Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Thursday, August 9, 2018

YOTE NI KWA MAPENZI YA MUNGU-30


 Tulifika kituo cha polisi…, na tulipofika tu, tukaona gari la yule mpelelezi wa awali likitaka  kutoka, walipotuona wakasimama gari, na yule mpelelezi akateremka kwenye gari lake kwa haraka akatufuata.

‘Vipi mbona mumechelewa hivyo, napiga simu yako haipatikani,….unajua kumetokea tatizo kubwa sana, na ndio hivi nafuatilia, yule mtu anajulikana kama mtaalamu katoroka…’akasema

‘Katoroka…!!, kwanini atoroke…?’ akauliza mpelelezi mwenzake

‘Yaani ni vitu vya ajabu kabisa, walinzi hawana la kusema, wao wanadai huenda walipuliziwa dawa…, wakashikwa na usingizi..na…lakini tutampata tu, na hili limenifanya nianze kumshuku vibaya huyu mtu na wenzake, maana tulishafikia hatua ya kutaka kumuachilia, …hatukuwa na kesi dhidi yake,  sasa kwanini atoroke ..’akasema mpelelezi.

‘Oh,…. huo ni uzembe…na….’akasema mpelelezi tuliyekuja naye…kabla hajamaliza kuongea, huyo mpelelezi mwingine akageuka kumuangalia Dalali,…

‘Wewe Dalali, unafahamu wapi mtaalamu anaweza kwenda, maana hajaweza kutoka nje ya hili jiji, njia zote zimehakikiwa hajatoka nje ya jiji hili…?’ akaulizwa Dalali

‘Mimi siwezi kufahamu afande…, sana sana ni huko kwa mwanamke wake…zaidi ya hapo mimi sijui…’akasema huku akionyesha uso wa mashaka.

‘Ni kwanini mtaalamu atoroke, maana sisi tulimshikilia tu kwa muda, ili kupata maelezo sahihi, kutokana na shutuma dhidi yake, na hatukuwa na kesi kubwa dhidi yake, nilitaka niwakutanishe tu, ili kulinganisha maelezo yenu,… sasa kwanini akatoroka…?’ akaulizwa

‘Mimi siwezi kujua afande..,..maana hata hivyo, mimi kiukweli sijui mumemkamata kwa kosa gani..’akasema Dalali.

‘Dalali,..kila hatua inayopita inazidi kunisukuma kwenye kuamini kuwa nyie mna makosa, sikuwa nimefikia hatua hii awali, nia yetu ni kulimaliza hili tatizo ili haki ipatikane, kwa vile deni lipo liangaliwe ni la nani hasa…sasa, naanza kuamini kuwa kuna kitu kipo nyuma ya hili deni,..na tutagundua tu….’akasema mpelelezi.

‘Mimi nina uhakika sina kosa, na ..mimi sijui kwanini huyo mtaalamu kakimbia, na kwanini afanye hivyo….kapaniki tu…, kiukweli afande mimi sijui kitu, ananitia mashaka hata mimi…’akasema.

‘Mtaalamu nirafiki yako mkubwa sana….kweli si kweli.?’ Akauliza mpelelezi

‘Nimeshawajibu hawa wenzako…yule sio urafiki yangu kivile ni rafiki wa  kikazi tu jamani, imetokea hivyo kwasababu ya shughuli zangu,…tafadhali nawaombeni msinipandikizie jambo ambalo halipo…’akasema Dalali.

‘Sawa ..umeshafikishwa hapa,..ukweli wako ndio utakaokuokoa,…na kwa ajili ya huyo mwenzako, itakubidi sasa unisubiria mpaka nirudi,..na wewe sasa utoroke…’akasema huyo mpelelezi

‘Sasa mimi nitakusubiria humu kwa vipi..eeh, yaani hata usipofika mapema ina maana mimi nilale humu kama mfungwa, hapana afande msinifanyie hivyo, mnanishikilia kwa kosa gani eeh, ngoja wakili wangu afike, sikubali ,..?’ akauliza Dalali, na huyo mpelelezi akaanza kuondoka, bila kujibu swali hilo aliyejibu alikuwa mpelelezi huyo tuliyekuja naye.

