Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Tuesday, September 25, 2018

YOTE NI KWA MAPENZI YA MUNGU-51



‘Hayo maswali yako muheshimiwa kwangu ni magumu sana kuyajibu,...lakini kwa vile umeniuliza na hapa ni mahakamani, mimi nitajaribu kuyajibu kama ifuatavyo, kwa ufupi,…kwanza, mimi sijaweka sahihi yangu kwenye huo mkopo,...kwenye hizo karatsi za kuchukulia au kwenye mkataba...'akatulia kidogo


'Na kwanini mimi niweke sahihi yangu,...kwanini... maana huo sio mkopo wangu, na hata kaka hajawahi kuniagiza niweke sahihi kwa niaba yake kwenye huo mkopo…’akasema

‘Je alishawahi kukuambia uweke sahihi kwa niaba yake…kwenye jambo fulani la kibenki…?’ akaulizwa

‘Niweke sahihi yake...!!!….mmh….kwa vipi , yeye ana sahihi yake, na mimi nina sahihi yangu,.. labda niweke sahihi nisema nimeweka sahihi hiyo kwa niaba yake, lakini sio kwa maswala ya kibenki, benki wana masharti yao jamani…’akasema na kukaa kimia

‘Na dole gumba je…?’ akaulizwa

‘Hapo ndio mnaweza kupata majibu yenu sasa..., mkiwa makini na hili swala, kwenye dole gumba ndio kwenye jibu,…jiulizeni tu, kweli  kuna mtu anaweza kuweka dole gumba kwa niaba ya  mtu mwingine..hilo halipo, au sio,… kama  hilo halipo, ina maana gani sasa, ...ina maana kuwa...eeh,  bro alihusika yeye mwenyewe…’akasema

Akageuka kumuangalia hakimu, na baadae akaendelea kuongea...


‘Na nasema hili,  sio kwamba, nasisitiza deni hilo ni la bro,...kuna namna ya kulithibitisha vinginevyo, mbona nitafurahia hilo,…lakini je hayo yalitendekaje,..akilini najaribu kuwaza, huenda kweli bro alifanya hivyo,..'akageuka kuangalia mbele, nahis alikuwa akitafuta wapi shemeji yake yupo.

'Nazungumza haya, sio kwamba nafurahia hilo jambo..kuwa nashabikia hilo deni kwa marehemu,..kiukweli mimi mwenyewe linanisumbua sana...mimi silifurahii hili jambo kabisa .. nitalifurahiaje wakati najua hilo deni litaiumiza familia yangu…lakini tutafanyaje,…kama bro, aliacha hilo deni,..hivi kiukweli mimi kama ndugu yake nilitakiwa nifanye nini sasa…, eeh, niambieni,…?’ akawa kama anauliza.


Alipoona hajibiwi akaendelea kusema;


‘Huyo kijana kadanganya, akisema mimi ndiye nimehusika na hilo deni, sio kweli,… 'akageuka kumuangalia hakimu.


'Nasema kutoka moyoni,...mimi sijachukua huo mkopo,…na-na..jamani, hivi hamuoni hali halisi, kama ningelichukua hayo mapesa yote, ningelikuwa hivi..eeh, si mngeliniona nikiwa na mabadiliko, Dalali, ninavyokipenda.... na wala, sikujua ..sikuwa na ufahamu wa hilo deni kabisa jamani…’akasema.


‘Lakini wewe ni tajiri, ukishirikiana na wenzako, wewe mtaalamu, na kijana wako, nyie mna vitega uchumi, kweli si kweli...?' akauliza na kwanza akakaa kimia

'Nyie…mna vitega uchumi vingi tu ambavyo vimekuja kugundulikana baadae kuwa wewe ulikuwa mpo ubia na huyo kijana wako kwenye miradi yake mingi tu, mkiwa mnatumia majina yasiyo rasmi,…ina maana kwa namna nyingine nyie wawili mpo shirika, kwahiyo mnaweza kufanya jambo mkapanga, na hiyo ilitokana na huo mkopo…’kabla hajamliza muulizaji, Dalali akasema;


‘Hapana muheshimiwa wakili…samahani kwa kukukatisha,…inaniuma sana, leo nateseka , nateswa, lakini hakuna anayelijali hilo,…''akasema


'Unateswa na nani...?' aakulizwa


'Hayo ya kwangu tuyaache, nitapambana nao, ..hawaniwezi....'akasema na kutulia kidogo.


