Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Wednesday, November 20, 2013

Mkuki ni kwa Nguruwe-32


Kwa vile kila mmoja alikuwa na kampuni yake, na utokana na taratibu zetu za kikazi,  hata nyumbani kulikuwa na baadhi ya vitu, ambavyo kila mmoja aliweka mahali pake, ili kusitokee mkanganyiko, na hata kwenye maktaba yetu, kulikuwa na makabati mawili , moja la kwangu na jingine ni la mume wangu.

Hakuna aliyekuwa akihangaika na kabati la mwenzake, labda uamua kumtuma mwenzako, kuwa nisaidie kunichukulia kitu fulani, na kwa vile humo tulikuwa tukiweza vile vitu muhimu, ambavyo havitakiwi kupotea, ilibidi kila mmoja awe na funguo zake, kwahiyo, hakuna liyekuwa akihangaika na kabati la mwenzake.

Kupotea kwa mkataba wangu, ambao niliuweka kwenye kabati langu, na mimi mwenyewe ndiye mwenye ufungua, kuliniweka kwenye njia panda, sikutaka hata siku moja kumshuku mume wangu kwa baya lolote, moyoni nilikuwa namuamini sana, na hii imekuwa ni tabia yangu, kuwa ukiwa kwenye nafasi yakuitwa rafiki yangu, basi huwa ninakuamini moja kwa moja, ....sasa mkataba wangu umepotea, na mtu ambaye anayeweza kuuchukua ni mume wangu, swali lilikuja kwa kutumia ufungua gani, na mimi ufungua za kabati langu ninao mimi mwenyewe.

Leo hii ninafika nyumbani ninamkuta mume wangu akiwa kwenye kabati langu, likiwa limefunguliwa, sikuamini, nina uhakika ufungua wangu ninao, upo kwenye mkoba wangu, kwa muda huo sikutaka kuhakikisha, ila nilisogea taratibu hadi pale alipochuchumaa mume wangu, na hakuonekana kushituka, ina maana akili yote ilikuwa kwenye hicho kitu alichokuwa akikitafuta, na alikuwa katoa vitu vyangu vingi na kuvisambaza sakafuni, kitu ambacho hakikunifurahisha, huwa nathamini sana hivyo vitu vyangu na kuvitunza katika usafi wa hali ya juu, leo vimesambazwa sakafuni.

‘Unafanya nini kwenye kabati langu...’nikamshitua...

Endelea na kisa chetu..............

Mume wangu aliposikia sauti yangu, alishituka, hadi ile karatasi aliyokuwa kashika mkononi ikamdondoka, kwanza alitulia na baadaye akajifanya kutokujali, na kuikota ile karatasi, halafu akainua kichwa chake na kuniangalia usoni, akasema;

‘Afadhali mke wangu umekuja, maana hapa akili yote imevurugika, nimetafuta pale nilipokuwa nimeweka ule mkataba, wangu wa zamani, nakala ya zamani, kwenye kabati langu, sijauona, sasa nikafikiria huenda upo hapa kwako...’akasema.

‘Hujanijibu swali langu, unafanya nini kwenye kabati langu, toka lini tukawa tunachangiana makabati, kila mmoja ana kabati lake na kila mmoja ana vitu vyake na humu naweka vitu vynagu vya kikazi, angalia jinsi gani ulivyoviweka ovyo sakafuni, ...huoni kuwa unataka kuniweka mimi mahala pabaya..vikiharibika, vikipotea, huoni....’nikasema.

‘Usijali mke wangu hakitaharibika kitu hapa, niamini mimi, mimi ni mume wako, nitahakikisha hakiharbiki kitu hapa, hata hivyo, akili yangu inanasa kila kitu ninachokifanya, yaani siku hizi mke wangu naona ajabu sana, nina akili ya ajabu sana, nitakirudisha kila kitu mahali pake...sisahau hata kidogo...’akasema.

‘Unatafuta nini kwenye kabati langu?’ nikamuuliza kwa hasira.

‘Mkataba...ulisema unahitaji ile nakala yangu ya zamani,  pale nilipokuwa nimeiweka, kule  kwenye kabati langu, siioni, siku hizi akili yangu inanituma mambo mengi, na nikiweka kitu sisahau pale nilipokiweka, sasa siuoni, imekuwaje tena...nilifikiria huenda umeuchukua wewe...au umeuchukuwa wewe nini, huenda umeuchukua, na kuuweka sehemu nyingine?’ akaniuliza huku akiendelea kupekua kwenye mafaili yangu.

