Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Tuesday, December 19, 2017

MKUKI KWA NGURUWE-44



Ni wakati nafika mlangoni ili nigonge mlinzi anifungulie mara kitu kikanigonga kwa nyumba kichwani, na giza likatanda,.....nikadondoka, na kupoteza fahamu….

Tuendelee na kisa chetu…

**********

Nilizindukana na kujikuta nipo hospitalini, akili ilipotulia nikagundua kuna mtu kakaa pembeni ya kitanda, …ndio nikamgundua kuwa alikuwa ni mume wangu, wakati huo alikuwa kajiinamia, nikajaribu kujiinua, lakini nikahisi maumivu ya kichwa, nikashikilia kichwa, na mara ndio mume wangu akagundua kuwa nimezindukana, kwa akanisogelea na kujaribu kunisaidia, nikainuka na kukaa vizuri,

‘Pole sana mke wangu unajisikiaje...’akasema kwa unyenyekevu.

‘Kwani kumetokea nini…mbona….oh, kuna kitu kilinigonga kichwani, ni nani kafanya hivyo…?’ nikauliza

‘Inaonekana kuna watu walitaka kukuumiza huko jela...’akasema

‘Kuniumiza kwasababu gani,…ni akina nani hao?’ nikawa nauliza maswali kwa mfululizo.

‘Hayo maswali kwasasa hayana msingi, cha muhimu ni kuwa upo salama, na hilo limesaidia kupatikana kwa dhamana yako haraka, kwani kuna watu walishaiwekea pingamizi, wakidai kuwa upo mahali salama, ungeliachiwa ungekuwa kwenye hatari zaidi...’akasema.

‘Oh, kumbe....’nikasema huku nikishika kichwa, sehemu ambayo nilifungwa bandejii na mume wangu akaniangalia kwa mashaka na kuuliza

‘Kwani unajisikiaje?’ akaniuliza huku akiweka mkono sehemu ile iliyowekwa bandeji na mimi nikawa najihami asije akanitonesha, na akaondoa mkono wake, na kuniangalia machoni. Alionekana huruma machoni…

‘Maumivu ya kichwa kwa mbali, lakini sio sana, haya niambie na wewe unaendeleaje, maana mgonjwa anamuuguza mgonjwa, nani zaidi sasa...?’ nikamuuliza

‘Mimi kwasasa sijambo, sina wasiwasi kabisa, nipo tayari kupambana na yaliyopo mbele yangu, japokuwa nachechemea, lakini sio kivile…na muhimu kwa sasa ni mazoezi tu...’akasema huku akijiweka vyema, kama vile anajiandaa kuongea.

‘Unajiandaa kupambana na yaliyopo mbele yako, yapi hayo mume wangu, unavyoongea ni kama umemlanga mtu au ni maswala ya kazi na maendeleo...?’ nikamuuliza

‘Dunia hii ilivyo, maisha yetu wanadamu yalivyo, kila siku ni mapambano, au sio, huwezi kulala tu, ukafanikiwa, ni lazima upambane, na mimi nimejifunza jambo hapo, ili ufanikiwe hakuna kulala..’akatulia kidogo.

Nilimuangalia kwa makini, na hayo maongezi yake nikahisi kama hayupo sawa, kwahiyo nikaogopa kuendelea kumuuliza maswali ya kumkwanza, nisije nikaharibu nikataka kubadili muelekeo wa maongezi kwa kusema;

‘Hivi huyu wakili wangu yupo wapi...maana nataka kujua mambo yanaendeleaje...aniambie kulitokea nini..nakumbuka nilikuwa mimi nay eye tu mle ndani, sasa…hapana, lakini sawa…labda…’ nikawa kama nauliza huku nikitafuta simu yangu, sikujua ipo wapi.

‘Wameondoka muda mfupi uliopita, watarudi, kuna mambo wanafuatulia, walisema zoezi limekamilika, sikuwaelewa,…kwani ....unatafuta simu yako, nahisi ipo kwenye mkoba wako, nikuletee?’akaniuliza.

