Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Tuesday, July 31, 2018

YOTE NI KWA MAPENZI YA MUNGU-27


‘Hakuna aliyekukataza kupokea simu…iwashe hiyo simu yako.’akasema mpelelezi.

Dalali akawa na mashaka sasa, lakini akaiwasha ile simu yake, na wakati anawasha ile simu ikaanza kuita….na sauti ikajaa kwenye chumba,...

Tuendelee na kisa chetu...

***********

‘Bosi umesikia habari hizo, eti mtaalamu kakamatwa na polisi,mimi sikuamini ….’sauti ikasema

‘Unasemaje, una uhakika, …kakamatwa!...khaa…, kwasababu gani, ok, ok….nipo kwenye kikao nitakupigia…’akasema na kabla  Dalali hajakata hiyo simu, huyo mtu akasema;

‘Vipi bosi kuhusu malipo yetu, maana mnada utafanyika kama kawaida, wale jamaa hawawezi kuzuia tena, hawana cha kutulipa ni maneno matupu tu, sasa utatulipa lini, unajua tena …’akasema

‘Nini…unasema nini malipo, malipo gani, nitakupigia baadaye….’akakata simu, na kubakia amesimama, akawa kuduwaa kama anawaza jambo, na mpelelezi akamuendea, na  kunyosha mkono.

‘Hebu nipe hiyo simu yako…nitakaa nayo, kuanzia sasa….’akaambiwa na hapo akashikwa na butwaa zaidi, akawa kama anataka kuiweka hiyo simu mfukoni, huku akisema;

‘Kwanini afande,…mbona una shaka sana, hao ni vijana wangu kwenye kazi zangu za Udalali…’akasema

‘Vijana wako, wanajuana na huyo mtaalamu …?’ akauliza mpelelezi

‘Mbona watu wengi wanamfahamu sana mtaalamu, na wameniambia hivyo kwa vile niliwatumia ujumbe wa maneno kumtafuta huyo mtalaamu, kwa vile mkewe anamtafuta pia,..’akasema

‘Sawa hamna shida, nikuulize tu, kakamatwa,kwa kosa gani..?’ akauliza mpelelezi

‘Hata mimi sijui, labda wewe utusaidie kuuliza huko ofisini kwenu…vinginevyo inabidi niende kuulizia mimi mwenyewe…’akasema Dalali sasa akionekaan hana raha.

‘Kwanini wewe uende kumuulizia wakati awali ulishasema kuwa wewe huna usuhuba na mtaalamu , wewe sio rafiki yake wa karibu..?’ akaulizwa.

‘Usuhuba ni wa kikazi tu, na ndio maana mkewe akaniuliza mimi , zaidi ya hapo sina udugu naye, au urafiki wa karibu saana, sema kutokana na kazi yangu wengi ninapowafanyia kazi nakuwa nimeshajenga udugu wa kikazi….na mkewe kaniamini, na mtu akikuamini hivyo utafanyaje, eeh, nafanya usamaria mwema…’akasema.

‘Haya nipe hiyo simu nitabakia nayo, mtu akikupigia,  mimi  nitakupatia, hamna shida…’akasema mpelelezi

‘Hii simu ni mali yangu, …au sio afande….’akasema na alipoona mpelelezi bado kamnyoshea mkono wa kutaka simu hiyo ipelekwe pale alipo, Dalali sasa akasema kwa shingo upande

‘Na kiukweli afande hii simu yangu  Itakusumbua bure, watu wengi wananipigia mimi mwenyewe ndio najua ipi simu ina muhimu kupokea kwa muda huu, wengine ni wasumbufu tu …’akasema.

 ‘Sikiliza mimi nipo kazini, na tendo lolote utakalolifanya kuanzia sasa litachukuliwa kama kitendo cha kunizua mimi nisifanye kazi yangu….’akasema afande.

‘Afande mimi nina haki zangu pia kweli si kweli.., kwanini uichukue simu yangu, kwani mimi ni mhalifu…?’ akauliza Dalali.

