Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Monday, August 27, 2018

YOTE NI KWA MAPENZI YA MUNGU-37



‘Kuna uvumi kuwa Dalali naye kafariki….’
Hiyo ilikuwa sauti ya mama mjane iliyonifanya nihisi mwili ukiinisha nguvu…shahid muhimu kama huyu kafariki, na ndiye tulitegemea kuwa atatusaidia kutoa ushahidi…sikuweza kusikiliza mengine aliyokuwa akinieleza, maana kwa muda huo, hisia ziliniambia niangalie nyuma….

Tuendelee na kisa chetu…

************

Niliwaona wapelelezi wale wawili wakija pale niliposimama kwa mwendo wa haraka, kwa jinsi walivyokuwa wakija, nikajua kuna jambo limetokea na huenda linanihusu na mimi, na mawazo ya haraka, yakahisi hao watu wanakuja kunikamata mimi, kwa jinsi walivyokuwa wakija uelekeo wangu..lakini kwa kosa gani..nikajiuliza hivyo tu.

Wakati nawaza hayo…, yule mlinzi, ambaye awali nilikuwa nimemkweza kwa kumuita docta,… yaonekana labda anawafahamu wawili hao…, kwani nilimuona naye akiwaangalia hao wapelelezi kwa uso wa mashaka..akiwa  kaduwaa..

Wale wapelelezi walitukaribia, yule mlinzi sasa akawa ananiangalia mimi kwa kunishuku, nahisi alikuwa akiwaza ninayowazia mimi, kuwa huenda hao watu wanakuja kunikamata mimi, kama kweli anawafahamu kuwa ni wapelelezi, maana wao walivalia kiraia.

‘Umefanya nini..?’ akaniuliza huyo mlinzi, na kabla sijamjibu kitu, mara jamaa hawa hapa, mbele yangu..…

Sasa cha ajabu, walinipita mimi, wakaelekea pale aliposimama huyo mlinzi, sasa ikawa zamu yangu kutaka kumuuliza huyo mlinzi wa hapo hospitalini,..’na wewe umefanya nini’…lakini kabla mawazo hayo hayajatoka, mara mlangoni wa hiyo wodi ukafunguka na kwa haraka  akatoka mtu.

Huyo mtu kainamisha kichwa chini…, kashikilia nguo mkononi,  na kipande cha sabuni, kama vile anakwenda kufua, huku kajifunga shika na jingine kajifunika sehemu ya kichwani…nikahisi kitu kichwani,…ule utembeaji..lakini sikuwa na uhakika na wazo hilo.

Unajua hapa ni hospitalini, wagonjwa wengine huwa wanaweza kuwa kama wamechanganyikiwa, kwa muda ule hakuna aliyeshuku kitu, huyo mtu hakutaka hata kutuangalia, kwa haraka akawa anatembea, kuelekea sehemu wanapofulia nguo, kwanza akaanika nguo moja ilikuwa mbichi, nyingine akabakia nazi mkononi..na huyo mlinzi, akasema;

‘Muda huu, haturuhusu kufua ngua unasikia wewe mgonjwa, huu sio muda wake…hizi za kufua utafua baadae…’akasema huyo mlinzi, na kabla hajajibiwa na yule mtu, askari hawa wawili wakajitambulisha, maana walikuwa wamevalia kiraia, ilionekana kama  huyo mlinzi anawafahamu. Hakujali kuangalia vitambulisho vyaoa, akasema;

‘Afande ni wasaidie nini…?’ akauliza, lakini sasa macho yake yalikuwa yakimuangalia yule mgonjwa, ambaye alionekana kukaidi..sasa alikuwa karibu na bomba, ..na …

‘Kuna mgonjwa wetu kalazwa hapa, tuna haraka kidogo…’wakasema wale wapelelezi.

‘Mgonjwa wenu gani huyo.., mimi siwezi kujua hilo labda …’kabla hajaelezea zaidi mpelelezi akaendelea kuongea.

‘Huyo mgonjwa  kaletwa huku bila taarifa yetu, kuna makosa yamefanyika hivyo, sasa twataka kuthibitisha tu, tumuone  kama yupo humu au la..ni jambo la haraka kidogo…’akasema mpelelezi…sasa akielekea mlangoni, hakusubiria huyo mlinzi, aulizie kwa dakitari..

‘Ni muhalifu au…?’ akuliza yule mlinzi akimuangalia huyo mpelelezi mwingine.

