Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Monday, January 1, 2018

MKUKI KWA NGURUWE-48


Mtoto wa marehemu alionekana mtu mwema kwangu…, na alikuwa tayari kuniambia mengi ambayo huenda yangelifanikisha malengo yangu, ya kutaka kujua ni kitu gani kinachoendelea, kitu gani kilichoweza kumbadilisha mume kiasi hicho..na je ni kweli ana mtoto nje ya ndoa..huo kwangu ungelikuwa ni ushahidi mkubwa sana...tatizo huyu mtoto wa marehemu akatoa sharti ambalo lilinipa wakati mgumu kulikubali,

Sio kwamba simpendi mume wangu, sio kwamba…simuamini, lakini kama ni kweli kayaafanya hayo ninayoyasikia, na kavunja mkataba, je haiwezi ikawa ndio njia, na sababu ya kutenda mengine makubwa zaidi ya hayo.....na je nikikubaliana naye si ndio sababu ya kupoteza mali na  juhudi zangu zote, je wazazi watanielewa kweli….

Nataka umsikilize mume wako..mkubaliane naye..mkisha kubaliana naye , mkawa kitu kimoja,basi sisi tutajitoa kabisa kwenye huo mkataba ulioandaliwa, mkataba huo ulionyesha kuwa baba ana hisa kwenye kampuni zako, ...’

‘Naweza kuonana na mama yako.....?’ nilimuomba hivyo..akili ikiwa imechanganywa na sharti hilo....

Endelea na kisa chetu.......

 Mara mume wangu akaja na gari lake, na ndani ya hilo gari alikuwepo mtu mwingine alikuwa ni wakili wake, walifika na hawakutaka hata kutusalimia, wakaingia ndani,..na mimi sikutaka kuwafuata, japokuwa ni adabu mgeni alifika umkaribishe, lakini kwa hali ilivyokuwa, ..sikujali tena….

‘Mume wako anaonekana hayupo vizuri…’akasema

‘Ni kawaida ..nahisi ni majukumu ya kazini kwake, ila sijui kwanini kamleta huyo wakili hapa nyumbani, ..kama watanihitajia wataniita..’nikasema

‘Yah….basi…kama haupo tayari, mama anaweza kuja wakati mwingine..’akasema

‘Kwanini, …nipo tayari,..hao wana mazungumzo yao, hayawezi kuzuia hili, kama wangenihitajia wangeniambia..si umeona..hawakutaka hata kusalimia, ina maana wana mazungumzo yao binafsi…’nikasema

‘Sawa…kiukweli mama, atashukuru sana kuongea na wewe, kwani hata yeye alikuwa na hamu sana ya kuonana na wewe, lakini kweney haya, yeye hana zaidi ya kuamua, zaidi ya yote ananitegemea mimi, yeye ni muwekezaji tu wa huko kijijini ...’akasema.

‘Kwanini alitaka kuonana na mimi, ni kuhusu mambo hayo hayo…?’ nikamuuliza

‘Pamoja na hayo yaliyotokea, yeye alishasikia sifa zako, za uchapa kazi wako, na kwa vile yeye ni mjasiriamali, alikuwa na hamu sana ya kuonana na mtu kama wewe, ajifunze mengi kutoka kwako, na ni muongeaji, atakusimulia mengi ambayo hata hukuyaka kuyafahamu, uwe mvumilivu tu...’akasema.

‘Kwani mama yako huko kijijini anafanya kazi gani hasa?’ nikamuuliza

‘Amejiajiri, ana miradi yake, ni mmoja wa viongozi wa akina mama, na hamu yake kubwa ni kuja kuwekeza hapa Dar kama itawezekana, lakini sio rahisi kama ujuavyo, gharama, masomo …, lakini hiyo ni mipango ya baadaye...’akasema.

‘Nahisi kwa mtizamo wangu, mumepanga kufanya hivyo kwa urithi wa baba yako, au sio..na baba yako ana vitega uchumi vingi, nasikia ana nyumba zaidi ya tano, .....?’nikauliza.

‘Nyumba zote tumepiga mnada, kwa ajili ya kulipa watu, waliopata madhara kutokana na mambo yake, ...sisi kama sisi, hatutaki chochote kutoka kwake,mali zake na miradi yake, kwetu sio muhimu, muhimu ni kulisafisha jina lake ili mungu amsamehe makosa yake,..’akasema.

