Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Wednesday, October 23, 2019

CHUMA ULETE 2


‘Chuma ulete...!..’nikang’aka. Na msimuliaji wa hiki kisa akatabasamu japo uso ulionekana na huzuni, na alikaa kimia kwa muda.

‘Una maana gani au ndio hizo imani za watu kuwa,...’ nikamuuliza pale nilipoaana yupo kimia.

'Ndio,...chuma ulete... ndivyo alivyoniambia hivyo mke wangu, mke ambaye awali hakupenda kabisa imani hizo za kishirikina,...uchawi tuseme...kiukweli nilishangaa kidogo, kwani awali hakuwa akiamini mambo hayo..'akasema, na kutulia kidogo

'Nikajaribu kumuasa mke wangu kihekima na kiimani, unajua tena...eeh...kuwa uchawi upo sikatai, lakini ukimuamini mungu, ukamuomba yeye, bila kuweka nafsi ya shiriki, huwezi kushindwa jambo..’akasema.

‘Na nikaendelea  kumuasa...’

''Mke wangu, tusiamini sana hayo mambo maana ukiyaamini sana hayo mambo, mwisho wake utaingia kwenye shirki, na imani yetu haitaki hivyo, ...nikamwambia mke wangu’’.

Awali alijifanya kunielewa, lakini mambo hayakuendelea hivyo....’msimuliaji akaendelea kuongea, na alipofika hapo alitulia kidogo.

'Kwa vipi...kwani kulitokea nini tena zaidi...'nikauliza sasa nikiwa na shauku zaidi.

'Sikuacha kumnasihi, mke wangu, nikijua kuwa mimi ndio  mume wake, na mimi ndiye kichwa cha familia,  unasikia sana...’akasema.

‘Sawa kabisa...’

‘Lakini..eeh, ndugu yangu wee, kumlea mtu mnzima ni kazi sana..ni mpaka yeye mwenyewe akubaliane na wewe...moyoni nikadhamiria kutumia nguvu japo kidogo.., mimi najua wengi watanilaumu sana kwa hilo, unajua ni kwanini nilitaka kufanya hivyo, kwa akili yangu, niliona bila hivyo, hataweza kuachana na ushetani huo...sumu ya ushetani, ilishapenyezwa kwenye ubongo wake,..’akatulia.

‘Sijakuelewa...’nikasema.

‘Yule mke niliyemuamini...ambaye nilikuwa namuasa jambo, ananisikia kwa unyenyekevu. Yule mke mpole, mwelekevu, hakuwa yeye tena, najuta kwanini nilimpatia nafasi hiyo ya kujichanganya...nahisi tamaa za nafsi na ushawishi wa mashoga, vilishamteka nafsi yake...’hapo akahema kwa nguvu.

‘Ndugu yangu makosa yaliendelea kujirudia, kidogo kidogo,akawa sasa haambiliki,hata kauli zake zikawa za kijeuri jeuri hivi, japo sio kwa moja kwa moja...kila hatua akawa ananipandisha presha...'akaendelea.

Niliumia sana..ilifika mahali naanza kukata tamaa, nilimpenda sana mke wangu, sikupenda abadilike, sikupenda, nije nianze kutumia nguvu, maana naogopa...naogopa sana kupiga,...naogopa sana, najijua nilivyo, nikianza..sirudi nyuma, nina hasira za mbali lakini zikipanda, ooh, ndugu yangu...sitaki kuua tena...’akasema na kushtuka, nahisi hakupenda kutamka hivyo.

‘Kuua tena, ina maana uliwahi kuua...?’ nikauliza kwa mshangao.

‘We acha tu, hayo yalishapita....samahani kwa hilo, limetoka tu..sija-jawahi..ku-kua bwana...’akasema sasa kwa kusita sita.

***********

Kisa kikaendelea....

Haikupita muda, hali ikaanza kubadilika, maisha yakaanza kuwa magumu, biashara haziendi , pesa haikamatiki...sikufichi,...kuna wakati imani ikaanza kushuka, maana unaambiwa mengi,..wanakushauri wengi..fikiria kutoka maduka hadi...genge la nyanya mbili tatu, na...ikawa mbaya zaidi ya hapo, hata ingelikuwa ni wewe....ila,  hata hivyo, sikufikia hatua ya ...kuamini maneno ya mke wangu...’akatulia kama anawaza jambo.

‘Maneno gani...?’ nikauliza kama sijui.

