Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Wednesday, March 7, 2018

MKUKI KWA NGURUWE-91


 Kuna mtu alikuwa analia, ikaja kugundulikana kuwa ni mume wa familia, ..na ndipo shahidi aliyekuwa akizungumza akasema, ;

‘Utalia sana,na hapo ndio nimeanza…’

Tuendelee na kisa chetu

*********

‘Wewe niache nilie, ujue mwanaume akilia kuna mazito, wewe hujui tu, wewe hujui ulivyoharibu, mumeniharibia maisha yangu,  na kwa hili utakuja kunikumbuka, …hutafanikiwa kamwe, na hiyo mipango yako na waliokudanganya, utakuja kujuta.. ’akasema mume wa familia.

‘Kufanikiwa, au kujuta kwangu sio hoja, hoja ni ukweli wote ubainike, ili haki iweze kutendeka, ndicho mimi ninachokitaka,  baada ya huu ukweli … kila mtu atabeba mzigo wake yeye mwenyewe,na maisha yataendelea tu…’akasema mzungumzaji.

‘Nilijua tu…haya sawa ngoja tuone…’akasema mume wa familia kwaunyonge.

‘Kwani.., wewe ulitakaje, kuwa haya yaendelee hivi hivi, wakati ukweli upo bayana, na ukweli ni kuwa dhuluma haitadumu, ni lazima mwisho wa siku utagundulikana tu, na ni heri nusu shari kuliko shari kamili. Kama nilivyosema awali mimi sio yule binti wa kijijini asiyejua kitu, asiye na ufahamu, ..elimu niliyopata japo kidogo, imenizindua, naifahamu sheria, naifahamu haki, ..na kwa hili nafahamu kabisa huna lako, utegemee huruma za mke wako tu..’akasema muongeaji.

‘Sawa…endelea kufungua bakuli lako, tuone mwisho wake utakuwaje,…ukitoka hapa unaelekea jela, unafikiri ni nani wa kukusaidia….hao watu eeh, hahaha unajidanganya tu..’akasema mume wa familia.

‘Ndugu mwenyekiti….’muongeaji akawa anataka kulalamika, ili aweze kuendelea maana mume wa familia anamkatiza kila akitaka kuendelea. Na kabla mwenyekiti hajasema kitu, mume wa familia sasa akasimama.

Wakili wake alipoona hivyo, akawa anajaribu kumzuia huyo mume wa familia, haikueleweka lengo la huyu mume wa familia kusimama ni nini, kuwa laba anataka , kuondoka au kumzuia muongeaji asiendelee kuongea.

‘Sikiliza,..niamini mimi haya yatakwisha, nakuambia ukweli haya yatakwisha, si unataka turejee kule tulipotoka, sawa, haya lakini tatizo polisi wanasubiria, jela inanukia…’akasema

Hapo mwenyekiti akaamua kuingilia kati na kusema;

‘Mume wa familia, usivuruge utaratibu, hebu kaa chini, nakuona sasa unaleta vurugu, kitu gani unaogopa, muache shahid aendelee, hapa kila mtu anataka kusikiliza ushahidi wake,..sitarudia tena kukuonya, kwasababu kikao hiki kina kibali kisheria, hatukufanya tu kama kikao cha mitaani, unasikia,….’akasema mwenyekiti.

 Hapo mume wa familia, akageuka na kukaa kwenye sehemu yake na wakili wake akawa anamnong’oneza kitu, wakawa wanaongea sasa kwa taratibu, nikaona kama wanakubaliana jambo. Na kabla muongeaji, shahidi hajaendelea wakili akanyosha mkono, kutaka kuongea, na hata kabla mwenyekiti hajamruhusu wakili huyo akawahi kusema;

‘Samahani mwenyekiti…kuna ombi kidogo kwa mume wa familia, naomba tumsikilize…’akasema wakili na kabla wakili hajamaliza kuongea, nahis walishafahamu kuwa hawataruhusiwa kuongea, akasema;.

‘Kwa vile umesema mdogo wangu kakamatwa na polisi, na mimi ndiye kaka yake, ninaomba mimi na wakili wangu tuende tukafuatilie utaratibu wa dhamana yake…’akasema hivyo akauliza

‘Nani kasema kakamatwa na polisi, mimi nimeuliza unafahamu wapo mdogo wako alipo, yawezekana kakamatwa..sawa. mimi sina uhakika na hilo, hayo ni maswala ya polisi. Walichoniambia nikuwa tusiwe na wasiwasi na huyo mtu, …kwahiyo huenda anaisaidia polisi..na watatoa taarifa kama kakamatwa au la..’akasema mwenyekiti

‘Kwani Polisi wamesemaje hasa..?’ akauliza wakili.

‘Polis walisema wanamfuatilia, pale nilipotoa taarifa kuwa huyo kijana ametoroka, maana ilikuwa niw ajibu wetu kutoa taarifa…wakasema watalifuatilia hilo.

