Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Friday, December 22, 2017

MKUKI KWA NGURUWE-45


‘Sikiliza nikuambie sasa, eeh,..mimi sikufahamu au kuukariri mkataba  kabla, kwahiyo sikuwa makini kwa kipengele kwa kipengele…mengi nilikuwa nafanya kuhakikisha nakufurahisha, eeh kwasababu nakupenda mke wangu.…’akasema
‘Watu wakawa wana..fikia hatua sasa hata ya kuniuliza, umeoa au umeolewa, unaona eeh vitu kama hivyo, mimi sikujali,..sasa matatizo yakaanza, kuna mambo mengine, nitakuja kukuelezea baadae, ..’akatulia

‘Marehemu nikakutana naye ndiye akanifungua macho, aliniuliza tatizo ni nini, awali sikumuambia, baadae kutokana na hayo matatizo …unajua, ikabidi nimuambie, kuwa kuna mkataba, na mkataba umekuwa ni mnyororo kwangu,..’ hapo akakaa kidogo, baadae akasema

‘Akaomba aupitie,nikampa, samahani kwa hilo…akausoma , akasema, mbona kila kitu kipo sawa, ni wewe tu hutimizi wajibu wako, unaogopa nini, hiki kipengele hapa kimekupa mamlaka, ..ilikuwa kama ndio naanza kukiona,…unaonaeeh..’akasema

‘Sasa kama ningelikaa kimia, huo mkataba ukafika kwa  wazazi wako, hicho kipengele sikuwa nimekiona eeh cha mamlaka ya mume, na vingine vingine,lakinikwa leo ni hiki cha mamlaka… mimi nina uhakika wazazi wako wangelikimbilia kuniwajibisha, na hapo ndoa ingelivunjika tu,..’akasema

Nilimuangalia tu, na aliponitupia jicho na kuiona hiyo hali niliyokuwa nayo usoni, haraka akajibaragua na kama anatabasamu hivi, halafu akasema;

‘Kwahiyo mke wangu, sasa mambo yote yapo shwari, usiwe na wasiwasi kabisa, sasa nitajitahidi kutimiza wajibu wangu, ..nimeshajielewa, na makosa yaliyopita ..si ndwele, tugange yajayo, na nachukua fursa hii kukushukuru sana wewe mke wangu,  uliona mbali sana…hata Marehem alikusifia kwa hilo…’akasema

‘Hahaha, mume wangu usinifanye mimi ni mjinga kiasi hicho, kuwa mumeweza kubadili mkataba, na mumetengeza mkataba mwingine ambao ndio huo unakufanya ujiamini saana..’nikasema

‘Kwanini unasema hivyo mke wangu..?’ akauliza

‘Hebu nijibu swali langu , ni kwanini mlibadili huo mkataba…najua mliubadili na marehemu kwa masilahi fulani…, sasa nataka kauli yako wewe, ni kwanini ukafanya hivyo, maana unaongea kama vile..hata sikuelewi…’nikasema sasa kwa ukali.

‘Ninachosema mke wangu ni hivi, kama wazazi wako eeh...wangeliuchukua ule mkataba, kabla ya mimi sijaupitia vyema, wangeliweza kutoa maamuzi na mimi nikakubalia tu, maana sikuwa na uelewa …maana wangeliangalia kosa, na adhabu ya kosa, lakini je vipengele vingine, vya kutulinda, mimi na wewe , je kipengele cha mamlaka yangu...’akasema.

‘Kwahiyo wewe ulikwenda kwa marehemu ukamwambia umefanya kosa, na mkataba unasema ukifanya kosa adhabu yake ni hivi, sasa ufanyeje, si ndio hivyo, ukampa mkataba, yeye akafany alichofanya, akakurejeshea na kusema sasa kila kitu kipo sawa, ..mume wangu wewe hujui hilo ni kosa mnagushi mkataba halali..haya ulipofanya hivyo mlikubaliana  malipo gani sasa, maana pesa huna, ulimlipa nini..?’ nikamuuliza

‘Mke wangu sio hivyo, hebu kwanza rejesha akili yako nyuma…’akatulia kidogo, na mimi nikatulia sikusema kitu.

