Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Friday, March 18, 2016

SIKIO LA KUFA HALISIKII DAWA-20 (hitimisho 2)



Wakati tupo tunaongea na huyo mshauri nasaha,mara mlango ukagongwa na akaingia jamaa , akiwa na koti refu na mkono kauweka mfukoni kuonyesha kuna kitu kakishikilia, akasimama mlangoni, kwa muonekano wake nilitambua kabisa huyo ni askari,….

Docta akamwangalia kama anataka kumuuliza ana shida gani, nahisi hata yeye alishagundua huyo mtu ni nani, au huenda anamfahamu,  lakini alivyoingia sio kistaarabu, maana aligonga mlango mara moja halafu akaingia,  na dakitari akasema...

 ‘Samahani bado nina wahudumia hawa, unaweza kusubiria kidogo.

‘Habari zenu, na samahani, mimi ni mtu wa usalama,   ,…’ haraka akatoa kitambulisho chake hewani.

‘Nyie wawili mnahitajika kituoni kuisaidia polisi,…’akasema na mshangao ukatawala kila mtu akilini akiwaza lake..

‘Kwanini…?’ nikauliza

‘Hayo mtaambiwa huko mkifika, simameni….’akasema

‘Huwezi kuja kutuamrisha hivyo, tuna haki zetu kama raia, tuambie kwanza kosa letu ni nini, …maana sisi tuna uhakika sio wahalifu…’mwenzangu akasema

‘Hii ni amri halali…mnahitajika kituoni, simameni ….’akasema kwa ukali akiwa ametowa karatasi nyingine yenye maelezo ya kuja kukamatwa kwetu, hakutupa muda wa kuisoma, alionyesha tu.

Tulimwangalia docta ushauri, naye alionekana kuwa na mashaka kidogo, baadaye akasema;.

‘Hawa ni wateja wangu wamekuja na matatizo yao, unapokuja na kuwakata mbele yangu sio taratibu nzuri, basi ungelisubiria wakitoka, kwa namna hii huoni unaniharibia biashara …’akasema dakitari.

‘Haya mtaongea huko mbele, na samahani dakitari kwa hilo, sisi tunatumiza wajibu wetu….utaambiwa ni kwanini…’akasema

Tulibakia kwanza kimia, hakuna aliyesimama.

‘Mnasikia simameni twende,….mpo chini ya ulinzi na lolote litakalokwenda kinyume na maagizo yangu litachukuliwa kama kukiuka amri halali ya serikali…’akasema na mshauri nasaha akasema

‘Sawa nyie fanyeni anavyotaka ni kawaida kutokana na hilo tukio, tutaongozana na mimi nitakwenda kuwatetea huko kituoni…’akasema na sisi tukawa hatuna jinsi tukatoka nje, na kuwakuta jamaa wengine wanne hawa walikuwa na silaha kabisa, nikaona sasa kuna tatizo tukawa hatuna namna, tukaingizwa kwenye landrover na safari ya kwenda kituoni ikaanza.

*********

Tulipofika kituoni tukaandikisha majina na maswali machache ya kazi tunafanya na pale hospitli tulifuata nini, tukawaambia tulifika kuulizia mgonjwa wetu…

‘Huyo mgonjwa wenu ni nani….?’ Wakauliza

‘Ni jamaa yetu tu…’tukasema

‘Jina lake ni nani, kwani hana jina, si jmaa yenu mnamfahamu au sio…’akasema

‘Kwa ujumla hatufahamu jina lake ila tunafahamu kuwa alikuja hapo kutibiwa, na bahati tumeambiwa hayupo…’tukasema

‘Nyie watu wa ajabu mlikwenda hospitali kumuona mgonjwa ambaye hamumfahamu hata jina lake, tusipotezeane muda jina lake ni nani…?’ akauliza

‘Tumekuambia kuwa hatufahamu jina lake…unataka tutunge jina la uwongo…’tukasema

‘Kwanini sasa mliingia kwa huyo dakitari ushauri badala ya wodini..?’ akauliza

‘Kwasababu huyo mgonjwa hatumkuta, ikabidi tufike kwa huyo mshauri tupate maelezo yake…’tukasema

‘Ndugu,…hili ni jambo nyeti, na msiposhirikiana nasi mnaweza kujikuta kwenye matatizo makubwa sana…’akasema

‘Sasa sisi tushirikiane nanyi kwa lipi…hatujui tumekamatwa kwa kosa gani, tunashindwa hata kujitetea…’tukasema

Huyo askari aliandika maelezo yake, tukaambiwa tuingie kwenye chumba kimoja wapo tukaambiwa tusubirie humo. Dakitari nasaha yeye libakia nje akiongea na hao watu wa usalama, baadaye sasa tukaanza kuitwa mmoja mmjoa na kukutana na jamaa aliyejitambulisha kuwa ni mpelelezi wa makosa ya ujasusi.