'Umasikini ni mtihani ndugu yangu, ...tatizo sasa ikawa kwa  mwenzangu yeye anaendelea kudai matumizi tu, hata pale ninapomwambia sina kitu na wakati mwingine anafikia hata kunikasirikia,..na kuanza kutoa maneno ya kashfa...sikupenda hilo....maana alivuka mpaka...’akaendelea bila kujali swali langu.

'Mke wangu hali unaiona, na mitihani hii ni kawaida kwenye familia, awali ulikuwa unavumilia nakueleza kitu unanielewa,... hivi nimekosea nini mke wangu, kosa langu mimi ni kukupatia uhuru, au...?’ nikamuuliza.

‘Hapana mume wangu, nahisi kosa ni la kwangu mimi....kukuambia ukweli...’akasema

‘Ukweli upi...?’ nikamuuliza.

‘Aaah..sitaki tena kuongea...maana wewe ndio mume...nitasema nini tena mbele yako, nina nini tena mtoto yatima,...wewe ndio baba, wewe ndio mama yangu...’akasema.

‘Nahitajia ushauri wenye tija, sio imani haba na mambo ya kuambiwa..’nikasema.

‘Nikushauri nini tena mume wangu, ushauri wangu nilishakuambia,..kwanza nilikuambia tujiunga na michezo ya kupeana, hukukubali, ..na..na hali hii ambayo nimeshaiona, wewe hutaki kuniamini..mume wangu tatizo lipo humu ndani...’akaniambia na kabla sijamkatisha akaniambia

‘Najua unanidharau, kwa vile ni mwanamke,..sio vibaya,...lakini ..mmh,...mimi  kuna mambo nayaona, ila wewe hutaki kuniamini....utakuja kunikumbuka kwa hili...’akasema kwa sauti ya unyonge.

‘Una maana gani...?’ nikauliza sasa nikimuangalia kwa mashaka mashaka.

‘Mume wangu, u-meingiliwa na chuma ulete...fanya haraka kabla hali haijawa mbaya...’akasema sasa akishika kichwa na kuangalia huku na huku kama ana wasiwasi ...na ile hali ya kukuna kuna kichwa, kama kinamuwasha ikanipa mashaka.

‘Nini.....’nikang’aka hivyo, nikimuangalia kwa kumkagua akijikuna kuna kichwani.
Kiukweli hadi hapo mimi  nilishaamini, mke wangu sio mwaminifu tena...nilimuona kama anajifanyiza tu, kunivunga mimi.

  Unakumbuka nilivyokuambia awali, huko nilipomtoa mke wangu, sifa yake kubwa ni uaminifu...hadi hapo niliona ni uwongo, labda ...walinidanganya...... awali ilikuwa hivyo sio sasa..na hebu niambie, hata kama ingelikuwa ni wewe..ungefanya nini hapo, maana sio mara moja, au mbili...imekuwa ni kawaida,..’akasema akiniangalia mimi usoni.

Hapo sikuwa na jibu la kumuambia, nikasubiria aendelee...

**********
Unajua tena, katika kuishi na watu unaweza ukawa na marafiki, na kati ya hao, ikatokea mmoja au hata wawili ukawaamini, japo mimi nina hulka yangu, sio rahisi kumuamini mtu,...hasa kwenye maswala ya imani, msimamo wangu ni thabiti.....kuna rafiki yangu mmoja, muungwana, ana busara sana, siku moja nikaongea naye nikitaka ushauri kwake.

‘Ndugu yangu kabla hujaanza kuingia huko, kwenye hasira, mkaja kukosana wewe na mke wako, hebu fanya uchunguzi wako wa kina..yawezekana tatizo lipo humo humo ndani, au...majirani,..siwezi kukupinga, au kupinga mawazo ya mkeo, maana hayo mambo yapo....’akanishauri.

‘Yawezekana tatizo lipo humo humo ndani kwa vipi...?’ nikauliza hivyo.

‘Yaani...yawezekana...ila...uchunguzi kwanza, usiwe na papara...’akasema.

‘Unajua ndugu yangu, mimi nimefanya kila uchunguzi, sijawahi kuona dalili ya kumshuku mtu baki, na nikuambie ukweli nyumbani kwangu watu hawaingii mara kwa mara, wananiogopa...’nikasema.

‘Sawa....lakini ...’nikamkatisha.

