Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Friday, January 12, 2018

MKUKI KWA NGURUWE-56


 Usiku huo kwangu ulikuwa wa historia,

Niliendelea kufuatana naye, nikawa sasa nachoka, lakini nitafanyaje, na ikafika sehemu sasa nikahisi anarudi nyumbani, nilipoona hivyo, nikajiuliza, haya akirudi nyumbani itakuwaje, mume sasa naanza kumuogopa!.

‘Haya tisa, usiku nitalalaje naye, akiamua kuniua, au kuleta fujo….?’ Nikajiuliza na muda huo bado nipo nyuma yake kila anapokwenda nipo naye. Kwa haraka wazo likanijia, ..nikampigia simu mdogo, huyu ndiye wanawezana.

‘Shemeji kuna tatizo gani?’ akaniuliza, alipopokea simu yangu

‘Nakuomba uje nyumbani, ni muhimu sana ...’nikasema

‘Kuna nini tena shemeji…unajua mimi bado nipo kazini, ?’ akauliza kwa mashaka, yeye kazi zake wakati mwingine anafanya hadi usiku

‘Kuna kitu nataka unisaidie kuhusu kaka yako,....’nikasema, sikutaka kumwambia ni nini kinaendelea kwa wakati ule, lakini nilifahamu nikimwambia kuwa ni mambo ya kaka yake, atakuja haraka.

‘Sawa nakuja shemji, lakini haumwi sana?’ akauliza

‘Haumwi sana.., ni jambo dogo tu nitakuambia ukifika nyumani kwangu, lakini kwa hivi sasa sipo nyumbani, nitakuarifu nikifika…’nikasema na kukata simu, sikutaka kumpa maelezo mengi

 Nikaendelea kumfuatilia mume wangu, badala ya kueleka nyumbani sasa anaelekea njia ya kwenda ofisini kwangu,…alipofika getini kuingia kwenye jengo la ofisini yangu akasimamisha gari, akapiga honi, na mlinzi akatoka, na nikasikia akimuuliza;

‘Mke wangu yupo ofisini kwake?’ akauliza

‘Hapana, sio muda wa kazi sa hizi…’akasema mlinzi

Wakati huo nilikuwa nimeshasimamisha gari langu, na hatua chache nyuma ya gari lake, na kwa vile mlinzi anaongea akiwa ndani kwa kupitia kidorisha, hakuweza kuona pale nilipokuwa nimesimamisha gari langu. Pale nikaona nikatoke ndani ya gari langi, ili niweze kusikia ni nini wanachokiongea,

Kwa haraka nikatoka kwenye gari langu na kusogea karibu kidogo na wao,sehemu ambayo hawo wawili hawawezi kuniona, nikawa nawasikiliza, nilisikia na maswali hayo ya kutaka kujua kuwa mimi nipo ofisi, akauliza ni kwanini sipo ofisini na yeye anajua kuwa mimi nipo ofisini

Mlinzi alimjibu vyema tu, japokuwa ilikuwa na maswali ya kushangaza, hapo nikaona nitumie mbinu, nikachukua simu yangu na kutuma ujumbe kwa yule mlinzi.

‘Mwambie mimi nipo nyumbani namsubiria, je yupo wapi...’nikatuma ujumbe huo wa maneno kwa yule mlinzi, ambaye kwa vile gari la mume wangu limemzuia, hakuweza kuliona gari langu, akasikia sauti ya ujumbe kwenye simu yake, akawa anausoma, halafu akamwambia mume wangu.

‘Mbona mke wako anasema yupo nyumbani anasema anakusubiri, anauliza wewe upo wapi...’akamwambia

‘Hapana mimi nina uhakika yupo ofisini kwake, nina uhakika huo, ..nataka kwenda kuonana naye fungua geti, unanifahamu mimi ni nani au sio...’akasema

‘Hapa ofisini kwasasa hayupo bosi, na haturuhusiwi kumfungulia mtu yoyote zaidi yake,  saa kazi zimepita na mke wako aliondoka mapema tu, hakuna mtu ndani, zaidi ya sisi walinzi huku nje...’yule mlinzi akasema

‘Mh, oh, ina maana muda wa kazi umekwisha, sio hamnijali mimi, ok, sawa,..oh, samahani, kwa usumbufu ....’akasema na kulirudisha  gari lake nyuma na kuligeuza, nikajua kwasasa atakuwa akielekea nyumbani.

