Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Monday, March 26, 2018

MKUKI KWA NGURUWE-101


‘Ndugu wajumbe hiki ni kikao cha hitimisho cha kikao kilichopita, kama mnakumbuka vyema, kikao kilichopita tulikikatisha kutokana na muda, na pia wajumbe walishachoka, na pia tukaomba wale wajumbe waliotarajia kusafiri waahirishe safari zao, lakini kutokana na mambo yaliyokuwa juu ya uwezo wetu, mengi hayakufanyika kwa wakati, kama mlivyoona wenyewe,...sintofahamu iliyotokea na baadhi ya wajumbe wa kikao hiki wakakamatwa.....’Mwenyekiti akaanza kuongea.

‘Poleni sana kwa mkasa huo, kama wanafamilia sote lilitugusa, ndio maana tulikuwa bega kwa bega kuwaombea dhamana wale waliokamatwa, lakini tulikataliwa kutokana na pingamizi za wanausalama hao...’akaendelea mwenyekiti.

‘Wakati mwingine tunaweza kuwalaumu polisi kwa jitihada zao, tukaona kuwa wanatusumbua, wanatumia mabavu nk, lakini wakati mwingine inakuwa haina jinsi, kwani  raia ambao walitakiwa kutoa ushirikiano, wanakuwa wagumu, wanaficha ukweli kwasababu zao binafsi, na hapo ndipo polisi wanapoamua kutumia nguvu...na wakati mwingine wanafanikiwa, au sio..'akasema mwenyekiti, na wajumbe wakikuwa kimia.

‘Siwezi kuwalaumu sana wale mliofanya hivyo, lakini kuna mambo ambayo nataka kuyaweka wazi kama wanafamilia, huenda wengine hawatanielewa, lakini ni vyema nikaeleza sera na taratibu za familia hii, mimi bado ni mwenyekiti wake, na kama bado mnanitambua hivyo, ni lazima nisimamie yale mamlaka ya kifamilia yetu hii kuu...’akatulia.

‘Katika familia hii, tumejitahidi sana kuwa mbali na kashifa,...na hili nimekuwa nikilirudia mara kwa mara katika kila kikao, na kile anayekuja kuoa kwetu, au tukimleta muolewaji hapa, ninajaribu kuwaasa kuhusu hili, lakini hali inazidi kubadilika, ...sijui kwanini, labda ndio karne hii ilivyo.

Kiukweli hili lililotokea limetutia doa kubwa, na sijui tutafanyaje ili tutaweza kujiisafisha, japokuwa tumesalimika kihivyo...mimi sitaacha kulisema hili...sikufurahia na kitendo hiki kabisa,, nawaonya tena, hili lisijirudie. Hatutaki kashfa kwenye hii familia, mnasikia…

'Ndioooh..'wajumbe wakasema

‘Hebu niwauliza ni nani anayependa kukaa jela, hivi jela ni kuzuri,....hivi ni nani anapenda kukaa na wasiwasi, akakosa raha na amani akawa anaishi kwa mashaka-mashaka, hakuna anayependa kuwa hivyo, sasa kama hatupendi  kuwa hivyo, kwanini tujiingize kwenye yale mambo ambayo tunayaona yanaleta kashfa, yanatuweka katika hali ya kukosa amani na usingizi, kwanini....?’ akawa kama anauliza.

‘Ndio maana katika familia hii tunalipinga sana hilo..., na wale wanao-olewa au kuoa ndani ya familia hii, nimewaonya na nitendelea kuwaonya tena na tena, hatutaki kashifa, na kama una dalili na mienendoo hiyo mibovu,...tutakusakama, mpaka ubadilike, au uondoke wewe mwenyewe maana hutufai.

‘Sasa basi, tunaanza kikao chetu, na ajenda moja kubwa, ni hitimisho ya ajenda muhimu ya matatizo ya familia husika…tunaweza kuiita ni ajenda ya hukumu. 

Lakini kabla ya hukumu, ningelipenda tuliweke wazi tukio zima lilivyokuwa, najua kila mmoja ana dukuduku la kufahamu ni nini kilitokea, ni nani hasa muuaji wa Makabrasha, huyu mmuaji kapatikana au bado.

Tunashukuru mungu kuwa wajumbe mpoo,..nani hayupo, maana kama kuna mtu hayupo ujue bado yupo na wenyewe polisi...

Sasa bila kupoteza muda,...nimeona hili ni muhimu, na niliongea na watu wa usalama, wakasema haina shida, tunaweza kuliongea tu,...kuwa mwenzetu mmoja hapa ambaye alishirikiana na polisi hadi kufanikisha juhudi za watu wa usalama, na tunavyoongea hapa, muuaji anaweza kuwa mbaroni, ...