‘Makosa ya ujasusi….?’ Tukauliza

‘Ndio muelewe hivyo, kuwa swala tunalolishughulikia ni nyeti, na kwahiyo mnahitajika kutoa ushirikiano unaostahiki, …’akasema na akaanza kuuliza maswali, na kwa jinsi alivyo alikuwa akifahamu vyema kumuingia mtu kirafiki mpaka unajikuta unaongea yote anayoyahitajia

Baadaye akasema

‘Mnajua msione kama mnasumbuliwa, lakini kwa hali kama hii inabidi kila anayehusika kwa namna moja au nyingine, iwe kwa mawasiliano,…au kwa njia yoyote,inabidi ahojiwe, na ushirikiano wenu ndio utakaotufanya tuweze kuikamilisha kazi yetu kwa haraka…’akasema

‘Kwahiyo tunaweza kuondoka…?’ tukauliza

‘Mimi nimemalizana nanyi, siwezi kuwaambia muondoke, subirini maagizo ya waliowakamata, …’akasema na kuondoka.

Tulirudishwa tena kwenye kile chumba, kulikuwa na joto, hewa nzito,lakini tutafanyje….walikuwepo jamaa wengine wa  makosa mbali mbali. Na tulipooona muda unakwenda tu, hakuna kinachoelezewa ikabidi tuanza kupaza sauti

‘Hawa watu vipi jamani…’tukaulizana, na baadaye akaja dakitari ushauri nasaha akasema kuwa mkuu wa kituo kasema hawezi kutuachia kwa leo kwani kuna uchunguzi unafanyika, kwani inaonyesha tuna mahusiano ya mawasiliano na hao washukiwa…

‘Washukiwa gani…?’ tukauliza

‘Ni pamoja na huyo mliyekuja kumuulizia, kwa hivi sasa kile aliyekuwa na mawasiliano naye anakamatwa, ni taratibu zao…’akasema

‘Lakini ushahidi unaonyesha kuwa huyo mdada alituandikia barua pepe tu, na alifanya hivyo ili kuelezea matatizo yake, sasa sisi inakuwaje tuingizwe huko….?’ Tukahoji

‘Hii ni kawaida ,…kutokana na sheria hizi za makosa hayo,…kwani huu ni uhalifu wa kimataifa, hamuwezi kuachiwa mpaka wajirisizhe wenyewe..kuna mawasiliano yanafanyika kuangalia nyendo zenu zote,…mitandao yenu yote itachunguzwa, …’akasema

‘Hiyo sio haki…’tukalalamika

‘Ndio sheria za ugaidi kwa hivi sasa….’akasema

‘Ugaidi…kwani hilo linaingilianaje na ugaidi!!!?’ tukauliza kwa  mshangao

‘Ndio imegundulikana kuwa kundi hilo, linahusiana na majasusi wa kimataifa ambao wamewekwa kwenye kundi la magaidi wa kimataifa…na huyo mliyemuuliza alikuwa akitumiwa na  hao watu ama bila kujijua au anafahamu na yupo kwenye kutekeleza majukumu aliyopangiwa….’akasema

‘Mhh, sasa hapo inanitia mashaka, lakini huyo mtu alikuwa mgonjwa kweli, na alihitajia huduma yenu, kweli si kweli, na mlihakikisha kuwa anaumwa,.. inakuwaje docta’ tukauliza

‘Msijali, inabidi mvumilia tu kidogo, na subira huvuta heri…’akasema na tukawa hatuna jinsi , jioni ikaingia, mara usiku….hakuna kinachoendelea,…ikabidi tulale hapo kituoni, mbu, …na harufu mbaya, …usiombe, kweli hujafa hujaumbika sikutarajia nitalazwa sehemu kama hiyo.