‘Mkoba wenyewe upo wapi, hata sijui…maana akili haipo..’nikasema

‘Mkoba wako huu hapa, walikuchukulia kila kitu chako, haina haja ya kurejea huko jela, kumbe ni uzembe wa watu tu, hukutakiwa kupelekwa huko…’akasema

‘Nilijua tu, walitaka kunikomoa, kuijengea kashfa, lakini hawatafanikiwa ukweli utabakia kuwa silaha ya mkweli,…’nikasema

Wakati huo mume wangu aliinuka kuchukua mkoba wangu uliokuwa umewekwa kwenye meza, alionekana akiinuka kwa shida, yaonyesha bado hajapona vyema ila anajikakamua tu. Akanipa simu yangu, nikaiwasha kwani ilikuwa imezimika, nikawa nimeishikilia mkononi.

‘Oh, hamna shida, ..hivi leo tarehe ngapi, ...’nikasema huku nikiangalia simu, akaniambia tarehe na saa, nikasema;

‘Ahsante sana mume wangu,..nikamtaja kwa jina lake, na yeye akatabasau na kusema

‘Ahsante mke wangu,…’ na kunitaja jina langu, siku nyingi sijasikia ukinitaja jina langu na mimi nikatabasamu, halafu nikasema;

‘Kama dhamana imepatikana basi iliyobakia ni kuangalia kesi hiyo itakwenda vipi, na huyo muuaji ajulikane ni nani, ili niwe huru kabisa....’nikasema.

‘Mke wangu, kuuwawa kwa Makabrasha kumenishitua sana, sikutegemea kabisa, ni kama bado namuona vile , yaani jana tu mtu mlikuwa naye, leo hayupo, keshatoweka duniani, hatutamuona tena,..na zaidi kafaje mpaka afikie adhabu hiyo.., hapo ndio inatisha zaidi…’akasema

‘Ni kweli pole sana, najua alikuwa wakili wako tegemezi na rafiki yako mpenzi, lakini yote ni mapenzi ya mungu..’nikasema

‘Mhh ndio hivyo,…kazi ni kazi ukiwa hai, hayupo tena, natakiwa kupambana mwenyewe…unajua nawaza sana baada ya hilo tukio kuwa sisi wanadamu si chochote...na wengine wanajiona wana nguvu, kwa vile tu wana mali….’akasema.

‘Mhh…mali,…. ni kweli mali ni mtihani, na usipokuwa na mali ni mtihani pia, au sio...’nikasema kama namuuliza.

‘Ni kweli,..hilo nimeliona ni mtihani kweli ukiwa huna kitu, na …ukaoa mke mwenye uwezo, unajikuta mwanaume huna kauli, …sikuongelei vibaya  mke wangu, ila nimekuwa nikiliwazia sana hilo…nafahamu wewe huna shida, mke wangu wewe ni mtu tofauti na wanawake wengine, lakini wewe utafanyanini, kama wazazi wanataka uwe watakavyo, eeh...’akasema

‘Kwanini unaongea hivyo, kwani kuna kitu gani kibaya umekiona dhidi yangu, au wazazi wangu, tulishaongea hayo sana tukayamaliza, au…kuna nini cha zaidi?’ nikamuuliza huku nikimwangalia usoni.

‘Haya yanayoanza kujitokeza, yananipa shida kweli kweli, ndio maana hata nilipokuwa hospitalini, nilikuwa nikihangaika kujua jinsi gani ya kuyaweka sawa, na nikawa natafuta njia ya kuyasawazisha, lakini mwili ulikuwa haukubali,..nilikuwa kwenye mtihani mkubwa sana...lakini sasa naona kila kitu kitakuwa sawa , ni swala tu la kukubaliana...’akasema.