‘Kwasababu huyu mwenzako kadai huo ni ushahidi wake…kama wewe unajiamini kuwa huna kosa, kwanini uogope kufanya hivyo…?’ akauliza afande.

‘Yeye kadai ni ushahidi wake,lakini kwa kosa gani nililofanya mimi,eeh… na je kosa hilo limefikishwa kituoni kwa utaratibu maalumu, mimi siogopi kabisa, najiamini kwa vile sina kosa,..?’ akauliza na kusema.

‘Usitake kupoteza muda hapa….au kwahiyo wewe unataka huyo mtu wa jamii afanye hivyo, afungue mashitaka dhidi yako, au…?..., maana mimi nionavyo hapa nyie mnajaribu kufanya mazungumzo yenye lengo la kubaini ukweli wa hilo deni, kuulizana kama yawezekana kosa limetokea hapa, na mimi hapa ni mlinzi wa usalama…’akasema

Hapo Dalali, akasimama na kusogea hadi pale alipokaa mpelelezi na kuitoa ile simu yake na kumkabidhi afande kwa shingo upande, huku akisema;

‘Sawa mimi sina shaka kabisa afande….ngoja nifanye utakavyo…’akasema

‘Haya sasa tufanye hivi,… wewe sogea ukae hapo karibu, ili simu yako ikipigwa tu, mimi nakupatia haraka iwezekanavyo…’akasema akiiweka ile simu mezani mbele yake.

‘Mhh…sawa, hamna shida..’akasema Dalali akisogea na kukaa karibu na alipokuwa mpelelezi.

‘Na tuendelee na maswali , maana naona yana kitu ambacho kinaweza kunisaidia hata mimi, nikaweza kulifunga jalada la hii kesi,…..ila sasa muda nao umekwenda...sasa ni saa ngapi, eeh....’akawa anaangalia saa yake na mara mlango ukagongwa.

**************

 Aliyeingia sasa hivi alikuwa yule Mpelelezi wa awali. Alionekana ana haraka, kwanza akituangalia kwa haraka , sekunde kadhaa, kama vile karizika na jambo fulani akaingia ndani.

Kwa upembeni nilimuona Dalali, akionyesha uso wa mashaka, lakini kama kawaida yake akajipotezea, huku akimuangalia huyo mpelelezi akiingia ndani.

Huyu mpelelezi ndiye aliyekuwa akiishughulikia hii kesi, tokea awali, alipoingia mwenzake akasimama, wakashikana mkono kusalimiana.


Wakati huo huo simu ya Dalali ikawa inaita, na Dalali alionekana kama ana shauku ya kuiendelea hiyo simu yake lakini hakuweza,…akajikausha tu, na huenda hapo alikuwa akiombea huyu mpigaji, asiendelee kupiga , lakini simu ikaendelea kuita..simu iko hatua chache na alipo Dalali, lakini hawezi kusimama kuichukua.

Mpelelezi akasogea pale ilipo hiyo simu, na akafanya kama alivyokuwa akifanya awali, na akaashiria Dalali, aichukue,…na hata kabla Dalali hajaishika, sauti ikatanda hewani. Simu hiyo ya Dalali ina sauti kubwa sana, ilitosha sauti ile kujaa mle ndani, kila mtu akawa anasikia.
Ilikuwa sauti ya mwanamke…
 
'Shemeji mbona mwenzako amekamatwa na polisi, ni kuhusu huo mchezo wenu mchafu au sio…?’ sauti ikauliza

‘Mchezo gani mchafu, mtani ..shemeji acha huo utani wako mimi nipo ofisini na wateja, usije kuniharibia talanta yangu, ulikuwa unasemaje…?’ akauliza Dalali na kusema huku akibenua mdomo kwa tabasamu la uwongo…kama kweli wanataniana.