‘Mnaonekana hamtaki ubaya wa baba yenu uwangilie na nyie au ni mbinu tu za kuataka kunihadaa, kiukweli mimi siwaamini, nikuambie ukweli kutoka moyoni mwangu, yaliyonikuta…yamenipa fundisho?’ nikauliza

‘Ndivyo tunavyotaka, lakini watu wengine wanaonekana kutokutuamini, sioni ajabu na wewe ukisema hivyo, lakini dhamira yetu ipo pale pale, hata kama hamtatuamini sisi tutafanya yale tunayoona ni sahihi, tukimaliza hayo, basi wale wenye nia njema na sisi watatuamini tu...’akasema

‘Mimi sina ubaya na nyie, kama kweli mna nia hiyo njema, ila sitaki mtu kuniingilia kwenye mambo yangu, ....baba yenu alianza hivyo, akajitahidi, na nilimkanya sana, bado hakuchoka, akatafuta mbinu mpaka akaweza kuingia kwenye mambo yangu hata bila ya mimi kufahamu..kama kweli mna nia njema mumeliona hilo, lakini nina iamni kuwa sio yeye, kuna mtu anamtumia…’nikamwambia.

‘Hayo mimi siyaamini sana, kuwa kuna mwanasiasa anamtumia, hapana,..mimi namfahamu baba, ni hulka yake, sawa anaweza kuwa anatumiwa, lakini yeye si ana akili….sijui lakini, maana huko mimi sija..paangalia sana..’akasema

‘Sawa pamoja na sharti lako hilo, ambalo mimi kwangu ni gumu, na mimi nina sharti langu, kama tutakubaliana, basi nitajua na nyie mpo na nia njema,…’nikasema

‘Sharti gani,…niambie tu , maana nia yetu ni kujenga…’akasema

‘Ili kweli niwaone kuwa hampo nyuma yake, na hamna nia njema, nawataka kwanza, nipate mkataba wangu, upo mkataba wangu wa asili kati yangu na mume wangu, baba yako aliuchukua, akaugushi na kutengeneza mkataba huo ambao mnao sasa…yeye aliyeubadili, na najua kabisa anao, ule wa asili, sasa nipeni huo, ....’nikasema na yeye akanikatiza kwa kusema;

‘Sisi hatujui lolote kuhusu mkataba wenu wa asili, na hatuna haja nao,  sisi mkataba tulioupata ambao hata wakili wetu anaufanyia kazo ndio huo, unaoonyesha  kuwepo kwa hisa za baba kwenye kampuni zenu, na ndio maana kwanza tulitaka kulithibitisha hilo, …’akasema

‘Mtathibitishaje, kwasababu kulithibitisha hilo ni kuwaona wahusika, je mumelifanya hilo…?’ nikamuuliza

‘Ndio…tumeongea na mume wako, amelithibitisha hilo...ila alisema kuwa hiyo ya umiliki wa hisa zaidi ya nusu, ya hisa, haikuwa ni hiari yake, ..kulikuwa na shinikizo fulani kwake, juu ya uwezo wake,, ila yeye alikubali tu ili mambo yaishe..na tukamuuliza ni shinikizo gani..’akasema.

‘Je yeye aliweza kuwaambia  ni kutokana na shinikizo gani?’ nikamuuliza

‘Hakutaka kusema ni shinikizo gani, lakini kwa vile tunamfahamu baba, kuwa akiwa anatafuta kitu, hasa mali, hajali aliyepo mbele yake, hatukutegemea kuwa watafikia hatua ya kushinikizana kiasi hicho, kwani haiingii akilini, mume wako akubali kumpa nusu ya hisa baba, kwa sababu ya deni, na ni kweli madeni yapo..kuna hati hizo,..lakini kwanini kuwe na shinikio..madeni ni madeni au sio…sasa ni nini, sisi hatukutaka kumlazimisha mume wake atuambie...’akasema.

‘Wewe hukugundua ni kitu gani, si ulisema ulifanya uchunguzi wako au sio…?’ nikamuuliza.

‘Hapana, sisi hatukutaka kuingilia huko kwa undani zaidi, ili iweje, kwani tunataak nini, …mmh, mimi naona yale niliyotaka kukuambia kwa sasa yanatosha, na kwa vile unataka kuongea na mama, ngoja nikamuite, muongee naye, nitamsubiria kwenye gari...na mume wako naona anaongea na wakili wake, sijui watanihitajia au la..nisingelipenda kuongea naye kwa leo…’akasema

‘Ina maana mumekuja na mama yako kumbe mbona hukuingia naye..yupo wapi…!?’ nikamuuliza kwa mshangao.

