Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Friday, January 5, 2018

MKUKI KWA NGURUWE-51


Ilikuwa siku maalumu ya kupokea taarifa kutoka kwa watu wangu, kuna vijana huwa nawapa kazi zangu, kwa kuwaamini, hasa zinazohusu mambo yangu binafsi, hata ya kikazi pia…nilifika ofisini na kumwamboa katibu muhutasi kuwa hao vijana wangu waitwe mmoja mmoja…na wakati nipo tayari, mara mlango ukagongwa...

‘Unaweza kuingia..’nikasema

Akaingia jamaa mmoja…yeye ni mtu wa masoko, lakini pamoja na kazi hiyoo yeye nimatumia kwa mambo ya uchunguzi ikibidi..ana utaalamu huo, na nilishampeleka shule kusomea upelelezi kidogo, inasaidia kwa kazi zangu…Nilimwambia kuwa nataka asomee upelelezi kidogo, kwa nia ya mashindano ya kibiashara, lakini pia nataka anisaidie kwenye kazi zangu.Tunaelewana sana.

‘Kutokana na uchunguzi wangu, mtu aliyechukua huo mkataba atakuwa ni mtu wa humo humo ndani, alitumiwa,…maana hakuna mtu wa nje aliyweza uingia kwenye ofisi yako, akaonekana…’akasema

‘Huyo mtu wa nje ni nani, uliweza kumtambua …?’ nikauliza

‘Imekuwa ngumu kidogo…’akasema

‘Je ni nani aliwahi kuifika kati ya watu niliokuambia uwachunguze, ?’ nikamuuliza

‘Mtu ambaye aliweza kufika mara kwa mara ni docta Yule unayemuita Rafiki wa mume wako,…’akasema

‘Ehe…je uliweza kufahamu, kama aliweza kuingia ofisini kwangu au kuongea labda na mfanyakazi wangu wa usafi…?’ nikamuuliza.?’ nikamuuliza

‘Yeye hata wakati ukiwepo alikuwa akifika kama alivyofika kipindi hiki…yeye hufika kwa minajili ya kikazi, akifuatilia malipo yake ya matibabu ya wagonjwa, ya wafanyakazi wako, na mara zote alizofika alikuwa akiishia mapokezi....’akasema.

‘Una uhakika na hilo…?’ nikamuuliza

‘Kwa uchunguzi wangu naweza kusema hivyo, sizani kama aliweza kuingia ofisini mwako,…’akasema

‘Mwingine ni nani…?’ nikamuuliza akilini mwangu nikianza kujiuliza kama docta anaweza kufanya kitu kama hicho, haiwezekani, kwasababu hana faida yoyote na huo mkataba…labda kumsaidia rafiki yake…hapana haiwezekani.

‘Na mwingine aliyeonekana, ni bosi, nina maana ....rafiki yako, kuna kupindi alifika kabla hajaondoka kusoma na pia aliporejea,..’akasema

‘Aliporejea..!?...alifuata nini…?’ nikamuuliza

‘Alikuja akikuulizia, lakini hakuweza kuingia ndani ya ofisi yako, naye aliishia mapokezi, na hakukaa sana, kwani aliambiwa haupo....’akasema

‘Na kabla…?’ nikauliza

‘Kabla ni kipindi ukiwepo, au…kama haupo, anaishia mapokezi tu…..’akasema

‘Kwahiyo hakuna mtu yoyoye mwingine ambaye tunayemshuku, aliyeonakana akiongoea na mfanyakazi wangu wa usafi, ambaye ndiye anayetunza ufunguo za ofisi yangu?’ nikamuuliza

‘Tatizo ni kuwa huyo mfanyakazi wako wa usafi, anaongea na watu wengi sana, sasa sio rahisi kuhisi yupi ni yupi, hata nilipotumia mbinu za ziadi kupata taarifa kwake, ilionekana kama tunamshutumu mtu ambaye hajafanya jambo kama hilo, nina uhakika kama ni mtu aliingia, yeye atakuwa hajui kabisa..’akasema.

