Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Friday, February 21, 2014

BAADA YA DHIKI FARAJA-15


Kesho yake nikafika ofisini, huku nikiwa bado nawazia, jinsi mdada alivyoweza kulitoa hilo gari lake, ...nikakumbuka jinsi ilivyokuwa siku ile, baada ya kufika kwenye hiyo hoteli, na kuongea na mlinzi, halafu nikapanda kuelekea juu.....


Nilipanda hadi rosheni ya pili, nikaelekea kwenye chumba alichonielekeza kwenye simu, nikagonga mlango, na haraka mlango ukafunguliwa, na kukutana uso kwa uso na mdada, akiwa anameremeta, kajipamba, utafikiri sio yeye, akaniangalia juu chini, na halafu akasema;

‘Upo tayari?’ akaniuliza huku akiendelea kunikagua

‘Nipo tayari kwa nini?’ nikamuuliza huku nikiwa nimekunja uso, sikupenda hali niliyoikuta humo , maana kulionekana kabisa kuna mabaya yanayoendelea humo, na kama ingeliwezekana, ningeondoka haraka, lakini mdada alishanitega, ....

‘Kushika milioni tano, hivi...kwa siku moja tu, kwa kazi ndogo tu, ...kinachotakiwa ni ujasiri na kujiamini,...’akasema huku akiniangalia moja kwa moja usoni, na sipenzi kumwangalia huyu mwanadada usoni, maana nikiyaangalia macho yake, mdomo wake...oh, nashindwa hata kuhema.

Hapo nikasema ngoja nijipe ujasiri, maana sijui huyu mwanamke anataka nifanye nini, anaweza kunitumbukiza kwenye biashara haramu,...nikimuangalai hizo nguo alizovaa na mshahara wake haviendani kabisa, na sasa anasema ana gari, pesa anazipatia wapi, kama sio biashara haramu..ni lazima niwe mwangalifu...nikawa nawaza hivyo, na kumwambia;

‘Kwanini unichague mimi, na unafahamu kuwa mimi sipendelei mambo yako, kwanini hukuwaita jamaa zako wengine?’ nikamuuliza

‘Maswali ya polisi siyataki, nimekuitia hapa kwa kazi, moja, ...hii ni kwa kukusaidia tu,...nisingelikuwa na haja na mtu kama wewe....’akasema na kunishika mkono akanivutia ndani.

Mikono yake ilipogusa mwili wangu, ilikuwa kama kitu cha ajabu kimeingia mwili wangu, kwanza nilihisi nimeshikwa na mkono wa mtoto mchanga, mikono yake ilikuwa laini sana, na nilihisi kama ina kitu cha ziada cha kunifanya mwili wangu uwe hauna mawasiliani na akili yangu tena...sikuweza kupinga,  nilijikuta nikimfuata nyuma kama mbwa anavyomfuata chatu.

Tulifika karibu na kitanda, na hadi tunafika hapo, nilikuwa kama mtu aliyezibwa akili, hadi aliposema;

‘Sasa sikiliza, unamuona huyu mshamba aliyelala hapo kitandani, keshazidiwa hana ujanja, nimeshamchukua picha za awali, bila kujua,....sasa hatua iliyobaki, ni kumbeba na kumtoa humu ndani, tunakwenda kumlaza nje...sehemu ile ya mapumziko,sitaki azindukane, akiwa humu,..’akasema.

‘Mimi ..mimi..mambo yako sitaki kabisa...’nikasema kwa kigugumizi.

‘Pili, kwenye nguo zake, kuna milioni kumi, alilipwa na jamaa mmoja tukiwa huko chini, hizo nitazichukua kufidia pesa zangu, alizozichukua,....lakini cha muhimu kwanza tumtoe humu ndani........’akasema.

‘Hapana mimi siwezi kufanya hayo, kwanza huo ni wizi, na...hapana....tabia ya wizi,mimi siijui...kama ndicho ulichoniitia hapa, mimi naondoa...’nikasema na kugeuka kutaka kuondoka, na mara nikasikia ujumbe ukiingia kwenye simu yangu, nikaitoa imu yangu na kuangalia ni nani kanitumia ujumbe muda kama huo, nikaangalia ni nani mtumaji, kulikuwa hakuna namba;

Nikaanza kuusoma huo ujumbe, ulikuwa ukitoka kwa huyu,.. huyu mdada, sijui aliutuma vipi na wakati huo nipo naye humo ndani, nikainua kichwa kumwangalia, yeye akatabasamu na kusema;

‘Mambo ya digitali hayo, kila ukipinga jambo ninalokuambia, mimi natoa ishara, meseji inaingi kwako, na zikizidi meseji tatu, moja moja ujumbe unakwenda kwa baba mkwe wako, na kwa mchumba wako...’akasema huku nikiwa naufungua huo ujumbe kwani ulikuwa na picha, ...loooh, ....yale yale mapicha mabaya.