‘Kukubaliana?? Ukiwa na maana gani hapo, kwani hatukuwa tumekubaliwana awali, mambo yalikuwa shwari au sio, au kuna tatizo, mume wangu nakuomba uniambie ukweli, kuna nini kinachoendelea…?’ nikauliza bila kujali lolote.

‘Kukubalina ni muhimu hasa kwa wote wanaohusika, ili mambo yaishe tu, kwani tunataka nini zaidi, alikuwepo Makabrasha aliyejiaminisha, msomi, tena wa nje, mjanja kweli kweli, ..anajua sheria, anajua mbinu za maisha, mbona kashindwa kujilinda, leo yupo wapi,…mmh,hapo ndio mimi naogopa sana..’akasema

‘Umeliona hilo eeeh, vyovyote utakavyofanya, ukatumia ujanja ujanja wa maisha, mwisho wake ..sote itakuwa hivyo, hakuna mjanja mbele ya mungu, sasa kama ulidhulumu , kama ulifany madhambi itakuwaje, inatakiwa mimi na wewe tuliwazie hilo, au sio mume wangu…’nikaongea , kuuma na kupilizia.

‘Ni kweli mke wangu, sasa tufanyeje ili mambo yawe sawa, ili tuwe kama zamani, unakumbuka tulivyokuwa tunaishi, …eeh, japokuwa kiundani, nilikuwa najihisi mnyonge…unanielewa hapo, mume nakuwa hivo hivyo…’akasema

‘Mume wangu tatizo nahisi kuna mtu kakuharibu akili yako, kwani mimi nilikunyanyapaa, kila kitu tulifanya kwa makubaliano au sio…na nilikubali kuwa pamoja na yote wewe ndiye mume wangu mwenye mamlaka ya mwanaume, haijalishi kitu, na kukufanya uwe na nguvu zaidi tukafungua kampuni yako mwenyewe, ili usiwe mnyonge…’nikasema

‘Ni kweli lakini bado ilikuwa sio kama yangu…nilikuwa sijalifahamu hilo..lakini nilipogundua kuwa ni mimi tu, nilikuwa sifuatilii mambo, …unajua hapo ndio namshukuru sana Makabrasha, kanionyesha mambo ambayo sikuwa nayafahamu, mola ampe makazi mema peponi…’akasema.

‘Mume wangu pamoja na yote hayo, kwanza nakuomba kama upo tayari, uniambie ukweli, sawa uliniomba msamaha, lakini kwa kosa gani, hujaniambia hilo, lakini pia haya yanayotokea, …mpaka wewe kutafuta wakili yana ishara gani, ni kwanini ukafanya hivyo..kama upo tayari nakuomba uniambie…’nikasema

‘Nipo tayari sana mke wangu na ndilo nililojiandaa nalo, sitaki tena kupoteza muda…’akasema

‘Sawa..msamaha mnzuri ni ule unakiri kosa ulilolifanya au sio…kiukweli na mungu ni shahidi au sio..sasa mume wangu nataka uniambie ukweli umefanya kosa gani, mpaka ukafikia kupatwa na ajali, ilikuwa ni tatizo gani…?’ nikamuuliza


‘Mke wangu kweli unataka kuambiwa ukweli..utavumilia huo kweli, hutanichukia, huta… lakini hata hivyo, mbona ukweli wote upo wazi tu,…mimi nakumbuka nilishakuambia na kukuomba msamaha au sio…lakini anyway, hilo halina shida, ila ukweli mara nyingi unauma, naogopa kukuumiza mke wangu ...’akasema

‘Mhh, kwanini ukweli uume, ..labda kama una mashaka, ...lakini kama una nia thabiti,ya kujua na kukubali kwa nia njema sizani kama utaumiza,...tatizo ni kuwa watu wengi hawataki kusema ukweli, wakichelea yatakayotokea baada ya ukweli…’nikasema tukichezeana akili hapo, kwanza nikitaka kumweka sawa nisije kumuathiri.