‘Kiukweli mimi ndiye niliyekuwa nikikuhitajia hapa…si nilikuambia kule wakati tunaondoka…ni kuhusiana na ajali ya marehemu kaka yako, kuna maswalii nitakuuliza…sasa haya yaliyotokea kwa mwenzako yanakugusa na wewe…’akasema mpelelezi anayeshughulikia kifo cha mume wa mjane.

‘Haya sasa mapya…yaani hamjui mnavyoniingiza kwenye hali mbaya ya kiuchumi, hivi mtailisha familia yangu, mnafahmu mimi sijaajiriwa nimejiajiri, na kipato changu chategemea kuzunguka, sina ofisi ya kusema inajiendesha hata kama sipo, jamani hebu jaribuni kinifikiria na mimi….’akalalamika Dalali

‘Tutaona hilo, …ushirikiano wako ndio utarahisha kuyamaliza haya mambo yote, na kama utatoa ushirikiani, mbona rahisi tu, wewe utakuwa huru,hatuna kosa la kukushikilia muda wote..’akaambiwa

‘Hapana, najua kabisa mlivyo, ndio maana mtaalamu akatoroka, mnamuweka mtu ndani, hammfungulii mashitaka, ..maneno yenu ndio hayo, unaisaidia polisi, mpaka lini, mtu anateseka, familia yake inateseka mwisho wa siku huna kosa,..mtamlipa nini huyo mtu….sasa sikilizeni msimamo wangu utakuwa ni ule ule… mimi sitajibu swali lolote kutoka kwenu, hadi hapo wakili wangu atakapofika…’akasema

‘Sawa,mimi nitakuuliza maswali, ukikaa kimia, nitaweka maelezo yangu,…na nitaendelea kukuuliza mpaka hapo utakaponijibu,… na Dalali, sisi hatutaki tu,..tukitaka utaongea tu,…’akasema mpelelezi na Dalali akamuangalia mpelelezi huyo kwa mashaka.

‘Lakini sisi kwa uungwan wetu, tunakupatia nafasi ya wewe kujituma , kushirikiana na sisi, ….unajua Dalali, lengo langu mimi, ilikuwa tu,… ni kumalizia uchunguzi wangu, kuhusiana na kifo cha kaka yako…’ akasema mpelelezi

‘Vyovyote iwavyo, mimi sitajibu swali mpaka wakili wangu awepo, ndio msimamo wangu…’Dalali akagoma kuongea

******
Ni siku ya pili nikafika kituoni, nikitokea hospitalini, kumuangalia mama mjane, ambaye alikuwa kumbe kesharuhusiwa, jana hiyo hiyo..jana hiyo hiyo alizindukana, na kuomba kurudi nyumbani, na kwa vile nilihitajika kufika kituoni, sikuweza kwenda kuonana naye tena…kuna ndugu yake alifika kumsaidia.

Nilipofika kituo cha polisi nikaambiwa nisubirie kwanza, kwani Dalali anamsubiria  wakili wake na amesema hawezi kuongea jambo lolote mpaka awepo huyo wakili wake , lakini baadae nikaambiwa huyo Dalali anataka tuonane naye.

 Niliingia  kwenye chumba maalumu cha maongezi, na humo sikumkuta mtu baadaye kidogo, Dalali akaletwa na askari, nilishangaa kidogo kwa jinsi alivyowekewa ulinzi wa namna hiyo, labda ni kutokana na kutoroka kwa huyo mtaalamu;.

