Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Tuesday, January 9, 2018

MKUKI KWA NGURUWE-54


‘Sikuwahii kumuona kwa sura,…maana kila nikimuota, anakuwa kambeba mtoto, halafu anageuka kunipa mgongo, usoni…simuoni, najaribu kumuangalia,..hapo hapo nashtuka kutoka usingizini… lakini kwa maumbile na wajihi namfahamu…’akasema

‘Kwanini unaficha ukweli mume wangu kwanini uanigiza uwongo…?’ nikamuuliza

‘Ukweli ndio huo ninaokuambia mke wangu, na ilikuwa ni njozi, na njozi kama hizo ni nyingi za ajabu, na…wakati mwingine nahisi kama ni kweli…’akasema

‘Kwanini unahisi hivyo..?’ nikamuuliza

‘Watu wanaongea….wanayosema ni kama kweli nilifanya…lakini nikija kwenye akili ya kawaida,…sikumbuki kitu, …nachanganyikiwa mke wangu, niamini, wewe hujui ni hali gani ninayopitia, najua utafikiria na..na…naigiza, lakini mungu mwenyewe anajua…’akasema hivyo

‘Sasa hiyo ndoto…iliishaje, na huyo mtoto ulimpataje..?’ akauliza

‘Ndoto!!? Eeh, ..ndoto, inakuwa hivi, ni…sehemu sehemu tu…ila hiyo ya mtoto kila ikija, haiishi, au ..hata sijui…wakati mwingine nahisi labda ni kwa vile…labda, nasema labda ni kwa vile.. nilitamani sana kuwa na mtoto wa kiume…si ndio hivyo…’akasema, hapo ndio akazidi kunipandisha munkari wa hasira.

‘Nasikia kwenye mkataba wenu, mumeandika kuwa mtoto wa kiume atapewa mamlaka ya kusimamia mali , kama wazazi watakuwa hawapo…na huyo mtoto umempata nje ya ndoa, ina maana anakuwa na haki zaidi ya watoto wa ndoa ni haki hiyo…?’ nikamuuliza

‘Mke wangu, hebu kwanza nipe nafasi ya kufikiri…nahisi ..sipo sawa,..na hayo ya mkataba,..kuna mkataba mwingine upo tena,…ooh , hata sikumbuki, …basi hilo la mkataba mwingine nitakuja kukuambia ni kwanini, kwanza tugange hili hapa…’akainua ule mkataba juu.

‘Nilishakuambia huo mkataba wako siutambui, na sitautambua,..na kwa vile umedhamiria kuung’ang’ania, sawa…mimi nitachukua hatia za kisheria, na ngoja sheria ichukue mkondo wake…’nikasema

‘Mke wangu mkataba huu ni nani aliubuni, nijibu swali hilo kwanza, halafu twende sawa…?’ akauliza

‘Huo uliubuni wewe na marehemu..’nikasema

‘Huo unaosema ulikuwepo, sijui ni gani,….aliubuniwa na nani…?’ akaniuliza

‘Huo, ambao ni wahalali, ambao tulikaa mimi na wewe na wakili wetu, sio huyo marehemu, ilikuwa ni wazo langu…nielewe hapo, usilete ujanja ujanja wako, mimi nazungumzia mkataba huo…ambao mumeuharibu nyie wawili…’nikasema hapo akanywea.

‘Sasa mke wangu ni hivi, kama unaona huu mkataba una kasoro,..kiukweli mimi sifahau,… tufanye jambo moja, ..tukae kikao, tujadili, tupitia vipengele kimoja baada ya kingine, kama kuna makosa, wakili si wapo, yupo wakwako na wa kwangu au sio, basi tutarekebisha hayo makosa, unaonaje hilo wazo langu…’akasema

‘Tatizo lako mume wangu, marehemu alikughilibu, unafikiri mimi ni mtoto wa jana,, huo ni ujanja wako, nia ni kukwepa sheria, unauogopa ule mkataba wa awali, kwa makosa uliyoyafanya,… kwahiyo unachotaka hapa ni kuvuta muda, ili uanzishwe mkataba mpya, na utaanza kufanya kazi lini…huo ujanja kawadanganye watoto sio mimi…’nikasema

‘Mke wangu nisaidie, unajua hali niliyo nayo inanitesa, si nimekuambia, kuwanahisikama bado kuna tatizo, na tatizo hilo kama walivyosema madocta, haliwezi kupona,..na toka siku ile waniambie hivyo, mimi nikawa sitaki hata kuhudhuria kiliniki zao…’akasema.