‘Na baadae nilipooongea nao tena, ndio wakasema wameshayaweka mambo sawa tuendee na kikao,na wakatahadharisha kuwa kikao chetu kisingilie maswala ya mauaji, ina maana kuna jambo kijana kaongea huko…’akasema mwenyekiti.

‘Kwa kauli hiyo mpaka hapo ina maana mdogo wake mteja wangu yupo mikononi mwa polisi …au sio?’akasema wakili

‘Yawezekana, ndio..sina uhakika huo, huenda yupo mikononi mwa polis lakini akiisaidia polisi, kama atakuwa kakamatwa kwasababu kadhaa, ni lazima watatufahamsisha, sisi ndio ndugu zake…’akasema mwenyekiti

Hapo mume wa familia akasimama, na wakili wake akamzuia wakawa wanaongea na wakili akasema;

‘Mteja wangu anasema kama yeye haruhusiwi kutoka, bas I ngoja mimi kama wakili wake nilifuatilie hilo, kwa niaba yake..’akasema wakili.

‘Hivi tunaelewana jamani,..huyo ni ndugu yetu, sote tunawajibika naye, kama ni swala la kufuatilia, sote tutaungana na kuona vipi tutamtetea, ..eeh, lakini hadi hivi sasa tupo chini ya amri ya polisi, kuwa asije akatoka mtu na kikao kikimaliza wao watakuja hapa, …’akasema mwenyekiti

‘Lakini mimi siwezi kuzuiwa maana, mimi ni wakili tu, kama mteja wangu kaniruhus mimi nitoke nifuatilie hilo, ni wajibu wangu kutii, mimi nipo kwa mamlaka yake sio kwa mamlaka ya hiki kikao..’akasema wakili

‘Haijalishi wewe ni nani mimi nafuata amri za watu wa usalama, …, kwani wewe wakili hauwezi kufanya makosa, muhimu tusubirie, tukimaliza kikao, wenyewe watafika hapa na kitakachoendelea baadae tutaambiwa, sawa, …shahid endelea…’akasema mwenyekiti.

********

Shahidi akaendelea…

‘ Baada ya Makabrasha kumweka sawa mume wa familia, bado kulikuwa na mambo hayajawekwa sawa kwa utaratibu wake, kwa upande wa wadhamini wake, hao waliomtuma alishafanya kazi yake, lakini sasa alikuwa akikamilisha mambo yanayohusiana na masilahi yake.

Aliniambia kwua katika mipango yake alihitajia kundi la watu, ambao ataweza kufanya kazi nao, kuachilia mbali sisi ambao tunakutana mara kwa mara, akasema bado anahitajia kiongozi ambaye atakuwa akiongoza hilo kundi.

‘Wewe si ndio kiongozi..?’ nikamuuliza

‘Hapana, mimi sitakiwi niwe kiongozi wa moja kwa moja, maana mimi ni mtu wa sheria, kazi yangu kubwa itakwua kuhakikisha sheria zipo sawa, hata hivyo …inavyoonekana mimi ndiye nitakuwa mkurugenzi mkuu kutokana na hisa zangu…lakini nahitajia mtedaji mkuu, kiongozi wa kusimamia mambo yote.

‘Ni nani huyo..?’ nikamuuliza

‘Ndio namtafuta,..ungelifaa kuwa wewe, lakini bado ..wewe bado unahitajia muda, yupo ambaye anafaa sana, lakini sijaweza kumshawishi…’akasema

‘Ni nani huyo..?’ akauliza mume wa familia

‘Haina haja kumfahamu kwasasa…ila zaidi ya hayo, tunahitajika kumuandaa huyo mtu kuja kuwa kiongozi wa baadae, wewe mume wa familia utakuwa na mamlaka yako, lakini hutaweza kuongoza hili kundi, hili kundi ni jingine, linahitajia mtu mwenye uelewa wa mambo mengi na jasiri ..’akasema

‘Kwanini mimi sifai, usielete watu wako hapa kwanza kampuni ni yangu, nay a mke wangu, bado unaona sisi hatufai, kwanini....?’ akauliza mume wa familia

‘Mimi ninakufahamu sana, kiongozi tunayemuhitajia anatakiwa mtu tofauti na mkeo kwasababu atakuwa mpinzani wa familia ya mkeo, …sihitajiki kujieleza sana kwa hilo, muhimu muelewe hivyo tu…’akasema

‘Hapana mimi sitakubaliana na hilo…’akasema mume wa familia.

‘Kumbuka mimi ndiye mkurugenzi mkuu, ninayemiliki zaidi ya nusu ya hisa, nina kura turufu…na uniamini, mimi nina maana yangu kubwa sana kulifanya hilo, mwenyewe utakuja kuona,…  tuombe mungu tu nizidi kuwepo..’akasem

‘Una maana gani kusema hivyo, kumbe mwenyewe unajua kuwa hutafanikiwa au sio..?’ akauliza

‘Kazi kama hizi ..ni za hatari, ..vyovyote iwavyo, lolote laweza kutokea, hilo siwezi kulipinga, ila kwangu mimi ..kisheria nimeshaanza kuweka kila kitu sawa,  hata hivyo maisha hayana ujanja, leo nipo kesho sipo,..ila nawahakikishia , kama nitaendelea kuwepo, mali zote hizo zitakuwa kwenye miliki yetu,  mikakati yote imekwenda sawa ni nyie tu kushirikiana na mimi ili muwe na uhakika wa maisha mazuri, …’akasema.

