Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Friday, March 9, 2018

MKUKI KWA NGURUWE-92



Watu wote walikuwa kimiya wakitaka kusikia kauli ya shahidi huyo mpya, hasa pale alipotoa ombi,kwa mwenyekiti, la kuomba jambo ambalo hakuliweka wazi,  na mwenyekiti akiwa na mashaka na huyo shahidi akamuuliza ni ombi gani hilo,

Tuendelee na kisa chetu..........


‘Kitu gani unachotuomba, ..?’ akauliza mwenyekiti

Badala ya shahidi kuongea, …yeye akatoka pale alipokuwa amekaa, akimpita mumewe, na kutembea kwa haraka hadi pale alipokaa mwenyekiti na kuanza kumnongoneza jambo…

Mwenyekiti, ilimshika kwa shutukizo, hata hivyo akawa makini kusikiliza kile anachonong’onezwa, huku mke wa mwenyekiti akiwa anatizama tukuio hilo kwa macho yenye shauku au mshangao fulani.

Kwa jinsi ilivyoonekana, mwenyekiti alionekana kama kutokukubaliana na hicho anachoongea huyo shahidi, akaonekana kama kupinga, kwa kutikisa kichwa mara kwa mara kama kukataa, lakini huyo shahidi hakuonekana kukata tamaa,...

Baadaye mwenyekiti akasema , kwa sauti ambayo tulimsikia ;

‘Nitampigia yeye mwenyewe, atajua ni nini la kufanya lakini mimi sitaki kabisa  utaratibu huo...’akasema.

Shahidi akaonyesha ishara kuwa hataki hayo wanayoongea yasikiwe na hapo mwenyekiti akashusha sauti..na wakaendelea kuongea kwa namna hiyo na shahidi akazidi kusisitiza jambo, na alipoona mwenyekiti hakubaliani naye, akainuka maana pale alikwua kamuinamia mwenyekiti.

Ilionekana sasa kakata tamaa, kwanza hakugeuka moja kwa moja kule alipotoka, alichofanya ni kusogea kinyume nyume akiwa kama katahayari, hatua moja mbili kinyume nyuma halafu kawa haraka  akageuka na kurudi sehemu yake.

Alipofika pale alipotakiwa kukaa,…maana yeye alikuwa akiongea akiwa pale pale sehemu aliyokuwepo, kinyume na wengine ambao walikuja mbele sehemu maalumu ya muongeaji,..alipofika pale karibu na mumewe, mumewe akamuuliza

‘Ulikuwa unamuambia nini mwenyekiti..?’ akauliza docta, lakini mdada hakumjibu mumewe, moja kwa moja akaanza kuongea;

‘Nafahamu kabisa wote humu ndani ni watu wenye hekima, akili na utashi wa kufikiri, haya nitakayowaelezea hapa ni mambo ambayo sikustahili kuwaelezea, ni mambo ambayo nilitakiwa niwaelezee polisi,..kwa utaratibu ulivyo, na hata mwenyekiti anafahamu hilo..’akatulia

‘Hata hivyo, mimi kwa uoni wangu, nahisi haki inaweza isitendeke, kama hali ilivyo itaendelea kuwa hivi..mimi ndiye niliyehusika moja kwa moja na tukio lilitokea ndani kwenye muhusika mkuu, hapa nikiwa na maana marehemu..na ndio maana polisi wananihitajia au sio…’akatulia akimuangalia mwenyekiti.

Lakini kuna mambo yalifanyika hata polisi hawafahamu, na sikutaka kuwaambia wao kwanza, kwasababu nafahamu kabisa watakumbilia kunishikilia, na wakifanya hivyo kuna mambo meng ya ushahidi yatapotea…

Sasa kwa ajili ya kuliweka hili jambo sawa, nimeamua kumuomba mwenyekiti aniruhusu niweze kuliezea hilo tukio kiundani zaidi, ili nyie muwe mashahidi wangu, na sitaongea uwongo, nataka niuseme ukweli wote ulivyokuwa,…leo nipo hapa, kesho naweza kuwa jela, na jela ni jela..huko nina maadui wengi, je nisipotoka hai,..je kesi hii ikichezewa faulo,..najuo hilo ndilo linataka kufanyika…’akasema