‘Hapo ndio kwenye mtihani,lakini kwetu sisi sizani kama kutakuwa na matatizo au sio mke wangu, sasa hivi hata nikiongea ukweli, najiamini, hakuna shida mke wangu kwahiyo leo ni siku ya ukweli, ukweli wote kutoka kwangu…’akasema

‘Kwanini sasa ujiamini, kwani zamani kulikuwa na kikwazo gani..?’ nikamuuliza

‘Nilikuwa sijafahamu haki zangu, lakini nashukuru kwa ushauri wako, na ushauri wa wakili wetu…unajua mke wangu una akili sana, wewe unaona mambo vyema kabisa, na ushauri wako unakuwa wenye manufaa sana, ingelifaa wewe uwe mshauri wa watu…’akasema

‘Una maana gani..?’ nikauliza

‘Hata rafiki yako anakusifia sana, …unajua kushauri mambo, bila kujali ..maana ukimshauri mtu eeh, akifanya inamsaidia na unajua tena …na mengi uliyomshauri yamemsaidia, na hata ukiangalia mengi uliyoyashauri kwenye familia yetu, tukayafuata imekuwa ni faraja sana…wewe unaangalia mambo kwa usawa, ukiwajali wenzako, marafiki zako, familia yako, unaonaeeh, na zaidi hasa ushahur huo ukiwa kwenye maandishi, ya kudumu ..yaani mimi sikuwa na mawazo hayo kabisa hata marehemu alisema wewe ni jembe…’akasema

‘Kwahiyo sasa umepona upo tayari kwa haya,…?’ nikamuuliza kwa mashaka

‘Ndio mke wangu, wala usiogope, kama huamini mpigie simu docta wangu, nimepona wewe tuongee , maana hili ni la muhimu sana, ili tuyamalize haya tuwe huru, nina imani baada ya haya, hakutakuwa na tatizo tena, ..kabisa niamini mke wangu…’akasema

‘ Mume wangu…mimi japokuwa bado nina mashaka na afya yako, lakini kiukweli nilikuwa nasubiria hatua hii, nilikuwa natamani sana, upone ili tuyamalize haya matatizo, japokuwa sasa yamezuka haya mambo mengine, ni shida kwakweli..sijui yataishaje, lakini tukimpata huyo muuaji, basi nina imani mambo tayakwisha, nina imani..nikitoka hapa tutalimaliza hili...’nikasema nikimwangalia, na yeye akawa akiangalia pembeni, nikamuuliza

‘Yah, hilo tutalifanyia kazi, kama mume , nina wajibu wa hilo…mke wangu niamini hilo tutalimaliza,…’akasema akitikisa kichwa.

‘Vipi hali yako kwa ujumla, kweli umepona vyema, maana tusije kanza kuongea hapa likazuka jingine,..?’ nikamuuliza tena….

‘Hahaha , mke wangu huamini, mimi nimepona, nilifuata masharti yao,kama walivyotaka, japokuwa ilikuwa kazi nzito, maana nilikuwa kama mfungwa, lakini kiukweli ilinisaidia sana, na waliponipima kwa mara ya mwisho waliniambia nimepona kabisa, walisema kila kitu kipo safi, hakuna matatizo tena, usiwe na wasiwasi na mimi mke wangu....’akasema.

‘Kwahiyo upo tayari kusema yote yaliyotokea, kuanzia yaliyotokea, ukaja kupata ajali, baadae nakumbuka ukaja hata kuniomba masamaha, nimekuwa nikijiuliza huo msamaha ulikuwa wa kosa gani, sasa je upo tayari kwa hilo , ....?’nikamuuliza.