Nikageuka kwa hasira nikimwangalia mdada, yeye akawa kanilegezea macho na kutabaamu, huku akisema kwa sauti ya kulegeza;

‘Masikini, mhasibu, ...ukikasirika sura inatisha,....’akasema, halafu akabadili sura na kuondoa tabasamu, akasema kama bosi anayeamrisha jambo

‘Upo tayari, tunakwenda kwa muda mpenzi hapa, ... au nitoe ishara nyingine...?’ akaniuliza na mimi nikawa bado namwangalia kwa hasira, akageuka kunipa mgongo,mara kweli sauti ya kuashiria kuwa kuna ujumbe umeingia kwenye simu yangu ukasikika, sikuamini kuwa ni yeye aliyetuma huo ujumbe.

Nikiwa bado namwangalia, nikabonyesha simu yangu, kufungua ujumbe, nikainama kuusoma, ni kwelu ulikuwa ukitoka kwake, na pembeni yake kuna sekunde zinajihesabu, na chini yake kuna maandishi mekundu, yakisema kumebakia ujumbe mmoja, kwenda kwa....nikaona namba ya baba mkwe...

‘Hivi wewe...’nikaanza kusema lakini yeye akaniwekea kidole chake kwenye mdomo wangu kama kuninyamazisha, na kusema;

‘Anza kazi, sitaki utani,....’akasema huku akimsogelea huyo jamaa na kuanza kumuinua...nikamwangalia baadaye nikaona haina haja, si kazi ndogo tu,nikasogea nikamsaidi kumuinua huyu jamaa na kumbeba,nikatoka naye nje, huku mdada akinifautilia kwa nyuma...

Yeye hakwenda mbali, alisimama pale mlangoni, akiniangalia, kuniacha niendelee mwenyewe.

Nilimbeba huyo jamaa hadi sehemu iliyopangwa viti, ni sehemu ya kumpumzika, kuna meza na viti, na pool table, nikambeba huyo jamaa hadi kwenye ile meza na kumlaza hapo, alikuwa uchi,na taulo ndogo tu, ambayo kwa muda huo ilikuwa begani kwangu.

Nilipomlaza pale juu ya ile meza ya kuchezea pool, nikachukua hiyo taulo na kumfunika sehemu zake za siri, na wakati nataka kuondoka mara mkono ukanishika kwa nyumba, hali hii ilinishitua,maana kulikuwa hakuna mtu mwingine, na huyo jamaa alikuwa kapoteza fahamu, hajijui, nilishituka karibu nidondoke, nikageuka kuangalia ni nani kanishika.

Alikuwa ni huyo huyo jamaa, ....inaonekana, ana fahamu kidogo, na aliweza kuinua mkono, na kujaribu kunishika, lakini tatizo la hayo madawa ukiyanyweshwa, mwili wote unalegea, unashindwa kuwa na nguvu, unaweza ukawa na fahamu kidogo ya kuona kinachoendelea lakini huwezi kuinua hata mkono, ...jamaa akasema kama vile mtu anaota usingizini;

‘Nisaidie ...simu yangu..... mpigie rafiki...’akasema na sauti ikakatika
‘Mpigie rafiki, rafiki yake ni nani, mimi nitamjuaje huyo rafiki...nikainama kumwangalia na wakati huo, alianza kukoroma kama vile mtu anakata roho, nikaona sasa haya ni makubwa,huenda jamaa ndio anakata roho...haya sasa ni mauaji.

Nikasita kuondoka, nikaona, ngoja nihakikishe, isije kuwa kweli, jamaa amekufa,nikamsogelea,  nikainama kumchunguza, alikuwa kimiya na nilihisi mapigo ya moyo kwa mbali sana, nikawaza sasa nimfanyie nini...

