Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Tuesday, January 7, 2014

Mkuki ni kwa Nguruwe-59



Niliwasiliana na mdogo wa mume wa familia, na akaniambia keshapewa ufungua na kaka yake na yupo njiani kwenda kuichukua hiyo silaha, kilichofanyika ni kutafuta mbinu za kumtoa mke wa familia eneo la nyumbani kwake na hiyo ilikuwa ni kazi rahisi tu, kwani mke wa familia hakuwa anafahamu ni nini kinaendelea kwahiyo hakuwa na wasiwasi wowote, ukumbuke wakati huo, mume wa familia bado yupo hospitalini anaigiza kuumwa.

Kilichofanyika ni mume wa familia kuigiza kuzidiwa, na wakati huo akawa anataka kuongea na mkewe, kwahiyo docta ikabidi ampigie mke wa familia simu kutoka hospitalini kuwa mume wa familia,kazidiwa ghafla, na anataak kuongea na y eye.  Ni kawaida kwa mwanandoa akisikia mwenzake kazidiwa, hutalala, utahitaji kuja kumuona, na ndivyo ilivyotokea, mke wa familia akaenda kumuona mume wake, na alipofika huko ikatafutwa njia ya kumchelewesha hadi mdogo wa mume wa familia aliweza kuichukua hiyo silaha.
Ilipoletwa .

Kwa upande wangu mimi nilishajiandaa, nilishaweka kamba ndefu, inayofika chini, ujue lile jengo lina rosheni,lakini kwa ajili ya kuiingiza hiyo silaha ndani, nilitumia rosheni ya pili, na jinsi ya kuifikisha kwenye chumba changu, nilitumia njia zangu nyingine, cha muhimu ilikuwa kuhakikisha kuwa mitambo ya kutizama matukio ilikuwa imezimwa, ..nilifanya hivyo nikiwa na uhakika kuwa mtoto wa Makabrasha hayupo.

Nikaichukua ile silaha na kuificha chumbani kwangu, kwani haikutakiwa kuwa mbali na mimi ili nikiihitaji nisipate taabu, nilihakikisha kuwa hayo yote niliyafanya kwa ujanja wa hali ya juu, kiasi kwamba , hata kama watakuwa wakinichunguza nyendo zangu kwenye mitandao yao wasifahamu kuwa nina kitu kama hicho halafu nikatoka kwenda kuendelea na shughuli zangu, wakati natoka, nikakutana na mtoto wa Makabrasha.

‘Mbona sipati ishara ya mawasiliano kutoka hapa, ni nani kazima mitambo ya usalama wa jengo ?’ akaniuliza akionyesha wasiwasi

‘Mitambo ya usalama wa jengo, ipo wapi hiyo...aah, mimi sijui mambo yenu na wala sijui kama imezimwa, na kwanini izimwe!?’ nikamuuliza kwa mshangao, na yeye akaniangalia kwa mashaka, halafu  akageuka  kuelekea kwenye chumba cha mitambo hiyo ilipo na mimi nikamfuatilia kwa nyuma kiujanja, hakujua kuwa nipo nyuma yake, mawazo yake yalikuwa kwenye hilo jambo analilifuatilia.

Akafika na kufungua mlango, akaingia ndani, na mimi kwa haraka nikaingia, chumba kilikuwa giza, ila kwa mngurumo wa hiyo mitambo, na kulikuwa baridi sana....hakugeuka nyuma, akawasha sehemu ambayo mimi nilizima, halafu akasogea kwenye meza yenye komputa, akaiwasha na kukagua kitu, akawa anaangalia ni nani aliyekaribia hicho chumba,  ni wazi kuwa ningelionekana mimi, sikuwa nafahamu jinsi gani ya kufuta matukio ya nyuma yake, akaiweka ile komputa sawa na kugeuka kuondoka, na ndio akaniona nimesimama nyuma yake. Akashituka na kuniangalia akiwa kakunja uso.