Dalali aliponiona  akajitahidi kutabasamu, ile ya dharau, japokuwa ya maumivu, alionekana uso umakunjamana, nahisi ni kutokana na hali ya humo ndani,…yeye ndio akaanza kuongea;

‘Ndugu yangu….,  umakuja sio, nimewaambia wewe naweza kuongea nawe, wala sijali kitu…japokuwa mimi nakutupia lawama wewe,  kuwa wewe ndiye chanzo cha haya yote. Sawa mimi mimi wamenishikilia hapa, nimekubali kuyabeba haya mateso kwa ajili ya familia yangu na marehemu..lakini kwanini, kosa langu ni lipi…, nataka wewe unijulishe hilo, kosa langu ni lipi, eeh, nimefanya dhambi gani..?’ akaniuliza

‘Kwani  mimi ndiye nimekuweka ndani, ungewauliza hao polisi, uliona nilivyokuwa nafanya kule nyumbani, nilitaka tuongee tu, tutafute uhalali wa hilo deni, hukutaka kusema ukweli,…huo ndio ukweli, hujasema ukweli… kuna kitu unatuficha…’nikasema.

‘Kitu gani nakificha ndugu yangu,… eeh, niambie….au labda unahisi hili na hili, kuwa labda mimi nahusika na hilo deni, au…niambie hivyo ili mimi nijue, nahusika kwa vipi, haiji akilini, mimi nihusikanaje na deni la benki…hebu tumieni akilizenu vyema jamani…’akasema

‘Nafsi yako inalifahamu hilo zaidi yangu mimi,..ila kiukweli unachosema sio sahihi, nimekuuliza maswali mengi, ukawa unadanganya,..na kwa ushahidi mbele ya polisi,sasa kwa ushauri tu, Dalali hebu kuwa mkweli, usisubirie hadi hali iwe mbaya zaidi, milango ya toba ikifungwa, utaumbuka, na sijui itakuwaje…’nikasema

‘Niliwaeleza ni kwanini niliongea vile,...ni kawaida, hata afande alinielewa, wakati mwingine inabidi uongee vile, ili kulinda masilahi yangu, lakini sina jingine zaidi ya hayo, sijui lolote kuhusu hilo deni zaidi ya huo ushahidi wa polisi,..huo ndio ukweli na ndivyo nitakavyosema popote pale…’akasema

‘Jana shemeji yako kapoteza fahamu, unajua ni kwanini alipoteza fahamu..?’ nikamuuliza, nay eye akatabasamu, halafu akaniangalia moja kwa moja usoni…

‘Mizimu hiyo,…imeshaanza kurejea hakuna zaidi pale…’akasema.

‘Mbona kaponea hospitalini, bila hata kutumia hizo dawa zako…’nikasema.

‘Unajuaje kuwa sikufanya dawa, kuna vitu alinifundisha mtaalamu ikitokea hivyo nafanya vipi, shemeji sio lengo sana la kutoa ujumbe wa mizimu, mizimu wao walilnga mtoto, unajua ni kwanini, ni kwasababu yeye atagusa hisia za wengi, na yeye ndiye damu hasa ya marehemu, shemeji...anatikiswa tu,...ndio maana nilipowaomba hao mizimu, walikubaliana na mimi, wanatupatia muda…’akasema.

‘Hahaha, Dalali..unajua unaongea sana, hivi huogopi kudanganya, unataka nini hasa, mali, utajiri...Dalali, Dalali, kumbuka haya maneno yangu....haki ya mayatima na wajane, ni bomu ulilolilalia..likilipuka, huponi,..’nikasema.

‘Ndio hapo tunapokosana mimi na wewe, mimi nawajali wale watoto kama watoto wangu, kawaulize kama hawatakuambia, wale watoto wananipenda sana mimi, nawajali ..hata mama yao,...sasa huko kunishutumu hivyo, sijui inatokea wapi,..ni kuhusu hiyo nyumba, ndugu yangu, nikuelezeje ili upate kunielewa, sio mimi,..ni benki..huo ndio ukweli,’ akasema akionyesha kuchoka.

‘Unajua ni kwanini shemeji yako alipoteza fahamu..ngoja nikuambie ukweli wake, ...na nilishangaa pale ulipofika na kukimbilia kashfa, unaonaeeh, ndio maana alichelewa huku nyuma, kumbe ndio hivyo, mnashikana kimahaba, ...Dalali, usifikrie watu wote wapo kama ulivyo wewe...'nikasema

'Ni hali ilivyojionyesha pale...'akasema

'Kuwa humuamini shemeji yako hadi ufikie kumkashfu, tuombe mungu hakuyasikia hayo maneno yako machafu, ...maana pale alishapoteza fahamu, hata hivyo, inakubidi wewe mwenyewe umuombe msamaha kwa kauli zako chafu…’nikasema.