‘Unafanya nini hapo, unapoteza muda, umebakia muda mchache, nguvu za madawa zitaisha akizindukana hapa, hutamuweza huyu, jamaa huyo ana nguvu za watu watatu..’ilikuwa sauti ya mdada, kumbe alishafika na mimi kwa haraka nikageuka, na kumwangalia, kabla sijasema neno akasema;

‘Mwache hapo, ....kuna mambo mengine ndani, ...’akasema kwa sauti ya kutoa amri.

Nikainuka pale nilipokuwa nimemuinamia huyo jamaa, nikamwangalia mdada kwa hasira, nikatembea hadi pale alipokuwa kasimama, nikampita na kurudi kwenye kile chumba,

Baadaye akaja, na kunishika shika mgongoni akasema;

‘Nafikiri hapo ulipo unafikiria mengi, na huenda umehaniweka kwenye kundi baya, kuwa pengine ....mmmh,, labda mimi ni muhuni au mimi ni jambazi, lakini nikuambie ukweli, mimi sina tabia hiyo kabisa...’akaendelea kunishika shika.

‘Nikuambie ukweli, hili ninalofanya ni katika harakati za kuwakomoa watu kama hao, nina usongo sana na watu wanaoitwa wa-na-u-me, . Nyie watu nyie, ....nina uongo sana na nyie,...ninawa-mind kichizi, walichonifanyia wenzako huko nyumba, nimeapa kuwa kila nikipata nafasi kama hii, nitafanya kila niwezalo, kulipiza kisasi...’akasema na kuniachilia, akasogea pembeni, huku akiwa kaangalia mlangoni.

‘Unamfahamu huyo jamaa...?’ akaniuliza huku akiwa kanipa mgongo.

‘Ninamfahamu, nani,...mimi simfahamu...nitawafahamu wapi wanaume zako...na mambo yako...kama walikufanyia mabaya na hao hao, sio mimi...?’ nikasema kwa sauti ya kukerwa.

‘Hahaha, sio wewe eeh, ndio maana nimekustahi,ila kama utashirikiana na mimi la sivyo, ...’akageuka kuniangalia.

‘Halafu,sauti yako hiyo inaonyesha wivu eeh,mmmh, masikini mhasibu, ananionea wivu, mmmh, ...nikuambie ukweli, huyo jamaa na wengine, waliowahi kuingia kwenye makucha yangu, hawana lolote kwangu...baada ya unyama niliofanyia huko nyuma, nilishaapa kuwa sitaki tena mtu anayeitwa mpenzi,...mwanamume..’akanisogelea na kunitoa na kidole kifuani.

‘Nikuambie wewe mtu, huyu mtu, ni katika wale watu, nilio-apa kuwa nikipaat mwanya wataipa fresh,na nahisi kwa jinsi ulivyoona, unahisi huyu jamaa kala ndizi,...kwa taarifa yako tu, hakuwahi hata kuimenya, zaidi ya kuibonyeza bonyeza akiangalia kama imeiva, na alipoona imeiva, akataka kuila...wewe sio kwa mdada, sio rahisi hivyo...’akakunja ngumi na akawa kama ananipga piga kifuani.

‘Huyo jamaa alikuwa na pupa, nikamtuliza,..., na wakati anataka kuimenya hiyo ndizi, dawa nilizomwekea bila ya yeye kujua, zikaanza kufanya kazi, na hapo hapo mimi nikaanza kufanya mambo yangu, mjini hapa...’akaongea bila wasiwasi.

‘Unaongea utafikiri ni jambo nzuri, ungelijua ninavyojisikia moyoni uingelipoteza muda kunisimulia..’nikasema na yeye bila kujali maneno yangu hayo akaendelea kunielezea;

‘Alipozidiwa, akawa hana ujanja, nikawa namfanya ninavyotaka,...ukiwa na akili na ujanja, mijitu kama nyie, naipeleka ninavyotaka...nyie si mna mikono, mna nguvu, mnaweza kuishika ndizi na kuiminya na kuimenya, na kuila mtakavyo,...wapii, ni kwa wajinga sio mimi, ...’akageuka na kunipa mgongo.

‘Lijamaa kikawa linakuja lenyewe, bwata-bwata, halina nguvu, kabla halijadondoka, nikaomba msaada kwa jamaa walinzi;

‘Jamaa yangu kalewa sana, naomba mnisaidie tumpeleke kwenye chumba chake...’nikamwambia mmoja wa walinzi anayenifahamu.
‘Umepata mdondo mwingine..wewe dada wewe...’akanitania, huku akimbeba hadi kwenye hiki chumba.