'Sasa hiyo kauli yako, kusema sisi, au mimi ni tajiri...sio sahihi, hivi unamfahamu vyema huyo kijana, kila alichokifanya kakifanya kwa kunitega, kulipiza kisasi, kwa hayo, anayohisi kuwa mimi nimemfanyia mama yake,..mengine mimi sijayafanya…’akasema


‘Tutaaminije hayo wakati ushahid upo , kuwa wewe uliyafanya ,…na kauli zako nyingi zimekuwa kinyume, na utetezi wako wa sasa, kuonyesha wewe  sio mkweli,..nyie wawili mnajua ni nini  mlichokifanya, na inavyoonekana huu ni mkakati wenu wa pamoja, ushahidi upo…’akambiwa.


‘Ni sawa tupo wabia kwenye miradi fulani, fulani,  lakini angalieni kiasi cha hisa, tulichopewa sisi wabia hewa…, ni nini tunachokipata hapo, sana sana kiasi hicho kinaishia kwenye kulipia madeni anayotudai, kama nilivyowaambia, huyo kijana ni mjanja sana, alituingiza kinamba na kutufanya sisi ..eti wakurugenzi, …’akatulia.


‘Huyo kijana ana..lengo lake, na lengo lake analifahamu yeye mwenyewe…mimi narudie tena, …sikujua jinsi gani deni hilo lilivyofanyika,..na mpaka sasa bado siamini, kama benki wanaweza kuchezewa kiasi hicho, kama ni kweli wamefanyiwa hivyo, mimi sitaweza kuwasamehe, maana wametutesa sana…’akasema.


Wakili akacheka na kutikisa kichwa, halafu akamuangalia Dalali machoni,…baadae akamuuliza…


‘Je kwa hali kama hii, baada ya maelezo ya kijana wako, je bado unakubaliana na benki, kuwa hilo deni ni la marehemu kaka yako, huoni kwamba ukiendelea kusema hivyo, au kuamini hivyo, wewe haupo katika kuisaidia familia yako, bali wewe unaangalia masilahi yako binafsi..?’ akaulizwa


‘Kiukweli ,  awali,… mimi sikukubaliana na hilo deni…, kuwa bro anaweza kukopa pesa nyingi hivyo, hata mimi kweli nisifahamu,…lakini sasaah…ushahidi upo wapi, kiukweli nilipoangalia ushahidi wa benki, nikajua ni kweli, bro alikopa hizo pesa, maana taratibu za benki zinajulikana,…niliangalia vitu muhimu,  sahihi ipo ya bro,…halafu kuna dole gumba, la bro, hilo nani anaweza kugushi,  …mimi nitasemaje hapo…’akatulia.


‘Hata mke wa marehemu alisema kuwa sahihi hiyo ni ya mume wake,..na zaidi ni baada ya mahakama kupitisha hukumu, mimi ningesemaje hapo jamani, hebu nisaidieni na nyie…’akasema.


Wakili akatabsamu na kusema;


‘Mbona hujasema , na mizimu yenu…au hiyo ilikuwa ni geresha yenu, kuwachezea watu…?’ akaulizwa.


‘Ndio, ndio…nilisahau hilo, ..na mizimu ikatusaidia,…lakini marehemu naye, aah, unajua, niseme ukweli, imani zake zilinitega sana akili yangu, na kunifanya niamini kila kitu anachoniambia…hata hilo la mizimu, liliniongezea imani kuwa kweli hilo deni ni la bro..’akasema.


‘Hayo ya mizimu si ilikuwa ni mbinu zeni za kuwatishia watu ili wakubaliane na hilo deni, sio mbinu zenu  wewe na marehemu, mtaalamu, tuambie ukweli, maana yeye hayupo hapa…?’ akaulizwa.


‘Ni kweli mimi na marehemu tunajuana,…kwa vile namuamini, na nilipomuomba anisaidie kwa hilo, akasema hivyo, kuna mizimu, …kiukweli nilimuamini, nilijua yeye ni rafiki yangu hawezi kunidaganya…’akasema.