‘Sisi tutakuwaje na maisha mazuri wakati hisa karibu zote unachukua wewe..?’ akauliza mume wa familia

‘Je ni kipi bora kukosa kabisa au hata kupata kidogo, eeh, maana kwa hali ilivyo ungelikosa kila kitu, hunishukuru mimi, …acha ubinafsi hapa,..’akasema kwa ukali.

‘Kama ni ubinafsi unao wewe sio mimi…’akasema mume wa familia.

‘Sikiliza…hivi unajua kashafa uliyotengeneza, ..kashifa hiyo ingekugharimu wewe kutimuliwa kwenye hiyo familia kwa fedheha, …pili ukumbuke kuwa kutokana na kashfa hiyo familia hiyo ipo kwenye wakati mgumu…’akasema

‘Kwa vipi…?’ akauliza mume wa familia.

‘Unaona, ndio maana nikasema uongozi unahitajia mtu anayeona mbali, anayefahamu mambo mengi kwa wakati mfupi, siwezi mimi kukufafanulia kila kitu, unasikia,..au nikuulize  wewe ulitakaje, …?’ akauliza

‘Sisi mimi nilitakaje, wewe umetumia ujanja wa kuhakikisha unanifirisi mimi, na familia yangu, unafikiri mke wangu atakubali kirahis hivyo, eeh, na..hapana hilo la kutafuta watu wengine kuja kuongoza hata mali za mke wangu sitakubaliana nalo..’akasema mume wa familia.

‘Tatizo bado hujanielewa,…unasikia,…kundi hilo, kwa namna moja halitamuhusisha mkeo moja kwa moja, maana mkeo ni  familia ya kundi pinzani, mkeo ataingia pale tu tutakapogusa mali..mbazo na yeye anazimiliki..vinginevyo yeye atakuja kuwa kama picha ..familia hiyo itafirisika, na wewe utakuwa juu…’akasema

‘Hizo ndoto….hahaha..’akasema mume wa familia.

‘Ndoto, ni kwa vile wewe huwezi kufuatilia, mambo ya hisa, kushuka na kupanda kwa tahamni za hisa za wawekezaji wakubwa, mkweo sasa hivi anayumba, kisiasa na kiuchumi, ..hilo kwako tuliache, kidogo kidogo utakuja kunielewa..’akasema

‘Mimi nakubali tu kwa vile sina jinsi, kwa vile unanitishia amani, vingnevyo nisingelikubali kabisa…’akasema mume wa familia.

‘Hizi jamani wewe mtu unataka nikupe nini,..ulitaka mimi nikusamehe madeno yote, ina maana mim iwe kazi yangu kukufanyia kazi zako,..nipate hasara, hebu niambie hayo madeni yangu yote ungeliwezaje kuyalipa, hebu jaribu kuwa na akili pana…’akasema wakili.

‘Nitakuja kuyalipa na hisa zangu zote utazirejesha, ..hilo na kuahidi ..’akasema mume wa familia

‘Hahaha, kwa hali uliyo nayo, sizani,labda mimi niwe sipo duniani, ..unafikiri hayo madeni ni kitu kidogo, ..eeh, hutaweza hilo sahau na ujipange nnavyotaka mimi, nataka nyie muwe matajiri, kwanini hutaki kunielewa…’akasema wakili huyo.

*********

Mikakati ikawa mingi, na mingine mimi sikuhusishwa kabisa niliweza kuigundua hiyo mikakati, wakati nikiwa kwenye kazi zangu, na nikiwauliza wanasema nisiwe na wasiwasi mane mengine sio lazima mimi nifahamu, ila kila kitu kimeshafanyiwa kazi, iliyobakia ni mambo machache ya kukamilisha, na hayo hayanihusu sana.

Kwahiyo mimi nikawa nasubiria, na wakati nasubiria ndio ikaja taarifa hiyo ya ajali…

‘Ile ajali ya mume wa familia, ilitokea katika harakati zile za kuchukua mkataba ule wa zamani ili ikabadiliswe na huo mpya wa kugushiwa, na hayo yote yaliwekewa muda maalumu kwa mume wa familia kuhakikisha nakala zote za zamani zmechukulia na kuharibiwa, na kuhakikisha kuwa hakuna nakala yoyote itakayobakia.

Tatizo sasa mume wa familia akawa na ziada ya kazi ya kuongea na mama mzazi, ili mtoto huyo aje kuwa sehemu ya warthi wake, aweze kutambulikana, na hilo lilitegemea sana mama yake, kwahiyo pamoja na mihangaiko ya kubadili hiyo mikataba bado alitakiwa kumshawishi mama wa mtoto huyo akubaliane naye. Mambo yote hayo yakapangiwa muda,…sijui ni kwanini, nahisi ni moja ya mbinu za marehemu kuhakikisha jamaa hapati muda wa kutafakari tena.

