Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Wednesday, March 5, 2014

BAADA YA DHIKI FARAJA-21


Nikiwa njiani kuelekea kwa mdada, garo moja dogo lililokuwa likiendeshwa kwa kasi, lilinipita na kuja kusimamishwa mbele yangu, ikanibidi nifunge breki za haraka, karibu kujigomga kwenye hilo gari, na mara wakatoka watu wawili, wakanizunguka, na mimi nikawa nimejiandaa kwa lolote maana siku hizi usalama ni mdogo, nilijua hawawezi kufanya lolote maana ilikuwa sehemu yenye watu,

‘Ndio pikipiki yenyewe hii...’mmoja akasema

‘Naona ndio yeye, namba ni zile zile...’akasema mwingine.

‘Ndugu tunaomba uvue kofia yako, tunataka utambuliho mdogo...’akasema huyo mwingine.

‘Mimi siwaelewi, ...mnataka nini kwangu?’ nikawauliza

‘Tunataka kuhakikisha kuwa ndio wewe au ni mtu mwingine...’akasema

‘Mnataka kuhakikisha nini, mimi siwaelewi, ...’nikasema kwa mshangao

‘Kama hutaki hakuna shida, ...hapa hatuwezi kukufanya lolote, muda ukifika, kama ni lazima, hutakuwa na muda wa kujitetea,...maana siku hizi kila mtu anajifanya mwandishi wa habari,...’akasema

‘Mimi sio mwandishi wa habari..’nikasema

‘Tunafahamu hilo, kuwa wewe sio mwandishi wa habari, ila unaiga kazi za watu kwa ajili ya utapeli,....kama ni wewe uliyefanya hivyo, tunakuonya uwe makini, maana umechezea kubaya...’akasema

‘Msinitishe kabisa nyie, mimi sifanyi kazi hiyo, kama mumetumwa, mwambie huyo aliyewatuma kuwa mimi siogopi kitu....na ole wenu nipate matatizo, nimeshawamaki sura zenu, nitahakikisha mnaenda jela...’nikasema kwa kujiamini.

‘Hahaha jela...ohoo,kwa taarifa yako,  huko ndipo nyumbani,...usijali,...jana tu mwenzangu katokea huko, ....’akasema na kumwangalia mwenzake, na walipoona watu wanakuja kujazana, wakakimbilia kwenye gari lao na kuondoka.

 Tukio hilo lilinifanya nizidi kuwa na wasiwasi, niliona sasa maisha yangu yapo hatarini, na yote haya ni kutokana na mdada, na sijui wamejuaje kuwa mimi siku hiyo niliigiza kama mwandishi wa habari kwa shinikizo la mdada,.....

‘Mdada kanitia mashakani, sijui nitafanya nini....’nikasema na huku naendelea na safari yangu hadi nikafika nyumba anapoishi mdada, akanifungulia mlinzi, na mlinzi aliponiona akasema;

‘Ohooo, mhasibu wa bosi umerudi tena...’akasema huku akifungua geti, na nilipoingia ndani nikamuuliza

‘Mdada yupo?’ nikamwangalai huku naangalia muelekea wa mlango wa ile nyumba, ulikuwa wazi

‘Unamuita kwa jina, ...huna nidhamu, eeh, sema bosi yupo,...simzarau bosi wangu, na ni bosi wako pia, au sio,...?’akasema huku kashika kiuno, halafu akawa kama kashituka akashusha mikono na kusimama kama askari, akasema;

‘Yupo, kajaa tele huko ndani, kaniambia kuna mgeni wangu atafika, sijui ndio wewe..ngoja nikamuulize...’akasema huku akiliangalia pikipiki langu kwa macho ya hamasa.