‘Tulikuwa naye, alikuwa na mambo yake, nikamwambia napitia kwako kwanza kujaribu kama utakubali kuongea na mimi, na yeye akawa anawasiliana na wateja wake kwenye simu, nikamuacha nje kwenye gari, yeye muda wote ni kuongea an simu, si unajua ujasiriamali ulivyo...’akasema

‘Sawa nitafurahi nikiongea naye, na samahani sana, kama sitaweza kukubaliana na ombi lenu, nalisema hili mapema, uelewe msimamo wangu, muhimu ni mkataba wangu wa awali, huo ndio utakuwa ufunguo wa makubaliano mengine bila huo, sizani kama tutaweza kukaa meza moja na mume wangu...’nikasema.

‘Hamna shada, ..nimefurahi sana kuongea na wewe nahii iwe ni mwanzo tu wa mazunguzmo yetu, na nina imani tutashirikiana kulimaliza hili jambo…na kama upo huo mkataba mwingine, kwanini usitolewe..usijali tutalimaliza hilo…haya ngoja mimi nikamuite mama aje muongee naye..’akasema na kusimama, tukashikana mkono, na akaondoka na kuniacha nikiwa nimesimama nikimwangalia anavyoondoka.

**********

Mke wa marehemu alikuwa wale akina mama wahangaikaji, wake wa shoka, hata jinsi alivyokuwa akitembea kuja pale nilipokaa alionekana ,mama mchapakazi kweli,...mwendo wake sio ule wa kike kike wa kutembea kimikogo, anatembea kama mwanajeshi

Alipofika pale nilipokaa mimi nikasimama kwa adabu na kwanza , akasimama hatua chache kutoka pale niliposimama, kwanza akaniangalia kama ananikagua, halafu akanisogelea tukakumbatiana, na kusalimiana.

‘Siamini kama ni wewe..’akasema

‘Kwa vipi dada...?’ nikamuuliza

‘Unafahamu, nimeziona  picha zako kwenye magazeti tu, kwenye majirida mbali mbali yakitangaza biashara zako, ..lakini unavyoonekana kwenye picha, sio sawa na nilivyokuona leo, leo upo kihalisia zaidi...’akasema

‘Kwani leo nipo vipi na huko kwenye magazeti naonekana vipi?’ nikamuuliza kwa mshangao kidogo

‘Tuyaache hayo, maana sisi akina mama tukikutana mengi tutakayoanza kuzungumzia,ni  mavazi, muonekano , sura, hata tutasahau jambo muhimu, na majukumu ya kila siku, mimi siku hizi sitaki kupoteza muda tena, na tangu nije hapa Dar, naona napoteza muda wangu bure tu na mambo yasiyonisaidia kitu...’akasema huku akikaa kwenye kiti.

Akaletewa kinywaji, na matunda…akapiga mafundo mawili, halafu akainua uso na kuniangalia, akasema;

‘Haya niambie kulikoni, hivi Samahani kidogo, hivi wewe na mume wako mna matatizo gani?’ akakimbilia kuniuliza hilo swali. Na kunifanya niingiwe ni tahayari kidogo

‘Mhh, kwanini…oh, kwanza nikupe pole za msiba wa mumeo,maana hatujaweza kukutana kwa sababu ya haya mambo yanayoendelea kwa sasa, pili sio kweli kama watu wanavyodai kuwa eti mimi ndiye nimemuua mume wako…, kwanini mimi nimuue mume wako..’nikasema.

‘Ni kweli kibinadamu, hisia hizo zipo, japokuwa mimi na mume wangu tulikuwa mbali sana, huwezi amini hilo, nimeishi kama sina mume,   lakini ki ndoa yeye ni mume wangu eeh…,siwezi kumkataa hadi kesho, japokuwa sasa ni marehemu..ila hutaamini yeye, kwa kauli yake, alishanifanya mimi sio mke wake....inasikitisha…’hapo akatulia kidogo.

‘Kwahiyo mlishatalikiana au..?’ nikamuuliza

‘Hamna talaka,..mimi sikukubaliana na hilo, …, kwahiyo bado alikuwa ni mume wangu, ndio maana sasa nimepewa cheo cha mjane, na hata kwenye mirathi yake sikuamini,kuona na mimi nipo kwenye orodha ya warithi,…ni ajabu kabisa, alikumbuka kuniweka nahisi hili kalifanya baade sana, sijui ni nani kamshawishi kufanya hivyo..hata hivyo kinafsi yangu, sikutaka chochote kutoka kwake,…mengine tuseme yote ni mapenzi ya mungu..’akasema akionyesha huzuni.