‘Na zaidi sitaki watu wakitoka hapa wawe na maneno yenye utata, nataka nyie mkitoka hapa muwe na ukweli,..ambao utaweza kuwasaidia wenye haki zao, kwasababu hili halitaishia hapa, hivi ni vita virefu vyenye hatua zake, leo hii nitakamatwa mimi, kesho itajengwa haoja nzito, ..nina wasiwasi sana na hili…’akatulia

Mwenyekiti sasa alikuwa akiongea na mkewe, wakawa nao hawakubaliani, inaonekana hilo swala sasa linakuwa nyeti, na mwenyekiti anakuwa kwenye wakati mgumu.

‘Najua nitakamatwa, na…mume wa familia …lakini je nikikamatwa mtakuja kuamini hayo watakayosema polisi, …kuhusu muuaji, …hebu kwanza niwarejeshe nyuma kidogo, nilipowahi kuongea na marehemu kabla ya kifo chake, aliniambia maneno ambayo nayakumbuka sana, na leo hii naona kama yanaweza kuleta mantiki japokwua tunaweza kusema aliyaongea kuhalalisha dhamira yake...

Mwenyekiti aliposikia hivyo, akainua simu yake na kumpigia mtu, na kumfanya shahidi atulie kwanza, na mwenyekiti akawa anaongea na simu huku akiwa kainama na alikuwa akiongea kwa sauti ndogo, kama vile hataki watu waliopo humo ndani kusikia anachoongea, na alipomaliza akasema;

‘Samahani kidogo, nilikuwa naweka mambo sawa, ...haya shahidi unaweza kuendelea na maelezo yako, lakini bado, sijarizika na hoja yako, endelea kutokana na ulivyoamriwa, unasikia, sehemu za kipolisi hapana, sija…endelea....’akasema mwenyekiti akionyesha kukerwa na kitu, na shahidi akatulia kwanza akimuangalia mwenyekiti na baadaye akasema;

‘Ni hivi...Makabrasha hayupo peke yake, japokuwa wenzake, wameamua kujifanya hawahusiki, na hata mimi sikuwahi kuwa na hawo wenzake kwa karibu,ila niliwahi kusikia wakiongea na Makabrasha wakipanga mipango yao..’akatulia akimuangalia mwenyekiti kwa uso wa kusubiria jambo.

Makabrasha alikuwa akitumika, …kuna watu wakubwa walikuwa juu yake na wao hawakutaka kufahamika,..na kwa nafasi yangu siwezi kusema lolote kuwahusu hao watu, lakini ni mambo ya kisiasa na upinzani wa Nyanja hizo,…

Kuna mtu mmoja ambaye alikuwa akifika mara kwa mara kuonana na Makabrasha,  …nitakuja kumuelezea mwishoni kama mambo yakienda sawa huyo alikuwa kama mtu kati, na mambo yake sio rahisi ni mjanja ..mwenyekiti, niendelee au  ....’akaelezea huyu shahidi akimuuliza mwenyekiti, na mwenyekiti akawa kimia tu, yaonekana alikuwa hataki hicho anachotaka kukielezea huyo shahidi.

‘Kwahiyo hili jambo sio swala dogo kama mnavyolifikiria nyie, ...mimi nitajitahidi kuelezea upande wa mtu wetu tu, ambaye anatuhusu sana,...huko kwingine hakuwahusu, kwahiyo ni bora nifuate sheria, lakini nitaelezea yale yenye kulata tija...kwa manufaa yenu, na kwa manufaa yangu pia,...’akainama kama anasoma jambo.

‘Nimesema nitawarejesha nyuma kidogo, ili muweze kunielewa, kwa wenye kuelewa wataelewa, na hata mkisikia leo nimekamatwa, au ku-uwawa, mjue jinsi gani ya kulieleza hili kwa jamii...’akasema sasa kwa sauti ndogo yenye kukatisha tamaa.