‘Sikiliza mume wangu, ..sijapendezewa kabisa na hiki ulichokifanya, ..na sio tabia yako, imekuwaje ...kuna nini unanitafuta?’ nikamuuliza huku nikiendelea kumwangalia.

‘Kwa vipi mke wangu, mimi ni mume wangu, ina maana sina haki ya kuangalia kwenye vitu vyako, ...mke wangu, tuaminiane, mimi kama mume wako nina haki ya kuangalia chochote kwenye mali zetu, ...au nimekosea?’ akaniuliza na safari hii alianza kurudisha vitu kwenye kabati, nikawa namwangalia tu.

Hutaamini baada ya dakika moja, alikuwa karudisha kila kitu kama kilivyokuwa...na akachukua ufungua akafunga , nikagundua ule ufungua aliotumia ni wa kuchongesha, aaaah, kumbe, ...

‘Huo ufungua uliupatia wapi?’ nikamuuliza.

‘Mbona ninao siku nyingi,...niliamua kuwa na nakala ya ufungua zote, maana wewe na mimi ni binadamu tu, unaweza kupoteza ufunguo zako, na mimi kama mume wa familia natakiwa kuwa makini kwa hilo ni muhimu kuhakikisha mambo yanakwenda vyema, ukipoteza ufunguo wako ninao wa akiba...kuna ubaya hapo ?’akasema akiwa kama ananiuliza, yaani anavyoongea, anavyoigiza sio yule mume ninayemfahamu.

‘Sio kwamba uliamua kuchongesha ili uweze kuja kuiba mkataba wangu, ili mkabadili na kuhakikisha nakala zote mumeziharibu, na pia ukaja ukachukua bastola yangu, nakumbuka wewe ulikuwa hutaki hata kuishika hiyo bastola,....imekuwaje sasa, uje uichukue na hiyo ndio imeafanya mauaji, ...na ole wako polisi wakifahamu hilo...’nikasema

‘Unasema, nilichongesha ili nije kuiba,.... kwa nini niibe, kuna mtu anaiba kitu chake, mbona mke wangu unaniangusha,...usisahau kuwa mimi ni mume wako, sio mtu mwingine yoyote,...’akasema,

Moyoni, akilini, na mwili mzima, nilikwua nimejawa na hasira, kama angelikuwa ni mtoto mdogo, ningemshika na kumchapa viboko, lakini huyu ni mtu mzima na ni mume wangu, nikabakia kukunja uso, na aliponiangalia usoni  jinsi nilivyobadilika, alisimama, na haraka akatoka nje ya hiyo makitaba.

Nilichukua mkoba wangu na kuutafuta ufungua wangu, ulikuwepo kwenye moja ya fungua zangu ninazotembea nazo, nikafungua lile kabati na kila kitu kilikuwa kwenye nafasi yake, na ule mkataba, ule waliotengeneza wao ulikuwa pale pale...’nikafunga lile kabati, na akilini mwangu nikapanga nikitoka hapo nabadili kila kitu, nitamwambia fundi abadili na kuweka kifaa cha ufungua kingine unachofungua kwa namba za siri.

Nilitoka mle makitaba na kuingia kwenye chumba chetu cha kulala, mume wangu hakuwepo humo, nikabadili nguo, na kuelekea sebuleni, chumba cha maongezi, na hapo nilimkuta mume wangu akiwa kakaa huku kashikilia mkataba, ..mwanzoni nilifikiria ni ule mkataba wa zamani, lakini ulikuwa ule ule waliougushi wao.

Nilimsogelea na kumwangalia, alikuwa katulia, na alionekana alikuwa akisoma sehemu hiyo kwa makini, na alipohisi nimesimama karibu yake, akauweka pembeni na kuniangalia, akatabasamu na kabla hajasema neno, nikasema;

‘Haya hebu niambie ukweli, ni kitu gani kinaendelea hapa kwenye nyumba yetu?’ nikamuuliza

‘Mhh, mke wangu, kwani kuna nini kibaya kimetokea, mimi sioni kama kuna kitu kibaya, labda nikuulize wewe, kuna tatizo lolote? ‘akauliza

‘Mume wangu, leo ni siku ya mwisho, sitakaa tuongee hivi tena, na nataka leo uniambie ukweli, tukimaliza hapa tujue ni nini cha kufanya, maana mimi nimeshachoka,vitendo vyako vimenichosha, kwanza umekiuka makubaliano yetu, umevunja mkataba wa ndoa, na hata sikuelewi, na hutaki kuniambia ukweli,  ....’nikasema na yeye akanitupia jicho, halafu akafungua ule mkataba wake, akawa kama anasoma jambo, mimi sikutaka hata kumsogelea na kuangalia anasoma kitu gani.