‘Swali kwa maelezo yako hayo, na kumbukumbu zilizopatikana zikiwa zimefichwa na huyo kijana wako,…Je kwa hivi sasa baada ya ushahidi huo wote, wewe bado …una imani hiyo kuwa hilo deni ni la kaka yako?’ akaulizwa, kulitokea pingamizi kutoka kwa hakimu wa benki, lakini kwa hivi sasa hakimu hakutaka pingamizi …


‘Mhh…hapo mimi aah…sijui mnataka mimi nisemeje,..kiukweli hadi sasa nachanganyikiwa, kwa namna nyingine mimi nimeaanza kumuhisi huyo kijana kuwa huenda alifanya jambo,.’akatulia kidogo.


‘Lakini najiuliza-aah…mmmh,…, alifanyaje sasa..eeh jamani..alifanyaje.., unajua benki ilivyo, labda kwa vile aliwahi kufanya kazi huko benki labda… lakini hata hivyo kwa vipi, si lazima wakubwa wake wapitishe eeh..…kwa upande mwingine kuna eeh,… kuna sahihi ya kaka, na zaidi kuna dole gumba, hapo mimi na ujanja wangu wote siwezi kuwa na uhakika wowote..’akasema


‘Kwahiyo unataka kusema nini hapo, kuwa huenda kijana wako ndiye alifanya hujuma na wewe ukatumbukizwa bila kujua, maana kwa ushahidi ulivyo, wewe unahusika kulifanikisha hilo deni…?’ akaulizwa.


‘Ushahidi upi sasa jamani…kwa vipi mimi nimeweza kulifanikisha hilo, niambie kwa vipi, sahihi ni yangu,..hapana, dole gumba ni langu, hapana…ushahidi upi ndugu muheshimiwa, kwa kauli tu ya huyo bwana mdogo,…mimi sijui kitu jamani, mnanionea bure, niambieni wenyewe…?’ akauliza kwa mashaka.


‘Kutokana na kauli ya Majaliwa, wewe ndiye ulikuwa mara nyingi unahusika kwenye kuchukua pesa za kaka yako…na ikatokea pesa zikachukuliwa bila ya ridhaa ya kaka yako,..na kwa ushahidi mwingine, kaka yako aliwahi kuandika barua benk  kulalamika, na zaidi kumbukumbu zote za benki nyumbani kwa marehemu zikapotea na wewe ndiye ulikuwa na mamlaka wakati shemeji yako hajitambui,..unakwepa nini hapo..’akaambiwa.


Hapo Dalali akakaa kimia…na wakili akaendelea kuuliza…


‘Je kaka yako hakuwahi kukulalamikia kuhusu hilo…kuwa kuna pesa zimechukuliwa benki bila ya ridhaa yake…?’ akauliza na akabakia kimia

‘Sasa tuambie ukweli,  wewe ndiye uliyekuwa ukitumwa kuchukua pesa benki na kaka yako…, sasa kama kaka yako alilalamika hivyo…kuwa kuna pesa zimechukuliwa bila ya ridhaa yake…, ni nani wa kumshuku, kama sio wewe...na zaidi ukifika benki wewe ulikuwa mkikutana  na Majaliwa, ushahidi upo…’akaambiwa.


Dalali, akahema kidogo, halafu akaanza kuzungumza, kwa sauti ya kinyonge kidogo…


‘Mhh…nakumbuka kuwa kweli kaka, alilalamika kuhusu hilo..lakini mimi sikuwa nachukua pesa bila ya kibali chake, …na aliponilalamikia mimi, kiukweli niliumia sana, ina maana bro haniamini…’akatulia

‘Hata hivyo, nikaja kujiuliza kama kweli hilo limeetndeka, basi bro ana haki kulalamika jambo nzuri, ni benki watuambie kwanini …na hizo pesa zimekwenda wapi, nikamshauri bro, aandike barua benki ya kulalamika…’akatulia


‘Hilo hukuwahi kulisema, ..awali uliulizwa ukasema hujui lolote kuhusu hiyo barua, sasa hivi unasema ni wewe ulimshauri kaka yako…’akaambiwa.