***********

Kukapambazuka kwa shida…na asubuhi tukaambiwa tujisafi, kupiga mswali kama unao….tusibirie kuitwa. Kiujumla, japokuwa nafanya kazi za kujitolea, na unatakiwa uwe tayari kupata shida, …lakini siku hiyo nilikereka sana, sikupendelea jinsi walivyotufanyia, lakini tukawa hatuna la kusema, kwani wao wamesimamia kwenye sheria hiyo ambayo haina cha kuulizwa…

Baadaye tukaitwa ofisini kwa mkuu wa kituo, na hapo tukakutana na maofisa watatu, kila mmoja alikuwa akihoji mambo yanayomstahiki, kuna wa maswali ya mtandao, kuna wa maswali ya uhalifu,  kuna wa maswali ya kisheria ,huyo wa kisheria alijifanya kama mtetezi fulani wa haki lakini ndani ya kazi zao, anauma na kupulizia, ili tu isionakane tumeonewa.

Maswali yao yalikuwa ni yale , …tulifika hapo hospitalini kumuona nani na kwanini..je huyo mtu tunamfahamu, na tulianza kufahamiana lini…ni kwanini akatuandikia sisi..na kwanini tukaamua kumfuatilia….tuna kibali gani cha kufanya hivyo, je tulishawahi kufanya hivyo tena, na kwanani…yaani maswali chungu mbovu

Baadaye tukaambiwa tusubiria, haikupita muda akaja jamaa mwingine ambaye naye ni askari upelelezi,akawa anaongea nasi sasa kirafiki zaidi, na alikuja na dakitari wetu wa ushauri,

‘Huyu ni mwanausalama anayeshughulikia hilo tatizo la mdada na kundi hilo la kijasusi..’akasema dakitari ushauri.

‘Nimeamua nimtambulishe kwenu ili muweze kumuuliza yote mnayohitajia kumuhusu huyo mdada, kama anastahiki kuwaambia, maana mimi sina kibali cha kuyaongea hayo, kama nilivyowaambia sasa hivi hili jambo lipo mikononi mwao …’akasema, na jamaa akasema

‘Ndugu zanguni, kama mlivyoambiwa, hili tatizo ni kubwa, na ni la kimataifa..msione kama mnasumbuliwa…dunia sasa ina mitihani mingi,na hili la ujasusi, sasa hivi yatambulikana kama ni ugaidi limekuwa na sura nyingi sana, ..’akatulia

‘Nyie mnafanya kazi za uandishi mnatakiwa muwe makini sana na mnachokiandika na watu mnaowasiliana nao,…kwani hawa wahalifu wanatumia kila nyanja kupenyeza mambo yao, wana wataalamu wa kila fani, na wengine mnaweza kujikuta mnatumiwa hata bila kujitambua…hawa ni wachawi wa kisasa’akasema akitabasamu kidogo

‘Maana wachawi wanaweza kumtumia mtu ambaye sio mchawi kutimiza malengo yao, wewe usiku unachukuliwa hujijui, unaenda kuwanga kwa nguvu za kichawi lakini wewe hujui na sio wewe mchawi…tunaambiwaga hivyo….’akasema

‘Kwahiyo,kwa hili swala mlilokuwa mkilifuatilia, tafadhali, mliache kabisa…huko mnapokwenda ni kubaya,…na bahati mbaya ni kuwa hata huyo mdada mwenyewe huenda alikuwa akitumiwa tu hajui kitu masikini.

‘Sasa bado tunalifuatilia, na tutahakikisha kuwa wote wanaohusika na kundi hilo,na lingiine kama lipo tutawakamata wote, tunashirikiana na wenzetu wa ncho jirani…’akasema

‘Unajua sisi hatuelewi afande, tumehusishwaje na mambo hayo, maana kazi yetu ni uandishi na uandishi hauna mipaka, kuwa hili ni la hivi au vile, tunachotakiwa ni kuielimisha jamii, pale linapotokea tukio, kwa mtindo huu hamuoni mtatufunga pingu huku mnataka tuandike..kinyume nyume,…….’tukasema

‘Ni bora kwa hivi sasa muelewe hivyo, kwani tupo kwenye mapambano na haya makundi haramu,….na sisi ndio tunaofahamu ni kwa namna gani inaweza kuleta madhara kama tutawapa uhuru huo wa kuandika kila kitu.

