Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Monday, January 8, 2018

MKUKI KWA NGURUWE-53


  Labda nielezee vizuri,... jinsi chumba chetu maalumu, tulichokiita ,maktaba kilivyokuwa,…
Kwa vile kila mmoja alikuwa na kampuni yake, na mara nyingi kulikuwa na kazi nyingine ilibidi tuzifanyie nyumbani,kila mtu kwa wakati wake, au siku nyingine tunakutana na kuwemo humo, …

Kutokana na hali hiyo, tukapanga kuwa maktaba hiyo ibororeshwe zaidi iwe kama ofisi ndogo ya nyumbani..na kwa vile kila mmoja ana ofisi yake, tukakubaliana kugawanywe sehemu mbili, lakini sio kuwa kuweka uzio kabisa, ni kwa mtindo wa makabati na meza, kutenga huku na kule,..kiukweli tulipatengeneza vizuri sana.


Hakuna aliyekuwa akihangaika na sehemu ya mwenzake, labda uamue tu kumtuma mwenzako, kuwa nisaidie kunichukulia kitu fulani kwenye sehemu ya vitu vyangu..sasa kila mmoja akawa anapaboresha sehemu yake kwa jinsi aonavyo yeye.

Kwangu nikaongeza kabati moja imara, ukiliona utasema ni meza au kabato la vipodozi na vitu vya kike lakini kwa ndani, nikaongeza sehemu maalumu ya kuweka vitu vyangu vya siri,..ambavyo sitaki mtu aviguse..hata mume wangu sehemu hiyo alikuwa haijui..Anaweza akawa anaifahamu, maana sikuwa namficha sana, lakini hakuwa na habari kabisa na vitu vya kabati hilo.

‘Hilo kabati lako la kike kike, sitaki hata kulisogelea,…’kuna siku aliwahi kuniambia hivyo

Sasa humo ndio niliweka nakala ya mkataba wangu, kwangu mkataba huo ulikua ni moja ya vitu muhimu sana ..nikimaliza kusoma kama kuna kitu nataka kukifuatilia, naurudisha hapo…

Kulikuwa na kabati la vitu vya kuchangiana, lakini pia ni maalumu kwa kumbukumbu zetu za nyumbani, hapo kila mtu angeliweza kuweka au kuchukua vitu,lakini mara nyingi,nimekuwa nikilitumia mimi mwenyewe tu na mume wngu hana habari nalo.

Lenyewe lina sehemu ya nje na ya ndani, unaweza ukachukua vitu vya nje, bila kujua kuwa kuna sehemu nyingine ya ndani,..sasa sehemu hiyo ya ndani, ndio kuna vikabati maalumu,..humo kuna nyaraka za nyumbani za kuchangia…na kuna sehemu maalumu, ndio kuna sehemu tunaifadhia silaha….

Kupotea kwa mkataba wangu,  kwenye kabati langu, na mimi mwenyewe ndiye mwenye ufungua, kuliniweka kwenye njia panda, sikutaka hata siku moja kumshuku mume wangu kwa baya lolote lile, yeye ni mimi, na mimi ni yeye, nilimuamini sana kutoka moyoni mwangu, ....sasa mkataba wangu umepotea, na mtu ambaye anayeweza kuuchukua ni mume wangu, swali lilikuja kwa kutumia ufungua gani, na mimi ufungua za kabati langu ninao mimi mwenyewe, na hakuna nakala ya akiba ambayo niliwahi kuiweka sehemu, na ufunguo zangu mara nyingi natembea nazo.

Leo hii ninafika nyumbani ninamkuta mume wangu akiwa kwenye kabati langu,..na kabati limefunguliwa, na ufungua zipo zimening’inia kwenye sehemu yake..na kulihakikisha hilo nilisogea taratibu hadi pale alipochuchumaa

Kwa muda huo hakuwa na habari kabisa kuwa nimeingia, na alionekana kuna kitu muhimu anakitafuta hasa pale aliposema

‘Mbo-mbo-na haipo ooh….’

Na kilichoniuzi zaidi ni kuona nyaraka muhimu za ofisi nyaraka ambazo kwangu ni muhimu sana, alikuwa kazisambaza chini, bila mpangilio maalumu, mimi napenda vitu vyangu viwe kwenye mpangilio maalmu,..hapo subira, ilinishinda ndio nikasema...

‘Unafanya nini kwenye kabati langu...’nikamshitua...

Tuendelee na kisa chetu..............

Mume wangu aliposikia sauti yangu, alishituka, hadi ile karatasi aliyokuwa kaishikilia mkononi kwa muda huo, ili ilimdondoka,… kwanza alitulia, kama anatafakari jambo,  na baadaye akajifanya kama hajali..na kwa haraka, akaikota ile karatasi, halafu . akageuza kichwa kidogo na kuniangalia usoni, halafu akasema;

‘Afadhali mke wangu umekuja, maana hapa akili yote imevurugika,..kauli zako za hivi karibuni zimenifanya nichanganyikiwe kabisa…’akasema na sasa akawa anaendeela kama kutafuta kitu.

‘Unajua, ..sijui ndio huku kuumwa,..hii ajali imenifanya niwe mtu wa ajabu kabisa,..uliposema kuhusu mkataba mwingine wa zamani,…nimekuwa nikihangaika kujiuliza ni upi huo…lakini kuna kitu,,…unasikia..’ sasa akaacha kutafuta na kukaa vyema sakafuni.