 Muda, ukawa ni sehemu kubwa ya kufanikisha malengo hayo, muda pia ukatumiwa kama namna na kumfanya mume wa familia awe na wakati mgumu ili asipate nafasi ya kutafakari zaidi, muda ukawa namna ya kuwaogofya wale wote wanahusika, kuwa wakichelewa kashfa zao zinatumwa kwa walengwa..mume wa familia,..hakujua hayo yote yote wenzake wameyaweka kwasababu maalumu.

 Siku hiyo mambo yalianza hivi----

Akiwa ofisi akapigiwa simu na Marehemu kuwa zile nakala zote za mikataba yao, zinahitajika kwa haraka, …na pia akaulizwa vipi mama wa kichanga keshamuweka sawa, maana yote ni muhimu sana, kwani asipomuweka sawa mama wa kichanga, huyo mtoto anaweza asiwe na nafasi kwenye mipangilio ya watoto wanaotakiwa kumiliki mali halali.

‘Kwanini, kwani hata asipokubaliana kwa sasa baadae si inawezekana, kuna tatizo gani hapo..?’ akauliza

‘Tunahitajia sahihi ya mama,..tunahitajia kukubali kwake, hatuwezi kupitisha jambo kama mama wa mtoto hajakubali, hiyo ni kazi yako kama kweli unampenda huyo mtoto na kama kweli unamuhitajia kama  mrithi wako wa baadae basi fanya juhudi ..’akaambiwa

‘Sawa…’akasema mume wa familia, hapo kichwa kinamgonga kweli, akachepuka na kumeza zile dawa, alizopewa, ..muda mchache baadae akajihis mwingine, akili ikawa na changamoto za dawa. Anarudi kwenye kikao hajaa vyema zimu ikalia, akaambiwa;

‘Lakini pia zile nakala za mkataba wenu , wewe na mkeo, zinahitajika kwa haraka, zoezi hilo halitaweza kufanyika kama hizo nakala zote hazipo, msimamizi anayesimamia idara hiyo, kasema hataweza kukamilisha hilo mpaka nakala zote ziwepo, ili ziharibiwe mbele yake..’akaambiwa.

‘Sawa…’akasema na kupekua kwenye briefcase yake, ndio akakumbuka nakala mmoja haipo, ..akakumbuka alipoiacha, hapo kwa haraka akawaambia wajumbe;

‘Jamani endeleeni na nikao, nipo, …msikatize kikao, kuna kitu cha haraka nakichukua hapo nje…’akasema akitoka na briefcase yake, akaingia kwenye gari, mbio, barabarani.

Akiwa barabarani, Makabrasha akaendelea kumsumbua  na simu, ni kama anamuona anavyohangaika,…akamwambia;

‘Na ukumbuke hiyo ndio salama yako, maana mkataba wa zamani ukiwepo, na kashfa ulizokutwa nazo zikibainika basi hutapata kitu… umeelewa, hiyo ni kwa faida yako,…’akaambiwa

‘Ni kweli…’akasema,  na ni kweli, kutokana na hizo kashfa, mbele ya mkataba wao alitakiwa akose kila kitu, na zaidi ni ndoa yake kufa, na ndoa ikifa yeye ana faida gani tena,,,;akatulia kidogo mzungumzaji, halafu akasema

 Kama mtausoma vyema huo mkataba, utaona hadi sasa mume wa familia hana ndoa, sisemi hili kwa uzushi, au kutilia fitina,  mkataba wao unasema nini kuhusu madhambi kama hayo, na ushahidi upo wazi…au amkane huyo mtoto kama sio wake, je anaweza kufanya hilo, hawezi kumkana, sasa chukulia hali hiyo, na ndio umepata mwanya kama huo, ungelifanyaje, ndio maana mume wa familia akakurupuka, hana amani, akili sio yake,….

Kwahiyo ndio akapanga akitoka hapo kwenye kikao chake cha kikazi…kikao ambacho alikiacha kikiendelea,..ili iwe ni ‘kinga’ kwake kama ikitokea jambo kuwa yeye siku hiyo alikuwa na kikao ofisini, …kwa usafri wa gari, alijua atakwenda kwa haraka, na kurudi na kuendelea na kikao.

Ili kukamilisha mambo yote hayo akaona ampitie mzazi, mama wa mtoto ili amuhakikishie mikakati yote na amshawishi  kuwa mambo sasa yapo sawa, na kutokana na shinikizo la yule mtu asiyejulikana, mtu wao..yaani wakili, ambaye ni marehemu.., atalimaliza..

Alipofika huko akashangaa kumuona mke wa familia yupo na huyo mdada aliyejifungua, na hili hakulitegemea kabisa,  yeye alijua kuwa mke wake atakuwa kazini, sasa iweje awepo pale, na kwa muda huo huo akapokea ujumbe wa simu ikimuhimiza kuwa nakala za mikataba yote ya zamani, zinahitajika kwa haraka iwezekenavyo. Na muda ni leoleo, ikishindikana ndio basi tena..