‘Hapa ni mahakamani…huenda nilisema hivyo kwa minajili fulani, lakini hapa sasa naongea ukweli ulivyokuwa…kuwa bro..ilikuwa ni  haki yake kulalamika hivyo, ilikuwa ni haki yake kuninyoshea kidole mimi….na nilipoongea na Bro, baada ya mimi kumthibitishia kuwa kweli sihusiki na hilo, akaandika barua  kuwalalamika benki…’akatulia


‘Na bahati mbaya,…sikuweza kupata nafasi ya kuliongelea hilo na bro, siku zikapita,…sijui banki walimjibu nini…na bahati mbaya zaidi haya yametokea… .’akasema kwa sauti ya unyonge.


‘Haya yametokea….’akasema wakili alipoona Dalali katulia

‘Kwanini haya yametokea…?’ akauliza wakili

‘Mimi sijui….’akasema


‘Ndio utasema hujui..haya yametokea  baada ya kuonekana kuwa njama zenu zimebainika, mkaona njia nzuri ni kumuangamiza kabisa huyo bro wako, …ili hayo malalamiko yapotee, ili muweze kumbambikia bro wako deni, na ndivyo ilivyotokea,, na ndivyo ilivyofanyika, unabisha nini  hapo bwana Dalali …’akaambiwa

Dalali akakohoa, na kusema;


‘Sio kweli jamani…naapa, ..haya ninayoyasema ni kweli tupu, mimi sihusiki na hilo deni,…labda huyo bwana mdogo aje atuthibitishie kauli zake hapa za kusema mimi nahusika, maana yeye alikuwepo huko benki kipindi hicho, je ni kweli nilishirikiana naye, aje hapa ayatamke hayo…’akasema


‘Kwa kauli yako hiyo unatuthibitishia kuwa kijana wako ndiye aliyewezesha hizo mbinu,, za kuchukua mkopo, na kuuwekeza kwa kaka yako…lakini sahihi ya kaka yako ilipatikanaje, hapo ni kazi yako wewe….kweli si kweli…?’ akaulizwa


‘Mimi sijui..na..na…’kabla hajaendelea akaendelea kuulizwa.


‘Ngoja tukusaidie mlivyofanya…baada ya huo mpango, mliouita mpango moto kutengezwa, wewe ulipewa jukumu ya kupatikana kwa sahihi ya kaka yako na dole gumba…’akasema wakili.


‘Hiyo haikuwa kazi ngumu kwako, ungeliweza kufika kwa kaka yako ukamvunga kwa vile anakuamini, yeye akaweka sahihi bila kusoma huo mkataba,..wewe uliweza kumdanganya kuwa huo ni mkatana wa kurekebisha akaunti yake ya benki…’akasema wakili, kwa kazi za kibenki, hilo lilikuwa jukumu la kijana wako, je hivyo si ndivyo mlivyofanya…?’ akaulizwa


‘Kamleteni huyo kijana wa benki,labda kama mimi hamuniamini… yeye mwenyewe ataweza kulielezea hilo…kama kweli kadai kuwa mimi nahusika, basi aje atamke hapa mbele yangu, …zaidi ya hayo, mimi nakataa hayo madai yako, ..sijapewa jukumu kama hilo, na sijui lolote kuhus huo mpango moto…’akasema.


Wakili akawa anaoma makabrasha yake, halafu kama kakumbuka jambo haraka akamuendea Dalali…


‘Kijana wako  kasema mama yake alikupenda sana,..na hakutakiwa akuingize wewe kwenye matatizo yoyote,..mbona wewe unamuingiza huyo kijana wako  kwenye matatizo, ina maana wewe hukuwa na upendo na mama yake, na wala hujali kitakachokuja kutokea kwa huyo kijana wako, au hizi ni mbinu mbinu tu za kupotea muda,…?’ akaulizwa.


‘Upendo…!! Hivi mnaelewa ni nini maana ya upendo, mnajua alichonifanyia huyo mwanamke..’akasema kwa sauti ya hasira kidogo, halafu akatikisa kichwa na kusema;


‘Jamani, mimi nilishawaambia, …mimi sitaki kuyasema hayo, maana yeye sasa ni marehemu, na sio vizuri, kuyaingiza haya mambo yake hapa…, ndio maana hadi leo, sijaweza kukubali moja kwa moja kuwa huyo mtoto ni mtoto wa kwangu, ila kama huyo kijana atakuja kwangu akasema kweli ananikubali mimi kama baba yake, nitakubali tu, yaishe, kwani wangapi wana watoto sio wao wa damu…’akasema.


