Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Monday, January 22, 2018

MKUKI KWA NGURUWE-63


 Sasa nikiwa nyumbani,… akili ikiwa haikubali kupokea hayo niliyoyaona , na kusikia,…bado nahisi sio ushahidi wa kutosha, bado...maana nimeshawahi kusimama mahamani nafahamu ...jinsi gani ya kumshawishi hakimu...

'Hata hivyo, ..hii ni hatua kubwa sana...'nikajipongeza, na hapo ndio nikaamua nijitulize kidogo kitandani ili kupumzisha akili yangu, lakini hata kabla sijafumba macho, mara nikasikia nina ugeni.

‘Nimekuambia napumzika, sitaki usumbufu, mbona hunielewi mdogo wangu....’nikamwambia msaidizi wangu wa nyumbani kwa hasira.

‘Lakini huyo aliyefika ni baba yako dada…’akasema

‘Oh, baba yangu!!.., kuna nini tena jamani…' nilijikuta nasema hivyo, maana bba sio mtu wa kufika kwangu mara kwa mara na akitaka kuja ataniarifu, ili sipoteze muda wake akute sipo...

'Samahani kwa kauli yangu, haya ..mkaribishe ndani, keshaingia ndani, ok, ok…haya nakuja…’hapo uchomvu ukaniishia, baba akifika kwangu ni kama bosi wa kampuni yako uneyemuogopa, na kumuheshimu sana kafika nyumbani kwako.

Kwa haraka nikajiweka vizuri na kuelekea chumba cha maongezi, nikamkuta baba akipata kinywaji, huku kasimama, kuonyesha kuwa hana hata muda wa kukaa, ...yeye nyumbani kwangu ni kama nyumbani kwake, akifika hasubiri kuhudumiwa, anakwenda kwenye jokofu anajisaidia mwenyewe… japokuwa anapaheshimu kama sehemu ya mkwe wake.

Alikuwa kasimama akingalia nje kwa kupitia dirishani na aliposikia nyayo za mtu akageuka na kunikagua kwa macho hata sijamsalimia akasema;

'Bint yangu upo sawa kweli…?’ akaniuliza aliponitupia jicho, unajua tena huyo ni mzazi wangu akikuangalia tu anafahamu kuwa upo sawa au una matatizo.

‘Nipo sawa baba, ni majukumu tu ya kila siku… na kuchoka choka kidogo..hamjambo wewe na mama, kupo salama huko..?' nikamuuliza hivyo

‘Upo sawa wakati upo nyumbani, unajua nilipitia kazini kwako nikaambiwa hujafika leo, unaumwa…?’ akaniuliza

‘Hapana baba mimi siumwi, zaidi ni mume wangu, nilikuwa na kazi, nikapanga kuwa nizifanyie huku nyumbani, lakini kila ukimaliza moja inakuja nyingine,, mpaka nikaona leo sitaweza kufika kazini kabisa,..kiukweli kazi nilizozifanya hapa  nyumbani leo, hata ningekuwa ofisini nisingezifanya hivyo..’nikajitetea

‘Lakini nyingi ni za kifamilia au sio..?’ akaniuliza kwa sauti ya kawaida tu

‘Ndio baba..’nikasema

‘Na hizo kazi za kifamilia , ndizo zinakufanya hata ushindwe kutuliza kichwa chako kwa ajili ya kazi za ofisini ambazo pia ni muhimu kwako, au sio..?’ akaniuliza nikajua baba ananitega kuna kitu kaja nacho anatafuta njia ya kuniingia.

‘Baba lakini mimi ni mzazi, ni mwanamke wa nyumbani pia, na zaidi unafahamu kuwa mume wangu ni mgonjwa, kwahiyo inanibidi niwajibike kote kote…’nikasema

‘Sawa sijalipinga hilo, ..nafahamu sana, lakini ukweli ni ukweli tu, kuwa majukumu ya nyumbani yamekuwa makubwa zaidi ya uwezo wako, …au sio, au niseme mitihani ya nyumbani umakuzidi, na bado hutaki kusaidiwa, sio mbaya..lakini nina uhakika hayo unaykabiliana nayo kwa sasa yanakuchanganya kichwa, kweli si kweli…’akasema

‘Ni kawaida tu baba…’nikasema

‘Ni kawaida tu eeh, hahaha…niambie ukweli ni nini kinachoendelea kwa hivi sasa ndani ya nyumba yenu..?’ kwanza alicheka lakini alipoongea hiyo 'niambie'  akapandisha sauti.