‘Mbona unaliangalia sana pikipiki langu?’ nikamuuliza na yeye akatabamu, na kuendelea kuangalia, na sasa alikuwa akiangalia namba za hiyo pikipiki,akatikisa kichwa kama kukubali

‘Sikukosea ndio hiyo hiyo...mimi ni mkali, ikufaulu kwa sababu ya umasikini, ningelikuwa mbali sana...’ akasema sasa akilishika shika na baadaye akasema;

‘Hata hivyo mimi nimelipenda sana hilo pikipiki,..naona hata watu wanaliulizia, ....’akasema halafu akasita kuongea

‘Wamekuulizia kuhusu nini?’ nikamuuliza

‘Mhh, nahisi wanakutafuta,au wanamtafuta mtu...’akasema

‘Akina nani hao watu?’ nikamuuliza

‘Siwajui bwana...tatizo lenu hamjui kula na vipofu...mmhh’akasema huku akiweka mikono mfukoni, akapiga miayo, halafu akageuka na kujifanya anaondoka, na mimi nikakumbuka safari iliyopita, nikatoa pesa mfukoni, nikamsogelea na kumhika mkono wake, halafu nikamshikisha ile pesa kwenye mkono wake, akaipokea kwa haraka na kuifutika mfukoni, akasema;

‘Mhasibu wewe bwana, unanijulia, maana nyie muda wote mnacheza na pesa, nyie hamlali na njaa,...unajua leo nilikuwa najiuliza nitakula nini, ...haya niambie,umeniuliza swali gani vile...?’ akageuka kuniangalia

‘Hao watu walioulizia pikipiki langu ni akina nani?’ nikauliza

‘Hawa watu bwana kwanza niliwashitukia, wao walikuja wakaanza kuniongelesha, wakijifanya watu wa ukaguzi wa mejengo, wakataak kujua mmumiliki, baadaye ikaona wanakuja na mengine, eti wanataka kufahamu ni mtu gani anafika fika hapa kwa mdada mara kwa mara, ...sijua lengo lao ni nini....wakanizuga mpaka, nikajikuta nimekutaja wewe kuwa uliwahi kufika, ...’akatulia

‘Kwanini unitaje, kwani walitaka kujua  nini hasa?’ nikamuuliza

‘Walitaka kujua ni nani anatembea na bosi mwenye pikipiki...nahisi wana mtu anamtaka bosi, nikawaambia bosi hahitajii watu wenye mkono mfupi,...wakauliza ni nani alifika hapa karibuni, nikawaambia bosi ni mtu mkubwa, ana mhasibu wake anakuja na pikipiki...’akasema

‘Ukawaambia hivyo?’ nikauliza

‘Ndio nilitaka kuwaonyesha kuwa bosi sio mtu mdogo kama wanavyofikiria wao,...na nilipotamka pikipiki, nikaona wakipeana ishara,...’akasema

‘Halafu wakasema nini?

‘Wakauliza namba za pikipiki yako, na mimi nikataka kuwaonyeshe kuwa mimi ni askari wa kweli, anayeweza kukariri namba kwa dakika chache,...kichwa changu sio mchezo, nilishaiweka namba ya pikipiki lako kichwani, nikawatajia namba ya pikipiki lako...baadaye wakaondoka....’akasema na hapo nikakumbuka wale watu walionisimamisha,..

‘Hao watu wapoje?’ nikamuuliza

‘Ni watu tu hivi, inaonekana ni wale wapuuzi wa mitaani kazi yao kupewa kazi, na hawaulizi kazi gani wanaifanya tu....watu wabaya sana hao, hata kuua wanaweza kuua kwasababu ya pesa...’akasema

‘Kama unafahamu hivyo kwanini ukaawaambia kuhusu mimi?’ nikamuuliza

‘Mwanzoni nilijua ni watu tu....lakini nilipofikiria sana na kujaribu kuwakumbuka ndio nikafahamu ni watu gani....lakini usijali, hawana lolote wale, wanatafuta ujiko kwa mtu wao, aliyewatuma, nahisi kuna mtu kawatuma kuangalia kama mdada ana mshikaji,...’akasema

‘Basi naomba ukamwambie mdada, nimeshafika...’nikasema na haraka akaenda na pindi akarudi na kuniambia mdada yupo tayari kuniona...

Nikaingia ndani na kumkuta mdada, akiwa kakaa kwenye sofa, huku kaweka miguu juu ya sofa kubwa, ni kama mtu aliyelala, na nilipoingia akawa ananiangalia moja kwa moja usoni, bila kupepesa macho, mpaka nikaingiwa na wasiwasi tena.

Baadaye nikamkaribia na kusimama nikawa na mimi namwangalia akatabasamu na kuuliza

‘Unaniogopa?’ akauliza huku akiendelea kuniangalia?

‘Kwanini nikuogope?’ nikamuuliza huku nikjaribu kutabasamu, lakini kiukweli moyoni nilikuwa na wasiwasi nikikumbuka tukio la siku ile.

