Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Tuesday, March 13, 2018

MKUKI KWA NGURUWE-93


 Shahidi akaendelea...

  Namkumbuka sana Marehemu kwenye kauli zake, aliwahi kuniambia hivi;

‘Katika hii dunia, kila mtu na hamsini zake, kama una uwezo wa kufanya hivi, na ukapata, basi fanya, kama kuna sehemu unaweza kuitumia kama ngazi ili na wewe ulipate tunda fanya hivyo..mimi maadui zangu wakubwa ni wakubwa, matajiri, hawa tutapambana nao hadi kifo..

Najiuliza tu , kwanini sasa polisi wanahangaika na watu wa chini, wakati, kwa mujibu wa kauli ya huyu mtu yeye maadui zake wakubwa ni watu wakubwa, matajiri, watu wenye nyazifa eeh, hao ndio wanaoweza kumuua, au sio,….

Yeye alifikia kutuambia, sisi tumekubali kuolewa na matajiri, sasa tuamue moja, kuwa na yeye kupambana na mafisadi wadhumulaji, kama alivyowaita yeye, au kuwa upande huo wa hao watu, anasema anapambana nao…kama hatutashirikiana naye basi tupo upande huo…kama tupo huko, basi tutakuja kupata shida, na tutakuwa miongoni mwa wasaliti wake.

Unajua huyu mtu, yeye pamoja ya yakuwa kasoma sana sheria, aliamua kuigeuka sheria, au kuitumia sheria atalavyo yeye, au sio, kwa maneno yake ni ili kwuasaidia wanyonge, ... akachanganya na ujanja-ujanja wake eeh, hasa aliousoma vitabuni, …akakaa na kubunu njia zinazojulikana kama blackmail.Sijui tafsiri yake ni nini kwa Kiswahili, ....’akasema na kumwangalia mwenyekiti.

Watu kama hawa wapo wengi, wanaishi kiujanja ujanja, wanakuja kwako, wanakupima udhaifu wako, wanakuona una njaa kali, wanaanza kupenyeza sera zao, na nyie bila kujua…maana keshawasoma, mnakuja kukubaliana naye.

Ndio  maana dunia ya leo imejaa vita unahisi ni kwanini..ni watu walishaumia, walikuwa wanasubira kisingizio tu, ili waweze kuzitoa hasira zao..hili watu hawalioni..hivi ni visasi kutoka ndani ya mioyo ya watu waliokuwa wakilalamika, wakisononeka, na mtu wetu akaamua kuwasaidia kwa kuchukua kutoka kwa matajiri kuleta kwao,

Swali hapa iweje sasa, hao wanaotaka kusaidiwa ndio wawe wauwaji,…maana polisi hadi sasa kwa ushahidi wao, wanaoshukiwa ni watu wa aina yetu, sio haooo een maadui za marehemu,…

 Nimepata muda wa kuishi na marehemu na amekuwa kila siku akinihubiria ili nibadilika ili niwe kama yeye,..huyu mtu ni mjanja kwenye ushawishi..

Siwezi kulikataa hilo, … ilifika mahali na mimi nikajenga chuki nikiona ukweli ulivyo,kuwa hayo anayoongea yana namna ya ukweli fulani…

Hata hivyo kiukweli wangu,  sikufikia hatua ya kutaka kuua, naogopa sana kumwaga damu ya mtu asiye na hatia, na ikizingatia kuwa mimi nimejifunza uaskari, na moja ya nidhamu ya uaskari, ni utii wa sheria bila shuruti, kuwalinda raia wema…sasa kwanini leo mimi niwe mshukiwa, sawa yawezekana, lakini kuna sababu au sio, ....

‘Nafahamu wengi watanishangaa, nikisema nimejifunza uaskari, naomba mlielewe hivyo, na mlichukulie hivyo hivyo…’

Ndio maana nikatoa ombi kwenu, kuwa haya nitakayo yaongea hapa, yaishie hapa hapa,, tukitoka hapa, kila mtu na hamsini zake, hayo mengine waachieni wahusika, wanajua ni nini wanachokifanya, lakini kama mtu atajitia kidomo domo, ....sawa nitakamatwa, kama mshukiwa, wa mauaji, lakini je ni kweli nilifanya hivyo...?’ akageuka kuwaangalia watu.

Nafahamu mpaka hapo nimewachanganya watu…mmh…, maana mlitaka msikie mnachokitaka nyie,..jibu la moja kwa moja ni nani muuaji, au sio.. lakini huko siwezi kufika hara hivyo, ninachotaka kwanza, muone tukio zima, ili nyie wenyewe mje kumpata muuaji halisi…..’hapo atakatulia kidogo akiwaangalia wajumbe.

**********

‘Sasa naomba nianze maelezo yangu kwa jinsi ilivyokuwa ....’akamuangalia mwenyekiti

‘Natumai kwa hivi sasa hakuna pingamizi…’

Alimuangalia mwenyekiti, mwenyekiti alikuwa katulia, kwa haraka akamwangalia mume wa familia ambaye naye alikuwa sasa kageuza kichwa nyuma kumwangalia huyo mdada anayeongea kwa hamasa, maana muongeaji alikuwa kiti cha nyuma cha mume wa familia, kiukweli hapo alipo, alikuwa kama haamini macho yake kwa kile anachokiona, kweli huyo mdada ni yule yule anayemfahamu yeye, au ni mwingine.

 ‘Ni hivi , kiuhalisia,..Mume wa familia alikuwa ameshapona muda mrefu tu,…’akasema hivyo, wajumbe wakawa kimia

‘Sio kupona kwa vile,… hapana,  bado likuwa na majereha, unajua ile ajali ilikuwa ni kubwa sana,..lakini sio kivile alivyokuwa akijionyeshea, mtu mpaka kubebwa, ..na vitu kama hivyo,… kuna muda alitakiwa aigize, ili kukamilisha mambo fulani fulani, hiyo ikiwa mipango ya Makabrasha…’akasema

‘Mume wa familia aliambiwa hilo ni kwa manufaa yake yeye mwenyewe ili mambo yakamilike kwanza kwani akiwa amepona, basi atakuja kukumbuna na mkataba wao, ambao ungemuhukumu kama mkosaji, mvunjaji wa sheria, kama walivyokubaliana kwenye mkatana wao, si mshapata picha ya mkataba wao ulivyokuwa…’akasema muonegaji kama anauliza wajumbe.