‘Hili la kupata ushauri kutoka kwa marehemu, ililikuwa ni kama hitimisho la mambo mengi yaliyokuwa yamejificha, huenda hata mimi sikuwa na mawazo hayo kabla, na sikuwa na uelewi wa kisheria kivile, unanielewa hapo, na sitakosea nikisema, matatizo yameanzia kwetu…sikulaumu,…wakati mwingine..inatokea, na hatuwezi kumkufuru mungu,.. labda nijilaumu mimi mwenyewe kwa kutokujua majukumu yangu...’akasema

‘Unasema….’nikasema hivyo tu

‘Kiukweli mke wangu Marehemu alikuwa rafiki yangu mkubwa sana, na mengi alikuwa akinishauri yeye, hata kabla ya hilo, na sikuwa na mtilia maanani kipindi ch aawali, niliona kama ananionea wivu,..lakini sasa yalipotokea matatizo…, ikabidi nimkumbuke…’akasema

‘Matatizo gani sasa, niambie..?’ nikamuuliza

 ‘Matatizo,….yah, ndio nikafikia kukuomba msamaha, lakini hayo nitakuja kukuambia kwa wakati muafaka, usiwe na wasiwasi mke wangu, kwanza ni kwanza, hili lililipo mbele yetu....’akasema

‘Kwahiyo sasa hivi unataka tuongelee nini hasa, hiyo kwanza ni kwanza ni nini..?’ nikamuuliza ilibidi nijishushe tu twende sawa na atakavyo yeye

‘Kuna mambo kidogo, tunahitajika kukubaliana hapa leo hii, ni muhimu sana, nataka tuyaongee, ni kuhusu mikataba tu, tukakubaliana basi kinachofuata ni utekelezaji tu...’akasema, na mimi  kwa vile sikujua anataka kuongelea jambo gani, nikasema;

‘Mhh, haya mambo gani hayo, mimi nakusikiliza wewe sasa...lakini mimi nitafurahi sana nikiusikia ukweli wote…’nikasema

‘Ukweli,…! Mke wangu usijali,..mimi nipo tayari, nitakuambia kila kitu hatu akwa hatua, sitaki nikuchanganye, lakini hili kwanza la muhimu, ambalo ni msingi wa mengine yote, na sio kubwa kihivyo, ni kukubaliana tu, na ni wajibu wangu kufanya hivyo, na wewe kunishauri, kwa vile wewe ni mke wangu..’akasema

‘Haya ongea ,..’nikasema

‘Kuna mambo kwenye mkataba yalikuwa yamekaa kimtego-tego  kwangu,…’akasema

‘Mambo gani sasa…?’ nikauliza kwa sauti mpaka akashtuka na kuniangalia machoni, halafu akasema

‘Yapo kwenye mkataba tutakuja kuyaona,lakini haina shida saana,…’akasema

‘Unaelewa ni nini maana ya mkataba, mkataba ni makubaliano ya watu wawili au zaidi au sio…sasa iweje mmoja achukue hatua ya kurekebisha mkataba uliokubalika bila ya idhini ya mwingine kwa masilahi yake…’nikauliza

‘Sio hivyo mke wangu, naona kama hujanielewa, hakuna kitu kilichobadilika, mke wangu…’akasema

‘Una uhakika hakuna kitu mumebadilisha, …usiseme uwongo mume wangu maana nitakuja kulithibitisha hilo,na nikifikia huko sheria itachukua mkondo wake,…’nikasema

‘Sheria itasimamia kwenye makubaliano yetu..au sio, haiwezi kuvuruga yale tuliokubaliana, na yapo wazi kwenye huo mkataba au sio..na mimi sijasema kuwa nitafanya kinyume cha makubaliano yetu, na kama ilitokea tutarudi kwenye kipengele cha msamaha, nilishalifanya hilo, na wewe ukanisamehe au sio, tena mbele ya mashahidi…’akasema

 ‘Kuna kipengele gani kilisema kuwa wewe kama mume unaweza kubadili mkataba bila ya mimi kuwepo, au cha kukupa mamlaka ufanye wewe uonavyo ni sahihi, bila ya mimi kuwepo, eeeh hata kama inanigusa na mimi..?’ nikauliza

‘Mke wangu kuna mambo yakitokea mimi kama mume ni lazima niwajibike…na hilo sio kwa mujibu wangu, mkataba unasema hivyo, mimi nina wajibu wa kuhakikisha familia yangu ipo salama, hebu ona mpaka watu wanafikia kuua,.. ujue watu hao hawana nia njema, sasa kama nisiposimama kiume itakuwaje…ilibidi mambo yawekwe sawa…’akasema.