‘Mbona huji kukaa karibu na mimi....njoo ukae hapa karibu na mimi..uiniogope....’akasema na mimi nikasita kidogo, lakini nikaona nisimfanye ajisikie vibaya nikaenda kukaa karibu naye, na akainuka na kushusha miguu chini, halafu akapitisha mkono wake nyuma ya mgongo wangu akawa kama ananiegemea, kama kudekea, akatulia kwa muda, halafu akaniangalia na kusema;

‘Nilikuwa na wasiwasi sana...’akasema

‘Wasiwasi wa nini mdada?’ nikamuuliza

‘Nilikuwa nawaza, huenda nilikuumiza, au hata kuku...ku..ua...’akasema kwa kusita

‘Kuniua, kwanini unie, kweli unaweza kuniua...hapana huwezi kufanya hivyo, ...’nikasema nikichelea kuongea zaidi.

‘Mhh,... ni kweli nahisi hivyo, ...maana huwa hali ikibibadilika, huwa sijitambui, na wala sijui yanayotokea muda huo..., lakini ninachojua mimi ni kuwa kuna hali , hasa nikianza kukumbuka mambo ya nyuma, ninakuwa na hasira mbaya sana, na muda huo siogopi, naweza hata kuua...’akasema huku akitikisa kichwa kama mtu aliyeguswa na mdudu nikamwangalia kwa mashaka.

‘Pole sana mdada, cha muhimu kwasasa ni kuangalia afya yako, kwani unajisikiaje kwa sasa...’nikamuuliza.

‘Najisikia kuwa na wewe karibu, na natamani kukushika hivi....’akanishikilia na kuwa kama ananikumbatia, na mimi nikawa najaribu kujitoa kwake, lakini nikakumbuka kuwa sitakiwi kumkasirisha, nikatulia, halafu yeye akaniachia na kusema;

‘Najua utakuwa unaniogopa, kuwa huenda hali kama hiyo iliyotokea,inaweza ikarudi tena, ni kweli bado kichwa hakijakaa sawa, inachukua muda, lakini hata hivyo, nakuomba, usiniogope, maana kama ungekuwa kama hao wanaume wengine, nahisi leo hii tungeliongea mengine, akili yangu inanituma kuwa wewe ni wangu...’akasema

‘Mhh, kwani uhisi hivyo, huwezi kufanya kitu kibaya kwangu...mmh, kwani ulishawahi kufanya hivyo kabla?’ nikamuuliza na yeye akainama na kushika shavu.

‘Waliniambia mengi, na sijui, sina uhakika...ila walisema, yule aliyenifanyia hivyo, nikiwa mdogo....hayupo duniani tena,...walisema siku nilipokutana naye, nilimfanya kitu kibaya sana, hakuna aliyeamini kuwa ni mimi nilifanya hivyo, ndio maana wakayamaliza kiaina....’akasema huku akipandisha miguu juu ya sofa akawa kama anajikunyata

‘Mungu wangu ulimfanya nini huyo mtu...?’ nikamuuliza

‘Nilimuua....nikamkata kata...’akasema na mara akasimama na kuanza kushikilia kichwa

‘Mdada, upo safi...?’ nikamuuliza

Na yeye akanionyeshea kwa mkono kama ishara ya kuniambia nitoke humo ndani haraka..lakini kabla sijafika mlangoni akanidaka,na sauti ile ile ya kiume ikaniambia;

‘Nilichokuita hapa ni kuwa,...ni lazima na wewe ufe,.....lakini huyu kiti wangu anajifanya kukupenda, sasa kama kweli anakupenda,... nataka umuoe huyu kiti wangu, na mimi nitamuachia kabisa, vinginevyo, kama usipomuoa yoyote utakayemuoa, hataweza kuishi na wewe atakuwa maiti...hahahaha..haya ondoka kajiandae kwa harusi...’akanisukuma kwa nguvu nikadondokea nje...

Nilidondokea nje, na haraka haraka nikiwa na wasiwasi..., na mara sauti kama ya yowe ikatoka ndani kwa mdada, nikasimama kugeuka kumwangalia,...wakati huo mlango bado ulikuwa wazi,... nilimuona mdada akiwa kama anayumbayumba na mara akadondoka sakafuni, akatulia kimiya, na mimi pale niliposimama nikawa najiuliza nifanye nini...