‘Baba nimekuambia ya kawaida tu, ni yale yale...'nikasema

'Akatikisa kichwa kama kukubali, halafu akaniangalia kwa makini akasema

'Haya niambie, huo ukawaida wake...'akasema

'Baba kwani kuna nini, mambo ni yale yale bado napambana nayo hatua kwa hatua naanza kuyakabili, najua mwanzo ni mgumu,…lakini hadi sasa nimeanza kuthibitishia baadhi ya mambo, ambayo yalikuwa yakiniumiza kichwa, na leo tu, nilikuwa nahitimisha baadhi ya hayo mambo, …’nikasema,

‘Binti unanifahamu sana, nikija hapa kwako ujue ni jambo nzito, ..najua kuna wagonjwa, lakini mgonjwa huyo, yupo huko hospitalini na huko anafanya mambo yake..ofisi kaihamishia huko..au sio.. hata hivyo, ni wajibu wangu kukutembea, lakini siwezi nikaja kwa kukushtukizia kama hivi, bila sababu maalumu,  naheshimu mila na desturi zetu kuwa hapa ni nyumbani kwa mkwe wangu hata kama hayupo…’akasema

‘Baba lakini hapa ni nyumbani kwa watoto wako unaweza kufika muda wowote utakavyo…’nikasema

'Binti…huyo jamaa anayetaka pesa kwa ajili ya kuuza ushahidi dhidi ya mume wako ni nani…?’ akaniuliza na moyo ukalipuka paaah, nikajua rungu jingine linaniangukia kichwani, kama baba kalifahamu hilo, je polisi..na je kuna nini kwenye huo ushahidi, na kwanini baba akalifahamu hilo…nikakaa kimia kwanza kutafakari huo mtego wa baba.

‘Ina maana gani, yaani kila mara ninapofanya jitahada ya kulisafisha jina langu, kwa sababu ya madhambi yenu, mnanipachika mzigo mwingine… ni kwanini mnafanya hivyo, mnataka wazazi wenu tufe kwa shinikizo la damu...au, halafu mje kulia..wakati chanzo ni nyie…’akawa kama anauliza

'Baba kwani...'nikataka kusema lakini yeye akaendelea kuongea,....

‘Ilikuwa ni wewe, kwa kashfa ya mauaji,..unajua jitihada gani nilizozifanya kuisafisha hiyo kashfa,…unakumbuka ilibidi hadi nikutane na waandishi wa habari kuliweka hilo bayana kuwa hauhisiki na hayo mauaji, baada ya ushahidi… haya,  hayo yakaisha, …sasa hili tena, kuna nini hapa kwenye nyumba yenu..’akasema kwa ukali

‘Baba, hata mimi ndio…nimesikia na…bado..hakuna uhakika kuwa ni kweli…ushahidi hakuna..’nikajitetea  hivyo.

'Sikilizeni, hili naliongea mbele yako, hata kama utanielewa vibaya, sitojali, maana kila dalili zipo....mume wako huko kuumwa kwake kwasasa kuna walakini, yaonekana kama anaiigiza tu...alishapona, ila anafanya hivyo kwasababu maalumu, hilo nakuambia wewe ulisikie hivyo…' hapo nikabaki kimia.

‘Na hata kama angelikuwepo yeye hapa ningelimwambia hivyo hivyo, …’akasema akinikodolea macho ya kutisha, baba hana mchezo akikuangalia unatamani ujifiche.

'Baba..." nikata kuongea akainiashiria kwa mkono kuwa hajamaliza kuongea.