Aliposema hivyo watu wakapiga makofi.

Sitaki mimi niongee hili mwenzenu ndiye ataongea hili, nasikia mahakama mahakama ilimpa onyo kwa kuingilia kazi za polis bila kibali, lakini kwa namna nyingine imemshukuru sana, na wamependekeza kama inafaa apate ajira huko huko, ni yeye mwenyewe tu.

Kwahiyo basi….tunakuomba, mke wa docta, uchukue nafasi hii utuliezee japokuwa kidogo, jinsi ilivyotokea hadi mkafanikiwa kumpata Muuaji, sasa hivi hakuna kikikwazo, kuelezea hilo au sio, au badoi haturuhusiwi maana mimi sijapewa taarifa na nilipoomba kibali cha kikao, niliambiwa niendelee tu hakuna shida...’akasema mwenyekiti,

Mke wa docta, akakohoa kidogo na kusema;

‘Mhh, naona hiyo mke wa docta, unaipenda sana mzee, hahaha, sawa sio shida, itaendelea kuwepo tu kama sifa..., japokuwa imeshafika mwisho…hata hivyo, sio mbaya, ila yupo atakayekuwa hivyo, mungu akipenda sio mimi tena....’akasema huyo msemaji, na mwenyekiti akadakia na kusema;

‘Samahani, unafahamu hilo halijawa wazi kwenye hiki kikao ndio maana tunaendelea kukuita hivyo mke wa docta, mimi kama mwenyekiti sijapata taarifa kamili, na hata kikao hiki ambacho ni wanafamilia, na wao wanahitajia kulisikia hilo....’akasema mwenyekiti

‘Kwakweli mazoea yana taabu, hata mimi mwenyewe huwa ninajisahau na kujiita mke wa docta, lakini ukweli ndio huo, na kuanzia leo ningelifurahia mkisema, aliyekuwa mke wa docta,...’akasema huku akiinamisha kichwa chini.

‘Hili msishangae, nimeamua hivyo kwa hiari yangu mwenyewe, baada ya kuona kuwa sitakuwa nimemtendea haki mwenzangu , kwa yale yaliyotokea mimi nimeona niwajibike, na kuwajibika kwa muungwana ni kuachia ngazi zu sio…na pia kutokana na kazi zangu mwenywe nimeona kuwa nahitaji kukaa mwenyewe ...maana huwezi kulazimisha jambo kama moyo hautaki.

‘Ni ukweli usiopingika kuwa tumeshamaliza taratibu zote za talaka, kisheria, na hivi mnavyoniona nipo mbioni kuelekea kijijini, huko nimeshajipanga, nina miradi yangu na maisha yangu, na nitakaa kwa muda hadi hapo nitakapoamua ni nini kingine cha kufanya, maana ukiingia kwenye hii fani, muda wote unahitajika, ..ila kiukweli kutokana na haya yaliyotokea nisingelipenda kufanya kazi za kutumwa-tumwa tena, inafikia sehemu unajizalilisha,...ndio kazi…, lakini jamii haiwezi kukuelewa, sasa hivi nataka kujituma, na kujiajiri....’akasema .

‘Kwanza kabisa nawaombeni sana radhi wajumbe wa kikao hiki na wanafamilia hii, kwa hayo yaliyotokea, mimi kama binadamu nimkosaji, na mkosaji anastahili kusamehewa, ...ni kweli nimekosa sana, hasa kwa mume wangu, yeye nimeshamuomba sana masamaha, na japokuwa kanikubalia, lakini bado nahisi sijasamehewa, moyoni nahisi hivyo…., maana kosa nililolifanya kwake ni kubwa sana,...’akasema huku akimgeukia docta.

Docta akatikisa kichwa kukubali tu...hakusema neno.

Naona nianze kutoa maelezo, japokuwa yameshapita, lakini kwa faida ya wanafamilia, nitaelezea ilivyokuwa;

‘Kwa ujumla aliyemua Makabrasha ni mtalaamu wa hali ya juu, alifanya hilo jambo kwa kuangalia nyakati, ..., na aliyapanga hayo mauaji kwa utaalamu wa aina yake...ilikuwa vigumu sana kumnasa, kwanza alienda na muda na pili akawa anatumia madhaifu ya watu, na kuyachanganya na matukio, kiasi kwamba polisi walifikia kuhisi huyu au yule, bila kupata ushaidi kamili.