‘Ukiangalia ni sawa, maana yeye alishaharibu, alishavunja mkataba au sio, kwa mujibu wa mkataba wao…na ili mkewe aendelea kuwa upande wake ni yeye aendelee kuwa mgonjwa, umeona hapo walivyocheza…kwa hali hiyo mume wa familia hakuwa na jinsi, ilibidi akubaliane na mtalaamu,, la sivyo ndoto yake ya muda mrefu ingelifutika..

Kiukweli mimi nilikuwa naumia sana, maana hayo yanavyoendelea nayaona, nayasikia, japokuwa nilijitahidi nisiyaingilie kiundani wake, …unajua tena, na mimi nilikuwa na yangu kwa upande wangu, kama nilivyosema huyu mtu alitunasa, na akawa anamvuruga kila mtu kwa upande wake..

 Sasa tuende kwa huyu marehemu,…

Mimi nikawa nimepewa kazi ndani ya ofisi ya Makabrasha, nikiwa kama muhudumu wake maalumu, lakini nia na lengo lake ni lile lile, sisi, au mimi niwe karibu naye, nisije nikaharibu mipangilio yake, kwahiyo nikawa napangiwa kazi hata za usiku, hizi kazi za usiku, eeh zilikuwa na mambo yake…ujue awali nilikuwa nafanya kazi huku na kule, yaani kwa bosi wangu na kwa huyu mtu. Bosi wangu alikuwa halifahamu hilo…

Sasa siku zilivyokwenda ndio nikawa sasa nafanya kazi kiukweli ukweli chini ya Makabrasha…, sio ile kama kibarua tena wa kazi maalumu za siku moja moja… utaniuliza nilikuwa nafanyaje kazi kama hizo hata za usiku huku nipo ndani ya ndoa yangu. Mume wangu hafahamu…

Kumbuka kuwa , kwa muda fulani, mimi niliaga kwenda kijijini, kabla ya kuwawa kwa Makabrsha, ilikuwa nfanya hivyo kila mara kukiwa na kazi maalumu za muda naaga kuwa nakwenda kijijini kwetu,…nikawa naenda na kurudi, najua mwenyewe jinsi gani nilikuwa nafanya,..hata marehemu alikuwa nimeaga kwa mume wangu kuja kwake, kipindi hicho za kazi za siku moja moja,…ila kipindi sasa nipo kwake, nilimuelezea hali halisi, akaelewa.

Na hata bosi wangu hakuwa anafahamu hiyo kazi yangu ya muda kwa makabrasha, na hata ikafika muda, kwa mujibu wa Makabrsha niache kazi nyingine zozote nilizokuwa nafanya niwe namfanyia yeye kazi tu..ndio nikaomba kuacha kazi kwa bosi wangu, na nilipoacha kweli nilikwenda kijijini nikaweka mambo yangu sawa, sasa nikarudi jijin nikiwa mtu mwingine..

Na kwa muda huo sikuwa nawasiliana sana na mume, kiukweli nilimtesa sana,  hakuwa na raha akiniona jinsi nilivyo..kwahiyo hata nilipomuambia kuwa nakwenda kuishi kijijini, hakukataa, mume wangu alitaka niwe na raha, niwe na uhuru, niweze kubadilika, niweze kuondokana na ile hali anayoniona nayo, mawazo…sina amani.

 Hadi hapo utaona kuwa kazi ndani ya himaya ya Makabrsha  ilishaanza siku nyingi hata kabla sijamuandikia rafiki yangu barua ya kuacha kazi kwake.

Kuacha akzi nyingine, shughuli nyingine, ilikuwa moja ya mikakati ya Makabrasha ili aweze kuwa karibu nami, ili awez kunitumia, hakujali kama nitavunja ndoa yangu au la. Na nataka muelewe hili, kuwa Makabrasha hakujua undani wangu na rafiki yangu kuwa nafanya kazi gani kwake, alijua kuwa nafanya kazi za kutangaza biashara zake tu, kiukweli kinje ndivyo nilivyokuwa najulikana hivyo.

Kwahiyo sasa rasmi nikaingia ndani ya jengo ambalo hata mimi sikulifahamu hivyo lilivyo kwa huko ndani, kuwa hilo jengo kwanza llikuwa likimilikiwa na marehemu, na humo ndani kuna mambo mengi ambayo hayajulikani kwa watu wa nje, na hata humo kuna wapangaji wa ofisi hawajui kinachoendelea huko chini, kuna ofisi za chini kwa chini, chini ya ardhi…. 

Wakati naingia humo, mipango mikubwa ya Makabrsha ilikuwa tayari imeshakamilishwa, mikataba imeshabadilishwa, na mikataba mipya imeshatayarishwa, na kuwekwa inapostahili, sasa Makabrasha akaanza kutoa makucha yake, akatayarisha mikataba mingine mipya ya kumuhalalisha yeye kama mumiliki mkuu wa baadhi ya makampuni likiwemo hilo la mume wa familia, lengo limashafikia penyewe, sasa Makabrsha sio yule wa zamani tena, mnanielewa hapo….

 Hadi hapo, mume wa familia, alikuwa hana nguvu tena, kwani alishawekwa kwenye mikono ya Makabrasha. Kashfa nzito ilishajengwa hata kwa kizazi cha mke wa familia, japokuwa familia ya mke ilikuwa bado gizani, haifahamu kinachoendelea, na ndilo lengo…na kiukweli hiyo kashfa ilivyotengenezwa kama ingevuja,.. basi,.. hata kizazi cha mke wafamilia , kwa mzee hapo, ingeliharibu jina , na mambo ya kisiasa yangeliharibika kabisa..

Marehemu hakutaka kuifikisha hiyo kashafa haraka kwa adui wa mzee, yeye alitaka kuitumia hiyo kashfa kwanza kwa masilahi yake, baadae ikibidi ndio angeuvijisha, na hapo siju….

Ndio maana mume wa familia akawa anauma hilo kwa magego, sio kwa ajili yake tu bali pia kwa ajili ya familia nzima ya mkewe, japokuwa chanzo cha hiyo kashifa ilitokea kwa mume wa familia….mnaona ilivyo…sio kitu kidogo….