‘Unaposema hivyo, mambo yawekwe sawa una maana gani hapo,?’ nikamuuliza

‘Nina maana gani eeh…ina maana mke wangu hulioni hilo, hebu jiulize ni kwanini Makabrasha akauwawa,…alichofanya yeye ni ushauri tu, na hatukuwa tumefikia mahali pa …undani zaidi, kabla hatujamalizana, kauwawa, masikini wa mungu…’akasema kiuonyonge.

‘Mume wangu upo sawa kweli wewe, mbona nakuuliza hivi unapindisha hivi upo sawa au ulikunywa kidogo leo , ulishaambiwa usinywe pombe …?’ nikamuuliza maana nilimuona anaongea sasa kama kalewa, lakini hana harufu ya pombe

‘Nipo sawa kabisa mke wangu, nafanya hivi ili unielewe, ili nikitoka hapa , mimi naenda kufanya kazi, usije kusema aah, nimekiuka mkataba, hapana…mkataba sasa ufanye kazi yake, mimi najiuliza hapo ni kwanini wakamuua Makabrasha…?’akasema


‘Kwanini unauliza hivyo, hata mimi sijui…’nikasema

‘Unaona eeh, wewe ni mke wangu , mambo kama hayo mimi ndiye nilitakiwa niwajibike, …lakini kwa pupa na tamaa za watu,  ndio ikafikia hapa,…kuna mambo yanahitajia umakini, sio jaziba, …’akasema

‘Una maana gani hapo kuwa unanishuku mimi,…  eeh mimi nimejikuta katikati ya mambo haya, na hata kushutumiwa kuwa mimi ndiye niliyemuua, wakati sijui kabisa ni nini kinachoendelea, lakini ukweli utajulikana tu…’nikasema

‘Umeonaeeh, sasa hiyo ni hatari..ina maanisha watu hao wapo tayari hata kuua, kisa ni nini, ..kwa vile kagusa kwenyewe, kwenye mali, au…labda walihis kuwa tumeingilia mambo yao hapana hatukuwa na lengo hilo, basi kama ni hivyo watakumaliza sote, next ni mimi…’akasema

‘Kwahiyo kumbe wewe kuna  watu unawashuku tayari je umeshawaambia polisi..?’ nikauliza

‘Aaah,..hiyo ni kazi yao bwana, sijaongea lolote na polisi, usiwe na wasiwasi kabisa na hilo…lakini kiuhalisia si inajionyesha, ni kwanini wamuue huyo wakili, ni kwanini…ina maana kuna sababu, na jiulize ni kwanini itokee kipindi hiki ambacho anahangaika kuyaweka mambo yetu sawa..’akasema

‘Mambo gani yetu..?’ nikamuuliza

‘Kama huo mkataba..’akasema

‘Ehee..mkataba una nini labda ambacho yeye alitaka kuweka sawa..?’ nikamuuliza

‘Yeye alishajitolea kuusimamia, kwa masilahi ya familia…unaona, hata kama ni kusimama mahalamani, ilimradi tu masilahi ya familia yetu yalindwe, na mimi nilikubali kushirikiana naye, na ndio tulikuwa kwenye mipango ya kukufafanulia hayo hatua kwa hatua, nina imani ingelimuelewa tu…sasa wamemuua..’akasema sauti kama ya kutaka kulia.

‘Kwahiyo unataka kusema kuwa kauliwa kwa vile alikuwa akihangaika kuyaweka mambo yenu sawa, kutengeza mkataba wenu wa kugushi, kwahiyo waliomuua ni hao ambao hawakubaliani na huo mkataba wenu wa kugushi, au sio..?’ nikamuuliza

‘Usiseme mkataba wenu wa kugushi, rekebisha kauli yako, huo ni mkataba wetu na wewe ndiye uliyebuni hayo, au sio, na kiukweli sio mkataba wa kugushi kabisa, niule ule mkataba, au umeshakuwa mkuki kwa nani…eeh, hapana usiwe na wasiwasi mke wangu, …na kiukweli hao wanaoupinga ni kwa mashaka yao tu, na na..ulikuwa hauwahusu au sio,…’akasema

‘Na ni nani hao…ambao mnawashuku kuwa hawatakubaliana na mkataba wenu wa kugushi,..ukisema hivyo moja kwa moja unamnyoshea mtu kidole, maana mkataba ule wa asili ulikuwa kati yangu mimi na wewe…

‘Sio swala la kushuku,..uhalisia unaonyesha..’akasema

‘Sasa ni nani, maana ukiacha wewe , mwingine kwenye mkataba huo ni wakili wetu, na mimi…kwahiyo unataka kusema nini hapo, kuwa ni mimi nimemuua Makabrasha si ndio hivyo..?’ nikamuuliza