'Najua utamtetea mume wako, najua kutokana na kauli za madocta utasema ni kweli anaumwa,..sawa anaumwa,..nisije nikakufuru, lakini hayo matendo anayoyafanya mbona yanapingana na ugonjwa wake…usifikiri mimi sijui matatizo kama hayo yapoje,….mimi sijazaliwa kesho, watu kama hao nimeshakutana nao sana..lakini hilo la kwake limezidi kipimo…’akatulia

'Baba lakini huyo aliyesema hivyo ni docta bingwa wa hayo matatizo...'nikasema

'Ni kweli, ..ni nani huyo docta bingwa

'Ni yule yule wa awali, nakumbuka uliwahi hata kuongea naye..'nikasema

'Ok...siku kadhaa alikuwa karibu sana na huyo mpinzani wangu wa kisiasa...unajua kwenye haya mambo kila kitu kimachunguzwa...kuonekana na huyo mpinzani wangu sio tija, maana yeye ni dakitari wa wote..lakini kwangu mimi inanipa maulizo mengi...lakini..'hapo akatulia

'Ina maana baba humuamini huyo docta...?' nikauliza

'Sio kwamba simuamini..lakini yeye kama docta anafuata vielelezo vyake, na huo ugonjwa, pamoja na mengine kinachoangalia zaidi nai matendo ya mtu, je mtu ukiijua huo ugonjwa ulivyo, ukaigiza sawa na hayo matendo, docta atagundua ...?' akasema

'Baba haiwezekani sio kwa madocta bingwa...'nikasema

'Mimi nikiwa shuleni, niliteguka nyonga, nikaenda kwa docta..na nikatibiwa, wakati natoka kwa huyo docta, nikajikakamua tu, ili kutokujilegeza, wakati kweli hapo naumia, huyo docta bingwa, akanijia na kusema siumwi...akachanga karatasi ya mapumziko,..lakini kweli naumwa...'akasema, na mimi nika kaa kimia

'Ninachotaka kukuambia ni hivyo, kuna magonjwa, docta anakuamini wewe, ukiigiza, hewala yeye atafanya nini, atahitimisha jinsi anavyoona kwa macho yake, hana makosa, ..unielewe hapo, mwenye makosa ni wewe unayeigiza, ..na hatari ya ugonjwa ulivyo ukiigiza ipo siku utakupata kiukweli...'akasema

'Baba mimi nawaamini sana madocta..'nikasema

'Hata mimi..sijasema siwaamini, ila kwenye tatizo, walakini hauchezi mbali hasa ukiwa unagusa kinyume na matarajio yako...tuombe mungu kuwa ni kweli, kuwa anaumwa kihivyo, lakini kama anaigiza, ...nakuambia hili, mume wako ataumbuka sana...'akasema

'Baba huyo mtu anaumwa, sema yeye anaweza akautumia huo ugonjwa...lakini mimi sina mawazo hayo mabaya, ninaamini kuwa anaumwa, mengine ..ni juu yake...'nikasema

‘Sasa sikiliza najua utarejea kauli yako kuwa labda nayasema haya kwa kutokuwajali watu wengine, au kwa vile sikupenda wewe uolewe na mtu kama huyo, au kama wengine wanavyosema kuwa labda nabagua,...lakini eeh, mimi kama mzazi sina makosa, kwa hilo, yoyote atafanya jitihada kuhakikisha bint yake anaolewa sehemu salama, na kwa hili wewe mwenyewe umeshajionea…na sitakosea nikisema bado…bado binti yangu upo kwenye mtihani mkubwa... ‘akahema na kuangalia pembeni.

