Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Thursday, August 23, 2018

YOTE NI KWA MAPENZI YA MUNGU-36


 Hali ya Dalali iliendelea kuwa mbaya, sasa ikabidi ahamishiwe kwenye wodi maalumu, bado akiwa kwenye hali hiyohiyo, japokuwa sasa alikuwa hapumulii mashine ya gesi, na mapigo ya moyo yalikuwa yakifanya kazi, ajabu mtu mwenyewe sasa alikuwa hawezi kuongea au kujiinua, yupo yupo tu.


‘Hii hali sio ya kawaida…tumejaribu kila njia, lakini mtu yupo kama alivyo hivyo…sasa sisi tumeshauriana na wenzangu, tumeona ahamishiwe hospitali za juu…’akasema docta.

‘Haya sisi tunawasikiliza nyie…’akasema muongeaji wa familia.
Wakati utaratibu wa uhamisho wa mgonjwa huyo kwenye hospitalini za juu ukifanyika,
Wandugu wakakaa kikao kijadiliana, na mmoja akasema;

‘Jamani hivi hamuoni, hili tatizo ni kama lile la mke wa marehemu, si ilikuwa hivi hivi jamani…’akasema mmoja wa wanafamilia.

‘Mhh,… yule mwanga, au ndio kageuza kibao kwa shemeji yake, …inabidi tulifuatilie hili jambo kwa watalaamu,, ..lakini kipindi kile aliyefuatilia tatizo la huyo mwanga, alikuwa  ni huyu huyu mgonjwa, sasa nani anaweza kufahamu wapi alikwenda, ili na sisi twende huko…?’ akauliza mwanandugu mwingine.

‘Mimi nafahamu ni kule kwa yule mtaalamu wa bondeni, maji machafu…’akasema jamaa mmoja

‘Oh, ndio yule, mimi wala simuamini…?’ akauliza mzee mmoja na kutoa hoja zake.

‘Ndio…nakumbuka mara kwa mara Dalali hupenda kuenda kwa huyo jamaa, labda tujaribu kwake kwanza tumsikie…’akasema huyo jamaa,

‘Sasa nani atalifuatilia hili…?’ wakauliza na kamati maalumu ikaundwa kulifuatilia hilo, akiwemo mke wa Dalali.  Na baadae taratibu za uhamisho kwa mgonjwa huyo zikakamilika,…Dalali akahamishwa, …

Hayo yakiendelea huko,

**********.
Huku kwa watu wa usalama,mambo yalikuwa nayo yakiendelea…

Mara taarifa zikawa zimevuma, kuwa Dalali hali yake ni mbaya sana ni ya kusikilizia,…na kwa umaarufu wa Dalali watu wakakimbilia hospitalini kuuliza….na walipofika hapo wakaambiwa Dalali hayupo hospitalini hiyo , na iliposikiwa hivyo, ndio ikaja taarifa nyingine kuwa Dalali hatupo naye duniani.

 Siki hiyo ndio nami nimeitwa kituo cha polisi kuonana na wapelelezi,..wakati naingia, ndio nakuta majadaliano makali,  humo nikawakuta wapelelezi wale wawili na wakili wao, na mbele yao kuna nyaraka mbali mbali, na nilipofika tu,…nikamsikia wakili akisema kwa hasira;

‘Huu ushahidi hauwezi kushindana na ushahidi wa benki, hapa mnataka kunita mimi aibu tu…, mimi siwezi kufanya kazi kama hii…’akasema huyo wakili muendesha mashitaka, na aliponiona naingia akanyamaza.

Nikasalimiana nao, na ndio wakaanza kunielezea hali halisi..

‘Kiukweli, hapa hatuna kesi kabisa, tunapoteza muda wetu bure na gharama, ambazo mwisho wa siku mtatakiwa kuzilipa…ushahidi wa benki una nguvu za kisheria, unaonyesha kabisa kuwa hilo deni ni la marehemu…’akasema huyo wakili

Nikabakia kimia;

‘Sasa nimeambiwa wewe ndiye msemaji wa familia kwa hivi sasa, ..mimi nashauri, kwa vile deni lipo, na linaonyesha ni la marehemu, hakuna haja ya kujiingiza kwenye gharama za kuendesha hii kesi, ujue ukishindwa utalipa deni na gharama zote za hiyo kesi…’akasema wakili.

