Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Tuesday, August 7, 2018

YOTE NI KWA MAPENZI YA MUNGU-29


‘Wakili wako atakukuta huko huko  kituoni, mimi sina muda tena wa kupoteza hapa,…unasikia Dalali…’akasema mpelelezi akitumia sauti yake ya kikazi zaidi.

Dalali, akajua sasa hana la kufanya, …na akawa anataka kuongea, mpelelezi akamkatiza kwa kusema;

‘Unajua nilipofika hapa, nilitaka mazungumzo yangu ikibidi yaishie humu humu ndani, japokuwa kulikuwa na shinikizo jingine…’akasema mpelelezi akimgeukia mama mjane.

‘Nilijua haya mambo yanaweza kuisha kifamilia zaidi,  lakini kwa vile nimeona nyendo zisizo za kawaida,  basi twende hivyo hivyo unavyotaka wewe…’akasema mpelelezi sasa akimshika mikono Dalali na Dalali hapo akawa hana jinsi bali kukubali, lakini kabla hajaanza kutembea kutoka nje, akageuka kumuangalia shemeji yake akasema;

‘Usijali shemu, haya yatakwisha…mimi sina kosa lolote , hawa wanajisumbua bure, muhimu ni deni lilipwe, hilo nitalipigania kwa nguvu zote, najua hilo ni dhima kwangu, na kama ikitokea mtoto kuumwa tena, wewe tumia hiyo dawa, itamsaidia tu…’akasema.

‘Sawa shemeji, jichunge tu..na uwe mkweli…’akasema mama mjane.

‘Ahsante,…usijali, nitakuwa mkweli kwa ajili ya familia yetu, mimi ndiye nimeachiwa majukumu yote na Bro, hawa watu hawajui tu…’akasema na kuanza kutembea kutoka nje. Na mpelelezi alipoona mimi nimebakia nyuma akasema kwa sauti akiwa huko huko nje…

 ‘Wewe mtu wa jamii, twende, ni lazima na wewe ufike huko kituoni, umesahau kuwa na wewe unahitajika huko …’akaniambia mpelelezi

‘Nakuja afande, ngoja niweka mambo mengine sawa, nivumilieni kidogo tu…’nikasema

‘Haya nakupa dakika tatu…’akasema mpelelezi

‘Anataka kufanya nini na shemeji yangu,…’akasema Dalali,

‘Ingia kwenye gari….atakuja…’nikasikia sauti ya mpelelezi sasa ikitoa amri.

Tuendelee na kisa chetu

**************

Mimi huku ndani,  nikamsogelea mama Mjane, kama vile sikutaka sauti yangu isikike huko nje maana mlango ulikuwa wazi,…mama mjane alikuwa kasimama huku akiangalia kule mlangoni, na alipoona nimemsogelea akaniangalia kwa mashaka kidogo….

‘Shemeji…oops, Dada…mambo sasa ndio yameanza hivyo, hakuna kurudi nyuma tena, kama na lolote la kuniambia muda ndio huu…’nikasema

‘Kama lipi, mimi nimeshakuambia kila kitu, au…?’ akaniuliza akiniangalia kwa macho ya kujiiba iba.

‘Ni hivi, wewe…, jaribu uwezavyo, sijui kwa vipi, lakini jaribu kwa kadri ya uwezo wako, ukijua hili ni pambano muhimu kwako, jaribu, na jaribu,…kumbuka kila kitu, ..chochote chaweza kusaidia hii kesi,… usiogope kusema kitu chochote, unanielewa, huwezi jua,…? ’nikasema.

‘Sa-sawa..lakini…’akawa anataka kuongea jambo lakini anasita kuliongea.

‘Lakini nini….usiogope kabisa, sasa hivi hakuna cha mizimu au uchawi wao, mtegemee mungu tu, hayo yalikuwa mambo yao ya kutishia watu, huyo mtu wako kabanwa, na kitisho alichokipata huko, sijui tena..kama yakitokea tena basi kweli yaweza kuwa hiyo mizimu, lakini sio kwa kupitia kwake,…na inavyoonekana mtaalamu ana kitu kinahusiana na hili tatizo, deni…bado nashindwa kuunganisha, lakini tutakuja kuona,…’ nikasema.

