Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Monday, May 28, 2018

YOTE MAPENZI YA MUNGU-4



                                                          *********
‘Lakini nikuulize unaniuliza haya maswali yote ili iweje….maana wewe hujui yaliyotokea kwasababu ya haya….na hadi mimi mwenye haki nikafikia kusema, basi  yote hayo tumeshamuachia mungu,…hunujui mimi ni nani, sio mdhaifi kihivyo, nimekuwa nikifanya kazi zinahusikana na maswala makubwa ya kupambana na watu….lakini kwa hili..hapana, sitaki tena….sasa sikiliza  nimekuambia hayo niliyoweza kukuambia,…yatosha,…nakuomba uondoke tu…’akasema na kujikuanyata.

************

Kauli  yake hiyo ilinifanya nivunjike nguvu kiasi, kwasababu hata mimi mwenyewe nilikuwa najiuliza, je ninavyomuuliza haya maswali yote huyu mama wa watu, hivi kweli ninaweza kumsaidia, maana kiukweli  huyu mama mjane na watoto wake wanahitajia msaada mkubwa sana tena wa haraka, isije ikawa na mpotezea muda wake bure na kumzidishia majonzi.

Ningeliweza kufanya lolote kama ningelikuwa na watu wa kunisaidia, watu wa kunisaidia mmoja wapo keshasema hawezi tena,.. kwa hatua iliyofikia kesi hiyo, kwa kauli yake hiyo kesi kwa ajili ya kufanya huyo mama apate haki yake ‘haina mshiko’ . Akiwa na maana kuwa, kesi hiyo haina nguvu ya kuitetea, kwani  nyaraka zote na ushahidi wote unaonyesha usahihi, kuwa mashamba yaliyouzwa yaliuzwa kihalili, yalikuwa mali ya wauzaji...na mlalamikaji hana ushahid wa hoja yake.

Sasa kwa hili la la nyumba….ambalo ndio muhimu kwangu, nitawezaje kulitatua, nyumba ni kweli ni mali ya mjane na watoto wake, nyaraka zinabainisha hivyo, wameipata kutokana na urithi…lakini nyumba hiyo, inahitajika kupigwa mnada,
Nilipowaza hivyo nikahema, na kumuangalia yule mama akiwa kajikunyata sasa akionyesha dhahiri anaogopa jambo…nahisi hiyo hali inayoendelea hapo ndio inamtisha, sijui kuna nini zaidi kinatokea, na amesema inatokea kwa watoto…

Niliwaangalia wale watoto , mawazo yangu yakanipeleka kuwawazia watoto wangu…kuwa huenda na mimi inaweza kutokea hivyo, na nisipofanya juhudi, inaweza kunikuta na mimi kama adhabu,..kwani akilini nilikumbuka jambo.

Sikiliza katika maisha yako, kumbuka jambo moja, wema unaowatendea wenzako hasa,…wanyonge wenye uhitajio , ni akiba kwako, usiogope kuwatendea hivyo, kwani malipo yake yatakuja kwko moja kwa moja au kupitia kwenye familia yako, na ukipuuzia, kwa vile sio familia yako, au sio wewe, adhabu yake itakuja kwko wewe au kwa familia yako…’ nikakumbuka usia wa jamaa aliyenifanya nijiunge kwenye maisha haya ya kutetea jamii kwa njia ya visa.

 Hapo hamasa ikanijaa,…Sikukata tamaa, ndio hapo nikamkumbuka  rafiki yangu mwingine aliyebobea kwenye sheria za namna hiyo, huwa namtumia kwenye matatizo kama hayo, ikibidi lakini, ..sio mara nyingi, kwa vile yeye ana majukumu mengi sana, ukilinganisha ya yule wa awali

‘Ni swala la kujaribu tu…’ nikasema kwa sauti ndogo,

Nakamtupia macho huyo mwanamama, ambaye kwasasa niliona michirizi ya machozi ikijichora usoni, mwake,..moyo wangu ukazidi kuumia…hapo hapo nikasema;