‘Tatizo gani…?’ nikamuuliza

‘Mimi sitaweza kuzaa tena…’akasema

‘Kwanini…?’ nikauliza

‘Kutokana na athari za ajali, uti wa mgongo umeathirika…’akasema

‘Mbona mimi hilo sijui, sijaambiwa na docta…?’ nikauliza

‘Hilo sikutaka wakuambie wewe …’akasema

‘Kwanini sasa umeamua kuniambia mimi..?’ nikauliza

‘Ni ili uone umuhimu wa watoto…mtoto wa kiume…’akasema

‘Hahaha, mtoto wa kiume ndiye kakufanya ukafanya haya yote, sasa unaona madhara yake,..umezini, umevunja mkataba wetu, na matokea yake ni nini, unaona madhara ya zinaa yalivyo, unatusumbua hata sisi tusiohusika, ndio huyo mtoto wa kiume unayemtaka, au sio…?’ nikauliza

‘Hapana mke wangu,…nielewe hapo, mimi nimekuwa nikiwaza sana, hadi naota, eeh, kwahiyo hali hiyo ndiyo inaniandama hadi kuja kufanya mambo ambayo siyakumbuki, mawazo…na docta kaniambia hiyo hali isipodhibitiwa naweza nika…potea, hata sijui…au kufanya mambo maovu…’akasema

‘Kama yapi…?’ nikauliza

‘Kama kuna kitu …kimeniudhi, au kukasirika, au ..si unajua tena wanadamu tulivyo, unaweza ukatamani hata kuua, ..mtu ambaye unaona ni kikwazo kwako…unielewe mke wangu naongea kama alivyosema docta…’akatulia alipoona namuangalia kwa mashaka na uso umejaa hasira.

‘Siwezi kuamini maneno yako …siku hizi sitakuamini tena, na haya yote unaongea tu, kujihami, au umeambiwa useme hivyo, uigize hivyo, ili nikubaliane na matakwa yako, na kwa hilo, usijisumbue kitu…’nikasema

‘Mimi nakuambia ukweli, kama utaamini sawa, kama hutaamini, shauri lako, ili yasije kutokea ukaja kujutia baadae,…’sasa akasema kwa sauti ya kawaida sio kama ile ya kudeka.

‘Kwahiyo hayo maovu umeshayafanya au..?’ akaniuliza

‘Maovu gani..?’ akaniuliza kwa mshangao tena

‘Si umesema kuna hali inaweza kukutokea kwasababu ya msongo wa mawazo, na hali hiyo inaweza kukutuma kufanya maovu…je umeshayafanya hayo maovu, usisingizie kuzini, maana hilo tendo, ulilifanya kabla ya ajali…’nikasema

‘Kuzini…?’ akauliza sasa akiwa kama anashangaa,

‘Acha ujanja wako bwana…nimeshakuelewa, na tusipoteze muda hapa, kuna maswali nataka kukuuliza, na ukumbuke kwenye mkataba wetu wa awali, ulisema tusije kudharauliana, kila mtu aheshimiwe kauli yake,…’nikasema

‘Lakini mimi sijazini…’akasema

‘Huyo mtoto ulimpataje..?’ nikamuuliza

‘Mtoto…!! Wa kiume eeh, nikuulize wewe,…’akasema hapo nikamuangalia machoni, nikamuona kweli anahangaika, kama kukumbuka jambo, lakini akilini nikajua anaigiza tu,

‘Mtoto, umesema mtoto,…yawezekana,..ni kweli labda sio ndoto,..mtoto wa kiume eeh, basi,…mke nisaidia jambo, tumtafute mtoto wetu, ..unaelewa,…’hapo akatulia aliponiona namuangalia kwa uso uliojaa hasira.