Nilipoongea hivyo huyo mama mjane akageukia kuangalia kule mlangoni, nikahisi huenda hayo majinamizi yamemrudia tena, kwa jinsi alivyokuwa akiangalia sana huko nje....lakini….

‘Mimi ninawasiwasi sana na hao ndugu zake shemeji…’akasema mama mjane, na hapo ndio nikamuelewa ni kwanini yupo vile.

‘Unaogopa lawama au sio…mbona bado haupo makini kuna nini unakiona…?’ nikauliza

‘Ndio,…wewe huwajui hawa watu walivyo,…’akasema.

‘Je inajalisha kitu, ni hilo kuhusu hao watu au kuna kitu kingine hujaniambia shemeji , maana mimi sasa nakwenda vitani, na wewe ndiye msaidizi wangu…’nikasema

‘Hakuna kitu kingine ni kuhusu hiyo familia ya akina shemeji,..inabidi nifanye jambo,..niwapigie simu…’akasema

‘Ok, sawa…na je ukiwapigia simu utawaambia nini, kuwa shemeji yako kakamatwa kwa kosa gani, inatakiwa afikishwe huko na huko watasema wamemchukua kwa kosa gani, au…?’nikasema na kabla hajajibu nikaendelea kusema;

‘Sawa sio mbaya unaweza kuwapigia tu…ila nikuuliza jambo, hivi tangia haya matatizo yatokee, wao kama ndugu wanakusaidia nini…?’ nikamuuliza.

‘Hakuna wanachonisaidia, wao ni lawama tu, wengine ndio hufikia kunisema vibaya kuwa haya nimeyataka mimi mwenyewe, mara nimemriuni hata huyu shemeji, haambiliki tena, yaani binadamu mie nina damu ya kunguni…’akasema

‘Umeona eeh…lakini wapigie tu…’nikasema

‘Nimewaza sana hilo…she-..kaka yangu, huyu Dalali ni mtu mwema kwa kweli, amekuwa akinisaidia bila kujali maneno ya ndugu zake, yupo tofauti na ndugu zake kabisa…, amenisaidia pale nilipohitajia msaada , kwahiyo kwangu mimi nashindwa kuelewa, itakuwaje,…je ndio …sijui unanielewa hapo…’akasema.

‘Lakini moyoni mwako unahisije, kuwa …huyu mtu hana hatia, au ana hatia…je unavymjua yeye alivyo, kweli …eeh, hawezi kufanya lolote baya, dhidi yako , hasa kwenye hii nyumba, au…hahusiki kwa lile,..kwa jinsi ulivyomsikia nikimuhoji…?’ nikamuuliza.

‘Aaah, sasa atahusikanaje maana yeye ndiye ..katika kusaidia kashika nafasi ya marehemu, katika kuwajibika na hii familia, mimi kama mimi siwezi kumshuku yeye,…huenda wapo watu wanamtumia,…sijui , nasema tu, huenda….naah…na-na kwa tamaa zake ndio kajiingiza huko, lakini kwanini afanye hivyo..nashindwa kusema lolote baya dhidi yake..’akasema

‘Nikuulize tu dada,…usinielewe vibaya, …Dalali hajawahi kukutamkia neno, kutokana na tamaa zake, neno la mapenzi..?’ nikamuuliza na hapo akashtuka, na akatikisa kichwa, halafu akasema;

‘Khaa, kwanini unasema hivyo…Dalali, japokuwa alikuwa mkubwa…walikuwa wakiishi hapa, wakawa wananiheshimu…mimi namzidi umri, na …ndio namfahamu alivyo, nimekuwa nikimkemea sana, ana tabia hiyo ya tamaa, ..na, na…uhuni siwezi kukuficha hilo, lakini ilikuwa ni ujana,…’akasema

‘Hahaha, shemeji…oh, unajua ushemeji umekaa zaidi ya udada, unamtetea sana shemeji yako, hapo kiushahidi yaonyesha ana nyumba ndogo, …unajua nikuambie kitu dada,  tabia na hula za watu hazijifichi, .ok, hebu niambie kwa tabia hiyo ya tamaa na uhuni, tuseme hivyo, yeye hakuwahi kukutongoza…?’ nikamuuliza

‘Mimi naona …sipendi kuyaongea hayo, ila naweza kusema ujanahuwa unakuwa hivyo…’akasema.