Nilipofika sikupoteza muda, nikamsalula nguo zote, huku akiwa na kimuhemuhe,..hizi dawa zilivyo, ni kuwa mwanzoni unaweza ukawa na hali ya kuweza kufanya jambo, na unaweza kuamrishwa fanya hivi, au vile na wewe unafanya tu...ila baadaye zinakuvunja nguvu kabisa, ...’akasema na kunifanya nikumbuke kile walichoawahi kunifanyia.

‘Jamaa muda huo linatokwa na mate kama mbwa koko,,...tamaa, umalaya umemjaa, lakini hakuweza kufanya alichokitamania, madawa yalishamlegeza, wakati huo nilishaweka mambo yangu safi,...picha zikawa zinachukuliwa..’akasema huku akitabasamu, na kuonyesha dharau mdomoni.

Mimi nikatikisa kichwa kama kumsikitikia, halafu nikageuka kuangalia pembeni, nikimuwazia huyo jamaa alivyokuwa, hajijui yupo uchi, ..ina maana siku ile na mimi nilifanyiwa hivyo.

‘Nilichofanya ni zoezi la kuigiza, kama jamaa anakula ndizi vile, kumbe hakuna kitu, ilimradi upatikane mtaji,...picha ninazozihitajia,...nikamaliza kazi ya kwanza, lakini hatua nyingine nisingeliweza kuifanya peke yangu, ni lazima nipate msaada ndio nikakupigia simu...’akaniangalia.

‘Nilipanga nikuite mapema, lakini nikaona wewe bado mshamba, halafu ...sijui labda ni kupenda, nakuonea huruma, ...vinginevyo, ningelikufanya kama ninavyowafanyai hawa, watu wanaoitwa wana-ume...nakaona nifanye hatua hii ya mwanzo peke yangu, nakufahamu sana,hujawa na akili za kutafuta pesa, ila sasa ujue umeshakuwa mtu wangu....’akasema.

‘Sikuelewi..unachoongea....ni upuuzi mtupu sitaki hata kuusikiliza...mimi sio mtu wako, niache kabisa na mambo yako...’nikasema nikitaka kuondoka.

‘Hahaha, sasa unataka kwenda wapi, hutaki pesa yako eeh, ....’akasema akiwa kashikilia bulungutu la pesa mkononi, nikamwangalia kwa hasira na kusema;

‘Japokuwa nina shida ya pesa lakini siwezi kuchukua hizo pesa chafu, ....’nikasema na yeye akanisogelea, akanishika shika ,safari hii, nikajarubu kumzuia, na muda huo nilikuwa bado nimevaa koti langu la kuendeshea pikipiki, ...huwa nikiendesha pikipiki muda kama huo, huwa navaa koti kubwa, kwa ajili ya kujikinga na baridi.

‘Nafahamu unaona aibu, lakini usijali, utazoea tu, saa hivi umeshayafulia maji nguo, huna budi kuyaoga, ...nilitaka nikuhusishe kwa kiasi hicho, ila kuna kazi moja nataka uifanye...’akasema

‘Kazi gani tena!?’ nikamuuliza nikiwa na wasiwasi.

‘Huyu jamaa alitaka kuniingiza mjini, nilishamlipa pesa za awali, kwa ajili ya kulitoa hilo gari, nilimtumia yeye, kwa vile ni bosi wa kitengo hicho, ni kweli, anawasaidia watu wengi, kwa mtindo wa nipe pesa nikufanyie chapuchapu,...pesa za uwani, hizo haziingii kwenye mahesabu ya kampuni.

‘Tatizo ni kuwa siku hizi amekuwa ghali sana,anadai mambo sasa yanafuatiliwa sana, kwahiyo anabeba hatari kubwa kuwasaidia watu, yeye anaita `kusaidia’, nilipokutana naye, akajifanya hana muda, huku anatamani kukutana na mimi, nikamjaribu tena ndio akapanga tukutane sehemu, tukaongea, akanipangia kiwango changu..na bado akitaka na rushwa ya ngono,...’akaangalia saa.