‘Je wewe ulikuwa ukimpenda mume wako?’ nikajikuta nikimuuliza hivyo.

‘Sana tu...huwezi amini, mimi nilikuwa nampenda sana mume wangu, na nikuambie ukweli,..hili watu hawalifahamu na hata mume wangu akitoa kauli zake hizo za kuwa hanitambui kama mke wake..alikuwa akisema hivyo akiwa kalewa tu…kuwa  mimi ndiye niliyemtaka yeye…awe mume wangu...’akasema na kunifanya niingiwe na hamu ya kuyafahamu maisha yao.

‘Hebu niambie ina maana wewe ndiye uliyemtongoza mume wako…au kwanini alikuwa akisema hivyo…, nisamehe kwa kuuliza haya, maana imenipa hamasa tu ya kufahamu…?’nikamuuliza

‘Hahaha, ndio hivyo, siwezi kulipinga hivyo..lakini sio kwamba alikuwa hanipendi, kihivyo, hapana, kipindi hicho tulikuwa kwenye ushindani wa kumpata yeye, unajua tena kijijini, na sisi tulijiona wasomi fulani..hivi, tukiwa darasa la sita, mwili na sura vilitudanganya…’akatabasamu.

‘Kulikuwa na kundi la mabint warembo wa hapo shuleni na kijini, nikiwemo mimi..unasikia…sasa, unajua tena, naongea haya..aah....tulikuwa mabinti watatu, warembo…kila mmoja anataka yeye ndiye ampate huyo mwanaume, kipindi hicho yeye ni kijana mtanashari eeh, na ana majigambo fulani, kiingereza mdomoni hakimtoki, ..’akatulia.

‘Mrembo..?’ nikauliza na yeye akacheka, halafu akasema

‘Kijijini bwana,..mwanaume akionekana msomi, kiingereza kingi…si unajua tena, huyu jamaa alikuwa msomo, kiukweli…na …ndio hivyo..basi bwana, sisi ni mabinti wadogo warembo wa hapo kijijini...ilikuwa hapatoshi, kushindana ni nani atachukuliwa na huyo msomo,..hahaha, ..lakini ndio hivyo, mwisho wa siku nikasimama mimi kidedea, ..tukawa wapenzi, japokuwa ni upenzi wa kijijini...’akasema.

‘Hongera, ...’nikasema

‘Unafahamu, mimi tangu nikiwa mtoto, nililelewa kwa shida, sikuwahi kupata raha, ...wazazi wangu hawakunidekeza, hawakuwa na kitu, kwahiyo ilikuwa ni maisha ya suluba, ..kula na kulala kwa shida, ..unajua maisha tena ya kijijini..basi ikatokea nikamfahamu huyo mwanaume…, kiajabu ajabu tu..’akasema huku akitabasamu.

‘Yeye nakumbuka tangu nimfahamu, alikuwa ni mtu wa kusoma vitabu tu...hata alipokuja huku mjini, na baaadaye akawa anafika fika, alikuwa muda mwingi ukimuona  kashikilia kitabu, hivi vitabu vya hadithi, alikuwa anapenda sana kusoma vitabu vya kizungu, nakumbuka kuna vitabu vyake, aliwahi kunionyesha, hata mimi baadaye nilipojiendeleza nimekuwa nikivisoma, hivi vinaitwa, eeh, Jemsi Hadley Chase, na Peri Masoni, nahisi ndio maana akajikita kwenye uanasheria...’akasema.

‘Siku ya kwanza kukutana kwetu, ilikuwa kama vile wanavyoonyesha kwenye sinema, maana ilikuwa ni kwenye shughuli, mimi nilikuwa kasichana, na bahati mbaya mwili wangu ulikuwa haraka, ni baadhi ya wasichana kijijini kwetu tuliokuwa kimwili haraka, ...ilikuwa siku hiyo nafanya usafi kuwaandalia wageni, mara wakati nawapelekea watu maji ya kunywa, nikagongana naye, ..akadondosha kitabu chake, kikalowana maji...maana kulikuwa na maji maji sakafuni, mimi nikakiokota na kukifuta kwa kitambaa changu cha mtandio. Picha ndio ilianzia hapo…

Nilipomaliza nikamkabidhi kitabu chake, kumbe mwenzangu wakati wote huo nahangaika kukifuta kile kitabu, alikuwa akinitizama, na hata namkabidhi hicho kitabu, bado alikuwa akinitizama tu machoni....hapo mimi bado mbichi nasoma, vititi saa sita..’akasema.

