Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Friday, August 23, 2013

WEMA HAUOZI-54


Mwanangu wakati mwingine haki inaweza ikawa ngumu kuipata, lakini kama unafahamu kuwa ni haki yako katu usikate tamaa,…itafute, kwani usipoitafuta wengine wanaweza kutumia mwanya huo kukunyang’anya haki yako. Mimi ninawashukuru sana wote walihakikisha kuwa haki yangu inapatikana, hasa mwanadada na kundi lake…’mama akaendelea kumuhadithia mwanae.

Ni siku ambayo mwanadada alirejea kutoka huko msituni walipokwenda kumtafuta mtaalamu, na wakati wanaondoka ilijulikana kuwa wanakwenda kumuomba aweze kubainisha zile sumu mbili ni ipi iliyokuwa sahihi, ili kuweza kuziwakilisha mahakami, ….

Na ilitajiwa kuwa haitachukua muda, masaa yalizi kwenda na jioni ikawa inagia, na hapo kila mwenya laki akaanza kulitoa moyoni, na hata mimi ilifikia muda nikakata tamaa kabisa hasa nikisikia maneni ya watu, kwani mengi yalianza kuongolewa, hasa yakihusishwa na imani za huo msitu na mambo ya kishirikina yaliyogubika hicho kijiji, eti kutokana na kesi yetu ilivyokuwa, wanadai eti mizimu imeshakasirika eti kwa vile mimi mwanamke ninadai haki ambayo ilitakiwa idaiwe na wanaume. Na wanadai kuna kiwingi cha popo,kimeonekana kikitokea milimani, na hiyo ni ishara ya kukasirika kwa mizimu.

Na wakati nawaza hivyo, akanitembelea mama mkwe, na tukawa tunaongea na yeye kama walivyokuwa akina mama wengine wenye umri kama wake, akaanza kunilaumu. Ikabidi nianze kujitetea kwa kusema;

‘Kwanini mimi nisiwe na haki wakati hiyo ninayodai ni jasho langu, ni pesa yangu niliyojengea hiyoo nyumba na duka, na kama tatizo ni kujenga kwenye eneo la familia, au eneo la marehemu mume wangu, lakini mimi pia ni mwanafamilia, mimi ni mzazi wa mtoto ambaye mnamtambua kama mwanafamilia…’nikawa najitetea lakini ilionekana kama mimi naleta siasa mpya kwenye familia.

‘Mizimu inakasirika mwanangu, kwingi cha hawo ndege, sijui ni ndege au ni wadudu, kimeonekana kikitokea milimani, hiyo ni ishara mbaya, hii inabashiria jambo baya limetokea,…na wengi wanahisi ni kwa vile wewe unataka kumiliki mali kama mwanamke, unataka kumiliki kitu ambacho ni wanaume tu wanastahili kumiliki, na pili wewe ulitakiwa urithiwe na mmoja wa wanafamilia ukakataa kwa vile unajiona unajiweza….mwanangu mimi kama mama mkwe wakp nakuomba ujirudi’akasema mama mkwe huku akiniangalia kwa wasiwasi, kama vile mimi ni kitu cha kuogofya.

‘Nikuulize mama yangu, mfano hiyo familia isingelikuwepo,…hawo wanaume wakunirithi wasingelikuwepo,  mimi nilitakiwa niweje, nikae tu, au nisimame barabarani niwe naomba,….?’ Akauliza.

‘Hayo ni mambo mengine, yanakubalika kama hali hiyo ipo, lakini hali kama hiyo haipo, wanafamilia wapo, wanaume wa familia wapo, kwanini ufikirie kitu ambacho hakipo,…nikuambia ukweli, wakati mwingine tusiwe na kiburi cha ubinafsi, kumbuka unapoolewa unatakiwa utii amri za hapo ulipoolewa, usilete mambo uliyokuja nayo…wazazi wako hawakukufunda kwa hilo, mimi sizani kuwa hawakukuelezea, ni kiburi chako tu….’akasema huyo mama.