‘Ni mshukiwa …wewe kamuone docta wako, lakini sisi twataka kuingia,..huyo docta atatukuta huko ndani, kama huyo mtu wetu yupo humo ndani…je huyo docta yupo wapi,..?’ akauliza huyo mpelelezi mwingine wakati yule mwingine alishaingia ndani.

‘Mhh…mimi nimeingia leo, sina taarifa za tokea jana,..unajua tena,..mimi kazi yangu ni kulinda hapa mlangoni..’akasema lakini sasa akawa anaangalia kule alipoelekea yule mtu aliyetoka humo wodini, akionyesha uso wa mashaka.

‘Hawa wagonjwa wengine bwana…sijui kaelekea wapi,..nimemuambia muda huu hakuna ruhusa ya kufua,..au hata kutoka nje..lakini hajanisikia,..sijui ni kiziwi huyu mtu…sijui ni yule mgonjwa aliyechanganyikiwa, niliwaambia juzi kuwa huyo mgonjwa hatakiwi kwenye hii wodi, unaona sasa..sijui kaenda wapi…’akasema huyo mlinzi, sasa akitembea kuelekea kule alipoelekea huyo mtu.

Haikupita muda, huyo mlinzi  akarudi kashikilia shuka…huku akionyesha uso wa kushangaa. Na mimi nikamuuliza;

‘Vipi…’ nikasema hivyo, na mimi nikiwa na mashaka fulani…

‘Yule mtu haonekani na hii shuka ndio alikuwa kajifunga, …sijui kachanganyikiwa, hata sijui..ngoja niwasiliane na wenzagu getini…’akasema sasa akipiga simu.

‘Mzee  Mtupe…’nikasema hivyo tu bila uhakika
Wkati huo yule mpelelezi mwingine alikuwa mlangoni akitaka naye kuingia, aliposikia hivyo akanigeukia, na kuniangalia…

‘Vipi kuna nini…?’ akauliza.

‘Hata sijui..hisia zangu zanitatanisha, mwenzako anasemaje huko ndani…?’ nikauliza.

Yule mpelelezi akawa kafungua mlango, akiangalia ndani…na mimi nikasema kwa sauti sasa;


‘Ni bora , muhakikishe, hatujui huyo mzee kafanya nini humo ndani, na kwanini katoka kinamna hiyo,..huenda mkakuta…’nikasema hivyo na huyu mlinzi akanikatisha na kusema;

‘Sio yule mzee bwana…huyo mzee atakuwa huko huko ndani, hajatoka…’akasema

Yule mpelelezi aliyebakia nje naye akaingia huko ndani, na haikupita muda, mmoja akatoka, na kuniangalia;

‘Mbona Dalali hayupo humu ndani…’akasema

‘Yupo nani kitandani kwake..?’ nikauliza

‘Unasema ni nani huyu mzee…, unamfahamu vyema, umemjuaje..?’ akaniuliza maswali hayo mfululizo. Bila kujibu swali langu.

‘Namjua, lakini simfahamu sana,…nilimuona akija kuelekea huku, nikawa najiuliza anakuja huku kufanya nini, na wakati namuuliza huyu mlinzi, ndio nanyie mkafika hapa..’kabla sijamaliza huyo mlinzi akasema;

‘Wewe si umesema huyo mzee ni baba yako…?’ akauliza huyo mlinzi kwa uso wa kushanga.

‘Nilikuwa nataka kujua anachofuata humo ndani, …ndio maana nikakudanganya hivyo,ila niweze kuonana naye, ..mimi nafahamu wapi anapoishi, anaishi karibu na yule mama mjane tunayefuatulia kesi yake..’nikasema na mpelelezi akasema;

‘Oh….’akasema hivyo na akawa anapiga simu yake kuelekeza watu wake, na alipomaliza, akageuka kuniangalia mimi.

‘Hebu nielezee vyema, ..’akasema huyu mpelelezi akinishika mkono kunisogeza pembeni, mabli na huyo mlinzi.
.
‘Afande utakuja kunielewa tu…mimi najaribu kuutafuta ukweli kivyangu, bila kuingilia kazi yenu, nikiwa tayari nitawaambia kila kitu.

‘Unasikia hapa tuna…’kabla hajamaliza docta akaja kwa haraka akiongozana na wasaidizi wake, wakatupita na kuingia ndani,..yule mlinzi akawa anahangaika naye kivyake kipiga simu huko getini.