*******

Nilimfuatilia hadi tukafika nyumbani

Tulipofika nyumbani, nikaliona gari la mdogo wake limeshafika, mjamaa, kwa akateremka kwenye gari, hakuangalia pembeni, kwa haraka haraka akakimbilia ndani, wala hakuangalia pembeni,

Mimi nikateremka na kukagua gari lake kama kila kitu kipo sawa, mlango kafunga, na nilipohakikisha kama kila kitu kipo sawa, nikaingia kwenye hilo gari, na kulisogeza sehemu salama, na mimi nikaingia kwenye gari langu na kuliingiza sehemu maalumu ya magari, halafu, kwa haraka nikakimbilia ndani.

Nilipofika ndani nilimuona mdogo wake, akiwa kakaa kwenye sofa, lakini mume wangu hakuwepo, nikamuuliza

‘Umemuona kaka yako akiingia?’ nikamuuliza

‘Ndio kaingia, lakini hakunisemesha, alionekana kama hanioni, kanipita kwa haraka akakimbilia chumbani kwenu, kwani kuna nini shemeji, maana hata machoni, sio w wa kawaida?’ akaniuliza

‘Nitakuambia, ila muhimu nataka ulale hapa leo, kesho inabidi tumpeleke kaka yako hospitalini,  kaka yako anaonekana kuchanganyikiwa kidogo....’nikasema.

‘Ina maana hiyo hali imejitokeza?’ akauliza, na mimi nikamuangalia kwa mshangao na kumuuliza;

‘Ina maana ulikuwa unafahamu kuwa kaka yako ana hali kama hiyo ya kuchanganyikiwa, kwanini unasema hiyo hali imejitokeza?’ nikamuuliza

‘Ndio nafahamu… kipindi kile akiwa kule hospitali kwenye uchunguzi walisema hivyo, lakini jinsi alivyokuwa na maendeleo mazuri wakati anaruhusiwa, tuliona kuwa haitaweza kutokea tatizo kama hilo, hata docta, rafiki yake, alisema huenda hiyo hali haitajitokeza tena, baada ya yeye kumfuatilia kwa muda.....’akasema

‘Sasa ndio hivyo imejitokeza, na kwa hali kama hiyo, kunahitajika mtu wa kuwa naye karibu wakati wote, naogopa usiku nisije nikashindwa, nikapitiwa na usingizi, ndio maana nikakuita. Sasa hivi cha kumsaidia hapa ni dawa, nahisi ndio maana walikuwa kuna madawa yale ya usingizi,..’nikasema

‘Ndio, sib ado zipo..?’ akauliza

‘Zipo tele tu, hazitumii siku hizi..’nikasema

‘Tunaweza kumpa au sio…’akasema

‘Sawa tutampa,ila wewe inabidi ulale hapa, sasa kama kuna lolote la kufuatilia huko kazini kwako nenda kalimalize urudi haraka , au wapigie simu, ...kuwa kuna dharura, hutarudi tena huko...’nikasema

‘Hakuna shinda shemeji mimi nimesha waaga kabisa,...’akasema na mara mume wangu akatoka  na kuniangalia alionekana kama kunishangaa, halafu akasema;

‘Mke wangu, sijui kuna nini kinaendelea kwenye kichwa changu...hivi nipo sawa kweli…’akasema akishika kichwa chake.

‘Kwani unajisikiaje?’ nikamuuliza

‘Hivi nikuulize ni lini tulikuwa tunaongea kuhusu mtoto, ukaniuliza kuwa labda mimi nina mtoto nje, tena mtoto mwenyewe wa kiume?’ akaniuliza akiniangalia kwa macho ya kujiuliza. Kidogo, macho yanaanza kurejea kwenye uhai, lakini…

‘Mchana, au…jioni hivi,…tuliongea ndio, kwani vipi?’ nikamuuliza

‘Nimekwenda kumfuatilia huyo mtoto, hayupo,... hayupo kabisa …nahisi kuna tatizo, unajua hata huyo mama anayekaa na huyo mtoto hayupo.....nahisi watakuwa wameamua kutukimbia na mtoto wetu, huenda wameamua kunisaliti, una uhakika, kuwa nina mtoto ....tuna mtoto wa kiume, una uhakika?’ akawa ananiuliza

