Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Monday, August 7, 2017

DUWA LA KUKU....30


Yule mzee aliagiza vitu vingi akawa anakula huku kainama, hakutaka kuinua kichwa, labda hakutaka watu wamuone, na alipomaliza, akaagiza maji ya kunwa, na mimi nakuchukua maji na gilasi nikafika mezani nikamumiminia na kumpa , akaipokea na alipotana kunywa akainua uso akaniangalia,..na mimi muda huo nimesimama mbele yake ili kama anataka maji mengine nimuongezee kwenye gilasi aliyokuwa kaishika!

Aliponitupia jicho, na macho yake kukutana na yangu, akashtuka, …na ulikuwa mshtuko kweli, sio ule mshituko wa kujificha, mpaka gilasi ya maji aliyokuwa kaishikilia, ikamponyoka, na kudondoka sakafuni ikavunjika, na kila mtu akasikia mlio wa hiyo gilasi ikivunjika, na mama mwenye mgahawa akasema kwa hasira…

‘Vipi wewe mzee leo, mbona unavunja vyombo vyangu…’akasema akimuangalia kwa mashaka, na yule jamaa alikuwa bado kaduwaa, akiniangalia mimi..
Haikutosha akaanza kulia na kusimama, akatoke kwenye meza na kunisogelea, akapiga magoti mbele yangu huku akisema
‘Samahani nisamehe…..’ huku akiwa kashikilia miguu yangu, ili nisiondoke…
Tuendelee na kisa chetu

***********

Kila mtu pale alishikwa na butwaa, ni kwanini huyo mbaba mtu mzima, japokuwa kwa uvaaji wake na jinsi anavyoonekana, alikuwa akionekana kama kachanganyikiwa,, manywele yamevurugika , madevu kayaachia, ya yenyewe yamevurugika, kwa ujumla hakuonekana katika hali ya kawaida, hasa kwa umri kama wake,…

Sasa analia na haitoshi, anakuja kunipigia magoti, kila mtu alihisi sio bure, yawezekana kukawa jambo kati yangu na huyo mbaba. Lakini kiukweli mimi nilikuwa simfahamu huyo mbaba, na sikumbuki kabisa kukutana na mtu kama huyo kwangu alikuwa mgeni kabisa.

 Yule mama, maana ndio alishakuwa mlezi wangu japokuwa,namlipa kodi, ananilipa mshahara wangu wa kila siku, lakini alishachukua dhamana ya kuwa mimi ni sawa na binti yake, sasa alipoona kile kitendo cha huyo mbaba, haraka  akasimama na kumkabili huyo mzee, lakini alishachelewa huyo mbaba alishapiga magoti, mbele yangu na kunishika miguuni…nilikuwa nimevaa dera refu sana,ikizingatia hali yangu.

Pale nilipo nilikuwa najisikia vibaya, natamani hata kutapika, moyo ukawa unanienda mbio,...nilitamani aniachie nisije kumdondokea, lakini kila nikijaribu kuinua mgu siwezi jamaa kanishikilia bara bara..

'Vipi wewe mzee unataka nini  kwa huyu bint yangu, si ameshakupa maji ya kunywa, unataka nini zaidi?...’akamuuliza.

Jamaa ni kama hasikii akawa kanishikilia na kulaza kichwa cheke miguuni mwangu huku akiinua uso kuniangalia, uso wa huruma huku machozi yakimtoka, mimi nikawa hata sielewe huyo mbaba ana nini kwangu
Kwa kitendo kile sikuweza kusogeza mguu, maana kanishikilia, nikisogeza mguu nitandondoka, na huku nimeshikilia jagi la maji.

‘Wewe mzee vipi, unataka nini, unajua unamfanya binti yangu ashindwe kuwajibika, hii sasa unatuletea vurugu kazini, na tutakuitia polisi…’akaambiwa

'Ninataka anisamehe…..ndio nitamuachia hu-huu mguu…’akasema

‘Akusamehe kwa lipi kwani umemfanyia nini kibaya…?’ mama akamuuliza

‘Mi-mi..na-na taka  niongee na ye-ye,  ili aweze kunisamehe..ta-fa-dhali mama ‘n-ti-ti-lie…’akasema sasa akijaribu kugeuza kichwa kumuangalia huyo mama.

Huyo mama kwanza akanitupia jicho, na halafu kuwatupia macho wateja wake, akainua mkono kuwaashiria wateja kuwa huyo mzee kachanganyikiwa wasimjali.

'Unasema, akusamehe, kwani ulimkosea nini, muachie awahudumia wateja…unatupotezea muda, hujui ni hasara kwetu…’akaambiwa

‘Nitawalipia hiyo hasara lakini ..na-na taka kuongea na –na , na huyu binti,…kwangu ni-ni muhimu , sa-sa-sana…’akasema

‘Hapana muachie kwanza,…’yule mama kajaribu kumuondoa huyo jamaa kwenye miguu yangu, lakini alikuwa kashikilia bara bara, na sasa mama akashikwa na mshangao, akajua sasa mzee mzima kazamiria

‘Sema sasa kakukosea nini..mtu atakusameheje wakati hakufahamu, na hafahamu kosa lake ni nini..?’ kaulizwa

'Yeye  mwenyewe anajua,….ndio maana nataka anisamehe,….’akasema akizidi kunishikilia miguuni.