‘Samahani kidogo, nikuulize tu,…je kwa kusema hivyo, una maanisha kuwa wewe umejiaminisha kuwa, hilo deni ni la marehemu si ndio hivyo…?’ nikauliza

‘Sio mimi, ni vielelezo na ushahidi…’akasema.

‘Ok,..unajua mimi, bado sikubaliani kabisa…sasa labda bado nikuulize wewe, kwa jinsi ulivyoona, hivyo vielelezo, nafsini mwako unaamini hivyo, kuwa hilo deni ni la marehemu …wewe kama wakili, wewe kama mzazi,.?’ Nikamuuliza tena hivyo, aliona kama namkera fulani hivi,  akaniangalia kwa macho ya kushangaa, halafu akasema;

‘Sikiliza ndugu, hapa hatuongei kiusanii, kinachoongea hapa ni ushahidi, ni sheria, na jinsi gani ya kumshawishi hakimu,..mimi nimepitia ushahid uliopa hapa, ..huu, hauwezi kusaidia lolote,…sasa kutoa hisia zangu haitasaidia kitu hapa…’akasema.

‘Nimekuuliza hilo swali nikiwa na maana moja,…hii kesi, ukitaka upate ushahdi wa kimaandishi, hutaweza kuupata, maana ulishaharibiwa na hao waliokusudia kufanya hivyo..’nikasema

‘Kama ni hivyo, ulitaka mimi nitetee vipi maandishi, nyaraka, au mashahidi wa kuaminika, ndio kitu cha kusaidia hapa, sio hisia ndugu yangu, ujue sisi ndio tunakwenda kufungua kesi ya kupinga hukumu,… kuwa hilo deni sio sahihi, sio la marehemu…’akasema.

‘Unajua mimi awali, niliomba hizo barua mbili ambazo  nahisi zinaweza kuwa na…namna fulani ya kuupata huo ushahidi…, pili nilishauri juhudi zifanyike ili tuwapate hao watu wawili, waliotoweka,… sasa sijui mumefikia wapi..’nikasema.

‘Hizo barua hazitasidia kitu, nimshazipitia,….kwasababu zenyewe hazina viambata vya kuzibeba,, unanielewa hapo,...ukiangalia hiyo barua ya benki, ina kiambatishi cha statement, lakini hiyo statement yenyewe inakuwa ushahid wa benki…’akasema.

‘Naomba niipitia kidogo…’nikasema na walisita kidogo baadae nikakabidhiwa,..ilikuwa imewekwa ndani ya karatasi ya nailoni,…kabla sijaipitia nikauliza swali.

‘Je kwenye alama za vidole, hamkupata kitu cha kusaidia,.?’ nikauliza

‘Hakuna cha kusaidia,..alama kwenye barua ya benki ni alama za vidole za marehemu , na juu ya bahasha kuna alama zingine, lakini hazijulikani ni za nani, …’wakasema

‘Kama hamjampata ni alma za nani, huo ni moja ya ushahidi..kama ingelikuwa ni marehemu peke yake tungelisema yeye ndiye aliyejaribu kuchoma huo ushahidi..ina maana kuna mtu yupo nyuma ya hili jambo..’nikasema.

‘Je alama za Dalali kwenye hiyo barua hazipo..?’ nikauliza

‘Kwenye hiyo barua ya benki hakuna alama za Dalali, au mtaalamu, …’akasema mpelelezi.

‘Ni nani sasa…washukiwa wote  alama zao haziendani na hizo alama zilizopo kwenye hiyo barua, ya benki…na kwenye ajali, alama zilizopo ni za Dalali, na ni uhakika kwa vile yeye ndiye alikuwa na hiyo barua, kwa mara ya mwisho…ila kuna alama nyingine inayofanana na hiyo barua nyingine…’akasema

‘Na ndio kusema hiyo alama ni ya huyo mchomaji wa hizo barua,,….na sio alama ya mama mwenye nyumba, Dalali au mtaalamu…’akasema;

‘Na hapo mpelelezi, akauliza swali, hivi ni kwanini mama mwenye nyumba alichukua tahadhari ya alama zake zisionekane kwenye hizo barua, alipoziona kwenye hilo shimo…?’ akauliza mpelelezi