‘Mwenyekiti nafahamu toka awali umekuwa makini na swala hili, nafahamu ni kwanini, na nafahamu kuwa wewe na polisi mnaaminiana sana, lakini nakupa angalizo, kuwa kumbukumbu nyingine walizokupa wewe, ni za uwongo, kuna mambo wameyaficha..’hapo akasema kwa sauti na mwenyekiti akataka kumkatiza shahidi.

‘Mwenyekiti hili inabidi nikuambie …maana naona utafanya nishindwe kabisa kuelezea kile ninachotaka kukuelezea,…hao polisi, siwalaumu maana wao wanafanya kazi kutokana na ushahidi…lakini ushahidi waliokuja kuupata ni wa uwongo, ukweli halisi ulishaharibiwa,,,kwa  makusudi, huenda ni katika mbinu zao kwa ajili ya kufanikisha kazi zao, au ni kwa ajili tu ya kuficha ukweli...mimi huko sitaongelea sana kuthibitisha hilo, lakini huo ndio ukweli, ..nakusihi mwenyekiti usiegemee kwenye ushahid wao wa moja kwa moja, kama ningepata nafsi ya kuliezelea hil kiundani ungelinielewa....’akasema

Mwenyekiti sasa akaniangalia mimi, na mimi pale nilipo nilitaka kumuambia mwenyekiti amruhusu tu mzungumzaji ili tuusikie huo ukweli, akam ni ukweli ili mambo yaishe, lakini kwa nafasi ya mwenyekiti ilikuwa ni ngumu sana, nililielewa hilo, siwezi kumlaumu mwenyekiti..lolote atakalofanya sasa linaweza kutafsiriwa vibaya,na inaweza kumweka mahali pabaya..

‘Nafahamu kabisa kuwa mwenyekiti hunifahamu undani wangu, zaidi ya historia ya wazazi wangu, ila kwa hapa Dar, hukuwahi kunifahamu nilichokuwa nikikifanya zaidi ungeliweza kunifahamu kwa kupitia kwa bosi wangu..zaidi ni kunielewa kuwa mimi ni mke wa docta, na wewe ulikuwa mstari wa mbele kuipinga ndoa yangu…’akatulia

‘Kiukweli mimi siwezi kukulaumu sana kwa hilo, ...kwa vile unafahamu sana asili ya huko nilipotoka, na kwa hekima zenu, haya yanayotokea kama tungeliwasikiliza nyie huenda haya yasingelitokea. Au sio ..?’ akawa kama anauliza

‘Lakini mimi nasema tu vyovyote iwavyo, yote ni maisha, haijalishi wewe unatokea nafasi gani katika maisha, uwe masikini au tajiri maisha yanawezekana, au sio, lakin kama mzazi ulijaribu kutimiza wajibu wako, na kwa hilo siwezi kukulaumu, ila sasa, dunia itabadilika vipi kama tukijitenga, ina maana wenye nacho watabakia kuwa nacho na wasio kuwa nacho wazidi kudidimia, hapo ndio namkumbuka marehemu....’akasema shahidi.

Marehemu aliniambia,…vyovyote iwavyo, tajiri hawezi kumuamini masikini, akishajua kuwa wewe ni masikini, na unatokea daraja hilo, itampa shida sana kumuamini mtu kama huyo..na vyovyote iwavyo, tajiri hatapenda kushirikiana kwenye utajiri wake na masikini, kwanini, ..ni kwa dhana ile ile ya kutokumuamini..

 Marehemu alitokea kwenye maisha duni, japokuwa alisoma, …ni maisha kama haya ya kwetu, …mimi nilikuja kuliamini hilo, kama alivyokuwa akiongea marehemu, ndio maana nikawa najichanganya, nikawa nahangaika , licha ya ndoa, wengi wananifahamu kama mama shughuli, leo nipo hapa kesho nipo kule, hata mshirika wangu hajui zaidi ya kunitumia kwa manufaa yake

‘Huyu mume wa familia hadi hii leo, hajaniamini kuwa mimi …nilivyo sasa sio kam yule aliyekuwa kipindi kile,, na zaidi kanitambua tu kama  mama shughuli..’akasema akimgeukia mume wa familia, ambaye naye kama wengine alikwua akimuangalai huyu mdada, kama mgeni fulani, sio kama yule mdada aliyekua akimfahamu.