‘Wewe umezini, una mtoto nje ya ndoa, ndio maana mlikaa wewe na marehemu mkaandika maelezo kuhus huyo mtoto wa nje, awe na haki sawa, haya uliyafanya ukiwa na akili zako timamu, kabla ya ajali…na siku ile ya ajali, ilitokea kwa vile ulikuwa una haraka ya kubadili mkataba wa awali, na huo wa kugushi…’nikasema

‘Unasema nini…?’ akaniuliza kwa mshangao

‘Ndio maana nakueleza kuwa kila jambo mimi nalifahamu…’nikasema


‘Mke wangu ...kwanza tuanze moja, hilo la mkataba, au sio, tumeshamalizana nalo kuwa mkataba uliopo ni huu, kama upo mwingine basi tutautafuta, tukubaliane hivyo, ili tuyamalize haya…’akasema

‘Na nikikubali, ili iweje…?’ nikauliza

‘Ili maisha yaendelee, tuendee na shughuli zetu za uzalishaji kama kawaida, kampuni hazifanyi kazi, …madeni yanaongezeka, watu wa kodi wamenijia juu, wataka kufunga kampuni,..na hali hiyo inaniweka kubaya,..naombe mke wangu uyamalize ili na mimi nipate nafuu, niondokane na dimbwi hili la mawazo na mashaka…’akasema

‘Hilo sitachoka kulirudia, hata mbele ya Mahakam, kuwa Mkataba ninaoufahamu mimi ni ule ule wa mwanzo, ambao haukuwahi kufanyiwa mabadiliko, hata kama utaumwa,..au… utachanganyikiwa hiyo umejitakia wewe mwenyewe…vinginevyo…’hapo nikatulia

‘Nakusikiliza mke wangu, vinginevyo,..nini…?’ akaniuliza

‘Uniambie ukweli wote…’nikasema

‘Ukweli gani sasa mke wangu mbona tunarudia kule kule, sasa sikiliza mke wangu tusipoteze muda, niambie kile unachokitaka…huo ukweli ni upi, eeh…na mimi  nitakujibu, naona tunapoteza muda bure, na mimi sijisikii vyema…’akasema, nikamtupia jicho, kiukweli hali aliyokuwa nayo, yaonekana kama kweli hayupo vyema, lakini sikujali tena moyo nafsi ilishakataa…hapohapo nikasema

‘Kwanza nataka unipe majibu kwa haya maswali nitakayokuuliza..’nikasema

‘Haya uliza…’akasema sasa akiwa kama anakata tamaa.

‘Na..kama usiponijibu tukitoka hapa wewe nenda kwa wakili wako na mimi kwa wakili wangu tunakwenda kukutana mahakamani, na ndoa hapo haipo tena, umeshaivunja wewe mwenyewe..na ukumbuke kwenye mkataba wetu wa awali kuna kipengele hicho, cha kupuuzana, .....’nikatulia kidogo

‘Nakusikiliza mke wangu uliza tu hayo maswali..kabla sijazidiwa kabisa, mwili hauna nguvu,…ki-ki-ukweli…! Sa-sawa..mimi sitakupuuza kabisa, hicho kipengere hata mimi nimekiona, .. lakini hilo la kuvunja ndoa sikubaliani nalo na halipo, na halitakuwepo.....’akasema.

Alipiga miayo, akajinyosha, halafu akaniangalia, na kusema

‘Sasa nipo tayari…’akasema

‘Kwanza kwanini mliamua kubadili huo mkataba bila ya kunishirikisha?’ nikamuuliza

‘Jibu nimeshakupa ama kwa kumbukumbu jibu ni hivi...mimi sijui kama kuna mabadiliko yoyote yaliyofanywa kwenye huu mkataba, naapa…, na ndio maana naona leo tukae kama yapo basi tukayafanye, mimi sina shida,, mimi nafahamu kuwa huu ndio mkataba wetu, kama kuna mkataba mwingine zaidi ya huu nionyeshwe basi, kwanini tupoteze muda...’akasema akionyesha kujiamini.