‘Nakumbuka hata wewe ulikuwa nayo, nakala yako au sio..na mimi ya kwangu, hii niliyo nayo mimi, ni ambayo niliitoa nakala , kutoka kwenye ila nakala ya mwanzo, nahisi ndio hiyo unayoiita nakala ya mkataba wa zamani, kweli si kweli..’akatulia

‘Sasa akili ikanijia,…kama wewe ulikuwa na nakala yako, kwanini usema kuwa imebadilishwa,…sasa nikawa natafuta ukweli..tatizo ni hili nakala yangu, ya zamani…eeh, siioni, nia nione kama kweli ipo tofauti na hii ambayo nilikwenda kuitoa nakala..unielewe hapo, nakala ni ile ile,, ila nilikwenda kuitoa nakala nyingine kwa ajili ya wakili..ni ile ile..

‘Cha ajabu, kwenye kabati langu haipo…ni ile ya zamani, unanielewa hapo, ambayo niliichukua na kuitoa nakala,…hapo kabisa..ipo hii ambayo ni nakala kutoka kwenye nakala hiyo…hii ya sasa unaiona imefifia kidogo,…kama imefutika futika vile lakin ikila kitu ni kile kile...sasa nikawa nahangaika weeeh, mwishowe nikasema, aah..’akasema na mimi nikamkatisha kwa kuuliza

‘Kwahiyo unatafuta nini hapa kwenye kabati langu, ndio mkataba au..?’ nikauliza

‘Kiukweli, nikuombe samahani kwa hilo..lakini sio kosa,..si ndio…niambie mke wangu hapo nimekosea nini…sawa, kiutu , ilitakiwa nifanye hivyo,..lakini nikuulize kwani..kuna kosa mtu akitafuta kitu kwenye sehemu za mke wake..mhh, kosa labda ni kwa vile sikukufahamisha mapema kwa vile…kuna vitu vyako vya kiofisi, lakini ofisi zi zetu wote au…ama kwa hilo, basi nikuombe samaha mke wangu…’akasema.

Aliinua macho na kunitizama..nilishikwa na kitu kama mshangao…hayo macho…sio yale ya mume wang ninayemfahamu…lakini sikujali hilo

‘Mume wangu, toka lini tukawa tunachangiana makabati, kila mmoja ana kabati lake na kila mmoja ana vitu vyake na humu naweka vitu vyagu vya kikazi, angalia jinsi gani ulivyoviweka ovyo vitu vyangu sakafuni, …kwanini jamani…’nikawa naviangalia vile vitu, sakafuni.

Hapo akatikisa kichwa, ni kama vile haamini, na akaehema kwa nguvu, halafu akaendelea na shughuli yake kama hajali, na mimi nikasema kwa hasira.

‘Mume wangu unafanya nini…unajua utaratibu wangu wa kikazi ulivyo,..kwa jinsi ulivyovuruga hivi…hata ule utaratibu wangu wa kumbukumbu za kwenye kabrsaha umeuharibu, itachukua muda tena kuutengeza vizuri,...huoni kuwa unataka kuniweka mimi mahala pabaya..vikiharibika hivi au vikipotea..unaniweka mimi kubaya....’nikasema.

‘Usijali kabisa mke wangu hakitaharibika kitu hapa, niamini mimi, mimi ni mume wako, nitahakikisha hakiharbiki kitu hapa, hata hivyo…kama nilivyokuambia, siku hizi akili yangu imekuwa ya ajabu kabisa, inanasa kila kitu ninachokifanya, yaani siku hizi mke wangu naona nipo mtu wa ajabu sana, nina akili mbili tofauti, hii ya ajabu, inakuja na kuondoka, ..wewe mwenyewe utaona, nitakirudisha kila kitu kwa mahali pake, bila hata kukosea wewe mwenyewe utaona...’akasema.

‘Kwahiyo umesema ulikuwa unatafuta nini humu,… mkataba wako kwenye kabati langu, kwanza ni mkataba upi huo, unajifanya nini hapa..?’ nikamuuliza kwa hasira.

‘Nakala ya zamani, ya mkataba...mwenyewe ulisema unahitaji ile nakala yangu ya zamani, si ndio hivyo…umesema bila hiyo huwezi kukaa kiti kimoja na mimi na wakili au sio..’akasema

‘Kwahiyo ipo kwenye kabati langu, uliiweka wewe..?’ nikamuuliza

‘Ni hivi…  pale nilipokuwa nimeiweka nakala yangu, kule  kwenye kabati langu, siioni, siku hizi akili yangu inanituma mambo mengi, na nikiweka kitu sisahau pale nilipokiweka, sasa ni ajabu kabisa kuwa  siuoni, imekuwaje tena, hapana lazima kuna tatizo...’akatulia sasa akianza kupanga karatasi zangu zilizokuwa sakafuni.

‘Mume wangu…tafadhali…’nikasema kabla sijamaliza akasema

‘’Najua utanifikiria vibaya, lakini sivyo hivyo…mimi nilijua labda wewe umeamua kuichukua il nakala yangu ya zamani,…na kwa bahati mbaya ukaja kuiweka hapa kwako, kiusalama zaidi, hapa kwako kuna usalama sana au sio…’ akasema, huku akiendelea kupekua kwenye mafaili yangu.

‘Sikiliza mume wangu, ..sijapendezewa kabisa na hiki kitendo ulichokifanya, ..na sio tabia yako, imekuwaje siku hizi, mume wangu, ...kuna nini unanitafuta wewe mume, kuna tatizo gani limekutokea ili niweze kukusaidia..kwanini unahangaika hivi mpaka unaniletea matatizo makubwa kwenye maisha yangu..?’ nikamuuliza huku nikiendelea kumwangalia.