‘Hilo ndilo nataka tuliongelee leo kama na wewe upo sawa,..maana wewe unaumwa, au tusubiri kwanza hayo mengine ila kuna hili la muhimu kidogo, mimi kama mume ninawajibu wa kuomba ushauri kwako, au sio, ni la haraka, halihitajii kusubiria, kama upo tayari, tuyajadili mimi na wewe...’akasema

‘Sawa itakuwa vyema…’nikasema nikiwa sijui anataka tujadili nini, zaidi nilitaka yeye aniambie ukweli

‘Mke wangu kuna mengi yametokea, na muda umepita, na shughuli nyingi zimesimama, kiasi kwamba mtu unashindwa uanzie wapi…lakini kuna haya yetu wenyewe, haya ndio msingi, na nazidi kushukuru kwa mawazo yak o ya kuona mbali,..sasa ni hivi,…’akatulia kidogo, na mimi nikasubiria.

‘Mimi nataka tuyamalize ikibidi leo, …ila nitakuwa mtomvu wa shukurani kama nitamsahau Marehemu, na ndio maana naona umuhimu wa kikao chetu, ili mengina yaishe , Marehemu alikuwa msaada wangu mkubwa, kiushauri, ....kanifungua macho, hasa kwenye maswala ya maandishi,....’akatulia kidogo.

‘Una maana gani maana naona unatumia maneno hayo ya maandishi, maandishi…?’ nikamuuliza

‘Hapo namaanisha mikataba...’akasema

‘Mikataba…mmh, tuna mkataba mmoja wangu mimi na wewe, au mingine ni ya kikazi au?’ nikauliza na kabla hajajibu nikaendelea kuongea

‘Au wewe una maanisha mkataba huo wa hiari ..?’ nikauliza

‘Huo huo, ..yah, hiyo mikataba ya hiari, …’akasema

‘Lakini,..unajua nilishindwa kukuuliza kwa vile ulikuwa unaumwa, nimeoana ajabu kubwa sana, mbona mkataba ule wa hiari, haupo tena, na sasa upo mkataba ambao sio ule wa awali…?’ nikauliza

‘Mke wangu, unasema nini…hapana, mkataba ni huo huo, au…?’ akauliza

‘Hahaha, nilijua tu, ni janja yako wewe na Makabrasha, au sio…ule mkataba wa hiari wa awali, umetoweka, na sasa upo mkataba wa kugushi, sasa niambie maandishi au mkataba unaozungumzia wewe ni upi, wa kugushi au ule wa awali…?’ nikauliza.

‘Mkataba wa kugushi!? Mke wangu hakuna mkataba wa kugushi, hilo neno kugushi limetokea wapi tena …na unasema umetoweka kwa vipi , ni kitu hakiingii akilini mke wangu, una…aah,..una- taka kusema nini hapo…’ akaniuliza na maneno ya mwisho akaigiza lafudhi ya kizungu sijui alikuwa na maana gani.

‘Kwahiyo unajifanya hujui kuwa wewe na Makabrsaha ndio mliofanya hayo!’nikamwambia huku nikimwangalia nikiwa na mashaka nisije nikazua balaa, lakini sikuona mabadiliko,, yeye kwanza akainamisha kichwa chini, na baadaye akasema;

‘Mke wangu nakupenda sana, .sitaki kukudanganya, kama nilivyosema huu ni muda wa kuambizana ukweli, na…kiukweli kuanzia sasa sitaki nikufiche kitu.,..nitakuambia kila kitu kilichofanyika, na nina imani utanielewa.’akasema

‘Sawa ukifanya hivyo, mbona tutaelewana tu, mimi sina shida, mwenye shida ni wewe tu ambaye ulihangaika na hadi kubadili mikataba, na ajali ikaja kukuta, nahisi ni katika kuhangaika huko, sijui ulikuwa unaogopa nini..’nikasema

‘Najua,…hilo sio siri, sasa ni hivi, kiukweli ilibidi nifanye jambo, maana nisingelikubali mimi na wewe tuje kuachana, kisa mkataba, hapana mimi nakupenda sana mke wangu,..bila kujali hayo…unasikia, mkataba na nini, ni katika kujihami tu, au sio… na mimi naahisi kuwa, nitailinda ndoa yangu kwa kila hali, hilo nakuahidi, mke wangu, ..’akasema

