu ni kuwa kwa hali inavyokwenda, kuna kuja kulaumiana hapa, na mimi sina uwezo wa kulipa gharama..na najiona kama vile nashinikizwa kwenye matatizo,…’akatulia.

‘Matatizo gani…?’ akauliza mpelelezi.

‘Mhh…naona kama nashutumiwa , ..na hatua iliyofikia hapa, kiukweli…inahitajika mtu anayefahamu sheria,  sitaweza kujidanganya kuwa ninafahamu kila kitu..’akasema Dalali.

‘Lakini….’nikataka kusema , nikakatizwa na mlio wa simu, ilikuwa ni simu ya Dalali
Dalali, akamuangalia mpelelezi,..halafu akaangalia simu yake  ni nani mpigaji, ..

‘Naweza kupokea hii..?’ akamuuliza mpelelezi

‘Endelea tu..’akasema mpelelezi

Dalali,…akapokea, kwa sasa hivi sauti ya nje ya spika ilikuwa haijawekwa, kwahiyo alichokuwa akiongea huyo mpigaji, tulikisia kwa mbali tu..lakini sio rahisi kuelewa vyema, na Dalali alikuwa kageukia upande mwingine kutupa sisi mgongo.

Akawa anasikiliza bila yeye kusema neno, na wakati anasikiliza akageuka kutuangalia,.. niliona uso wake ukibadilika, halafu akasema;

‘Una uhakika,…ndio nakuuliza una uhakika hayupo kwake, kaenda wapi sasa, mimi sijui, tafuteni kaenda wapi, eeh, unasema, hajui,..haiwezekani, nani,, ….?’ Akauliza na akawa anasikiliza halafu akasema;

‘Ndio….nimemtumia ujumbe wa maneno hajajibu, nikampigia simu yake, hipatikani,…..kuna nini kwani..?’ akasikilza  baadaye akakata simu,kwa hasira …usoni akawa kakunja ndita, makunjazi,kuashiria kukasirika... akageuka kuniangalia mimi , akajaribu kukunjua hizo ndita,  akasema;

‘Haya niambie kinachofuata maana sioni haja ya kuulizwa maswali ya kunikandamiza mimi…ni lazima wakili wangu afike kwanza, au unasemaje wewe muuliza maswali…na afande, nataka kufahamu jambo moja.., je mimi ni muhalifu…?’ akauliza

‘Tukuulize wewe je wewe unajihisi vipi, kuwa muhalifu, je kuna kosa umelifanya..?’ nikamuuliza

‘Mimi sina kosa…’akasema

‘Sasa kama huna kosa, wewe una wasiwasi gani, na kwanini kama huna kosa ,kwanini ukimbilie kuita wakili….huoni huo ni ushahidi kwangu ..’nikasema

‘Hahaha..ushahidi ushahidi, sasa hivi kila kitu ni ushahidi na wewe huo ushahidi ni wa nini, kama kweli huna nia mbaya na mimi…?’ akauliza

‘Siliza Dalali, tusipoteze muda mwingi,…mimi nataka tuende sawa, sio kwa ugomvi, na nia hapa ni kuelimishana , ili tuupate ukweli halisi, mimi nina mbinu zangu za kuupata ukweli, hasa kwa njia hii ya maswali..’nikasema

‘Unafanya makosa sana…’akasema

‘Usiwe na shaka Dalali,…tulishaanza kuulizana awali, au sio, na hadi hapo umeshanielewa nia yangu ni nini…kwahiyo tuendelee tu, na mwisho wake tutaupata muafaka,..’nikasema halafu nikamgeukia Mpelelezi,

‘Au sio afande…?’ nikamuuliza mpelelezi.

‘Nyie endeleeni tu, ila wakubwa huko wananishinikiza, leo iwe ni mwisho, na wewe tukitoka hapa twende kituoni,….’akasema.

‘Hamna shida afande…’nikasema na Dalali akawa anatabasamu ile ya dharau, akasema;

‘Ni kweli afande,..hata mimi simuamini huyu mtu..kamghilibu shemeji hapa, na anaweza kutuingiza kwenye matatizo…’akasema, na mimi sikujali hayo maelezo yake nikasema;

‘Sasa nataka tuanze kuliangalia hilo deni, baada ya kuona kuwa, hayo mambo mengine ya kiimani,..mizimu sijui… hayana msingi kwenye hilo deni….’nikasema

‘Hapana,..yana msingi , huwezu kutulazimishia hivyo,..usitake kuniweka mimi matatani, hayo yana msingi wake, sema wewe huelewi tu…’akasema

‘Nimeshaelewa,…ila nikuulize kwa hilo ni kwanini mtaalama kakimbia na kujificha, kama kweli hana jambo na hili jambo, kama kweli anayoyafanya ni sahihi, kwanini akimbie, kujificha huoni inatia shaka…?’ nikamuuliza

‘Hilo la kukimbia na kujificha, ni wewe unasema hivyo, hakuna ushahidi kuwa kweli kakimbia, au kajificha, mimi sijaupata ushahidi huo, ni dhana zako tu…’akasema.