‘Anayenifahamu vyema kwenye uhalisia wa sasa, ni  rafiki wa mke wa familia, kwani yeye ndiye aliyekuwa bosi wangu, yeye ndiye aliyenibadilisha kutoka binti wa kijijini hadi kuwa mdada anayejitambua, mdada jasiri..lakini ujasiri nilio nao una kikomo chake, maisha ya binadamu yana mahali unafika uanshindwa, ndio maana hata docta aliponishauri mambo mambo ya kujibadili, alivyotaka yeye, alishindwa, kwanini….maji yalishanifika shingoni..

‘Inabidi niwaambie haya ili mje kuyaunganisha na tukio nzima, naomba msinichoke, nataka niliongee hili ili kila mtu alielewe ili kesho na kesho kutwa msije kuongopewa,
Sawa mwenyekiti amekuwa akiniuliza hili swali mara kwa mara, je ni wewe ulimuua, je ni nani kamuua marehemu..

Sio rahisi kulitamka jibu lake hivyo..naweza nikatamka, ndio ni mimi, au ndio sio mimi..huoni hapo kuna ‘ndio’…yawezekana nimetamka hivyo kumlinda mtu au kujilinda mimi mwenyewe, ndio maana nataka ukweli, na hali halisi isikikwe kwanza, kabala ya hitimisho ..’akatulia

‘Ndugu zangu…nawaambia haya, ili siku ya kesi, mjazane mahakamani ili ikiwezekana muwe mashahidi wa kuitafuta haki,…namuomba mungu kama mambo haya yatakwisha kwa amani, basi sitaki tena kazi hizi za hatari..sitaki tena …’akaonyesha mikono kama kunawa.

‘Lakini nataka maisha niliyopitia yawe ni funzo kwa wengine.., kiukweli mimi nimeshajipanga kivyangu, maisha ni popote, hata kijijini inawezekana....hilo nimeamini na ndivyo nataka maisha yangu yawe huko. Kama sitakiwa jela,…

Mzungumzaji akamuangalia mwenyekiti, ni kama anasubiria kitu kwa mwenyekiti, lakini mwenyekiti alikuwa katulia tu.

‘Mimi ninachotaka kuwaelezea ni jinsi gani ilivyotokea, siku Makabrasha alipouwawa, hili mwenyekiti hataki, kwa vile linagusa taratibu za kipolisi, lakini utalikwepaje wakati limefungamana na hii kadhia nzima,..’akasema

‘Ni kweli mimi nilikuwepo kwenye hilo jengo, lakini huwezi kufikia hatua hii ya .......na kwanini ilifanyika hivyo, kuna mambo muhimu lazima yafahamike kwetu , kwenu ..nina maana hiyo…..’akatulia kidogo akimwangalia mwenyekiti, kama anachelea kuongea jambo, lakini mwenyekiti akamuashiria asendelee kuongea hilo analotaka kuongea;

***********
‘Makabrasha alikuwa na maadui wengi, na wengi wao, walifikia hata kumlaani,na inapofikia hatua wanadamu wenzako wanakulaani, wanatamani hata ufe, ujue wewe huna thamani tena katika hii dunia, hata kama ni tajiri, lakini ndani ya mioyo ya watu, wewe ni mfu, ...’akatulia.

Kwa jinsi ilivyo mzungumzaji alikuwa anasubiria kibali cha mwenyekiti, na mwenyekiti alionekana naye akisubiria kibali kutoka kwa watu wa usalama, kwahiyo mzungumzaji akawa anaongea kwa kutegea akivuta muda, muda ukawa unakwenda.

Mwenyekiti alikuwa katulia kama anawaza jambo, lakini baadaye akachukua simu yake na kumpigia mtu akawa anasikiliza na kuwafanya watu watulie wakisubiria hata shahidi huyo alionekana mwingi wa wasiwasi , hadi mwenyekiti alipomaliza kuongea na simu, halafu akaonyeshea kidole gumba, kuashiria mambo yapo shwari..