‘Oh, wewe mtu, unakuwa kama mzimu, yaani ulikuwa ukinifuatilia nyuma, huku nilishawaambia hatakiwi watu kuingia huku, niambie umefuata nini, na inaonyesha wewe ndiye uliyefika huku, ...?’akasema kwa hasira.

‘Baba yako alinituma kufanya usafi...kwani kuna wagen muhimu alitarajia kuwa watakuja kumtembelea...’nikasema lakini nilifahamu kabisa kuwa kama ni usafi, huwa eneo hilo sijawahi kufika kufanya usafi na, yeye akasema;

‘Hata kama ni usafi, toka lini ukaja kufanya usafi eneo hili, wakati mimi sipo, haiwezekani, na hata kama ulifanya usafi kwanini ukazima mtambo mkubwa, ?’ akaniuliza kwa mashaka.

‘Niliona kuwa eneo hili ni chafu, ndio nikaja kulifanyia usafi, ...na sijui kama nilizima, ndio kuna wakati nadeki, nikaona nisije nikarushwa mimi nikazima, nikijua kuwa ni swichi ya umeme, ....mimi mambo yenu hayo siyajui’nikasema

‘Ni nani alikupa ufungua wa chumba hiki?’ akaniuliza

‘Unauliza jibu, ninapotaka kufanya usafi, nilishawahi kuja kwako kukuuliza ufunguo, mimi ninafahamu wapi funguo zote zipo, kwanini unaniuliza maswali mengi, mbona siku nyingine hujawahi kuniuliza, kwani ni mara ya kwanza kuja kufanya usafi hapa, na kwanini huendi kumuuliza baba yako, kama una wasiwasi na mimi, mbona unaniwekea vikwazao visivyo na msingi..mzee wako ananiamini ndio maana kaniajiri niwe karibu naye.’nikamwambia.

‘Leo iwe ni mwisho kuingia kwenye chumba hiki, tatizo ni kuwa umezima mtambio mkubwa ambao unafanya tusiwe na mawasiliano tukiwa nje, na hili nahisi umelifanya makusudi....’akaniambia na mimi nikatabasamu kumlegezea, nilishafahamu uzaifu wao, mtoto kama baba, akategeka, na kunisogelea, huku akisema;

‘Tatizo lako wewe kwasababu ya tabia yako unahisi kila mtu ni kama wewe....’nikasema huku nikijerembua. Wakati mwingine ukiwa katika kazi kama yangu inabidi utumie kila mbinu, lakini akili kichwani mwako. Na alipoliona lile jicho, mtoto kama baba, akasawajika, nikamuona mate yakimtoka, akasahahu alichokuwa akiniuliza mara akasema;

‘Kwanza nikulize  lile ombi langu vipi,..?’ akanisogelea baada ya kuzima kitu kwenye mitambi, sikujua ni kwanini, na akanisogelea kujaribu kunishika na mimi nikasogea pembeni na kusema;

‘Ombi lako lipi, ooh, na wewe bwana, kwanini unakuwa na tabia mbaya, nilishakuambia upuuzi kama huo, siutaki, msinione nipo humu ndani mkafikiria mimi ni Malaya, kwanza kuhusu huo upuuzi wako nitamuuliza baba yako...kama yupo tayari kuchangia na mtoto wake...haya,’nikasema na yeye akageuka kuondoka, na kusema;

‘Hivi wewe baba unamuona mtu wa maana kwako, ombi langu kwako ni siri yangu mimi na wewe, eti ukamuulize baba, unataka nilaaniwe nini....wewe jivunge tu, ipo siku utaingia kwenye anga zangu, unafikiri mzee yule atakuwa na wewe milele, akikuchoka anakutupa chini, wangapi walikuwa naye sasa hawatakiw hata kumsogelea, ...wewe jidanganye kwake, ukifikiria umefika....’akasema.