‘Sawa, nimekusikia..’nikasema

‘Na ndoa hapa nina maana ya kila kitu, familia, mali, na..maisha yetu ya kila siku, kufungwa kwako ilikuwa moja ya pigo kwangu, ..sikuwepo nyumbani, nilikuwa naumwa, nilitakiwa kama ni kufungwa nifungwe mimi…’akasema

‘Kwani wewe ndio uliua..?’ nikamuuliza

‘Hapana, wewe wanakushuku tu, kama wanakushuku, na mimi nipo, ningeliwaambia wanifunge mimi,…hadi hapo ukweli utakapopatikana, lakini nilikuwa sijiwezi, naumwa, nipo hospitalini,ningelifanya nini..ni mtihani..lakini sasa nipo ngangari, tutapambana na hao watu…’akasema

‘Kwahiyo kwa kifupi ni kweli kuwa uliubadili mkataba wetu kutoka ule wa asili na kutengeneza mwingine wa kitapeli..’nikasema nikimuangalia, maana hapo nilitumia lugha ya kumkwanza, lakini hakubadilika, alikuwa vile vile wa kujiamini.

‘Mke wangu, usitumie lugha hiyo, ‘kubadili’ …maana kiukweli hakuna kitu kama hicho, kwa lugha yako hiyo ya kubadili, au kugushi hakuna kitu kama hicho eeh,....mimi kama mume wako niliona ni heri nifanye jambo, kuilinda ndoa yetu, na nilichofanya ni sahihi kabisa, kwa mujibu wa mkataba unavyosema.. ‘akasema

‘Kwahiyo ulibadili mkataba kwa kutaka hayo unayoyataka wewe, na kujiwekea hayo mamlaka ya kufanya utakavyo.., nataka jibu tu hapo, kweli au si kweli, je wewe na mkabrasha mlibadili kitu kwenye mkataba, niambie ukweli tu hapo..?’ nikauliza

‘Mke wangu…’akataka kujitetea

‘Hilo ni muhimu kwangu, kauli yako ni muhimu sana, ni kweli au si kweli, ukijibu hilo itakuwa ni faraja kwangu, niambie ukweli,..mlibadili huo mkataba au sio, ni kwanini mlifanya hivyo, nataka jibu la ukweli, kwasababu umesema leo utaniambia ukweli..sio ndio hivyo..?’ nikamuuliza

‘Ndio..leo nitakuambia kila kiu ..muda ukiruhusu, ni wewe tu..’akasema

‘Haya jibu swali langu…’nikamwambia..

NB: Muda umekwisha, sehemu hii itaendelea…kuna tukio muhimu sana hapa hutaamini..ngoja niliweke sawa, lakin ngoja nitangulize kipande hiki.

WAZO LA LEO: Mkataba ni kitu cha makubaliano, na mkataba ulio sahihi ni ule pande mbili zinahusika, na kukubaliana,..mikataba mingi hasa ya ajira, inakuwa ya pande moja, na muajiriwa anakuwa hana hiyari, ni kukubali tu, huu sio mkataba sahihi.


Kuna mikataba ya mauziano ya bidhaa, kusiwe na ujanja ujanja wa kutapeliana, hii ni dhuluma, hata kama ukishinda kumshawishi mwenzako ukamdhulumu hili ni deni kwako. Lakini pia kuna mikataba ya hiari kati ya pande mbili, ni lazima kila pande irizike na kila kipengele. Tukumbuke mkiwa wawili mwenyezimungu yupo kati yanu, au hata mkiwa wengi mwenyezimungu yupo analithibitisha hilo, hadi kwenye nafsi zetu, kudanganyana ni kujidanganya wenyewe. Tusipende kudhulumu kwa njia hii dhuluma ni dhuluma na madhara yake ni makubwa .
Ni mimi: emu-three

No comments :