‘Swali la pili...’nikasema

‘Aaah, umerizika na jibu langu kwanza, sijakupuuza mimi, kwanza turiziane?’ akaniuliza

‘Hujanijibu swali langu, sijarizika na jibu lako, lakini tusipoteze muda, hapo kwangu naona kama umenipuuza tuendelee na swali jingine’nikasema

‘Unataka niseme nini mke wangu sasa, mbona unaniweka kwenye wakati mgumu, au wewe una majibu unayataka, basi niambie hayo majibu,...’akasema

‘Swali la pili, je una mtoto nje, uliyezaa huko nje ya ndoa....?’ nikamuuliza

‘Jibu la swali hilo,…eeh,… sina uhakika na hilo, nakumbuka ndoto inasema hivyo, ila kiuhalisia mimi sina uhakika, kama huyo mtoto yupo basi niletewe, itakuwa heri na kwangu pia, ili nispate shida ya mawazo na mashaka, kiukweli hilo linanipa shida sana mke wangu,....’akashika kichwa chake kwa mikono yote miwili.

‘Usijifanye mjanja wa kujizulia ugonjwa wa kuchanganyikiwa, usinifanye mimi mtoto mdogo,  wewe ulishapona, huo ni ujanja ujanja wako tu, wa kutaka kunighilibu, nijibu swali langu, je wewe una mtoto nje, na ulizaa nani?’ nikamuuliza.

‘Kama wewe unadai nina mtoto,…mimi sijui..na ndoto huwezi kuiamini, au sio…sasa kama yupo na umeshamuona niletee ili iwe ushahidi..na utakuwa umenisaidia na mimi, hilo ndilo jibu langu…’akasema

‘Kwahiyo wewe unataka ushahidi…si ndio…basi utaupata, na je ukiupata nichukue hatua gani..?’ nikauliza

‘Mkataba huu utahukumu..ndio ulioupendekeza wewe au sio, tutaangalia sheria inasemaje, au sio…vinginevyo…’akasema na kutulia kama anawaza jambo

‘Vinginevyo nini…?’ nikamuuliza nilimuona akihangaika kama anasumbuliwa na kitu kichwani, ..lakini kama nilivyosema awali, huruma ilishaondoka, sikujali tena

‘Mke wangu naomba unipe muda, nikafanyie uchunguzi,…’akasema

‘Uchunguzi wa nini tena…?’ nikauliza

‘Kuhusu hilo la mtoto… sikumbuki hilo kabisa, sina uhakika siwezi kukudanganya,..ndoto nyingi niliota zinakuwa kama za ukweli…kuna …unasikia mke wangu, lakini ni siri yetu, hata…siku marehemu anauwawa, ok, tuache tu…’akasema sasa akinitolea macho.

‘Hayo utayasema mbele ya mahakama,…na mimi nitakuwa shahidi, na ukumbuke hapo sitasimama upande wako,…kuna mengi nayafahamu dhidi yako, siku hiyo ndio utayasikia…’nikasema

‘Mke wangu nisaidie, mimi ni mume wako…nahisi kama nimetenda kosa…isije ikawa ni kweli…labda nimeua kweli…’akasema sasa akinitolea macho

‘Umeua…?’ nikamuuuliza

‘Sijui…mke wangu sijui…ndoto zinaniandama, siwezi kulala….nisaidie mke wangu….’akasema akiwa kama ananiomba kwa mikono

‘Umemuua nani…?’ niikamuuliza

‘Usirudie hiyo kauli tena, mimi sijaua, au sio, ni ndoto tu mke wangu,…naogopa mke wangu, usije kusema hivyo tena, unasikia, …’akasema kweli sasa akionyesha kuhaha

‘Swali la tatu, ni nani mwanamke mliyezaa naye?’ nikamuuliza, sikujali huko kuhaha kwake, japokuwa kiukweli nilimuona akipata shida.

‘Mwanamke niliyezaa naye!?..mungu wangu, ni nini tena hiki…!’akashika kichwa

‘Jibu swali acha ujanja…’nikasema

‘Mke gani jamani, mke wangu ni wewe, nimezaa na wewe, nimekumbuka mwanamke niliyemuona kwenye ndoto ni wewe…wewe ndiye aliyemchukua mtoto, ukakimbia naye, unasema sio wangu, sio wa halali…ukataka kwenda kumtupa,  ni wewe, niambie mtoto wangu yupo wapi, niambie ....’akasema  sasa anasimama kwa hasira akinielekea mimi.