‘Nikahangaika weee, mpaka nikapata kiasi kidogo,...nikampa, alisema nimtumie kwa mtandao, kwenye namba zake za muda, ni mjanja sana,...namba hiyo akishaitumia mara moja, anaiharibu, haisajiliwi,.... nikamlipa kianzio, ...ili alitoe hilo gari halafu nitakuja kummalizia nikipata pesa nyingine,..akanishitukia,... unafahamu alichosema;

‘Huwa mimi silipwi nusu nusu, kama huna pesa basi na hizo ulizotoa usahau, kwani kiendacho kwa mganga hakirudi....unaona alivyo,..jamaa huyu ni tajiri kweli, lakini hatosheki, ana majumba ya kifahari,...magari, kwa ajili ya pesa hizo za magumashi...kodi ya mlalahoi inateketea...na sasa anataka kunilia pesa yangu, hajui nilivyoipata...’akasema huku akiangalia saa.

‘Nikamwambia hapa umepotea maboya, utazitoa hizo pesa na nyingine nyingi, na nitahakikisha utajiri ulio nao, tunagawana....nilimwambia hivyo wazi wazi, akajua natania, nikawa namuwinda, ndio wewe ukaja kuajiriwa...

‘Wale wenzako waliofukuzwa, walinisaidia sana hadi nikalipata hilo gari, nikajua saa wewe kazi yako ni kuhakikisha linatoka bandarini...lakini kumbe oh, anyway, tuyache hayo...kwani huyu jamaa saa anamaliza kazi, ...’akasema na kuangalia saa yake.

‘Jana huyu jamaa kajileta mwenyewe, akaingia kwenye anga zangu, ...’akasema huku akijiangalia kama anajikagua, huku akitabaamu.

‘Alikuwa ananitafuta sana huyu jamaa, ananitamani, ....lakini mimi sikuwa namtaka, simpendi, namchukia, nina usongo naye....japo kuwa ni tajiri,na wanaume matajiri wanapendwa, lakini sio kwangu mimi, ninachopenda ni pesa, hata hivyo mimi, namuhehimu sana mke wake, ...isongelikuwa hivyo, ningelishamfanyia kitu mbaya siku nyingi.

‘Aliponichoharibu ni kunitapeli mimi pesa zangu, nikaona sasa kamchefua mtoto wa mjini, atalisugua gaga, nikaapa kuwa nitamuonyesha,...’

‘Alikuja akanikuta nakunywa, na aliponiona na nilivyovalia,mhh, macho hayakuficha uchu wake, ....akaisha, na mimi nikajifanya nipo tayari naye, tukanywa pamoja, ...nikajaribu kumkumbushia kuhusu gari langu akasema atanisaidia kulitoa gari langu, lakini kwa masharti kwanza anifanye hawara yake, na akirizika nami, gari atalitoa bila hata ya kutoa pesa nyingine, ..’akasema

‘Wakati nipo hapo tunakunywa nikimweka sawa, ili nipate muda wa kufanya mambo yangu, mara akaongea na jamaa mwingine...’akasema

‘Jamaa gani?’ nikamuuliza na yeye akaangalia saa, na alikuwa kama hakusikiliza wali langu akaendelea kusema;

‘Wakati tunakunywa, simu yake iliita, akaongea kwenye simu na huyo jamaa, na akamwambia huyo jamaa alete huo mzigo hapa kwenye hii hoteli..nikasema sasa jamaa kaisha huo mzigo ni wangu, anarudisha pesa yangu, na riba juu...’akasema

‘Ulijuaje kuwa ni mzigo wa pesa...?’ nikamuuliza.

‘Walikuwa wanawasiliana nawasikia,hadi kuwekeana kiwango, jamaa alitaka kunionyesha kuwa yeye ni mtu wa mapesa kimoyo moyo nikasema....hizo ni zangu, alipomaliza kuongea na huyo jamaa nikwambia;

‘Kweli wewe kiboko, yaani unadai pesa zote hizo, halafu unataka akuletee huku kwenye mabaa, huogopi vibaka...yeye akanicheka, na kusema;

‘Hizo nazo pesa....hahaha, milioni kumi ni pesa ndogo kwangu, ..hivyo ni vijisenti kwangu, na hata sina haja ya kuzipeleka benki, ...’akasema, nikasema kweli nchi yetu inaliwa, kuna watu mabadhirifu, wanakufuru,wanakula bila huruma ...lakini mimi nitapambana nao....’akasema huku akikunja uso kuonyesha chuki

‘Hivi hizo pesa zote sizingesaidia shule, madawa, ...angalia kijijini watu wanavyoteseka, watu wanajenga mahekalu...kwanini na mimi nisichukue nafasi hii kuzimega,..maana ukiwaachia hawa mafisadi, watakula huku wanatuanifu kuwa sisi hatujaenda shule, utaenda shule na nini....’akasema kama ananiuliza.