Kabla sijafika huko kwenye mpango rasmi…

Nikisema mpango rasmi, ina maana mpango ambao ndani yake ilipatikana kifo cha Makabrsaha, huo mpango sikutakiwa kuu-ongelea hapa, au kuongea lolote kuhusuiana na huo mpango,….huo mpango natafutwa nao, na kama nafahamu lolote nipo hatarini..

Walitaka kuniua…hahaha, lakini mungu ni mkubwa,…polis wakavumishiwa kuwa ni watu wanaotaka kulipiza kisasi cha marehemu,..sio kweli jamani, ni kwa vile mimi ndiye ninayefahamu kila kitu…

 Sasa huo mpango umetumika kama ushahidi,… lakini katika namna ya upotoshaji, kwa namna maalumu..ndio maana mimi nataka niongee hapa kila kitu jinsi ilivyotokea, ili kama ni haki, basi haki kweli ije kutendeka..

Sasa kama mimi ndiye muuaji, au sio…nataka niwajibike kiukweli, na nyie mkiwa mashahidi, na kama yupo mwingine aliyeshirikiana nami, basi atanifuatia, au sio…nataka hili niliondoe kwanye nafsi yangu ili niwe huru…

Sasa.., ngoja niwarejeshe kwenye mazungumzo yangu ya mwisho na mume wa familia; nawarejsha huko maana hayo mazungumzo ndio ushahidi mkubwa wa polisi, huo ndio ushahidi unaowafanya mpaka sasa watuone sisi kuwa ndio wauwaji, labda, ni kweli, labda sio kweli, mimi sitaki nijihukumu, nataka nyie na baadae mahakama ije inihukumu kihalali, au sio…

Sasa tuwe tayari, na huu ushahidi…mimi nitauongea, ila ..kila kitu kipo kwenye video, utayasikia haya nitakayoyaongea, video hiyo imechakachuliwa kuna mengine hayapo……

**********a

‘Ina maana wewe hadi hapo umeshakubali kuwa wewe utakuwa mtumwa wa Makabrasha wa kudumu…?’ nikamuuliza mume wa familia

‘Nitafanya nini kwa sasa, huyu jamaa ana siri zangu nyingi, ana mambo yangu mengi, ambayo akimuonyesha mke wangu au wakwe zangu, nitafukuzwa kama mwizi, kwahiyo inabidi nimkubalie kila kitu...’akaniambia na mimi nikawa sina njia ya kumsaidia. Mimi nikamwambia

‘Kwa usalama wako ni bora ufanye hivyo maana humjui huyo mtu alivyo, huyo mtu kwa namna nyingine ni mbaya, anaweza kuyafanya hayo, na akahakikisha unazalilika mpaka utatamani kujiua,..lakini usichoke mimi nipo nyuma yako maana pamoja na hayo namfahamu vingine alivyo..’nikamwambia hivyo.

Mimi nilishaamua kuwa nilimalize hilo, kwani kama nisipofanya jambo, hali hiyo itaendelea kututesa katika maisha yetu yote, tutakuwa watumwa wa mtu mmoja, na hata kama tutaendelea kuishi kwenye ndoa zetu, itakuwa ni ndoa ya jina tu,..

Kwa mfano mimi nilitakiwa kumtii huyu mtu kama mtumwa wake, kila anachokitaka nimfanyie, hata kuzalilika, sasa kulikuwa na manufaa gani hapo,..na nitazalilika hivyo mpaka lini,..hata hivyo,..basi tena,.. nikaona nijitolee tu muhanga, nifanye kazi yangu, nitimize wajibu wangu, ili kulimaliza hili tatizo kabisa, lakini kwa vipi kwa mtu kama Makabrasha, wanasema mtu mwenye tabia hii kamwe haiachi labda auwawe…’akasema na kutabasamu.

‘Usijali, mshirika, mimi nitajitolea kwa ajili yako....kama utanikumbuka sawa, nafanya haya kwa vile nakupenda, japokuwa penzi kwako kwangu kwa hivi sasa halipo tena, siwezi kukulaumu, japokuwa, inauma sana,....nimeshakuona kuwa wewe unanitumia ili upate unachokitaka, huna tofauti na Makabrasha...’nikamwambia siku hiyo.

‘Kwanini unasema hivyo, mimi mbona  nakupenda sana, umeshasahau tulivyoahidiana kule kijijini...kwa hali niliyo nayo, nashindwa kutimiza ahadi zetu zote, unafahamu ni kwa nini…wakati mwingine haya yanayotokea ni kwasababu nashindwa kuvumilia,..hata mimi nateseka kwa hilo nawaza sana, ..wewe hujui tu, ndio maana naamua kunywa kupoteza mawazo…sasa yametokea haya ya kutokea, sikupenda..ila nasema mimi ninakupenda, lakini kwa hali kama hii tutafanyaje,....’akasema

‘Najua..’nikasema

‘Wewe huoni sasa naumwa, na pia natakiwa niumwe ugonjwa wa kuigiza,…lakini hata bila kuigiza kuumwa..kuumwa bado kupo,  hali niliyo nayo sio rahisi kuelezea, wakati mwingine nashindwa hata kuelewa mimi ninaumwa nini hasa..’akasema

‘Si umeumia, kwani hilo halijulikani..’nikasema

‘Aheri ya kuumia viungi kuliko kuumia moyoni, wewe hujui tu, aheri ya kuumwa magonjwa yanayojulikana, kuliko kuumwa magonjwa yasiyojulikana, nateseka tu wewe hujui..kichwa akili wakati mwingine inakuwa sio ya kwangu..mimi hata sijui nimekuwaje…’akasema

‘Kiukweli kwa vile nampenda huyu mtu, iliniuma sana alipoongea hivyo, siku ile nakumbuka nilitaka niongee na docta nijue huyu mtu ana tatizo gani, sikuweza..kutokana na muda, lakini akilini nilihisi huyu mtu kuna kitu kafanyiwa tofauti na matibabu yake..

‘Mimi nakuambia ukweli, hapa nilipo, siwezi kujijua naumwa nini..lakini naahidi mimi nikipona tu na yeye akifanikiwa alivyopanga iwe, nitatafuta njia ya kumkomoa, tutarudisha mali yetu yote...hata kama nikwa kumua, mimi nitamua kwa mkono wangu.., sitaogopa hilo, maana yeye mwenyewe hatujali, wewe huoni hilo…’akaniambia hivyo.