Hata mimi mwenyewe sikuwa na uhakika na kile nilichokuwa nikikiwaza kwani hata yule niliyemuwaza kuwa ndiye, mwisho wa siku nilijikuta nakosa ushahidi kamili, na hata nilipotoa wazo kwa polisi, wao walishia kuniona mimi ndiye muuaji.

Wao walishakusanya ushaidi wao wa kutosha kwa muuaji, kuwa ni mimi , nikishirikiana na mume wa familia, kwani mimi ndiye niliyekuwepo kwenye hilo jengo, na silaha niliagiza mimi, na silaha iliyotumika nilikuwa nayo mimi, na sababu za kumuua marehemu nilikuwa nazo mimi, na nilishawahi kutamka kuwa nitafanya hivyo......

Mwishowe nikapewa mimi jukumu la kumpata huyo muuaji, kama sio mimi, kilichonisaidia ni kuwa humo ndani ya watu wao kuna watu wananifahamu japokuwa ni kwa siri kubwa, na wananiamini,..pia  nafahamu sheria na jinsi ya kujitetea, na kwahiyo hawakuwa na jinsi bali ni kunitumia mimi.

Kwa pamoja tukafanya jambo lililoshindikana.

**********

Kwanza niliwaambia ili kumpata huyo muuaji, kwanza tumchambue huyo mtu, aliyefanya hayo mauji, anaweza kuwa na sifa gani,… kwani mimi nilikuwepo humo ndani, na mazingira ya humo ndani nilishayasoma karibu yote.

'Humo ndani hawezi kuingia mtu akafanya mauaji kama hayafahamu mazingira ya humo..'nikawaambia

'Maana kuna vifaa vya hali ya juu vya kuhisi silaha...kuna walinzi wa seehmu ya kuingilia na walinzi wa nje wasiojulikana wapi walipo, wanatumia mitandao tu, kwahiyo ni lazima mtu huyu alifahamu hilo, pili awe,analifahamu hilo jengo vyema kiramani.., maana mauaji hayo yalifanyika kwa muda mfupi, na kwa tahadhari ya hali ya juu, ...

Niliwaambia kuwa mtu huyo inaonekana kama alipita mlangoni ni mtu nayefahamika, na hata walinzi hawakuwa na shaka naye, 'kama alipitia mlangoni,..', na angelipitia wapi maana mlango ni mmoja na mlangoni hapo ndio utaruhusiwa kwenda juu au chini,..

Jengo hilo lina juu na chini, watu wengi hawafahamu hilo...na sehemu ya chini haitambulishwi kabisa, zaidi ya marehemu na watu wake maalumu.


Nikawaambia huyo muuaji, alipomaliza hiyo kazi atakuwa alikimbilia vyumba vya chini na kukaa huko hadi hali ilipotulia, ...na ina maana huyu muuaji ana chumba maalumu cha kujificha huko chini, sasa ni nani anayelifahamu hilo jengo vyema, zaidi ya Makabrasha na mjenzi wake....hapo ikawa kazi kumtafuta mtu anayejulikana kuwa analifahamu hilo jengo vyema, ..

‘Lakini pia mtu huyo awe anafahamu mtandao wa ulinzi wa lile jengo, awe anaweza kuusimamia huo mtandao, bila watu kujua, na awe anaweza kuona ni kitu gani kinafanyika ndani ya hilo jengo, ina maana basi kwasabbau hii huyo mtu hawezi kuwa ni mmoja, ni lazima walishirikiana watu wawili....

‘Kwa hoja hizo, hakuna zaidi ya Makabrasha mwenyewe,..’wakasema

'Mimi nina tetesi na watu watatu, ...'nikasema

'Kwa uchunguzi wangu niliwachuja mpaka nikabakiwa na watu watatu, mjenzi wa hilo jengo, mtu wa karibu wa Makabrasha na mtoto wake Marehemu, kati ya watu hao nahisi mmoja atakuwa anahusika, au wawili walikula njama ya pamoja.lakini huyo wa tatu hana nguvu, …huyu wa tatu namuondoa

'Mjenzi wa hilo jengo nilishamchunguza sana nikaona kuwa haweza kufanya kitu kama hicho, tunabakiwa na watu wawili ninaowafahamu mimi …’nikasema

‘Tuambie ni nani na nani

‘Mmoja ni mtu aliyaminika sana na Makabrasha, na huyo ni mtu mwanifu sana kwa Makabrsha, lakini huwezi kumuona akiwa karibu na Makabrasha, mtu huyu  hajulikani sana machoni mwa watu, maana hajionyeshi, kuwa ana mahusiano na marehemu.. Anayemfahamu huyo mtu kuwa ana ukaribu na Marehemu ni mtoto wake, na mimi tu

‘Ni nani huyo mtu..?’ wakaniuliza.