‘Kwanini unasema leo ni siku ya mwisho,hapana usiseme hivyo, tupo wote, na kila siku tutaongea, maana wewe ni mke wangu, na mimi ni mume wako, ....’akasema na kutulia, na aliponiona nipo kimiya akasema;

‘Kwani mke wangu situlishaelewana, na ndio maana nilikuwa nataka niutafute ile nakala yangu ya zamani,ya mkataba huu, nilikuwa nayo, naikumbuka sana,, na wewe unaihitajia, sijui kwanini unapenda nakala zile za zaamni uliweka alama zako nini, sehemu muhimu, au....hauna tofauti kabisa na huu, ni ganda tu, limekuwa jipya, lakini ndani kila kitu kipo sawasawa, vilevile....’akasema.

‘Hebu angalia, mwenyewe, ....’akasema huku akinipa ule mkataba, na mimi sikuugusa na wala sikuinua mkono wangu, nikawa namwangalai usoni nikasema.

‘Kwanza hebu niambia kwanini mlichukua hatua ya kuubadili huo mkataba bila makaubaliano na mimi?’ nikamuuliza

‘Mke wangu, mimi nakumbuka , hilo swali nilishakujibu, hakuna aliyebadili huo mkataba,mbona huniamini mke wangu,...hebu niambie ni wapi huo mkataba umebadilishwa, na kama ulibadilishwa kwanini sahihi yako, ipo ....unaona eeh, mke wangu hakuna kitu kimefanyika bila ya rizaa yako na wakili wetu wa familia, ...sahihi zenu zipo vile vile’akasema.

‘Kwahiyo kumbe bado upo na msimamo wako ule ule,....hutaki kusema ukweli, hutaki kuniambia ni nini kinachoendelea, na ni ni kusudio lako,au kusudio lenu, na washirika wako....’nikasema huku nimemkazia macho, yeye akaniangalia mara moja halafu akatabsamu, na kusema;

‘Kwani mke wangu kuna nini, mbona sikuelewi, kuna tatizo gani...hebu niambie , tusaidiane, huenda mimi nipo dunia nyingine, huenda kuna kitu umekigundua kwangu na unaogopa kuniambia, au nimebadilika, baada ya kuumwa, nimekuwa toauti, ...’akasema na mimi nikamwangalia mume wangu, na nikawa kama simuelewi, hivi huyu mtu yupo sawa, au ana matatizo, mbona sio yule mume ninayemfahamu,..maana namuuliza kitu na yeye kwanza hajali, na pili anakuwa kama hajui ninachomuuliza, haoni kuwa kafanya makosa.Anaigiza au ni kweli, hapana huu ni ujanja ujanja wake tu.

‘Mume wangu , pengine, hujanifahamu , pengine unafikiria kuwa nakutania, pengine, nahitajika kuchukua hatua nyingine ndio utanielewa,....hivi unajidanganya nini, hivi wewe hufahamu kuwa hilo unalolifanya linaweza likavunja ndoa yetu...’nikamwambia na yeye hapo akashituka.

‘Unasema nini..kuvunja ndoa yetu, hapana mke wangu, hilo halipo, na halitatokea, albda niwe nimekufa....kwanini unasema hivyo?’ akaniuliza na safari hii akawa ananiangalai usoni,akionyesha wasiwasi.

'Kutokana na makubaliano yetu ya awali, hata kama mumeugushi huo mkataba wetu, mkaweka mambo ya kukulinda, hata kama unajifanya mjanja sana,lakini ukumbuke kuwa makubaliano yetu ya awali yapo pale pale, na moja ya makubaliano yetu ni kuwa mmoja akivunja miiko ya ndoa, na akafanya tendo ovu, kama la kuzini nje, ...na kukawa na ushahidi wa kutosha, basi ....’akanikatisha.

‘Mke wangu unasema nini,....sijawahi kufanya hivyo,.....ni nani akakuambia nimezini, ....na na...mbona sikuelewi..nimezini na nani , umedanganywa mke wangu, temea mate chini, sijawahi, ..nakupenda wewe tu mke wangu, kweli kabisa....sikumbuki, zamani eeh, hapana ile ilikuwa ni ndoto tu, sio kweli.....’akawa kama anahangaika akigeuza kichwa huku na huku, huku usoni akionyesha kuchanganyikiwa.