‘Kwahiyo wewe una uhakika kuwa huyo jamaa hajakimbia, kuna sehemu yupo, sasa kwanini akaacha simu yake nyumbani…, kwanini akawa akatumia namba nyingine..?’ nikauliza.

‘Kusahau simu ni jambo linatokea kwa kila mtu..., hata mimi niliwahi kumpigia siku moja.., akawa hayupo, na mkewe akapokea, hilo sio sababu ya kumdhania vibaya, …na huko alipo angelitumia namba gani sasa, hebu uwe mwerevu kidogo..’akasema Dalali.

‘Hana simu, ila kaweza kukumbuka namba yako,…na wewe ulidai kuwa yeye sio rafiki yako wa karibu..?’ nikamuuliza

‘Mimi nitajuaje, labda aliandika hizo namba mahali,..na kiukweli…ukiwa nashida unaweza kupiga namba yoyote..mbona kitu kipo wazi, ..ndugu yangu, mimi nina mashaka na shule yako…’akasema

‘Hiyo namba aliyopigia ina jina la mwanamke…’nikasema

‘Umejuaje…?’ akauliza

‘Shule yangu niliyopitia imefundisha hilo…na kama tumefahamu kuwa hiyo namba ni ya mwanamke..na pia tumefahamu ni wapi alipo….’nikasema

‘Hahaha..sawa fanyeni muwezavyo, hata mimi itanisaidia ili kufahamu kama hayupo kwenye matatizo, na ni muhimu kwangu pia…’akasema

‘Kwa vile ni rafiki yako au sio..?’ nikasema

‘Hilo sio muhimu, hata wewe nimekutana nawe hapa, nikisikia huonekani, kwa vile nimeshazoeana nitajitahis kusaidia kukutafuta, hukusikia mkewe alivyo sema

‘Mkewe alisema nini…?’ nikamuuliza

‘Uwe na werevu bwana…hata hilo nikuambie, ina maana wewe hukusikia, mkewe akisema ana wasiwasi, hajui  wapi alipo mumewe..’akasema

‘Lakini wewe si umeshawasiliana naye, kwanini hukumuondoa wasiwasi huo mkewe, ili ajue kuwa mumewe hayupo kwenye matatizo,…si umeongea naye au?..akakuambiaje..?’ nikauliza

‘Hajasema wapi alipo, …na unajua tena wanawake, ningelimuelezea hivyo, ningelizi kumtia wasiwasi..kwanza hiyo namba aliyopiga haiaminiki…hata nikimpatia mkewe, anaweza akapiga asimpate…atakuwa kaomba kwa jirani, sio vizuri kumpatia hiyo namba kwa hivi sasa…’akasema

‘Lakini hiyo namba ni ya mwanamke au sio…nahisi unamfahamu , unaogopa utawagombanisha, au sio,…sema ukweli bwana…’nikasema

‘Hahaha, hayo unayasema wewe…na aliyeongea sio mwanamke, ni sauti ya kiume…’akasema

‘Una uhakika ni sauti ya mtaalamu mwenyewe..?’ nikamuuliza.

‘Kwanini nisiwe na uhakika nayo au….’akasema na kusita,

 ‘Basi huo ndio werevu, ...mimi nilikutega tu, na wewe umetegeka,…kumbe unafahamu kabisa huyo aliyekupigia kwa namba nyingine ndiye mtaalamu, kwanini ulitaka kutuficha sisi…?’ nikauliza

‘Nimeshawaambia…hayo ya mtaalamu huko alipo mimi sijui, ..hayanihusu mimi…yeye ana shughuli nyingi, na anaweza kafanya hivyo kwasababu zake, siwezi kujua…’akasema

‘Swali hapo tunahitajia jibu, je huyo aliyekupigia baadae ni mtaalamu au sio mtaalamu..?’ nikauliza

‘Sio mtaalamu…’akasema, nikageuka kumuangalia mpelelezi, na mpelelezi akatabasamu kidogo.

'Kama huyo sio mtaalamu, ni nani basi....unataka tulithibitishe hilo kuwa aliyeongea ni mtaalamu...?' 

NB: Ngoja niishie hapa maana nipo kwenye mitihani ya maisha.


WAZO LA LEO: Kauli inaweza kuleta sintofahamu , kwa jinsi ulivyoitoa, hata kama ulikuwa na nia njema tu. Ni busara sana pale tunapoongea tukajaribu kuangalia mazingira, hali halisi ..isije ikawa kauli yakuumiza sehemu ya kubembeleza, isije ikawa kauli yakuongea majonzi kwenye kutoa pole. Isije ikawa kauli ya dharau,..kwenye kuelimisha jambo. Ulimi uchingwe sana kwenye kuongea. Ndio wazo la leo
Ni mimi: emu-three

No comments :