‘Baba lakini kwani kuna nini…?’ nikamuuliza

"Kuna nini!!, mhhh....wajifanya hujui sio, …eti kuna nini,...'akatikisa kichwa halafu akaendelea kuongea

'Binti...umejifanya kunificha mengi lakini mengine hayafichiki,..je wewe husomi magazeti, hata kama ni ya udaku, lakini ndiyo watu wengi wanayasoma, na hao watu wengi eeh, ndio hao wapiga kura wangu…unafikiriaje…wakisoma kashfa kama hizo, unafikiri kwa mtizamo wako wao watasemaje, sio kwamba nawadharau, lakini akili zao zitawatuma hivyo, kuwa ni kweli,...upeo wa kufikiria kwa kila mtu unatofautiana, au sio…’akasema

‘Sisomagi hayo magazeti baba…’nikasema

‘Ndio najua...mkurugenzi mkuu usome magazeti kama hayo,...hahaha, ni sawa wewe..huwezi kuyasoma hayo maana hayagusi masilahi yako,..lakini kwangu mimi ni muhimu sana kuyasoma, kila gazeti mimi nasoma hata yale yanayoandika uchafu....ili kujua kila kitu kwa watu wangu..., kila kitu kinachohusu wapiga kura wangu, ni muhimu kwangu,....na wengi wa hao ndio hao, wanaoyaamini hayo magazeti, na mpinzani wangu ndiye anayatuumia sana hayo magazeti unajua ni kwanini…’akasema

‘Kwani, wamesema nini baba…?’ ikabidi nimuulize 

‘MKWE WA MWANASIASA MKONGWE ANASHUKIWA KWA KUMUUA WAKILI WAKE, kichwa cha habari kikubwa, na kidogo....'WAKILI MTETEZI WA WANYONGE…’ hicho kichwa cha habari hapo, …unafahamu athari za maelezo hayo tu,..kwenye uwanja wangu wa kisiasa…na hapo hujasoma huko ndani…huko, nasikia, nasikia zipo nyingi tu, zikianisha kashfa na uchafu dhidi ya mumeo…’akasema

‘Mauchafu gani…?’ nikauliza nikijifanya sijui lolote

‘Mumeo kamwe hawamtaji kwa jina lake…kwangu mimi wananitaja kwa jina alngu mkongwe wa siasa so and so…, ni kwanini…na ni kwanini yeye wanamtaja kama mkwe wangu...kwanini…uone kwanini nawaonya sana kuhusu kashfa..’akasimama

'Baba mimi sijui maana sijalisoma hilo gazeti...'nikasema

‘Ukiangalia hata maoni ya watu kunihusu mimi, kiwango cha uaminifu kwangu kinashuka na wambeya wameshapata la kuongea, na ikitoka hapo, nisipofanya jambo hata magezeti haya ya kawaida wataanza kundika…unataka mimi nifanye nini hapo, niendelee kukaa kimia au sio..., nikae kimia tu kwa vile wewe binti yangu kipenzi,...hutaki mimi niingilie  mambo yenu au sio, ..eeh, hebu hapo niashauri mimi…’akasema

'Lakini baba…’nikataka kujitetea, na yeye akanikatisha kwa kusema;

'Lakini baba..lakini baba…najua unataka kusema nini,  kuwa familia yako haihusiani na maisha yangu ya kisiasa, kuwa hizi ni familia mbili tofauti , kila mtu na maisha yake,..au sio...hilo wewe wasema, lakini sio wapinzani wangu....'akasema

'Mhh...'nikaguna hivyo.

‘Umenielewa hapo, kama ingelikuwa ni hivyo, utakavyo wewe,  ni kwanini hao waandishi hawaandiki wakirejea familia yako tu , wewe na mume wako, wanaandika kwa majina makubwa, ‘mkwe wa…’ …kwanini, kwanini..…ndio maana ni lazima niwajibike…’akasema

‘Baba, niachie hiyo kazi, naomba nilifahamu hilo gazeti , mimi nitakwenda ofisini kwao, ikibidi tuwafungulia mashitaka..’nikasema

‘Utakwenda kufanya nini wakati jeraha limeshavuja damu..unajifanya wewe unafahamu kuliko mimi, eeh..haya nenda kaonane nao, ...utawaambia wasiandike kuhusu mimi,…unajua ni nini wataandika kesho yake…unalifahamu hilo…BINTI WA KIGOGO WA SIASA KAVAMIA OFISI YA MAGAZETI, kitakachofuata ni nini, waandishi watafika nyumbani kwangu, hata wale waliokuwa wamekaa kimia, …’ akatulia akiangalia saa yake.