‘Ni tahadhari tu, huyo mama kaenda shule, anajua tahadhari ya hilo…mimi sioni kama mama mwenye nyumba anaweza kuhusika na hilo..’nikasema

‘Usimtetee…hapa yoyote anaweza kuhusika…’akasema mpelelezi

Basi nikawa nazipitia ile statement na barua, …niliona kiasi ambacho mlalamikaji alikuwa akikilalamikia, na kwenye statement inaonyesha hivyo, ..na ikaja salio, kuna statement nyingine mpya ambayo, ndio inabeba deni la nyuma, na kiasi kilichokopwa,..ni kiasi kikubwa sana,…

‘Je benki hawawezi kupata..statemeny mpya kama hii, ya nyumba ambayo inaendeleza bila kukata sehemu mbili, salio la zamani na la sasa..?’ nikauliza.

‘Benki wao wanasema haiwezekani maana mashine yao iliharibika, na kumbukumbu zilichukuliwa hivyo kama salio kutoka kwenye taarifa za kimahesabu, na wakati wanachukua taarifa hizo, salio lilikuwepo ndio hilo…’akasema

‘Salio lilikuwepo bila deni, au sio..?’ nikauliza

‘Ndio..hilo deni lilikuja kujitokeza kwenye statement hiyo ya pili, kwahiyo sio rahisi kupata maelezo ya awali yakiendeleza hadi sasa..’akasema.

‘Je kuna kumbukumbu gani za zamani zilizopo, kwa mfano barua kama hii je ipo benki, barua ambayo aliandika marehemu kulalamika..?’ nikauliza

‘Kumbukumbu zote za zamani ziliharibika..ikiwemo faili zilizopo barua kama hii, na banki imesaidiwa kupata hii nakala....’wakasema

‘Sasa kuna ushahidi gani wa kusadikisha kuwa hilo deni ni la marehemu kuacha hii statement iliyoambatishwa hapa…?’

‘Upo mkataba, …zipo nyaraka za kuonyesha kuchukuliwa kwa hizo pesa na sahihi ya mchukuaji, hiyo haina shaka, ndio maana benki wana kila sababu ya kuamini kuwa deni hilo ni la marehemu….’akasema.

‘Mhh..kumbukumbu za zamani ziliungua, lakini kumbukumbu hizi zipo, …kwanini hizi hazikuungua..?’ nikauliza

‘ Kuna kumbukumbu ambazo zilikuwa kwenye kabati la ndani,hizo hazikuungua, na nyaraka zake ni pamoja na mikataba ya mikopo huo…’akasema wakili.

Nikaipitia tena ile barua na statement..sikuona cha kusaidia..kiukweli hapo nami nikaanza kuhisi mtihani mkubwa jinsi gani ya kuthibitisha huo ukweli kuwa hilo deni kweli sio la marehemu…moto umeunguza vitu vya ofsini, moto umeunguza gari na kuua mtu…moto…moto ukaja kuchoma hata kumbukumbu za marehemu nyumbani kwake

‘Kuna nini kwenye moto…’nikasema na wao wakaniangalia tu

‘Moto si moto bwana, ili uharibu kumbukumbu kabisa inabidi kuchoma moto…’akasema mpelelezi.

 ‘Mimi naona watu wa kutusaidia kwa hii kesi ni hao jamaa wawili…’nikasema

‘Bila kumbukumbu za maandishi itasaidia nini, hata kama tukiwapata, maana wao wanajua hizo kumbukumbu hakuna, kwahiyo kwa vyovyote iwavyo hawatakubali....’akasema wakili

‘Ina maana ushahidi wote ni lazima uwe wa kimaandishi..?’ nikauliza kama vile mimi sijui lolote kuhusu sheria.

‘Kwa ajili ya hii kesi ya benk, maandishi ni kitu muhimu sana, bila maandishi hatuwezi kushinda, benki wana maandishi,..nikiwa na maana mkataba, na hati ambazo zinaonyesha kuwa kweli marehemu alichukua huo mkopo..’akasema

Na mara simu yangu ikalia..nikapokea kwa haraka nilijua ni nani kapiga hiyo simu

‘Vipi umemfuatilia hadi wapi..?’ nikauliza

‘Wapi, hospitalini gani…?’ nikauliza na kusikiliza kwa makini baadae nikawageukia wenzangu, na kusema;

‘Mtu wenu namba mbili aliyetoroka mahabusu kapatikana..’nikasema

‘Kapatikana wapi..?’ wakuliza wale wapelelezi wawili kwa pamoja.