Simu yangu ikaita, ...nikaangalia alikuwa ni bosi, nikaipokea na kusema

‘Ndio bosi...

‘Kuna usalama huko, mdada anaendeleaje?’ akaniuliza

‘Hali imebadilika ghafla...’nikasema

‘Ondoka hapo haraka, ....nitampigia simu dakitari wake, aje hapo...’akasema na kukata simu, na mimi nikaushika mlango na kutaka kufunga, mara mdada akajitingisha, na kuinua kichwa, akasema kwa sauti yake ya kawaida;

‘Usiondoke, ...sitakuambia nilichokuitia....’akasema


********

Nilikuwa nje ya geti la nyumba ya mdada, nikiwa najiandaa kuondoka, mara gari la bosi likaja, na nyuma yake kukaja gari jingine likuwa na mwendo kasi, likasimama nyuma ya gari la bosi na kupiga honi, bosi akasogeza gari lake, na hilo gari jingine likaingia ndani,nahisi lilikuwa gari la huyo dakitari wa mdada, bosi akaniuliza.

‘Vipi bado upo hapa, mdada anaendeleaje?’ akaniuliza hakuingiza gari ndani, na bado alikuwa ndani ya gari,lakini alikuwa akiongea na mimi akiwa kashusha kiyoo cha gari lake.

‘Mdada alikuwa kama kapoteza fahamu hali ilipomrejea, na alipozindukana akaniambia nisiondoke, hata hivyo mimi naogopa huenda akizindukana anaweza kufanya lolote dhidi yangu....’nikasema

‘Kwani ilikuwaje?’ akaniuliza

‘Nilipofika tu, akawa anaelezea, kuwa alikuwa na wasiwasi, kuwa huenda aliniumiza au hata kuniua...nilijaribu kumsihi asiongelee hayo mambo, lakini kila tulipojaribu kuongea mambo mengine, ikawa mara kwa mara anajikuta akiongea jambo linalogusa mambo yake ya huko nyuma...’nikatulia kidogo

‘Kama lipi aliloliongelea ambalo lilifikia hatua ya kumfanya abadilike...?’ akaniuliza

‘Alisema mimi nisimuogope maana sipo kama wanaume wengine, kama ningelikuwa sawa na wanaume wengine, huenda angalishanifanya kitu kibaya,...’nikatulia

‘Hivyo tu,..nahisi kuna jambo atakuwa akliongelea likampandisha hasira, mliongea nini zaidi...?’akauliza bosi

‘Alisema huenda huko nyuma alishawahi kuua....’nikasema

‘Kuua, hapana...hiyo sio kweli...!?’ bosi akawa kama kashituka kusikia hivyo, akageuka kuangalia kule mlangoni, akasema

‘Hilo liachie hapo hapo....kama alisema hivyo, huenda alisema kwa kuchanganyikiwa, usije ukamsimulia mtu hayo maneno tena,...je kuna jingine zaidi ya hilo?’ akaniuliza

‘Mhh, hilo jingine ni kubwa zaidi, linanifanya niogope,...’nikasema

‘Lipi hilo,...amesema na wewe atakuua, au kitu kama hicho, ndio unaogopa?’ akaniuliza

‘Kasema ni muoe...la sivyo...’nikatulia

‘Atakuua..’akamalizia, bosi,

‘Mhh, kitu kama hicho, ..ila kwa kauli ya moja kwa moja alisema nitakaye muoa na kumuacha yeye, huyo mwanamke atakuwa maiti...’nikasema

‘Mhh,....unaonaeeh, kazi ipo, lakini, hayo ni maneno tu, yasahau kwa sasa...cha muhimu ni huyu mtu apone na asahau mambo yake ya nyuma, na mimi naanza kuhisi kuwa wewe unaweza kuwa msaada wake mkubwa, maana naona kakuamini sana..’akasema bosi.