‘Ni mlinzi wake wa karibu, ...lakini sio wa kukaa naye !..’ nikasema

'Kwa vipi...?' wakauliza

'Huyu anamlinda Makabrsha kwa mtandao,..na akiona shaka tu anawapigia walinzi wa karibu wa Makabrasha...yeye anavyoingia kwenye jengo, wengi hawafahamu, wakati mwingine wanamuita 'mzuka'...

'Ni nani huyo...?' wakauliza

'Basi nikawatajia huyo mtu ni nani na wapi anaishi, polisi hawakutaka zaidi kwanza, wakaanza kumfanyia uchunguzi bila hata ya yeye mwenyewe kufahamu, ikaja kugundulikana kuwa ni kweli siku hiyo ya mauaji huyo mlinzi kweli alikuwepo sehemu yake.

**************

Lakini muda mchache baadae mtu huyo alipigiwa simu, mkewe alikuwa mjamnzito, akawa anahitajika nyumbani kwake kwa haraka, kumbe mkewe alikuwa mbioni kujifungua, kwahiyo akaondoka sehemu yake hiyo baada ya kuwasiliana na Marehemu mwenyewe

Na ushahidi upo, muda mwingi, alikuwa hospitalini, na muda aliotoka hapo hospitalini kurudi nyumbani ulikuwa muda ambao mauaji yalishafanyika, kwahiyo akawa hahusiki kwa upelelezi wa polisi..kwahiyo akaambiwa huyo mtoe

‘Haya tuambie huyo wa pili ni nani,....?’ wakaniuliza

‘Ni mtoto wa Makabrasha,...’ nikawaambia na wao wakaguna na kuniambia, haya tuelezee toka lini mtoto akamuua baba yake...lakini ngoja tuone,

Wakachunguza nyendo za huyo mtu kwa siku hiyo, ikaonekana kweli siku hiyo hakuwahi kufika kwenye hilo jengo, hata mimi pamoja na kumweka kwenye orodha hiyo, sikuwa nimempa nafasi ya kuwa muuaji...maana haya mimi mwenyewe nafahamu kuwa siku ile muda wote hakuonekana kwenye jengo, na kama angelionekana walinzi wangeliniambia,…’nikasema

‘Una uhakika gani kuwa walinzi walikuambia ukweli wote..?’ wakaniuliza

‘Kuna watu wangu humo humo wasingeliweza kunificha mimi,…kwahiyo yeye haiwezekani kuwa aliingia humo, atakuwa alipitia wapi, na isitoshe yeye ni mtoto wa marehemu, kwahiyo mimi siwezi kumshuku sana yeye.

‘Ni nani mwingine ambaye ana sifa hizo zote..?’ nikaulizwa

Hapo sasa nikawa sina la kusema, ina maana aliyebakia ni mimi, ....’

‘Na wa tatu ni wewe au sio....’wakasema polisi na hapo ndio walipasubiria ili kuninasa mimi

‘Ni mimi…! Hapana…sijamuua Makabrasha…’nikajikuta nimesema hivyo, na wao wakacheka,

‘Sasa nani mwingine..tuliyajua haya yote, tulitaka ujilete wewe mwenyewe na hoja zako hizo sio kwamba tulikuwa hatujazifanyia kazi, tulishazifanyia kazi, lakini tulitaka tukuone labda mwenzetu una hoja za ziada, aliyebakia ni nani, kama sio wewe..’wakasema

‘Lakini  mimi nisingeliweza kumuua Makabrasha, kama ningelitaka kufanya hivyo, ningelishamuua siku nyingi tu, na kwa namna nyingine kabisa, .....’nikajitetea.

‘Tuambie ukweli, maana wewe ulisema alikufanyia mambo mengi mabaya na ulikuwa na hasira naye na sifa zote za huyo muuaji unazo wewe kama ulivyozibainisha wewe mwenyewe.., kama sio wewe ni nani mwingine..?’ polisi wakaniuliza.

‘Mimi nataka tusaidiane kwa hili, nina uhakika muuaji yupo, na anatuchezea akili, ila sio mimi, ila yupo...ninachowaomba ni jambo moja, nipeni muda nitamtafuta huyo muuaji,wa halali…’nikasema

‘Jambo gani…?’ wakauliza

‘Kwanza…nataka ijulikane kuwa bado nipo humu rumande, muwe mnanipa nafasi ya kutoka kila ninapohitaji kutoka, ili niendelee na uchunguzi wangu, nina uhakika tutampata huyo muuaji, lakini kwa njia zangu nijuavyo mimi..nawaomba msiniingilia kabisa...’nikawaambia.