‘Yupo hospitali ndogo ya wiliya, ila kwa hivi sasa, kaandikiwa uhamisho wa kwenda hospitali kuu  ya muhimbili…hali yake ni mbaya sana…’nikasema

‘Anaumwa nini huyo mtu.?’ Akauliza wakili.

‘Alikuwa na jereha la risasi,…wakati anatoroka alijeruhiwa kwa risasi,..sasa lile jeraha limeozesha mguu…na hataki huo mguu  ukatwe…’nikasema

‘Oh…sasa tumempata mmoja…’akasema mpelelezi akionyesha furaha fulani.

‘Sawa, lakini hata kama mumempata huyo mtu mmoja,, bado kuna kazi ya kumshawishi, nyie awali mlikuwa naye au sio.. , mlimuhoji alisema nini…hapa sioni maelezo yake, zaidi ya kuwa alitoroka..?’ akauliza wakili

‘Hakupenda kuongea…kila jambo alimtupia Dalali…hata baada ya kufinywa kidogo,…aliishia kusema anayejua zaidi ni Dalali,.. na alipoona kuwa anaweza kuongea , maana asingeliweza kuvumilia, ndio akatoroka…’akasema mpelelezi.

‘Kwahiyo mnahisi kuna jambo analifahamu ..kwa jinsi mlivyomuhoji…?’ akaulizwa

‘Ni mjanja sana..alikuwa makini kwa hilo…kiukweli hakuna tulichopata kutoka kwake, yeye anadai kazi yake ni kuhudumia wateja, na kuhusu hilo deni , Dalali ndiye alifika kwake kuomba msaada wake, ..’akasema

‘Msaada gani…?’ akauliza wakili

‘Hilo deni lipotee, na yeye akasema, akamwambia Dalali hilo deni ni kweli la marehemu, na alisema hivyo kutokana na jinsi alivyoona kwenye kuangalizia kwake,…unasikia, kuangalizia kwake, akiwa na maana ya ramali.

‘Kwahiyo yeye anakiri kuwa aliona hivyo, kuwa deni ni la marehemu, na hayo mambo ya mizimu je.?’ Nikauliza

‘Alisema,.. yeye alivyoangalia, ndio alijua kuwa matatizo yote yanatokana na hilo deni, ndio maana mizimu ilifika kuitesa hiyo familia,..ili deni lilipwe, ili marehemu aweza kupata makazi mema…’akasema.

‘Kwahiyo maelezo yao yanafanana na ya Dalali…?’ nikauliza

‘Yanafanana ndio..’akasema mpelelezi.

‘Sasa kumuona sasa hivi itasaidia nini…?’ akauliza wakili

‘Kwanini alitoroka, hiyo inaweza kumfanya aongee…ngoja tujaribu kumuona…’akasema mpelelezi

‘Itasaidia tu..nahisi anajua zaidi ya hicho alichokisema, tukimbana sana kwa maswwali…’mimi nikasema

Wapelelezi wale wawili wakasimama, na wakili akawa anawaangalia tu

‘Inabidi tukuache muheshimiwa, unaweza kuongea na mtu wa jamii kumalizana naye huenda tukarudi hapa haraka iwezekanavyo…’akasema mpelelezi

‘Na mimi nataka niandamane nanyie kama hamtojali…, nataka nisikilize anachoongea au hata mimi nimuhoji pia..’nikasema na wapelelezi wale wawili  waliangaliana baadae wakakubali;

‘Sawa twende…’wakasema

Basi tukaondoka na hao wapelelezi wawili, tukamuacha wakili muendesha mashitaka akipitia vielelezo vilivyopo mbeleni mwake.

Wakati tunatoka nikapokea simu ya mama mjane.

‘Vipi dada..?’ nikamuuliza

‘Kuna taarifa kuwa mnada utafanyika, kwenye wiki hii, hakimu aliyetoa hukumu kawakubalia benki wapige hii nyumba mnada…’akasema.