‘Hapana, sio wewe mke wangu, wewe hauwezi kufanya hivyo, wewe ndio mimi, wewe ni familia yangu, mimi nawashuku wale wasiotaka mimi na wewe tuishi kwa furaha na amani….maadui wa ndoa yetu…’akasema

‘Akina nani hao sasa..ni, wazazi wangu au..?’ nikauliza

‘Sijawataja wao, na mimi siwezi kuwashuku wakwe zangu kihivyo, acha polisi wafanye kazi yao…na ..ni hivi mke wangu, shaka shaka ni lazima ziwepo au sio, inawezekana kabisa wakawa watu wengine tu, wakitumia mgongo wa watu tunaowafahamu, na hilo ni lazima tulifanyie kazi, tuwatafute ni akina nani hao, sisi kwa upande wetu tutakuwa tumenawa mikono au sio…’akasema

‘Sasa niambie ukweli, unataka nini sasa….maana kama hutaki kuniambia ni kwanini ukachukua maamuzi ya kubadili huo mkataba..sizani kama tutaelewana, kwa hali kama hiyo sitaweza kukuamini kamwe..?’ nikamuuliza.

*********

‘Hata mimi mume wako huniamini, hahaha, utaniamini tu, wewe ni mke wangu, huwezi kwenda kinyume na mimi, au sio, na ukweli upi basi, ndio huu ninaokuambia, tulianzia kwenye hii fitina ya mkataba, hii haikuja hivi hivi tu…lakini marehemu akaigundua, na kunionya kwa hilo, ahsante marehemu…’akasema.

‘Mume wangu utaniambia ukweli au uondoke zako..?’ nikamuuliza.

‘Mimi ni mume wako, nitakuambia ukweli wote usijali, si ndio nimeanzia hapo kwenye mkataba, kuwa hauna shaka, mimi nilikuwa sifahamu yaliyomo, sasa nimeyafahamu na ndio maana nimeanza kuufanyia kazi au..?’ akasema na kuuliza.

 ‘Sikiliza mume wangu, usije ukajidanganya na huo mkataba wa kugushi, ukajiona kuwa upo salama, huo mkataba ni wa kugushi, ni ukiukwaji wa sheria, na hilo tunaweza kulithibitisha  kisheria, kuwa huo mkataba wa sasa ni wa kugushi...hata kama kila mbinu zimetumika,… kuubadili na kusambaza nakala kila mahali husika,.. haisaidii kitu , kwani wakili aliyesimamia hiyo hayupo, ..’nikasema.

‘Hakuna kosa kwenye huo mkataba mke wangu, kila kitu kipo sawa-sawa, na sijui kwanini unauita mkataba wa kugushi, wakati ni wewe mwenyewe ulikuja na wazo hilo,iweje leo maneno yako uyapinge, au una ogopa nini, usiogope mke wangu mimi nipo ...’akasema.

‘Huo mkataba mpya mimi siutambui, maana sikushirikishwa,..kwanza ni mkataba wa nani na nani, ...nasema hivi ukinielewa nina maana gani,  na usinione mimi ni mjinga kihivyo….sasa ni hivi ili tuelewane mimi na wewe, nauhitajia ule mkataba wa mwanzo kwanza…’nikasema

‘Mkataba wa mwanzo upi tena mke wangu…?’ akauliza

‘Mume wangu usitake tubishane hapa, nikuuliza tu, kama uliona kuwa kuna marekebisho, ilikuwa ni haja gani kuhangaika hivyo, ungelianiambia tu, kuwa kuna sehemu hupendezwi nazo, basi mimi na wewe tungelikaa tuone tufanye nini au, huo ndio uungwana ...’nikasema.

‘Na mimi narudia tena kukuambia mke wangu, mimi sijui kama kuna mkataba uliogushiwa, upi huo uliogushiwa, kwani kuna mikataba mingapi, mkataba niujuao ni huo huo, na kama kuna kitu basi tutakaa tutaongea , hilo halina shaka, ila kwa leo eeh...!’akasema na kunifanya sasa nianza kukasirika, nilishaona mume wangu kadhamiria.

‘Mume wangu acha hayo maneno...kwa kauli yako ya kuzunguka zunguka, kuna muda ulisema kama wazazi wetu waneguchukua kama ulivyo, ndoa yetu ingelivunjika, je hivyo vipengele vya awali vya kuuvunja  ndoa, ni vipi na hivyo vya sasa vya kufanya isivunjike ni vipi, mume wangu nakuona kuwa mkweli tuyamalize haya mambo kwa amani,....’nikasema.