‘Hatuwezi kukuachia kwasababu sasa hivi wewe ni mshukiwa namba moja,na pili kuna tetesi kuwa kuna watu wanataka kukuua, ni tetesi, na tetesi hatuwezi kuzipuuzia,….sasa ni kwanini wanataka kukuua, ndio hapo tunamashaka...’wakaniambia.

‘Kwanini watake kuniua mimi…, kama sio kwamba wao ndio wauwaji, na sasa wameona  kuwa nilikuwa mbioni kuwafichua ndio maana wanataka kuniua, kwanini hamjiulizi hilo, nipeni hiyo nafasi, nina uhakika tutampata huyo muuaji halisi kuliko kuning'ang'ania mimi, niamini mimi, mimi sijamuua Makabrasha,..’nikawaambia polisi.

‘Hebu tuambie huo mpango wako wa kumpata muuaji,...?’ akaniuliza mpelelezi wao, nikamuambia hii kazi nataka kushirikiana na mmoja wa wapelelezi wao ninaowaaamini mimi…

‘Akina nani…?’ wakaniuliza na mimi nikawatajia, maana nawafahamu  nimeshawahi kufanya kazi na watu hao, ni wasiri wangu wa kubwa,...hata hivyo wakataka wafahamu mipangilio yangu ipoje.

‘Mimi nawaomba jambo moja, mimi nitaendelea kuwepo humu, ila muda fulani fulani nipeni ruhusa ya kutoka, na nyuma yangu wawepo hao wapelelezi, kwa kificho, wasijulikane kabisa,…’nikawaambia.

Na pili  chombo cha kuvaa ambacho, nikikivaa mtaniona kila ninapokwenda...’ wakaitana na kukaa kikao chao, wakajadiliana na baadaye wakanikubalia, lakini ni baada ya mabishano yao marefu, kwani wao walitaka kila hatua niwe pamoja nao, nikawaambia kwa njia hiyo hatufanikiwa. ..

‘Siku ya kwanza sikufanikiwa, na ya pili,….ikawa sasa kuna kukata tamaa, yaonekana mimi najaribu kupoteza muda, …ujue hadi hapo bado na wao walikuwa hawana ushahidi wa uhakika kuwa mimi ndiye muuaji...ni kwanini kuna watu wanataka kuniua mimi...ni kwanini....., vinginevyo wasingelipatia hiyo nafasi.

 Siku ya tatu, ndio mambo yakajileta, na siku zote hizo nilikuwa nikienda kwenye hoteli moja ambayo jamaa hawo ninaowashuku hupenda kwenda kustarehe hapo, na humo kuna seehmu maalumu marehemu aliweka vifaa vyake pia, ...vya kuangalia jengo lake kwa mbalia...humo kuna kila starehe, na nilijua udhaifu wao, ni pombe na umalaya...

 ‘Mimi nikajiweka kinamna, nilipewa gari, la kifahari, na pesa kidogo, nikajifanya kama binti wa geti kali, nilijibadili kabisa, na ungeniona usingelinitambua kuwa ni mimi, huwa nikiwa kazini nabadilika kabisa,....maumbile, mwendo, sauti...huwezi amini...

‘Wanaume kwa uroho wao, waliponiona ile siku ya kwanza, wakaanza kunimezea mate, maana nilitokelezea, hata ingelikuwa ni nani, angenitaka. Wakwanza nikamtolea nje, maana sikuwa na haja naye, akaja mwingine na mwingine, hadi siku ya tatu alipokuja mtu wangu ninayemtaka....

‘Mtu niliyemlenga sana na huyu mlinzi wa karibu wa Marehemu, mimi huyu nilimweka kwenye shuku zangu...

Kwa kipindi hiki, sasa anafanya kazi kwa mtoto wa Makabrasha, huyu nilikuwa bado sijakata tamaa naye, ..hisia zangu zilinituma kuwa huyu mtu atakuwa anahusika kwa namna mja au nyingine...na hasa nilipoona bado anaendelee kuwa karibu na mtoto wa Makabrasha, nikajua kuna kifo kingine kitakuja,...

Jingine hawa watu wawili, mtoto wa marehemu na huyu mlinzi walikuwa hawaivani kabisa, kipindi cha uhai wa marehemu,...walikuwa ni maadui, leo hii wanaelewana, hapa nikatilia shaka..ni kwanini....