‘Sasa alipaje ufunguo….?’ Nikauliza

‘Hapo hatukuweza kupata ukweli,….’akasema

‘Ina maana kwa uchunguzi wako,…maana nimekupa kazi hiyo ili nimpate huyo mtu, wewe umegundua nini, angalau kidogo cha kusaidia…au umeshindwa kumpata…?’ nikamuuliza

‘Mwanzoni nilimuhisi katibu wako muhutasi, kwasababu yeye ana haki ya kuingia na kutoka ofisi kwako, lakini nilipofuatilia nyendo zake, niliona hahusiki, maana alikuwa likizo kipindi chote hicho ambapo wewe hukuwepo ofisini.’akasema

‘Kwa kifupi bado hujamgundua ni nani alifanya hivyo..?’ nikauliza

‘Kiukweli bado bosi, tatizo wewe hutaki tufanye tuonavyo sisi, wewe umeteka tufanye utakavyo wewe sasa inakuwa ni ngumu kidogo, ukitaka tumgundue kwa njia zetu, tupe hiyo nafasi, tutampata tu,…’akasema

‘Hapana msifanye hivyo, nilitaka kufahamu mambo machache kutoka kwenu sitaki kuleta utata kwa hili, unanielewa, basi tusipoteze muda, wewe endelea na kazi zako…’nikasema

‘Sawa bosi….’akasema hivyo na kuondoka.

Wa pili alikuwa mtu ambaye nilimpa kazi ya kuchunguza nyendo za mume wangu kipindi hicho, kabla hajapata ajali..akasema;

‘Siku mume wako alipopata ajali, alionekana akiwa katokea maeneo ya rafiki yako,kwahiyo huenda alipita hapo,au alitokea hapo kwa rafiki yako ...’akasema

‘Huna uhakika kuwa alitokea kwa rafiki yangu…?’ nikauliza

‘Uhakika wa moja kwa moja haupo…kwasababu hakuonekana akiingia au kutokea kwenye nyumba ya rafiki yako,…’akasema

‘Kwahiyo ni kweli kuwa alipita tu…?’ nikauliza

‘Mara nyingi yeye anasafisha gari lake kwa muosha magari karibu na anapoishi rafiki yako,…cha ajabu muosha magari, japokuwa hayupo, lakini nilimfuatilia mpaka huko kijijini kwao, nikaweza kuongea naye, hakuataka kabisa kuongea na mimi, ila baada ya kumpatia chochote, ndio akaongea

‘Anasemaje..na kwanini kaondoka hapa Dar..?’ nikamuuliza

‘Anasema maisha yamemshinda tu, kaona akafanyie shughuli zake kijijini…’akasema

‘Ehe,siku hiyo ilikuwaje…akiwa kazini kwake,..hakuwahi kuosha gari la mume wangu..?’ nikamuuliza

‘Anadai hakuwahi kuosha gari la mume wako, hakumbuki kabisa..anasema yeye anaosha magari ya watu wengi, na sio kazi yake kukariri..lakini ana uhakika hakuwahi kuosha gari la mume wako, …’akasema

‘Ni kweli au anaogopa tu kusema ukweli..?’ nikauliza

‘Nimetumia kila mbinu hajakubali hilo, nahisi hakuwahi kuosha, au hakumbuki kweli, sizani kama angetuficha...’akasema

‘Kwahiyo ni kweli kuwa mume wangu alipita tu maeneo hayo na hakuwahi kufika kwa rafiki yangu..?’ nikauliza

‘Itakuwa hivyo, ila waliomuona akiendesha gari, wanasema alikuwa katokea maeneo ya huko, na alikuwa akiendesha kwa mwendo kazi sana, nikama vile alikuwa akiwahi  jambo, na.....hakuwa amelewa kabisa, kwani ofisini kulikuwa na kikao, na alipotoka kwenye kikao hakupitia kwenye ulevi..’akasema

‘Hakupita kwenye ulevi, aliyekuambia hivyo, amejuaje, …ina maana alifahamu anapoelekea …alipokwenda mume wangu..?’ nikauliza

‘Wanafahamu wapi anapokunywa mara kwa mara..na hao walimuona akitoka ofisini, na kuendesha gari…kuelekea upande mwingine, hawakufuatilia,…na tulijaribu kutafuta mtu mwingine …hakuna aliyemuona akielekea kwa rafiki yako…’akasema