‘Ninasema hivyo kwasababu..mke wangu nilishamkanya,..sitaki majirani waingie ndani, mimi naafahamu sana majirani wangu...kwahiyo, kama ni kukutana na hao watu watakuwa wanakutana huko huko nje hasa  hao mashoga , waliomuharibu akili yake...mimi sina mfanyakazi wa ndani au ndugu ninayeishi naye, ni mimi na mke wangu tu...’nikasema.

‘Kwahiyo shaka yako kubwa ..ni kwa mke wako..si ndio hivyo..?’ akaniuliza.

‘Siwezi mshuku mtu wa nje..sijui unanielewa hapo...shuku itakwendaje nje kwanza, eeh... pesa ipotee humo humo ndani...na nipo mimi na mke wangu, nitamshukuje mtu wa nje kwa vipi, mlango haujavunjwa,...sijui unanielewa hapo....’nikasema kumuamboa huyo rafiki yangu.

‘Basi...vuta subira..ngoja nilifanyie hilo kazi rafiki yangu..’akaniambia huyo rafiki yangu. Kwa pale, sikuelewa, atalifanyiaje kazi, hata hivyo sikutaka kumdadisi, nikaachana naye...maana akili ilikuwa na mikakati mingine ya kibiashara.

***********

Siku moja  nikarudi nyumbani mapema....nilikuwa na pesa nimekopa mahali..., kwa ajili yakuanzisha biashara tena.., niliona nianze mtindo huo wa kukopa na kurejesha, labda nitafanikiwa, japo nianze kidogo kidogo.

Nilishapanga bajeti yangu vyema, iliyobaki ni kununua vifaa na kuingia sokoni,..kiukweli nilishapanga nitoke, kihivyo, ...na ndoto nyingi za Alinicha ziliuteka ubongo wangu, si unajua tena, ukikwama, na ukaja kuzishika pesa, ...mmh, akili inakuwa na mengi sana.

Pamoja  na shauku ya biashara,...bado  mwili ulikuwa hauna nguvu, sijui kwanini siku ile ilikuwa hivyo, na hali ile..ilinianza pale nilipozishika hizo pesa, nahisi hivyo.....maana hata kula sasa kulikuwa kwa shida, mawazo mengi kupitiliza.

Nikafika nyumbani...sikumkuta mke wangu, nikajua katoka kidogo, nikavua koti langu, nikatundika kwenye kabati la nguo...sikuwa na shaka, kwenye lile koti ndio niliweka pesa, nikajilaza kitandani...sijui usingizi ulitoka wapi, ...mwili ukalegea,...sijui nielezeje, nikashikwa na usinginzi mnzito ajabu,...nashtuka nasikia mke wangu anaongea nje...anaagana na mtu.

‘Kwaheri ...’

‘Kwaheri...’

Mimi kwa haraka  nikashtuka nikikumbuka natakiwa kwenda kununua bidhaa muda umeshapita, hata sijui kama nitakuta maduka ya jumla yapo wazi..sikukata tamaa, na sikupenda nilale na hizo pesa ndani, nikiogopa hayo yanayoendelea, hapo ilishafika jioni kama saa kumi na moja hivi.

Nikachukua koti langu,..nikavaa, wakati navaa,  mke wangu akaingia, aliponiona akashtuka, na kusema;

‘Oh, la azizi wangu umerudi mapema leo....,vipi kuna tatizo, sikujua kaam upo humu ndani.. kumbuka kauli hiyo,...’

‘Ndio mke wangu,...ume-rudi saa ngapi...?’ nikauliza, na kbla hajanijibu nikasikia mtu anagonga mlango.

‘Ni nani tena, kwanza sikiliza ,maana nimechelewa, nataka kutoka, nikirudi tutaongea vizuri..’nikasema,

Mke wangu akatulia akinisikiliza huku mtu anayegonga mlango anaendelea.

‘Sasa sikiliza....chukua pesa hii ufanye fanye mambo, japo ni pesa ya kukopa, lakini aheri, ntoe kidogo, tule chakula kizuri leo japo kidogo...au sio mke wangu’nikasema sasa naingiza mkono mfukoni kutoa pesa,..mkono ukazunguka kwenye mfuko wa koti...moyo ukaanza kunienda mbio, siamini.....


WAZO LA LEO: Tusiwe na tabia ya kuzania dhana mbaya, kabla hatujafanya uchunguzi wa kutosha,..dhana mbaya, hupunguza imani moyoni.
Ni mimi: emu-three

No comments :