‘Mama sijakataa mambo ya kifamilia, sijapinga mambo ya kifamilia, ila ninachotaka ni ile haki yangu, kama ulivyoona, sikutakiwa niseme nyumba hiyo nimejenga kwa pesa zangu wakati kweli nilijenga kwa pesa zangu, sasa imejulikana ukweli, kuwa nilijenga kwa pesa zangu, na nilijua kuwa nyie kama akina mama, wanawake wenzangu mungeniunga mkono….’akamwangalia mama huyo kwa macho ya huruma na mama huyo akatikisa kichwa kukataa.

‘Haki hiyo haipo….nielewe…haki ni yako na mume wako, na haki hiyo umefungwa ndani ya mamlaka ya mume wako,….mbona ni kitu kidogo tu cha kuelewa…..’akasema huyo mama akionyesha kukunja uso.

‘Mama hivi ni kweli,…unaamini hayo, hivi ni haki na kweli kuwa sisi wanawake, hatutakiwi, kudai haki zetu hata kama ni haki yako kiukweli, …mimi naona kuna walakini hapo, kama mzazi, baba wa watoto hayupo,ni nani anastahili kuchukua nafasi yake, ….lakini hata hivyo, hapo sidai kitu cha mtu,ninachodai ni kile change, je ni kweli kuwa mwanamke hastahili kumiliki kilicho haki yake,…ndivyo mila inasema hivyo, sio kwamba ni mbinu za watu wachache wanaotaka kunufaika na jasho la watu wengine….?’ Akauliza mwanamama.

‘Tatizo lako wewe ndio mnaojiita kizazi kipya, hatukuwezi…mbishi na una kiburi, na tabia kama hiyo kwenye ndoa haifai, …haifai kabisa, sisi wenzako tumeshaanza kukuogopa kuwa unatuletea vurugu kwenye familia, tangu uolewe kwenye familia  yetu, hatuna amani , kila siku unaongelewa wewe, sasa hebu angalia mabalaa ya msiiba inavyofululiza kwenye hii familia, hatujui itatokea nini tena huko, na mguu wangu huu ulikuja kukupa taarifa nyingine mbaya…’akasema na mwanamama akashituka

‘Taarifa gani tena hiyo mama, mungu wangu, isije ikawa ni ile ndoto…’akasema huku akishika kichwa kuashiria wasiwasi.

‘Ndoto gani, ..unaonaeee, hiyo ndio mizimu imekasirika, na inataka kutuadhibu, tunachoombea ni mtoto wetu huyo apone, lakini kama hatapona, hatuna budu kuchukua hatua kubwa zaidi, ili mkosi huu uondoke kwenye familia yetu…sisi akina mama wa familia itabidi tuingilie kati, maana utatumalizia watoto na waume zetu.’akasema huyo mama

‘Lakini kuna nini mama, mbona umefika na mambo  mara ya mzimu,mara sijui apone, kwani ni nani anaumwa? ….’akauliza na kumwangalia mama huyo na mama huyo akawa kaangalai pembeni kama vile anakwepa kumwambia huyo mama, kuashiria ni taarifa ya kutisha.

‘Mama kuna nini, mbona hutaki kunielezea hiyo taarifa, kuna nini , maana jana usiku niliota marehemu mume wangu kaja, akiwa amelowana damu, na kuniamba kuwa niende nikampokee shemeji yangu kituoni…’akasema

‘Ndio hay o hayo, unaona mpaka unaletewa ishara na marehemu mume wako lakini hutaki kuamini…damu maana yake ni nini, sio baalaa hilo…’akasema huyo mama, akasema akimwangalia mwana mama kwa macho kama mtu aliyeona kitu cha kuogofya.

‘Basi nikashangaa, na kumuuliza mume wangu,…marehemu, ….mbona mwili wako umejaa damu, kuna nini kimekutokea, …yeye akawa hasemi na alikuwa kasimama kwa mbele yangu, na nilipomuuliza hivyo, akainama kujiangalia,akawa kama anajishangaa, na kusema, mmh, ina maana damu hizi kanipaka ndugu yangu, …akageuka kurudi huko alipotoka, nikawa namuita ili anifahamishe zaidi lakini hakugeuka akatoweka, na mimi nikashituka kutoka usingizini…’akasema mwanamama.