‘Mke wangu, mimi sijui mambo ya kugushi mkataba,...mimi sio mwanasheria, nitagushi vipi mkataba, na mkataba huandikwa na wanasheria, baada ya mimi na wewe kukubaliana, tulikubaliana au sio…na mwanasheria akafanya kazi yake, na ndio mkataba ninao ufahamu mimi,...’akasema.

‘Una uhakika na hayo unayoyasema…mume wangu usitake tupelekane kubaya, mimi sipo hivyo, kawaida yangu ni haki na ukweli, kwanini tusiwe hivyo mume wangu unataka nini lakini, niambie…?’ nikamuuliza na yeye kwanza akaniangalia, halafu akaangalia chini na kusema;

‘Mke wangu, mimi nina uhakika na hilo ninalolisema, nimeshakuambia kuwa mimi nakupenda sana kweli si kweli,…, na hayo yaliyofanyika, yalifanyika kwa nia njema tu, ya kuilinda ndoa yetu,  na nakuhakikishia kuwa mkataba wetu upo vile vile na mambo yake mazuri tu…, na mimi nitakuwa mume mwenye mamlaka kama mwanaume, sio mwanaume jina tu...’akasema

‘Una maana gani kusema hivyo?’ nikamuuliza.

‘Mkataba ndivyo unavyosema hivyo...kuwa mimi kama mume nitakuwa na mamlaka ya uongozi wa familia, nitaweza kupitisha maamuzi, kama nionavyo ni sahihi kwa masilahi ya familia, hilo halihitajii mjadala, au sio…hata bila kuwa na mkataba hilo lipo wazi, kwanini hunielewi…?’ Akaniuliza

‘Huo mkataba  wa kugushi ndio unasema hivyo, hicho kipengele ni kigeni kwangu ..’nikasema

‘Na...wewe utakuwa msaidizi wangu, na hiyo ndio kawaida ya mume na mke, mambo mengine ni ya kuiga tu, ..hayana maana kwetu, ndio hata Marehemu aliyaona, lakini sio kitu kikubwa sana, maana mimi ndio nilitakiwa nilione hilo, na mimi ndio natakiwa kusema..au sio,…’akauliza na mimi nikaa kimia

‘Mke wangu, kikawaida eeh, mimi ndio natakiwa kuwa kiongozi wa familia,na ikibidi kurekebisha jambo kwa masilahi ya familia, sihitaji kibali au sio…ili kuikoa familia, na kila kitu, huo ndio ukweli, zaidi ya hayo, mimi natakiwa kuilinda familia yangu, ukisaidiwa na wewe mke wako, kwani hapo kuna makosa, ni maneno yale yale...’akasema.

‘Haya unayoyaongea wewe yapo kwenye huo mkataba wa kugushi au sio sio kwenye mkataba sahihi tuliainisha wazi kuwa, ili kuondoa utata,  kila jambo litafanyika kwa makubaliano,….na hili uliliongeza wewe siku ile ya majadiliano,…na tulikubaliana kabisa kuwa asilimia kubwa ya mambo yetu yapo kwenye mkataba, kwahiyo kama kuna kasoro, au jambo lolote limejitokeza lenye sintofahamu basi, tukae tujadiliane..’nikasema

‘Sawa kabisa,…’akasema

‘Na hii ina maana gani, mkataba hauwezi kubadilika mpaka kuwe na kikao cha kukubaliana, akiwemo wakili wetu, sasa hayo ya mume kujiamulia mwenyewe akiona kuna sababu, yanatoka wapi,, na kwanini kuwe na mabadiliko, kuna nini kilitokea,…?’ nikamuuliza

‘Mkataba ni ule ule mke wangu, hakuna kilichobadilika, hata ukiuangalia, eeh, ni mambo yale yale, na yote…tulikubaliana mimi na wewe ..na wakili wetu…wewe ni wasiwasi wako tu’akasema.

‘Tatizo lako, Makabrasha alikuingiza kwenye anga zake za ulaghai, na umesahau kuwa wewe sio mwanasheria, huyo mtetezi wako sasa hivi hayupo tena duniani, kuna mambo ya kisheria huyafahamu,...na hayo yatakupeleka pabaya,...mkataba  uliokubalika kisheria ni ule tuliokaa mimi na wewe tukakubalina sio huo uliokaa wewe na mwanasheria wako, ....’nikasema.