‘Lakini bosi mimi nina mchumba wangu tayari, ambaye siwezi kumuacha,...na kama akisikia hivi nitakuwa matatani....’nikasema

‘Sasa utafanya nini..hata hivyo sijakushauri kuwa umueche mchumba wako, yote ni maswala ya muda, cha muhimu, ni kumsaidia huyu mtu apone,...mengine yatajileta yenyewe....’akasema

‘Mhh, hayo sasa yananiweka kubaya, hujui yaliyotokea huko kijijini, .....mkwe wangu hataweza kuvumilia haya,akisikia ataniweka ndani...’nikasema

‘Lakini kama ulifahamu hivyo,..kwanini ukajenga urafiki na mdada, unakumbuka tangu mwanzoni nilishakukanya sana kuhusu mdada, ....’akasema bosi.

‘Sasa nitafanya nini bosi?’ nikamuuliza

‘Kwanza malizana na mdada,...ni muhimu mkamalizana naye haraka iwezekanavyo, ili ajijue nafasi yake, ...’akasema

‘Kwa vipi?’ nikamuliza

‘Katika maisha hakuna jambo jema, kama kuambiana ukweli, ...nikuanavyo wewe kiukweli unampenda sana mdada, na huenda kuliko hata huyo mchumba wako,...kosa mnalolifanya ni tamaa, mnashindwa kudhibiti tamaa zenu,...’akasema bosi.

‘Tamaa, lakini mimi sikuwahi, kumtaka mdada, ni yeye....’nikakatisha maneno.

‘Alikushika kwa nguvu, alikutaka yeye kwa nguvu, siamini kuwa mdada anaweza kufanya hivyo, yeye ni mwanamke tu,...au hiyo hali iliwahi kutokea ikakulazimisha kumtaka huyo mdada kwa nguvu...?’ akaniuliza.

‘Hapana haijawahi kutokea kabla, kama ilivyotokea hivi sasa...’nikasema

‘Sasa ni hinikizo gani lilitokea hadi uwe mpenzi wako, maana sizani kama anaweza kukuambia maswala ya kuoana, kama hakuna mapenzi, mahuiano ya karibu,..hebu niambie ukweli kulitokea nini?’ akaniuliza

‘Bosi hakuna kitu kama hicho, naona mdada ananishinikiza tu, na sizani kama anafanya hivyo kwa ajili ya mapenzi ya kweli....’nikasema

‘Mimi namfahamu sana, mdada, kiukweli anakupenda sana,...na nina uhakika mkiwa naye pamoja, hilo tatizo lake litakwisha, nahisi anakuona wewe kama msiri wake, na unaweza kumvumilia, kama hakuna shinikizo jingine ambalo hutaki kuniambia...’akasea bosi.

‘Hakuna shinikizo jingine bosi...ningekuambia...’nikasema

‘Haya kama unanificha shauri lako,..’akasema na tukawa kimiya kwa muda, halafu akasema;

‘Ingia ndani ya gari, wakati tunamsubiria dakitari akimalizana na mdada, nikuhadithie sehemu nyingine ya mfulululizo wa visa vya maisha yangu...’akasema bosi

‘Kwahiyo nisubiri?’ nikauliza

‘Kama mdada alipozindukana alikuambia umsubiri, ni vyema ukafanya hivyo, huenda kuna kitu muhimu anataka kukuambia...’akasema

‘Sawa haya ...nitashukuru kusikia simulizi la maisha yako huenda likaniondoa haya mawazo na wasiwasi niliyo nayo..’nikasema

*******

‘Kwenye sehemu iliyopita, unakumbuka vyema kuwa tulifikia pale nilijifungua, kuwa mungu alinijalia nikajifungua salama, na kesho yake ndio nikaruhusiwa kutoka hapo hospitalini maana sikuwa na tatizo lolote. Na muda wa kutoka mume wangu alikuwa hajui, kwani niliporuhusiwa tu mimi nikaondoka hapo hopitalini, hata hivyo, kwa vile nilikuwa nafahamu kuwa mume wangu alikuwa anaumwa, sikupenda kumsumbua kuwa aje kunichukua.

Nilipotoka hapo hospitalini,  nilielekea moja kwa moja nyumbani, na nilipofika nyumbani ilikuwa muda wa mchana, niliwakuta wanafamilia wote wakiwa wanapata mlo wa mchana,hakuna aliyejali kusimama kunipokea mtoto, au ile hali yakuonyesha kuwa nimemleta mgeni, basi kila mmoja awe na bashasha ya kumuona, na kumpokea, hawakufanya hivyo, tofauti na alivyopokelewa mtoto wangu wa kwanza.