‘Hiyo ndoto mama…binti yangu, hiyo ina ishara mbaya, ni mumeo alikutembelea kukupa ujumbe,…,kama angelikuwepo mtaalamu angekuagulia, angeitafsiri vyema hiyo ndoto,….lakini mtaalamu katoweka, nasikia alikuja mahakamani, na baadaye akasema anarudi kwa mizimu, I wanasema , kasema kuwa anatumikia kifungo kwa kukiuka baadhi ya masharti,…sijui mimi siamini hayo, yule mtu ni mtaalamu kweli, anasaidia watu, leo hii anasingiziwa ubaya….kama kuna kifungo, basi, tunamuombea amalize hicho kifungo, ili aje kutusaidia…’akasema huyo mama.

‘Huyu mtaalamu alivunja masharti au alikuwa ni tapeli tu, hivi mama kweli nyie mnamuamini huyo mtu, hamuoni kuwa ndio yeye aliyewapandikiza watu fitina kuwa mama mkunga ni mchawi, wakati sio kweli, je hizo ndizo kazi zake, hilo mumeliona, …'akasema na huyo mama akawa anamuangalia huyo mwanamama kwa macho ya dharau.

'Mama hebu jiulize ni mangapi aliyoyafanya ya hadaa ambayo hamjaambiwa,…Huyo atakuwa kahusikia na mambo mengi mabaya, pale mahakamani alikwua akijikosha tu…mimi simwamini hata chembe…’akasema mwanamama na yule mama akawa anamwangalia mwanamama kwa mshangao, na akainuka haraka.

‘Wewe mtoto, mbona wataka kutuletea balaa, unaongea kitu gani, hivi unamfahamu huyo mtaalamu, kila mnachoongea ndani, anakifahamu..hata kama unateta na mume wako chumbani kwa siri, kesho yake anakujia na kuwaambia yote mliyokuwa mkiongea wewe na mume wako…ole wako, ndio maana tunataka uondoke kwenye hii familia, kwani utatuletea majanga…wewe sio mtu mwema, kabisa,….’akasema

‘Ndivyo mlivyopanga hivyo…ndivyo mnavyojidanganya ehe…?’ akauliza mwanamama.

‘Wewe kuondoka haijapitishwa bado,…tulikuwa tunasmubiria huyo mwanasheria aje aitishe kikao, na sisi tutalitoa hilo hadharani, …lakini sasa unaona, kwa vile huyo kawa kiongozi, na anaukaribu na wewe, mabala yamemtokea, mkosi, …wewe mume hatakiwi akuguse,..sasa tunakuambia, kama mwanasheria atafariki, basi, hatuna budi kufanya hivyo..tutakufukuza…’akasema

‘Kama mwanasheria atafariki, kwani vipi, kwani anaumwa….mbona alikuwepo mahakamani akiwa na afya yake…?’ akauliza mwanamama kwa mshangao.

‘Mguu wangu huu ulikuja kwako kukupa hiyo taarifa, kuwa mwanasheria kaletwa kutoka msituni akiwa hajitambui, kapigwa risasi, ….na hali yake ni mbaya sana, na madakitari wanahangaika kujitahidi kama wanaweza kuokoa uhai wake, lakini inavyosadikiwa ni kuwa keshafariki, hayo mengine ni kupoteza muda tu na hiyo ndoto yako, mmh, naona ni hayo hayo..’akasema huyo mama na mwanamama akashika kichwa, akakaa chini, akasimama ….

‘Yupo hospitali gani?’ akauliza mwanamama

‘Unauliza hospitali gani, itakusaidia nini wewe, wakati wewe ndio mkosi wa familia, enenda huko ulipotoka, utuachie familia yetu, tangu uolewe hapa umekuwa ni gubu, tatizo,nuksi, hujioni….tunakuomba sana, kabla mambo hayajawa mabaya zaidi ufungashe uondoke..tuachie mjuukuu wangu maana huyo ni damu yetu, mimi sitashindwa kumlea…wapo akina mama zake wadogo watamlea…’akasema huyo mama, na mwanamama alikuwa hamsikilizi.

Mwanamama akawa anajiandaa kuondoka kwenda huko hospitalini hakutaka kumsikiliza huyo mama tena, alikuwa anataka kwenda kujionea mwenyewe au kusikia ni nini kimetokea kwa shemeji yake huyo.