 Hapo akili ikazidi kuchanganywa, alijua kabisa mkewe akitoka hapo atarudi nyumbani, na hataweza tena kuchukua ile nakala ya mkewe , ambayo aliisahau kwa bahati mbaya usiku, yenye shida ilikuwa ni nikala moja ya mkewe maana yake alishaichukua anayo…

‘Sitaweza kuongea na huyu mtu kwa leo, lakini ni lazima niwahi kuzipata hizo nakala za mkataba ..kwa manufaa yangu..’alikuwa akisema hivyo, alinihadithia jinsi siku hiyo ilivyokuwa na wakati mgumu kwake..

Ya mungu mengi, …wakati Makabrasha keshafanikisha namna ya kumweka sawa msajili wa hiyo mikataba, na wakati huo wanasubiria nakala hizo walizokuwa nazo wahusika wakuu,akaja taarifa jamaa kapatwa na jail, yupo kwenye hali mbaya..

Ukumbuke kabla ya hilo zoezi, Makabrasha alishafanya vitisho vingi ambavyo vilizidi kumchanganya mume wa familia,…na mume wa familia kuna muda akawa analalamika kuumwa na kichwa Makabrasha ndiye aliyemtafutia dawa, akasema hizo dawa zitamsaidia sana hayo maumivi ya kichwa, mimi nilikuja kuzipeleka hizo dawa kwa wataalamu baadae lakini zikaonekana ni dawa  zakuharibu akili…’akatulia kidogo.

‘Kiukweli Makabrasha anaifahamu kazi yake vyema, kwenye kucheka atacheka, kwenye kazi, vitisho, atakutisha kweli,...alijipanga vyema,kwahiyo kila muda kwake ilikuwa ina mbinu zake na kila jambo lilikuwa na plani A na B, ikishindikana moja nyingine itachukua nafasi yake, hakuwa mtu wa mchezo.

Hizo dawa alipewa kabla ya ajali na baadae akawa anaendelea nazo baada ya ajali mwenyewe anasema akisikia kichwa kinauma sana,  akinywa hizo dawa kichwa kinapona, lakini hakujua hiyo ahueni ilikuwa inazaa tatizo jingine. Na ndio hayo yakawa yanatokea baadae ni sababu ya hizo dawa, .hata mimi sikuwa na ufahamu wa hizo dawa, nimekuja kuligundua hilo baadae sana...

 Sasa alipogundua kuwa mkewe hayupo kazini, yupo kwa rafiki yake, na anatakiwa kuwahi kuchukua zile nakala azifikishe kwa walengwa, si ndio akatoka hapo kwa mwendo kasi, akili pale ilikuwa sio yake tena, keshapata vitisho, kamuona mkewe na muda hautoshi, na zile dawa huenda alizitumia asubuhi,zilikuwa bado kichwani akilini ikawa inaota mengine, haoni kabisa kama yupo kwenye mwendo kasi, tahamaki ndio hiyo ajali..ilikuwa ni ajali mbaya sana.

Ajali haina kinga….!

Ajali hiyo ingelichelewesha mambo mengi, lakini kwa Makabrasha ikaonekana ni bahati nyingine nzuri tu kuitumia, tunaweza kusema kwake ilikuwa ni bahati nzuri ya kufanikisha mambo mengine.., japokuwa ilikuwa ni ajali kwa rafiki yake..

Hutaamini  ajali hiyo ikaja kutumiwa kama kisingizio cha kufanikisha mambo mengine mengi tu, kama mlivyosikia kwenye maelezo yaliyotolewa awali. Mtu anaumwa yupo hospitalini, mara yupo uwanja wa ndege, mtu anaumwa, yupo hospitalini mara yupo nyumbani….inaeleweka kweli….! Lakini kiukweli ajali ile ilikuwa mbaya, na kuna madhara makubwa aliyapata kwenye uti wa mgongo, hili halina shaka.

Sasa baada ya ajali ni nani anaweza kutumiwa ili kufanikisha hayo yaliyopangwa, nakala za mikataba ile ni muhimu sana, akatafutwa mtu wa haraka, ambaye yupo karibu na mume wa familia ambaye anaweza kuficha siri, hata kama…na akipewa maagizo atayafanya kwa haraka..

Uwe na kujali fulani,…, ndio hapo wakamchukua  mdogo wa mume wa familia, yeye kwa asilimia kubwa hakufahamu chochote kinachoendelea zaidi ya kutumwa , na hakutakiwa afahamu kitu gani kinachoendelea, kazi yale ilikuwa kumtii kaka yake,na kaka yake ahakikishe hilo. Sizani kama alikuwa anafahamu undani wa hayo yote, kwani nimjuavyo, kama angelifahamu undani wake, mengine asingelikubali.

‘Sasa hapo utajiuliza iweje wakati mtu hajiwezi yupo hospitalini, maana hadi anafikishwa hosp alikuwa hajiwezi, sasa huyu marehemu alijua ampe dawa gani ili aongee kila kitu cha kusaidia, na maongezi yake yasaidie…dawa hizo zilitumika pia.