‘Hujapendezewa na mimi, kwanini…..hapana mke wangu usinifikirie vibaya kabisa,…na mke wangu, nikuulize, wewe si mke wangu, nimekuoa kwa taratibu zote za ndoa, au sio…je nikifanya hivi kuna kosa gani…?’ akauliza

‘Kuja kupekua kwenye kabati langu, tena kuna mambo ya kofisi, je mimi nikifike kwenye kabati lako nikafany ahivyo utafurahia,…kila siku unazidi  kunichefua, kuna kitu gani kinakusumbua hivyo…’nikasema na kumuuliza

‘Hakuna kitu kinanisumbua, ila kwanza nijibu swali langu halafu nitakuambia tatizo ni nini….swali langu ni hivi…, wewe si mke wangu..?’ akauliza na mimi nilikaa kimia, akauliza tena

‘Mke wangu nauliza tena, samahani nijibu tu, wewe si mke wangu…?’ akauliza na mimi nikaona isiwe shida nikajibu

‘Ndio..’nikasema hivyo tu.

‘Sasa kama ni hivyo, nina makosa gani kumkagua mke wangu…’akasema

‘Mume wangu acha maneno yako ya mitaani, kunikagua kwa vipi..?’ nikauliza

‘Kama mimi ni mume wako, kila chako ni change au sio…na pia changu ni chako au sio..tuseme kiukweli kutoka haki za kindoa, achilia mbali mambo ya mikataba, achilia mbali sheria za kidunia,...na hata ukirudi kwenye mkataba kama umeusome vyema inasema hivyo hivyo,… na wewe mwenyewe ni mmoja wa waanzilishi wa huo mkataba wetu na sahihi yako ipo, usikate ukweli mke wangu, ach ubinafsi…’akasema

‘Mimi siutambui huo mkataba wenu wa kugushi..’nikasema kwa hasira,…mume wangu kwanza akatabsamu, halafu taratibu akanigeukia, na kuniangalia…

Kama kuna mtu kampanga mume wangu, basi huyu kafanya kazi kubwa sana, anavyofanya sio kuigiza, utafikiri ni kweli kabisa, yaani utafirikia naongea na mto tofuati sio kama yule mume ninayemfahamu ukimuambia kitu hewala, hewala..tu.

‘Hapana…sio wa kugushi mke wangu, kwanini unasema hivyo,…ni ule ule tulioutengeza pamoja…,tuwe wakweli hata mkataba wa halali wa ndoa, unasemaje, mimi ni mume wako, na wewe ni mke wangu, kwanini sasa isiwe halali kwangu kufanya ya halali…hili ni halali kwangu au sio…nakagua vitu vya mke wangu, ambaye ni mke wangu, au sio,…?’ akauliza.

‘Usipoteze lengo…tafadhali…’nikasema

***************

‘Mke wangu nikuulize tu, kwanini huniamini,..eeh, na …na ..kimkataba…, mimi kama mume wako nina haki ya kuangalia chochote kwenye mali zetu, ...au nimekosea..kasome mkataba vyema…?’ akaniuliza na safari hii alianza kurudisha vitu kwenye kabati, nikawa namwangalia tu.

Hutaamini baada ya dakika moja, alikuwa karudisha kila kitu kama kilivyokuwa awali, halafu akaniangalia, kama vile anataka mimi nikague kama kila kitu kipo sawa, baadae akainama na kufunga, ufunguo ulikuwa umening’inia pale pale…alipogakikisha kafunga, akauchomoa ufungu…, nikagundua kuwa ufunguo ule ni kuchongesha, aaaah, kumbe, ...

‘Huo ufungua uliupatia wapi?’ nikamuuliza, sasa nikijaribu kuukagua huo ufungua, na yeye kwa haraka akauweka mfukoni mwake.

‘Mbona ninao siku nyingi mke wangu...niliamua kuwa na nakala ya ufungua zote, maana sisi sote ni binadamu tu, tunaweza kupoteza ufunguo, kwahiyo kuna haja ya kila mmoja awe na nakala za mwenzake, ni vibaya kufanya hivyo, au…’akasema kama ananiuliza

‘Hilo ulilifanya lini bila ya mimi kufahamu..?’ nikamuuliza

‘Hilo la kuchongesha ufunguo…?!! Mmh, mke wangu umesahau jambo kuwa mimi ni mume wako, natakiwa kuwa mbele kwa ajili ya familia yetu,..ni lazima niwe makini kwa kila kitu, na usalama wetu, na mali zetu pia, kwahiyo hilo sio la kuniuliza, nilifanya muda tu,..na hivi sasa nina uhakika kila kitu kipo salama au kufanya hivyo,..ni-ni..nimekosea mke wangu…’akasema

 Alisema hivyo sasa akiwa kamaliza kupanga kila kitu, akawa kama akumbuka kitu, kwa haraka sana  akageuza kichwa kule kwenye kabati la pamoja, lipo wazi…kwa haraka ya ajabu, akaliendea, akahakiki kama kila kitu kipo sawa, huyoo, akalifunga.

‘Umeona eeh…kila kitu kipo sawa..kama kilivyokuwa..umeonaeeh,…’akapitisha macho huku na kule, baada y akurizika akaniangalia mimi.

‘Twende…’akasema

‘Mume wangu usijifanye mjanja sana, unajua mimi nafahamu kila kitu, hizo zote ni mbinu zenu, kwanza mumefanya njama za kubadili mkataba, ili kutengeneza mkataba utakaokidhi matakwa yako, na mkafanya mbinu ya kuhakikisha nakala zote za mkataba huo wa kugushi zipo kile idara, lakini mumesahau kitu kimoja…’nikasema

‘Kitu gani mke wangu…’hapo akasema kama kashtuka, halafu akajifanya yupo sawa.