‘Nani kakupatia hiyo taarifa..?’ nikauliza

‘Wakili…’akasema

‘Wakili yupi..?’ nikauliza

‘Yule wa zamani…’akasema

‘Hamna shida,….nakuuliza  jambo moja, unafahamu mzee mtupe ana uhusiano gani na mtaalamu..?’ nikamuuliza hilo swali.

‘Mhh, mimi sijui…labda nije kumuuliza mpangaji wake mmoja anayemfahamu ..’akasema

‘Hapana, usifanye hivyo, …nitajua mwenyewe tu..’nikasema na kukata simu.
Tukafika hospitalini, na kujitambulisha, ..kwanza ilionekana kama madakitari hawataki kusema kuwa huyo mgonjwa yupo au hayupo, na walipobanwa sana, wakasema jamaa zake hawakutaka mtu huyo afahamike kuwa yupo hapo.

‘Sisi ni polisi, na huyo mtu anatafutwa kwa uhalifu..’akaambiwa docta, na docta hakuwa na la kufanya akawaonyesha wapi huyo mgonjwa alipolazwa.

‘Lakini bado hawezi kuongea, kwasababu imebidi tukate huo mguu wake…’akasema docta

‘Kwanini ..?’ akaulizwa.

‘Ulishaanza kuoza, na unatoa harufu kali, sio kawaida…na kuoza huko kumetengeneza kansa,…’akasema docta.

‘Oh, kansa hiyo ina athari gani kwake…’akauliza mpelelezi.

‘Kiukweli kansa hiyo imeenda mbali sana, na tunaangalia jereha lilivyo, ili ikiwezekana aanze matibabu ya mionzi, kiukweli hali yake sio nzuri…’akasema docta.

‘Tunaweza kuongea naye…kama hali ndio hivyo..?’ akauliza mpelelezi

‘Kiukweli, haiwezekani kwa hivi sasa…’akasema docta.

‘Docta, kama uwezekano wa huyo mtu kuishi ni mdogo, tunataka tupate maelezo yake kidogo, fanya ufanyavyo, huyo mtu anashukiwa kwa uhalifu…’akasema mpelelezi.

‘Ngoja kwanza tuone…’akasema docta, na akaingia huko ndani, na baadae docta akatoka, na kusema;

‘Sawa mnaweza kuongea naye, lakini kwa haraka, dawa niliyompatia haiwezi kudumu kwa muda mrefu..’akasema docta.

************

Tuliingia kwenye hicho chumba alicholazwa huyo mgonjwa, pamoja na madawa ya hospitalini, bado harufu ya kitu kuoza ilisikika…

Wapelelezi wakamsogelea mtaalamu..mtaalamu alikuwa kafungua macho, na alipowaona hao watu wawili nikaona macho yakimcheza cheza;

‘Mtaalamu, sema ukweli wako, ili tuweze kukusaidia..hali uliyo nayo unahitajika wewe kwenda India kwa matibabu zaidi…,sasa ongea ukweli ili tuweze kukupatia hiyo nafasi…’akasema mpelelezi.

‘Si-s-wezi ku-ku-pona,..na si-s-na cha kuwaambia, Da-la-li, ata-wa-wasai-diaah, ni-ni acheini, ni-ni fe tu, ta-tayari…si-sipo-poni…ma-ma-teso ya.ya me-zidi, bo-bora ku-kufa tu…’akaweza kusema hivyo.

‘Je kweli deni ni la marehemu, ujuavyo wewe…?’ akaulizwa.

‘Mi-mi…Si-s-i..ju-ju—iii, si-we-zi..kku-se-ma…’ akasema hivyo

‘Kwanini huwezi kusema, upo tayari ufe , hutaki kutibiwa wewe..?’ akaulizwa
Akabakia kimia…
‘Ajali ya gari, lililomuua marehemu alisababisha nani…?’ akaulizwa

‘S-si jui…si-we-zzz-ku-kusema..mi-i-i-ko…’akasema hivyo.

Na mimi hapo nikaona nijaribu bahati yangu.