Nyanja hii ya uandishi sasa hivi ni silaha kubwa inayotumiwa, na hawa watu, kwa propaganda, potofu, kuhofisha, kupelekeana taarifa, na vitu kama hivyo, ndio ni vigumu sana kuisimamia hii fani maana nayo ina sheria zake, lakini inapobidi ni lazima tuingilie kati..’akasema

‘Kwahiyo kwa hivi sisi ni bora msielewe zaidi, itawasaidia,…lakini hata hivyo, inabidi niwaelezee yale yanayostahiki kuwaambia ili muwe na tahadhari,…’akasema

‘Kundi hilo alilokuwa nalo huyo mdada lilikuwa ni wakala wa kundi la kimataifa la ujasusi, ni magaidi kwa jina jingine, maana ugaidi ni mpana sana,tofauti na wengi mnavyofahamu,…’akasema

Kundi hilo liliweka tawi lake huko kijijini …na wapo sehemu mbali mbali wametawanya ki aina kutegemeana na fani za jamii…wapo hadi huku , huku mjini nakadhalika, sasa hilo la huko kijijini alipokuwa huyo mdada ni kundi lililopewa kazi ya kuuza madawa ya kulevya, vingine vilitumika kama viini macho…

‘Kundi hilo ili liweze kufanya kazi zao linahitajia pesa, na pesa zao mara nyingi zinapatikana kwenye biashara haramu kama hizo, au kuiba, kutapeli…sasa kwa upande wa hilo kundi huko kijijini alipotoka huyu mdada, wao walijitambulisha kama waigizaji, watengenezaji filamu, na vitu kama hivyo…huku wanauza madawa, wanaafnya biashara za ngono, wakitengeneza kanda za ngono…ni vitu nyie mtaviona vya kawaida kwa hivi sasa lakini lengo lao ni pana zaidi huko mbele.

Kizazi kinazoea….jamii inaharibika..jamii inakuja kujikuta ipo na vijana wasio na nguvu, legevu, walevi, wamepandikiziwa sumu ya kuchukiana, …..maana madawa hayo yana namna zake,yanaharibu mwili,  ubongo, nguvu, kizazi……hilo hamlioni kwa sasa, lakini siku zinavyozidi kwenda ni hatari kweli kweli….na hiyo ni mbinu nyingine ya kumshinda adui…maana sisi wanatuona ni maadui zao kwa vile hatuwaruhusu kufanya watakavyo, dawa ni kuharibu nguvu kazi…

‘Sasa hao waliopelekwa huko kijijini walipewa hiyo kazi ya kutafuta pesa, na kuchunguza mambo mbali mbali yanayoendelea huko kijijini,…mnafahamu kile kijiji kina nini, ni kwanini wakilenga wao,…mnafahamu?’ akauliza na kwa kweli hatukuwa tunafahamu chochote, tukasema hatufahamu

‘Kijiji kile kinasadikiwa kuwa na madini, mali asili nyingi sana zinapatikana eneo hilo…., serikali inafahamu hilo, ina mikakati yake, lakini hawa watu nao wana mikakati yao, wanajua ni kwanini wanafanya hivyo,  kujiandaa kwa ajili ya kuja kuwekeza hapo….ni mambo ambayo ukiyaangalia juu juu huwezi kuyatambua athari zake baadaye…ni watu wanaona mbali miaka mia,ambayo hata wao hawatakuwepo!

‘Hivi niwaulize kama vijana pale, eneo hilo, …..na sio eneo hilo tu tuzungumzie nchi kwa ujumla, nguvu kazi ikiathirika hivyo, haina nguvu, wagonjwa, hawana elimu,..kazi yao ni kubwia madawa, kulewa,  kuiga iga mambo ya starehe tu, wawekezaji wakafika kuwekeza, ni nani atakuja kufanya kazi kwenye hayo makampuni, …..?’ akauliza

‘Ni wao …na watu wao….’tukasema

‘Eeeh, ndio hivyo,…maana vijana, watakuwa hakuna, hawana nguvu, hawana elimu, wameathirika, wagonjwa watakuwa ni wengi,….na ukomo wa maisha yao utakuwa ni mfupi tu,… ni lazima wao watakuja na nguvu  kazi  zao au waagize sehemu nyingine, na kwa maana hiyo wageni watajaa makazini,  ….tutamlalamikia nani…’akasema

‘Hili tunatakiwa kuliangalia kwa mbali zaidi,…leo hii tunataka kuwekeza kwenye ardhi…unajua kwenye hiyo ardhi kuna nini, hawa wajukuu na vitukuu watakuta nini,…ndio lengo lao, huo ni mfano mdogo tu….lakini pia mali asili itachukuliwa bila ya kuwepo msimamizi mwenye uchungu wa nchi, maana hakuna mzawa kwenye usimamizi wao ….hayo nyie hamyaoni kwasasa, sisi watu wa usalama tunayajua hayo,  ndio maana tunafanya kazi yetu.