‘Shemu unajua matatizo humjia mwanadamu, na yanapokujia inabidi upambane nayo,maana hujui kwanini yamekujia, huenda ni namna ya kuvuka daraja fulani la maendeleo, au kuondokana na dhiki, shida, au hara hatari fulani,..kwahiyo hutakiwi kukata tamaa, ni ku jaribu kila uwezavyo, kupambana na huo mtihani,..ila iwe kwa njia ya haki, usikate tamaa na hata kukufuru, kuwa kwanini mimi tu, mbona mimi naonewa sana na mungu…’nikasema

‘Ndio hivyo kiubinadamu tena…., na usemavyo hivyo, unafikiri mimi nilikata tamaa, hapana, nilijitahidi kadri nilivyoweza, lakini ikafikia sehemu nikanyosha mkono, wewe hayajakukuta haya, yangekukuta halafu uwe ni mama wa watoto kama hawa, nina imani ungelifanya kama nilivyofanya mimi, ni nini nataka,…mali eeh…dhidi ya uhai wa watoto wangu, hapana,… wacha wachukue…’akasema

‘Ina maana waliwatishia au walifanya nini cha kuwaumiza watoto wako….?’ Nikamuuliza

‘Sitaki hata kuyaongela hayo, wewe amini hivyo, ..na msimamo wangu ndio huo huo….’akasema

‘Ni kweli kihulka,…inafikia hivyo, mama na watoto wake, na ikizingatiwa, labda hukuwa na ndugu wa karibu wa kukusaidia, au sio…lakini mimi sasa nimejitolea kuwa ndugu yako, tupambane kwa pamoja, kama kweli unaamini hivyo, kuwa mali zilikuwa zako, na hilo deni kweli sio halali…’nikasema

‘Wenzako walisema hivyo hivyo, kiwapi…’akasema

‘Akina nani…?’ nikamuuliza

‘Si hao walisema watanisaidia, …’akasema

‘Nataka nionane nao, nione wapi walikwamia…’nikasema

‘Si umesema umeongea nao, wakasema nini…kuwa imeshindikana, kuwa sina ushahidi au sio…ni kweli, ushahidi sina, nyaraka zote zinaonyesha kuwa kweli sina haki..utafanya nini…hakuna,…’akasema

‘Mimi sikati tamaa haraka hivyo, ngoja na mimi nijaribu,…nipe nafasi hiyo…’nikasema lakini moyoni bado nikiwa na mashaka. Nitafanya nini sasa,…sana sana nitategemea miujiza ya mungu.

‘Hahaha…tatizo hujui tu, halafu nitakulipa nini, masikini mie….usija kuja kujutia baadae kuwa umepoteza muda wako, hujapata kitu, na mimi sina malipo ya kukulipa…’akasema sasa akiniangalia kwa mashaka.

‘Mimi sifanyi haya kwa ajili ya malipo, …na nikuambie kitu, kesi kama hizi, hujilipa zenyewe, kama walikudhulumu,…watakulipa kwa adhabu juu…lakini hayo ya malipo sio tija yangu, sifikirii hilo kabisa, tija yangu ni kwa hawa watoto, na wewe mwenyewe..tija yangu ni haki yenu…’nikasema

‘Aaah..mimi naona unanipotezea muda wangu tu…na kuniachia matatizo hapa…’akasema sasa akigeukia upande mwingine.

‘Sikiliza, wakati nasubiria simu fulani,  mimi nataka kuendelea kukuuliza mambo machache machache…, nakuomba tafadhali, jipe moyo, omba kwa mungu, sote tuombe kwake, yeye ndiye tegemeo letu ..najua hii hali ya humu inakutisha, ningelisema basi twende kwangu,…lakini hapana kwa hivi sasa twatakiwa tupambane na hao maadui zako humu humu… sehemu nzuri ya vita ni eneo wanalolipenda maadui..…’nikasema huku nikihisi mwili ukinisisimuka, na moyo kunienda mbio.