‘Kwa jinsi mlivyokuwa pale, kwa yoyote yule angeliwafikiria hivyo, najua nimekosa,...kwa hilo mimi mwenyewe  nitamuomba shemeji,anisamehe…lakini…mimi na wewe tutawindana kama paka na panya, umeshatangaza uadui na mimi..’akasema.

‘Mimi sijui hilo…kwanza nikuulize huo uadui ni wa nini..kwasababu ya kuutafuta ukweli eeh?...ndio hapo naamini, kuwa ukweli na uwongo huwa haviivani, au sio.?.haya niambie umesema unataka kuongea na mimi, ni kuhus nini…?’ nikamuuliza.

‘Si nimeshakuuliza, mimi nina kosa gani, mpaka nafikia kushikiliwa hapa…?’ akauliza.

‘Jibu lake nimeshakupatia, au sio, waulize polisi waliokuleta hapa…’nikasema.

‘Sio kweli ndugu…kuna zaidi ya hilo, ..’akasema.

‘Zaidi ya hilo ni…wewe umekataa kutoa ushirikiano, kwanini unakataa kusema ukweli, kwanini unakataa kuhojiwa tu, na sasa unadai mpaka wakili wako awepo, huoni kwa watu kama hao, watakuwa wanakutilia mashaka…’nikasema

‘Sikiliza sasa nikuambie jambo moja, mimi nitatoka hapa, na kila kitu kitafanyika kama mahakama ilivyo taka, na sio mimi,…ni mahakama, na sio mimi, ni bro, ni deni lake lilipwe, na mimi kwa hilo nitapambana na kila mtu anayenizuia, siwezi kukubali kaka yangu ateseke huko alipo…, eti kwa vile kafariki, hapana lazima hilo deni lilipwe….’akasema akijikuna, suti ilikuwa imejikunja kunja.

‘Ni kweli kama ni deni lake la halali, litalipwa, na tutajitahidi kuongea na watu benki tuone jinsi gani watasaidia hilo…lakini kabla ya hapo, ni lazima tujirizishe, au sio….na…na…hadi hatua hii , kwangu mimi naona hilo deni sio halali kwa marehemu…’nikasema

 ‘Sawa, kama umeona hivyo, mimi sikupingi, ila sasa, kwa nia njema tu, toa ushahidi, ili tuweze kulimaliza hili, mimi sina tatizo na hilo..sio kwamba nalazimisha hapana, ushahidi upo wapi…eeh, niambie…’akasema

‘Hatua kwa hatua,…ushahidi utatolewa, na ushahidi mwingine utakuja kujitoa wenyewe bila hata ya kutumia nguvu, nina imani hiyo…’nikasema.

‘Maneno matupu hayatasaidia ndugu yangu, wewe mwenyewe unafahamu utaratibu wa kimahakama…. hebu nielewe ndugu yangu…, mimi nipo tayari kusaidia hapo, kama utapatika ushahidi… lakini sio kwa maneno, mimi nilikuwepo mahakamani, wao wanahitajia ushahisi, …sasa unao, sijui kama tunaelewana hapo…’akasema

‘Ushahidi utakuwepo, wa kimaandishi na mashahidi, na mimi nilishakuambia wewe ni mmoja wa ushahidi wangu..hujanielewa tu…’nikasema

Dalali akaniangalia, akionyesha uso wa kukata tamaa, baadae akasema;

‘Sasa kuna jingine ambao nilitaka kukuambia… . ile familia ilikuwa ikinitegemea mimi,  nibangaize huku na kule, ndio ipate kula, mama mjane na watoto wake,.ni watu wa kuhudumiwa, eeh..unanisikia sana…’akasema na mimi nikabakia kimia

‘Sasa kwa vile mimi nimeshikiliwa hapa,..hilo sasa ni jukumu lako, hakikisha ile familia inapata kula, na huduma zote za msingi…unasikia ndugu ?….ndio hivyo, ili muone ni  kwa jinsi gani nilikuwa napata shida, …mimi ndio ilifikia nifanye hata yale yasiyofanyika, watu hawajui tu…’akatulia kidogo.