‘Hahaha..nyie wawili mkikutana hamnaga kazi nzuri, siwaamini kabisa, jiulize ni kwanini mwenzako kakamatwa na polisi…nakumbuka weye ulisema huyo mwenzako hawezi kukamatwa na polisi hata siku moja maana yeye analindwa na mashetani…je mashetani wamekimbia malaika nini…hahaha..’hiyo sauti ya mwanamke ikasema na kucheka

‘Sikiliza shemeji..’akasema Dalali.

‘Nisikilize nini wewe, sa hizi unaniita shemeji, shemeji, upo na mkeo nini,…sasa wewe ndio usikilize mimi, mwenzako  kaondoka hapa bila kuacha hata senti moja, mimi sio kituo cha kulea waume waliokimbia wake zao...umenisikia…’sauti ya kike sasa ikiongea kwa jaziba, huyo mwanamke ana sauti nzito.

Kwa upande nilimuona mama mjane akitikisa kichwa cha kusikitikika. Na Dalali akaliona hilo, akasema;

‘Wewe mwanamke acha utani wako, wengine wanaweza kufikiria ni kweli, nimekuambia nipo ofisini…’akasema

‘Hahahaha…leo unalo, na usikate simu maana nina ujumbe muhimu sana kwako, ukinikatia simu na wewe nitakukata pasipokatika…’sauti ikasema

Dalali akawa anahangaika kutaka kuzima hiyo simu, mpelelezi akawa anamuashiria aendelee kuongea, na Dalali, akawa sasa kashikilia sehemu ya kuzima simu, na sauti ikawa inaendelea kuongea;
 
'Shemeji unanisikia lakini, naona sauti zinakuwa mbili mbili, sio hoja,…kama upo na mkeo mimi sijali, maana mumenifanya mimi ni  jamvi la wageni, au sio, nataka na yeye alielewe hilo, nyie watu wawili mkome kabisa na tabia zenu mbovu..isingelikuwa ni pesa, mimi ningejua cha kuwafanya… , sasa ni hivi, nataka pesa yangu..’sauti ikasema.

'Nitakupigia baadae shemeji tafadhali nielewe…’akasema Dalali.

'Utanipigia ndio..ni lazima ufanye hivyo..ila lazima ujumbe huu ufike kwako kwanza..mimi ndiye nimekupigia, kwa gharama zangu…, huyo ni rafiki yako jana kalala hapa kwangu, najua kakimbia huko alipotoka, nilimsikia mkiongea naye .…sasa wewe ukija kwangu…’akatulia.

Kuna mtu alikuwa akimuongelesha huko alipo, kama anamuita … na sauti ilikuwa ya kukasirika, hivi, na yeye akasema akiongea na huyo mtu mwingine;

‘Fanya utakayo, mimi nisipoongea na hawa wanaume utaipatia wapi hiyo pesa, ….baadae nitakuja…’akasema.

‘Nimekuelewa shemeji….naona unataka kutuchina kwa ajili ya wanaume wako...’Dalali akasema

‘Hahah shemeji shemeji,..uje kwangu ili ujue ni kwanini mwenzako kakamatwa, ukienda kichwa kichwa huko polisi na wewe utaswekwa ndani, dili yenu itawaumbua kabisa, nyie mtaona tu..’akasema

‘Dili gani na wewe…?’ akuliza Dalali

‘Wataka niiseme kwenye simu, hahaha, shauri lako, mdomo wangu hauna zipu, wewe njoo, mwenzako alijikuta anaropoka ovyo, unacheza na mtoto mie,.…ukija uje na pesa yangu, mimi sasa sijali kama huo mnada utafanyika au la....kwanza niambie, huo mnada utafanyika lini ..nimesikia umesitishwa?’ sauti ikauliza.

'Shemeji nimekuambia nitakupigia,…’akasema Dalali.
 