‘Ndio huo huo mke wangu, wewe una nakala yako, na mimi nakala yangu, nenda unapoziweka ukazichukue,…lakini mimi nina nyingine hapa, na nisisahau nakala nyingine ipo huko kwenye vyombo vya sheria… hakuna mkataba mwingine...kila kitu kipo vile vile, hakuna kilichobadilika, na wewe na mimi tuliweka sahihi zetu na ya mwanasheria wetu, ndio hivyo...’akasema.

‘Mwanasheria gani?’ nikamuuliza.

‘Mwanasheria wetu wa familia, ..ngoja nikuonyeshe mkataba wetu, ninao nakala yetu hapa..hakuna kitu kilichobadilika, ni mambo madogo madogo tu ulikuwa huyajui labda, ndio yanakuchanganya, eeh, usijali kabisa, hata kama wamemuua Makabrasha kuwa labda, nitakosa mtetezi, mimi mwenyewe nitajitetea,..na haya yote mke angu ni kwa ajili ya masilahi yetu sote...’akasema huku akiutoa huo mkataba

Na wakati anafanya hivyo macho yangu yakahisi kama kuna mtu kasimama kwa nje, nahisi alikuwa akisikiliza tunachoongea, akasogea kidogo, …sikuweza kumtambua ni nani,...nikataka kumpa ishara mume wangu, lakini hakuwa makini na yeye akawa ananionyesha sehemu zile za sahihi akasema;

‘Huu ndio mkataba wetu,..unaona hii hapa ni sahihi yangu, hii ni ya kwako, hii ni sahihi ya mwanasheria wetu wa familia, mkataba ni ule ule, utabadilishwaje na nani afanye hivyo...hakuna kilichobadilika kabisa , ...unaonaeeh...’akasema huku akifungua fungua huo mkataba, na mimi nikawa namuangalia tu

‘Mume wangu usitake tufikishane huko..huko unapokwenda ni kubaya, usikubali hayo mambo aliyokudanganya Makabrasha, ..huyo jamaa anajulikana sana kwa hadaa na ulaghai, hata watu wa usalama wanalitambua hilo..sasa na wewe usiwe mshirika wake, tunachotakiwa kwasasa ni kusahihisha yale makosa yaliyotokea, ili tuanze pale tulipoishia, ..’nikasema

‘Ndio hivyo mke wangu ndio maana hata kama unataka basi hata huu mkataba tuachane nao au sio, na mimi niwe na mamlaka yangu kama mume wako au sio, mbona wengine wanaishi tu  bila hata ya mikataba unaona eeh, ni kwanini sisi, sababu ya mali au...’akasema

‘Sikiliza mume wangu,….tusilazimishe migogoro isiyo na msingi, na tusitake kulazimisha chuki na uhasama, wakati kuna njia nzuri ya haki, yenye kuleta mariziano na maafikiano,...hebu nikuulize hivi wewe unachotaka hasa ni kitu gani, niambie ukweli ?’ nikamuuliza mwishoni.

‘Nakupenda sana mke wangu , sitaki mimi na wewe tuachane, mimi nataka ndoa yetu idumu na tuishi kwa amani na upendo...’akasema

‘Ni nani kasema hatupendana na hiyo hoja ya kuachana inatoka wapi, eeh, kuna nini kimeileta hiyo hoja ya kuachana?’ nikamuuliza.

‘Mkataba…eeh, …je ikiingia fitina, na wewe ukaridhia nayo, wakaja wazazi wako ukasema mkataba huu unasema hivyo, itakuwaje, fitina ni mbaya mke wangu, kuna watu walishajenga majungu, na hata rafiki yako analifahamu hilo, nina uhakika hadi anaondoka bado mlikuwa hamjawa sawa, kweli si kweli, na wewe ndiye ulikuwa mshauri wake mkuu, kila jambo anafanya kutokana na ushauri wako,…lakini hayo yamepita kila kitu kipo sawa sasa, au sio,...’akasema

‘Ndivyo alivyokuambia kuwa kila alichokifanya kinatokana na ushauri wangu..?’ nikamuuliza

‘Rejea hoja yetu , kuhusu mkataba ni nani alitoa pendekezo hilo, lengo lake hasa ilikuwa ni nini, sema ukweli wako wote, na je sio kweli kuwa wewe na rafiki yako, mlikuwa mnashauriana mambo mbali mbali, tatizo lako wewe mke wngu unasahau, unashauri baadae ikigeuka unakana, usiwe hivyo, mkuki usiwe kwa nguruwe tu…’akasema