‘Mimi hivyo vita siviwezi kabisa,..nimeshanyisha mikono juu, nimesarenda….’akasema na sauti yake ikakatishwa na mlio wa simu yangu, kwa haraka nikaangalia mpigaji, ilikuwa namba ngeni kwangu.

‘Halloh ni nani mwenzangu…?’ nikauliza

‘Mimi ni rafiki yako katika harakati…’akasema, nikashangaa kwa nini hajajitaja jina lake.

‘Jitambulishe…’nikasema

‘Ni hivi…nimepata fununu kuwa unataka kumsaidia mama mmoja mwenye matatizo, ambaye aandai kuwa kadhulumuwa mali yake, …’akasema.

‘Anadai,…ina maana sio kweli…?’ nikauliza

‘Ndio ukweli ulivyo…’akasema

‘Ni nani kakuambia hayo kuwa mimi nataka kufuatilia hiyo kesi..?’ nikauliza, na badala ya kunijibu swali langu akasema;

‘Unataka msaada wangu au hutaki…?’ akauliza..na mimi nikahisi huenda kuna kitu naweza kukipata hapo,ila moyoni nilishahidi ni tapeli fulani hivi.

‘Kwanza tutambuane, maana sio kila sauti ina muelekeo chanya, siwezi  kukubali au kukataa jambo la sauti tu… muhimu tujuane wewe ni nani…’nikasema.

‘Hiyo kesi mimi ninaifahamu sana…tatizo kubwa inavyoonekana mume na mke walikuwa wanafichana baadhi ya mambo yao,..hilo ni kosa kubwa kwa wanandoa…angalia sasa, mume kaondoka, kamuachia mkewe na watoto matatizo,  mke hajui ni nini mume wake alikifanya,…kuna mali za watu zilitambulikana kuwa ni zao, kuna madeni……yote sasa yamebakia mikononi mwa wanafamilia hao…’akasema

‘Ehe…endelea..’nikasema

‘Haya nakuambia kwa vile mimi nilikuwa bega kwa geba kumsaidia huyo mama…’sauti ikasema

‘Sawa mimi nakusikiliza, endelea…ulimsaidiaje labda….’nikasema.

‘Ni kweli mama huyo na watoto wake wanahitajia msaada wa hali na mali, nilikutana nao, nikafuatilia kila kitu hatua kwa hatua…na ikafikai sehemu nikaona hakuna jinsi ya kufanya, lakini huyo mama akasisitiza kuwa mahakama ndio itaamua, ikiamua basi, hana la kufanya, basi ikabidi tufike hadi Mahakamani,… sheri a ilitubana,…huwezi ukakana nyaraka na ushahidi , huo ni msingi mkubwa wa kushinda kesi,…huwezi ukaukana ukweli, au sio…maana wewe unautumia sana…’akatulia.

‘Huwezi kufanya jambo kinyume na hayo,, ili tu umrizishe huyo mama na watoto wake, kiukweli hata mimi nilipata shida sana, jinsi gani ya kusaidia, nilitumia ujuizi wangu wote, ukichanganya na huruma ya ki-ubinadamu, lakini …nilikwama, kwahiyo ninachoweza kukusaidia ni kuwa, kama wataka kumsaidia huyo mama, kwa hivi sasa, acha mambo yaendelee kama yalivyo…’akatulia kidogo.

‘Mambo gani sasa…?’ nikauliza.

‘Ya kisheria…’ akasema, na kabla sijasema zaidi akasema;

‘Kumbe hata jambo lenyewe hujalifahamu vyema…’akasema

‘Mambo gani hayo ya kisheria,..nifafanulie..?’ nikauliza.

‘Kama hayo yaliyopitishwa, kuwa nyumba hiyo ipigwe mnada,..hiyo ni kwa mujibu wa mahakama, ni sheria imepitishwa hapo, huwezi kupingana na mahakama…’akasema

‘Lakini naweza kukweka pingamizi, kama nahisi nimeonewa au sio…?’ nikauliza

‘Ndio..lakini sio kwa kesi ya huyo mama unapoteza muda wako bure…’akasema

‘Sikiliza…na kwa ziada, sio kwamba mahakama imependa imtupe huyo mjane tu na watoto wake, mahakama imeweka namna ya kumsaida huyo mjane na watoto kuwa, pesa itakayopatikana,iangalia pande zote mbili, nilijitahidi sana hili kupatikana…’akatulia.