‘Hajatoka mtu mzee huko getini…kuweni nauhakika,..kuna tatizo huku ndani,…ndio afande, bora uje…’akasema huyo mlinzi. Sasa akionekana kachanganyikiwa.

Yule mpelelezi, akasema;

‘Kuna tatizo kubwa,…na ni kwanini umefanya yale tuliyokukataza, unajua mimi nitashindwa kukulinda tena, mwenzangu hakuelewi…’akasema

‘Kwani mumegundua kuna tatizo  gani mkuu..?’ nikauliza, na huyo mpelelezi akawa hanisikiliza alikuwa akihangaika kupiga simu kwa watu wake…na mimi nikasema;

‘Je ningelikaa kimia haya yangelijulikanaje…, au….ila mimi sijakiuka maagizo yenu, nimefanya kazi yangu kama raia mwema, kuchunguza tukio, ili niwe na uhakika nalo, baadae nije kuwaambia.

Mpelelezi sasa akawa anaendelea kupiga simu kuwasiliana na watu wake…na baadae akaingia ndani ya wodi, bila kunisemasha kitu.. na mimi nikataka kumfuata, huyo mlinzi akanizuia;

‘Wewe huwezi kuingia ndani kwa hivi sasa..’akasema.

‘Wewe vipi, huoni tupo kazini, au unanielewaje mimi…?’ nikamuuliza, na huyo mlinzi, akawa kama hanisikiliza. Nikataka kuingia akanizuia..

‘Sasa kwanini unanizuia hujui mimi nipo na hao watu, au,..’nikasema, lakini sikutaka kubishana naye, nikasubiria tu hapo nje…, baadae nikaona askari wengine wakifika, na haikupita muda mpelelezi akatoka , sasa akiwa na docta wakawa wanaongea;

‘Anaweza kupona..?’ akauliza

‘Siwezi kuwa na uhakika,…sumu aliyopewa ni kali sana, ngoja tuone, kama haijafanya madhara yake…’akasema

‘Lakini ni nani huyo mtu, maana sio…?’ akauliza mpelelezi kabla hajamaliza docta akasema;

‘Kwa taarifa za kadi yake anaitwa..mmh…’akataja jina, halafu akamalizia kwa kusema
alimaarufu,.. Dalali…’akasema docta

‘Hapana…haiwezekani akawa ndio yeye, mimi ninamfahamu huyo Dalali, huyo sio yeye,..kuna makosa yamefanyika hapo..’akasema mpelelezi

‘Hizi hapa ni nyaraka zake, tulizozipokea na huyo mgonjwa, sasa hatuwezi kujua kuwa ndio yeye au la,…’akasema docta docta akionyesha kadi aliyoandikiwa.

Mpelelezi akaikagua ..na kutikisa kichwa cha kushangaa

‘Mhh..kuna tatizo hapa…’akasema mpelelezi.

‘Mimi sijui…’akasema Docta akichukua ile kadi yenye maelezo.

**********

Mpelelezi akawa sasa anapokea siku kutoka kwa watu wake,…na badae alipotulia,akanifuata, na kuniambia;

‘Usiondoke,…nina maswali ya kukuuliza wewe, nahisi kuna kitu unatuficha, huyo mzee katoweka watu wake wa karibu wanadai mzee huyo aliaga nyumbani kwake kuwa anasafiri, na wewe umesema umeomuona…’akasema

‘Ok, kwahiyo kwa hivi sasa atakuwa yupo safarini huko aliposema anasafiri..’mimi nikasema hivyo.

‘Tumeshaweka watu huko njiani wanafuatilia magari yote yanayokwenda huko..’akasema

‘Yeye sio mjinga, atakuwa ametafyta usafiri wa haraka ili afike huko mapema…’nikasema na huyo mpelelezi akawa anapiga simu kwa watu wake..na mimi nikasema;


‘Kwanini kwanza unasema kuna kitu nawaficha, niwafiche kitu gani mimi, wakati hili swala linaniumiza kichwa na mimii, huyo mzee nimemuona mimi mwenyewe akielea huku na nikamuona akiongea na huyu mlinzi akaruhusiwa kuingia ndani…, muulizeni hata huyo mlinzi…?’ nikamuuliza

‘Wewe ulituacha pale ukawa unamfuatilia huyo mzee, kama ndio huyo mzee kweli,…ni kama ulifahamu kuna jambo linakwenda kufanyika, hapo mimi unanitia mashaka, ulijuaje hayo yote…?’ akaniuliza

Hapo ikawa sina budi… nikamuelezea ilivyotokea tokea awali hadi nikamtuma mtu wangu wamfuatilie,  huyo mzee…mtu wangu akasema huyo mzee kaelekea huku hospitalini…nikawa na mashaka nahilo..na bahati nzuri ndio nikamuona… hapo, nikahisi kuna jambo linaloendelea;…’nikatulia

‘Ok…’akasema huyo afande hivyo.