‘Sikiliza, usijifanye kuigiza mambo hapa, hebu niambie ukweli, wewe huna mtoto nje ya ndoa?’ nikamuuliza

‘Mtoto, nje ya ndoa....sikumbuki, nakumbuka kuota hivyo....na nikiwa kwenye ndoto, nikajiona nina mtoto , tena mtoto wa kiume...lakini mama yake akakimbia naye...nikashituak kwenye usingizi,..ilikuwa ni ndoto tu, sio kweli, japokuwa mke wangu, nilitamani sana kuwa na mtoto wa kiume, alkini basi tena, ...basi tena, inauma sana, basi tena, ajali imeharibu kila kitu....’akasema huku akishika shavu kama mkiwa.mimi sikujali nilihisi kuwa auanigiza tu.

‘Nasikia kwenye mkataba wenu, mumeandika kuwa watoto wote watakuwa na haki sawa, wa kike na wa kiume,...lakini hapo hapo kwenye hicho kipengele, mkasema mtoto wa kiume atapewa mamlaka ya kusimamia mali , kama wazazi watakuwa hawapo, huo ndio usawa, .....huyo wakili wako alikuwa akiangalia mambo kwa kujipendelea,.je kipengele hicho kilitoka wapi na kwenye mkataba wetu wa awali hilo halikuwepo, sisi tulikubaliana kuwa watoto wote ni watoto wetu, na wana nafasi ya kumiliki mali yetu, kutokana na urithi tutakao utayarisha....unakumbuka hilo?’ nikamuuliza

‘Unaonaeeh, sehemu hiyo inasema hivyo, eeh hebu ngoja na mimi niisome, kwani kuna tatizo gani kwenye maelezo hayo, kama unaona kuna matatizo, basi tuone jinsi gani ya kubadili, ili ilete maana unayotaka wewe, na kama kuna sehemu nyingine huzipendi, basi tuziangalia, tuzibadili, unasemaje mke wangu...na maelezo hayo nafikiri ni kwa mtizamo wa ujumla, leo tuna watoto wa kike, lakini sio mwisho wa kuzaa, ....ingawaje...’akasita

‘Ingawaje, nini,...kuwa hutaweza kuzaa tena, kama hutaweza kuzaa tena kwasababu ya matatizo yaliyokupata kwanini mkaongeza hicho kipengele, kinachomgusa mtoto wa kiume, wewe unafahamu fika kuwa una watoto wa kike tu, huyo wa kiume mliyemtaja hapo ni nani?’ nikamuuliza.

‘Mke wangu, ...kwanza tuanze moja, halafu huko tutafahamishana, kama kuna makosa tutaparekebisha, mmh, kwanza hebu kaa, tuusome wote wawili,  naona sasa tunakwenda pamoja, kuwa mkataba huu ni ule ule, au sio, ....?’ akaniuliza

‘Mkataba ninaoufahamu mimi ni ule ule wa mwanzo, ambao haukuwahi kufanyiwa mabadiliko, na hilo tuliliongelea kuwa kama kutatokea baadaye tukaona kuwa kuna umuhimu wa kufanya mabadiliko, ..mabadiliko hayo yatatakiwa kukubaliana kwa pande zote mbili, mimi na wewe..je hayo mabadiliko mliyoyafanya mlinishirikisha?’ nikamuuliza

‘Mabadiliko gani hayo mke wangu, ...mbona sikuelewei mke wangu,...leo hii mimi nilitaka nikuulize kuwa kama unaona kuna jambo halipo sawa, basi tukae tuangalie , maana naona kama wewe hukubaliani na mambo fulani fulani kwenye huu mkataba...niambie ni mambo gani huyakubali, unataka tuyabadili, ili tumuite wakili wetu, tuone tutafanya nini..hilo ni la msingi sana,...’akasema huku akiufungua fungua huo mkataba.