‘Siku hiyo huyu jamaa akanijia,...nilikuwa nimekaa meza ya peke yanu nikionekana kumsubiria mtu...nashangaa mtu huyu.... na alionekana kuwa na pesa kweli, nikahisi wana jambo wamelifanya, nikajibaragua na baadaye tukaelewana, hakunitambua kabisa kuwa ni mimi, hata ingelikuwa nani, asingelitambua, ...

‘Tukaanza kuongea kidogo, moja likazaa jingine, tukawa marafiki wa muda mfupi, mimi naifahamu sana hiyo kazi, nina uzoefu nayo, jinsi ya kuwanasa hawa viumbe waitwao wanaume,..sijisifii, lakini sijawahi kufanya makosa, najua madhaifu yao yapo wapi.....jamaa bila kujijua akanasa kwenye anga zangu....sikumchelewesaha, wakati anakwenda kujisaidia mimi nikaweka kitu kwenye kinywaji chake.

‘Kuna aina ya madawa ukimwekea mtu, analewa haraka, anakuwa kama kapagawa hivi...lakini hapotezi fahamu, wanaitumia sana majasusi wanapotaka kupata taarifa kwa mtu,...niliiomba kwa watu wa usalama, wakanigaia, na hiyo ndiyo ilikuwa silaha yangu, sikutaka bastola hapo...

Aliporudii kutoka kujisaidia, nikaendelea kumelegezea, kwanza alijaribu kuwa muangalifu,…unajua tena watu waliopitia uaskari walivyo,..lakini hakunielewa, ikafika muda akajisahau na kuanza kunywa kile kinywaji,..nilimuona kama anasita lakini huyo akanywa,..mara kaanza kulegea, na akili ikaanza kumtoka, na mimi hapo hapo nikamwambia;

‘Mimi ni mchumba wa mtu, sitaki kuonekana onekana hadharani hivi, nilikuja hapa tu kupotza mawazo,…nataka kuondoka,…’nikasema

‘Oooh, hapana, usiwe na wasiwasi, kuna sehemu tunaweza kwenda hutaonekana kabisa, unasikia, unajua mimi nimevutiwa sana na wewe,…kiukweli wewe nai maalumu, unsikia, sikilizaa…twende sehemu pesa sio shida…’akasema

‘Usinihadae,…nawafahamu sana nyie waume, nikiharibu kwangu utakuja kunikimbia, na mimi sitakubali…’nikasema;

‘Kuna sehemu naifahamu, twende.....’ akasema, basi nikajifanya nimekubali kwa shingo upande.

Nikamwambia atangulie nje…nitakuja…

‘Sikiliza wewe acha gari lako hapa, huyu mlinzi wa hapa namafahmu, atakulindia kwa muda wowote unaoutaka, …au unasemaje, usijali kabisa..’akasema, na alionekana kweli kazimia kwangu

Basi tukatoka hapo kwa kupitia mlango wa nyuma, yeye akaniambia nibakie nyuma, ili yeye atangulia akaongee na mlinzi, basi akafanya hivyo, baadae nikajitokeza na tukakutana kwenye gari lake, kabla sijaingia kwenye gari lake ndio akaniuliza.

‘Huwa unafika hapa mara kwa mara..?’ akaniuliza

‘Ndio, lakini mara nyingi nafika na mchumba wangu, sema kasafiri, lakini kwa vile ni sehemu nimeizoea, ..siachi kufika, lakini ni mtu ambaye anaweza kuja ghafla,..si unajua tena…’nikasema

‘Ok..akija,…gari lipo, au sio, na sisi tukirudi nitahakikisha unaingia mlango wa nyuma,…unaonaeeh, atajua ulitoka kidogo au sio…’akasema

‘Hata hivyo sura yao sio ngeni sana kwangu…’ akasema hapoo nikashtuka ina maana keshanigundua nini..lakini nilikuwa na uhakika hawezi kunifahamu, maana kuna utaalamu wa kubadili nyusi, na rangi za macho, na nywele, sikuhitaji kuvaa ngozi bandia,...mimi katika kazi yangu hiii wanapenda kuniita kinyonga, ....naweza tukawa pamoja sasa hivi nikaingia chumbani nikitoka hunikumbuki tena....