‘Kama alivyofanywa mama yako au sio, hata hivyo  mimi sijawahi kukuambia kuwa nina haja na baba yako, ...baba yako ndiye kanilazimsiha kuja kwa ajili ya mambo yake, mimi nina mume wangu, nina maisha yangu mazuri tu, na mume wangu nampenda, kama isingelikuwa haya mambo yenu unafikiri ningelikuwa hapa, na ipo siku mtajuta kwa hayo mnayoyafanyia....’nikamwambia.

‘Hayo unayafanyiwa ni yenu na baba, mimi siyajui, ...na vitisho vyako, kwangu havina nafasi, nafahamu ni nini ninachokifanya kwa nafasi gani, usinitishe kabisa, mimi ninafahamu sheria, na sijawahi kukulazimisha kwa lolote lile, na hata hivyo ombi langu lipo pale pale, usiponinitimizia najua jinsi gani ya kukupata...’akaniambia

‘Utafanya nini...?’ nikamuuliza

‘Siri zako zote anazozitumia baba kwa ajili ya kukupata wewe ninazo mimi, zipo kwenye mtandao, yeye akizihitajia mpaka aingie kwenye mtandao, na mimi ndiye nimezihifadhi, sasa utanidanganay nini, nikiamua kuzitumia dhidi yako, siutaumbuka wewe...sasa uamue moja kuwa na mimi au na baba..’akasema.

‘Nakuambia hivi ni bora umenifahamisha hayo, nitamuambia baba yako hizo mbinu zako, kama atasema yupo tayari kuchangia na mtoto wake, mimi sina hiana, mimi hapa ni mtumwa wake....’nikamwambia.

‘Hivi wewe una akili kweli,...kila kitu utamwambia baba, ole wako umwambie....’akasema

‘Sasa tuelewane, ili nisimwambia unifundishe jinsi gani ya kutumia huo mtandao, jinsi ya kutengeneza picha na kuziweka kwenye huo mtandao..’nikamwambia.

‘Unataka nikifundishe ili uje uzifute, ..hilo umenoa..lakini naweza kukufundisha kama utanikubalia maombi yangu...kama upo tayari, tuonane usiku wa leo, nitakuja, nitakufundisha lakini malipo yake ni ...maombi yangu...na safari hii sikubali, kama ulivyonidanganya siku ile, nikija ..nikakufundisha, ni lazima utimize maombi yangu, la sivyo, na mimi nitaweza kukufanyia kitu ambacho hutaweza kunisahau....ujue na mimi ni wakili kama baba’akasema na mimi sikumjibu, nikaondoka, huku moyoni nikiwa nimeshajiweka katika nafasi nzuri.

Yeye akarudi kwenye mtandao, na kuwasha kitu alichokuwa amekizima awali, na akawa anafuta matukio yasiyo muhimu,...nikawa namwangalia, wakati huo alikuwa hanijali tena, alipomaliza akanigeukia na kuniuliza ninasubiri nini

‘Nakusubiri wewe bosi kama kuna kazi ya kufanya, ...’nikasema

‘Ishia huko kaendelee na kazi zako, tutaonana baadaye ...’akasema na kuondoka.

 Mimi nina akili za ajabu sana, ukinionyesha kitu, au nikaona unavyofanya, akili yangu hunasa haraka sana, nilishaona jisni anavyoweka neno lake la siri, nikalinasa bila ya hata ya yeye kujua, nilijifanya sijui lolote kuhusu kmputa na mitandao, na neno hilo la siri nililigundua siku moja wakati anahangaika kunibembeleza nimkubalia matakwa yake...hapo hapo nikatumia ujanja kumuomba anifundishe jinsi jengo hilo lilivyo, maana ni jengo kubwa, na ndio siku hiyo nikagundua kuwa kumbe jengo hilo lina sehemu ya chini ya ardhi, ...