‘Na ajali iliyopotea mtu wa kwanza kufika kwenye hilo gari alikuwa ni marehemu alifuata nini, na alijuaje kuwa ajali hiyo itatokea,… marehemu alikuwa sio mtu wa mchezo..sijui siku ile walipokutana wakati mgonjwa yupo taabani, waliongea nini...hilo tutamuuliza mume wa familia.

  Nisije kulisahau hili….Kuna mtu mwingine ambaye alikuwa kinara wa hayo yote, akiwa kama msaidizi wa Makabrasha, ambaye hadi sasa watu hawajamgundua…huyu mtu ni hatari kuliko watu wanavyomfikiria…’hapo akatulia kidogo.

Huyu mtu ni hatari hata kuliko Makabrasha mwenyewe maana tatizo lake kunwa ni kuwa ana papara, hajatulia kama alivyokuwa akitulia baba yake kabla hajaingia kwenye mapambano, mtu huyu ni nyoka yenye sumu, ni mbaya sana, si mwingine ni mtoto wake mwenyewe marehemu.

Huyu aliweza kupenya kwenye sehemu mbali mbali na kupata taarifa nyeti. Huyu anajua siri nyingi tu za baba yake,..na ndiye alitarajiwa kuwa mrithi wake mkuu, kwa mtizamo wa wengi lakini ikaja kutokea tofauti, ..hapa hatuna uhakika ni kitu gani hasa kilifanyika…maana imeshangaza kuona aliyepewa  majukumu hayo ya kifamilia ni mtoto mwingine.

Ni kweli mtoto huyu kisheria ndiye aliyetakiwa kuchukua hayo majukumu, lakini mtoto huyu hakuwa karibu na baba yake, hawakuwa wanaelewana kutokana na tabia za baba yake, mtoto huyu alikuwa akitaka mambo ya halali, sio kama alivyokuwa akitaka baba yake, kwahiyo walikuwa hawapatani kabisa, sasa iweje yeye apewe majukumu ya kifamilia, majukumu ambayo ndani yake kuna magumashi mengi.

 Sasa maswali mengi nahisi hapa polisi watakuwa wakijiuliza sana, huyu aliyetarajiw akwua kinaraka kwanini hata kwenye mirathi awe ni mtu wa tatu…ujue huyu mtu kiukweli hata ndani ya familia alikuwa hajulikani sana zaidi ya kujuliana na baba yake…. Na ukumbuke huyo ni mtoto wa nje tu wa Makabrasha, hakuzaliwa kwa mke anayejulikana, alizaliwa na mwanamke wa nje tu..Hapa kuna jambo,…sijaweza kuliweka sawa, mtanisaidia..

***********

Mipango ilipokamilika na mikataba halali iliyokuwemo kabla ikaharibiwa, na kuwekwa mikataba iliyogushiwa, na kilichobakia ulikuwa mkataba mpya ambao ulionyesha dhamira ya Makabrasha, na huo ulileta sintofahamu, lakini kwa vile Makabrasha alishajiandaa kwa hilo, akatoa vitisho vyake, na mume wa familia akasalimu amri. Na kila kitu kikawa kimekamilika

Kilichokuja kuharibu sasa ni huo utaratibu wa nakala kuhifadhiwa kwenye mtandao, sijui kwanini Makabrasha hakulifikiria hilo mapema, sijui kwanini hata huyo mtu wa masijala hakuwahi kumuambia Makabrasha kuhusu hilo, kama angelifikira hilo mapema, isingelikuwa kazi nguku kwa huyu mtu.

Kwa Makabrasha mambo ya mitandao anaifahamu sana , na ana watu wake wanaoweza kufanya zaidi ya hapo,..na hadi hapo kila mtu anayehitajika alishakuwa mikononi mwake. Nakumbuka siku zoezi hilo lilipokamilika, alifanya shereeh fupi y akujipongeza na kujinadi kuwa sasa yeye ni kaam yule mtaalamu wa kile kisa cha dunia yangu

Hadi hapo alikuwa ameshawaweka matajiri wengi mkononi, alikuwa na hisa karibu kwenye makampuni mwengi makubwa, alikuwa akila sahani moja na wanasiasa wakubwa, aliyekuwa amebakia ndio huyu mkwe wa mume wa familia. Sasa aktika kuongea ndio nikagundua jambo

‘Sasa hata mkuu wangu hataniweza…’akasema

‘Mkuu wako!!! , kumbe kuna mtu yupo juu yako..?’ nikamuuliza

‘Hahaha, hivi ningelipatia wapi pesa nyingi ya kufanikisha haya yote..yupo mkuu, na sio yupo, wapo, wakuu, wafadhili wangu…ila muhimu ndio huyo mpinzani wa ..baba mkwe,…, lakini yeye hawezi kuniingilia kwenye mali zangu, ana yake na mimi ninayangu, ila mimi nitamwezesha kufika juu, akifanikiwa yeye, na mimi nimefanikiwa…’akasema na kucheka kicheko cha kishetani..