'Wewe mzee mimi sikujui, na sijawahi kukuona hata siku moja, niachie nifanye kazi …’nikalalamika, 

 .
'Nitakuachia lakini mpaka,ukubali kuwa utanisamehe…..’akasema

'Nikusamehe nini sasa, kwani ulinikosea nini, mimi sikujui na sijui kosa ulilonifanyia, haya niachie uniambie kosa langu, …’nikasema.

'Ina maana umenisahau mimi…, mungu wangu sasa hili ni balaa, ..'akasema sasa akazidi kunishikilia, huku analia

‘Nisamehe, nisamehe….’akawa anasema hivyo hivyo tu.

 Ikawa sasa ni vurugu, maana wateja wanataka huduma, mzee hataki kuniachia, kang'ang'ania miguu yangu, ikabidi sasa wateja waingilie kati na kumuondoa huyo mzee kwa nguvu, na kitendo hicho kilinifanya mimi niwe kwenye wakati mgumu.

 Lakini wateja walikuwa na nguvu, wakatumia nguvu na kumuondoa miguuni mwangu baada ya kumgonga gonga kidogo mabegani, na juu kwa juu wakambeba na kumtoa nje…na aliponiachilia nikakimbilia sehemu ya haja na kutapika, na nikasubiria mpaka hali ikawa njema ndio nikarudi ndani.

Nilipofika nikakuta wameshamtoa nje...

Na hata baada kumtoa nje, bado akawa  analia , kama anavyolia mtoto mdogo…, na kuomba watu wasimfanyie hivyo, maana bila ya mimi kumsamehe akifa ataenda kuangamia..kauli hiyo ikawashtua wengi, na ukazudka mjadala ni kwanini huyo mzee akatoa maneno makali kama hayo. Wengine wakazua visa vya watu kama hao na wakadai maneno mengine ya watu kama hao, yana ukweli ndani yake.

'Niacheni, nataka nimuombe msamaha, nimemkosea sana  siwezi kuondoka hapa mpaka nipate nafasi ya kuongea naye ili aweze kunisamehe….’akazidi kusisitiza.

 'Basi sikiliza mzee, muache huyo binti afanye kazi yake..unajua hapo yupo kazini,..akishamaliza kazi yake ndio mtaongea naye akujue wewe ni nani na ulimkosea nini, si sawa mzee…’akaambiwa na akazidi kusema.

 'Jaman mnajua ya kesho nyie,…bahati haiji mara mbili, je nikifa kabla hajanisamehe mnataka mimi nikaangamie…’akasema.

'Mungu atakujalia hutakufa mzee, je usingelimuona leo, mpaka hapo mwenyezimungu keshafahamu dhamira yako njema na ukizidi kumsumbua sasa itakuwa sio busara, utashikwa na kupelekwa milembe, unakufahamu milembe wewe..?’ akauliza
‘Mimi sio kichaa, kwanini wanipeleke Milembe, hamjui mimi nina matatizo gani, ….hamjui mimi na huyo binti tuna mahusiano gani, …je kama mimi ni baba yake..’akasema na watu hapo wakasema.

‘Aaah, kumbe, ..lakini hata hivyo mzee, subiria kwanza…’akaambiwa.

‘’Huyo sio baba yangu, baba yangu alishafariki…’nikasema kujitetea, na watu wakaniambia ninyamaze, kwani nikiongea nitamzidishia ukichaa huyo mzee.

***************

 Mzee akakaa hapo nje huku akilia akawa anaimba kama mtoto mdogo,…

‘Nisamehe , nisamehe, binti yangu,…nakuomba unisamehe binti yangu…’ basi akalia wewe mpaka akachoka, akawa kimia, tukajua labda kaondoka, watu wanachungulia nje wanamkuta kakaa hapo mlangoni, na kila anayetoka anamkagua kwa macho, na akiona kimia, anatulia huku akiwa kashikilia kichwa ile ya huruma.

 Baadae watu wachache waliokuwa wamebakia wakaanza kumuhoji mama mama mwenye mgahawa

'Huyu mtu ni nani…mbona hatujawahi kumuona..?’ akaulizwa

'Hata mimi simfahamu vyema, nimeanza kumfahamu hivi karibuni tu, alianza kuja, kunywa chai hapa, na awali nikajua hataweza kunilipa, kutokana na jinsi alivyo, yupo kama kachanganyikiwa, kama mnavyomuona hivyo, aheri leo ni msafi kidogo, siku nyingine utamkuta varu varu…lakini cha ajabu, akimaliza kula ni lazima alipe, sijui paesa anazipatia wapi,…’basi akatulia kidogo akikanda chapati zake.