‘Nina uhakika, mliamua kuchongesha hizo ufunguo, ili wewe uje kuiba mkataba wangu, ili mkabadili na kuhakikisha nakala za awali, mumeziharibu, na pia ukaja ukachukua bastola yangu, nakumbuka wewe ulikuwa hutaki hata kuishika hiyo bastola,....imekuwaje sasa…?’ nikamuuliza

‘Bastola!!!…mke wangu, toka lini nikagusa silaha yako, mimi naogopa sana siliha hiyo, aah, hapo umezidi, bastola, mimi na bastola wapi na wapi…’akasema

‘Na kwa taarifa yako, silaha iliyotumika kwenye hayo mauaji ya wakili wako,..ni hiyo bastola, na wewe ndiye mwingine mwenye nakala ya kabati hilo, mimi wamegundua kuwa sihusiki, sasa wao wanamtafuta huyo mtu mwingine mwenye nakala ya hilo kabati, kumbe ni wewe,  ole wako polisi wakifahamu hilo...’nikasema

‘Unasema nini mke wangu, sijakuelewa hapo bado, kwanini mimi nilichongesha ili nije kuiba, hahaha, hapo mke wangu unakosea sana,.... kwa nini niibe, kuna mtu anaiba kitu chake, mbona mke wangu unaniangusha,...usisahau kuwa mimi ni mume wako, sio mtu mwingine yoyote,...’akasema,

Moyoni, akilini, nilikwua nimejawa na hasira, lakini nilikumbuka jinsi alivyokuwa akinishauri docta, kuwa nisije kulogwa na kusema mume wangu kapona, kwani hapo alipo ikitokea tena,… mshtuko,… akapatwa na kiharusi (stroke) basi, sitaweza kumponya tena!

Hapo mimi.., nikabakia kukunja uso, na aliponiangalia usoni  jinsi nilivyobadilika, aligeuka kwa haraka akatoka nje ya hiyo makitaba…alikuwa anatembea kwa mwendo wa haraka …kama haumwi, kikawaida yeye anatembea kwa shida, kwa kuchechemea..!

**********

Nilichukua mkoba wangu na kuutafuta ufunguo wangu, ulikuwepo kwenye moja ya fungua zangu ninazotembea nazo, nikafungua lile kabati na kila kitu kilikuwa kwenye nafasi yake, na ule mkataba wa kugushi upo hapo hapo..

Sikutaka hata kuukagua kama ni ule ule wa kugushi au ni ule wa awali nikafunga lile kabati vyema, na akilini mwangu nikapanga nikitoka hapo nabadili ufunguo zote na naweka taratibu mpya za kufungua hilo kabati kwa namba za siri.

Nilitoka mle makitaba na kuingia kwenye chumba chetu cha kulala, kuna mlango wa kuingilia huko,..nilitarajia nitamkuta mume wangu kalala huko,..lakini hakuwepo, mimi kwa haraka, nikabadili nguo, na kuelekea sebuleni, chumba cha maongezi.

Chumba cha maongezi, nilimkuta mume wangu akiwa kakaa huku kashikilia mkataba, ..mwanzoni nilifikiria ni ule mkataba wa zamani, lakini ulikuwa ule ule waliougushi wao, niliugundua kwa jinsi ulivyo juu, ..jalada lake limefifia kidogo.

Nilimsogelea na kumwangalia, alikuwa katulia, hana wasiwasi, na alionekana alikuwa akisoma sehemu fulani kwenye huo mkataba, kwa makini, na alipohisi nimesimama karibu yake, akauweka pembeni huo mkataba, na kuinua uso kuniangalia, akatabasamu na kabla hajasema neno, nikasema;

‘Haya hebu niambie ukweli, ni kitu gani kinachoendelea hapa kwenye nyumba yetu?’ nikamuuliza..yeye akasogea kidogo, kama kunipa nafasi nikae karibu yake, sikufanya hivyo.

‘Mke wangu hebu kwanza kaa, njoo ukae karibu yangu,…mimi ni mume wako wala usiniogope, kuwa labda kwa vile naumwa, ninaweza kukudhuru, hapana, hilo halitaweza kutokea abadani, ninakupenda sana mke wangu…’akasema

Na mimi nikakaa, lakini sio karibu yake kihivyo, akasema

‘Mhh, mke wangu, kwani kuna nini kibaya umeiona kimetokea ambacho kinakufanya useme hivyo,…, mimi sioni kama kuna kitu kibaya kimetokea, hiyo ajali isiwe ni sababu ya kuharibu maisha yetu, ajali ni ajali tu, na ajali haina kinga, na mengine yanatokea ni…maisha tu…’akasema na mimi hapo nikabakia kimia kwanza.

‘Mke wangu haya yanaweza kumtokea yoyote, hasa sisi tunaotumia vifaa vya moto..kilichotokea kwangu sio uzembe, sio…au kama watu wanavyosema,..ilitokea tu..na hali ninayokwenda nayo itakwisha tu, nisaidie nipone kabisa…’akasema

Hapo nilitaka kumuambia kumbe kweli hajapona, maana wakati mwingine ukimuuliza anasema kapona lakini hapo anajifanya hajapona kabisa.

‘Ni haki yako kunisaidia..nikikosea,…nikifanya kinyuma na kawaida, ujue ni madhara hayo ya ajali..na hapa nilipo, sio kwamba nakumbuka kila kitu kihivyo, inatokea …nika-ka-sahau,..yawezekana, wakati mwingine nahis kama nipo kwenye njozi, lakini kiukweli nimepona, au sio…’akasema, na mimi sikumjibu kitu.