‘Je kama ulikuwa unaionea huruma kihivyo,..hiyo familia mbona unaacha wanafukuzwa kwenye sehemu yao halali ya kuishi , na unashabikia kwa nguvu zote , hiyo nyumba yao ipigwe mnada….au ulitaka uwapatia nyumba yako moja wapo,..kama umeweza kumjengea hata bibi yako wa nyumba ndogo,sizani kama utashindwa hilo,…’nikasema  kama utani na yeye akacheka, akitikisa kichwa

‘Wewe mjanja sana wewe,  eti nyumba ndogo, acha hiyo kabisa…najua unaelekea wapi….hahaha hunipati ng’ooo…’akasema sasa akipiga miayo, na akawa ananyosha-nyosha tai yake vyema, halafu, akaniangalia na kusema;

‘Dalali nikuulize jambo…sio kuuliza, bali ni kukushauri je …upo tayari kutubu dhambi zako, ukausema ukweli wote, kuhusiana na hilo deni, ili haya mambo yaishe kwa haraka….?’ Kwanza akatabasamu, halafu akanikazia macho na kusema;

‘Kutubu dhambi,…hahaha, dhambi gani hiyo.., eeh, mimi sina kosa wamenishikilia hapa bure tu, na mim nitawashitakia kwa hili, yaani kutii amri ya mahakama ndio nipata adhabu hii, nitamuuliza hakimu, je mimi kufanya hivyo, kutii amri yake nimekosa nini…’akatulia kama anasubiria jibu kutoka kwangu, na mimi nikawa nimetulia tu, halafu kwa sauti ya chini, akaniuliza

‘Hebu hata wewe niambie mimi nina kosa gani hapo… , maana haya yote umeyaanzisha wewe…na sio mimi , kiukweli wanaoharakisha hilo ni watu wa benki, mimi naingia hapo kwa vile mizimu imenijia na kunihakikishia kuwa hilo deni ni la marehemu..sasa ulitaka mimi nifanye nini hapo eeh, nia-ambie..?’ akauliza akinikazia macho.

‘Hivi hukusikia kuwa mtaalamu katoroka, hebu jiulize ni kwanini akatoroka, na kabla ya hapo alishahojiwa, je unajua aliongea nini, na baada ya kuhojiwa sana, hadi kufikia kuongea ukweli…sasa aliongea hadi polisi wafikie kukuleta huku kituoni…? ‘ nikamuuliza , akacheka kweli kweli, halafu akatikisa kichwa, akasema

‘Mtaalamu katoroka kwa vile anaona anateseka bure, na polisi hawawezi kumuachia kirahisi…hawana jipya hawa watu, hwana shitaka dhidi yaken hali kama hiyo, ..hata ingelikuwa mimi, …kama kuna upenyo huo..wa ku-roka aah.., kwanini nisitoroke, sema yeye anaweza kutumia utaalamu wake, mimi siuwezi huo huo utallamu wake unaoneeh….’akasema hivyo

‘Ni hivi ngoja nikuambie ilivyotokea kwa mtaalamu..’nikasema

‘Hadithi….’akasema hivyo, na mimi sikumjali nikaendelea kuongea

‘Mtaalamu alipobanwa sana na maswali na mbinu za kipolisi, akaongea mambo mengi tu…, na aliyoyaongea, anajua yatamuweka yeye matatani, na kwa vile kaambiwa mtakutanishwa wewe na yeye, akaona sasa keshakusaliti, ndio akaamua kutoroka…’nikasema

‘Hahaha…kaongea mambo gani ya kunisaliti mimi…?’ akauliza

‘Kuwa wewe unafahamu kuhusu hilo deni, ..wewe ulifika kwake, kuomba yeye afanye mambo yake ili hilo deni liendelee kuwa ni la kaka yako,..alipoulizwa hilo deni hasa ni la nani, akasema wewe ndiye unafahamu ukweli wa hilo deni…, wewe hukutaka kuusema huo ukweli kwake…, ila wewe ulitaka ifanyike namna deni hilo liwe ni la marehemu, zifanyike hujuma za kushinikiza, na ndio hivyo, nyumba ipigwe mnada,…’nikasema.