‘Chunga huo ulimi wako, …kauli yako hiyo ikisikiwa na wenyewe, itakuwa ushahidi, hata akitokea huyo mtu akauliwa na mtu mwingine, wanaweza kutumia kauli yako hiyo kama ushahidi …usipende kuropoka ropoka kauli kama hizo ovyo…’nikamkanya hivyo.

‘Sawa mpenzi..nimekuelewa…’alisema hivyo huyo mume wa familia

Nayazungumza haya maneno alivyoyatamka bila kuficha kitu…maana haya mazungumzo yapo kwenye ushahidi walio nao polisi! Ina maana hadi hapo polisi wamesharizika kuwa wameshampata muuaji tayari, sasa jiulize kwanini wamechukua muda kumkamata huyo muhusika, na kila kitu wanacho,…wanashindwa kufanya hivyo kwasababu bado kuna utata au sio, hiyo pekee haiwezi kuhalalisha kuwa yeye ni muuaji, ..lakini sio hivyo tu, tuendelee na haya mazungumzo kama ushahidi wa polisi…

 Kuna kitu wanakiitai …’motive’ au motisha wa kuyafanya hayo mauji…ni nini ..huyu mshukiwa ana kitu gani, cha kuweza kuyafany haya, maana aliyemuua Makabrsha lazima ana jambo, je huyu mtu ana jambo gani dhidi yake…hicho ndicho walikuwa wakikitafuta, je walikipata,..sasa wakati wanatafuta wakajikuta wanapata taarifa nyingine za utata!

Mwenyekiti nisamehe hapo kidogo, nitaendelea kutoa maelezo kutokana na ushahidi wao kwa manufaa yetu na hata kwako pia..…

Alipozungumza hivyo, awali mwenyekiti alitaka kumzuia lakini baadae akaonekana kutulia akamuangalia tu huyo muongeaji…kiukweli mwenyekiti alionekana kuwa na wakati mgumu, nafikiri ni kutokana na huo mkanganyiko wa ushahidi…

 Wakati nipo naongea na mwenzangu, tunamuongelea Makabrasha niliwahi kumwambia hivi

‘Kwa hivi sasa hatumuwezi tena Makabrasha, huyu jamaa keshajizatiti, na kiukweli kama akiendelea kuwepo duniani, sisi tutaendelea kuwa watumwa wake, na hata ndoa zetu hizi sizani kama tutaweza kuishi kwa amani na furaha..’niliongea hivyo

‘Ni kweli, sasa ..oh, … mimi naona..tumuue huyu mtu,..hakuna jinsi..’yeye akasema hivyo.

‘Nimeshakuambia, achana na hiyo lugha yako,…’nikasema

‘Sasa hebu niambie,  utawezaje kuishi kwa amani kama huyu jamaa kila siku anatutushia amani..na ukumbuke hadi sasa huyu jamaa yetu ameshafanikisha mambo yake…’akasema

‘Bado wewe hujakamilisha na wewe ukikamilisha tu, kila kitu kimeshawekwa mikononi mwake, na wewe itabidi utii amri kutoka kwake, kwahiyo nafsi iliyobakia ni kupitia kwako, utafanyaje sasa…’nikamwambia.

‘Sawa nimekuelewa..hata hivyo sitaweza kumkatalia, maana nikimkatalia itakuwaje, labda hapo hapo nifanye jambo,…iwe mwisho wa haya yote,..au nitumie hiyo silaha, kum-maliza..japokuwa naogopa mimi…kwani nim-maliza watu watajua, eeh, mimi naumwa nipo hospitalini…au nimtafute mtu, anifanyie hiyo kazi, unasemaje..au sasa hebu nishauri, tutafanyaje kwa hali kama hii..?’ akaniuliza

‘Sasa hivi unaniuliza eeh, tutafanyaje…, kamuulize Makabrasha,…’nikasema hivyo.

‘Kwanini unasema hivyo, wewe ulitaka nifanye nini mimi…huoni hali tuliyo nayo,…mimi nikijulikana tu, kuwa wewe na mimi kitu kimoja, unafikiri itakuwaje, lakini Makabrasha anafahamu kila kitu ana ushahid wa kutosha, huoni kuwa keshatuwahi, tufanyeje sasa…’akasema

‘Nakuambia haya kwa vile tokea awali nikikushauri, eeh… utulie, tuwe makini, ukawa hunisikilizi, sasa hivi yamekufika shingoni unaniuliza tufanye nini, mimi sijui la kufanya hadi sasa, kiukweli ndio hivyo, mipango ipo mingi, lakini …siwezi ..nina wakati mgumu sana…’ nikasema nikionekana kuwaza.

‘Tusikate tamaa au sio..’akasema

‘Kiukweli ninachoweza kusema niliyo nayo mimi mwenyewe ni mazito zaidi ya haya unayoniuliza wewe tufanye nini… kwahiyo kwa hivi sasa niache kwanza na yangu, wewe endelea na Makabrasha wako, yeye si ndio wakili wako, na yeye ndio bwana wako, nikiwa na maana wewe ni mtumwa wake..si ndio hivyo, k.’nikamwambia.

‘Hivi wewe unajiamini nini , wewe unafahamu vyema huyu mtu alivyo, bila ya mimi na wewe kushirikiana, hatutafika popote, njama zake ni kututengenisha, kutokosanisha…sasa mimi nakuonya kama una jambo dhidi yake, unataka ulifanye kivyako, utakuwa unajitakia matatizo,achana na huyo mtu....’akasema.

‘Mimi ni askari, ninafahamu ni kitu gani ninachokitaka kukifanya, ninachohitajia kwa hivi sasa ni silaha tu,...sina silaha,na sitaki kuazima silaha kwa aliyekuwa bosi wangu, nimeshaacha kazi kwake, na nataka iwe hivyo, mhh...’nikamwambia.

‘Wewe ni askari!!!?...’akasema hivyo kwa mshtuko..

‘Ina maana zile ndoto zako umezifanyia kazi, hahaha siamini,..sio kweli, bado wewe unaota ndoto zako..usidanganyike , kazi hizo hazikufai, wewe ni mwanamke, ukijiingiza huko, utajiharibia maisha yako, na hivi, huo uaskari umejifunzia wapi, hahaha…unafikiri uaskari ni mchezo eeh….’akasema kucheka sana..ukumbuke haya yote yalikuwa yakirekodiwa na marehemu.