‘Kwa vipi…?’ nikauliza

‘Tulishaongea na benk, na wao wana ubinadamu wao,…unajua benki zetu pamoja na kujalia biashara zao, lakini wana namna ya kusaidia jamii, wao wamepanga namna ya kufanya, deni lilipwe, na kutokana na hayo malipo, wao watasaidia katika sehemu ya hilo deni, liweze kumsaidia huyo mama pia..’akasema

‘Kwahiyo wewe ndiye ulitoa wazo hilo, au sio…?’ nikauliza

‘Ndio, ni kwa namna ya kuona jinsi gani hiyo familia na yenyewe itapata chochote…’akasema

‘Mhh….endelea…’nikasema

‘Na, ..hata hivyo bado kutakuwa na pesa ya ziada kutokana na mauzo ya hiyo nyumba ..pesa itakayobakia baada ya kulipwa hilo deni na nyingi tu…’akatulia.

‘Ok….endelea…’nikasema

‘Unasikia, ..maana kiukweli nyumba hiyo ina gharama sana akipatikana mteja mnzuri, bado mama atakuwa na kianzio cha maisha yake, anaweza hata kujenga kibanda chake cha kuwakimu, lakini ni baada ya kutoa gharama mbali mbali za utendaji…’akasema

‘Ambazo ndio hizo na nyie mnanimezea mate…’nikasema

‘Una maana gani kusema hivyo,..tatizo lako wewe umelichukau hilo jambo juu, juu…’akasema

‘Sawa, ndio maana nataka nielewe…..na mlivyokubaliana ...huyu mama na mtoto wataishije…?’ nikauliza.

‘Ehee…hilo ndio la muhimu la kusaidia, wewe kama msamaria mwema, unaweza kuingiza mguu wako kwenye shemu hiyo, inakuhus kabisa, andika, ili watokee watu wamsaidie huyo mama…’akasema

‘Sio niandike ili apate haki yake…’nikasema

‘Sikiliza…kinachotakiwa kwako wewe ni kuongea na …huyo shemeji yake. Kwanza ungelikutana na huyo jamaaa wala usingelihangaika sana…anajua kila kitu, na hata ukimuuliza huyo mama atakuambia ukweli…huyo shemeji yake ni mtu mwema sana…, yeye  yupo tayari kumsaidia huyo mama, sehemu ya kuishi, niliacha wakiwa wanajadili hilo, sijapata marejesho…’akasema

‘Kama hujapata marejesho, kwanini mnakimbilia kupiga mnada hiyo nyumba, ndivyo mahakama ilisema hivyo…?’ nikauliza

‘Sikiliza, wewe ongea na shemeji yake huyo mama,  yeye ndiye mwenye majukumu  na ndiye aliyekuwa kapewa hiyo familia kuihudumia, unaona hao watoto eeh, ni bado wadogo, na huyo mama alikuwa hajiwezi kabisa huyo shemeji yake kajitolea kwa hali na mali…’akasema

‘Kwahiyo ni nini unachokifanya kwa hivi sasa kwa ajili ya huyo mama…?’ nikauliza.