‘Sawa, tuwe wa kweli sote, je kuna vipengele kwenye mkataba mlivirekebisha wewe na Makabrasha tumalizane na hilo…?’ nikauliza

‘Hapana, hakuna kilichobadilika, …zaidi ni kuhakikisha kuwa mume ana mamlaka yake, mimi hizo sehemu nilikuwa sijazisomi, nilipozisoma na kuziona nikajua kumbe nilikuwa siwajibiki..’akasma

‘Haya sawa, sasa nikuulize ni nini lengo la hayo yote , ni ndoa au ni mali…?’ nikamuuliza na hapo akashituka na kuniangalia machoni.

‘Mke wangu nimesema kuwa nakupenda sana....sipiganii mali hapa.., ninachopigania ni ndoa yetu,ndoa ni kila kitu humo..ni kwanini  niipiganie mali wakati ipo , mali tunayo au sio, tuna vitega uchumi vingi, ni swala tu la kuviendeleza....huwezi kupigania kitu chako, eti mke wangu, mbona sikuelewi...’akasema.

‘Kwa hatua mliyofikia, hakuna jinsi, ni lazima ule mkataba wa asili uwepo, na huo wenu uwepo, tuangalia je ni kweli hakuna kitu kilichobadilishwa, najua kuna madhambi umeyafanya, na kulikuwa na vipengele vya kukuwajibisha, ukaogoa, ndio maana ukakimbilia huko kwa Makabrasha.’nikasema

‘Usimsingizie marehemu uwongo, yeye sio kazi yake kuondoa kitu kwenye mkataba, maana sio yeye aliyeutunga,..kazi yake kubwa ilikuwa ni kunifafanua na kunishauri, yeye ni kweli, alipitia mkataba wetu, akausoma, na kuniambia upo safi kabisa, akanionyesha hivyo vipengele muhimu ambayo mimi nilikuwa sivitilii manani, vya mamlaka yangu...’akasema.

‘Kwahiyo ndio ukafanya ulivyoona kuwa ni sahihi,..hata kama mimi sijarizia, ?’ nikamuuliza

‘Nimefuata mkataba unavyosema, au sio mke wangu, na .., kama ilitokea kukosea huko nyuma, ni kwa bahati mbaya, ndio maana nilikuomba msamaha kipindi kile, unakumbuka,… sisi kama wana ndoa wakati mwingine tunakosea kama wanadamu, na kama mkataba unavyosema mtu ukikosea unatakiwa kutubu, na kuomba msamaha, nilitimiza hayo au sio ...’akasema

‘Mume wangu sitaki kusikia hayo tena, tafadhali, nakuomba uondoke, nataka kupumzika, naona unazidi kunichanganya tu, hayo ni mambo yenu na marehemu, naomba usiongelee tena kuhusu huo mkataba wenu wa kugushi....’nikasema

‘Lakini mke wangu kuna jambo jingine muhimu kabla sijaondoka, ...kuna mtu anasubiri, maamuzi yangu mimi na wewe’akasema

‘Nani anasubiri hayo maamuzi yangu mimi na wewe, na hapa tulikuwa tunaongea tu, na wewe mwenyewe ulisema kuwa haya ni mimi na wewe,huyo mtu mwingine inamuhusu nini hapa …na nikuambie kitu,hakuna maamuzi yoyote yamepita hapa, ..hatujakubaliana lolote hapa.mimi siutambui huko mkataba wenu, nitakubaliana na mkataba wetu ule wa awali zaidi ya hapo mimi sipo.’nikasema.

‘Kuna mtu muhimu sana, alikuwa anasubiria haya maamuzi yetu, ni haki yake lakini, na mimi nilikuja kutimiza wajibu wangu, kuomba ushauri wako…’akasema

‘Mtu gani huyo, na ana haki gani hiyo…?’ nikauliza

‘Ni mtoto wa marehemu, anahitajia maamuzi yetu, ...’akasema, na hapo nikahisi moyo ukiniruka, ni kama mtu kakushtua ukiwa hujui

‘Nimeshakuambia hakuna maamuzi yoyote yaliyopitishwa hapa, kama una lako jambo endelea kivyako, na kama umedhamiria hayo uliyokusudia, basi tutapambana mbele ya sheria, wewe si mjanja, sawa endelea na mpango wako huo, kila la heri ..’nikasema