Nilishamuona kabla, na tulikuwa tukimuongelea shuleni, wasichana na tama zetu…lakini hilo la kukutana kihivyo, ilikuwa siku hiyo, na ndio nikaweza kujuana naye, na kuanza kujenga urafiki, na urafiki ukatibua nyongo…’akatulia

‘Kwa vipi…?’ nikauliza

‘Alinibebesha mimba..na kunifanya nifukuzwe nyumbani kwa wazazi wangu..’akasema

‘Mungu wangu…’nikasema hivyo

‘Nilikwenda kuishi kwa bibi, mpaka nikajifungua...hebu fikiria, darasa la sita enzi hizo, unabebeshwa mimba,hata darasa la saba sikumaliza, ingawaje baadaye nikijisomesha, kujiendeleza,…usinione hivi , nilijisomesha hadi sekondari, kiaina aina.

‘Basi aliponipa mimba, wazazi wangu wakafahamu, palikuwa hapatoshi jamaa huyo akakimbilia mjini, sio kweli kuwa alikuja huku mjini kwa ajili ya masomo, hapana,..ni lugha ya kudanganya , kuficha ukweli, yeye alikimbia kuogopa balaa la wazazi wangu....’akasema

‘Lakini umesema yeye anasema ni wewe ndiye uliyemtongoza, naona hapo inaonyesha yeye alikupenda pendo la awali,...au sio, lile pendo watu mnaonana hapo hapo, kunajengeka hisia za kupendana au sio...’nikasema.

‘Baada ya pale,…kwenye shughuli… siunajau tena mambo ya shule, nikawahadithia wenzangu, basi, marafiki zangu kila mmoja akataka ampate yeye, na kila mmoja akawa anajibaragua kwake, kijinsi ajuavyo yeye, mimi ikaniuma sana, wivu tena… ina maana kuwaelezea wenzangu ndio imekuwa nongwa..basi nikaona nisilaze damu, ...’akasema.

‘Nilipoona wenzangu wanambana sana huyo kijana, kila mara wapo naye, nikaamua kumwambia ukweli, ilikuwa ni kazi nzito kujielezea si unajua tena wasichana…, lakini mwisho wa siku alikubali kuwa hata yeye ananipenda sana tangu siku ile kwenye shughuli, ya kudondosha kitabu,...mambo yakakolea sasa kuanzia hapo, ikawa mimi na yeye, nikawa nachapwa nyumbani kwa ajili yake, sikusikia,...haniambii  mtu...na asiyesikia la mkuu huvunjika mguu...ikatokea kama mchezo tu, mimba hiyo...’akatulia.

‘Kiukweli mimba ilikuwa ni bahati mbaya, maana pamoja na urafiki wetu huo, hatukuwa na mambo ya kisasa, haya ya kimjini mjini, hapana...ilikuwa ni kukaa pamoja kuongea, kutaniana, kukimbizana,...ila siku hiyo sikumbuki ni kitu gani kilitokea, na tukajikuta tumefanya jambo ambalo ndilo lilimleta huyu mtoto wangu duniani, mliyetoka kuongea naye....’akatulia kidogo.

‘Nilitenda hilo mara moja, na ikawa ndio tiketi ya shida, ...shida kweli...na nikuambie ukweli, mtoto huyo alinitesa kweli kweli…ilikuwa ni mimba ya fundisho, na sikutaka kuzaa tena..licha ya mimba yake, na hata malezi yake…, nilimlea kwa shida sana, huwezi amini. Siwezi hata kukusimulia, ....hata hivyo.. mungu hakunitupa mja wake, mateso hayo yalinijenga..nikawa mke-dume, aliyejengeka kijasiri, unaniona nilivyo hata kutembea kwangu..na nilitaka mtoto wangu awe hivyo hivyo, sikupenda awe mtoto wa ovyo ovyo, nilijitahidi kumlea kihali niliyoona ni njema kwake..’akasema.

‘Ina maana ulipomzaa huyo mtoto, hukupata msaada kutoka kwa mume wako?’ nikamuuliza.