‘Ina maana hadi sasa hujaamini kuwa huyo mtoto ni wako, wakati wewe ndiye ulimbaka huyo mwanamke…na kwa kitendo hicho ukamsababishia mimba …au unamshuku nani kwa hiyo mimba, kaka yako au nani mwingine…?’ kabla hajamaliza, Dalali kwa hamaki , akasema


‘Kaka yangu..!!! Ni nani kasema hivyo,…hapana jamani, mimi siongelei hilo kuhusu kaka yangu hapa, siwezi kumshuku kaka yangu kwa hilo, kaka yangu hakuwa na tabia hiyo chafu,..mimi hapa naongelea kumuhusu mtaalamu…’hapa akatulia kidogo.


‘Mtaalamu…alifanyaje kuhusiana na huko kwa wewe kumbaka mdada wa watu baada ya wewe kumtegea kwa madawa ya kulevya…?’ akaulizwa


‘Muheshimiwa…mimi nasema hivi,  pamoja na ya kuwa mtaalamu alikuwa ni rafiki yangu, lakini  eeh, samahani kwa kauli hii, mungu anisamehe tu…mimi nilikuwa namshuku mtaalamu vibaya, kuwa huenda….’akatulia kama anasita kuongea


‘Ongea..au unautafuta uwongo mznzuri…’akaambiwa

‘Mmhh….unajua kama binadamu tuna madhaifu yetu, ..hasa kwenye maswala ya mapenzi…moyo huwa hauamini…hasa ukiona mpenzi wako yupo karibu na …na…kibinadamu inakuwa hivyo…, mtu unaweza kujenga shaka-shaka…na nilijenga shaka shaka hizo kwa mtaalamu kuhusiana na huyo binti…’akasema


‘Shaka shaka gani, tufafanulie hapo Dalali…?’ akaulizwa

‘Mara nyingi, mtaalamu, alikuwa anapenda kuwa karibu na huyo binti, na alishawahi kunisifia kuwa huyo bint ni mnzuri..na..akifika kwetu, ni lazima amuite, amtume kitu…unaona…na mambo mengine tu..kiujumla moyoni nilikuwa naumia, maana mimi nilishampenda huyo binti…na alipokuja kunishauri jambo, ndio kabisa nikajua tayari…’akatulia kidogo.


‘Alikushauri nini…?’ akaulizwa na badala ya kujibu swali hilo akaendelea kuongea;


‘Ila jamani…mimi siwezi kuwa na uhakika wa moja kwa moja, na hili hapa tunamsema marehemu, na nyie mumenilazimisha niyaseme haya....maana sikuwahi kuwafumania ile ya moja kwa moja, hapana, niliona dalili hizo tu, moyo wangu ukajenga wivu..na siwezi kukataa mpaka leo, bado …aah, mwenyezimungu nisamahe tu, bado naamimi mtaalamu, ali…aah…ali…jamani sitaki kuyasema haya mume-nifanya ni-ni ya-seme tu……’akatulia akionyesha huzuni fulani.


Wakili akatabasamu na kutikisa kichwa kusikitika, halafu ..akamuangalia Dalali..


‘Unataka kusema huenda huyo mtoto ni wa mtalaamu..lakini ukumbuke, kutokana na maandishi ya mama yake Majaliwa,..yeye aliandika kuwa wewe ndiye uliweka dawa..za kumpoteza fahamu , na ukatumia mwanya huo kumbaka, kweli hukufanya hivyo…?’ akaulizwa.


‘Unajua hizo dawa alinipatia nani,..?’ akauliza.


‘Je hukufanya hivyo…?’ akaulizwa tena


‘Ndio nilifanya, lakini…’watu wakacheka.


‘Ulimbaka..usiogope kusema hivyo…haya tuambie ulimbakaje, au ulifanyaje kwa lugha unayotaka wewe…’akaambiwa



‘Hizo dawa, alinipatia  huyo huyo mtaalamu, na ndiye alinifundisha hilo…’akasema


‘Yeye ndiye aliyekufundisha kumbaka binti wa watu…una uhakika na hilo, unamsema vibaya marehemu..?’ akauliza wakili.