‘Wewe mwanaume…hebu acha huo mchezo wa kuigiza…’nikasema sasa akawa ananisogelea katoa macho, anatetemeka, mimi nikasogea, na nilipoona hali inazidi, nigeuka na kukimbilia mbali na yeye, mara akadondoka sakafuni, na nikasikia kama akakoroma nikajua nimeua…

***********
 Nikarudi pale alipolala sakafuni…niliona sasa katulia, nikashika mapigo ya moyo, nikaona yanapiga kwa mbali, lakini inatia mashaka, haraka nikachukua simu, nikitaka kumpigia docta, mara mtu huyo katikisika

Nikaacha simu, na kumuangalia….akaanza kujiinua, halafu akakaa…akawa sasa anaangalia huku na kule, mara akasimama,..huku anayumba yumba

‘Kumetokea nini…?’ akauliza

‘Hebu kaa pale maswali yanaendelea…’nikasema

‘Maswali!!, maswali gani…?’ akauliza

`Swali la nne, je ni wewe uliyechukua mikataba kwenye kabati langu, la hapa na kule ofisini ?’ nikauliza

‘Mimi.!!!...ofisini kwako, lini,..?’ akawa anashangaa , akageuka akauona ule mkataba, kwa haraka akauchukua na kuishikilia mkononi, halafu akageuka kuniangalia..halafu, akageuka kuangalia mlango unaolekea maktaba, akaangalia saa;

‘Mbona umewahi leo kutoka kazini, …?’ akaniuliza

‘Swali jingine…umeniupuuza kunijibu swali la awali, hiyo inanakiliwa kwenye kumbukumbu, wakili sikia hiyo…’nikasema, akageuka huku na kule kama anatafuta mtu, nahisi ni hapo niliposema wakili sikia hiyo, hakuelewa mimi nina maana gani.

Swali la tano…, Je siku makabrasha alipouliwa ulikwenda kwake kufanya nini?’ swali hili likamfanya ashituke na kugeuka akaniangalia kwa mashaka, akageuka na kuangalia mlango wa kutoka nje, kama anaogopa vile, baadae …, akasema;

‘Ma-mamamaah...ina maana ni kweli.....haiwezekani, mke wangu kumetokea nini, ulirudi ulinikuta nipo wapi, niambie mara moja, maana hii ni dalili mbaya, mke wangu tafadhali...halafu alishazikwa, ….au..sikumbuki mimi, hivi kweli eeh…’akasimama sasa..na kuanza kutoka nje

‘Unakwenda wapi, haujamalizana, nimeshakuambia nikitoka hapa mimi naelekea kwa wakili wetu, nafuata hatua nyingine, tutakutana mahakamani...’nikasema lakini mwenzangu alikuwa anaondoka, haangalii nyuma akasema;

‘Nawahi mazishi....’akatoka, mimi nilicheka kidogo na kusema

‘Janja yako...nafikiri wewe hunifahamu eehe...’na mimi nikamfuatilia huko huko nje, nilitaka hili tatizo nilimalize leo, nimuachie hiyo kazi wakili, sasa asonge mbele, tulifikishe hili tatizo kwenye vyombo vya sheria,…

Kwa haraka na mimi nikatoka nje, nikamuona akiingia kwenye gari lake, na mara simu yangu ikaita, nikaipokea kabla sijaangalia mpigaji ni nani. Huyo mtu akasema;

‘Mimi ni docta .....’akasema kumbe alikuwa yule docta aliyemtibia mume wangu, nikashukuru maana nilikuwa na mpango wa kumpigia, kuhakiki haya anayoyafanya mume wangu kuwa ni ya ukweli au anaigiza tu.