‘Endelea shahidi uwanja ni wako, nimeshafikisha ujumbe wako, ila kama ujuavyo, baada ya maelezo yako, hakuna jinsi, vyovyote iwavyo, utanisamehe kwa hilo.....’akasema mwenyekiti na shahidi bado akiwa na wasiwasi akasema;.

‘Katika maisha yetu haya, watu wana matatizo yao, wengine hawajui wataishi vipi, wanahangaika usiku na mchana, ili wapate angalau riziki zao...lakini maisha ni magumu, usiombe..., watu hawa wenye maisha magumu, kamwe hawana utulivu wa moyo…’akaguka huku na kule kama anawasiwasi fulani.

‘Nazungumzia maisha yangu nilipotokea au sio, nazungumzia maisha ya watu kama Makabrasga walipotokea, nazungumzia maisha kama ya mume wa familia alipotokea,…watu wa chini, watu ambao hawana amani ndani ya nafsi zao, japokuwa kiwili wili utamuona yupo,...ndivyo maisha ya walio wengi yalivyo, watu kama hawa wanatafuta upenyo litokee jambo watoe hasira zao, litokee jambo watumie kama sababu...’akasema na kugeuka kumwangalia mume wa familia.

‘Watu wana matatizo yao makazini mwao, wananyonywa, wanachokifanya hakiliangani kabisa na kile wanachokipata, nguvu kazi yao inatumika vibaya, kazi wanayoifanya na malipo yake ni viti viwili tofauti, anayefaidika ni tajiri, na hata akipata ziaida ya kupindukia ni nadra sana kukumbuka,...hakuna anayewajali, wanahangaika, kupata, agalau huduma muhimu, angalau mahitajio muhimu, lakini kipato chao hakikidhi hata hizo huduma muhimu. Watu hawa wakipata njia, wanaweza kufanya jambo baya sana. 

Watu  wahali ya chini, wanachokipata ni kama vile wenzetu wanavyosema tonge mdomoni, hata mdomoni kwenyewe ni kama onja –onja, unategemea huyu mtu atakuwa na amani kweli...huyu akipata nafasi ya kufanya unyama ataufanya unyama kweli, ..hata kuua kwake itakuwa ni sehemu ya kama kulipiza kisasi..

Watu wana matatizo sana huko kijijini , usione watu wapo kimiya, mtu analima mvua hakuna, pembejeo hakuna, anatumia jembe la mkono, mtu huyu kila siku anakatwa kodi, kila anachonunua, ni kodi, akigeuka huku kodi, mtoto wake wanadaiwa ada, yeye anaumwa magonjwa yasiyohesabika, akienda hospitalini, hakuna dawa, akipatacho nini…anayefaidika san asana ni huyu mnunuzi anayekuja kununua kwa  mkulima na kwenda kuwauzia wengine,..sio mkulima..huyu mtu akipata nafasi unafikiri atafanya nini..

Sio kwamba naongea haya kuwatetea watu, kama Marehemu, kama mume wa familia au kama mimi,  naonega kiuhalisia, maana kwa bahati nzuri nimetokea huko na uzuri nimeweza kuishi na matajiri, nimeyaona hayo hata kwenye kazi zangu, hivyo…ndivyo ilivyo, asikudanganye mtu…ndio maana hata mwenyekiti hataki kuniamini..unafikiri ni kwanini..ni hulka,..za matajiri dhidi ya masikini..

Mwenyekiti pale akakuna kichwa, kama kusikitika, lakini…hakusema neno

 ‘Siku tulipoongea na mwenzangu tuliyajadili haya maisha yalivyo, na siku nilipoongea na Makabrasha kabla ya kifo chake yeye aliniambia hayo..ni muhimu sana myasikie...