‘Hamna kitu kama hicho mume wangu, nilikuwa nakutania tu, nilikuwa nakuuliza kama kukupima akili yako, kwani vipi tena ...’nikasema

‘Huo sio utani mke wangu, nikweli nina..tuna mtoto...ni lazima tumchukue mtoto wetu, Yule mama eeh,  hawezi kumlea kabisa…eti siku moja anadai kuwa mtoto ni wake na mimi hanitambui…wewe, hahaha, eti yeye ni mama yake na mimi sina haki naye,..’akasema

‘Mama yake!! Kwani mama yake ni nani…?’ nikamuuliza bila kujali kuwa namuongezea mawazo

‘Mama yake, eeh!!!,…mama yake si wewe, tatizo wewe umechanganyikiwa, sijui kwanini, hivi kwanini ulitaka kumtupa mtoto wetu…niambie ni kwanini, sasa mimi namtaka mtoto wangu , leo hii hii…hili sio jambo la mdhaha, mimi namtaka mtoto wangu haraka…’akasema kwa hasira sasa.

‘Sikiliza mume wangu tutamtafuta huyo mtoto kesho, unasikia, kesho tutakwenda mimi na wewe hadi kwa huyo mama yake unasikia, usiwe na wasiwasi…’nikasema

Kidogo akatulia, na akatizama saa yake mkononi, halafu akasema;

‘Tatizo ni huyo  Makabrasha nilimpa kazi sasa sijui imekuwaje, unajua nimefika hadi ofisin kwake, ili aweze kulifuatilia hili jambo kisheria, yaani hiyo ndio njia sahihi, kwenye sheria, na mikataba ikiwepo, mtu hawezi kuvuka kihunzi, sheria itambana,…kiukweli mimi siwezi kuacha damu yangu ipotee hivi hivi, halafu mtoto mwenyewe ni wa kiume,…’akasema na mimi hapo nikawa kimia

‘Mke wangu, si wewe ulikuwa unataka mtoto wa kiume, ni wewe au ni mimi, …haah, ndio, sote tulikuwa tunataka mtoto wa kiume si ndio hivyo…?’ akauliza

‘Ndi-ndio hivyo…, mungu lakini hatuja-jalia kumpata mtoto wa kiume.., tutampata tu, mungu akipenda…’nikasema

‘Keshatujalia bwana, wewe vipi, si ndio huyo, huyo mwanamke ni mwizi tu…kamchukua, nikuulize kwanini ulikuwa unataka kumtupa, mtoto wetu…eeh..?’ akanigeukia tena kwa hasira.

‘Si nimekuambia mume wangu kesho tutamfuata sijamtupa..’nikasema

‘Yah…kesho,..maana yule ni mwizi tu, unasiki,a huyo ni mtoto wetu, …sasa tuyaache hayo, wakili atalishughulikia hilo, Yule wakili hana mchezo, yaani vyovyote utakavyo, anakufanyia, ni mjanja kweli kweli, sasa mke wangu, ni kuhusu ule mkataba wetu, eeh, si unaujua  eeh…’akasema

‘Ndio ule wa zamani…’nikasema

‘Kwani kuna wa zamani na wa sasa…mke wngu umechanganyikiwa nini…ngoja nityampigia wakili aje, tumalizane, nataka tulimalize leo hii , hii, sitaki cha zamani na sasa, mkataba ni mmoja, au sio mke wangu..?’ akaniuliza na mimi hapo nikamuuliza

‘Huyo wakili ni nani ..?’ nikamuuliza

‘Si Makabrasha, na wewe bwana umeshamsahau tena, ndio huyo huyo, sasa hivi nimetoka ofisini kwake, yeye hayupo, walinzi wake wababaishaji, eti wanadai, kafariki, hawa watu bwana, kama hawampendi mtu watamzushia uwongo tu , hivi kuna mtu anaweza kumzulia mwingine kifo, ngoja nitamuambia, na Yule atafukuzwa kazi, wewe subiria tu…’akasema

‘Basi usijali mume wangu…hilo tutalifuatilia hiyo kesho usiwe na wasiwasi kabisa…’nikasema

‘Sawa kabisa mke wangu, mtoto yule ni wa kwetu, kwahiyo tuna watoto hawa....’akasema akionyesha vidole vitatu.