‘Au mke wangu niambie …, labda mimi sijui, maana muda mrefu nimekuwa hopsitalini, je kuna tatizo lolote…nipo tofauti, nimechanganyikiwa labda..niambie ukweli au…? ‘akauliza

‘Mume wangu, leo ni siku ya mwisho, sitakaa tuongee hivi tena, labda kuwe na kuelawana, na kuelewana kwetu, nimeshakuambia,kutakuja pale tu, wewe utakapokubali kuniambia ukweli, wote na pili ule mkataba wa asili uweppo mezani…’nikasema

‘Eheee,…wewe unautaka ukweli, lakini,…ukweli upi.. hamna shida, mimi nitakuambia kila kitu, ila sasa nikuulize unataka mimi nikuambia ukweli gani labda, nisaidie hapo mke wangu…’akasema

‘Leo ni siku ambayo…kama hutaniambia ukweli, sijui…maana tukimaliza hapa ni utekelezaji,…hata kama utauficha huo mkataba,…na vinginevyo,..tutafikishana mahakamani, au….’hapo nikatulia, alipogeuka kuniangalia

‘Mahakamani, kuna nini cha kwenda huko, hapana mahakamani hapafai, yetu tutayamaliza hapa hapa nyumbani au sio....?’ akauliza

‘Vitendo vyako vimenichosha, kwanza umekiuka makubaliano yetu, umevunja mkataba wa ndoa, na hata sikuelewi,…. na hutaki kuniambia ukweli,  ...ni kwanini lakini, kwanini unanitesa hivyo, una lengo gani na mimi…?’ nikamuuliza na yeye akanitupia jicho, halafu akafungua ule mkataba wake, akawa kama anasoma jambo, mimi sikutaka hata kumsogelea na kuangalia anasoma kitu gani.

‘Kwanini unasema ….eeeh,maana tukimaliza hapa na utekelezaji, ama twende mahakamani,…hapana usiseme hivyo, tupo wote, na kila siku tutaongea tu huo ndio utaratibu wa mke na mume au sio..hata bila mikataba, hilo la kuongea ni jambo la kawaida kwa mke na mume, sasa niambie nimekufanya nini kibaya, mpaka useme hivyo…?’ akasema na kuuliza, na aliponiona nipo kimiya akasema;

‘Kwani mke wangu situlishaelewana, na ndio maana nilikuwa nataka niutafute ile nakala yangu ya zamani,…ili tukae tulianganishe kama kuna maneno yameongezeka au kupungua,…sijaiona kabisa..na ya kwako ipo pale pale au sio…kwanini tuandikie mate,..nenda kaulete, ..tulinganishe tuone kama kuna utofauti wowote, utakuta kitu ni kile kile neno kwa neno....’akasema.

‘Mume wangu…’nikataka kusema, yeye akanisogelea akiwa kafungua mkataba wake na kusema…

‘Hebu angalia, mwenyewe, ....maneno ni yale yale..hebu soma uone…’akasema huku akinipa ule mkataba, na mimi sikuugusa na wala sikuinua mkono wangu, nikawa namwangalai usoni nikasema.

‘Mume wangu kwanini upo hivyo, upo sawa kweli wewe, ni kwanini hutaki ku-usema ukweli, ni kwanini mlichukua hatua ya kuubadili huo mkataba bila makaubaliano na mimi…niambie tu ukweli, ili twende sawa….?’ nikamuuliza

‘Mke wangu, mimi nakumbuka , hilo swali nilishakujibu, hakuna aliyebadili huo mkataba,mbona huniamini mke wangu, mimi nipo sawa kabisa, kifahamu, au..?, tuache kuhusu mimi, eeh,...hebu niambie ni wapi huo mkataba umebadilishwa, na kama ulibadilishwa kwanini sahihi yako iendelee kuwepo hapo, huoni unakosea kabisa kisheria….eeh, niambie sahihi zote za wahusika sizipo, angalia hapa, hii sio sahihi yako…hata ukienda mahakamani watahakiki hilo…’akasema.

‘Kwahiyo kumbe bado upo na msimamo wako ule ule,....hutaki kusema ukweli, hutaki kuniambia ni nini kinachoendelea, na ni ni kusudio lako,au kusudio lenu, na washirika wako....eeh,  na sasa watoto wanadai wanachohisi ni haki yao , si ndio unataka hivyo…’nikasema huku nimemkazia macho, yeye akaniangalia mara moja halafu akatabsamu, na kusema;

‘Haki ni haki tu…tusiibeze haki, au sio, na…hayo niachie mimi, na nikuulize tena mke wangu, labda kuna kitu wewe unakihis hakipo sawa, ni kitu gani, niambie ukweli, kama ni mkataba upo vile vile..na kwanini mtu afanye ufoji huo, agushi, kwanini,...hebu niambie wewe…?’ akaniuliza

Mimi hapo nikakaa kimia.

‘Mke wangu , tusaidiane, huenda mimi nipo dunia nyingine, huenda kuna kitu umekigundua kwangu na unaogopa kuniambia, au nimebadilika, baada ya kuumwa, nimekuwa tofauti, ...’akasema

Hapo nikasimama,..nilitaka kuondoka kabisa kwa hasira…, lakini nikajiuliza  nitakuwa nimefanya nini sasa, leo ni lazima nimbane mpaka asema ukweli wote hawezi kujifanya mjanja hivyo hapo ndio..nikageuka kumuangalia,

Yeye akawa anausoma ule mkataba, hajali kabisa, hana wasiwasi….