Basi, yule jamaa akasema kwa vile naogopa, atanipelekea sehemu ambayo anaiona ni salama zaidi ambayo sio mbali na hapo.., tukaingia kwenye gari lake, na kuanza kuendesha, kama nilivyotarajia nikaona tunelekea uwanja wa ndege, nikajua ni kule kule, na mtego umefanikiwa,

Tukafika karibu na jengo la Marehemu, jamaa huyo hakulipeleka moja kwa moja kwenye maegesho ya mgari, akalipitisha kwa nyuma, hadi sehemu nyingine, kunapohifadhiwa magari ya jengo la pili yake, akachukua ufungua na kufungua geti, kulikuwa na geti dogo la jengo hilo la pili kwa nyuma....kulikuwa hakuna walinzi.

‘Huku ni wapi? Nikamuuliza

‘Huku ni kwa rafiki yangu, ila nataka tuingie kwenye hilo jengo hapo, ni la marehemu, kuna hoteli ya ndani kwa ndani, humo tutastarehe tupendavyo, huyo mchumba wako hatakuona kabisa..’akasema kwa sauti ya kuonyesha hayo dawa imemchukua na sikupenda hiyo dawa iishe nguvu kabla hatujaingia ndani.

Tulipoingia kwenye hilo geti dogo, nikaona akifungua mfuniko, kama ile mifuniko ya mashimo ya maji machafu, nikamuuliza;

‘Unafanya nini ...mbona unafungua mifuniko ya choo?’ nikamuuliza

‘Usijali hii ni njia muhimu ya kuingia ndani, hakuna anayeifahamu zaidi yangu mimi na marehemu na mtoto wa marehemu....’akasema.

‘Huyo marehemu unayemtaja ni nani?’ nikamuuliza

‘Mhh, alikuwa akiitwa Makabrasha ameshafariki....’akasema

‘Mhh, yaani kafariki na kuliacha jengo nzuri hivyo, na wewe ni mtoto wake?’ nikamuuliza

‘Hapana yupo mtoto wake, ndiye anayelimiki hilo jengo kwa sasa..’akasema

‘Na huyo mtoto wake ni nani anaonekana ni tajiri sana....?’ nikamuuliza

‘Achana naye, akikuona wewe najua ataninyang’anya anapenda sana kuninyanganya mawindo yangu...sio mtu mzuri, ...hana huruma, akikuambia utakuwa chakula cha mchwa utakuwa kweli...haogopi, ...’akasema.

‘Una maana gani..?’ nikauliza

‘Usiwe na wasiwasi upo na mimi, …najua yeye ku-ua mtu sio tatizo….sio mtu wa mchezo ila kwangu ananiheshimu, ukiwa nami hakuna shaka…hata hivyo mimi ndiye ninayefahamu siri zake…’akasema na moyoni nikasema sawa kabisa.

‘Kumbe kuna njia hii ...’ hapo nikasema kimoyo moyo…nikatulia kwanza, sikutaka kumuuliza sana, asije akanitilia mashaka, akafungua kile kifuniko na kuninyoshea mkono kuwa nisogee pale, hakufahamu kuwa mimi ni mkakamavu wa kijeshi.

‘Sasa tunaingia,…njia hii ni safi kabisa, kwa nje kunaonekana hivyo, lakini ukiaanza kuingia ndani utazikuta ngazi, unateremka nazo..hizo zinakwenda moja kwa moja hadi kwenye hilo jengo la marehemu, hii ni sehem yake maalumu ya usalama, ni njia za dharura...’akasema.

‘Oh, kwanini awe na njia za namna hii, mnauza madawa ya kulevya nini?’ nikamuuliza

‘Matajiri wengi wana mbinu zao za kuishi, wanajihami kwa kila njia...’akasema.

‘Sasa kama ni hivyo huyo marehemu alikufa kwa ugonjwa au aliuwawa?’ nikamuuliza

‘Walimua bwana,..alikuwa bosi wangu, nikiwa na shida, ananisaidia, sasa nimebakia na huyu mnyama, ananifanya kama mtumwa wake, inabidi nitumie mbinu za kumuibia, sina ujanja...kama jana nimemchomoa mamilioni ya pesa..bila hata kufahamu, akabakia kusema kaibiwa na watu wa benki...’akasema.

‘Oh kumbe walimuua, jamaa wa watu, kwanini walimuua....?’ nikamuuliza

‘Mambo ya mali hayo, unafikiri, ukiwa na watoto waroho, wanawake waroho, na una mali, ujue upo hatarini, na ikizingatiwa kuwa hata marehemu mwenyewe alizipata mali hizo kwa dhuluma..kwahiy ndio hivyo maisha ya dhuluma mwisho wake ndio huo.....’akasema na kutulia.