‘Hilo naweza kuamini kuwa hakuwa huko kwa rafiki yangu maana mimi mwenyewe nilikuwa huko, kama angelifika mimi ningelimuona.’nikasema

‘Sasa ajali yake ilitokea kwa vile alikuwa kwenye mwendo kazi, na alipokuwa akata kona..ndio akakumbana na hilo gari jingine..akafunga breki lakini zilikataa, ndio ikapatikana na hiyo ajali...., alikuwa mwepesi kuruka nje..,na wakati anatoka alionekana, akiwa na mkoba, .....’akasema

‘Aliruka kabla…mmh, hapo, unataka kusema nini, na huo mkoba wa…komputa au…?’ akauliza

‘Ni mikoba hii ya kawaida, na kwa vile aliumia sana, aliyekuja kumsaidia, anasema mume wako hakutaka kabisa kuachana na huo mkoba, na kuna mmoja alitaka kumsaidia, lakini akakataa,...’akasema.

‘Na alipofika mlangoni mwa nyumba yenu, alionekana kupiga simu,..ndio akaja jirani yenu mmoja…ndiye aliyemsadia hadi kwa nyumbani kwa docta..na huyo docta ndiye aliyemsaidia kwa huduma ya kwanza...’akasema.

‘Mlipochunguza nyendo zake za huku nyuma , mligundua nini?’ nikamuuliza.

‘Mara nyingi alikuwa akienda kunywa na rafiki yake, yule docta, na wakati mwingine akiwa peke yake, alionekana mpweke, na hakupenda kukaa na watu asiowafahamu…’akasema

‘Na zaidi ya huyo docta ni nani wengine alipenda kunywa nao…nikimaanisha wanawake labda?’ nikauliza

‘Kiukweli hao hawakosekani, wakiwa kwenye makundi, …lakini haikuonyesha wazi kuwa ana rafiki wa kike wa kupitisha naye muda…’akasema

‘Hakuna mwanamke ambaye alikuwa naye karibu sana..hakuna hata mmoja..?’ nikauliza

‘Mwanamke ambaye mara nyingi anakuwa naye karibu ni rafiki yako, huyo anayesoma huko nje, yeye mara kwa mara walikuwa wakionekana naye, najua hata wewe mwenyewe unalifahamu hilo, ni hata mkiwa wote yeye anakuwepo, au sio, huwezi kumshuku vibaya..na wengine ni wafanyakazi wake, au wa ofisi anayoifanyia kazi...’akasema.

‘Je mume wangu hakuwahi kumsindikiza rafiki yangu huyo hadi kwake,, na hata kuingia kwake, na hata kukaa kwa muda mrefu wa kutilia mashaka, au japokuwa kwa muda mfupi?’ akaulizwa.

‘Ndio, mara nyingi tu, huwa wanamfikisha kwake, na kuondoka, kuna muda wanafika na kukaa humo kwa kipindi kirefu tu, kwa vile ni rafiki yako, hatujaona kama kuna lolote baya, sizani kama wanaweza kuvuka mipaka, ulisema wewe unamuamini kwahiyo hata sisi tumechukulia hivyo....’akasema

‘Kwa uchunguzi wako, hakuna dalili zozote za mahusiano ya kimapenzi kati ya rafiki yangu, na mume wangu,..?’ nikauliza

‘Hatukiliona hilo…hawajawahi kulionyesha hilo hadharani…, maana hata wakiwa kwenye starehe, walionekana wakijali, kuheshimiana, na mume wako sio mtu wa kufanya mambo ya aibu anajichunga sana, kama alivyo rafiki yako, hatukuweza kulibaini hilo…’akasema.

‘Na huyo rafiki yangu hakuwa na mahusiano na mdogo wa mume wangu..?’ nikauliza

‘Kwa uchunguzi wetu, yaonekana rafiki yako hayupo karibu sana na huyo shemeji yako, na yaonekana kama hawaelewani kina namna fulani, kwahiyo haiwezekani wakawa wapenzi....’akasema

‘Haiwezekani, ina maana mume wangu hakuwa na rafiki mwingine wa kike.....sasa huyo mtoto ninayesikia anaye ni kutoka kwa mwanamke gani?’ nikauliza