‘Hapana mume wangu sisi tuna watoto wawili,....’nikajikuta nimesema hivyo

‘Usinibishie mimi, ...., mimi ndio najua, mimi ndio mume wako,...tuna watoto hawa…w-nne, ...na ...’akasema

‘Wanne tena…’nikasema, na kabla hajanijibu, ndugu yake akakohoa, sijui ni makusudi au ilitokea tu, na hapo hapo akageuka ndio akamuona mdogo wake, kwanza alimuangalia kama anamshangaa, baadae, akatabasamu na kwa haraka akamsogelea, kama vile anataka kumkumbatia, lakini mdogo wake akanyosha mkono wakashikana kusalimiana.

‘Jembe,…hahaha! Jembe langu umekuja, sasa mambo safi, utanisaidia kazi moja..kuna kazi moja usiku huu huu…unazijua zile zetu, kwanza sina pesa, lazima tufanye dili la nguvu, pili, kuna yale mambo yetu,..mmh,…, hiyo ni siri yetu,..unasikia, sitaki mke wangu afahamu,...unasikia jembe....’akasema na hayo maneno kuwa hataki mimi nifahamu akawa kama anamnong’oneza, .

Mdogo wake akawa anamwangalia kaka yake kwa mashaka.Nilimuonyeshea ishara akubali tu, na mdogo wake, akamsogelea kaka yake na wakawa kama wanakumbatiana, nilimuona mdogo wake akijizuia kutoa machozi. Nahisi kuna hisia za kulia zilitaka kumjia, anampenda kaka yake pamoja na wakati mwingine hawaelewani.

Niligeuka na kuangalia pembeni, maana kwa hali kama ile hata mimi mwenyewe hiyo hali ilinijia, nikiwazia mbali, kuwa huenda mume wangu ndio hivyo kaharibikiwa hatapona tena, karibu hata mimi nilitaka kutoa machozi,..kiukweli mimi nilishajua kuwa mume wangu keshapona, na tunatakiwa kuganga yajayo.

‘Sasa hili tatizo litaisha lini..?’ nikajikuta nimejiuliza hivi tena kwa sauti, na sijui kama walinisikia, kumbe kweli walinisikia kwani mume wangu akasema;

‘Kesho…unasikia mke wangu, kesho, litaisha,..’akasema mume wangu hivyo, sijui alikuwa na maana gani, na muda huo alikuwa bado kamuangalia ndugu yake, wanaongea

Na ndugu yake akaingilia kati na kumuongelesha kitu kingine muda huo huo, kwahiyo wakawa wanaongea sasa wao wawili , na mimi nikaa kimia…kama vile mimi sipo, na kuna wakati anamuambia mdogo wake kuwa hayo ni ya siri hata mke wangu hatakiwi kujua, keshasahau kuwa na mimi nipo hapo karibu.

‘Sasa hili ni tatizo…’nikajisema kimoyo moyo sasa.

Kwa muda huo nikamkumbuka docta rafiki wa mume wangu, nilitamani nimpigie mambo kama hayo angenishauri vizuri tu, lakini kwa hapo nisingeliweza kufanya lolote

Aliendelea kuongea na mdogo wake mambo mengi tu, na kama kweli hayo anayoyaelezea kayafanya basi mume wangu yupo kwenye mambo ya hatari ambayo yatamweka pabaya.

‘Mdogo wangu, tuna mtoto wa kiume, nilikuambia, ukanibishia ni kweli sio ndoto, sasa nimeamini…’akasema na mdogo wake akawa anaitikia tu

‘Tatizo ni hawa wanawake hawaeleweki kabisa, mambo mengine ya siri wanaharibu, sasa kaharibu…na mke wangu akijua mmh..lakini usijali nitayamaliza tu…si unanifahamu, ..we acha tu..’akasema na mdogo wake akawa ananiangalia mimi, hapo akaharibu, kwani mume wangu akageuka kuangalia nyuma, ndio akaniona...

Aliponiona akawa kama kashtuka, halafu akasema

‘Oh kumbe upo, umekuja saa ngapi…oh, nilikuwa nongea na bwana mdogoo, siunajua tena, huyu ndiye mtu wangu kabisa..lakini mke wangu kama tulivyoongea, eeh, usiniangushe, Yule ni mtoto wetu kabisa, ukimuona utaniambia…wanafanana na watoto wetu kabisa,…’akasema.