'Nataka pesa yangu, na umwambie huyo mwenzako, ujanja wake wa kutishia watu kwa uchawi wake, mimi haniwezi kabisa…mimi siogopi uchawi wake, kwetu nimeaga vizuri tu…na nawaambia mwaka huu mtakoma ubishi, ile enzi ya utapeli utapeli imekwisha, sasa kazi tu, mnada,  mnada, upo wapi sasa…’sauti ikasema.
.
'Shemu...'Dalali, sasa hakujali amri ya mpelelezi akakata simu.
 
Wapelelezi hawa wawili, wakaangaliana na bila kusema neno, wakasogea pembeni, wakawa wanaongea kwa sauti ya chini chini, hatukuweza kusikia wanachokiongea. Na hapo Dalali akapata muda wa kuzima ile simu yake. Kwani ilishaanza kuita tena.

Mimi sikujali hicho kitendo chake, akilini nilishakuwa na yangu ya kutafakari. Hadi hapo sikuwa umuhimu sana na huyo Mtaalamu, akili yangu ilikuwa ikitafuta jinsi gani hilo deni lilitokea, kama limetoka kihalali, na benki wameaminisha hivyo,..je inawezekanaje hilo deni lihamie kwa marahemu, inawezekana kweli…
 
 Sasa kama ni kweli hilo deni ni la marehemu,…kitu ambacho mimi bado sijaamini, inakuwaje Dalali alishabikie …labda Dalali anasaka tonge la kupata ujira wa udalali kwa kupitia  kivuli cha madalali wenzake, na ndio maana waunde mizimu, hapana hapa kuna kitu kimejificha, ni kitu gani hicho..? nikawa najiuliza hivyo…

Na wakati nawaza hivyo, nikamsikia mpelelezi yule wa awali akisema kwa sauti niliyoweza kuisikia japokuwa kwa shinda;
 
'Ushahidi wote waonyesha hivyo, kuwa hilo ni deni la marehemu hakuna ubishi, lakini haya yanayotokea kushinikiza lilipwe, kinyume na benki ndio inatia doa, au sio …’akasema mpelelezi aliyeingia.

' Ni kweli hata mimi hapo ndio natia shaka, kama ni deni la marehem iweje haya mengine yote kutokea ..na huyu mtu wa jamii anataka kuthibitisha nini sasa, maana maswali yake yamifungua macho, nahisi kuna kitu kimejificha..?’ akauliza mpelelezi aliyekuwepo na kutoa maelezo yake..

‘Siunajua anavyofanya kazi zake, muache aifanye, wala usimzuie..baada ya hapo utafanya yako unayotaka,..kama kakosea utajua la kufanya, lakini tuone kwanza atagundua nini…na kwa vile amedai anao ushahidi, na ni vyema tuone huo ushahidi kabla hatujachukua hatua nyingine, unakumbuka yaliyowahi kutokea huko nyuma, yasirudie tena….’akasema mpelelezi aliyeingia.

‘Sawa, ndio maana sikutaka kumzuia kwanza kwa kuchelea hilo, hata hivyo, nina yangu, ni lazima niifunge hii kesi kwa upande wangu, sijui nyie huko..maana kwangu sijaona kitu cha kutilia mashaka…ila kuna kitu nimekiona, kwa huyu Dalali, sio mkweli,..ngoja tuone kwanza..’akasema

‘Sasa ..bado mnaendelea maana mnasubiriwa siumesikia amri ya wakubwa huko juu, nimetoa msaada bila utaratibu, ..lakini hilo nitamaliza hamna shida,…’akasema mpelelezi aliyeingia

‘Kwahiyo ulikuja kuniarifu au kumchukua mtu wa jamii..?’ akauliza

‘Hapana…nimepitia tu hapa, nilikuwa na safari nyingine, kuna mzee mmoja nilimpitia kumuhoji,…na nikaona labda naweza kumuhoji kidogo huyo Dalali, ila kama mnaendelea naye mimi naweza kuondoka, nitarudi baadae,..’akasema mpelelezi aliyeingia

‘Kumuhoji mzee gani..?’ akauliza.