‘Mtoto…mmh, hapana, ..kwa uchunguzi wetu, ....hilo halikuweza kuonekana, kwani kama ulivyotaka, ni kuwa tuchunguze bila kuweka tetesi, tuwe na uhakika na hicho tulichokifanya, na sisi hatukuona au kugundua mwanamke mwenye mahusiano na mume wako…’akasema

‘Na ni kweli mumegundua kuwa hana mtoto nje…?’ nikauliza

‘Hilo hatujaligundua, hatuwezi kusema kitu ambacho hatuna uhakika nacho kama ulivyotaka..kama unataka tulifanyie kazi hilo, kuwa kama ana mtoto nje, tunaweza kulifanyia uchunguzi, lakini kwa mipaka uliyotuwekea sisi hatujagundua chochote kuhusu mtoto wa nje…’akasema

‘Sawa, ndivyo nilitaka,…sikutaka hayo myafanyie kazi, kama kesi, hakuna kesi hapa ni kutaka kujirizisha tu,..ila kuna kitu nataka unifanyie, nenda huko alipojifungulia huyo rafiki yangu uone kama utagundua baba wa huyo mtoto wake, je alizaa na nani, unaweza kulifanyia kazi hilo…?’ nikamuuliza

‘Naweza bosi…’akasema

‘Unajua …awali sikutaka ulifanye hilo, sasa kalifanyie kazi, na pili, utafute kama kweli mume wangu ana mtoto nje, mmh, yah, lakini usifanye kuonyesha mimi nataka kulifahamu hilo, chukua muda, unanielewa…’nikasema

‘Sawa nakuelewa bosi, ila kuna kitu, nilitaka kukuambia,....ila wewe ulisema tusihangaike sana na rafiki yako na ..na…’akasita kidogo

‘Niambie ni kitu gani…?’ nikauliza

‘Ulisema haina haja ya kumchunguza rafiki yako, na ulisema kuna mwanaume aliwahi kufika hospitalini,..wa kwanza, kuna kitu kama hicho, ila ulisema haina haja ya kulichunguza hilo, lakini kwa uchunguizi wetu mwanaume wa kwanza kumtembea pale hospilaini alikuwa ni mume wako, hakuna mwingine …..’akasema.

‘Unasema kweli,…haiwezekani, mbona rafiki yangu alinificha hilo.., na hata mume wangu, mmh..hapa kuna kitu,..una uhakika na hilo..!?’ nikauliza kwa mshangao

‘Ndio…nina uhakika na hilo…’akasema na alitaka kuongea jambo, lakini mimi nikamtiza kwa swali jingine

‘Je vyanzo vyenu viliwahi kumuona mtoto wa rafiki yangu, kisura,..anafananaje?’ akaulizwa

‘Ni kitu ambacho wengi wetu waliona ni ajabu, kwani mtoto huyo amekuwa akifichwa sana, hajawahi kuonekana sura yake na mtu yoyote....’akasema

‘Haiwezekani, ina maana na ujanja wenu wote hamkuweza kuiona sura ya huyo mtoto wake, hajawahi kupiga picha, ?’ nikawauliza

‘Unamfahamu sana rafiki yako huyo, kazi za uchunguzi, ulinzi na usalama anazifahamu sana, na akiamua kufanya jambo, analifanya kwa makini sana, nahisi hakupenda kabisa mtu kuiona sura ya mtoto wake…’akasema

‘Mhh..haiwezekani, kwahiyo nyie hamjafahamu yupo je…?’ nikamuuliza

‘Wengine wanasema ana sura ya kihindi, wengine ana sura ya kizungu,…sasa hatujui kwakweli, nahisi basi atakuwa akimvalisha vitu ambavyo huwezi kabisa kugundua sura ya mtoto ya asili, nahisi alikuwa akimvalisha nywela za bandia hata sura za bandia....’akasema.

‘Sura ya kihindi, hahaha..hapana mimi nimemuona ni mwafrika kabisa…’nikasema

‘Ndivyo watu waliobahatika kumuona wanadai hivyo…’akasema

‘Unahisi ni kwanini amefanya hivyo....?.’nikawauliza

‘Huenda hataki baba wa mtoto huyo ajulikane, au huyo baba amfahamu huyo mtoto kuwa ni wake...’akasema

‘Kwanini?’ nikamuuliza

‘Huenda ni kuogopa  kashifa...  Au yeye mwenyewe rafiki yako hataki baba wa mtoto huyo afahamu kuwa ni mtoto wake....’akasema.