‘Sawa, sawa nimekuelewa, sasa unywe dawa ukalale…’nikasema

‘Mimi nilale saa hizi, ...hapana bado naongea na bwana mdogo…’akasema

‘Unatakiwa kunywa dawa zako kwanza huu ndio muda wake..’nikasema nikijua akizinywa hizo dawa, atazidiwa, ataishia kulala tu

‘Dawa kwani mimi naumwa bwana, usiharibu mada,…’akasema na kumgeukia mdogo wake

‘Unaona ndio mambo siyataki haya, hawa akina mama…mmh, unajua bwana mdogo nikuambie kitu, hapa  nikutoka tu, sisi tutoke hapa twende sehemu, tukafanye mambo yetu, halafu kitaeleweka, au sio..mimi hapa sina pesa, tutapata wapi pesa..dili kwanza..au sio?’ akasema sasa akiwa kanisahau kidogo, akasimama na kumshika mdogo wake mkono ili waondoke.

 ‘Sasa mke wangu nataka kutoka na mdogo wangu, tutaonana baadaye...’akasema na mdogo wake akawa anasita kuondoka, na wakati huo kashikwa mkono ili watoke naye

‘Kaka hebu kunywa dawa kwanza ni muhimu, si unajua afya ni bora kuliko mambo mengine, mimi nipo, tutatoka tu..’akasema mdogo wake

‘Usimsikilize shemeji yako,..twende bwana, amri, kaka akiongea jambo ni amri,..twende, halafu.., tutarudi, kwani dawa zitaharibika…’sasa akawa anamvuta mdogo wake waondoke.

‘Mke wangu usijali, mimi nitarudi, sifanyi fujo, mwenyewe utaona, hapa,..nikiwa na hili jembe, sina wasiwasi, huyu ndiye mimi, ukimuona huyu umeniona mimi, hata nikifa leo, usije ukamtupa mdogo wangu huyu, unasikia…’akawa anaongea sasa kama kalewa.

‘Mume wangu…mbona haupo sawa…’nikasema

‘Nani kasema sipo sawa, halafu wewe mjanja kweli kweli,…hahaha, umejuaje,…nilipoingia ndani, kuondoa mawazo, nilikunywa kidogo tu…kidogo…, hahaha, hamuwezi kininyima starehe yangu, hahaha’ akacheka sana tu

‘Sasa sikiliza, huyu ni jembe langu,,....usije ukamnyanyasa mdogo wangu, hata kama nimekufa, mimi nitafufuka na kuja kumtetea, nampenda sana mdogo wangu huyu, achana na Yule mwingine, Yule … Yule anajifanya mtakatifu saana,.....hili ndilo jembe langu...’akasema na kumshika mdogo wake mkono, wakatoka naye nje…

Nilibakia mle ndani nikiwa sijui nifanye nini, …lakini kwa vile sasa yupo na mdogo wake, nilihisi amani kidogo,…

‘Ngoja sasa nione kitakachofuata,..hili ni langu tena..’nikasema

 Na hata kabla sijasimama, ili nielekee chumbani, mara simu yangu ikaita, moyo phaaa! Mlio wa simu sasa unanipa kero, naogopa na kuogopa…

Nikaangalia mpigaji,.. ilikuwa ni namba ya nje, kidogo nikatulia, nikijua huyo  atakuwa ni yule rafiki yangu anayesoma nje….

**********

‘Habari za huko?’ nikauliza

‘Nzuri tu, bosi, tumemaliza mitihani mmoja kesho tunafanya mwingine, na huenda nikaja huko siku za karibuni...’akasema

‘Itakuwa vizuri sana, maana kuna mambo nataka tuyamalize...’nikasema

‘Yale yale..au?’ akauliza

‘Ndio,..yale yale, na hapa tunapozungumza mume wangu anaonekana hayupo sawa..kachanganyikiwa…’nikasema

‘Mhh, hiyo hali imeshajitokeza tena  ehe..?’ akawa kama anauliza

‘Ina maana unafahamu?’ nikamuuliza

‘Ndio, nilipofika kwa docta wake, moja ya jambo alilonielezea ni hilo, nilijua na wewe unafahamu..’akasema

‘Hapana…’nikasema

‘Basi ni hivyo uwe makini naye sana…na bora umueleze docta yake achukue hatua anaweza kufanya jambo baya...’akasema

‘Kwanini docta alikuambia wewe na hayo ni mambo ya siri ya mgonjwa au mke wake ?’ nikauliza

‘Umesahau kuwa mimi ni ndugu yako wa karibu na hakuniambia kwa nia mbaya,  ...’akasema

‘Ni ndugu yangu wa karibu,ehe, ...kweli wewe ni ndugu yangu wa karibu, kama ungelikuwa ni ndugu yangu wa karibu ungelinifanyia hayo uliyonifanyia…’nikasema kwa hasira

‘Yapi tena bosi, mbona kila siku unakuja na hoja mpya, ...?’ akauliza.