Basi mimi nikamzoea, na kuanza kumtania kuwa yeye ni mume wangu,…wewe,..hapendi kutaniwa hivyo….’akasema

'Ukimuita hivyo anasemaje…?’ akaulizwa

'Hapendi, hapendi kutaniwa hivyo, yeye anasema ana mke wake mnzur, hahitaji mke mwingine, mke wake ni mnzuri sana anampenda yeye tu….’akasema

‘Hukumuuliza huyo mke wake ni nani na yupo wapi..?’ akaulizwa

‘Ukimuuliza hivyo anasema , nisimuingilie maisha yake, mke wake hataki kusemwa kwa watu, maana akijua yeye ni mume wake atajisikia vibaya, kwahiyo nisimuulize zaidi kuhusu mke wake…’akasema huyo mama.

'Hujamuuliza anaishi wapi, …maana hapo watu wakimuuliza anasema tu, mwambieni anisemehe,..mwambieni anisamehe, imekuwa kama wimbo….?’ Akaulizwa mama

'Nilimuuliza hilo swali akasema yeye anaishi duniani, potepote pale hapa duniani  ni nyumbani kwake, …’akasema huyo mama.

‘Sasa hapo ni mtihani, lakini …sio bure…’wakasema wateja.

'Huyo kachanganyikiwa, watu kama hao, kuchanganyikiwa kwao, inawezekana alikosana na mke wake, au maswala ya ajira na maisha yakamuwia magumu, akawaza sana mpaka akachanganyikiwa,..ninachojiuliza pesa anapatia wapi, labda akitoka hapa anakuwa omba omba…’akasema huyo mama.

'Yawezekana huyo binti yako anamfahamu, tuambie bintim, usikatae kwa vile yupo hivyo, kama ni mzazi wako sema, au kama alikufanyia,…maana wengine huwashika wanawake kwa nguvu..’wateja wakanigeukia mimi kwa maswali.

‘Ukweli wa mungu, mimi simfahamu huyo mtu, ni mara yangu ya kwanza kuonana naye..huyo kachanganyikiwa tu, au ananifananisha…’nikajitetea.

'Unajua leo naona mwezi mpya, maana siku zote anakuja hapa anakunywa chai yake na kuondoka, harudi tena mpaka kesho yake,…’akasema

‘Sasa leo mnaye mpaka kieleweke…’akasema mteja mmoja

‘Tutamuitia polisi…’akasema mama

‘Hapana msifanye hivyo, hebu msikilizeni kwanza, huenda akawa na jambo muhimu kwenu, msimzarau tu , kwa vile anaonekana kachanganyikiwa…’wakashauriwa hivyo.

'Au ndio yeye kampa mimba huyo bint yako, hataki tu kusema ukweli…’mteja mwingine akaropoka

'Hapana huyu binti yangu hajapewa ujauzito na huyo mzee, nyie hamuoni huyo mzee na binti mdogo kaam huyu wapi na wapi…’akasema huyo mama.

'Sasa mtuambie mama, bint yako kapewa mimba na nani, maana hilo swali kila siku tunaulizana, tukikuuliza huyo binti kaolewa unasema bado anayetaka alete posa, sasa utaoaje mke na mimb ya watu…’akasema jamaa mwingine.

'Wewe kama umpenda lete posa, ukipenda boga penda na majani yake, vyote ni vyakula tu, mtoto akikua anaweza kukufaa wewe kuliko huyo wa kumzaa wewe mwenyewe..’akasema huyo mama
‘Haya mama Ntilia, ngoja tusubiria hatima ya huyo jamaa, ila msimfukuze mpaka atimize lengo lake, ikibid binti amkubalia tu, kuwa kamsamehe, si inatosha,…’akasema

‘Siwezi kukubali tu bila kujua kanikosea nini..’nikadakia mimi niliposikia kauli hiyo.

‘Mimi nitakuambia mwenyewe mimi ni nani na kwanini nakuomba unisamehe..tafadhali naomba nipe nafasi niongee, lakini ningeliomba iwe faragha maana yaliyotokea sio vyema kila mtu akayasikia, tafadhali, msinione nipo hivi, lakini wakati mwingine ninakuwa na akili yangu timamu..nawaombeni sana waungwana mnielewe, sitaki kufanya  vurugu….’jamaa akasema sasa akwia kasimama mlangoni.

Mimi pale milipo, kila nikimuangalia mtu huyu nahisi vibaya, sijui ni kwanini, nahisi kama kutapika, moyo unanienda mbio, lakini alipokuja safari hii hiyo hali ikawa imetulia.



NB: Jamaa anataka kufunguka, ni nani huyu 



WAZO LA LEO: Pindi kukitokea uhasama kati ya pande mbili, lililo jema ni kuwakutanisha wahusika hasimu ili wao waweze kujieleza na kujitetea wakiwa na msuluhishi kati yao, msuluhisi ambaye hana masilahi na uhasama huo. Ni vabaya sana nyie watu wa pembeni kuhukumu bila ukweli kuwa bayana, nyie wapambe mnaweza mkaja kuhukumiwa siku ya mwisho kwa kupandikiza chuki na fitina, pindi mabaya zaidi yakitokea kati ya wahasimu hao. Kumbukeni fitina ni mbaya sana zaidi ya uchawi.
Ni mimi: emu-three

No comments :