‘Msaada gani, angelipata wapi pesa za kunisaidia wakati huo, wakati huo wa awali, yeye mwenyewe alikuwa kula kulala..hana mbele wala nyuma, na aliponipa mimba akakimbilia mjini kujificha, hakuonekana, hadi nilipojifungua na alifika kwa mara ya kwanza mtoto anatembea,hamjui ,.....na sikutaka hata kuongea naye..’akasema.

‘Ikawaje sasa mpaka mkafunga ndoa?’ nikamuuliza

‘Wazazi wangu waliweka shinikizo..kuwa ni lazima anioe...huoni , hata nikiwa naye naonekana mimi ni mkubwa kuliko yeye, lakini ni kwasababu ya maisha, na mwanamke mara nyingi anaonekana mkubwa, kama mkiwa umri karibu sawa..sisi wanawake tunakuwa haraka haraka, na ukizaa ndio basi tena...’akasema.

‘Basi ikabidi kweli anioe, kuepusha shari,  japokuwa hakutaka, alishaniona sifai tena..japokuwa mimi nilikuwa nampenda kweli kweli,...hata tulipoona hatukuweza kuishi kwa upendo, ilionekana kama ndoa ya lazima, akawa ananinyanyasa, ...yaani sikuwa na raha na yeye, na hakutaka hata kutembea na mimi, yaani kutembee mitaani kama mke na mume, haikuwahi kutokea....aliniona simfai, mwanamke wa kijijini, mshamba,  asiyejua kujiremba...na yeye keshakulia mjini, anawafahamu warembo wa mjini, eeh..’akasema akibenua mdomo kwa dharau.

‘Basi bwana, ..mimi nikawa mama wa kijijini, sikujali, bado nilimtambua yeye kama mume wangu, yeye akawa anishi mjini , mimi kijijini, sikujali, nikawa napigika kijijini, maisha ya shida, anakuja mara moja au mbili kwa mwaka, ..hanitumii pesa, akibahatisha ni mara moja kwa miezi mitatu, ni pesa yenyewe pesa basi, nikawa nahangaika kivyangu kumlea mwanangu, sikujali na wala sikukata tamaa...’akasema.

‘Nikawa naletewa taarifa za ajabu ajabu kutoka huko mjini, kuwa mume wangu ana wanawake, sio mwanamke, ana wanawake, anawabadili kama nguo...ikafika mahali nikamuuliza, na kumshitaki kwa wazee, nilivyosikia, hutaamini kibao kiligeukia kwangu, kuwa mimi nasikiliza majungu, ni wapi nilimuona na hawo wanawake,...iliniuma sana, kwani mmoja wa wanawake zake, namfahamu, alikuja kuniambia yeye mwenyewe, kuwa mimi nitabakia huko kijijini yeye atakuwa akistarehe na huyo mume wangu, eti sababu mimi nilimuibia yeye...’akasema.

‘Mwanzoni nilipata shida sana, na ikafikia hatua nikaamua kumwendea huko mjini, ili nikapate huo ushahidi wanaoutaka wazee, najuta kwanini nilifanya hivyo, maana nilizalilika,....sitasahau, kwani siku hiyo nikiwa nimevalia zile nguo zetu, kwetu kijijini niliziona za maana , gauni refu...mikono mirefu, kitambaa kichwani,...nikaingia dar, ilikuwa ni mara ya tatu, nilishawahi kufika kabla.

‘Nilikuwa nafahamu wapi mume wangu huyo anaishi, nikafika bila hata ya yeye kufahamu, ilikuwa saa kumi kumi hivi, nikafika nyumbani kwake, ...kulikuwa na mvua mvua inaanza kunyesha, nikafike eneo alikopanga chumba, alikuwa na chumba kimoja, maisha muda huo hayajamnyookea,…anasoma na kufanya kazi, nikagonga mlango , mara akatokea mwanamke na khanga moja kiunoni, akafungua mlango, huku akisema kwa nyodo.

‘Hivi nani hawa wanaharibuu starehe za wenzao, ni Malaya gani wewe...’akasema huku akinifungulia mlango, na kuniona mimi, akashikwa na butwaa, maana ananifahamu, ndio huyo aliyeniambia, kuwa mimi ndiye nilimuibia mchumba wake..kiukweli, yeye alionekana mrembo kwa maisha aliyokuwa akiishi ya mjini, mimi nimeshachakaa na maisha magumu ya kijijini, na kuzaa .