‘Kwahiyo baba wataka mimi nifanye nini…?’ niamuuliza

‘Wapinzani wangu wa kisiasa wameshaona uchochoro wakuniharibia mimi ni kupitia nyie wawili..hawachezi mbali na nyie sasa mumekuwa 'super stars,..' lakini wa nini basi,...…wameshawasoma na kufahamu madhaifu yenu, na mume wako kafanywa ndondocha, na sio ndondocha wa ucahwi,...ila wanamtumia,...bila hata ya yeye kufahamu,..sasa hivi wanatafuta kila mbinu za kuhakikisha mgogoro wenu hauishi, bali unafichua kashfa zaidi na zaidi....’akatikisa kichwa kama anasikitika.

'Sasa baba....'nikataka kusema wazo langu lakin hakutaka kunipa muda.

‘Mimi siogopi kupambana na hao watu…lakini nawahofia nyie…mtaumia,..na kwenye vita macho hayaoni,..aliyepo mbele yako ni adui yako, sasa kama nyie mumewekwa kama kinga yao, nitafanya nini…mwishowe nitaishia kusema bahati mbaya, na nani ataumia kama sio mama yako....’akasema

‘Kwahiyo baba unataka kusema nini hapo..?’ nikauliza

‘Nitasema nini ..eeh, niambie nitasema nini, wakati binti yangu, mkurugenzi mkuu wa kampuni A nd Z, yupo, eeh,..mke jasiri, eeh…hata siku moja hawakutaji kwa MRS mumeo,wanataja binti ya, na kwa mumeo, 'mkwe wa…' sijui unanielewa lakini…hata siku moja hawawezei kutaja mazuri yako kwa kurejea jina langu, ila mabaya wanafanya hivyo,….ujue ni kwanini nawaandama …mimi sitaki kupoteza muda wangu kwa maisha yenu..maana nyie sasa ni familia tegemezi, lakini kwa haya mimi nitafana nini...’ akatulia.

Hapo nikaanza kuvutia hisia kujua ni kwanini baba kafika kwangu kwa hasira

*************

'Huyo mtu anayenitishia mimi, kuwa nisipojitoa kwenye uchaguzi ujao, atauweka uchafu wa familia yangu ni nani..najua keshawasiliana na wewe…sasa sikiliza , sitaki ufanye anavyotaka yeye, kufanya hivyo ni udhaifu..unasikia hata kama mume wako atakwenda jela…pambana kwenye haki na ukweli, unasikia...’akasema

‘Lakini hakuna ukweli wa hilo au sio baba…?’ nikasema

‘Ninachotaka ni wewe kutokukubaliana na yeye, kwa hivi sasa hawezi kukutana na wewe uso kwa uso,... anatumia mbinu za simu tu, kukusumbua...anafahamu mkikutana na yeye atakamatwa, na sio kwamba polisi wameshindwa kumkamata, lakini kuna kitu kinaendelea hapo, wewe huwezi kukufahamu, ila sisi tuliopo kwenye huo ulingi wa siasa tunakifahamu ni nini...unasikia  bila kukuficha kinachoendelea kwa sasa ni mambo yetu ya kisiasa…’akasema

'Kwahiyo baba, mimi nifanye nini..ndio swali la msingi hapo....?' nikauliza

'Kwanza jichungeni..niliwaambia jamani, kuweni mbali na kashfa, ukasema nini...hilo nikuachie kwa vile ni familia yako..haya nimewaacha matokea yake ndio haya...nilijua tu haya yatakuja kutokea, lakin nitafanya nini, na wewe ushapenda, haya kupenda sio kubaya, lakini mtu uliyempenda, habebeki...utaumia binti yangu...'akasema

'Baba mimi nalifanyia kazi, wewe mwenyewe utaona,...kama ni kweli, baba, niamini ...ila sitaki kufanya jambo bila kuwa na uhakika,...na uhakika huo, wataubainisha wao wenyewe, baba, niamini mimi...'nikasema