‘Hahaha, wewe mtunga hadithi kweli….lakini kiuhakika hiyo hadithi yako, haijakaa vyema kabisa, ifikirie tena…..mtaalamu haweza kuogopa kukutana na mimi, …na kwanini asingeliniambia hilo hata kwa simu, kuwa kafanya hivyo…kwahiyo  hayo maneno yako umeyatunga wewe, yeye hajasema hivyo…’akasema.

‘Wewe kwanini hujiulize ni kwanini akatoroka,…..ina maana yeye hafahamu kosa la kutoroka polisi lilivyo kubwa, kama kweli hana kosa…?’ nikauliza.

‘Tutakuja kulifahamu hilo…ngoja wakili wangu afike, maana analifanyia hilo kazi, na mimi mwenyewe nitakuja kuufaham ukweli wote…’akatulia kidogo

‘Ndugu yangu,..unapoongea hivyo, kuwa sijui eti mimi nafahamu ukweli wote kuhusu hilo deni, eeh, ina maana wewe unawafanya benki ni wajinga, hawana kumbukumbu za uhakika, haah, ndugu yangu wewe, fikiria hadithi nyingine sio hiyo…’akasema.

‘Dalali wewe una nyumba ngapi…?’ nikamuuliza na hapo akashtuka kidogo, halafu akatabasamu, akatikisa kichwa na kusema;

‘Unaona…wewe hadi hapo huna hoja tena…, sasa unakimbilia kuangalia mali zangu, unatakia nini hilo…nikiwa na nyumba moja au mbili inakuhusu nini…’akasema

‘Inanihusu sana, maana shemeji yako alipofahamu kuwa wewe una nyumba tatu za kifahari, ulizopangisha mashirika , nyumba moja umemjengea nyumba ndogo yako, na wewe unaishi na ile nyumba, ile nyumba yenyewe unayoishi, ni ya gharama sana, shemeji yako…alishtuka sana, …’nikasema hivyo na Dalali, nikamuona akihangaika.

‘Ina maana..umemdanganya shemeji…ku-ku---wa..’kabla hajamaliza mlango ukafunguliwa, na jamaa mmoja mwenye suti kali, aliingia mkononi kashikilia briefcase yake,…naona ni jamii za akina Dalali, watu wa kujiona

 ‘Karibu wakili wangu…’akasema Dalali akijaribu kuwa na tabasamu mdomoni na mimi nikasema;

‘Hatakusaidia kitu,…ukweli wako ndio utakusaidia,…kumbuka hujajibu swali langu…’nikasema

‘Muheshimiwa,…karibu, sana…’akasema akisimama kusalimiana na huyo jamaa.

Mimi nikawa bado nimemkazia macho Dalali.

Na kabla huyu jamaa hajapata muda wa kuongea, mara mlango ukafunguliwa, akatokeza askari mmoja, na kutuangalia, hakusema kitu..

NB: Kazi imeanza, je kuna nini kwenye haya yote; nyumba, kupoteza fahamu kwa mama mjane..na kutoroka kwa mtaalamu?


WAZO LA LEO: Tunaweza kuuficha ukweli kwasababu ya masilahi madogo tu, tukasahau haki za watu wengine,..tukashindwa kuwa na hata huruma na jinsi gani watu hao wanavyoteseka, kwa kukosa haki zao, na huenda haki hizo zingeliwasaidia wahanga hao kwenye haja zao muhimu, ikiwemo matibabu, na mengineyo, na huenda kwa kukosa haki hizo wengine watafikia kupoteza maisha, kwasababu hiyo tu….huwezi jua,..je utawezaje kulilipa hilo deni mbele ya mola. 
Ni mimi: emu-three

No comments :