‘Mzee mtupe, kuna maswala anafunganishwa nayo, ila haya msingi,…’akasema mpelelezi aliyeingia.

‘Na huyo mtaalamu vipi..?’ akauliza.

‘Unaju ahuyu jamaa nilikuwa natafuta namna ya kumpata tu, amekuwa akitoa maneno ya kujinadi kuwa yeye, hata akifanya kosa hawezi kukamatwa na polisi kutokana na nguvu zake za giza,…sasa tumeshamkamata…’akasema

‘Kwa hivyo, mbona….’akauliza mwenzake.

‘Hatujamkamata kwa kauli zake hizo…, hapaka kuna kosa kalifanya, hujiulizi ni kwanini alikimbi akwenda kujificha,..ila pamoja na hayo kuna haya yanayohusina na mwenzake huyo Dalali, japokuwa keshakana na kusema yeye hahusiki, maswala yote mengine aulizwe Dalali,..…’akasema mpelelezi.

‘Ndio nataka kufahamu kakamatwa kwa makosa gani, ni haya haya ya deni, au kuna mengine zaidi..?’ akauliza

‘Utakuja kuliona hilo baadae,…kuna tuhuma nyingi zimeelekezwa kwake na pia kuna makosa yanawashirikisa wote wawili sasa kuhusu hilo la deni, bado hatuna ushahidi nalo,tunamtegemea huyo mtu wa jamii, aliyepeleka hayo mashitaka,…na vyovyote iwavyo, ninachotaka mimi ni kulimaliza kabisa hili tatizo kama deni lipo lilipwe, au lipate mwenye uhalali nalo. Ili haki ije kutendeka...au sio…’akasema.

‘Kwahiyo hawa watu wameshafikisha rasmi mashitaka, kuwa deni hilo sio halali, ofisini..?’ akauliza huyo mpelelezi aliyekuwepo

‘Ndio wakili wao kafanya hivyo….japokuwa sio rasmi, wanasema wanakusanya ushahidi…’akasema.

‘Imekaa vizuri kweli hiyo mashitaka bila ushahidi, huoni ..ok, ik, ila mimi nataka hili jambo limalizike haraka iwezekanavyo..linatupotezea muda wetu bure…’akasema mpelelezi, na kugeuka kumuangalia Dalali, aliyekuwa akiirejesha simu yake mezani ikiwa imezimwa.

***********

Dalali alipoona kaonekana akizima simu, akajibaragua na kujifanya kama anajinyosha, na mpelelezi akamuangalia tu, baadae alipoona mwenzake anataka kuondoka, akamsogelea na kumuuliza;

‘Sasa huyo Mtaalamu anasemaje kuhusiana na deni…sijui mnada, maana hapo sijaona kosa lake..?’ akauliza mpelelezi aliyekuwepo

'Inavyoonyesha ni tamaa tu za mali, kupitia ujira wa Udalali, kuwa Dalali alimjia na kumtaka amtengenezee njia za mafanikio, kwani kuna pesa anatarajia kuipata, ila hakuambiwa ni pesa gani, lakini hiyo pesa ina mikono mingi, sasa anataka yeye awe na mamlaka nayo, unajua tena watu washirikina walivyo ….’akasema mpelelezi aliyeingia

‘Unayaamini hayo maneno, kuwa ni hivyo tu…?’ akauliza

‘Kuna mengine ya mizimu sijui, eti kuna deni, hilo deni limeleta madhara kwenye familia husika,, na kaliona hivyo kwenye vipimo vyake sijui…’akasema

‘Mhh, sasa hayo utayathibitishaje kuwa ni kweli au si kweli…?’ akauliza

‘Ndio maana nimeamua abakie kwanza kituoni, kuna vitu nilitaka kuhakiki kwa wawili hao, kabla sijarejea kwake,…ngoja tuendelee naye kwanza..’akasema mpelelezi .