‘Mtaalamu, ukweli unaweza ukawa dawa ya matatizo uliyo nayo,  kuumwa sio kufa, lakini wakati mwingine inabidi kujiandaa na kifo…ukifa, unakwenda kukutana na yule asiyedanganyika, ni heri ukatubu kabla ya siku haijafika,..mtaalamu huenda kauli yako ikasaidia,...sema ukweli wako ujisaidia, hapa duniani na kesho ahera…’nikasema.

Hapo mtaalamu akabakia kimia, …nikaona machozi yakitoka machoni mwa huyo mtu.

‘Mtaalamu, sema ukweli wako kabla mlango wa toba haujafungwa…kumbuka ukweli unaweza ukawa ndio dawa ya matatizo uliyo nayo, miiko mbele ya mungu haitakusaidia…’nikasema.

‘Mo-mo-to,…’akasema

‘Moto una nini…?’ nikauliza

‘M-mtu wa-wa wa…wa…ba..ba..benk…’akasema hivyo kwa kujitahidi sana,..pumzi ilikuwa haitaki kutoka,,…na alipotamka hivyo, akatulia… nikaona machozi ya kitoka machoni mwake, …na hakuweza kuongea tena, na ikawa ndio maneno yake ya mwisho.

Docta alikuja akatuambia tutoke nje, na baadae akaja kutuambia Mtaalamu hayupo duniani tena

***********

Ikabidi tuanza safari ya kurudi ofisini, na wakati tunatoka, nikamuona mzee Mtupe…alikuwa hajatuona..nikawaambia wapelelezi hao, kuna mtu nataka kuonana naye mara moja..

‘Sisi hatuwezi kukusubiria…’wakasema

‘Hamna shida…’nikasema..huku nikielekea kule alipo huyo mzee,..huyo mzee alikuwa akitembea kwa haraka..nikawa ninamfuata nyuma, alikuwa akielekea wodi nyingine, nikawa namfuatilia, …mpaka kwenye wodi aliyokuwa akienda.

Nikatulia,….baadae akaongea na mlinzi anayelinda hiyo wodi maana ulikuwa sio muda wa kuona wagonjwa, nikaona akiruhusiwa kuingia, na alipoingia ndani nikaenda kuongea na yule dakitari.

‘Baba yangu kafika hapa, ..?’ nikauliza

‘Baba yako nani..?’ akauliza

‘Mzee mtupe..’nikasema

‘Mimi simjui mzee yoyote anayeitwa mzee Mto-pe..’akasema.

‘Docta mzee wangu kaja wodi hii,… kuna mgonjwa tunamtafuta sasa nataka kuwa na uhakika tu…’nikasema na huyo mlinzi akasema;

‘Kuna mzee kaingia hapo wodini, anamtafuta mgonjwa, msubirie akitoka utamuona..’akasema akilini nikawaza ni mgonjwa gani mwingine kaja kumuona huyu mzee, na mara simu yangu ikalia, nikaona ni mama mjane tena;

‘Unasemaje..?’ nikauliza.

‘Nasikia mtaalamu naye amafariki..’akasema

‘Nani mwingine kafariki..?’ nikauliza

‘Sina uhakika lakini…, kuna uvumi kuwa Dalali naye kafariki…ila ndugu zake hawataki kuliongelea hilo…’akasema mama mjane.

Hapo, nikajua ni kwanini mzee huyu kaingia humo, nikasogea pale alipo docta na mara kwa nyuma yangu nikaona wapelelezi wakija pale nilipo. Nikawa najiuliza hao watu wanakuja wodi hiyo kufuata nini,na niliwaacha wakisema wanarudi ofisini.


WAZO LA LEO: Tumeshajua kuwa tumekosa, kwanini hatutaki kutubu, kuomba msamaha kwa wale tuliowakosea, na huenda tumeshapata dalili kabisa kuwa dhambi ndio sababu ya mitihani tuliyo nayo, bado hatutaki kutubia,.. ..kwasababu gani, kwasababu ya mali…!!!, Je tuna uhakika gani kuwa tukiipata mali hiyo tutaweza kuitumia,…inawezekana ukaipata hiyo mali, lakini usiweze kuitumia, mwenye mamlaka akachukua roho yako..halahala jamani,..tuwahi kutubia makosa yetu, kabla milango ya toba haijafungwa, hatujui lini milango hiyo itafungwa.
Ni mimi: emu-three

No comments :