‘Ni wewe....?’ akauliza kwanza kwa aibu lakini baadaye akabadilika na kugeuka kuangalia ndani, na kusema kwa sauti iliyojaa dharau;

‘Haya wewe bwana, kuna mgeni wako nje..’akasema na kuingia ndani, na mimi nikaingia na kumkuta mume wangu akiwa na taulo kiunoni, kakaa kwenye sofa, akageuka na kuniona, hakuonyesha ile dalili ya kushituka akasema;

‘Wewe mwanamke ni nani kakuambia uje bila taarifa, bila ya kibali changu, nataka nikiinuka hapa haupo ..rudi huko, huko ulipotoka..’akasema huku haniangalii usoni...’

‘Mume wangu niende wapi, ..wakati nimekuja kwako, ..nitapata wapi basi muda kama huu?’ nikamuuliza kwa adabu zile za kijijini, huku moyo unaniuma kweli.

‘Utajua mwenyewe....kwani ni nani alikuambia uje, nilishakuambia kuwa mimi sikutaki...unang’ang’ania tu kuwa wewe ni mke wangu, hebu jiangalie wewe ulivyo, una hadhi gani, na shepu gani ya kuwa mke wangu, ...huoni aibu, eti kusema `mume wangu’, sikiliza rudi huko huko ulipotoka,unasikia...’akasema na kusimama,

Mimi sikusogea nikasimama pale pale, na yeye bila kujali kuwa kavaa taulo, akaanza kunisukumia nje huku yule mwanamke wake, akiniangalia kwa nyodo kashikilia kiuno...sikuona taabu, awali nikapambana naye , lakini mwanaume ni mwanaume,…akanitoa nje..nilikaa pale nje, kibarazani hadi walipomaliza mambo yao, ...’akasema huku akitabasamu tu.

‘Ina maana hawakujali, na bado walikuwa wakiendelea na starehe zao?’ nikamuuliza.

‘Yaani tena kwa karaha, maana walijua nipo hapo nje, na mvua inanyesha..lakini kila kilichokuwa kikifanyika huko ndani, nilikuwa nakisikia, kwa dharau..ili kunionyesha kuwa mimi sina maana..’nililowana, maana kibaraza kilikuwa hakina sehemu nzuri ya kujificha, na walipomaliza starehe zako, wakatoka wakaenda bafuni kuoga, wakavalia, wakaondoka, sijui walipokwenda, nikabakia hapo hapo..nje,sijui niende wapi…nalia…nifanyeje sasa, na kuja mjini nilipanga nije kupambana na hao wanawake wanaoniibia.

‘Bahati nzuri jirani yao, akanikaribisha ndani, akanipa nguo nikabadili, akanipikia tukala, japokuwa chakula hakikushuka vyema, na huyo huyo jirani yake ndiye aliyenisaidia nauli, kesho yake asubuhi nikaondoka nikarudi nilikotoka,...hebu ona huo unyama, hata nauli hakunipa...nimesaidiwa na majirani ambao waliniambia mume wangu kila siku anakuja ni mke mwingine...na sijui kwa vipi hakupata ukimwi...’akasema huku akikunja uso.

‘Niliporudi kijijini, nikamsimulia mama yangu hayo nailiyoyaona, akasema, hayo ndio yo niliyoyataka, waliniambia sikusikia, ni kweli , walinisema sana, kipindi hicho, nilipoanza mahusiano na marehemu, wazazi wangu walichapa sana, lakini sikuwasikia, na hayo yaliyokuja kutokea nilikiri kuwa ilikuwa ni dhambi zangu ndizo ziliandama ngoja nipatilizwe, ...nilitubu sana, nililia sana, lakini itasaidia nini…’akasema.

‘Niliishi kijijini kwa shida, hadi nilipokutana na huyo mume wako....’akasema

‘Na mume wangu..!! ?’ nikauliza nikianza kuwa na hamasa zaidi kwani huko ndipo nilipataka kufahamu ukweli zaidi wa mume wangu.

‘Ndio na …mume wako,…’akasema

‘Mkawa….eeh..’nikasema hivyo

‘Hahaha…mume wako kwangu namuona kama mdogo wangu, lakini alinionea huruma sana, kwani alikuwa akiniona ninavyoteseka, yeye alikuwa akihangaika na shughuli zake anapita kwetu ananiachia chochote,, huwa alikuwa akiniita shemeji....basi ndivyo tulivyozoeana. Hakuwahi kupita hapo bila kuniacha kitu.