‘Na mara nyingi watu kama hao wanauliwa na watu wao wa karibu, ..hasa nyie mliokuwa mkifanya naye kazi karibu…’nikasema na kucheka,  na yeye akasema

‘Hahaha…acha zako hizo,…keshaondoka basi …acha sisi tutumie, japokuwa kiukweli nilikuwa na mpenda sana…’akasema

'Kwahiyo ina maana waliomuua ni mtoto wake, au mke wake, au walishirikiana kumuua....au ni wewe ?' nikamuuliza, hapo akabakia kimia.

Akafungua mlango wa kuingia kwenye jengo, huku akiwa kimiya, halafu akaniangalia na kusema;

'Tumeshafika...karibu hoteli ya maraha ya Marehemu, hapa usiwe na wasiwasi kabisa....'akasema na mimi nikamuuliza

'Mhh, wasije kuniua na mimi, nimeshaanza kuogopa,…kama watu wanafikia kumuua tajiri kama huyo sembuse mimi....'nikasema

‘Hahaha usijali , mimi nitakulinda usijali kabisa, ..’akasema

‘Mbona hukuweza kumlinda bosi wako…?’ nikamuuliza na hapo kidogo akashtuka.

‘Mbona maswali yako yapo hivyo, usiwe na wasiwasi…’akasema

‘Hapana mimi sipendi maisha ya mashaka mashaka, …ndio maana nakuhoji, ili nijue nipo sehemu kweli salama…’nikasema

‘Usijali…’akasema

‘Au nimekosea kukuuliza…’nikasema

‘Hapana wewe uliza tu…’akawa anaongea kilevi kilevi.

‘Mimi ukinambia jambo napenda kujiuliza uliza sana…ni nani alimuua huyu mtu wa watu naogopa sana, mtu tajiri kama huyu anauliwa,…si alikuwa mtu mwema, anasaidia watu au sio..?’ nikamuuliza,

‘Alikuwa mwema, wakati mwingine, wakti mwingine ndio hivyo kutafuta, sasa kutafutwa na yeye akawahiwa, ndio maisha ajali kazini,…, unajua ukimuongelea nakumbuka mbali sana, nilimpenda sana, lakini kazi ni kazi, utafanyaje …’akasema

‘Kama ulimpenda kwanini hukusaidia polis wampate huyo muuaji wake, ..au muuaji unamfahamu au ni wewe?’ nikamuuliza na hapo akatabasamu, halafu akatikisa kichwa na kusema;

‘We acha…ndio maana nakuambia ni ajali kazini, alikuwa sio mtu rahisi kihivyo, mmh, sasa sikiliza tusiongee sana hayo, au…’akasema na kunywa, alionekana kama dawa inaisha nguvu nilitaka nipate mwanya wa kumuongezea nyingine,..na kweli ikapatikana kwenye gilasi yangu mwenyewe, ndio nikaweza, na kujivunga kama nakunywa, aliporudi nikawa nimebadili zile gilasi kia-aina, akanywa.

‘Mbona hujanijibu swali langu, mimi huwa nikiuliza swali mtu asiponijibu nakuwa na mashaka naye…’nikasema

‘Swali gani mpenzi, uliza chochote mimi nitakujibu,..unasikia chochote…’akasema

‘Ni nani alimuua huyu tajiri wa watu jamani…?’ nikamuuliza hapa, akatikisa kichwa kusikitika, inaonekana kweli inamchukua hiyo hali ya kumbukumbu, na anakuwa kama anawaza mbali, au kuogopa, vyote viwili,…nikasubiria jibu

NB: Tuishie hapa kwa leo..naombeni maoni yenu maana kisa kinafikia ukingoni, je kuna kitu tumekisahau....



WAZO LA LEO: Mali na watoto ni mtihani mkubwa kwa wazazi, ukiwa navyo ni ufahari,...lakini vyote hivi vina mitihani yake.  Mali ikiwa ni ya halali, inaweza isiwe ni tatizo, muhimu ni jinsi gani y kuitendea haki yake. Ama kwa watoto ujue jinsi gani ya kuwalea..wawe na elimu na maadili mema. Elimu pekee haitoshi. Elimu bila maadili mema inaweza kugeuka kuwa tatizo pia, wasomi wangapi wazuri lakini wanafanya mambo ya hatari kwenye jamii, kwa kutumia elimu yao, ukichunguza sana ni kutokana na ukosefu wa maadili mema,...

Tumuombe mola atupe mali za halali zenye tija, na watoto wema, wenye elimu na maadili mema. Aamin

Ni mimi: emu-three

No comments :