Usiku wake, nilitaka niingie kwenye hiyo mitambo, kwani ndio siku peke yake ningeliweza kufanya jambo, nilichofanya ni kuchelewesha kununua mafuta ya genetaror, nilijua mara kwa mra umeme unakatika, na mimi ndiye niliyekuwa nahifadhi fedha za matumizi madogo madogo ya ofisi, na nilitakiwa kuhakikisha mafuta ya genetor yapo,

Nilijua ikifika saa tatu, mafuta yatakuwa yamekwisha, na siku hiyo umeme ulikuwa hakuna, huku nikiomba huyo mtoto wa huyo  jamaa hafiki, au anachelewa, nilishangaa kweli siku hiyo kwani mpaka saa tatu alikuwa hajafika,....mara genetaror likazima, kukawa kizaa, zaa, giza, nilijua kwa jinsi ili mitambo ilivyo ikifika nusu saa itakuwa imezima, hapo nikajichelewesha kufuatilia, hadi nusu saa ikapita, ndio nikajitokeza

‘Mbona generator limezima, hujanunua mafuta..’akaniuliza Makabrasha

‘Naona nimepitiwa mambo yamekuwa mengi, ...nimemtuma mlinzi akanunue...’nikasema

‘Huo ni uzembe, unafahamu umuhimu wa umeme kwenye hikli jengo, huoni watu wabaya wanaweza kutumia mwanya huu kufanya lolote...’akasema na mimi nikaachana naye na kukimbilia kwenye hicho chumba. Kama nilivyojua, sehemu ile ya kuangalia matukio ya jengo ilikuwa imeshazima, kwa haraka nikakimbilia kwenye ile komputa inayohifadhi matukio  na kumbukumbu mbali mbali, ilikuwa bado inafanya kazi, nikaingia sehemu ninayoitaka

Ilichukua muda kidogo kupata kumbukumbu ninazozitaka, ....nilikuta kumbukumbu nyingi za watu mbali mbali, ambazo kama zingeliwekwa hewani, nafikiri watu wengi wangeliumbuka, sikutaka kuangalia zaidi, kwani mambo niliyoyaona humo yanatisha,mimi nikazifutilia mbali, na kuhakikisha hazipo kwenye sehemu ya mabaki ya vitu vilivyofutwa, nikaangalia sehemu inayoangalia matukio ya jengo hadi umeme ulipozimika, nikazifuta.

Nikaenda sehemu wanapohifadhia picha za video  ambazo zilikuwa zinaonyesha mtu aliyefika kwenye hicho chumba karibu, nikajiona ni mimi peke yangu nikaifuta hiyo kumbukumbu, halafu nikatafuta sehemu ya kuzuia kamera za humo ndani zisichukue matukio hadi itakapokubaliwa tena ,nikaiweka OFF,  ina maana kuanzia hapo hadi hapo mtu mwingine atakapokuja kuikubali kuonyesha matukio, kutakuwa hakuna kitu kitakachoonyeshwa, nilipoamaliza nikatoka kwa haraka, na wakati natoka tu, genetaror likaanza kunguruma na umeme ukarudi.

‘Ulikuwa wapi wewe nakutafuta sehemu zote,..naona mitambo ya usalama humu ndani imezima, sio kawaida, hata umeme ukizimika inaweza kuhimili hata saa nzima, ..kuna tatizo,....’akasema Makabrasha huku akielekea kwenye chumba cha usalama, lakini baadaye akatoka huku akiongea peke yake.

‘Naona kuna tatizo kwenye mitambo ya usalama, ..siwezi kuingia kwenye komputa ya usalama, sijui huyu mtoto kafanya kitu gani,..kabadilisha neno la siri...’akawa anaongea huku akinipita na mimi nikamwambia.