'Hahaha, siwezi kumuamini mtoto wangu, mtoto ni mtoto tu..kwa hivi sasa huwez kunidanganya,...'akasema

'Haya baba...'nikasema

‘Sasa narudia tena,…sitaki..umsikilize huyo tapeli, kama atawasiliana na wewe..nijulishe haraka…na kuanzia sasa nitaanza kuingilia mambo yenu yote, kuanzia kazini, hata ya nyumbani…siwezi kuvumilia tena…na hii sasa ni vita ya kisiasa, najua yenu ni ya kifamilia, lakini wameivumisha iwe hivyo, sasa kazi ni kwako, uwe na baba yako au uwe na maadui wa baba yako...’akasema

'Unasema nini baba…! Huoni ndio utajiharibia kabisa, haya yangu usijiingize baba, nakuomba tafadhali, huyo mume wangu ninajua jinsi gani ya kumweka sawa, mpaka hatima yake, siwezi kumuacha, hilo baba nilishakuambia…’nikasema

'Najua...nafahamu sana,..ila nakuambia hivi, kama ni mume wako, kama ni familia tegemezi, kwanini sasa nipo mbali na nyie, madongo yakirushwa kwenu yanailenga na mimi,  je nitaweza kuvumilia hayo, nikae kimia tu…, au nifanye kama mnavyotaka wewe na mama yako, kuwa niachane na mambo ya kisiasa, hicho ni kifo cha kondoo,. mimi sikulelewa hivyo, nitapambana, unasikia, huyo ndiye baba yako…’akasema

‘Baba hapana, mimi sijasema hilo, ila mimi sikupenda mambo yangu yahusishwe na nyie..mimi nina familia yangu, na nyie ni familia tegemezi..japokuwa kwa namna fulanii tunategemeana, …ndio maana nilitaka niende nikaongee na hao watu.., waandishi wa hilo gazeti….’nikasema

‘Usije kufanya kosa hilo…’akasema sasa akitaka kuondoka, lakini hakuondoka, akanigeukia tena na kuuliza swali hili….

‘Je ni kweli mume wako ndiye aliyemuua Makabrasha…’baba akaniuliza

‘Hapana baba sio yeye…’nikasema

‘Silaha iliyotumika si yako, na uliweka kwenye kabati maalumu, ni nani aliyefungua kabati lako na kuitoa hiyo silaha..?’ akaniuliza

‘Baba kuna tetesi tu bado nazifanyia kazi, ila nimeshamfahamu , nitakuja kukuambia kwa wakati muafaka ..’nikasema

‘Ni kweli kuwa mume wako alifika huko kwa Makabrasha siku ya tukio, ..alikwenda kufanya nini..?’ akaniuliza

‘Nahisi ni kwa vile huyo marehemu alishakuwa ni wakili wake, kwahiyo alikwenda kuongea naye maswala yao..na ndio nimeanza kuupata ukweli huo leo, lakini bado naufanyia kazi, haujawa na uhakika wa kiushahidi…’nikasema

‘Mume wako si alikuwa mgonjwa..aliwezaje kufika huko..?’ akaniuliza

‘Kuna dalili, kuwa akiingiwa na hisia fulani anakuwa na nguvu za ajabu ugonjwa hutoweka, akafanya mambo, kihisia,..kwa vitendo..ni aina ya ugonjwa wa ajabu tu..’nikasema hapo atabasamu na kusema.

'Ugonjwa huo unawezesha yeye kuongea, kufanya ya ukweli, hata marehemu aweze kuelewana naye,..marehemu hakuwa magonjwa, ..ya kuwa walikutana kwenye njozi, au...usinifanye mimi mjinga eeh, hivi..inakuja akilini hiyo,..ok, sawa, tuliacha hilo kama lilivyo...lakini mimi simini...'akasema

'Kufanya hivyo alivyofanya si ile ya kindoto za usiku, ila hilo la mchana akauwa na hisia za kawaida, akili za kawaida, ila anapata nguvu ya ajabu, ni kama mashetani hivi, yanamuongoza, kama nilivyoelezwa hivyo, ila ni katika aina hiyo y akuchanganyikiwa,..ipo hivyo baba...'nikasema