‘Kuna kipindi niliumwa sana...karibu ya kufa, hatukuwa na hata senti nyumbani, sina pesa ya kununua dawa, kwani nikwenda hospitalini na kuandikiwa dawa za kununua, ...hatuna pesa, na tatizo hilo lilikuwa kubwa, hadi nikaambiwa nikafanyiwe upasuaji, ..nipelekwe mjini, sina pesa, wazazi hawana pesa , na mume wangu alipoambiwa hakujali..alitaka nife tu...’akatulia.

‘Namshukuru sana mume wako, nafahamu kipindi hicho, alikuwa hajaku-oa...kama sikosei, akauza mbuzi wake, akapata pesa, na kuzileta nyumbani, hatukuamini, akasema amekuja kunisaidia ili nikatibiwe...na kweli nikapelekwa mjini nikafanyiwa upasuaji, nikatibiwa nikapona..sitamsahau mume wako...’akasema.

‘Je alifanya hivyo kwa sababu gani hasa?’ nikamuuliza

‘Yeye, alisema alifanya hivyo, kwa vile mume wangu ni rafiki yake ,mume wangu  alikuwa akimfundisha fundisha ufundi wa magari, ..udereva,..unafahamu mambo ya kijijini, basi wakaivana, sijui zaidi ya hapo ilitokeaje wakaivana kiasi hicho, kwahiyo yeye alinitambua kama shemeji , mke wa rafiki yake, akanijali kihivyo.....na ujirani mwema tu...’akasema.

‘Kwahiyo kwetu sisi , kama familia, tunamthamini sana mume wako, ni mtu mwema sana, mume wako ana roho nzuri , uliza huko kijijini, alipenda kuwasaidia sana watu,..sio mimi tu, ..yeye alikuwa na tabia yake ya kupenda kusaidia watu, .. japokuwa familia yao ina tabia ambayo wengi wanaiona sio nzuri, baba yale ni mlevi kupindukia, na mama yake akawa hivyo hivyo....basi ni familia ya shida, lakini yeye akawa anajibidisha na maisha yake, kuhangaika kivyake..hadi hapo mlipokutana naye...’akasema.

‘Mhh, kweli umenifungua masikio, hayo yaliyokukuta ni makubwa, mimi niliona nipo kwenye mitihani, lakini kumbe wapo wengine wanakutana na mitihani zaidi ya unavyowazia, wewe ya kwako ilikuwa zaidi, sasa ikawaje, maana muda umekwenda, kuna mambo ulitaka kuongea na mimi na mimi nataka kujua…eeh..?’ nikamuuliza. Na sote tukageuka kuangalia kule mlango mwa nyumba yangu, kulikuwa na jambo…

‘Sasa ikawaje…oh, namuona mume wako anatoka, nilionana naye hapo nje wakati anaingia, tukaongea kidogo…ana haraka zake…?’ akasema,na ni wakati huo mume wangu alikuwa akitoka na wakili wake, na aligeuka akatuona ni kama vile ndio anatuona kwa mara ya kwanza, ikabidi sasa aje pale tulipokaa…..

....NB: Nimejitolea leo kuleta sehemu hii…Ni kisa mkasa, lakini kwa huyu mama kuna mengi ya kujifunza, tutakuja kuona ilikuwaje kati ya mama huyu na mume wake, na kwanini alifika huku mjini, je inaweza ikawa njia ya kumfanya mdada abadili nia yake na kumsamehe mume wake..tuzidi kuwemo..?


WAZO LA LEO: Maisha yana mitihani yake, ukiona kwako ni kugumu, ujue kuwa kuna wenzako kwao ni kugumu mara mbili zaidi yako, ukipatwa na mitihani, ujue kuna wengine mitihani hiyo ni mazoezi tu ya nyumbani(homework), kwahiyo ili uone uhalisia waangalie hawa waliopo chini yako, ambao wanataabika zaidi yako.


Na ili uvuke huo mtihani waangalia walipo juu yako, jifunze kutoka kwao,uwe na wivu wa maendeleo...usikate tamaa, pambana, lakini kwenye njia iliyo sahihi, ukijua kuwa wewe sio wa kwanza kupata mitihani kama hiyo, wapo waliopata mitihani hiyo na wakaishinda, kwanini wewe usiweze...kumbuka jambo moja, kila kitu kila jambo lina ugumu wake, lakini  baada ya dhiki, mara nyingi huwa ni faraja, hasa kwa wale wenye kuvumilia na kujibidisha kwenye shughuli zao.., huku wakimtegemea mola wao.
Ni mimi: emu-three

No comments :