Nazungumza hapa nikiwa naangalia huo mkanda uliorekodiwa na marehemu ambao sasa upo mikononi mwa polisi…

‘Kusema mimi ni askari sina maana ya kuwa mimi ni polisi, huoni mitaani kuna migambo, usalama shirikishi, hayo yawezekana au sio, na mafunzo ya hapa na pale yamenifanya mimi nijiamini hivyo, kuwa mimi ni askari ..’nikasema

‘Sawa vyovyote iwavyo, usije kujilinganisha wewe na Makabrasha, kuwa utaweza kupambana na yeye, yeye kijizatiti kwa kila hali, unamfahamu alivyo, sio...’akasema

‘Hahaha, mimi ndio nikukanye wewe , maana mimi namfahamu zaidi ya unavyomfahamu wewe, nikuambie ukweli…’nikasema

 ‘Hahaha wewe mwanamke, haha, yule ni rafiki yangu, tumakulia pamoja japokuwa ni mkubwa wangu, na mara nyingi nikikwama nakuwa naye, hadi sasa, useme mimi simfahamu,….wewe ndio humfahamu unaigiza ndoto zako tu, haya niambia lini umejifunza kutumia silaha?’ akaniuliza.

‘Mimi nafaham kutumia silaha kama unvyofahamu wewe kutumia kijiko wakati wa kula,...’nikasema kwa mbwembwe , na yeye akaniangalia kwa macho ya mshangao, nikaendelea kumwambia;

‘Nipe hiyo silaha uone nitakavyoitumia, hilo kwangu ni dogo sana, na cha muhimu kwa sasa ni mimi kuipata hiyo silaha, sio jinsi gani ya kuitumia au kutaka kujua nilijifunza wapi kutumia silaha, huu sio wakati wa kuulizana hayo, ...cha muhimu kwa sasa ni muda, tunakimbizana na muda, sitaki huyu mtu aendelee kuwatesa watu...’nikamwambia.

Hapo akatulia kwa makini, baadae akasema;

‘Mhh, haya,... ndio maana kila mara upo na rafiki wa mke wangu, najua ni yeye kakufundisha ujinga huo.., lakini  uwe makini na silaha, mimi sipendi sana kushika shika silaha, sina ujanja huo...’akasema.

 Haya wajumbe kwa polisi hadi hapo wanaweza kumshuku tena huyu mtu, eeh, keshatoka hapo, kwa maneno hayo, sasa endeleeni kuyashika hayo mazungumzo, ambao ndio ushahidi wa polisi,.. awali muhusika alionekana ni mume wa familia, sasa uhusika wa mauaji unamtoka, ni nani mwingine

Kwa kauli zangu niliwahi kusema , …najua kutumia silaha,..mumeona hapo, pili natamani huy mtu afe akiendelea kuishi ni shida, au sio…nataka nielezee kila kitu kama ushahidi wa polis ulivyo, ili nikitoka hapa na kufikishwa kizimbani mje kuwa mashahidi wangu…kwa vile nastahiki au sio..niendee au nisiendee…’akasema akimuangalia mwenyekiti.

Mwenyekiti alibakia kimia, hakusema neno, ila wajumbe kwa pamoja wakasema.

‘Andelea, endelea..’wajumbe wakasema.

**********
 Hapa bado nipo na mwenzangu tunaongea,…kama ushahidi wa polisi ulivyo….

‘Mimi ninahitaji sana silaha kipindi kama hiki, lakini sitaki mtu afahamu kuwa nina silaha,..hasa rafiki wa mke wako, na nimekuambia haya tu, iwe siri yako, mimi nitamuwinda huyu mtu hadi kieleweke,…’nikasema

‘Mhh..haya bwana…’akasema mume wa familia

‘Kwa hivi sasa nahitaji sana silaha, na tatizo ni muda, ningeenda kuazima kwa watu wangu ninaowafahamu, japokuwa sipendi iwe hivyo, lakini muda,…na mimi sitaki ushahidi zaidi kwa watu wengine, nikiazima kwao, utakuwa ni ushahidi , na kwa hili sitakie liwe hivyo…hapo nje wapo watu walionileta  wananisubiria.’nikamwambia.

‘Oh, nimekumbuka jambo, ..unajua sisi tunayo silaha, silaha ya mke wangu,…’akasema

‘Mhh..kweli,..lakini utaipataje..?’ nikamuuliza

‘Mimi ninaweza kukupatia hiyo silaha sio kazi kubwa kwangu, nina ufunguo za makabato yote hadi hivi sasa…lakini mimi najiuliza tu, …nina wasiwasi na hilo, wewe unahitajia silaha ya nini, unataka kumuua nani, usiniambie umefikia hatua ya kutaka kumuua Makabrasha?’ akaniuliza kwa mashaka.

‘Hahaha, mimi sio muuaji bwana, ..na wala ….mimi sitaki kumuua mtu yoyote, na sina mpango huo, ila ikibidi..sitasita kufanya hivyo kwa kujilinda,..au ikibidi sana, kama ni lazima nitafanya hivyo kwa masilahi ya wengi, ni bora nifungwe lakini wengi wawe huru au sio….’nikasema nikiwaza jinsi gani ya kumfamisha mtu kama huyo.

‘Hapana hadi hapo unanipa mashaka..’akasema

‘Silaha ni muhimu sana kwangu kwa hivi sasa, kuliko wakati mwingine wowote…’nikamwambia hivyo

‘Nakuomba tafadhali usije ukafanya makosa kama hayo, nakuhitajia sana katika maisha yangu, na ukumbuke mimi ndio wewe na pendo letu ni la asili haliwezi kufutika abadani…sisi ni kama mapacha kwenye pendo,…’akasema akiniangalia kwa macho yaliyojaa huruma.