‘Nahisi huyu mzee, alikuwa kwenye wodi ya huyo marehemu, na alipotoka huko ndio akaelekea huku…kwa mawazo mengine, yeye alitaka kumuwahi huyo mtu kabla nyie hamjafika hapa…’nikasema

‘Lakini…’mpalelezi akataka kuongea lakini hakuendelea..baadae akasema;

‘Kwahiyo inavyoonekana huyo mzee, ndiye kamnywesha huyo mgonjwa sumu, kwanini atake kumuua huyo mtu…?’ akauliza huyo mpelelezi.

‘Hiyo ni kazi yenu kutafuta, nikianza kuelezea ninavyofahamu mimi ninaweza kutunga kitabu, ila…muhimu ni kumtafuta Dalali…..’nikasema

‘Dalali, Dalali…sijui kwanini walinzi hawakuwa makin naye,…wao wanasema kwa hali aliyokuwa nayo, asingeliweza kufanya lolote ndio maana hawakutaka kumfuatilia,…’akasema.

‘Huyo mlinzi aliyekuwa anamlinda mnamuamini kweli..?’ nikauliza

‘Kwanini unasema hivyo, yule mtu wetu, hawezi….’akataka kuendelea na mimi nikamkatiza kwa kusema;

‘Ndio hivyo, kwa hisia zangu, nahisi huyo mzee, labda,…kwa hoja nyingine, labda alitumwa kuja kumuua Dalali,…lakini akakosea, lakini hapana kwanini amuue Dalali, mmh, nahisi hivi, huenda, huyo mtu alitakiwa auwawe.., ili hiyo propaganda ya Dalali kufa iaminike,… ije kuonekana kuwa kweli Dalali, kafariki…’nikasema.

‘Sijakuelewa hapo…’akasema mpelelezi.

‘Dalali aliletwa hapa, akiwa ana hali mbaya,..kwa mujibu wa taarifa za hospitalini alipokuwepo awali..kama ni kweli alikuwa hivyo, atawezaje kutoroka, na je ni kweli alifikishwa hapa,…?’ nikauliza;

Wakati huo huyo mpelelezi mwingine alikuwa akiongea na docta, na wakawa kama hawaelewani jambo….na baadae huyo mpelelezi akaja pale tulipokuwa tumesimama, …akasema;

‘Mhh,.. huyo mgonjwa hali yake ni mbaya sana, sijui kama atapona, na wagonjwa walimuona huyo mzee, aliyeingia awali,…wanasema huyo mzee, alifika akawa anamywesha huyo mgonjwa juice..maana huyo mgonjwa alikuwa hajiwezi, akawa kama anamlazimisha kunywa....’akasema mpelelezi.

‘Huyo mgonjwa alifika lini…kwa taarifa ya docta..?’ nikauliza

‘Ni jana, muda ambao Dalali alikuwa analetwa huku…’akasema mpelelezi

‘Kwahiyo Dalali hakuwahi kufikishwa hapa hospitalini, na huyu mzee basi atakuwa analifahamu hilo, au sio…?’ nikauliza

‘Ndio hivyo…aliyeletwa hapo ndio muhanga wa hiyo sumu, lakini  vielelezo ni vya Dalali…’akasema

‘Gari gani lilimchukua Dalali kule hospitalini…?’ nikauliza

‘Ni gari lililotafutwa na wanandugu sio la wagonjwa,…’akasema

‘Sasa kwanini, ,maana huyo ni mshukiwa wenu, si alikuwa kwenye ulinzi wenu au…?’ nikauliza

‘Unajua kutokana na ushahidi uliopatikana, hatukuona umuhimu wa kumshikilia Dalali kama mshukiwa, kwahiyo hata walinzi wetu, walishaondoka, tungemshikilia kwa kosa gani…’akasema huyo mpelelezi.