‘Dada nina maana yangu kubwa sana kukuliza hilo, nimekuambia kila kitu kinahitajika usikizarau, je aliwahi kukufanyia hivyo,..?’ nikamuuliza

‘Ndio…aliwahi na nilimfokea sana, akajuta sana, na alijua labda nitamuambia kaka yake, lakini sikuwahi kufanya hivyo, nilijua ni ujana…wakati mwingine nilikuwa namfuma akichungulia mlangoni,..sasa vitu kama hivyo, mimi na akili yangu nitasemaje..ni ujana, namkanya , na kumsihi,…’akasema na niliona alijisikia vibaya kuongea hayo, yaonekana hakutaka kuyasema hayo.

‘Nakuelewa sana Dada, unajua nataka unifahamu, kwanini nakuuliza haya, tabia ya mtu hujengeka na hulka yake, tokea utotoni, ujanani…..kuna matendo yanajijenga hivyo, yapo ya kihulka, wengine hujidhibiti, jinsi umri unavyokwenda, wengine wanashindwa, vitu kama wivu,.uwongo, uhuni nakadhalika, haya yanaweza kuleta picha ya mtu alivyo..’nikasema.

‘Lakini kwangu mimi niliona kuwa ni ujana tu, na tokea siku ile …aliniogopa sana….nahisi ni kwa vile alijua labda, nitakuwa nimemuambia kaka yake au nitamuambia kaka yake…na ingelitokea hivyo, , ningekuwa na tabia ya kuwachukia, …wangeondoka hapa mapema sana, kaka yao hataki mchezo, kuna maswala ya kusamehe, alishawaambia, lakini, wizi…umalaya, ushirikina,…mmh..’akasema.

‘Je katika maisha mengine, maana hapo kuna wizi, na uwongo..…hajawahi kukushawishi jambo, …au kufanya jambo la aina hiyo, na ikafikia hadi kumkalisha chini na kumkanya, jambo ambalo sio la kawaida…kufanya kitu kama hicho,….’nikaachia hapo.

‘Kama nilivyosema huyu mtu nimeishie naye…alionyesha tabia kama hizo, lakini kwa kulinganisha , yeye alikuwa na afadhali sana, nilimweka vizuri, akaja kuwa tu mwema kabisa,…kuna kipindi niliamua kuwa naye karibu sana, ili kumbadili…mpaka watu wakanishisi vibaya…sikuwa na nia mbaya…’akasema

‘Je aliwahi kukushauri kitu, mfano kakosea, …au kutokana na tamaa, kuwa mfanye jambo,kinyume na matakwa ya mumeo,…sisemei mambo ya mahusiano hapo, nazungumzia, tabia nyingine,…?’ nikamuuliza.

‘Kuna kipindi alikuwa na shida kubwa sana…karibu afungwe…akaniomba nifanye jambo, ili aweze kupata pesa, kwa kupitia kwa kaka yake, …maana asingeliweza kumuambia kaka yake kitu kama hicho,….na mimi nilikuwa kama mzazi wao, mtu wao wa karibu wa kulilia shida zao…lilinipa shida sana hilo tukio….’aliposema hivyo, moyoni nikasema safi kabisa.

‘Hebu niambie hapo…ilikuwaje,….kuna kitu hapo tunaweza kukiunganisha kikatusaidia…’nikasema na hapo nikaona mdada akinywea, nahisi alijuta kwanini kaniambia.

‘Lakini nilimpinga sana, sitaki kwenda kiundani ilikuwa ni kitu gani, tafadhali nielewe, ..na mimi…nikatafuta mbinu nyingine za kumsaidia, nikakopa kwenye vikoba, nikawa nakatwa, kidogo kidogo, na likaisha hivyo, kutokana na hilo, akawa ni mtu anynijali sana,..sasa mimi siwezi kufahamu zaidi kama kuna mengine ,na yangelikuwepo ningeyafahamu…’akasema.

‘Dada…niambie ukweli…mume wako hajawahi kukulamikia lolote kuhusu maswala ya benki, kupotea pesa, na kitu kama hicho..?’ nikamuuliza na hapo akabakia kaduwaa kidogo, kama anatafakari.