‘Mke wangu usifike huko…’akasema

‘Usipoleta mkataba ule wa awali tutafika huko, maana nakuona hutaki kunielewa,  na hutaki kusema ukweli, usihadaike na tamaa za watu wengine, kumbuka tulipotoka, na kila mara nilikuwa nakuasa, acha tamaa, tushikamane, tuwe kitu kimoja, sasa haya yote yanatoka wapi, unataka nini husemi…, au kuna kitu gani kimetokea, hutaki kuniambia ukweli,…kwa hali hii bora uondoke, hapa sijisikii vyema nataka kupumzika,…’nikasema

‘Sawa kama umechoka hujisikii vyema mimi nitafuata mkataba unavyosema, au sio, mkataba umenipa mamlaka ya kufanya yale yaliyosahihi kwa masilahi ya familia, na na nilichokuja kuonana na wewe ni kupata ushauri, …wewe pumzika, mambo mengine niachie mimi, au sio mke wangu…’akasema.

 ‘Au sio kuhusu nini…mimi sijakushauri kitu hapa..’nikasema kwa hasira

‘Mke wangu si umesema niondoke,unataka kupumzika, au?’ akaniuliza huku akigeuka kuniangalia.

‘Sina cha kuongea na wewe hadi hapo utakapoleta ule mkataba wa zamani, na kuniambia ukweli wote, vinginevyo hatutaelewana...’nikasema.

‘Hamna shida mke wangu, ..tutaongea tu, wewe pumzika,  mimi ni mume wako wa halali, hakuna kibaya kitakachotokea, yote niachie mimi, mimi nitatimiza kila kitu kama tulivyoainisha kwenye mkataba wetu..’akasema kwa kujiamini.

Na mara mlango ukafunguliwa,kwa nje, lakin hao watu hawakuingia, ulionekana mkono tu,..nahisi ni zaidi ya mmoja maana nilisikia wakiongea, walikuwa wakibishana jambo …mara mlango ukafunguliwa wote sasa, nikaweza kuwaona wapo watu wawili, kwa upeo wangu.

 Huyu mmoja alikuwa karibu sana na mlango, nilipomchunguza kwa makini nikaona kama anafanana sana na marehemu nahisi atakuwa ndio huyo mtoto wa marehemu, kwa muda huo alikuwa akitaka kuingia ndani, na mume wangu akawa kamuwahi na akamzuia,akisema;

‘Mke wangu kachoka, naona mambo yote nitayamaliza mimi mwenyewe, tunaweza kuongea huko mbele ya safari, au ulikuwa unasemaje…?’ akauliza sasa wakiwa wamesimama mlangoni kwa nje.

‘Huyu ndiye yule wakili wangu niliyekuambia, atachukua nafasi ya baba yangu..’sauti yule ambaye nahisi ndio mtoto wa marehemu ikasema. Na hapo hapo nikachukua simu yangu kwa siri, nikawaweka sawa kwenye kiyoo cha simu na kuwapiga picha, huku nikimchunguza huyo mtu mwingine ambaye ni wakili kwa kauli ya huyo mtoto wa marehemu, kwa hisia zangu nilimuona ni kama aina za Marehemu, kwa hisia zangu tu.

‘Habari yako muheshimiwa, …’ mume wangu akasalimia, na wakati anasalimia ndio akagundua kuwa mlango bado upo wazi, akasogea na kushika mlango na kuufunga. Hata hivyo nilikuwa tayari nimeshawapiga picha.

Na mimi nilipohakikisha mlango umefungwa,   kwa haraka nikampigia simu wakili wangu.

‘Sikiliza kama ulivyonishauri haya ni mazungumzo yangu mimi na mume wangu nimeyarekodi, na picha zao nakutumia sasa hivi, yasikilize na wewe utajua ni nini cha kufanya , wahi kabla hawajafanya lolote, sawa...’

NB: Doa la tamaa limeshagusa mtima, ibilisi hachezi mbali hapo,...je itakuwaje, Kwa leo inatosha.



WAZO LA LEO: Imani ya kweli ya ucha mungu ni pale upomjali mwenzako, na ukawa tayari kutoa hata kile unachokipenda kumsaidia mwenzako, na ukajali jirani zako, lakini hayo yote kwa ajili ya mwenyezimungu sio kwa ria. Je ni wangapi wapo tayari kuona mwenzake anapata kabla yake, au zaidi yake, ni wangapi wanayajali matatizi ya wengine, ni wangapi wanaona mali ni kitu tu cha kupita, awe tayari kusaidia wengine, hapa ni mtihani! 

Ni mimi: emu-three

No comments :