Tamaa ya Makabrasha sasa ilionekana wazi, kwani baada ya hapo, akatayarisha mkataba wa makubaliano kati yake na wamiliki wa makapuni na yakimuweka yeye kuwa kama mumiliki wa hisa nyingi kwenye kampuni ya mume wa familia,kama alivyozoanisha kwenye huo mkataba.

Yeye hakuishia hapo,akatayarishwa mkataba mwingine ambao mali yangu ikiwemo hospitali ya mume wangu yeye pia awe na hisa na nayo yalishafikia hatua ya mwisho, na kama kikao kile cha kusaini huo mkataba kingelipita basi ungelisikia makali yake, lakini hakikufanikiwa kwani ndio siku Makabrasha aliuwawa...’akasema na kutulia, mwenyekiti alipoona mungumzaji katulia akamuuliza.

‘Kwahiyo kutokana na maelezo yako wewe, inavyoonekana kabisa ni wewe mlishirikiana na mpenzi wako, yaani mume wa familia kumzimisha huyo mtu au sio..hatuingilii mambo ya polisi, ila hadi hapo inavyoonekana ni hivyo, mengine ni kazi ya polisi, au sio, ? akauliza mwenyekiti akiangalia saa yake.

‘Ndugu mwenyekiti umenionya nisiingilie huko, lakini nikifanya hivyo, ina maana kuwa ukweli halisi wa kifo hicho hautweza kujulikana …’akasema mzungumzaji.

‘Kwahiyo unataka uendelee, natamani ufanye hivyo, ila uwe makini..maana wahusika wenyewe wapo huko nje wanasikiliza..’akasema na wajumbe wakatizama nje, hawakuona mtu, na mzungumzaji yeye akaendelea kuongea…

‘Kifo cha Makabrasha ni tukio ambalo halikutarajiwa…japokuwa huyu mtu alikuwa na maadui wengi sana, lakini kutokana na jinsi alivyokuwa amejiweka ulinzi wa kila namna kutoka ofisini kwake hadi nyumbani, alikuwa na albi,..uhakikisho wa kujilinda kuwa hana kosa,

Kwa namna hiyo maadui zake, au yoyote aliyeathirika na mambo yake alikuwa na kisasi naye, …tatizo ikawa ni nani wa kumvika paka kengele,..na watu hujiuliza ni kwanini hakikutokea mapema, kwanini kifo chake kije kutokea muda huo. Muda ambao kampeni zinaanza..muda ambao watu wake wangemuhitajia sana, kwa mantiki hii polisi wanawaondoa watu wake kama washukiwa au sio…!!

‘Kumbuka kauli yake, ..sasa hivi hawataniweza tena, hata hao mabosi wangu, ..kauli hii imeficha siri kubwa sana, kuwa kwa kusema hata mabosi zangu ina maana kulikuwa na msigishano mwingien kati yake na mabosi zake walishafikia sehemu wanamuogopa, lakini kwa polis hilo halina nguvu, kwanini, jiulizeni sana hapo…’akatulia.

‘Lakini angalia haya aliyoyafanya, ina maana kama siku ile ule mkataba ungeliwekwa sahihi na mume wa familia, basi…mume wa familia angelikuwa hana chake, docta, na wengineo wengi, ambao walitegwa na huyu jamaa, na kwa mtaji huo wangalipoteza hisa za makampuni yao, na wengine huenda ingekuwa ndio mwisho wa utajiri wao, je hawa wanaweza kuwa washukiwa wakubwa, kwa mtizamo wa polisi ndio…ndio maana hapa tunashukiwa, hapa ndio kutapatokana muaaji kwa mtizamo wa polisi...

Mkataba ule ulikuwa na mambo mengi sana..iliyokuwa imebakia ni sahihi moja ya mume wa familia, wengine kwa namna moja walisharubuniwa, kuacha mume wangu ambaye bado alikuwa anasua sua, lakini hata yeye alishawekwa sawa, anajua kwa vipi..

Hadi hapo swali la kujiuliza huo mkataba mkubwa ambao, uliwajumuisha watu wengi, upo wapi…’akawa kama anauliza

Japokuwa kila mmoja alikuwa na mkataba wake wa kukubaliana ambao ulikuwa ni siri kati yake na hao watu, ama kuuziana hisa au wanajua wenyewe, lakini kulikuwa mkataba mkuu,…

Siku ile mume wa familia naye alitakiwa kufika, kukubali kuwa madeni yake yatalipwa kwa kuuza hisa zaidi ya asilimia hamsini kwa Makabrasha, na ilitakiwa siki hiyo kila kitu kikamilike, kwani akitoka hapo anakwenda kusajili hiyo mikataba yake kwa wahusika.

‘Ina maana kulikuwa na mkataba mwingine ambao ni mkubwa zaidi..?’ akauliza mwenyekiti.

‘Ndio…huo ndio ulikuwa funga kazi, docta na wengineo walishaweka sahihi zao, au sio docta,…? ‘ akamuuliza docta

Docta akaduwaa, halafu akatikisa kichwa kukubali, lakini sio ile ya kukubali kabisa kabisa.