Nilimuangalia mume wangu, kiukweli nilimuona kama sio Yule mume ninayemfahamu kabisa,…maana mume niliyemzoea alikuwa nikimuuliza jambo, tunakubaliana, tunaongea yanakwisha, lakini huyu wa sasa, wala hanijali, na pili amekuwa kama yupo mbali, kama alivyosema, ni kama yupo dunia nyingine tofauti ya ukweli….

‘Mume wangu , pengine, hujanifahamu , pengine unafikiria kuwa nakutania, pengine, nahitajika kuchukua hatua nyingine ndio utanielewa,....’nikasema na kutulia kidogo.

‘Nakusikiliza endelea…’akasema hivyo akiendelea kuusoma huo mkataba.

‘Hivi unajidanganya nini, hivi wewe hufahamu kuwa hilo unalolifanya linaweza likakufunga, na hata kukuvunjia ndoa yako, unayoringia nayo wakati wewe mwenyewe umeshaivunja…ukweli ndio huo, umeshaivunja ndoa yako,..hebu niambie imebakia nini…sasa...’nikamwambia na yeye hapo akashituka, na kuinua uso kuniangalia...

‘Unasema nini..kuvunja ndoa yetu, hapana mke wangu, hilo halipo, na hali-hali-tatokea abadani,  labda mimi niwe nimekufa....kwanza kwanini unasema hivyo?’ akaniuliza na safari hii akawa ananiangalia moja kwa moja usoni,akionyesha wasiwasi. Kikweli kuna kitu kwenye macho yake nakiona sio cha kawaida….lhata hivyo, hali ya kujali haikuwepo tena.

'Kutokana na makubaliano yetu ya awali, hata kama mumeugushi huo mkataba halali, na kupandikiza huo wa kwenu, na kuweka mambo yenu ya kujihami…lakini ukumbuke, kugushi ni dhambi, kugushi nyaraka za kiheria ni kosa kubwa sana…sasa jiulize unataka kufanya hivyo kwa ajili ya nani…’nikasema

‘Hapo jiulize wewe mwenyewe…’akasema kwa kujiamini kabisa

‘Sawa nikuambie kitu.., hata kama unajifanya mjanja sana,lakini ukumbuke kuwa makubaliano yetu ya awali yapo pale pale, na moja ya makubaliano yetu ni kuwa mmoja akivunja miiko ya ndoa..unaifahamu hiyo miiko, ile mikubwa…’nikasema

‘Kama upi huo…?’ akauliza

‘Kuzini…kutembea nje ya ndoa…’nikasema

‘Nini, …wewe mke wangu ni nani anaweza kufanya dhambi hiyo, hapana…mimi nakubali hilo ni kosa, ..na kwenye mkataba wetu inasemaje..hebu kidogo…’akasma na sasa akifungua mkataba wake, na akawa kama ansoma

‘Yah, hapa kupo wazi…ni kosa, ila sasa unajua kiubinadamu, eeh..si semi hivyo kwa vile, labda..hapana mimi sijafanya, ikitokea wewe ukafanya hivyo, kwanza kuwepo na ushahidi…wa bayana, lakini pia…sisi ni wanandoa, tumzee, tuna watoto…mmoja akaghafilika, kutokana na sababu…maana huwezi kufanya dhambi kama hiyo bila sababu…’akasema

‘Sababu gani,…hakuna sababu hapo, kuzini ni kuzini tu…’nikasema kwa hasira.

‘Je kama imetokana na wewe..’akasema

‘Kwa vipi..?’ nikauliza

‘Tuache hayo, ila hapa kwenye mkataba inasema hivi, kama …itatokea hivyo, kwasababu za kujitetea, kuna sababu japo kidogo, ya kujitetea, inayoingia akilini, japokuwa..ushahidi upo, na mmoja akaomba msamaha, ukakubalika, basi,..ni kusameheana ya kale yaishe watu wagenge yajayo,…hiki ni kipengere cha nyongeza..’akasema

‘Hivi wewe mume wangu kweli hilo lilikuwepo…?’ nikamuuliza.

‘Si ndio nimesoma hapa…hebu soma wewe mwenyewe…lakini pia kuna vipengele vingine hakuna haja ya kivisoma,…kama vile mume wakiona kuna haja, ya kufanya jambo lenye tija kwa familia,..yeye kama kiongozi wa familia anaweza…ni vipengele vye kujitetea,..vinasaidia kisheria,..lakini muhimu ni kusameheana …’akasema

‘Kwahiyo uliongeza hivyo, ulipobaini kuwa umezini….?’ Nikamuuliza

‘Nani kazini,…mimi,…mke wangu unanifahamu nilivyo, mimi….hapana sijaweza kufanya hivyo, kwanza ni nini kuzini….mmh…hivi kuna kipengele hapa…’akawa anafunua kutafuta.