`Nashukuru, huenda nikakuhitajia tena, endelea na uchunguzi....’

*******

Baadaye alikuja mtu ambaye nilimpa kazi ya kuchunguza kifo cha Makabrasha, yeye aliwahi kufanyia kazi za upelelezi, lakini kwasababu za kiafya akaacha kazi, ..na hata alipopona hakutaka tena kuirudia hiyo kazi, akawa anafanya kazi hiyo binafsi, na yeye akatoa taarifa yake.

‘Kifo cha Makabrasha, kimefunikwa kiaina, nahisi hata polisi walishachoka na tabia ya huyo mtu, na waliona kufa kwake ni bora tu, japokuwa walifanya juhudi ya kumtafuta muuaji, lakini hawakufika popote, wakahitimisha walivyoona wao....’akasema

‘Kwanini unasema hivyo?’

‘Kwasababu ya matendo ya marehemu,  kwani alifikia hatua ya kuwawekea hata hao polisi mitego, akiwanasa kwenye mambo yanayoenda kinyume na maadili ya kazi zao, anawarekodi, na huja kutumia kumbukumbu hizo kuwatishia, kuwa wakifanya lolote na yeye atawalipua, kwahiyo hata wao, wakawa hawana jinsi, ila kufuata anavyotaka yeye....unaona eeh..’akasema

‘Kwahiyo unataka kusema nini?’ nikamuuliza

‘Ninachotaka kukuambia ni kuwa ukweli wa kifo cha Makabrasha hautaweza kugundulikana kiraisi unaweza ukaweka shaka shaka kuwa huenda hata hao watu wa usalama wanajua kitu fulani,lakini hawataki..kiukweli, haipo wazi, na hata wao hawajachukulia kifo chake kwenye uzito wake...’akasema

‘Haiwezekani, ina maana watu wa usalama wanaweza kuhusika..hiyo dhana unaiwekaje hapo…?’ nikauliza

‘Sijasema wanaweza kuhusika, ila wanaweza kujua jambo..unielewe hapo..’akasema

‘Sasa ni nani anaweza kuhusika kwa uchunguzi wako, sizani kama muuaji anaweza kupotea hivi hivi..?’ nikauliza

‘Huyo muuaji aliyefanya hayo mauaji, ni mtu ambaye alijua ni nini anakifanya, na inaokena sio mauaji ya kukurupuka, ni mtu alijiandaa kwa muda mrefu, huenda alikuwa kwenye hilo jengo, siku mbili kabla akimvizia..’akasema

‘Kwa vipi…?’ nikauliza

‘Ni lazima huyo mtu awe anafahamu taratibu zote za marehemu, ratiba yake, na..anafahamu mfumo mnzima wa mawasiliani, na mfumo wa jengo na ofisi ya Makabrasha...’akasema.

‘Mapka kufahamu mfumo, ina maana basi anaweza kuwa alihusika na ujenzi wa hilop jengo au..?’ nikamuuliza

‘Anaweza asiwe ni mjenzi, badi ni mtu aliyelisoma hilo jengo…maana ukisema ni mjenzi wa hlo jengo, huyo jamaa tunamfahamu, na kwa muda sasa wapo mikoni kuna ujenzi wanafanya huko, lakini wanaweza kuuza siri za mjengo huo,..huyo mtu aliyefanya hayo mauaji sio wa kawaida, ni mtaalamu kweli kweli.....kwani kwa jinsi alivyoingia, na kwajinsi alivyoweza kusoma mfumo wa mawasiliano, na mtandao uliokuwa umewekwa humo ndani,, ...sio mtu wa kawaida....’akasema

‘Haya niambie kutokana na uchunguzi wenu Makabrasha aliuwawa kivipi, na kwanini?’ nikamuuliza

‘Huyo mtu inawezekana alikuwepo humo ndani kwa siku mbili kabla, kama nilivyosema, na silaha aliyoitumia, itakuwa ililetwa usiku wake, na ikaingizwa kwa kupitia nyuma ya ukuta....’akasema

‘Kwanini unasema hivyo..?’ nikauliza

‘Kwasababu kama ingelipitia kwenye njia ya kawaida, kupitia mlangoni, ...kungelitokea milio ya kuashiria hivyo.....kuna mfumo mle ndani, wa kugundua kuwa mtu kabeba kitu cha hatari, kuna mfumo wa kuchukua kumbukumbu za matukio, ina maana kila anayeingia ataonekana,..lakini cha ajabu siku hiyo ya tukio, hayo yote hayakuonekana kwenye mtandao uliowekwa humo ndani...’akasema.