‘Ok..ok...'hapo akacheka, halafu akaendelea kuuliza,...'Pale kwenye jengo, kuna vyombo vya kuashiria hatari, pindi mtu akiingia na silaha, pia yupo askari mkaguzi, ana ujuzi wa hali ya juu,...silaha ilipitishwaje, ujue huyo muuaji alikuwa nje..si ndio..na huko kote kuna hiyo mitambo ya ishara ya hatari, akasogea hadi chumba alichokuwa marehemu, na humo kwenye chumba kuna mitambo yake ya ziada, haikupiga kelele...umegundua nini hapo..?’ akaniuliza

‘Bado nalifanyia kazi…’nikasema

‘Pale kwenye jengo kuna mitambo ya kurekodi matukio, je ni kwanini siku hiyo haikuweza kufanya kazi, au je kuna mtu aliifuta…unamuelewa huyo mtu…?’ akaniuliza

‘Baba bado sijampata baba, mitambo ya kurekodi matukio, kama ilivyokuwa mitambo ya kutoa ishara ya hatari, imekuwa ni kitendawili baba, nahisi kuna jambo hapo…’nikasema

‘Uliweza kuongea na mtoto wa marehemu mkubwa,..kuna lolote kakuambia kuhusu ni nani aliyehusika na mauaji ya baba yake..?’ akaniuliza

‘Niliongea naye, lakini hajasema kuwa ni nani, wanadai kuwa ni maadui zake tu…’nikasema

‘Unahisi ni kwanini wanataka kuficha ukweli wa hayo mauaji ya baba yao, wakati ni watoto wake..?’ akaniuliza

‘Sijajua bado, bado nalifanyia kazi…’nikasema

‘Ni nani aliweza kuiba mkataba wako ule wa ofisini, huo wa nyumbani,..sawa labda ni mume wako,ndiye aliweza kuuchukua, kabla, je wa huko ofisini ni nani alifanya hivyo…?’ akaniuliza

‘Baba nitakuamba yote hayo bado nakusanya ushahidi..’nikasema

‘Je ukiupata huo mkataba utafanya kama mlivyokubaliana, jinsi mkataba unavyosema au utamsamehe mumeo wako..?’ akaniuliza

‘Baba kila kitu kitajieleza kwa wakati muafaka,…kwa hivi sasa siwezi kusema neno…’nikasema

‘Huyo ni mume wa watoto wako au sio…utasema nini kwa watoto wako iwapo utaamua kuachana na mume wako..kama mkataba unavyosema, au si ndio hivyo....nasema kama, sio kwamba nataka iwe hivyo…?’ akaniuliza

‘Baba siwezi kukujibu hilo swali lako kwa hivi sasa, muda ndio utasema….’nikasema

'Sasa ni muda, sio mkataba tena,..kwa vile unao, au sio...'akasema

'Sio hivyo baba...'nikasema

‘Na leo hii ulikutana  na watu gani, ..?’ akaniuliza na hapo nikashtuka..

‘Ni watu wa usalama..’nikasema

‘Je wameweza kufanikisha lengo lako..?’ akaniuliza

‘Kwa kiasi fulani ndio…’nikasema

‘Kwahiyo huyo shemeji yako kasema ukweli wote,..je kakubali kuwa kayafanya hayo, na je ni kweli mtoto wa rafiki yako, yawezekana kuwa yeye ndiye baba yake..?’ akaniuliza hapo maswali mengi kwa wakati mmoja, ni kama vile hataji nijibu ila kuna kitu anataka nikielewe,..na hapo nikajua kuwa baba anafahamu zaidi na y a ninavyofikiria mimi…

‘Baba naomba unipe muda, nitakujulisha yote hayo ikibidi…kwani,eeh, nahisi  kuna kitu umekigundua zaidi ya ninavyojua mimi, unaweza kunieleza, maana bado nipo kwenye michakato ya kukusanya ushahidi..?’ nikamuuliza