‘Mimi bado naendelea kuongea na benki, ili kuona ni namna gani zaidi wanaweza kumsaidia huyo mama, kama kuwasomesha hao watoto..na zaidi ya hapo, wao kam benki wana fursa nyingi, huyo mama alikuwa muajiriwa, wanaweza hata kumuajiri…., banki ni watu wazuri sana, wana vitengo kama hivyo vy kusaidia jamii.…’akasema

‘Naweza kuonana na wewe wapi..?’ nikamuuliza

‘Kwa hivi sasa nina shughuli nyingi, nimeamua kukupigia simu tu, baada ya jamaa yangu kuniambia kuna mtu anaulizia tena kuhusu  hii kesi,..kiukweli kesi hii ilishanichosha sana..na ni mambo ya kawaida kwenye utendaji wetu, ila …kuna mambo mengi nimekutana nayo, ni ya kawaida…ila ni kesi ngumu sijawahi kukutana nayo kabla…, na hata hivyo, kila kitu kipo wazi…’akasema

‘Kwa kauli yako hiyo najikuta kuwa na maswali mengi…lakini naona haifai kuongea yote hapa kwenye simu, sio vyema au sio, hakuna ushahidi wa kudumu,…ila …kama wewe ndiye uliyekuwa ukiishughulikia hii kesi, japokuwa sikujui wewe ni nani, nakuomba  jambo moja, kama kweli wewe ni mkweli…kama kweli wewe ndivyo ulivyo kama ulivyosema, nakumba jambo moja…’nikasema

‘Jambo gani hilo…?’ akauliza kwa sauti ya mashaka.

‘Uahirishe kidogo hilo zoezi la kuipiga hiyo nyumba mnada…’nikasema

‘Haaaah, wee, unataka mimi nipambana na sheria,… sio mimi,…mimi sipo hivyo kabisa,.. hayo ni maamuzi ya mahakama ndugu yangu, hilo siwezi, …kabisa kabisa…’akasema

‘Nikuulize jambo moja, je mahaama ndio ilipanga tarehe ya kufanya huo mnada…?’ nikauliza n ahapo akatulia kidogo, halafu akasema

‘Hayo ni maswala ya benki…baada ya kuthibitishwa kuwa wana haki ya kufanya hivyo, ndio wao wakapanga tarehe hiyo…’akasema

‘Katika hukumu, …ilisema nini kuhusu tarehe na haki za huyu mama…?’ nikauliza

‘Siwezi kukusomea hilo kwa hivi sasa, kwanza wewe huna haki ya hayo yote au sio, ni mpaka niwe na uhakika kuwa wewe unahitajia hayo kama nani, kwa huyo mama…’akasema

‘Sasa hivi unanigeuka kuwa hujui ninachokifanya mimi…’nikasema

‘Najua, lakini hilo unaloniulizia ni jambo la kisheria,..unasikia,…kama ikibidi nitakuonyesha, lakini mpaka niwe na uhakika wa kisheria kuwa wewe ni nani kwa ajili ya huyo mama…’akasema

‘Swali je unaweza kumsaidia huyo mama, ili hilo zoezi liahirishwe au mimi niende mahakamani, kuweka pingamizi…’nikasema

‘Hahahaha..umenifanya mimi nicheke, unajua usiingile mambo usiyo na ujuzi nayo,…hilo sio swala dogo kama unavyofikiria wewe, wewe huna uwezo huo, ili lifanyike hilo, inahitajika wakili, mwenye uwezo mkubwa,…’akasema

‘Kama wewe…’nikasema
‘Mimi ndio nimefikia hapo, siwezi tena kuifanya hiyo kazi…’akasema

‘Kwanini, unaogopa…kuna kitu unakiogopa au sio..?’ nikauliza

‘Ndugu yangu nina kesi nafuatilia, siwezi kuongea na wewe zaidi….’akasema

‘Ndio maana nataka tukutane na wewe, au niende mahakamani nipate kibali cha kuonana na wewe..’nikasema

‘Sikiliza…ok, nitakupigia…’hapo akakata simu, haikupita muda, akapiga simu, na kuniuliza;

‘Kwahiyo wewe umeshaongea na huyo shemeji ya huyo mama..?’ akauliza

‘Bado…’nikasema

‘Ongea naye kwanza..’akasema

‘Kwahiyo hayo yakiendelea, utafanya kama nilivyokuomba…’nikasema

‘Siwezi, nakuambia ukweli ulivyo…’akasema

‘Sawa ngoja na mimi nifanye nijuavyo mimi…’nikasema

‘Utafanya nini ndugu yangu wewe…, usidanganyike, kama ni huruma mimi nina huruma sana,..lakini kwa hilo, huna ujanja, utapoteza muda wako, na pengine..ukaja kupata matatizo, na muulize huyo mama, shida gani anayoipata, huwaonei huruma hao watoto ,kifupi mimi siwezi kufanya lolote kwa hatua iliyofikia…’akasema
‘Mimi naona unakimbilia kunitisha, au…?’ nikauliza