Haya nyie kalieni starehe, kuandika story za ngono, mapicha ya ngono, wenzenu wanawekeza kiakili…..baadaye mnakuja kulalamika…tuamuke jamani, mfumo huo umetengenezwa kiakili, msiponaswa kwenye madawa, kwenye siasa, mtanaswa kwenye vinywaji,..au kwenye vyakula,…hivi vyakula tunavyoagiza kutoka nje, tujiulize kwanini hatulimi wenyewe, samaki wapo wengi tu, kwanini…humo humo kwenye makopo ya vyakula nk wenzenu wamewekeza….sasa nyie kalieni kupiga makofi, kushangilia….’akasema na sisi tukacheke kidogo.

‘Sasa kwa hilo,…hapo kijijini,  wao wakawa wanapitisha madawa kwenye makasha ya kanda za video kitaalamu zaidi, huwezi kujua wanavyopaki, hizo dawa kuna za kuelewesha kuna za kuharibu akili, kuna za kupandikiza maradhi,….,

Vijana wanalewa hawajijui, wanashawishiwa kufanya machafu, ….haya ndio wakawa kuendesha biashara za ngono, na kuigiza video za ngono kisiri siri, maana akili sio zao tena…hata humu mjini yapo haya, nadanganya, sasa jaribu kutumia nguvu kuzuia mambo hayo usikie watu wakavyolalamika…utaambiwa haki za binadamu! Hivi kufanya hivyo hukiuki haki za binadamu, niwaulize nyie…’akasema

‘Haya yote ni mbinu, …na hatujui,….hakuna kitu kibaya kama kutawaliwa kifikira…elimu yetu ni ya kuiga iga tu…hata kile tunachokifahamu ni kuiga tu, wazee wetu waliweza kuwekeza na tungeliweza kuendeleza nguvu zao kitaalamu tungelikuwa mbali…viwanda hakuna vimekufa, kwanini, ilipangwa iwe hivyo, waje wawekezaji,….hayo yalifanyoka kitaalamu… , yote hayo kwa manufaa ya hao majasusi….jamii haijui!

Majasusi hawa wa kimataifa ni wakatili sana….wanaua bila huruma, na kuua kwao ndio hiyo wanatumia madawa yasiyoweza kugundulikana, mnajiona mnalewa kumbe mumekunywa sumu….madawa haya haya ya kutibia wanapandikiza sumu, ni ndogo lakini athari yake baadaye ni kubwa….ni vitu vinafanyika kitaalamu sana!

Haya huko maofisini kwenye makampuni hayo waliyowekeza wao wanatumia nguvu zenu kwa mshahara mdogo, wananeemeka wao, wakijua ukomo wa maisha yenu ni mdogo, ukichoka unatafutiwa mbinu unafukuzwa, wanaweka watu wao….huko siwezi kuenda zaidi, ila …..nawaombeni muamuke, badilisheni mfumo wenu wa maisha, tujitegemee!

‘Hili nawaambia nyie waandishi  ili muwe makini,  saidieni jamii kuwaelimisha, andikeni yenye tija, msiwe bendera tu kufuata upepo. Kila kitu cha nje mnaona ndicho bora, yaani hata utamaduni, hata kula….hahaha…’akatikisa kichwa

 Na kwa hili tukio la huyu mdada...mkijifanya mnajua mkaanza kulifuatilia mjue mnaingia kwenye mdomo wa mamba, hayo waachieni wataalamu wanaijua hiyo kazi…maana mtaingia kwenye anga za hao watu wasio na ubinadamu…na zaidi mtaishia kueneza uchafu wao bila hata nyie kutambua….

‘Kama nyie mnaandika stori za ngono, stori za kutumia madawa ya kuelevya kama vile ni jambo la kawaida, mjue nyie mumeshakuwa wakala wao…mnaharibu jamii…mnakiua kizazi kinachochipukia, na ndio lengo lao…kwahiyo mnatumiwa hata nyie wenyewe kujijua..na wasomaji wa mambo hayo ni wengi,na wengi wao ni vijana…..