‘Oh, afande..afande…sasa hamuoni kuwa nyie ndio mumesababisha haya yote..’nikamlaumu na yeye akaniangalia kwa uso wa kutahayari, akasema;

‘Sisi tunafanya kazi zenu kwa utaratibu maalumu, huyo sio mhalfu, na hakuna jambo la kumshikilia kama muhalifu….’akasema

‘Sasa mumeweza kuongea na hao ndugu waliomchukua,..?’ nikamuuliza

‘Kwa kosa gani sasa…?’ nikamuuliza

‘Udanganyifu…walitakiwa wamlete huyo Dalali hapa, lakini hawakufanya hivyo, ni kwanini walifanya hivyo…hapo ndio tutaanzia kesi yetu,..maana sasa imeleta sura nyingine..hiyo ni kazi yetu, huna haja ya kuniuliza hilo swali..’akasema huyo mpelelezi

 ‘Lakini tutawakamata wote…’akasema huyo mpelelezi mwingine akiendelea kuwasiliana na watu wake.

‘Kwahiyo sasa mnasemaje, maana mliniambia hii kesi haina mshiko, je kwa haya yanayotokea bado mtaendelea kuwa na msimamo wenu huo, na..…?’ nikauliza

‘Hatujajua kuwa hili lilitokea lina uhusiano na hiyo kesi yako,. Kama tutathibistiha hivyo, basi tumeshajua kuwa kuna kesi ya kufuatilia…’akasema huyo mpelelezi. Na mara docta akafika, na kumuita huyo mpelelezi pembeni, wakawa wanaongea.

Baadae huyo mpelelezi akamuita mwenzake, wakawa wanaongea kwa muda hivi, baadae docta akaambiwa jambo, na huyo docta akaondoka kwa haraka

‘Unamuamini huyo docta lakini..?’ akauliza mpelelezi

‘Namuamini, hakuna shida, sasa hivi tutafuatilia kitu kila kitu…’akasema huyo mwenzake,

‘Kwahiyo sasa hivi tunaweza kuondoka, …’akasema huyo mpelelezi, akimgeukia huyo mlinzi;

‘Sasa wewe sikiliza…hapa atakuwepo mtu wetu..mtasaidiana naye, na…kama atakuja ndugu wa huyo mgonjwa, mwambie aongee na huyo mtu wetu, unasikia…’akaambiwa, na huyo mlinzi akasema.

‘Sawa afande…’akasema huyo mlinzi kiukakamavu sasa maana awali alishaanza kuogopa.

‘Tunakwenda wapi sasa..?’ nikauliza
‘Inabidi twende wote kituoni, kuna maswali tunahitajia majibu kutoka kwako…’wakasema na mimi sikutaka kuwakaidi, tukaelekea kwenye gari lao na kuelekea kituoni.

‘Wewe mtu wa jamii unasemaje sasa..?’ akaniuliza na mpelelezi mwenzake ndiye akamuelezea yale niliyomuambia;

‘Mzee Mtupe..huyo mzee, anataka nini..?’ akauliza mpelelezi.

‘Mimi nahisi anatumiwa, na ..yawezekana ni mpelelezi wa mshukiwa mkuu..’nikasema.

‘Mshukiwa mkuu kwa mtizamo wako ni nani…?’ akaniuliza mpelelezi

‘Kama ningekuwa namfahamu kesi hii ingelikuwa imekwisha, na siwezi kusema maoni yangu kwa hivi sasa, maana nikiyasema yanaweza yakawa hayaaminiki,..sasa hiyo ni kazi yenu au sio, na mimi siwezi kuiingilia,..ila kwangu mimi, hili tukio, ni ushahidi tosha kuwa ..hilo deni lipo nyuma ya madeni mengine nyuma yake…, au kuna jambo jingine zaidi ya hilo hilo deni, na hilo deni ni kiini macho tu..’nikasema.

‘Ukiwa na maana gani…?’ akauliza mpelelezi.

‘Je hilo deni la marehemu linaweza kuyafanya haya yote, watu wafikie mpaka kuuana, na ni watu wangapi wapo nyuma ya hilo deni,…,..hebu lifikirieni hili..mimi nahisi …kuna tatizo kubwa, na hilo tatizo nahisi limejificha huko-huko benki…’nikasema

‘Ndugu wa jamii, sisi tumeshafanya uchunguzi wa kina huko benki…kwa hivi sasa wafanyakazi wote waliopo pale ni wageni, hawajui lolote kuhisiana na mambo ya kipindi hicho, zaidi ya kumbukumbu za maandishi…’akasema

‘Hizo kumbukumbu za maandishi zina viambatishi gani vya kusaidikisha hizo taarifa za madeni..?’ nikauliza