Sikujali, mimi nilipitiliza moja kwa moja na kuelekea kwenye kibanda changu, kile kibanda ambacho kila kitu kinafanyika humo humo, nilijua hakutakuwa na huruma kuwa kwa vile nina mtoto mchanga, nikalale nyumba kubwa yenye nafasi, hata mimi sikupendelea iwe hivyo, maana ningelikuwa sina amani zaidi.

Nilipofika kwangu, nikishindwa hata nianzie wapi,nikaona ni bora kwanza niondoe kwa kujimwagia maji, nilipofanya hivyo, nikamuogesha mtoto wangu.

Bahati nzuri nilikuta ndizi, nahisi mume wangu alinunua kwa ajili yangu, lakini hakuweza kuzipika, mimi nikazichemsha, ili niweze kupata japo kitu tumboni ili mtoto apate maziwa..baada ya hapo nikaona nipate usingizi kidogo...

Kweli nikapumzika na kujihisi kama mtu aliyetua mzigo mkubwa ..mzigo niliokuwa nao miezi tisa, nikamgeukia mtoto wangu, kumwangalia alikuwa kalala, na nikimwangalia nikawa naona faraja na kujihisi mwenye bahati, nikukumbuka kauli ya dakitari ya kunikatisha tamaa, kuwa nimechelewa kufika.

Huku namwangalia mtoto wangu, huku nawazia maisha yaliyopo mbele yangu, maana hapo nina mtoto mchanga, nina mwingine ambaye naye bado mdogo,...ina maana natakiwa kuwahudumia, bila kukata tamaa, na kazi yenyewe ni ya duka, na hivi sasa ina maana kazi imesimama, maana mume wangu ana migangaiko yake, asingeliweza kukaa dukani

Na hali kama hiyo, ilinifanya niombe mungu niwe na nguvu haraka, hata ikiwezekana kesho yake nikaendelee na kazi yangu, ili tupate riziki,..lakini isingeliwekana kutokana kiafya, ....hata hivyo kazi za nyumbani zipo pale pale, usafi wa ndani, kufua nguo, hasa za mtoto, hilo sikuwa na mtu na kunisaidia, na wakati nawaza hilo, mara mlango ukagongwa.

‘Karibu, mlango upo wazi...’nikasema

Akaingia msichana wa kazi, ...wa familia, akiwa kabeba chakula, nikashangaa sana, nikajua hapo huenda wameingiwa na huruma na ndugu yao,ambaye anaumwa, ndio maana wameleta chakula, kwa mshangao nikakipokea hicho chakula.

Nikamuamusha mume wangu kuwa ajaribu kupata hicho chakula , na kwa ujumla hicho ndicho tulichoweza kupata kutoka kwao, bila kujali kuwa mzazi ana chakula chake maalumu, lakini sikujali.

Usiku huo nikalala fofo, ilikuwa kama mtu ambaye hajawahi kulala kwa muda mrefu na akapata mwanya wa kulala,..unalala hata bila kugeuka, na kulipopambazuka tu, nilipomaliza kumnyonyesha mtoto, nikasema hakuna kupoteza muda,nikaanza kazi za ndani kufua nguo chafu, kwani unapojifungua nguo nyingi zinakuwa chafu, usafi wa ndani... kazi ilikuwa kama kawaida.

‘Mke wangu utajiumiza, kwani ni lazima ufanye kila kitu, muombe huyo mfanyakazi wa familia akusaidie....’ akasema mume wangu.

‘Nitafanyaje, huoni wanavyotusimanga, ni lazima nifanya kazi zangu mwenyewe...’ nikasema na yeye akawa hana la kujibu. Ilibidi niwe ninaamuka asubuhi kufanya usafi kufua nguo za mtoto, na pilika pilika zote za nyumbani bila kupumzika, kwani yule mfanyakazi wetu alishaondoka kwao, kwa vile hatukuwa na cha kumlipa, aliyekuwa akisaidia mara moja moja ni mfanyakazi wa familia.


Nilifanya kazi zangu zote bila kuchoka na kujisahau kama nimetoka jana tu kwenye leba ya uzazi,ila sikuwa na jinsi niliangalia nyumba kama mtu niliye kuwa mzima wa afya kabisa,ila kama unavyojua hasara yake inakuja badae nilipoanza kupata maumivu ya mgongo kupita kiasi. Mgongo ukawa unaniuma, lakini nitafanya nini.