‘Mimi sijui, lakini tunaweza kujaribu pamoja huenda tukagundua jinsi gani ya kuingia, tukiwa wawili?’ nikamuuliza

‘Hio haikuhusu, ngoja nimpigie simu huyu mwanangu, japokuwa tumekorofishana, lakini hili ni muhimu, ni lazima afike, nahisi kuna tatizo , nahisi ....akili inaniashiria kuna tatizo,..toka jana  nilipoanza kukorofishana na huyu kijana, nimehisi kuna kitu ambachp sio cha kawaida, jana kaondoka kwa mihasira, na ndio maana hajafika mpaka muda huu..’akasema

‘Mumekorofishana nini tena na mtoto wako kipenzi?’ nikamuuliza

‘Unafahamu hawa vijana  wana tamaa sana, wao wakiona kitu kipo, hawajiulizi kimefika fikaje hadi hatua hiyo, hawafahamu kuwa sisi wazazi wao tumetumia miaka mingi kujenga hicho walichokikuta, wao wanataka kupata kwa muda mfupi,...hata kama ni ujenzi ukiutaka uumalize kwe muda mfupi, utakuwa hauna imara,..inahiatji muda,...tatizo kubwa yeye hajui mipangilio yangu ipoje...’akasema akiwa kasimama karibu yangu.

‘Kwani yeye anataka nini?’ nikamuuliza na akataka kuondoka, lakini akageuka na kuniangalia, akasema;

‘Huyu kijana analalamika, kwanini mwanangu huyu anayeishi huko nje, ninamjali eti kuliko yeye, na kumfanya mrithi wa kwanza, kama mktaba unavyosema, eti yeye anaona hilo sio sahihi, anataka mimi nikifa yeye ndiye ashikilie nafasi yangu, awe ndiye kiongozi wa familia, sio huyo kaka yao aliyepo nje, huyu ana akili kweli, hajui yule ana haki zote kuliko yeye, ...’akasema

‘Lakini hata ingelikuwa mimi ningdai hivyo hivyo, kwasababu huyo kaka yao yupo nje, hajui chochote kinachoendelea hapa, na nakumbuka uliwahi kuniambia huyo mtoto wako wa Ulaya hampatani, na aliondoka na kukuambia hana haja na mali yako ..sasa kwanini unajipendekeza kwake....?’ nikamuuliza

‘Wewe hujui mambo ya wazazi na watoto, hata kama mtoto hampatani kwasababu kadhaa, lakini yeye atabakia kuwa mtoto wangu wa kwanza, na yeye nilimzaa na mke wangu wa ndoa, ana haki zote. Huyu niliye naye hapa nimemzaa kwenye nyumba ndogo,..nilimsomesha na kumuandikisha kama watoto wangu wengine, na nimeona anastahili kuwa karibu na mimi,  na ndio maana nimemuweka nafasi ya pili, atakuwa chini ya huyo kaka yao anayeishi huko Ulaya, kuna tatizo gani hapo....’akasema.

‘Kwahiyo wewe na mtoto wako mkaishia wapi?’nikamuuliza

‘Yeye alikuja na mipango yake, uone jinsi mtoto huyu alivyo balaa, kakaa sijui na mama yake, wakapanga mambo mengi tu, jinsi ya kugawanya mali  eti keshaandaa na mikataba ya kifamilia, kama vile mimi ninakufa karibuni, kwenye mikatba hiyo, ambayo ni kama urithi, , ...na yeye awe ni mrithi wangu , yaani kiongozi wa familia, mimi nikifa...hana akili kabisa, nimemwambia huo uchuro siutaki, kama ni mikataba ya urithi, mimi nimeshaupanga na ninafahamu ni nani awe kiongozi wa familia, kama mimi nikifa..lakini sijafa, na sitaraji kufa leo...siumwi,, sina tatizo la kiafya..kwanini anakuja na mipango hiyo, wana matatizo sana hawa watu....’akasema akijiangalia.