‘Hali yako docta tena nilikuwa nataka kuongea na wewe..’nikasema

‘Ndio ...ndio maana hata mimi nilitaka kujua hali ya mume wako, anaendeleaje kwani kipindi kile cha matibabu, kulikuwa na docta mwenzangu, ambaye alikuwa akimwangalia kwa upande wa kumbukumbu, na alitaka kujua kama kuna hali yoyote inayojitokea kwake..yupo hapa nyumbani ?’ akaniuliza

‘Ndi-ndio…lakini anatoka..’nikasema

‘Sasa Yule docta wake kaja leo ndio karudi toka safari’akasema

‘Kwahiyo anasemaje…?’ nikauliza nikionyesha kushangaa.

‘Sijui kama mliwahi kuongea naye kipindi kile, kuna kitu kwa mume wako ambacho alikigundua, na kwa muda ule  hilo hatukuwa tumelitila maanani sana..lakini kuna matukio yalitokea…kipindi hicho docta ameshaondoka…’akasema

‘Matukio gani…?’ nikauliza

‘Kusahau..au kujiwa na kitu kama njozi…anaweza akalala, na kuota, akafanya vitu kwa vitendo, au mchana, akawa kama kalala, akafanya mambo tofauti na utashi wake, inakuwa kama njozi…’akasema

‘Unasema nini…?’ nikauliza kwa mshangao.

‘Kuna matukio yalitokea akatoweka hapa hosp, na baadae akarudi, akiulizwa kafanya nini, anakuwa hakumbuki,…au akakumbuka jambo, akafanya kwa umakini zaidi, au anakuwa na akili ya ajabu unaweza kumuuliza jambo, akakujibu kwa umakini sana,..na hali hiyo ikiisha, hawezi kufanya hivyo…’akasema

‘Docta …’nikasema sasa nikianza kuingiwa na mashaka.
‘Sasa docta wake kaja, na kaniambia hayo yanaweza kumtokea mgonjwa wa namna hiyo, inatakiwa kuwa makini naye sana, kwani anaweza kufanya jambo la hatari....’akasema

‘Unasema nini docta mbona hamkuwahi kuniambia kitu kama hichoo’nikasema kwa hasira.

‘Baada ya uchunguzi, ...kipindi kile tulipokuwa naye, alionyesha dalili, kuwa kapona, na mwenzangu akawa keshaondoka, ...tulimwambia yule docta mnayeishi naye, maana wakati huo wewe ulikuwa na matatizo… ulikuwa jela,..sasa kwa vile mwenzangu karudi leo na tukawa tunafuatilia jarida la mume wako..’akasema

‘Docta …’nikataka kusema lakini yeye akaendelea kuongea

‘Sasa… kwanini, mume wako hafiki kwenye kliniki yake maana hiyo ingelisaidia kujua hatua za maendeleo yake, yeye aliandikiwa afike kila mara hapa hospitali kwa kliniki yake,hajafika kama tulivyomuagiza, ndio maana tukaamua tukupigie’akasema.

‘Docta mimi ninaweza kuwashitaki, ..hilo ni kosa kubwa sana, maana sasa hivi nimemuona mume wangu kama kachanganyikiwa, na mimi nilifikiria kuwa anajifanya..kwasababu nimekuwa nikimuuliza maswali., anajibu kama anaigiza, kuwa hajui, mara anasema kasahau, mara aliota,..katoka sasa hivi na gari, yupo kama ...’nikasema.

‘Mfuatilieni haraka,...na mleteni hapa hospitalini hiyo dalili inaweza kuleta matatizo mengine docta wake yupo, na akiondoka itachukua muda kurudi. ....’akasema docta, na mimi nikakata simu yake na kuingia kwenye gari langu, nikijaribu kumfuatilia, sikujua kabisa kaelekea wapi.....oh, ina maana mume wangu akchanganyikiwa kweli....

NB: Kwa leo ndio hivyo,


WAZO LA LEO: Kwa wandoa mmoja anapoumwa, ni vyema mkajaliana kwanza, hata kama kulikuwa na sintofahamu, migongano ya kindoa, ya kifamilia, na mitihani mingine ya kimaisha, hayo yote ya kibinafsi, na masilahi yawekwe kando kwanzao, muangalie swala la afya, swala la ugonjwa, kwani afya ni bora kuliko mali, kuliko hayo mnayokosana nayo..na huenda huo ukawa na mtihani katika kutatua matatizo yenu.

Ni mimi: emu-three

No comments :