‘Hapana achana na huo mkataba wa kugushi, nijibu swali langu,…’nikasema kwa ukali,

‘Kabla sijakujibu swali, twende pole pole, kwani huo mkataba unaojua wewe ulisemaje…?’ akauliza

‘Unajifanya hujui..ni hivyo…kama umezini, ina maana umetembea nje ya ndoa,… kukawa na ushahidi wa kutosha, basi ndoa haipo..na huna haki tena kwenye mali zilizochumwa kwenye ndoa…’nikasema

‘Wauuuh…hiyo mpya kwangu…’akasema

‘Na kwenye kile kikao, wewe mwenyewe ulilisitiza sana hilo kwa kujiamini,..na ukasema ushahidi ni lazima uwepo, nikakuuliza ushahidi gani na watu wanafanya kwa siri, ulisema wewe mwenyewe, mtu kama huyo ataumbuka, anaweza akapata mtoto , huo ni ushaidi tosha,..ikipimwa ikahakikiwa kwa DNA, basi huo ni ushahidi wa kisheria, unabisha…’nikasema

‘Kikao gani hicho..?’ akauliza akionyesha mshangao

‘Utabisha lakini mbele ya sheria, utanaswa tu…na kwa vile hutaki kukiri kosa, ukasema ukweli, basi mimi kuanzia leo, najiandaa kwenda mahakamani…’nikasema

‘Mke wangu unakwenda mahakamani kwa kosa gani, mimi nimefanya kosa gani…?’ akaniuliza

‘La kuvunja mkataba wa ndoa, na kugushi mkataba halali wa ndoa…’nikasema

‘Nimevunja mkataba wa ndoa…!! ?’ akauliza kwa mshangao

‘Ndio umezini…’nikasema

‘Kuzini….’akasema hivyo, sasa akawa anatoa macho kama kuogopa

‘Mimi,…hapana, sijawahi kufanya hivyo, hata kama ulitoa kibali hicho, lakini mimi sijafanya…’akasema hivyo akiongea kwa haraka haraka kiasi kwamba sikumsikia vyema.

Akatulia kama anasubiria mimi niongee, kiukweli, ukimuangalia mume alivyo, ni kama mtu aliyechanganyikiwa, hajui kabisa anachokisema, lakini hakuweza kunishawishi kwa hali hiyo, kangu mimi , nilimuona kama anaigiza tu.

‘Ndio wewe umezini, usijitete hapa, kubali tuyamalize, hapa hapa…maana tukifika huko mbele mimi ninao ushahidi…’nikasema na nilitaka aulize ushahidi gani lakini hakuuliza hivyo, yeye akasema

‘Mke wangu unasema nini,....sijawahi kufanya hivyo,.....ni nani kakuambia nimezini, ....na na...mbona sikuelewi..nimezini na nani , umedanganywa mke wangu, temea mate chini, sijawahi, ..kamwe…’akawa sasa kama anahangaika hivi.

‘Usijifanye mjanja,..leo imefika mwisho wako, ..leteni mkataba ule wa zamani tuyamalize kwa amani, mimi nitakusamehe, lakini kama haupo huo mkataba wa zamani, basi kitakachofuatia hapo ni mimi kwenda mahakamani..’nikasema

‘Mke wangu…’akasema hivyo na mimi nikaa kimia, na akarudia tena... , ‘mke wangu kwanini unalirudia hilo, mimi nakupenda sana mke wangu, kweli kabisa....hilo la mkataba wa zamani, silijui mimi, sikumbuki kama kuna mkataba mwingine zaidi wa huu, kama ungelikuwepo,ningeuleta, tuyamalize mimi na wewe mbona tumekuwa wa kuridhiana mambo,ulishawahi kuniambia jambo nikakataa..eeh…sasa huo mkataba  ..upo wapi huo…’akasema

 ‘Sikiliza,… usijifanye kuigiza mambo hapa,..najua yote hayo, mumepanga uigize hivyo..ujifanye umechanganyikiwa, ujifanye hukumbuki kitu….na ujanja wako umeshafika mwisho,..sasa ni muda wa wewe kuniambia ukweli ili tuyamalize kwa amani,..kwani unataka nini, niambie…sasa nakuulize tena kwa amani, ..je sio kweli kuwa wewe una mtoto nje ya ndoa?’ nikamuuliza

Kwanza ilikuwa kama kapatwa na kitu kimemfinya hivi, akashtuka, na alitulia kidogo, halafu akainua uso, na kuniangalia…kiukweli hayo macho yake sijayaona kabla…akaniangalia, ..mpaka mimi sasa niangalia pembeni..

‘Mtoto nje wa ndoa…!!!’akasema hivyo halafu akatulia, …hakusema neno, mpaka nilipouliza tena..

‘Nimekuuliza hivi, sio kweli kuwa wewe una mtoto nje wa ndoa, ambaye hata kwenye mkataba wenu mwingine wewe umemuandikishia urithi, na kwenye huu mkataba wangu mimi na wewe wa kugushi, kuna maneno mumeyaongezea kuwepo kwake, ili na yeye atambulikane na apewe haki sawa na wengine, sio kweli ..na hapo hapo nakuuliza ni kwanini kipengele hicho mkakiongezea maneno kama hayo, kama sio kweli….?’ Nikamuuliza

‘Mkataba unasema hivyo au sio..huu mkataba, niliona sio, mkataba wetu mimi na wewe au sio…sasa ngoja nikuonyeshe hapo…unaona hapa, na huu ndio mkataba wetu au sio…, umeukubali mwenyewe..kwahiyo hiyo sehemu inasemaje, nikumbushe kidogo mke wangu, mimi nashahau sahau wakati mwingine…’akasema

‘Hapo hukumbuki vyema, lakini kwenye kurudisha vitu kwenye kabati, hukusahau kitu..hapa kwa hivi sasa huna akili za ajabu,..huoni kuwa unajifunga wewe mwenyewe…’nikasema


‘Hahaha, hapana mke wangu, sijifungi bwana…ila wewe wanipambikia mambo, huyo mtoto eeh,....mke wangu kiukweli mimi sikumbuki hilo, ila kuna kitu nataka nikuambie ukweli, ..hebu kaa kwanza, nitakuambia kila kitu…’akasema na mimi sikukaa, akainaimisha kichwa chini kwanza kama anawaza jambo…

‘Mke wangu nimekuwa nikiota ndoto ya ajabu sana, kuwa kweli mimi nina mtoto, tena mtoto huyo ni wa kiume….’akasema

‘Hahaha, umeshaanza kukubali, …haya sema ukweli wote mimi sasa nitakusikiliza…’nikasema sasa nikikaa.