‘Mimi siwezi kufaya kosa kama hilo, niamini, mimi siwezi kuua, nitafanya hivyo, ikiwa ni lazima, najua sheria, najua ….na kwanini niue, kama ningelitaka kufanya hivyo ningelishafanya hilo jambo mapema sana, ...’nikatulia na yeye akainamisha kichwa chini…hayo mtayaona vyema kwenye ushahidi, ..naongea kama ilivyo

‘Sawa…naombea iwe hivyo…’akasema

‘Mimi nahitajia hiyo silaha kwa ajili ya kujilinda mimi mwenyewe, na zaidi ni katika kujihami..na sio kwa muda wote, ni kwa muda maalumu tu,..kwahiyo muda wake ukifika, nikiwa na hiyo silaha nitakuwa na amani sana, ninakuwa kama nina wasaidizi watano nyuma yangu, ..’nikamwambia na nikweli nikiwa an silaha, hunibabaishi, wanaonifahamu wanalijua hilo.

‘Unasema hiyo silaha ni kwa ajili ya kujihami, lakini hapo mimi nahisi kuna kitu kikubwa unataka kukifanya, wewe unanificha, …sikiliza sitapenda nije kusikia jambo kubwa limekutokea, nitajutia sana, na huenda na mimi, nikajiua…’akasema

‘Kuna jambo nataka kulifanya usiku wa leo, na asubuhi yake, ni muhimu sana niwe na wasaidizi wangu, na wasaidizi wangu ndio hiyo silaha..kama sitapata silaha, sitawezi kulifanya hilo ninalotaka kulifanya..huyu jamaa yetu kajizatiti kweli kweli, ana walinzi, ana mitandao ya ulinzi, ana mitambo ya ulinzi,.. kwahiyo hata nikiwa na silaha,…najiuliza nitafanya nini nayo, unaona hapo, kwahiyo kama ni kwa ajili ya kumdhuru huyo mtu, hilo mimi siliwezi....’nikamwambia.

‘Naona wewe unalako jambo, na kwa huyo mtu, wewe utajitakia matatizo makubwa, nahisi wewe hujamfahamu  Makabrasha vyema....na nikuulize hivi yule mtoto wake mkorofi si bado anafika fika hapo kwa baba yake, je huyo mtu utawezaje kumdhibiti….maana yule ni kichaa, eti kasomea sheria, mbona haviendani! ...’akasema

‘Umeona eeh..huyo huyo… mtoto kama baba,..’nikasema

‘Kwahiyo kumbe unataka kumuua huyo mtu…’akasema

‘Hapana, nani kasema nataka kumuua mtu,…nielewe mimi hapo, sina haja ya kumuua mtu, sio kazi yangu kufanya hivyo,..kwani mpaka sasa nimeshajitolea kiasi gani, kama ningelitaka kufanya hivyo, nisingejizalilisha hivyo, unasikia, mimi naweza kufanya lolote, lakin kwanini nifanye hivyo, hapana....’nikasema

‘Sasa haya bwana,….maana ni kweli hadi sasa tulishaamua kuwapa kila kitu, ili tu..wasije kutuchafulia majina yetu, na sipendi kwakweli, lakini hakuna jinsi, wa kulaumiwa ni sisi, najua kabisa,wakwe zangu watakuwa wanasubiria hili kwa hamu, nifukuzwe kama mbwa, maana, ushahidi upo..ndio maana nasema ni heri kujitolea hivyo kwasasa, huku tukitafuta njia muafaka, au sio…’akasema

‘Umeonaeeh, nashukuru sasa unaanza kunielewa, kuwa tatizo ni wewe, wewe ndio mkosaji ,…’nikamwambia.

‘Sote ndio sababu ya haya yote…huo ndio ukweli..’akasema na mimi hapo nikabakia kimia, akaendelea kuongea.

‘Sawa waweza kusema mimi ndiye nimewakose watu hao zaidi…najihisi kuwa mbaya kuliko…, sijui kwanini,..hivi kweli ni kwanini..kwanini mimi nakuwa na tamaa kupita kiasi, nilikosa nini,..mmh, haya yote yasingelitokea,…’akawa anaongea kwa kujijutia, lakini baadae nikasikia akisema

‘Hata hivyo…kiuhalisia  mikataba ile inanipa nafsi nyingine ya kufanya jambo, huenda nikashinda, unajua huo mkataba, unanipa mimi mamlaka ya kufanya kila jambo, kama mume wa familia....’akaniambia.

‘Upi huo..huo wa kugushi au,…hahaha, unafikiri mimi sifahamu janja yenu..’nikasema

‘Mimi sijui kama ni wa kugushi..’akasema

‘Haya sawa, vyovyote iwavyo, lakini wewe hujaliangalia hilo kwa mapana yake, hapo ulipo kwa lolote utakalolifanya kwa sasa, bado upo kwenye matatizo, hasa ya ndoa yako..’nikasema

‘Sawa lakini kwanini tusjaribu kwanza…’akasema

‘Tusi-au usi…mimi sihusiki na hayo mambo yenu,…kumbuka kuwa huo mikataba wa kugushi eeh, ni danganya toto, si chochoteni swala la muda tu..na hata hivyo hata ukiutumia je ni kweli utakuwa na amani na mke wako, atakubaliana na hilo..kiukweli nakuambia hili unisikie, hutaweza kuwa na amani, mke wako hataweza kutulia kwa hilo, na hataweza kukupatia hicho unachokitaka,..yeye sio mjinga, ni lazima atahangaika mpaka aupate ukweli, je huoni kuwa akiupata huo ukweli ndio itakuwa njia ya kuyabaini haya yote..na huku  kwa upande wa pili unakuwa mtumwa wa Makabrasha, hatujui mwisho wake utakuwaje unaona ilivyo...'akasema.

'Ni sawa, ..sasa tufanyeje,…?’ akauliza na mimi nikakaa kimia, akaendelea kuongea.

‘Ndio maana mimi ikifikia hapo, nasema bora tu iwe hivyo…nitakuwa mtumwa wa Makabrsha sawa, lakini nitakuwa na mali, au sio..na nina uhakika itafika muda, maana usinione nipo hivyo, natafuta njia, nahangaika lazima kuna namna na yeye eeh…nitamnasa tu, najua ipo siku ataingia kwenye anga zangu, ipo siku, ni lazima nifanye jambo, ngoja nione cha kufanya…’akasema

‘Hahaha, kwa Makabrasha..unajisumbua,…, hapo ulipo kila unachokipanga keshakifahamu, kama mwanga vile… wakati mwingine huyu mtu simuamini kama ni mtu wa kawaida,  kila ukipanga jambo analifahamu kabla..wewe hujaligundua hilo ...?' nikamuuliza.