Kuna muda niliingiwa na wazo la kuwaambia wazazi wangu kutokana na hali iliyokuwa hapo, ili kama wanaweza kunisaidia,lakini nilikumbuka nilivyowaambia mwanzoni na kauli yako ilinikatisha tamaa;

‘Unasema nini, hayo ndio maisha ya ndoa, vumilia, ndoa ndivyo ilivyo, kuna mitihani ya kukosa na kupata...’akasema baba.

‘Lakini baba ni msaada wa muda, nikijifungua, maana nijuavyo, pale sitapata msaada wowote...’nikamwambia.

‘Tulishakusaidia mtoto wa kwanza, huyu sasa ni jukumu la familia yako,....’nikaambiwa

Nilihangaika na kazi za nyumbani, na kidogo kilichopatikana kutoka kwa mume wangu, tukawa tunakula hicho hicho, kwani alishajisikia vyema na kwenda kuhangaika.

 Baada ya mda kidogo nilirejea katika biashara zangu na kazi zangu za kila siku, hapo ilibidi nijipange jinsi ya kule watoto na jinsi ya kuhangaika na biashara, hakuna aliyetaka kunisaidia, na wakiona nahangaika hivyo bila kulalamika, ndio wanzidi kunipandikizia fitina.

Sikujali niliwaangalia watoto wangu wawili kadri ya uwezo wangu, japokuwa kuna muda shemeji alikuwa akimchukua huyo mtoto mkubwa, lakini sikuwa na amani kwani hata akimchukua na kwenda kukaa na wenzao, yeye alikuwa akitengwa, na kunyanyapaliwa;

‘Wewe mdowezi, wewe upo hivi....’akawa anaambiwa, na mimi hali kama hiyo sikuweza, niliona ni bora nikae na watoto wangu wakati wote.

Kuna mda watoto wanacheza pamoja, ikitokea ugomvi tu, anayeangaliwa kuwa ni mbaya ni mtoto wangu, vurugu zikawa kila siku, visa vya kuzuliwa vikawa vinaongezeka kutoka kwa mawifi.

Mimi nikawa nasononeka moyoni, kwani sikufahia kuona watoto wangu wanatengwa na kunyanyaswa na ndugu za mume wangu niliumia ila sikuwa na jinsi ,nilikaza moyo na kukabiliana na kila linaloninijia...hata hivyo, ilikuwa kama wanataka kunikomoa kwani kila siku kulikuwa na jipya la hakuna aliyekuwa upande wangu niliona hata mume wangu hakuweza kunisaidia tena.

Mambo yalikua magumu mpaka nikakumbuka usemi kuwa kuolewa ni tabu ,ndoa ni ndoana,..na kama ni taabu bai mimi ilizidia, na kama ni ndoa basi mimi ilikuwa imenishika pabaya.

‘Mungu wangu nakuomba unisaidie niondokane na mateso haya...’nikawa mara kwa mara namuomba mungu wangu.

Ilikuwa kama walikamia kuwa wanionyeshe kila aina ya uovu kwangu, zaidi sasa walilenga kwa watoto, nikawa sina amani, nikiona watoto wangu wanapigwa, wanatukanwa, hawana raha na wenzao, nikasema sasa basi, lakini basi nifanye nini

Wazo likanijia, kuwa nihame kabisa kwenye hiyo nyumba, maana kinachotutesa , hasa watoto, ni kuwa ni lazima watataka kucheza na wenzao, na wakicheza na wenzao, ndipo kunapotokea visa, ili waonekane wao ni wabaya, na kusimangwa kuwa wao ni masikini, omba omba....

Nikaona basi, ... nikasema basi sasa inatosha, ni lazima nitafute njia nyingine, ni lazima nitoke hapo, nikaanza kutafuta chumba au nyumba ya kupanga. Hilo kwanza nililifanya kimiya kimiya bila hata kumjulisha mume wangu

Kwa bahati nzuri nikapata nyumba ya bei rahisi kati kati ya mjini, nikauza baadhi ya vitu vyangu vya dhahabu vilikuwa vimebakia na kupata kodi ya kuanzia na nilipohakikisha nimefanikiwa hilo, ndio nikaja kumwambia mume wangu kuwa nimepata nyumba, kwahiyo tunahitajika kuhamia kwenye nyumba hiyo;

‘Wewe una akili kweli, tutapata wapi kodi ya kulipia hiyo nyumba?’ akaniuliza

‘Swala la kodi niachie mwenyewe, cha muhimu ni kujiandaa kesho tunahama hapa...’nikamwambia na yeye akaniangalia kwa mashaka, hakusema neno, akakubali shingo upande.