‘Lakini  kufa sio lazima uumwe, wewe kama ulivyo, kutokana na mambo yako unayoyafanya,una maadui kila kona, wakija kuku-ua, watu,....’nikasema

‘Kweli hilo ni la kuangalia sana, ndio maana umeme ulipozimika, nimeshituka sana, sitaki uzembe huu utokee tena, ...unanisikia, ....sasa nisikilize kwa makini, kesh o huyu mpenzi wako anakuja, ...’akasema

‘Mpenzi wangu gani, mimi ni mke wa mtu.?’ Nikamuuliza

‘Hebu acha utoto, nikisema mpenzi unanielewa ni nani, ..nimeshamweka sawa anakuja kuweka sahihi yake kwenye hiyo mikataba ambayo itanifanya mimi, niwe na haki ya kumiliki, hisa kwenye makampuni yao, kilaini kabisa....kwahiyo wewe na wenzako mlitambue hilo, ...na tatizo ni huyu mtoto wangu anakuja na sera zake za ajabu ajabu, anataka na yeye awe na hisa,...anataka kunikorofisha,...’akasema kwa hasira

‘Mimi ninawashangaa kweli kweli, yaani mumeshaanza kugombea mali za watu, hata kabla hamjazipata, mumeshaanza kumiliki hata kabla humajamilikishwa, kweli akili zenu wote ni za  kishetani wewe na mtoto wako,  na mimi nahisi hamtafanikiwa kwa hilo, na mkifanikiwa mtakuja kupigana baba na mtoto wake....’nikasema

‘Kama mimi nipo hai, hakuna cha mtoto wala mama yao atakyeweza kunitawala, mimi ndiye mwenye amri, wote wanalifahamu hilo, najua kabisa huyo mtoto anaendeshwa na mama yake, na mama yake nilishamwambia simtambui tena, tulishamalizana na yeye zamani, hana nafasi kwangu tena...hatukuwahi kufunga ndoa na yeye, alikuwa mpenzi wangu wa kupita tu, nikampa mimba ndio akapatikana huyo kichaa.’akasema kwa  hasira.

‘Aaah, kumbe, una wangapi, huyo alikuwa mpenzi wako wa zamani, nahisi wapo wengi wa namna hiyo, huyo wakati huo ulimuona mpenzi, sasa hafai, au ni kwa vile kazeeka,au?’nikamuuliza

‘Namfahamu sana huyo mwanamke, ana tamaa sana, hatuivani kabisa, na mtoto wake kachukua tabia zake zote, na kama ataendelea na hiyo tabia sizani kama tutaivana, na...namuona atakuwa  kikwazo katika mipangilio yangu ya kimaisha kinyume na nilivyotarajia...’ akatikisa kichwa kusikitika halafu akaendelea kusema;

‘Sijui kwanini hanisikilizi mimi, na anakuwa akimsikiliza sana mama yake, ujue huyu mtoto mimi ndiye nimefundisha ujanja wa kimaisha , alipomaliza kisomo chake akataka kufanya kama alivyosoma, nikamwambia dunia hii, ina utaratibu, lakini ndani ya hizo taratibu kuna njia za mikato, uking’ang’ania, njia hiyo hiyo, utasubiri wee, na hutaweza kufika kwa wakati muafaka, wakati mwingine, unakatisha njia,...nikamfunza jinsi gani ya kuitumia elimu yake kutafuta maendeleo mpaka akaiva, sasa namuona ananipanda kichwani...’akasema huku akikunja uso kwa hasira.

‘Kwahiyo sasa mtoto kama baba yake...au kama wanavyosema  mtoto wa nyoka ni nyoka’nikasema kwa dharau huku nikijifanya kutabasamu .

‘Huyo haniwezi kabisa na hataweza kunifikia mimi, yeye anachukulia mambo kwa pupa, mimi natumia ujanja, hekima na akili, ndio maana unaona nimefanikiwa kwa kiasi hiki kikubwa, unaona jumba hili, ni nani anaweza kujua nimelijnga vipi,..ni akili, ..usione watu wana majumba, utajiri, ukfikiria ni kirahisi hivyo, ni kutumia akili, ujanja...ndio hivyo, wewe zubaa tu,...’akashika kichwa kwa kidole chake huku akiangalia juu, kama vile anaangalia hilo jengo.