Yeye alipenda kusema ‘system,’ akiwa na maana wale wenye mamlaka, wale waliopewa dhamana, …na zaidi wenye uwezo, hasa wawekezaji,…yeye marehemu aliwahi kuniambia hivi

‘Huko kwenye system(utawala, na wenye mamlaka, matajiri na wawekezaji, akiwa na maana hiyo),...ndio haki za wanyonge zinapopotelea, wahujumu, walaghai, wadhulumaji,mafisadi, wamejificha huko…, na huko ndipo kwenye watu wanaojifanya ni watetezi wa wanyonge, wakija kwenye majukwaa wanakuja kwa lugha nzuri tu, na wanajua jinsi gani ya kuwadanganya wanachi..

‘Mimi kama mimi, najau wengi wananichukia sana, ila mimi nimepata kuutumia ujuzi wahuu na taaluma yangu hii kuchukua kile walichoiba kwa wananchi na kukirejesha kwa wananchi…’akasema na mimi sikumuamini kwa kauli hizo..hadi nilipofuatilia kwenye ofisi yake na kuyaona hayo kwa vitendo.

Hili hamuwezi kuliamini, ndivyo marehemu alikuwa hivyo, kwanini hamuoni hilo, ukweli wa upande wake wa pili umefichwa, ila yeye alikuwa na vitega uchumi vichache tu, mali yake nyingi, aliyokuwa akipata, yeye alikuwa akiwapeleka masikini, wazee wasiojiweza kule kijijini kwao, ndio maana hadi leo ukienda kule mtu huyo anaheshimika sana

Watu walikuwa wakijiuliza ni kwanini mtu mkorofi kama huyu hafungwi, hakamatwi..huyu mtu aliheshimika, kwa wasiojiweza, alipata Baraka zao, kwa upande huo alikuwa na watetezi, huku akitumia kila mwanya wa sheria kujilinda…’akatulia

‘Hili wengi wataliona ni la ajabu, maana mazuri ya mtu huyu yakichanganyikana na mabaya yake..na mazuri yake ilivyo, hupotea tu..,..na hasa ukiwa kwenye usawa wa mtu wa daraja la chini kama sisi, ni nani atakuamini hata utende wema vipi..mimi mwenyewe kipindi nilichofanya kazi kwake nilikuwa nikishiriki kwenye kazi za kuwahudumia wale wasiojiweza kutoka kwenye mfuko wake maalumu aliouweka kwa kazi hiyo…

Makabrasha alikuwa akiwalipia,wasiojiweza shule, alikuwa akiwasaidia mayatima, alikuwa akiwasaidia wagonjwa kwenda kutibiwa nje.., angalia kumbukumbu zake, mtaziona hizo, lakini kumbukumbu hizi zilikuja kupotea, mimi niliziona na shule alizojenga, nazifahamu, lakini hakutaka watu wafahamu hilo, ni kwanini…mimi sijui.

‘ Zaidi ni kuwa huyu mtu alikuwa akitumiwa na huyo mpinzani wako mzee, mpinzani wako alikuwa mjanja, alikuwa akiuma na kupilizia, akienda kijijini, anawekeza kwa watu kama hao, na …ndio hivyo, mambo ya kisiasa yalivyo au sio…

Labda sera hizi huyo mpinzani wako… alizipata kutoka kwa marehemu, kuchukua kwa matajiri kurejesha kwa wayonge, japokuwa yeye alitumia njia hizo mbaya kuzipata hizo pesa au mali, na yeye aliona njia hizo ndio rahis kwake,, ..huyo ndiye Makabrasha.

Simtetezi jamani..ila nazungumza hali halisi, na sisemi haya kwa nia ya kutaka kujitetea hata mimi, ila kwenye ukweli tusema,..haya yatakusaidia hata wewe mwenyekiti, kuwa katika maisha, msijiangalie nyie wenyewe kama matajiri, kuwa masikini hafai kuoa au kulewa na tajiri, ili mfanikiwe jichanganyeni na masikini, wasaidieni masikini, ili na wao wawaone nyie kwa jicho la rehema.