‘Mhh…mume wangu ni msiri sana hasa kwa ndugu zake..wakikosea jambo, yeye alikuwa akiwaita sirini, kwenye maktaba yake, atamsema wa kumsema, na hapendi kuwaita wengi, ni kila mmoja kwa zamu yake, alikuwa hapendi kabisa kumsema mtu mbele ya watu wengine,…’akatulia

‘Na wewe ukikosea ilikuwaje..?’ nikamuuliza , na hakuelewa lengo la swali langu akasema;

‘Hata mimi nikikosa, atatafuta nafasi, hata kunitoa nje, anaweza kusema anataka tukale nje, hotelini, huko mtakula, baadae unaanza kukuambia hilo jambo, atakusema weee, kiukweli mume wangu alikuwa mtu wa peke yake, nilimpenda sana…na hata sijui kama atatokea mtu kama huyo,…kiukweli, hapana …’hapo machozi yakaanza kumtoka.

‘Naelewa …umemkosa mume muhimu sana katika maisha yako…’nikasema

‘Kiukweli hapa nilipo nimekufa nusu… isingelikuwa watoto wangu, niliona ni heri nimfuate tu…kiukweli..nilijaribu hata kujiua..lakini nilipofikiria watoto wangu..nikashindwa,…nilikimbilia kunywa maziwa… sasa hebu fikiria hii hali, nipo hai wanafanyiwa hivi, je ningekuwa sipo ingelikuwaje…’akasema.

‘Sawa dada..ila nikuulize tu, wewe kwa uoni wako, huoni kuwa shemeji yako, anaweza kuwa kaungana na huyo mtaalamu, ili kufanikisha hili tatizo….?’ Nikamuuliza.

‘Mimi sijui..ukisema hivyo, unataka mimi nimuhisi shemeji yangu uchawi…maana kama ni kweli wanahusika hivyo,..basi watakuwa ni wachawi, kama ni kweli, sijui kama nitawasamehe,..hapana shemeji yangu hawezi kufanya kitu kama hicho…’akatulia.

‘Nakuuliza tena, wewe kwa jinsi ulivyoona, ..haiwezekani ikawa hivyo, kuwa kuna kitu shemei na huyo mtaalamu wamefanya pamoja,..nataka kufahamu msimamo wako hapo…’nikasema

‘Ni tamaa ya kupata pesa, kwa vile hilo deni lipo, ila…siamini kuwa ni deni la marehemu mume wangu…’akatulia

‘Sasa kwa vile  eeh,…deni lipo, labda ni makosa ya benki..mimi sijui…, japokuwa kiukweli ilivyo kwa benki, ni ngumu sana kutokea kitu kama hicho, sasa sijui ilitokeaje…, nashindwa kuamini hilo pia,…’akatulia.

‘Sasa kwa vile hilo deni lipo na wameona hivyo..kwa ushahidi wao kuwa ni deni la marehemu, na wao wanataka pesa yao irudi wao watafanya nini…, ndio wakafikia hapo kuwa hii nyumba ipigwe mnada,…sasa huyu Dalali anaingiaje hapo, ninavyohisi mimi, yeye anaingia hapo kwa vile anataka na yeye afaidi huo ujira wa mnada…’akasema

‘Unaamini hivyo,…kuwa yaweza kuwa hivyo…mhh…hapana, ni kiasi cha gharama ya kupiga huo mnada, sizani kama ni pesa nyingi hivyo, za kutolewa macho na watu wengi hivyo…mhh, anyway…nimekuelewa…’nikasema hivyo.

‘Hawa watu walivyo, wanafanya kazi kwa asilimia ya lile deni…na huenda kuna zaidi ya hapo, waliahidiwa hivyo na benki, …hapo siwezi kujua,…ulipoongea hapo, hata mimi najiuliza kwanini awaambie watu wengi, …mmh, hapo hata mimi naanza kuingiwa na mashaka…’akasema mama mjane

‘Umeona eeh…ni zaidi ya ushuru wa mnada,..ni zaidi ya …kulipwa deni lenyewe, maana deni litalipwa benki, wao hawawezi kupata sehemu ya hilo deni, …sasa ni kitu gani kipo nyuma ya hilo deni…ndio maana nataka wewe ufikiria sana, ukumbuke sana..unanielewa…usinione hivi, kuwa namuandama shemeji yako bure…nahisi kuna jambo…’nikasema.