‘Sawa…nitawasikiliza nyie, vinginevyo mimi nitaifunga hii kesi, hasa kwa upande wangu kuwa ajali ilikuwa ya kawaida tu…’akasema mpelelezi aliyekuwepo, na hapo wakawa wanaongea kwa utaratibu sana.

**************

Dalali ambaye lijitahidi kusikiliza wanachoongea wapelelezi hao, lakini kwa upande aliokaa yeye, kama aliweza kusikia ni machache,..ni yale tu, waliyoyaongea kwa sauti, na alipoona, haambulii kitu ndio akamgeukia shemeji yake..

'Shemeji umesikia, hakuna ushahidi zaidi ya ushahidi wa benki
, mengine ni fitina tu… na hili lina nipa nguvu ya kuendelea kutetea haki za Bro, kama alikuwa na deni, basi lilipwe, au sio shemeji…'akasema Dalali, akimuangalia shemeji yake.

'Ina maana kumbe ni kweli shemeji, wewe ndio unashabikia udalali ili nyumba ya watoto ipigwe mnada, ili na wewe upate cha juu…au mimi sikuelewa hapo?’ shemeji yake akamuuliza na Dalali kwanza akanitupia jicho mimi kabla hajajibu.

'Shemeji hizo ni fitina tu, mnada kisheria ni lazima ufanyike, na mimi ningelifanya nini hapo eeh, ningewezaje kuuzuia hilo, na mimi siwezi kushabikia hilo,…, eti  kwa vile na mimi ni Dalali  hapana hayo yanakwenda kivyake na mimi nipo kivyangu…’akasema Dalali.

‘Sasa kwanini kila mtu anakunyoshea kidole wewe kama wewe ndiye muhusika mkuu kwenye huo udalali wa kuiuza hii nyumba huoni kuwa ni aibu, nyumba ni mali ya watoto na wewe ni baba yao mlezi, wewe unashabikia iuzwe…?’ akauliza shemeji.

‘Mimi ni kiongozi wa umoja wa madalali, nielewe hapo…ndio maana kila jambo likifanyika mimi natakiwa nihusike, vinginevyo, mimi ningekaa pembeni..nilijitahidi kufanya hivyo awali, kwa vile inanihusu nikaambiwa nijiuzulu uongozi…’akasema

'Mimi hata sielewi, ina maana umeamini kabisa kuwa hilo deni ni la kaka yako, …maana nilivyosikia ni ajenda tu za mnada, huyo mtaalamu kasema hivyo hivyo, na huyo hawara wenu kasema hivyo hivyo, kila mtu aliyepiga simu hapo kakusemea wewe kuwa ndiwe msimamuzi wa huo mnada. Na wanahitajia pesa kutoka kwako, na nikiangalia kwa makini, ninaona hivyo..kuwa wewe unafurahia hilo jambo,..’akasema mama mjane.

'Shemeji nikuulize kitu, mnada ukifanyika pesa za kusimamia mnada analipwa nani ..?’ akauliza Dalali.

'Mimi sijui ..na kwanini unaniuliza hivyo…’akasema shemeji mtu.

'Atalipwa mwenye kampuni hiyo ya mnada, sio mimi lakini, na kwa vile ni lazima mnada ufanyike…basi mimi nitapata nini hapo, nikae pembeni, wachukue kila kitu, nyumba na pesa ya mnada,…lazima na mimi nidai changu kama mshirika na kiongozi…’akasema
.
'Kwahiyo wewe juhudu zako zote ni ili upate hiyo pesa ya mnada…?’ akauliza mama mjane.

‘Pamoja na hilo…pia ni kuhakikisha pesa imepatikana nzuri, ili benki wakichukua pesa yao, na sisi, eeh, tupate salio kubwa la kuweza kujenga nyumba nyingine hata kama ni ndogo, umeniona nilivyojipanga hapo, sio nisuse  tukae kimia, kila kitu kichukuliwe, utakuwa ni ujinga…’akasema Dalali.