‘Oh, samhanai mama, mimi inabidi niende huko hospitalini, ..’akasema mwanamama

‘Nakuuliza ili ukafanye nini, …kwani wewe ni dakitari, wewe ni mkosi tu, unachopeleka huko ni kilio, ambacho tunakisubiria muda wowote kitatangazwa, na hiyo kesi yako itaahirishwa, na ukiendelea nayo tena, janga jingine litatokea,…wewe mwanamke huna jema katika familia hii, ndio maana nimekuja kukushauri kwa nia njema uondoke…’akasema huyo mama, na kabla hajamaliza mlango ukagongwa.

Mwanamama akainuka haraka na kwenda kufungua mlango, na macho yake yakatua kwa mwanadada aliyeonekana kuchafuka na nguo zina alama za damu, alikuwa kachoka, na macho yake yalikuwa kama yamevimba, kama mtu aliyekuwa akilia, ..

‘Kuna usalama huko?’ akuliza yule mama alipoona mwanadada akiingia akiwa kachoka.

‘Usalama upo, msiwe na wasiwasi, sasa hivi mambo haya yanakwisha,….kila jambo baya lina mwisho wake, cha muhimu ni sisi sasa kuungana kwa pamoja, na kuwepo kesho kwa wingi mahakamani, lakini kwa jinsi ilivyo , huenda kesho kesi  inaweza isifanyike….tumeshapeleka maombi, kwani kuna mambo mengi ya kufuatailia, ikiwemo ushahidi mpya na muhimu uliopatikana huko msituni..’akasema mwanadada akijipweteka kwenye sofa.

‘Ushahidi gani tena, kwani mwanasheria alipigwaje risasi na huko msituni hakuhitajiki kutumiwa silaha?’ akauliza yule mama.

‘Yaliyotokea ni bahati mbaya, lakini ni katika kumkamata  huyo mhalifu wetu, na mwanasheria alijitolea mhanga, na ndipo ajali hiyo ikamkuta, lakini haikudhamiriwa iwe hivyo…’akasema mwanadada akimwangalia huyo mama.

‘Yote hayo ndio mikosi yenyewe niliyokuwa nikimwambia huyu mwenzako,… ndio maana nilikuwa namshauri huyu mwenzako, kabla hali haijawa mbaya zaidi, yeye ni bora aondoke, atuachie maisha yetu ya amani, kwani tangu afike kwenye hii familia ni mikosi…angalia hayo yanayotokea sasa..hamuoni hilo jamani….’akaana kubwabwaja huyo mama, na mwanadada akamkatisha na kusema;

‘Wewe mama, huyu mwanamama, hana mkosi wowote, ingelikuwa unaufahamu wa mbali ungelimshukuru sana huyu mwanamama,ungelikuwa una maono ya mbali, ungesema asante mungu umetuletea  nuru, huyo mwanamama ndiye nuru ya familia yenu, kwani kutokana na yeye mtaweza kufahamu haki zenu, zilizokuwa zimeanza kutekwa na mjanja mmoja…’akasema mwanadada.

‘Nakufahamu sana wewe, huwa unajiona umesoma, unajifanya unafahamu sheria, sheria na mizimu wapi na wapi…wao wana sheria zao,….huwezi kuwaangilia, …sikilizeni niwaambie, hamtafanikiwa kamwe….kwa mtaji huo mtaishia kubaya…..’akasema huyo mama akiinuka kutaka kuondoka, na akawa kama kakumbuka jambo, akauliza;

‘Na unasema huyo mwanasheria keshafariki au …ndio mnajidanganya kuwa atapona kweli…nasikia alishakata kauli, wakati analetwa, ilibakia kupewa maji tu…hawo madakitari wanachotaka ni ushahidi tu, ili kazi yao ionekane…’akasema huyo mama, na mwanadada akamwangalia huyo mama kwa jicho baya na kusema;

‘Wewe mama, ningeliongea vibaya kama usingelikuwa mama mkwe, mama chunga sana mdomo wako, jaribu kuwa na hekima, jaribu kutuliza moyo wako, na kuomba heri badala ya shari,…kumbuka japokuwa hujamzaa wewe lakini huyo ni mwanao, hukustahili kuongea hivyo…kwanini unamuongelea mabaya,unajua mama mabaya mengine tunajiumbia  sisi wenyewe bila kujua, huu sio wakati wa kuongea mambo kama hayo,….yule sasa hivi yupo kwenye mikono ya madakitari, na wanafahamu kuwa anaweza akapona, tunachotakiwa ni kumuombea apone,….’akasema mwanadada akijaribu kuzuia kutoa kilio.