‘Ili uingie kwenye jengo hilo kuna njia moja tu, na ukishaingia kwenye jengo, ili upande juu, kuna njia moja tu, na huko kote waliweka vinasa matukio na sauti,..hebu fikiri, kote huko hakukuonekana hilo tukio, kumefutwa kabisa..ina maana huyo mtu hakutaka kabisa kuonekana chochote siku hiyo..

‘Na ina maana basi hata kama huyo mtu aliingia na silaha, ...labda akamuhonga mlinzi, lakini angelipita wapi na hiyo silaha,  kwasababu mawasiliano ya kudhibiti hiyo hali ipo sehemu ya siri, huko juu, ...inawezekana basi walinzi wawe wamekula njama,...’akasema

‘Si ndio hapo hata mimi nashindwa kuelewa na kwanini polis wasimkamate hata Yule mlinzi, wangembana nahisi angeweza kuwafahamisha jambo..’nikasema

‘Alikamatwa, lakini hawakuweza kupata chochote kutoka kwake…’akasema

‘Pale mlangoni huwezi kuingia na silaha, pamoja na kukaguliwa na mlindi lakini pia kuna mtambo,...mtu akipita silaha, kuna kelele za kuashiria hatari, na hizo kelele, zingelijulikana kwa watu wote, pale huwezi kuingia na silaha mle ndani kabisa,....’akasema.

‘Sasa hiyo silaha iliingiaje humo ndani…?’ nikauliza

‘Hiyo silaha itakuwa ilipitishwa nyuma ya jengo, na walichofanya ni kutengeneza kamba ndefu, iliyoshuka hadi chini, na mtu aliyekuwa chini, akaifunga ile silaha kwenye hiyo kamba, na huyo aliyekuwa juu, akavuta hadi juu, na kuhakikisha, haipiti sehemu zenye kuhisi au kugundua kitu cha hatari..na huenda kwa muda huo, huyo mtu alikuwa keshazima viwambo vya hatari vya ndani....’akasema.

‘Mtu huyo asingeliweza kuzima viwambo hivyo kwa jengo zima, walinzi wa chini wangeliona hilo, na wangeliweka kwenye taarifa zao, hakuna taarifa kama hiyo, na hata tulipojaribu kufanya uchunguzi kwa watu hao, haukukuwa na dalili zozote kama hizo siku hiyo...’akasema

‘Kwahiyo muuaji, atakuwa alikuwa ndani, na muda ulipofika, akafanya kazi yake kirahisi, akaondoka..na cha ajabu basi hata tukio lenyewe,hilo la mauaji halipo...polisi wanadai kuwa walioona baadhi ya sehemu ya tukio hilo, lakini sio kweli..hakuna  kitu kama hicho,...kuna mtu aliyekuja kuondoa kila kitu...cha siku hiyo, na huyo mtu alifahamu ni nini anakifanya , ...’akasema.

‘Kwahiyo hamkuweza kugundua lolote, kwa njia zenu, kuwa huenda mtu fulani anaweza kuhusika?’ nikamuuliza.

‘Huyo aliyefanya hivyo ni mtaalamu, kweli..hatukuweza, na kwa vile polisi wenyewe wamesalimu amri na kuona kuwa ni kifo cha kulipiza kisasi, mimi naona haina haja ya kuhangaika sana..ila kuna kitu ninachoshangaaa,...’akasema

‘Kitu gani....?’ nikauliza

‘Siku ile ya tukio, kuna watu wanasema kuna mtu, japokuwa alijibadili, lakini anafanana na mume wako kimaumbile’akasema

‘Unataka kusema nini hapo?’ nikamuuliza

‘Mume wako alikuwepo kwenye hilo jengo, wakati tukio hilo linafanyika, na polisi hawakuligundua hilo, ..kama wangeligundua hilo, nina imani kuwa mume wako angelikuwa hatarini, wangemshika....mimi nilijaribu kufanya uchunguzi wangu, na hata kuongea na mume wako, lakini hakutaka kutoa ushirikiano...je kuna njia yoyote naweza kuongea naye,...?’ akaniuliza.