Siku ile aliyekuwa amebakia ni mume wa familia, yeye si mgonjwa, yupo hospitalini,lakini hiyo hali indewe kwa makini, au sio…lakini pia ni lazima na yeye aweke sahihi yake, ili nakala zote za mikataba zifikishwe kwa wahusika, mume wa familia anauza kampuni yake kwa mtu mwingine kwa hasara…au sio mume wa familia..’ akauliza muongeaji .

Kwa hali kama hiyo lolote lingeliweza kutokea, kwa hali kaam hiyo watu wengi walikuwa na hasira na mtu huyo,….na walishajua kuwa siku hiyo ndio siku ya hitimisho, wakichelewa …hawatakuwa na cha kwao…mauaji yakafanyika, na mikataba ikatoweka, iliyobakia ilikuwa na mume wa familia, jiulizeni kwanini ikawa hivyo..!

 Ina maana huyo aliyefanya hiyo kazi, ya kummaliza Makabrsha aliutaka huo mkataba mkuu..mkataba uliobeba mambo mengi, ambao ungempa mamlaka Makabrsha, na mikataba mingine ya watu mbali mbali pia haikuonekana tena..ukabakia wa mume wa familia..polisi waliwafuatilia wale wote waliowahi kuandikishana na marehemu, lakini wote hawana habari…hawajui, ..ni kwanini.

Swali kwanini polis waendelee kuwaona watu kadhaa ndio wauaji, wakati hali kama hiyo wauaji wanaweza wakawa mapapa makubwa tu…mumeona hapo ilivyo..ni kwanini, hivi mnanielewa lakini, kwanini …washukiwa wawe akina sisi, ambao, hatuna kitu …ni kwanini..

‘Ndugu mwenyekiti nahis hapo wewe una jibu zaidi ya sisi, ambao, tunajikuta kama nyasi zinazoumia baada ya mafahali kupigana, lakini ni lazima iwe hivyo…au sio mwenyekiti..’akasema shahidi na mwenyekiti akatabasamu na tabasamu lake likakatishwa na simu

 Simu ya mwenyekiti ikalia…na mwenyekiti akapokea akawa anasikiliza kwa muda tu, na alipomaliza akasema

‘Mpaka hapo, tunaweza kusema kuwa ..wewe na mume wa familia mtakuwa mnafahamu ni nani muuaji, kama sio nyie wawili, kweli si kweli,…?’ akauliza mwenyekiti

‘Hahaha, mzee usiwe na pupa, subiria usikilize zaidi utaharibu kila kitu, kama utawasikiliza hao watu … je mzee haupo tayari kusikiliza sehemu ambayo itakusaidia hata wewe kwenye kupambana na huyo adui yako,…’akasema kama anauliza

‘Ninahamu sana ya kusikia hilo, lakini polisi hawataki …’akasema

‘Unajua kwanini hawataki, ..?’ akauliza muongeaji.

‘Mimi sijui, lakini ni muhimu kufuata sheria, au sio..?’ akauliza wajumbe

‘Lakini mwenyekiti, ngoja muongeaji aendelee ili tuone ukweli ulipo, kwasababu huenda haki isitendeke hapo, nahisi kama siasa inataka kuingilia haki…kwanini na sisi kama wanafamilia, tusifahamu ukweli,…’akasema mke wake

‘Sawa ngoja tuvunje sheria kidogo, ili tusikie zaidi, ..sawa shahidi unaweza kuendelea japokua tunakiuka sheria..’akasema mwenyekiti.

‘Sawa ndugu mwenyekiti, ila…kabla sijaingia sehemu hiyo ya pili, nawaombeni kitu kimoja...’akasita kidogo, na kuchukau leso kufuta jasho.

Mwenyekiti hapo akashikwa na butwaa huku akiangalia saa yake na simu ikawa analia kuashiria ujumbe wa sauti, yeye akazarau kuusoma huo ujumbe akasema;

‘Kitu gani unachotuomba, ..?’ akauliza mwenyekiti akiwa kashikilia simu tu, huku anamuangalia huyo shahidi kwa macho ya shauku, na mashaka fulani

‘Ni hivi ndugu mwenyekiti...’akaanza hivyo shahidi , huku simu ya mwenyekiti ikianza kuita…

NB: Je itakuwaje, ndio hitimisho au?


WAZO LA LEO:Kila mtu ana ndoto zake, na ndoto nyingine ni za kufikirika tu, hatuwezi kupanga kununua gari , kujenga nyumba, au kufanya jambo kubwa wakati uwezo huo hatuna. Tunaweza kuweka malengo hayo, kwa mipangilio ya kimaisha, lakini  hatuwezi kulazimisha yale yaliyo juu ya uweze wetu, tupange kutokana na uwezo na kipato chetu. Zaidi ya hapo tutaingiwa na tamaa mbaya, ambayo mwisho wake ni kutenda dhuluma.
Ni mimi: emu-three

No comments :