‘Najua, yeye atakuwa kawekeza namna ya kupata mazungumzo…alishawahi kuniambia hilo, ana vifaa vya kunasia sauti, na matukio…lakini hataniweza ..hata mimi ni mjanja pia, wewe utaona tu ..’akasema kwa kujiamini.

'Haya bwana, ..hivi nikuulize kitu, hivi wewe  unaifahamu vyema familia ya mke wako..walivyo , wakwe zako,…achilia mbali utajiri wao, unawafahamu kuwa wanakuchunguza kila mara, unafahamu kuwa wana namna zao za kugundua mambo, na huenda walishakufahamu  ulichokifanya?’ nikamuuliza

‘Nawafahamu sana, uzuri wao, hawahangaiki sana na mambo ambayo sio muhimu kwao,…wanajifanya kufuata sheria,..zaidi ya hayo, kama ujuavyo wananichukia sana..walifikia sehemu wakasalimu amri..na kuniheshimu kama mkwe wao…ndio maana kwa hili nitajitolea kwa ajili yao, wananidai kwakweli, nijaitolea kuhakikisha kuwa hii kashafa imefutika…’akasema

‘Mhh….sasa nakuona umebadilika, sawa..lakini umeshachelewa,  familia ya mke wako, sio ya kuchezea, mimi nimeshaichunguza vyema tu, ni heri ya huyu Makabrasha anayetumia njia za mkato, lakini familia ya mkeo wako ni watu wa sheria…kumbuka hilo, umeshakiuka sheria, na sheria ndio itakuhukumu..kwahiyo hadi sasa jihesabu kuwa sio mkwe wao tena,…’nikasema.

‘Haahaha…ndio hapo nakubali niwe tu mtumwa wa Makabrsha, alichofanya namvulia kofia…sasa nikuulize hadi hapa ulitaka mimi nifanye nini…?’ akaniuliza

‘Hdi hapa umeshachelewa, kama ungelinisikia toka mwanzo, haya yote yasingelifika hapa, tamaa zako za kimwili, na akili fupi ya kufikiri ndio imekufikisha hapo ulipo, na hata sijui itakuwaje huko baadae, lakini acha iwe hivyo upate fundisho, mtoto mwingine bila kumchapa hawezi kukua, na wewe bila kuonja jela, sizani kam utaweza kubadilika…’nikasema

‘Usinizalilishe kihivyo…’akasema kwa hasira.

‘Huo ndio ukweli sio tusi, ,...sijui kama kweli haya yataisha kwa amani, na hata yakiisha kwa amani, sijui kama ndoa yako itakuwepo tena, na baya zaidi unaweza ukaishia jela, wakikuhurumia sana, watakutupa kijijini ukawe omba omba...’nikamwambia.

‘Thubutu, hilo halitatokea..ndio maana nakuambia hadi hapa namshukuru sana Makabrasha, kafanya nisichoweza kukifikiria,…ok, likitokea la kutokea, basi utafanya nini,..lakini muhimu jitahada…mimi nina imani tufanikiwa,...’akasema

‘Hahaha, unajipa moyo sio, utafanya nini wewe kufanikiwa hizo ndoto zenu za mchana…....?’ nikamuuliza

‘Tuyaache hayo, kwanza hebu niambie hiyo silaha unahitajia ni kwa makusudio gani hasa, ..kiukweli ukiniambia ukweli mimi nitakusaidia, kuipata hiyo silaha, ila nina mashaka na wewe hivi kweli wewe unaweza kuitumia..?’ akaniuliza.

‘Ni kuhusu huyo mtoto wake, yeye ndiye namuogopa sana, anataka kunifanya mimi kama anavyonifanya baba yake, siwezi kuzalilika kiasi hicho, silaha itanifanya nimdhibiti...nataka silaha ya kujilinda..’nikamwambia bila kumfafanulia mambo mengine ambayo niliyapanga kichwani mwangu,sikuwa namuamini sana kwenye mambo hayo ya kivita..

‘Kama kweli unahitaji hiyo silaha kwa jaili ya kujilinda sawa… mimi nitafanya kila mbinu hadi niipate hiyo silaha,..hilo niachie mimi , nitachukua silaha ya mke wangu…’akasema

‘Kwa vipi…?’ nikamuuliza

‘Kwa vile ni vigumu kutoka humu,…mimi nitamtumia mdogo wangu..ila tukubaliane kitu…maana ujua hiyo silaha sio yangu, kwahiyo hiyo silaha itakuwa inaletwa kwako usiku kama ukiwa na kazi za usiku, asubuhi tunairudisha mahali pake..unasemaje kuhus mpango huo…?’ akaniuliza.

‘Kama unaweza kuipata hiyo silaha,  itasaidia sana, nahitaji kuwa nayo sanasana usiku wa leo, na asubuhi utakapokwenda kukutana na Makabrasha, baada ya hapo inaweza isiwe na kazi tena, sitaihitajia kila siku ...’nikamwambia na yeye akaniangalia kwa mshangao, hakuamini kuwa mimi ninaweza kutumia silaha.

‘Sawa hilo litafanyika, usijali..’akasema

‘Sikiliza kwa makini, kesho ukifika kuonana na Makabrasha,..’nikasema

‘Wewe umejuaje hilo..!!!?’

‘Hayo sio muhimu wewe kufahamu fanya ninavyokuagiza, unasikia..’akasema

‘Ok sawa, wataka mimi nifanye nini…?’ akauliza

‘Mimi nataka wewe uwe unamchelewesha ili nipate muda wa kusimamisha mitandao yake ya ulinzi, na ...kwa vile mtoto wake, atakuwa hayupo, ...kama alivyodai, japokuwa simuamini, ...nitaweza kufanya mengine bila kujulikana, yote inategemeana na muda, muda ni kitu muhimu kwenye mapambano kama hayo...’nikamwambia.

‘Kwani unataka kufanya nini, mbona unanificha, maana mengi yameshafanyika, mikataba karibu yote nimeshaisaini kukubali, umebakia huo mmoja tu,.....na wewe mwenyewe umeshasaini mkataba wako, kilichobakia ni mume wako tu, na yeye nasikia alishakubali kuweka saini  yake ..’akasema mume wa familia.

‘Mhh..hayo ya mume wangu achana nayo…’akasema

‘Kwanini, au.kwanza niambie mume wako ulishaongea naye...?’ akaniuliza.