‘Kwahiyo yote hayo umemfundisha mtoto wako?’ nikamuuliza

‘Tatizo yeye hataki kutliza kichwa, yeye anataka mambo kwa pupa, ana tamaa za haraka, hata sijui kwanini ameweza kufaulu masom o yake ya uanasheria, kazi hii hataiweza kama atakuwa na tabia ya namna hiyo, ya pupa, na ninavyomuona hatafika mbali, hebu angalia, anataka kunirithi nikiwa hai...sijui kwa hali kama hiyo, tunaweza kukaa pamoja,....lakini mimi kama baba, nitamdhibiti tu, ninamfahamu vyema na wapi pa kumnasa, hana ujanja mbele yangu, hanijui akili zangu zilivyo...’akasema.

Na mara simu yake ikalia, akaipokea bila kuiangalia, na mara akakunja sura ya uso wake na kuonekana kukasirika, akasema kwa sauti ya iliyojaa hasira;

‘Kwanini unasema hutafika leo, wakati unafahamu umuhimu wa wewe kuwepo leo, nataka uje hapa haraka,...kwanza kuna matatizo kwenye mitambo ya usalama, na pia ni wajibu wako kuwepo hapa, ili tukamilishe kazi , achana na tamaa zako hizo, nasema mimi kama baba uje hapa haraka,.....’akasema

‘Unasema nini, unanijibu mimi hivyo, kuwa hutafika,mpaka nikubaliane na matakwa yako, ina maana unanilazimisha kufanya unavyotaka wewe, hivi unaelewa unaongea na nani...unasema nini, ina maana umeshaota mapembe sasa eeh,...’akawa anaongea huku mwenzako huko anaongea, na mwisho akasema;

‘Sikiliza wewe mtoto, kama nimekuzaa mimi, utakuja hapa, kama una baba yako mwingine usije , usijione kuwa umekuwa sasa,...na kujiona hunihitaji tena,  hujui ninaweza kukufanya lolote ukasahaulika katika hii dunia..’akasema na kusikiliza simu kwa muda halafu akaibamiza simu chini , na simu hiyo ikapasuka vipande vipande, na kusema;

‘Mwanaharamu mkubwa wewe...tutaona,....’akageuka na kuelekea ofisini kwake, ukumbuke hapo tulikuwa tunaongea kwenye varanda, na mimi nikachekelea kimoyo moyo, na kurudi chumbani kwangu, sikutaka kumfuata ofisini kwake, kwani nilijua kwa hali aliyonayo hatutaweza kusikilizana.

Mimi kwa hali kama hiyo , ilikuwa kama vita vya kunguru, faraja kwangu, kmoyomoyo nikijua sasa sehemu muhimu imekamilika, japokuwa sikuwa nimeamini kabia kuwa huyo mtoto wa marehemu hatafika, namfahamu sana, yeye na baba yake hawaeleweki, wao ni waarabu wa pemba, wanajua sana, kwahiyo nikachukua tahadhari,..

Nilikwenda kuongea na mlinzi mmoja ninayemuamini , nikamwambia , kama huyo mtoto wa bosi akija , anipigie simu kwa haraka,...kwani sehemu kubwa ya mitambo ya kunasa matukio ilikuwa haichukui picha, kwahiyo ningeliweza kufanya lolote bila kujulikana, kwa kiasi fulani nilikuwa na amani kidogo, nikasuburia muda muafaka, wa kumalizia kazi ambayo nilishaianza.