‘Hapana, haina haja, inatosha....’nikasema.

‘Lakini nina uhakika sio yeye aliyefanya hayo mauaji, ila nahisi atakuwa anamfahamu huyo muuaji....’akasema

‘Kwanini unasema hivyo?’ nikamuuliza

‘Mume wako sio mtaalamu sana wa kutumia silaha, huyo muuaji, anafahamu kutumia silaha, na alifahamu wapi pa kulenga, ...ni mtaalamu kweli kweli, na alijua akilenga wapi mtu haponi....na kwahiyo huyo mtu atakuwa kapitia jeshi au kitu kama hicho, sio raia wa kaiwada tu..ni mtu anayefahamu ni nini anakifanya.’akasema

‘Nashukuru kwa taarifa yako....’ nilisema hivyo, na sikutaka kujua zaidi,…na hasa niliposikia kuwa mume wangu keshagundulikana kuwa alikuwepo humo kwenye jengo, na ina maana hata polisi watakuwa wameshagundua, sasa ni kwanini hajamkamata…

Nilihitajia muda wa kuliwazia hilo, na huyo jamaa akawa anataka kuondoka, halafu akasema;

‘Yule mdada, rafiki yako…unamuamini sana…?’ akauliza

‘Kwanini…?’ nikauliza

‘Nakuuliz tu…kuna kitu nimekigundua, nitakuja kukuambia, lakini kwa hivi sasa bado sijamuelewa, ndio ni mtu wako wa karibu, lakini…kuna kitu simuelewi..mbona walikuwa karibu sana na marehemu…’akasema

‘Kwa vipi…?’ nikamuuliza

‘Kuna matukio mbali mbali wameonakana wakiwa pamoja, wanaongea, na mara nyingi, rafiki yako anakuwa hayupo wazi kuonekana, ina maana wanaongea kwa siri, na hataki watu wafahamu kuwa anawasiliana na huyo marehemu…’akasema

‘Kwani siku hiyo ya tukio walionekana na marehemu…?’ nikauliza

‘Ndio..lakini kwa njia hiyo hiyo…’akasema

‘Unahisi yeye anaweza kuwa muuaji…?’ nikauliza

‘Sijasema hivyo, na wala haijagundulikana hivyo,…na hawezi kufanya kosa hilo.. lakini ngoja nilifanyie kazi, nipe muda,…’akasema

‘Nauliza hivi, kwa hisia zako mpaka hapo anaweza akawa ndiye muuaji..?’ nikauliza na huyo jamaa akaanza kuondoka, baada ya kutikisa kichwa tu,.. hakusema neno.


WAZO LA LEO: Dhana mbaya, au tetesi zisizo kuwa na uhakika, zaweza kukushinikiza kufanya jambo lisilo faa, tuweni makini sana na dhana, au mambo ya kusikia, hasa atika dunia hii ya utandawazi, ukisikia jambo, au kusoma jambo, lihakiki kwanza ukweli wake, kabla hujasema neno, au kabla hujaamini ukweli wake, fanya uchunguzi kwanza, ili kujiaminisha, usikimbilie kushutumu au kutoa kauli zenye kuumiza, kulaani au kuhukumu watu wengine.

Tukumbukeni ulimi na kalamu(mitandao) inaweza kuwa ni chanzo cha fitina mbaya kwa jamii, tuweni makini sana kwa hili, siku ya hukumu kila kitu tutaulizwa, na kwanini tuwe sababu ya kuumiza wengine,..maandishi tu yaweza kuua, yanaweza kutesa nafasi ya mtu na huwezi kujua ni namna gani mtu huyo ataumia, mauimvu thamani yake ni kubwa sana, utawezaje kuilipa hiyo. 

Tumuombe mola wetu atusamehe na atupe hekima ya kuandika membo yenye maana kwa jamii..!
Ni mimi: emu-three

No comments :