‘Sio vitisho,….mimi nakuambia kama mtu ninayekufahamu na kukujali,..hebu nikuulize wewe…umefika hapo kwa huyo mama, hebu muulize vyema,…ni mambo ya ajabu yanatokea humo, sio kwamba mimi nayaogopa, hapana, lakini ni mateso kwa hao watoto,…’akasema

‘Kwanini yatokee hivyo, kama hao watu wana haki ya hayo waliyoyadai…?’ nikauliza

‘Mimi sijui… ila kwa vile sheria ipo wazi, kwanini tupoteze muda, kwanini hiyo familia iendelee kuteseka, wakati kuna uhakika kuwa hawatashinda hiyo kesi, mimi sioni haja ya kuwatesa hao watoto, unaona dhamira yangu ilivyo, naangalia namna nyingine ya kuwasaidia, anyway..kama huwezi kunisikiliza fanya upendavyo…’mara simu ikakatika.

Kwa haraka nikaichukua ile namba nikatafuta jinsi ya kumtambua mtumiaji wa hiyo namba, na ilionekana ni namba mpya haijasajiliwa…

Nilitaka nimfahamu ni nani, kama kweli ni mwanasheria, hatakuwa na namna ya kujificha, nikaiweka ile namba,…nikajaribu kama kumtumia pesa, nikaona haisomi mumulikaji wa hiyo namba. Ina maana hiyo namba haijasajiliwa, hapo nikawa na ushahid muhimu kwangu.

‘Oh lakini ni nani huyu…?’ nikasema kwa sauti, na yule mama akaniangalia.

‘Eti ni nani aliyekuwa akiishughulia kesi yako…wakili au…mtetezi ?’ nikamuuliza.

Yule mama akaniangalia kwa makini, nikama vile alikuwa akiogopa kusema neno, na mara ujumbe wa maneno ukaingia kwa namba ile ile, ukisema;

‘Mimi nitajitahidi kufanya utakavyo, lakini na wewe utii sheria…acha hayo mambo ya kisheria yaendelee kama yalivyo,…sina muda tena na hiyo kesi, kama upo tayari jibu endelea…’
Hapo nikatabasamu..nikamuangalia yule mama, yule mama akawa ananiangalia tu kwa mashaka.

 ‘Ni lazima nimfahamu huyu mtu ni nani…’nikasema sasa nikitaka kumpigia jamaa yangu mmoja mtu wa mitandao, …najua hatanisaidia sana, maana kama namba haijasajiliwa huwezi kumfahamu mpigaji wa hiyo simu.

Nikampigia huyo jamaa yangu, na kumuomba ajaribu kumtafuta mpigaji wa hiyo namba,na wapi alipo

Baada ya muda akanipatia majibu;

Mpigaji wa hiyo namba, hajulikani maana hiyo namba haijasajiliwa, ila huyo mpigaji yupo maeneo ya……..

Niliposikia hivyo, nikasimama, 

Kwa haraka nikatoka nje….


WAZO LA LEO: Kabla ya kutoa hukumu ya jambo lolote ni muhimu sana tuwe tumejirizisha kwa kusikiliza pande zote, pamoja na ushahidi na mashahidi, laini pia , ni vyema tukawachunguza hao wahusika vyema, maana wengine ni wajanja wa kuongea, ni wajanja wa hali na mali. Wengine ni wadhaifu wa kuongea. Na ukichunguza historia zao, unaweza kugundua tabia na mienendo ya wahusika, hili linaweza kusaidia katika kufikia hitimisho ya kesi za kijamii.
Ni mimi: emu-three

No comments :