Nilikuwa najiamini maana sasa nina silaha, na nikiwa tayari , au nikisikia kuwa huyo jamaa kafika nitakwenda kuichukua, sikuwa na haraka nayo sana, nikatembea kuelekea  ofisi ya siri ya Makabrasha, nikafungua, na kulitafuta kabati maalumu anapoweka nyaraka zake, nikachukua kile ninachokihitajia, na kurudi chumbani kwangu.

Kabla sijafika huko nikakumbuka kazi nyingine ya kufanya, kwani siku hiyo niliipanga iwe siku ya mwisho ya kukaa kwenye hilo jengo, nikaelekea sehemu ninapoweka vitu vyangu muhimu ambavyo nimevihifadhi mbali na chumba changu, sikutaka waje wavikute chumbani kwangu, kama ikitokea kuvitafuta, nikaviweka sawa, halafu nikarudi chumbani kwangu,sasa nikijiandaa kwenda kuichukua silaha yangu, sikutaka iwe mbali na mimi na wakati nafika chumbani kwangu, simu yangu ikaita, alikuwa mtoto wa Makabrasha,

‘Unasemaje?’ nikamuuliza kwa sauti isiyotaka kuongea,

‘Samahani sitaweza kufika kwenye shule niliyokuahidi, lakini ombi langu lipo palepale,na kwanini mitambo hapo haifanyi kazi,  ...umeingia tena humo ndani?’akasema na kuniuliza

‘Umesema hutakuja, ina maana mkataba huo umekufa, labda useme kuna jingine..na kuhusu swala la mitambo hayo unayafahamu wewe, wewe ndio mtaalamu, huenda ulifanya hivyo makusdi kumuonyesha baba yako kuwa wewe ni zaidi au..?’nikasema kama namuuliza

‘Wewe nimeshakufahamu, wewe unajifanya ni mjanja, lakini ujue kuna wajanja zaidi yako, kuna kazi naifanya ikimalizika nitaangalia, kama nitakuja au la, ..lakini kwa vile hatujaafikia na mzee ninaweza nisifike, na kama nikifika, nitahitaji maelezo ya kina kwanini umezima mitambo, na kwasasa siwezi kuona chochote kinachoendelea hapo, utakuwa ni wewe tu...na hilo litakufanya utimize ombo langu, la sivyo, ...’akasema

‘Una uhakika gani na hilo?’ nikamuuliza

‘Utaona....mimi huwa sichezewi, mimi ni mtaalamu, nafahamu sana hiyo mitambo, na kawaida yangu, nikitaka jambo ni lazima nilipate, muulize baba atakuambia, ndio maana nipo naye karibu, ananifahamu sana, lakini naona kama kanisahau kwenye mikataba yake, nitamkumbusha hilo, na ,..’akasema lakini akawa kama anakatiza, inaonekana alikuwa akiongeleshwa na mtu mwingine, aliyekuwa karibu naye, nahisi atakuwa ni mama yake au kuna mwanamke yupo naye. Mimi nikacheka na kusema;

‘Hahaha..mtoto kama baba, mnagombea mali ya dhuluma eeh, nina uhakika kuwa dhuluma hiyo itawapeleka pabaya...na mwisho wake umeshafika, ..wewe njoo nakusubiri kwa hamu, kwanza baba yako ameshakushitukia, ....’nikasema na nikasikia akikata simu kwa hasira huku akisonya.

NB: Je huyo jamaa alifika?  na kama alifika kulitokea nini na je ombi lake lilitimizwa,ni nini kitatokea kwa Makarasha, tuonane kwenye sehemu ijayo ya hitimisho la kisa hiki.


WAZO LA LEO:Tuwe makini na malezi ya watoto wetu, kama tunafanya shughuli zisizo na manufaa kwa watoto wetu kwa maisha yao ya badaye, ni bora tusiwahusishe. Tuwajengee watoto wetu misingi mema ya maisha yao ya baadaye, tukikwepa makosa tuliyoyafanya, ili wao waweze kuishi maisha bora, na kujenga kizazi bora cha baadaye.

Ni mimi: emu-three

No comments :