‘Nisikilize kwanza…yeye, alipoona nampenda huyo binti, akaniuliza je namtaka huyo bint, ..kwa vile mimi nampenda na nimejaribu kila njia,..nimeshindwa, nikasema ndio..ndio akanipatia hizo dawa…’akatulia.


‘Ehee, endelea…’akasema wakili.


‘Kiukweli mimi…, sikutaka kulifanya hilo, kiukweli baada ya hilo tendo, nilijilaumu sana,..binti wa watu…na..niliogopa sana, akija kumwambia bro, sijui itakuwaje,…ikabiid nitoroke nyumbani kwenda kuishi kwa ..ndugu yetu mwingine..lakini sasa yalishatokea,..sijui kwanini sikuweza kulifikiria hilo jambo wakati ule, aliponishauri huyo mtaalamu, na zaidi aliniambia kuwa yeye hufanya…ndi- ndio tabia yake…’akasema na watu wakacheka..


‘Ndio tabia yake kufanya nini…?’ akaulizwa.


‘Akiwataka wanawake huwa anawafanyia hivyo, kuna mashetani yake yanataka yeye afanye hivyo, aliniambia hivyo-hivyo…na anafanya hivyo,..ili dawa zake zifanye kazi vyema…’akatulia


‘Sipendi kuyaongea haya….ila ndivyo aliniambia, kuwa..kuna aina ya shetani, ili aweze kumsaidia kwenye ammbo yake, inabidi yeye atembee na  mabinti wadogo…’akatulia


‘Oooh…unajua mumenilazimisha nyie….mimi niliapishwa nay eye nisije kulisema hili,..lakini sasa, aah, hata sijui itakuwaje,..nimeshasema..mizimu inisamehe tu…’akasema Dalali, sasa akionyesha kuogopa kabisa.


Mimi pale nilipokaa, nikawaza jambo, nikamsogelea huyo wakili  , nikamwambia…


‘Hapa tutapoteza muda mwingi bure kuna kitu muhimu bado hatujakigundua hapa…ukweli kuhusu sahihi na dole gumba, vilitoka wapi,..huko kwingine tunazunguka tu, na bado hatujapata ushahidi wa hilo, sahihi na dole gumba, lilipatikanaje..’nikasema kumuambia wakili, …


‘Sawa…wewe usijali,…tutafika huko….’akasema wakili na kumgeukia Dalali.




‘Tuachane hayo ya kumbaka binti wa watu, kazi mliyoifanya wewe na mtaalamu, hebu sasa…turejee kwenye ajenda yetu, jinsi mlivyoweza kuipata sahihi ya marehemu…ilikuwaje sahihi ya kaka yako ikapatikana kwenye hilo deni…wakati hata wewe unaamini kuwa hilo deni sio…la kaka yako..?


‘Mimi hilo sijui, ndio maana napata shida kulikataa hilo deni….’akasema,


Dalali alipojibu hivyo, mimi  nikamsogelea huyo wakili nakimwambia;



‘Samahani muheshimiwa, ninaweza kumuhoji huyu mtu kidogo, kuna kitu ……?’ nikauliza na hakimu wakati huo, alikuwa akiongea na wazee wa baraza,…nahisi aliona muda mwingi umetumika kwa huyo shahidi…


‘Sawa endelea,  ‘kabla hajaniruhusu akasema


‘Muheshimiwa hakimu, nipo na msaidizi wangu hapa leo,…nataka amuhoji kidogo huyu shahidi,  …’akasema wakili, wakili wa benki akasimama na kutoa pingamizi

‘Anasimama kama nani…shahidi au…?’ akauliza hakimu

‘Kama msaidizi wangu kwa leo…kuna ushahid anautaka kuupata kutoka kwa huyu mshukiwa…itasaidia sana kulimaliza hili tatizo la jinsi sahihi ya marehemu ilivyopatikana…’akasema wakili

Hakimu akaniangalia kwa makini, halafu akasema

‘Ni kweli, hata hivyo, wewe ulipewa nafasi ya shahid na hukuweza kumalizia ushahidi wako je ndio huo unataka kuendelea nao…na kwanini unataka kumuhoji huyo shahidi…?’ akauliza hakimu.