‘Taarifa zipo, kuna nyaraka halali,na sis tumezithibitisha kuwa nihalali, hakuna ubishiwa hilo….’akasema

‘Hivyo tu…hamjiuliza ni kwanini kwa mfano madeni yawepo na nyaraka zake ziwepo, wakati huo wanadai kumbukumbu za nyuma zimeharibika…’nikasema

‘Sikiliza sisi tumefanya kazi yetu kwa mujibu wa taratibu zetu… tumejaribu kuwatafuta wafanyakazi wa zamani,..wengi tulioweza kuwapata wanakiri kuwa kweli humo benki kulikuwa na tatizo,…ndio maana wengi walifukuzwa,..na walioshitakwia wakishitakiwa,..na wengi walishamaliza kifungo…na hao waliomaliza kifungo, wengi, hawapo kwenye hali nzuri..’akasema

‘Uliwahi kuongea nao…?’ nikauliza
‘Kwa mujibu wa hao tulioongea nao, ambao wanalalamika pia kuwa walionewa, wakidai kuwa waliohusika walikuwa wakubwa wa vitengo , wao walitumiwa tu....’akasema

‘Je uliwahi kukutana na hao wakubwa wa vitengo..?’ nikauliza.

‘Hawapatikani, na hawajulikani wapi walipo…wengine walikuwa ni wageni wamesharudishwa  kwao….’akasema mpelelezi.

‘Kwa maana hiyo hata hilo deni litakuwa sio sahihi kwa marehemu, benki wanatakiwa wawajibike kwa hilo, na wanashinikiza hivyo, kwa vile kuna mtu kapewa hiyo zabuni ya kufuatilia hayo madeni, kazi yake kubwa ni kuhakikisha hayo madeni yamelipwa, sasa,..kuna haja ya kumuangalia na huyo mtu……’nikasema.

‘Hilo deni kwa ushahidi wa nyaraka na kumbukumbu zilizopo ni deni la marehemu…’akasema mpelelezi

‘Sasa kwanini haya yanatokea, mbona hamjiuliza hilo…na huyo mzabuni, atasema hiyo, na atajitahidi kuthibitisha hilo..je nyie mumefanya juhudu gani kupambana na huyo mtu..maana yeye hapo yupo kwa ajili ya pesa, akipoteza mdaiwa mmoja kama huyo atakuwa kapoteza pesa nyingi sana…je..mliwahi kumuhoji huyo mtu..?’ nikauliza

‘Ndio maana tunasema, hadi sasa hatuna uhakika wa moja kwa moja kuwa haya yanayotokea sasa hivi kweli yana uhusiano na hiyo kesi yako, kama tutapata ushahid wa kutosha basi, …tutalifanyia kazi..’akasema mpelelezi, bilka kujibu swali langu.. na wakati huo wakili wao wa kuendesha hizo kesi alikuwa anawasikiliza tu.

Baadae huyo wakili akasema;

‘Kwa taarifa niliyoipokea, mahakama inasema hukumu iliyotolewa awali ya kupiga mnada hiyo nyumba ni ya halali,…kwa mujibu wa mkataba, na kwa mujibu wa sheria, kwahiyo, zoezi hilo linatakiwa kuendelea,…’akasema wakili.

‘Lakini mwenyewe si umeona haya yanayotokea,..kama hilo zoezi litafanyika haki za watu zitapotea bure, ni lazima zoezi hili lisimamishwe mpaka upelelezi wa kina ufanyike,…’nikasema.

‘Ukumbuke kuwa ni mahakama imeamua…sasa kama kuna ushahidi wa kumshawishi hakimu,..abatilishe uamuzi wake, … nipeni, ili niweze kuweka pingamizi…siwezi kuongea maneno tu, na ushahidi kama huu ambao hauna mshiko…’akasema huyo wakili, na hao wapelelezi wawili wakaangaliana na mara simu ikalia..

‘Ndio..nani…Dalali,..kafanyaje, una uhakika, hospitali gani…na nani....…’mpelelezi akawa anasikiliza huku akionyesha uso wenye mashaka.

Tukawa tunasubiria amalize kuongea…

NB: Mambo hayo…


WAZO LA LEO: Haki ya mtu haipotei bure,…inaweza kucheleweshwa tu..hadi muda muafaka.., lakini mwisho wa siku haki itabakia kuwa haki na mwenye haki yake ataipata haki yake kama ni haki yake.

Ni mimi: emu-three

No comments :