‘Sasa, kwahiyo ndio imefikia hapo , mnada unafanyika kesho au..unajua mimi …hata sielewe, ina maana…’mama mjane akakatiza kuongea pale alipoona mpelelezi yule wa awali anataka kuondoka.
 
'Unajua shemeji, sisi madalali tuna umoja wetu, baada ya kuona kuwa ni lazma mnada ufanyike, sikuweza kujitoa, nikaona ni heri kupata chochote, kuliko kukosa kabisa…ndio lengo langu kubwa mimi sina jambo lolote kwenye hilo deni, kama anavyodai huyo mtu wako uliyemleta…’akasema sasa akinigeukia mimi.

Mimi nikaona hilo lisipite bure, nikamuangalia Dalali, moja kwa moja usoni, na kusema;

‘Tatizo sio hilo deni,..deni lipo sawa… tatizo ni uhalali wa hilo deni kwa marehemu…kutokana na ushabiki wako, mimi bado nina shaka na hilo deni, na nataka nionane na huyo muhasibu mliyeongea naye huko benki…’nikasema.

‘Nenda benki ndugu yangu, utaongea naye sana na nina uhakika utarudi kwangu na kuniambia, kumbe ni kweli, nilikuwa napoteza muda wangu bure,..…ila ukumbuke haya mambo ni ya muda sasa, nahisi utakuwa umechelewa,…’akasema Dalali.

‘Kwanini nimechelewa…?’ nikauliza

‘Ile benki imepitia mabadiliko mengi sana,..nilivyosikia, baadhi ya wafanyakazi wengi wa zamani hawapo tena…sizani kama huyo mhasibu bado yupo, sijui lakini maana sijafika huko muda, na nikifika siingii ndani, nitaenda kufanya nini, wakati sina salio huko,…’akasema.

‘Nilikuuliza swali, je muhasibu huyo aliyekuja kukuangalizia hilo deni, ulipokwenda kuhakiki, ndiye huyo aliyekuwepo kipindi kile marahemu akiwepo…?’ nikamuuliza.

‘Sina uhakika huo…kiukweli sikumbuki…siwezi kukudanganya kwa hilo, sina jibu, …nikuambie kitu majibu ya maswali yako kama hayo ya kibenki, utayapata huko huko benki..’akasema.

‘Sawa nautmabua huo sasa, kama ushahidi wangu mwingine…’nikasema.

‘Ushahidi, ushahidi huna lolote wewe, wenzako wamenishindwa utaniweza wewe bwana, na ushahidi kwa nani…’akasema Dalali.

Kabla sijamjibu sauti ya mpelelezi….

‘Ushahidi gani huo wewe mtu wa jamii…?’ aliyeuliza sasa alikuwa mpelelezi ambaye alirejea kwenye kiti chake, na Dalali alikuwa kageuka kumpa mgongo hakujua kuwa mpelelezi amesharudi, aliposikia sauti yake alishtuka hadi kiti kikatikisika.


WAZO ZA LEO: Kila mtu nafsini mwake hupenda kuangalia yale yanayomrizisha, wengine hata hawajali uhalali wa hayo mambo, ilimradi atafanikiwa kwenye malengo yake. Wapo wacha mungu wanaofanya ibada lakini kwenye nafsi zao, wanajua kabisa kuna matendo hawapo sawa, wanadhuluma, kimatendo wapo mbali na ucha mungu wao. Ukiwauliza, watasema, tumekubaliana, amekubali, amerizika, lakini nafsini anajua kukubali huko, kwa mwenzake yeye kamdhulumu. Tunamdanganya nani hapo, kuwa sisi ni wajanja sana…imani ya kweli ya ucha mungu hupimwa hapo, kujali wengine kama unavyojijali wewe mwenyewe, kuitenda haki , haki yake, na mwenye haki apate haki yake, hata kama wewe utakosa kwa vile ulitakiwa ukose..
Ni mimi: emu-three

No comments :