 ‘Na kweli haikupita muda, mara huyo jamaa aliyeongea naye kwenye simu akaja,...akampa hizo pesa kwa siri, na kuondoka, lakini mimi nilishaona, na wakati huo nimeshafanya vitu vyangu, nilipoona jamaa yupo lepelepe, nikamshika mkono na kuelekea huku kwenye chumba, alicholipia yeye mwenyewe...ndio nikafanya vitu vyangu...’akasema.

‘Sasa unataka kumfanya nini,...?’ nikamuuliza.

‘Huyu jamaa ana mke, na mke wake sio mtu wa ovyo,...akiligundua hili, kutawaka moto, ...ndio maana nimemfanyia hivi, ili gari langu litoke haraka iweakanvyo, huyu jamaa ana uwezo huo...’akasema.

‘Nataka akizindukana hapa, ayakute machafu yake kwenye simu yangu na nyingine nimeshazituma mahali salama, hata kama simu hii itaibiwa au kupotea, bado mapicha hayo yapo mahali...mimi mjanja...’akasema  huku akionyesha mbwembwe.

‘Akizinduka hapo atakutana na picha ya matendo yake kwenye simu yake...japokuwa hayakufanyika kiukweli..lakini kwa jinsi nilivyoigiza utafikiria ni kweli kafanya hivyo...hata wewe nikikuonyesha utafikiria kuna kitu kimefanyika, lakini hakuna kitu kama hicho mimi sio mjinga...’akasema huku akionyesha kidole kwenye kichwa chake.

‘Kwahiyo unataka kumfanyia kama ulivyonifanyia mimi?’ nikamuuliza akatabasamu na kusema;

‘Huyu jamaa ni malaya, mwizi, na tapeli ..anatumia wadhifa wake, kwa masilahi yake,...mkewe ni muheshimiwa, ana heshima zake, na alishamwambia mume wake huyu, akija kugundua kuwa anamsaliti, atamuumbua na hata hiyo kazi anayotamba nayo, ...’akaniangalia.

‘Hawa watu hawa,...mungu atawalaani sana, kazi aliyo nayo ndio anayoringia,....hataki kabisa kutoka kwenye hicho kitengo, anajua jinsi gani ya kula na vipofu, wakubwa wanamlinda kwa vile anajua jinsi gani ya kuwaweka sawa,...yupo kwenye idara nyeti, anachota mapesa anavyotaka, lakini kibaya ni kuwa hatosheki....’akasema huku akikunja uso.

‘Sasa akiyaona matendo yake hayo, na nikimtishia kuwa nampelekea mkewe, nina uhakika atafanya kila ninachokitaka...mimi namfahamu sana, pamoja na yote hayo, lakini kwa mkewe, kafika...namfahamu kuliko navyojifahamu yeye mwenyewe...zaidi ya hayo nitamtishia kuwa nitayaweka hayo machafu yake hadharani...kwenye maudaku...atasugua gaga, nakuambia ukweli..., ndio maana nikakuhitajia hapa....’akasema huku akiangalia saa yake.

‘Unanihitajia nini mimi..hapana nililofanya linatosha na ninajuta kwanini nimekuja, mimi sitaki kujiingiza kwenye mambo yako ya kipuuzi, mimi nataka kuondoka...’nikamwambia.

‘Unaondoka? Wewe vipi bwana, kazi hatujamaliza, ...nafahamu sasa hivi atakuwa kazindukana, kinachotakiwa wewe ni kujifanya mwandishi wa habari....atakuja mbio mbio akijiona yupo kwenye hiyo hali,atapita wapi, nataka akitika huko alipo akukute upo hapo nje,...wewe kaa hapo nje mlengoni, akitokea anza kumpiga picha...’akasema na akaenda kwenye mkoba wake akatoa kamera ndogo.

‘Unaiona hii hapa..., ni kamera ya kisasa kabisa..., utakuwa nayo hapo nje, ....akijitokeza tu,...anza kazi yako, usitake nikufundishe kila kitu....hapo nitamzima makali yake ya kuleta vurugu,...wewe hakikisha unajitambulisha kama mwandishi wa habari...’akasema na mara akatoa kitambulisho cha kuning’iniza akanivalisha.