‘Mhh….mimi sijui zaidi ya hapo…nifanyaje sasa…?’ akauliza

‘Sasa hivi wewe wapigie hao ndugu zake simu…waambie Dalali kachukuliwa kituo cha polisi, wakikuuliza kuhusu nini, waambie hata wewe hujui kitu…usiongee sana…’nikasema

‘Ina maana polisi wameshagundua kitu, kuwa huenda shemeji anahusika na …na, lolote lile kuhusiana na hilo deni,…?’ akauliza  mama mjane

‘Kiukweli siwezi kujua hilo, hawajaniambia bado, ila..…kiukweli shemeji yako amejitahidi sana, kukuonyesha kuwa anakujali…amejitahidi kwa vile anakufahamu, udhaifu wako…ila uelewe kitu hapo, nafsi ya mtu ina siri kubwa sana, watu wengi wanavyotenda, wanavyojionyesha kwa wenzao, sivyo hivyo walivyo ndani ya nafsi zao,…’nikasema

‘Ni kweli…’akasema.

‘Wengine wanaigiza tu…hawa wanaofanya hivyo…kuigiza wema…lakini nafsini mwako wana chuki…,waogope sana, ni aheri yule anayekuonyesha waziwazi, sisemi hivyo, kwa nia mbaya ya kukujengea chuki wewe na shemeji yako, hapana,..na hadi sasa sijawa na uhakika huo , kuwa huenda shemeji yako ana nia hiyo mbaya, bado tunatafuta ukweli…’nikasema

‘Sawa nimekuelewa kaka yangu…’akasema

‘Unajua Dalali ana nyumba ngapi…?’ nikamuuliza

‘Mhh, nyumba ngapi…hapana yeye ana nyumba yake anayoishi na mkewe, …’akasema

‘Ok..labda aliwajengea….ila ilivyogundulikana ana nyumba kubwa tatu, kapangisha makampuni,..na hiyo moja anaishi nyumba ndogo…’nikasema

‘Nini….una uhakika…!?’akainamisha kichwa chini kama anawaza jambo

‘Ndio maana nakuambia hivi…umjuavyo shemeji yako …sivyo alivyo, yawezekana ni kutokana na kazi zake,…sio shida…hilo hatuliangalii sana..ila kwa hali kama hii, inabidi atuambie kajengaje…’nikasema

‘Siamini….ina maana, hata haiwezekani…’akasema

‘Je sasa upo tayari kusema ukweli, kuhusu shemeji yako, vinginevyo atawafanya nyote wajinga,..na watakaoumia ni wewe na mtoto,…’nikasema

Mama mjane taratibu akachuchuma, mara akakaa chini….pale nilipo niakaanza kuingiwa na wasiwasi ...ni kitu gani tena hiki...ikanibidi na mimi nichuchumae karibu yake...nikawa nasita kumshikilia, na kabla hata sijafanya kitu ..mara akawa anayumba kama anataka kudondokea sakafuni, nikamzuia kwa mkono, kwa kitendo hicho, karibu nidondoke chini.

Kwa jinsi nilivyochuchuma,...ilibidi niwe na balansi ya kutosha, kumzuia, ...maana alikuwa kama kalegea hivi...ila machoni alionekana yupo sawa,...

'Una nini tena...?' nikauliza.

'Ku-kumbe ni kweli...hapana haiwezekani...'akasema na mara huyo akanidondokea sasa...uzito ukanifanya na mimi nikae sakafuni, akawa kalaza kichwa kwenye magoi yangu...kwa haraka sasa najitahidi nisimame ili nimweke sawa, na mara mlangoni sauti ikatoka

‘Mwanajamii unafanya nini muda wote huo huku ndani...oooh,…’ilikuwa sauti ya Dalali,  alikuwa kasimama mlangoni, na nyuma yake yupo mpelelezi.

NB: Tuendelee


WAZO LA LEO: Watu wengine walivyo nafsini mwao sivyo walivyo kivitendo,…wanaweza kuongea tu, ili kurizisha watu wengine, ili kuonekana ni wema, ili…kujenga ujiko....kuhakikisha wanafanikisha malengo yao, lakini nafsi zao zimejaa usiri mkubwa, …usiri unaweza kuwa wa chuki, husuda, nk…, na..kama wangeliweza kufichua hicho walichokadria ndani ya nafsi zao, huenda ungelikimbia. Nafsi ni kichaka cha hisia mbali mbali, nzuri na mbaya. Muhimu tuweni na subira kwa kila jambo.
Ni mimi: emu-three

No comments :