‘Haya yetu macho, ila narejea kuwaonya, sisi ni akina mama tunametoka mbali, na tunafahamu sana mambo ya hapa,, nyie mumekuja juzi juzi tu hapa, hamjui vyema hii miji yetu hamjui mambo ya kimila, msipotulizana, mtaishia kubaya…na ilivyo, mwenzenu huyu ana mkosi, ana nuksi, …’akasema akianza kuondoka.

‘Sio kosa lako mama, ni kosa la elimu, ambayo imekuwa adimu hapa kijijini, ni kosa la wajanja walioamua kutumia udhaifi wenu huo, kuwapandikiza fitina na kuwajaza hofu. Watu hawo ni wabaya kuliko hata huyo mchawi mnayemzania kuwa yupo, hakuna mchawi,  mchawi ni nyinyi wenyewe…’akasema mwanadada na yule mama akasimama akiwa kaweka mikono kiuononi.

‘Unasema nini wewe binti, hebu rudio huo usemi wako tena, kuwa eti kuwa sisi ni wachawi,…’akasema huyo mama akiuma meno kwa hasira….

‘Mama naomba unielewe, labda  natumia lugha ngumu kwako ambayo unashindwa kunielewa, nasema hivi, hapa kijijini hakuna uchawi, hakuna kulogana, hizo ni hisia mlizopandikizwa kiujanja na huyo mnayemuita mtaalamu, ..kama ni mchawi , basi huyo mnayemuita mtalaamu, ndiye anayestahili kuitwa mchawi,..huyo ndiye mchawi wenu’akasema mwanadada akiinuka kutaka kwenda bafuni kuoga.

‘Mhh, nyie watoto nyie, …mbona mnaleta balaa, hizo kauli zenu zinanitisha, na naona ni bora niondoke hapa haraka msije mkaniangaiza na mimi, oooh, jamani kizazi hiki kina nini, hivi mnamfahamu nyema huyo mtaalamu, au mnamsikia tu…?’ akawa kama anauliza na mwanadada akasema

‘Tunamfahamu sana, yeye ni jambazi, tapeli, na mwizi, na kama ni mtu anayestahili kuitwa mchawi, basi huyo ndiye mchawi wa hiki kijiji,…..amekuwa akiwatapeli, kuwahadaa, na kuwapuambza kiakili, na hilo tumalithibitisha na yeye kakiri mwenyewe, na yupo tayari kuelezea kila kitu, mahakamani, maana za mwizi ni arubaini, na mwisho wa ubaya ni fedheha tu,…’akasema mwanadada akisimama na kumgeukia mwanamama, akasema

‘Mwanamama nakuomba ujitayarishe, tunakwenda hospitalini, nasikia mgonjwa alipata fahamu kidogo, akaomba kuwa twende ana mazngumzo na sisi, ni muhimu sana….’akasema na mwanamama ambaye bado alikuwa na mshituko akasema;

‘Mimi sina cha kujiandaa zaidi, …nipo tayari twende….’akasema

‘Huyo anawaita kuwaaga…ndio safari hiyo, oh, mwanangu jamani…’akasema na kujifanya analia, huku anaondoka

NB: Mbona hitimisho linakuwa mbali.


WAZO LA LEO: Uwoga ni udhaifu wa akili, na ukitawalia na hisia hizi za uwoga, kuogopa, mambo yasiyoonekana kama uchawi, na mamo kama hayo, utashindwa kufanya mambo ya maendelea,wakati mwingine, kwa udhaifu huo, tunageuka kuwa wachawi wenyewe, na kujiloga wenyewe, kwa kujiumbia matatizo, …..cha muhimu, ondoa hisia hasi, na jenga muelekeo chanya, kuwa inawezekana, na nitafanikiwa…huku ukijibidisha katika kutafuta mambo ya heri.

Ni mimi: emu-three

No comments :