Vijana hivi sasa wanaathirika kisaikolojia bila kujijua….badala ya kusoma vitu vya kuelimisha vyenye tija,wakazalisha wakaleta maendeleo jamii ikaishi kwa maelewano na amani,  wao, wanaishia kusoma vitu vya kuwaharibu kiakili, hii mitandao ni moja ya nyenzo zao, yapo mazuri, lakini humo humo wameshaweka mambo yao,…muwe makini jamani…hiki mnachokifanya mtakuja kuulizwa na muumba…’akasema

 ‘Lakini sisi lengo letu ilikuwa kuja kumuokoa mdada…’tukajitetea

‘Kumuokoa mdada!!!,….hahaha…nyie mnaweza kumuokoa mdada?….mnatania’akasema akitukazia macho yenye mshangao huku akicheka kidogo

‘Kwa vipi hebu niambieni….?’ akauliza

‘Sasa sisi tungelifanya nini…?’ tukamuuliza

‘Huyo msingeliweza kuja kumuokoa hamngeliweza, ….na hamuwezi…, kabisa msingeliweza hilo nawaambia….’akasema

‘Una maana gani kusema hivyo,kwani imekuwaje kwa mdada, samahani kwa hilo swali maana tutaondoka bado tukiwa na maswali mengi , je imekuwaje kwake, maana sisi hatukupoteza muda kufika hapa….?’ Tukauliza

‘Kwanza jiulizeni hiyo barua pepe ilifika lini kwenu, hiyo ya kutoka kwa mdada…na leo ni siku ya ngapi..sasa mnaokoa nini hapo..’akasema

‘Kwanini unasema hivyo…maana sisi tuliipata hiyo barua pepe jana usiku…na asubuhi na mapema, tukawahi kuja ili tuweze kuona kama tunaweza, kumuokoa…’tukasema

‘Tukio la huyo mdada limetokea lini, ni wiki ya tatu sasa….au sio docta, …wiki ya tatu, leo mnakuja kumuokoa mdada, hahaha…ili sasa muone wenzenu walivyo mbele yenu,…’akasema na sisi tukabakia kuangaliana

‘Ina maana….’tukataka kujiuliza

‘Mumechelewa sana…., ndio maana nasema hamungeliweza kuja kumuokoa…mpaka lengo lao litimie, huenda kweli mdada aliwaandikia akijua mtaweza kufanya hivyo, kwasababu hajui , na kama mungekutana naye leo, mkasema mumekuja kumuokoa ataona nyie ni wahuni tu,… wenzenu wapo mbele yenu kwa kila jambo…’akasema

‘Lakini hiyo barua pepe yaonyesha kabisa imetumwa muda huo na kufika kwetu muda huo….tuliichunguza kabla hatujafika hapa sisi tuna utaalamu huo…’tukasema

‘Ndio maana tunawaambia sisi watu wa usalama tunajua ni nini tunachokifanya,… mtaona tunawaingilia kwenye kazi zenu lakini ni lazima tufanye hivyo,kwa masilahi ya jamii, kwa masilahi ya vizazi vijavyo, hata kama leo mtatuona wabaya…’akasema

‘Oh, hii ajabu kabisa….haiwezekani, kwahiyo afande unataka kusema nini, ina maana mdada hakuweza, au imekuwaje kwa mdada….yupo wapi….?’ Tukajikuta tunauliza kile ambacho tumeambiwa tusifuatilie. Afande alituangalia kwa makini halafu akasimama na kutoa simu, akapiga namba halafu akasema;

‘Mleteni….’


WAZO LA LEO: Jamii zetu zinaharibiwa kwa mengi, ipo mitihani ya kawaida na ipo mitihani ya ya kupangwa na watu kwa masilahi yao na hayo yamepangwa kwa mbinu za hali ya juu kweli, inahitaji tafakuri la ziada….kuna umamboleo unaoathiri tamaduni na fikira za watu nk…..nia ni, ili kuwanufaisha wenye tamaa zao, watajirikie na wazidi kutawa!  kwa kutumia misemo kama ile ya ‘walionacho waendelee kuwa nacho, na wasio kuwa nacho wazidi kukosa…’. Hayo yapo na yanendelea, tusipokuwa makini, tutaishia kusindikiza na kuwapiga makofi wenzetu huku wakiendelea kuneemeka, na huku wengine wanasafiri kwenda mwezini. Tuamuke, …

Ni mimi: emu-three

No comments :