‘Muheshimiwa hakimu..kuna utata kwenye hii kesi, utata upo kwenye jinsi gani sahihi ya marehemu ilipatikana, na dole gumba…hapa kuna kitu kimejificha, na mtu wa kutusaidia, ni huyu na kijana wake..naomba nimuulize maswali machache…’nikasema na hakimu akaangalia, saa na kusema

‘Sawa endelea…’akasema hakimu

Mimi nikamsogelea Dalali,…nikamuangalia machoni, halafu nikasema;

‘Dalali hebu simama…’nikasema na Dalali akaniangalia kwa macho ya kushangaa

‘Nisimame, nitasimamaje, na wakati,…mimi siwezi kutembea…na…’akasita, mimi nikatoa picha, na kumuonyesha

‘Hii picha hapa ni ya nani…?’ nikamuuliza

‘Ya kwangu…’akasema

‘Ukiwa umevaaa nguo za hospitalini, hapa ulikuwa unakwenda wapi…?’ nikamuuliza

‘Sikiliza muheshimiwa…haya ndio mambo nimeanza kuyalalamikia hapa , kuwa kuna hali inanitokea, nachukuliwa bila kujijua…sijui kinachoendelea, …napelekwa,..wakati mwingine hadi baharini…’akatulia.


‘Jamani mnaweza kuyaamini hayo…’nikasema nikimuangalia hakimu.


‘Kwani anaweza kutembea…?’ akauliza hakimu

‘Kuna video hapa inaweza kulithibitisha hilo,..huyu mtu pale hospitalini alipolazwa, amekuwa akitoka usiku na kwenda baharini, sehemu nilipogundua hizo nyaraka za benki, sasa atuambie aliwezaje kutembea, aliwezaje kufika huko,…?’ nikauliza


‘Ni kweli Dalali, unaweza kutembea , kwanini sasa unatudanganya…?’ akuliza hakimu


‘Muheshimiwa hakimu, mimi siwezi kutembea,..hayo yanayofanyika ni ….kitu mimi sikijui….ni…’akawa analalamika kwa mikono.


 Ple mimi nikamuangalia Dalali usoni…nikijua kile nilichokitaka kwake nimeshakipata , kumjenga hofu, kwa haraka nikasema;


‘Naomba kitambulisho chako…’nikamwambia Dalali,  na Dalali kwanza akasita baadae akakitoa kitambulisho chake,..na kunikabidhi, hisia zangu ziliniambia kuna jambo,..na nilipokiangalia kile kitambulishi, nikahisi mwili mzima ukinisisimuka,…nikatikisa kichwa,  kukubali, na tabasamu likajaa mdomoni, halafu nikamuuliza;


‘Dalali hapa kwenye kitambulishi ndio sahihi yako..?’ nikamuuliza.


‘Ndio kuna tatizo gani kwenye sahihi yangu..?’ akauliza na mimi nikachukua ile karatasi ya malipo ya mkopo, nikaangalia, halafu nikageuka kumuangalia wakili..nikamuonyesha sehemu ya sahihi, nikamuuliza huyo wakili…


‘Unaona nini hapo…?’ nikamuuliza wakili naye akabakia kushangaa, halafu akasema;


‘Oh…Sahihi zinafanana…’akasema, hapo nikamgeukia Dalali,

‘Dalali sasa umepatikana….’nikasema kwa sauti na Dalali akawa kanitolea macho ya kujiuliza tu..


NB: Je ndio hitimisho hilo, NI DALALI AU NI MAJALIWA?



WAZO LA LEO: Kibinadamu ni rahisi sana kumshuku mwingine ubaya, …na hata kujaribu kuthibitisha ubaya wake,..lakini kumbe ubaya huo, tunaowashuku wengine na kuwanyoshea vidole, sisi wenyewe tunao..na huenda tuao ubaya zaidi ya ubaya wa huyo tunayemnyoshea kidole. 

Ni sawa kibinadamu tunatakiwa kushauriana, kukatazana mabaya,.na kuelekezana mema, huenda katika kufanay hivyo hata sisi wenyewe tunaweza kujirudi…lakini iliyo vyema, kabla ya kutoa ushauri huo, au kuelekezana au kunyoshea wengine vidole, tuanza kwanza kwetu sisi wenyewe, kwa vitendo, ushauri wa vitendo hujenga mahusiano mema zaidi. Ushauri wa vitendo ni mwalimu mnzuri
Ni mimi: emu-three

No comments :