‘Unaona kitambulisho hicho ni geresha, hatakuwa na muda wa kukikagau kuwa ni halali..muda atakuwa kachanganyikiwa, nafahamu kabisa atakimbia...nitamsamehe avae nguo zake....’akasema

‘Mengine niachie mimi, ni lazima gari kesho nilipate, keshaingia kwenye anga zangu....’akainua ngumi juu kuashiria ushindi, mimi akilini mwangu nikawa najiuliza ana maana gani kusema kuwa ameshanilipa malipo ya kazi yangu, sikumuelewa....

Nilizindukana kwenye mawazo hayo, nilipoitwa na bosi...


*********

Jioni nilikutana na bosi, ...

‘Vipi mbona nakuona kama umechanganyikiwa, kuna nini tena, maana kila siku nakuona uanazidi kuwa kama sio yule mhasibu wa awali, niambie ukweli, kuna kitu gani kinakusumbua?’ akaniuliza bosi.

‘Mambo ya kawaida tu bosi ....’nikasema.

‘Ukiwa na tatizo, kama limekushinda, jaribu kumtafuta rafiki mwaminifu , mwambia, huenda uapata msaada, lakini hakikisha kuwa kweli huyo ni rafiki wa kweli, kwani wengine, wanachukulia matatizo yaw engine, kufadikia...’akasema bosi.

‘Mimi nipo tayari kukusaidia kimawazo kama unaniamini...’akasema

‘Nakuamini sana bosi kama kweli nina tatizo nitakuambia, kwa hivi saa,... najaribu kuyatatua mwenyewe...’nikasema.

‘Cha muhimu, angalia afya yako kwanza, ...kuwaza sana, ni ugonjwa, na madhara yake ni makubwa sana, kuliko hata hicho unachokiwazia,..fika sehemu uone kama kuna uwezekano wa kulitatua hilo jambo au la, kama haiwezekani, basi...na usibebe mzigo usiouweza, usijiingize kwenye mambo usiyoyafahamu, hasa yale yenye utata, achana na ushabiki, achana na ushindani, kujionyesha kuwa na mimi nimo au ni zaidi...’akasema bosi.

‘Mimi sitaki kukulazimisha sana kuniambia mambo yako, nataka tu tuendelee na kisa chetu...

‘Unakumbuka tulipoishia, wakati, nimefikia muda wa kujifungua, na nikamshauri mume wangu kuwa ni bora nikajifungulie kwetu, kuliko kujifungulia hapo. Mume wangu alionekana kutokukubaliana na ushauri wangu mwanzoni.

‘Mume wangu nimetoa ushauri huo kutokana na hali ya hapa nyumbani ilivyo, kiusalama, kama unavyoona, mimi sina mtu anayenijali, au kunisiliza, ....mama bado hanitambui, ananitambua kwenye kazi tu, ....je ikatokea nimeshikwa na uchungu,na wewe haupo, ni nani atanisaidia, ...?’ nikamuulza

‘Mama yupo, dada zangu wapo, watakusaidia, hawawezi kukuacha ukiwa kwenye hali hiyo, wao ni binadamu...’akasema

‘Unasema hivyo kwa vile hushindi hapa nyumbani, nikuambie ukweli, mama mpaka sasa hajaniweka moyoni, kuwa mimi ni mke wako,...mawifi zangu, ndio kabisa, wote wanatafuta kila mbinu niondoke hapa,... unafikiri nikishikwa na uchungu watahangaika kunisaidia?’ nikamuuliza

‘Hakuna mtu anayeweza kukuacha ukiwa katika hali kama hiyo, ....nina uhakika mama atakusaidia...’akasema mume wangu.

‘Hapana mimi hilo sikubaliani nalo, nataka nikajifungulie kwetu, mama yangu yupo atanisaidia....’nikasema

 Baada ya majadiliano marefu, mume wangu akakubali niende nikajifungulie kwetu, kazi ikawa jinsi ya kulifikisha hilo kwa familia yake, ambayo, walijifanya kuwa nawazarau, kwanini, niamue kwenda kwetu, wakati wao wapo, hata hivyo, shauri hilo likapita,nikafunga safari kwenda kwetu.