‘Naona hujanielewa, nataka unipe majibu kwa haya maswali haya nitakayokuuliza,kama usiponijibu nachukulia kuwa umenipuuza, na kwahiyo nichukue hatua nyingine ambayo hatima yake ni kuvunja ndoa yetu, siwezi tena kukuvumilia,kwahiyo nataak unijibu haya maswali , na unielewe, .....’nikatulia kidogo

‘Nakusikiliza mke wangu uliza tu hayo maswali, lakini hilo la kuvunja ndoa sikubaliani nalo na halipo, na halitakuwepo.....’akasema

‘Kwanza kwanini mliamua kubadili huo mkatana bila ya kunishirikisha?’ nikamuuliza

‘Jibu nimeshakupa au unataka nirudie, ...mimi sijui kama kuna mabadiliko yoyote, na ndio maana naona leo tukae kama yapo basi tukayafanye, ukikubaliana na hilo,. Mimi sina shida,, mimi nafahamu kuwa huu ndio mkataba wetu, kama kuna mkataba mwingine zaidi ya huu nionyeshe...’akasema akionyesha kujiamini.

‘Swali la pili...’nikasema

‘Aaah, umerizika na jibu langu kwanza?’ akaniuliza

‘Hujanijibu swali langu, sijarizika,...na naona umenipuuza, tuendelee na swali jingine’nikasema

‘Unataka niseme nini mke wangu uone sijakupuuza, kama nimekuambia ukweli, na unaukana huo ukweli, wewe ulitaka niseme nini, hebu nifafanulie...’akasema

‘Swali la pili, je una mtoto nje,....?’ nikamuuliza

‘Hilo swali ...nimeshakaumbia, sina uhakika na hilo, nakumbuka nili-ilikuwa ni ndoto ..niliota hivyo, ...na najaribu kufuatailia, nione ukweli wake, maana kuna muda ninakuwa kama sio mimi, unafahamu mke wangu nahisi nina tatizo, ...sina uhakika,nakumbuka  hata docta aliwahi kuniambia kuwa kuna wakat hali kama hiyo inaweza kunitokea,....’akashika kichwa chake kwa mikono yote miwili.

‘Lakini , inawezekana kweli eeh, nina mtoto nje, ...yupo wapi....hapana, mke wangu huenda tuna mtoto wa kiume, tushukuru sana,..lakini yupo wapi...!’akawa kama anajiuliza na uso ulionyesha kutafakari, ..ukimwangalia inonyesha picha kabisa, kuwa anahangaika kutafuata ukweli

‘Usijifanye mjanja wa kujizulia ugonjwa wa kuchanganyikiwa, usinifanye mimi mtoto mdogo,  wewe ulishapona, huo ni ujanja ujanja wako tu, wa kutaka kunighilibu, nijibu swali langu, je wewe una mtoto nje, na ulizaa nani?’ nikamuuliza.

‘Nina mtoto nje na nilizaa na nani.?’ akawa ananiuliza mimi, na aliponiangalia na kuniona nimemkazia macho akasema;.

‘Mke wangu naomba unipe muda, nikafanyie uchunguzi, sikumbuki hilo kabisa, sina uhakika siwezi kukudanganya,..ina maana kweli mimi nina mtoto nje, ....mbona simjui, au ile ndoto ni ya kweli....mke wangu una uhakika na hilo , kuwa huenda nina mtoto nje, na mtoto mwenyewe ni wa kiume,...mke wangu, kumbe tuna mtoto mwingine,...hata kama sitaweza kuzaa tena, lakini tuna mtoto wetu, tena wa kiume...’akawa anaonyesha uso wa furaha, na kuniangalia, halafu akaangalia chini.

‘Swali la tatu, ni nani mwanamke mliyezaa naye?’ nikamuuliza

‘Mwanamke niliyezaa naye..!?, wewe ndiye mke wangu, niliyezaa na wewe....yule aliyemchukua mtoto sio mke wangu, mke wngu ni wewe.....unasikia,mke wangu ni wewe na watoto wote ni wetu, ....’akasema na akawa kama anahangaika kufikiria halafu akasema;

‘Kwanza hebu tumalizane na hilo la mkataba umeshaukubali kuwa ni ule ule , au la...?’ akawa kama anapoteza malengo.

`Swali la nne, je ni wewe uliyechukua mikataba kwenye kabati langu, la hapa na kule ofisini ?’ nikauliza

‘Mimi....ofisini kwako, lini,..?’ akawa anajishika kuonyesha ni yeye, halafu akaonyesha mkono kushangaa, halafu akasema;

‘Mke wangu mbona sikumbuki kufika huko ofisini kwako, tangu nianze kuumwa, sijawahi kukanyaga ofisini kwako’akasema

‘Swali jingine, Je siku makabrasha alipouliwa ulikwenda kwake kufanya nini?’ swali hili likamfanya ashituke na kugeuka kuniangalia, alitulia hivyo kwa muda, na akawa kama anakumbuka jambo, halafu akashika kichwa, na alitulia hivyo kwa muda, halafu akasema;

‘Ma-mamamaah...ina maana ni kweli....ooh, jamani rafiki yangu, ...haiwezekani, kwanini wamemuua, tena mbele yangu...’akasimama,

‘Mke wangu hivi mazishi yake ni lini, nataka kwenda kumuona nimuulize kwanini, ameondoka kabla hatujamalizana, ..kwanini..ooh, kichwa kichwa..ooh, ...’akawa anahangaika, na mara akageuka akaanza kutembea kwa mwendo wa haraka, kuelekea mlangoni.