  Swali kama huyo mtu alikuwa hivyo, ni kwanini akauwawa,…..na ni nani hao waliofanya hivyo,…ndicho wengi wanakisubiria hapa au sio…lakini ukweli kwanza uili mje muone mazingira yaliyokuja hadi huyu mtu akauwawa..na sio rahisi kama watu wanvyoona..sio rahisi mtu mwenye akili zake kubonyeza trigger…
Na hilo halikufanyika …kirahisi hivyo,…kumbuka mazingira ya marehemuilikuwa ulinzi hadi akitembea ana vitu vya kumsaidia kumlinda, ikitokea hatari akibonyeza kitufe fulani, walinzi wake wameshafika…na kila anachoongea kilirekodiwa, mwisho wa siku anafuta kile alisichokitaka..huyu ndiye marehemu..

Swali alikujaje kuuwawa…kuna kitu mjifunze ukitaka kuficha kiatu, sehemu nzuri ni sehemu kunapowekwa viatu au sio..na mbaya wa mtu ni mtuwe au sio…adui wa mtu ni rafiki yake mkubwa,…sio rahis kwa mtu huyu aliyejilinda hivyo kuuwawa kirahis hivyo tena ndani ya sehemu yenye kila zana zake za kujilinda,…

Hamfahamu ofisi yake ilivyo..humu aliwekeza kila kitu chenye kumsaidia kujilinda, nahisi alitumia pesa nyingi sana, na yeye alikuwa akisema, akiwa ofisini kwake, anajihisi yupo salama kuliko sehemu yoyote…lakini humo humo ndio alipouwawa,..jiulize ni kwanini, …

Polisi hadi leo, hawajawa na uhakika …japokuwa wanadai kuwa wameshaupata ushahid lakini je ushahidi huo ni kamilifu,…kumbuka ukweli wote ulishaharibiwa, kilichobakia ni yale yale aliyokuwa akiyafanya marehemu..yamemrudia,…sasa je ni kweli kuwa hao washukiwa ndio kweli walifanya hivyo, na kama walifanya hivyo walitumia mbinu gani…

Kumbuka ulinzi, kumbuka zana zilizopo hapo,..je masikini anaweza kuvuka hivyo vihunzi…hahaha…ni movie yenye ujasiri…

Mwenyekiti, sasa naingia sehemu nyeti,…naomba univumilie, na naomba haya mazungumzo …wakili, haya ni mazungumzo nyeti, weka vitega masikio vyema, weka vitega sauti vyema, ili mkipae kile chenye uhakika,…najua baada ya hili,..nitakuwa nikibebwa kama muuaji, lakini ..ni bora niongee huu ukweli, ili mwisho wa siku, kama nitaonekana mimi ndiye muuji, basi niwe shujaa…’akasema na kuinamisha kichwa chini.

‘Shujaa wa mauaji, hapana…’aliyesema hili ni mama

‘Nianze mwenyekiti…?’ akauliza mzungumzaji, akimuangalia huyo mama, …na mwenyekiti, akawa anaangalia saa yake, na hakusema kitu pale pale akaangalia dirishani, akanyosha kidole kuwa muongeaji asubiri kidogo…

WAZO LA LEO: Kifo hakina hodi, kifo kila mtu kitamkuta kwa wakati wake, hata kama upo ndani ya handaki, hata kama wewe ni tajiri kupindukia ukawa unalindwa hata ukiwa chooni, hata kama umejizungushia gilasi zisizopitisha risasi, siku ikifika imefika,..hata kama wewe ni masikini, siku ikifika imefika,…

Sasa kama hivyo, kumbe kuna mwenye mamlaka na uhai wetu, ambaye hawezekani, asiye na mfano wake, alipangalo kuwa liwe litakuwa,basi ni kwanini hatumuogopi yeye, tukamtii yeye, kwanini tunafikia mahali tunatakabari, tunakiuka maadili mema, tunaghilibika kwa tamaa za mali, utajiri, utawala, kama vile tutaishi milele, tuikumbuke siku hiyo ambayo, mtu ataicha mali yake, watoto wake, mpenzi wake,…utawala wake, imebakia kauli,..’yote ni mapenzi ya mungu…’


Ewe mola wetu tujalie tuwe na mwisho mwema…Aamin.
Ni mimi: emu-three

No comments :