‘Unayafahamu sana.....’nikasema.

‘Bosi nakuomba bosi, usichukulie hayo mambo kwa hasira, nikirudi tutaongea, nina imani hakitaharibika kitu..’akasema

‘Kama ni kweli, ninavyosikia, kama ni kweli, wewe umezaa na mume wangu...sizani kama tutakaa kwenye meza moja tuongee, hilo sahau, na nilishakuambia, kama kuna mtu anataka ubaya na mimi ...basi atembee na mume wangu, sitajali kama ni nani, hata kama ni ndugu yangu wa tumbo moja, nitafanya yale yale niliyowahi kukuambia...’nikasema.

‘Lakini...’akaanza kujitetea.

‘Sasa hivi mume wangu anaumwa, na hali aliyo nayo siwezi kufanya lolote, lakini akipona tu,...kama ni kweli, basi, ...mkataba utafanya kazi yake, na mengine yatafuta baadaye....’nikasema.

‘Mkataba upi bosi ...maana kama nilivyoona, na kuambiwa, kwenye mkataba hakuna tatizo, ...mume wako ana uhuru wa kufanya lolote, huoni kwamba ukitumia huo mkataba utakuwa umejimaliza wewe mwenyewe..’akasema

‘Kumbe hata hayo ya mkataba unayafahamu au sio…naanza kupata picha, sasa kama ndivyo mlivyopanga hivyo, tutapambana mahakamani…si ndio ujanja wenu huo, kuwa mumegushi mkataba ili mtoto wake aje kurithi mali yangu, au sio?’ nikauliza

‘Mimi sijapanga lolote, mimi niliitwa kuja huko kwa dharura, na nilipofika hapo, nikajikuta naingizwa kwenye mambo ambayo hata siyafahamu, na kuhusu mtoto, mtoto ni wangu, hana baba,..hayo ni yao, na ndoto zao, wala usiwe na wasiwasi na mtoto wangu…’akasema

‘Kwahiyo wewe kilichokurudisha huku, ilikuwa nini hasa…?’ nikauliza

‘Mimi sikurudi kwasababu hiyo, nilirudi kwasababu niliambiwa kibali change kina matatizo, kwahiyo nahitajika kurudi kukirekebisha, kwanza nilijua ni wewe umefanya hivyo, ili kuondoa udhamini wako, nikaona isiwe shida, na bahati nziri akapatikana mdhamini mwingine,…sasa sijui kama ni wewe ulifanya hivyo, au kuna jingine ndani yake, mimi sikutaka kulichunguza muhimu nimalize haya masomo mengine nitakuja kuyafahamu baadae…’akasema

‘Usinidanganye kila kitu nimeshakifahamu, na kwanini hukuniuliza, kuhakikisha hilo, na kwanini nifanye hivyo, maana mpaka unakuja mimi sijui lolote kuhusu ujio wako, nimesikia siku ulipofika, ndugu yangu, dunia hii ni mapito, acheni hayo jamani…’nikasema

‘Kiukweli, utaamini utakavyo, sikulaumu kwa hilo,… lakini ukweli ninaokuambia mimi ni huo, kuwa hiyo mipango yao sikuwa na ufahamu nayo kabisa,....walipanga wao wenyewe, ..kama ningelifahamu hivyo nisingelikuja huko kabisa, ningetumia njia nyingine ya kulimaliza, bila hata ya wao kuhusika,…mimi kilichonirejesha hapo ni taratibu za kibali changu…’akasema

‘Tutakutana tu…dhuluma hata siku moja haidumu,..kiukweli kama ni kweli, umefanya kosa kubwa sana ambalo …sizani kama naweza kukusamehe,..mpaka sasa sijaamini hilo, siwezi kuamini kuwa wewe unaweza kunifanyia hivyo, …’nikasema