‘Kuhusu nini..?’ nikamuuliza

‘Kuhusu nini! Si kuhusu haya, ili…usije kuharibu kote kote, sitaki uje kupata shida, maana hili ni letu sote, ni muhimu tutimize lengp letu kwanza mengine yatafuata baadae au sio..?’ akasema

‘Siwezi kufanya ujinga kama huo, unafikiri mimi ni mjinga kama wewe...kanisainisha huo mkataba, nimekubali kufanya hivyo, lakini siwezi kuongea na mume wangu, kuhusu haya mambo, ..nafahamu kabisa mume wangu hawezi kukubaliana na hilo.., sana sana, hiyo itakuwa, ni kunitafutia njia ya kupewa talaka haraka..ndio maana nahitaji hiyo silaha...’nikamwambia.

‘Kumbe...ni kwa ajili yako tu…ili wewe usipewe talaka haraka, je mim, itanisaidia nini hapo,..ujue mimi ndiye nabeba dhamana ya hiyo kitu, kukitokea tatizo ni mini nitawajibika, au sio...’akasema kwa shingo upande.

‘Tatizo gani, mimi ni kwa ajili ya kujilinda, …hakuna…’kabla hajamaliza

 Kwenye simu yangu ukaingia ujumbe ukiniarifu kuwa  muda wangu wa kuongea na huyo mtu umekwisha ninasubiriwa nje tuondoke.

‘Kuna nini…?’ akauliza

‘Natakiwa kuondoka, muda umekwisha..’nikasema

‘Ndio hayo…tutaendelea hivi mpaka lini..’akalalamika.

 Kwenye huo ujumbe , pamoja na hili la kuwa muda umekwisha wa kuongea na mgonjwa, pia kulikuwa nanyongeza ‘nisisahau kuwa usiku wa leo kuna kazi…’

‘Kuna kazi..sawa..’nikajikuta nimesema hivyo, mimi nilifahamu hilo, lakini kuna kitu kilinitia mashaka mume wangu, alinitumia ujumbe kuwa anataka kuja huko kujijini, kunifuata , yeye anajua nipo huko kijijini… itakuwaje…je akifika huko kijijini akinikosa itakuwaje…kiukweli hapo akili ilishaanza kutatika.

‘Je hiyo silaha inaweza kupatikana  kwa usiku wa leo, ...?’nikamuuliza nikiwa sasa najua hilo jambo lifanyika na mimi nitoweke, niende kwetu kijijini, huko nitatulia kwa muda, nikisubiria matokeo.

‘Nitajitahidi..lakini….’akasema

Nikianza kuondoka, na wakati huo, mume wa familia alikuwa akitaka kuongea jambo, mimi sikuweza kumpa nafasi tena.

Nilipofika mlangoni nikageuka kumuangalia mume wa familia, maana alikatiza kuongea, sikuwa na uhakika na kauli yake, nikasema

‘Mimi naondoka, …ni muhimu..’nikasema

 ‘Hilo niachie mimi, ...silaha itapatikana, na natumai hutaifanyia jambo la kijinga...’akasema na mimi nikasimama, ghafla nikageuka na kurudi pale kitandani, nikamwambia, kwa sauti ya chini chini;

‘Usiku wa leo kuna tafrija kwenye lile jengo, itakuwa ni nafasi nzuri ya mimi kuweza kuipenyeza hiyo silaha bila kujulikana,..je una uhakika leo itapatikana,…?, kama kweli itapatikana usiku wa leo muda wa saa tano hivi, itakuwa vyema, je mke wako hawezi kuhisi kuwa silaha yake haipo, hilo ni muhimu kufahamu?’ nikamuuliza.

‘Mara nyingi haitumii hiyo silaha.., ipo kwenye kabati lake siku zote, sijawahi kumuona akiichukua kwa muda mrefu sasa.., hata kama kuna tukio la hatari, kama ilivyokuwa zamani, sijui kwanini,  ipo tu..sizani kama atakuwa na wasiwasi nayo...’akaniambia.

‘Basi wewe jitahidi, mtume mdogo wako,akaichukue ...mimi nitawasiliana na yeye, nione jinsi gani nitakavyoichukua hiyo silaha, lakini asifike sehemu ya mapokezi, anyway mimi nitaongea naye baada yaw ewe kuwa na uhakika wa kuipata sawa, au sio..’akasema

‘Hilo kwa ajili ya kuipta haina shaka…mengine nyie wawili mtajua, jinsi gani na wapi pa kukutana naye, kazi yangu ni kuhakikisha hiyo silaha umeipata au sio…’akasema

‘Ni muhimu yeye asije kuonekana yupo na mimi, au kuonekana karibu na hilo jengo, najua hata akionekana na mimi, nitakuwa sio mimi, hayo nayafahamu mimi mwenyewe, ..ok, tumemalizana, au kuna jingine...’nikamwambia.



Na mpaka hapo tukawa tumekubaliana hivyo...na tulikuwa tukiongea nje kwenye eneo analochukulia mazoezi ya viungo kwasababu ya matatizo yake ya ajali.

‘Na kweli usiku ule nikaipata hiyo silaha, silaha iliyokuja kumuua Makabrasha,...swali ni je niilipata pata vipi hiyo silaha, na ilitumikaje, nitawaelezea yote hayo..kama mwenyekiti ataniruhusu….’akasema na kutulia kidogo, akamwangalia mwenyekiti.

Mwenyekiti alikuwa akiangalia saa, na mara shahidi huyu akaenda pale alipokaa mwenyekiti wakawa wananong’ona, sikujua wanaongea kitu gani, lakini walipomaliza kuongea, mwenyekiti alichukua simu na kumpigia mtu, huku akiwa kamuangalia huyo shahidi kama vile anaogopa jambo kutoka kwa huyo shahidi.
. ...
NB: Je silaha hiyo ilifikaje kwa shahidi, na je ilitumikaje kumuua Makabrasha na je kwanini shahidi huyu anaongea sana na mwenyekiti, tukutane sehemu ya tatu ya hitimisho la kisa hiki.

WAZO LA LEO: Kila hila mbaya, ina walakini wake, na mwisho wa hila mbaya, ni kuumbuka tu, hakuna hila mbaye yenye kudumu.


Ni mimi: emu-three

No comments :