‘Ushahidi!! Ushahid wa nini, wakati una meno, hutaki kuyatumia, wakati…una kila kitu lakini bado unakumbatia uchafu…mwanangu hii ni dunia, sio wote wanaokuchekea wakakuonyesha meno, ni wazuri kwako, sio wote wanaosema 'i love you' wanamaanisha hivyo, wengine wanamaanisha kile ulicho nacho ambacho sio wewe…’akasema

‘Naelewa hilo baba..’nikasema

‘Nikuambie kitu, unaishi na nyoka, tena mwenye sumu, lakini wewe hujui, ukiwa umelala wenzako wanakuwangia…na sia maana ya uchawi, mimi siamini uchawi, ila nakuambia hivi,..tumia akili yako vyema..'akasema

'Baba usiwe na shaka na mimi...'nikasema

'Ni lazima niwe na shaka na nyie....kwa hayo yanayotokea, unasikia,,..ninachokushauri kwa sasa, uwe makini na hilo..sitaki kukushauri jambo baya, kama nina uhakika kuwa ni baya, na siwezi kukaa kimia, nikijua unakwenda kuteketea, ina maana gani kuwa mimi ni mzazi wako,...ila ..vyovyote iwavyo,…usiwaamini watu wote tena…na usikubali kila jambo bila kushauriana na wakili wako, na wakili wako ni mtu, unielewe hapo,ila muhimu…taarifa yoyote itakayokuja kwako uwe makini nayo, unanisikia..’akasema

‘Sawa baba nimekuelewa baba…’nikasema

‘Na rafiki yako anarudi lini…?’ akaniuliza

‘Hajaniambia bado..’nikasema hapo akashika kichwa kama kuna kitu kinamkera, halafu akaanza kutembea kuondoka, lakini kabla hajatoka mlango akawa anaongea huku anatembea kuondoka.

‘Nilikuambia siku ile..mume wako anahusika na kifo cha Makabrasha ukanibishia, sawa…sio mbaya,…nilikuambia mume wako anatumika  na wanasiasa ukaniona naleta mambo ya kisiasa nyumbani kwako, nalo hilo sio baya...’ akatulia kama anawaza jambo lakini kila nikitaka kuongea ananikatiz kwa kuongea

‘Na...nilikuamba, marafiki zako ndio maadui zako, wachuje ili ujue ni nani rafiki wa kweli,.. ukasema nini …nakufitinisha wewe na marafiki zako…sasa nakuambia hivi…wanaokuja kwako kwa lugha za wema, hao hao ndio chambo cha kupooza jitahada zako, usiwaamini, unasikia, sasa na hilo puuza, na endelea kulala uone itakavyokuwa, mimi sijamlea binti yangu alale kipindi cha vita… kwaheri..…’huyo akandoka zake.

Kiukweli baba alipoondoka sikuweza kulala tena, akili yangu ilianza kuwaza mengi, nikaona nispoteze muda,..muda ni mali, ..nikavaa nguo zangu maalumu, nikahakikisha kila kitu kipo sawa, na haraka nikatoka, nje…

‘Vita imeanza…’nilisema hivyo tu, na kwenye simu yangu ukalia mlio wa ujumbe, nikajua ni taarifa kutoka kwa watu wangu sikutaka kuusoma, kwanza ni kufanya nilichotaka kukifanya..kuhakiki ushahidi wa `shemeji..'


WAZO LA LEO: Dunia ilivyo sio wote watakaofurahia jitihada na maendeleo yako, wapo watakaokusifia na wengine watakukatisha tamaa na wengine watakubeza, na hata hao watakaokuja na kukusifia kwa jitahada zako na maendeleo yako, sio kweli wanamaanisha hilo wanalolisema, kutoka kwenye nafsi zao. Hiyo ndio kiwalimwengu kilivyo. Muhimu pambana na jitahada zako, huku ukimtegemea mola wako kwenye kila jambo la heri, kwani yeye ndiye anayefahamu ya siri na ya dhahiri…muhimi simamia kwenye njia ya kweli na ya haki..uatafanikiwa tu..japo mwanzo ni mgumu. 
Ni mimi: emu-three

No comments :