Mungu alinisaidia nilipofika kwetu, nikajafungua salama, mtoto wa kike, nilikaa kwetu hadi nikamaliza siku 40 ndipo mume wangu akaja kunichukua tukarudi huko ukweni, napaita ukweni, maana, ni sehemu ya familia ya mume wangu, sio sehemu yake ya kujitegemea, na nilipofika nilishangaa , safari hii walinipokea kwa furaha, na wakawa na hamu sana na mtoto.

Japokuwa lilikuwa jambo jema, lakini mimi kama binadamu nilijiuliza hayo mabadiliko yametokea wapi, huku nyuma kulitokea nini , hadi wafikie kunikubali, na kumfurahia huyo mtoto, nikahisi labda ni kwa vile alikuwa ni mtoto wa kike

Kwenye familia hiyo kulikuwa hakuna mtoto wa kike aliyezaliwa katika kipindi changu hicho, kwahiyo huyo alikuwa mtoto wa kwanza wa kike, katika wanawake waliokuwepo hapo wa umri wangu, nahisi ndio hivyo, kwahiyo wakaonyesha aina fulani ya upendo kwake, na mtoto wangu akawa anashinda kwa mama mkwe siku nzima na kipindi hicho kukawa hakuna taabu, na siku zikaenda. Nikamshukru mungu kwa hilo.

Siku moja kukatokea ugomvi baina ya wifi yangu na mume wangu sasa hapo kesi yote ikaniangukia mie na mama mkwe akaniita na kuniambia eti nimemroga mtoto wake na kuanzia leo nisikanyage kwao.

‘Mama mbona mimi sielewi mambo hayo, ...nitamlogaji mtoto wako?’ nikamuuliza nikiwa hata sielewi, huko kuloga unaloga vipi, huwa nasikia tu, uchawi, lakini sijaujua jinsi unavyofanya kazi.

‘Unafikiri mimi ni mjinga, katika umri wangu huu, nafahamu mengi, mtoto wangu hakuwa vipi, nilikuwa nikimshauri kitu ananisikia, ...ulipokutana naye tu, akabadilika, ..angalia jinsi alivyo, utafikiri zezeta fulani, ...hanisikii kabisa, anakusikiliza wewe....’akasema mama mkwe.

‘Mama nakuapia kwa mungu, mimi mambo hayo siyajui, na mtoto wako sikumtaka mimi, yote hayo ni mapenzi ya mungu kapanga tu tuwe naye, lakini kiukweli, yeye andiye aliyekuja kwetu kunioa, na sikuwa namfahamu kabla...’nikajitetea.

‘Huniambii kitu hapa, kuanzia leo sikutaki hapa nyumbani kwangu, hapa hapakai wachawi, nimemwambia mume wako, kama anakung’ang’ania kwa vile haelewi kitu, kwa jinni ulivyo mtengeneza basi atafute sehemu nyingine ya kuishi...’akasema mama.

‘Mama sasa sisi tutakwenda wapi,..unajua hali yetu ilivyo, mume wangu hana nyumba, hana uwezo huo kwa sasa...’nikasema.

‘Hilo mtajijua wenyewe, ulipokwenda kwenu kuutafuta huo uchawi, ulituambia...sasa hiyo ni amri, uondoke kabisa hapa,..sitaki hata kukuona, mchawi mkubwa wewe..’akasema kwa hasira, na alionyesha kweli, anahisi hivyo,..

Niliumia sana, maana tangu nizaliwe sijawahi kuamini hayo mambo, na hata wazazi wangu wapo mbali kabisa na mambo hayo, leo hii nasingiziwa uchawi, na kuambiwa nimeenda kwetu kuchukua huo uchawi, ina maana familia yetu ni wachawi....sikuweza kuvumilia shutuma hiyo,...nikasema mume wangu akija ni lazima nimwambie, aamua moja wazazi wake au mimi.....

NB: Nakabiliwa na mitihani mbali mbali ya kimaisha, ikiwemo tatizo la mtandao, mtandao kwangu umekuwa mgumu kupatiana, ni tatizo...ndio maana ile spidi ya awali inapungua..hata hivyo nitajitahidi tuwe pamoja.


WAZO LA LEO: Uzushi, fitina, imani za kishirikina na uwongo, ni adui mkubwa wa amani katika jamii. Mambo haya yakizoeleka, amani, huyumba, watu watachukiana, na kuwekeana visasi, ndio maana wanasema fitina ni mbaya hata kuliko uchawi.
 

Ni mimi: emu-three

1 comment :

Anonymous said...

Huyu mkaka ananiudhi kweli yaan jail ile inamwita