Kuondoka hapo, sikuchukua chochote zaidi ya godoro, tukaenda kuanza maisha mapya, ya kununua kila kitu...ilikuwa ni kazi nzito lakini hatukuwa na jinsi, tukajitahidi hivyo hivyo,lakini tukiwa na uhuru, hakuna mtu wa kutunyanyasa tena.

Tukiwa katika maisha hayo magumu, nikawa naingiwa na hamasa ya kufanya kitu kikubwa zaidi, nikijiuliza iweje wengine wafanikiwe, waweze mimi nihindwe, na hapo wazo la shule, yale tuliyojifunza kuhusu mikopo, na jinsi nilivyosikia kwa watu wengine, kuwa mikopo inaweza kutumika vyema, na kuleta maendeleo, hilo wazo lilinijia kichwani na hamasa ya kupata mkopo ukanijia....nikaona na mimi lazima nijaribu kuchukua mkopo.

Baada miezi kadhaa ya kuliwazia hilo huku nahangaika na biashara yangu hiyo, ikafikia muda nikasema sasa naweza, ....nikichukua mkopo nitaweza kupata marejesho ya miezi kadhaa, hadi deni kuisha,...hata hivyo sikutaka kukukimbilia mikopo mikubwa, na sikutaka kukimbilia benki, nikaona nimtafute rafiki yangu yoyote mwenye uwezo, nichukue kutoka kwake.

Nikamkumbuka mmoja wa marafiki zangu, yeye ni mfanyabiashara na alikuwa yupo kiwango cha juu, nikaona nimjaribu yeye kwanza, na siku hiyo nikamtembelea kwenye shughuli zake,na nikaongea naye;

‘Rafiki yangu, nimekuja nina wazo ...nina maombi, naona bishara yangu inasua sua, na wateja kweli wapo, lakini nina shida, ya mtaji, mtaji wangu ni mdogo sana...’nikasema

‘Kwahiyo unataka kusema nini?’ akaniuliza.

‘Kama unaweza kunikopesha mkopo kidogo, ili niweze kuongeza bidhaa kidogo’nikamwambia.

‘Lakini mimi sio benki, na wala sifanyi kazi ya kukopesha.....'akasema

'Nafahamu hivyo, lakini unaweza ukawa na akiba, au ukajitolea ili kunisaidia mimi rafiki yako..'nikasema.

'Ni kweli, wewe ni rafiki yangu na napenda sana kukusaidia, lakini maswala ya mikopo yana mitihani yake, mikopo imevunja udugu, na urafiki, ninaweza kukukopesha,ikaja kuwa mtihani kwangu, hasa kwenye marejesho, je ulishaongea hilo swala kwa mume wako? 'akaniuliza.

‘Mume wangu hana matatizo, yeye ana shughuli zake, na shughuli ya duka ndio tegemezi letu, hata nikimwambia hataweza kulipinga....’nikasema.

‘Ili nikukopeshe ni vyema umwambie kwanza mume wako akikubali sawa...mimi nitakukopesha kiai nitakachoweza..., sio kwamba sikuamini, lakini maswala ya mikopo yana mitihani yake kuna leo na kesho...’akasema


NB, je mume atakubali, na akikataa itakuwaje, ...


WAZO LA LEO: Maendeleo hayaji kirahisi, wakati mwingine, kuna vikwazo vikubwa ambavyo vinaweza kukufanya ukafikiria mambo mengine mabaya. Tujue kuwa matatizo ni sehemu ya maisha, na huenda kwenye matatizo hayo ndio unaweza ukajenga usugu,ujasiri na uzoefu, wa mafanikio . Badala ya kukata tamaa, tuyatumie matatizo na shida zetu, kama njia ya kutufunua akili, kwa mafanikio,...Tujaribu, tusiogope kwa nia njema, tutafanikiwa.
Ni mimi: emu-three

No comments :