‘Sasa tulia basi nikuambie..hiyo ni ndoto jamani…’akasema

‘Haya wewe singizia vyovyote vile, ..una mtoto wa kiume au sio, na huyo ndiye kakufanya ubadili hadi huo mkataba…’nikasema

‘Sikiliza kwanza, nikuhadithis hiyo ndoto, sio kweli, ni ndoto,..ndoto,..kuota usiku, na kwa bahati mbaya,…nimekuwa nikiota hiyo ndoto sana baada ya ajali,…wakati nilipoanza kupata kumbukumbu zangu…kuwa nina mtoto wa kiume,’ akasema

‘Una mtoto wa kiume au sio, sasa swali ulizaa na nani huyo mtoto…?’ nikauliza

 ‘Kwanza nikuulize wewe huyo mtoto yupo au hayupo…?’ akaniuliza mimi sasa.

‘Unaniuliza mimi tena…’nikasema

‘Mke wangu nisaidie kujibu hilo swali, maana nateseka sana, kumuwaza, kama yupo, ni heri sana kwangu na kwetu kama familia…’akasema

‘Mume wangu…nimechoka, na maneno yako,…nakuuliza tena hili swali, kama ni ndoto au ni kweli, je una mtoto nje ya ndoa, kauli yako ndiyo itathibitisha hili, kama hayupo, basi hatakuwepo,…ilo uweke akilini, kimkataba na kila hali, sasa kama yupo, ni vyema hilo uliweke wazi,…’nikasema

‘Kama hayupo..hatakuwepo, au sio…’akasema sasa akitabasamu.

‘Ndio hivyo, ukitoa kauli yako sasa hivi, kuwa hakuna mtoto wa nje..ndio hatakuwepo hivyo…, akitokea…huyo shetani, au sio….’nikasema, nikijua kama yupo hawezi kumkana.

‘Usiseme hivyo, damu ni nzito kuliko maji…’akasema

‘Hahaha, umeona eeh, hebu rudia tena…?’ nikauliza kama sikusikia

‘Nasema hivi, usiite watoto wa nje mashetani, kwani wao wana kosa gani,…’ akauliza

‘Kwahiyo wewe unaye, ili tusimuite ni shetani, sema ukweli wako usimkane mtoto wako…?’ nikamuuliza

‘Mimi sijui….’hapo akasema hivyo

‘Haya niambie uliota nini…?’ nikamuuliza

‘Ehee hapo sasa tuendelee na ndoto yangu, na tusaidiane kwa hili, ninaota mara nyingi tu, kuwa tuna mtoto wakiume, tatizo sasa ni huyo mama yake,..hataki ..’akasema

‘Hataki nini..?’ nikauliza

‘Hataki huyo mtoto atambulikane kwa jamii…’akasema

‘Kwanini, ni kashfa au..?’ nikamuuliza

‘Sijui,…ni ndoto, inanitesa sana, sasa nataka wewe unisaidie kwa hilo, akili yangu inawaza sana hilo, na zaidi ni kauli ya madocta,..hawajaniambia wazi wazi, lakini nayo ilikuwa kama ndoto…’akasema

‘Wamesemaje…hao madocta..?’ nikamuuliza

‘Mimi sitaweza kuzaa tena…’akasema kwa sauti ya unyonge..

‘Hayo ni ya kwako, nikuulize tena, ni nani mama wa huyo mtoto..?’ nikamuuliza

‘Huyo mwanamke…cha ajabu kabisa, alikimbia na huyo mtoto na ghafla, sasa wakati nahangaika, eeh…puuh, ajali..na ghafla, nikashtuka kutoka usingizi…’akasema

‘Mume wangu acha ujanja…’nikasema

‘Sasa nikuambie kingine mke wangu, huyo mtoto wetu anafanana kabisa na watoto wetu utafikiri mapacha..sasa najiuliza ni kwanini huyo mwanamke akimbie na mtoto wetu,…’akawa kama anataka kulia.

‘Nakuuliza hivi,…huyo mama aliyekimbia na huyo mtoto si unamfahamu…?’ nikamuuliza

‘Ndio namfahamu, kwanini nisimfahamu…’akasema

‘Ni nani sasa…?’ nikamuuliza na hapo akainua uso, akanitizama na sasa niliona dalili za machoni machoni kwake…anataka kama kulia, moyoni sikuwa na huruma naye tena, kila kitu cha huruma kilikuwa kimefungwa, nikamkazia macho yaliyojaa hasira nikisubiria jibu lake.

NB: MBONA NDEFU HIVI


WAZO LA LEO: Huwezi ukahalalisha dhambi kwa kutengeneza dhambi nyingine juu yake…, usifanye dhambi ili kuficha dhambi uliyowahi kuifanya, dawa ya dhambi ni kutubu, na kutubu kupo kwa namna nyingi, …moja wapo ni kukiri kosa, kwa Yule uliyemtendea ukamuomba msamaha, akikubali kutoka moyoni kuwa kakusamehe, basi hapo huna shaka…lakini kutumia ujanja wa kuhadaa ili kosa lisionekane kosa na ili Yule uliyemkosea aseme tu kakusamehe,…bila ya ridhaa yake kutoka moyoni, bado utakuwa kwenye deni ya dhambi.
Ni mimi: emu-three

No comments :