‘Unakwenda wapi, haujamalizana, nimeshakuambia nikitoka hapa mimi naelekea kwa wali wetu, nafuata hatua nyingine, tutakutana mahakamani...’nikasema lakini mwenzangu alikuwa anaondoka, haangalii nyuma akasema;

‘Nawahi mazishi....’akatoka, mimi nilicheka kidogo na kusema

‘Janja yako...nafikiri wewe hunifahamu eehe...’nikatoka nje, nikamuona akiingia kwenye gari lake, na mara simu yangu ikaita, nikaipokea kabla sijaangalia mpigaji ni nani. Huyo mtu akasema;

‘Mimi ni docta .....’akasema kumbe alikuwa yule docta aliyemtibia mume wangu, nikashukuru maana nilikuwa na mpango wa kumpigia, kuhakiki haya anayoyafanya mume wangu ni ya ukweli au anaigiza tu.

‘Hali yako docta tena nilikuwa nataka kuongea na wewe..’nikasema

‘Ndio ...ndio maana hata mimi nilitaka kujua hali ya mume wako, anaendeleaje kwani kipindi kile cha matibabu, kulikuwa na docta mwenzangu, ambaye alikuwa akimwangalia kwa upande wa kumbukumbu, na alitaka kujua kama kuna hali yoyote inayojitokea kwake..yupo hapa leo ndio karudi toka safari’akasema

‘Kama hali ipi?’ nikauliza nikionyesha kushangaa.

‘Sijui kama aliwahi kukugusia ila hilo hatukuwa tumelitila maanani sana, maana kipindi chote alichokuwa kwenye uchunguzi, haikuwahi kutokea...kuna hali ya kusahausahau, hilo linaweza kumtokea mara kwa mara, na anaweza pia akafanya mambo ambayo hakuwa akiyafanya zamani, anaweza akawa na mabadiliko mabadiliko, unaweza hata kumuona ni mtu tofauti kabisa, sasa hali kama hiyo ukiiona imetokea, tafadhali tujulishe....’akasema

‘Unasema nini docta mbona hamkuwahi kuniambia kitu kama hichoo’nikasema kwa hasira.

‘Baada ya uchunguzi, ...kipindi kile tulipokuwa naye, alionyesha dalili, kuwa kapona, na mwenzangu akawa kaondoka, ...tulimwambia yule docta mnayeishi naye, maana wakati huo wewe ulikuwa na matatizo , ulikuwa jela,..sasa kwa vile mwenzangu karudi leo na tukawa tunafuatilia jarida la mume wako, na  sijui kwanini, kwani mume wako alitakiwa kufika mara kwa mara hapa hospitali kwa kliniki yake,hajafika kama tulivyomuagiza, ndio maana tukaamua tukupigie’akasema.

‘Docta mimi ninaweza kuwashitaki, ..hilo ni kosa kubwa sana, maana sasa hivi nimemuona mume wangu kama kachanganyikiwa, na mimi nilifikiria kuwa anajifanya..kwasababu nimekuwa nikimuuliza maswali., anajibu kama anaigiza, kuwa hajui, mara anasema kasahau, mara aliota,..katoka sasa hivi na gari, yupo kama ...’nikasema.

‘Mfuatilieni haraka,...na mleteni hapa. ....’akasema docta, na mimi nikakata simu yake na kuingia kwenye gari langu, nikijaribu kumfuatilia, sikujua kabisa kaelekea wapi.....oh, ina maana mume wangu akchanganyikiwa kweli....

NB: Kwa leo ndio hivyo,


WAZO LA LEO: Kwa wandoa mmoja anapoumwa, ni vyema mkajaliana kwanza, hata kama kulikuwa na sintofahamu, migongano, na mitihani ya hapa na pale, hayo yote myasahau na muangalia afya zenu kwanza, kwani afya ni bora kuliko mali.

Ni mimi: emu-three

No comments :