‘Bosi, niamini haya ninayokuambia, sikuwa nafahamu lolote…mimi nilipofika tu, yakatokea hayo yaliyotokea, kama nilivyokuambia awali, na ndio nikauona huo mkataba, sijui lolote jingine, na hata kama nimeweka sahihi yangu hapo, sihusiki, na hawatafanikiwa mipango yao ....’akasema

‘Sawa, endelea kunidanganya, najua nalipa fadhila zangu kwenu, lakini ahadi yangu na dhamira yangu ipo pale pale, mwenyewe utaona ukirudi , labda upotelee huko huko, hilo nakuahidi, nyie si ni wajanja sana, ngoja urudi ....’nikasema kwa sauti ya dhamira

‘Jamani dada, ...bosi, usinifikirie hivyo kabisa, sipo kabisa kwenye hayo mambo yao, ndio maana wakatumia mbinu hizo walizotumia, ...hebu niambie mimi ningelifanya nini kwa hali kama hiyo,...Bosi, nakuhakikishia mimi nikirudi tutayamaliza hayo, wala sipotei, nitarudi...’akasema

‘Najua utarudi labda na ndoto ya kuwa  mke mwenza, au mshirika mwenza, au nani utakavyojua mwenyewe na hawara wako ?’ nikamuuliza

‘Mimi sielewi una maana gani kusema hivyo bosi..hayo yametoka wapi tena, mimi ni mdogo wako jamani…’akasema

‘Unaelewa sana nina maana gani, sasa hivi sipo kule kwenye kuamini kinyume chake, wengi waliniona mjinga kuwa ukweli upo, lakini akili imefungwa, sasa akilio imefunguka, na sitaamini uwongo wenu tena, na sitaki utetezi wako wowote....’nikasema.

‘Basi wewe subiri nirudi, naona hapa kwenye simu  hatutaelewana, ila nakuhakikishia kuwa sijui lolote kwenye mambo yao, na mimi siwezi kufanya jambo baya dhidi yako, na ukiona nimefanya jambo, ujue ni kutokana na ushauri wako, sijawahi kukusaliti mimi, niamini hivyo....’akasema

‘Niliwahi kukushauri uje ufanye ufusuka na mume wangu?’ nikamuuliza

‘Bosi, ufuska gani jamani, mmh mimi naona hapa hatutalewana tena,...kwahivi sasa, naomba uniache ili nimalize masomo yangu kwanza, hayo na mengine mengi tutayamaliza tu.., hakuna tatizo kabisa....mimi sijawahi kufanya jambo kinyume na matakwa yako, kweli si kweli ?  sema ukweli wako, na kwahiyo hata hili, litakwisha tu kwa amani, hilo nakuthibitishia, ...’akasema

‘Sina amani na msaliti mimi,..rafiki anyekuwa nyoka, sina amani nay eye tena,….wewe hujui nitavyoteseka huku, hujui kabisa, wewe na mwenzako ni nyoka wanafiki wakubwa....’nikasema

‘ Oh imekuwa hayo..lakini sawa, samahani kwa hilo, nina imani yatakwisha tu bosi, pole sana,…’akasema na nikahisi analia

‘Unalia nini sasa…’nikasema

‘Inaniuma sana…hujui hata mimi ninavyoumia, sikutarajia haya kabisa,  ila mimi nakuthibitishia kuwa hilo litakwisha kwa amani tu, kama utanielewa, maana unavyofikiria wewe sivyo kabisa, samahani sana kwa kukufikisha hapo, na matatizo yote yanayokukumba,… nakuomba niwahi darasani tafadhali,  kwaheri,… nisalimie shemeji na watoto, ..’akasema na kukata simu.

NB: Kisa kinarudi kuleee..hii ni kuashiria kuwa mambo sasa yanaanza kuwekwa hadharani.


WAZO LA LEO: Tuwe makini na kauli zetu , ulimi unaweza ukasababisha mema na mabaya,ukiutumia vyema ulimi wako unaweza ukaleta faida kubwa kwenye jamii, lakini ulimi huo huo,  ukiutumia vibaya, unaweza ukaleta majanga makubwa kwenye jamii za watu, tena wenye elimu zao.  Ulimi unaweza kugeuza marafiki wakawa maadui. Tumuombe mola wetu atujalie tuweze kudhibiti ndimi zetu, ili jamii ziishi kwa amani na upendo.

Ni mimi: emu-three

No comments :