‘Nani huyoo atakuja…?’ ilikuwa sauti ya mke wa mzee Majaliwa, na
kutufanya sote tugeukie huko upande sauti lipotokea, na mimi pale moyo ukaanza
kudunda dunda, nikajua sasa kumekucha, sasa hali itabadilika , wote walio-niona
mimi ni mwema, mtu mzuri, mwenye adabu, watakuja kuniona mimi ni mtu mbaya, muuaji..
Tuendelee na kisa chetu…
**************
Baba hakupenda hicho walichokuwa wakizungumza kizungumzwe kwa binti
yake, hakupenda hilo jambo liendelee kuisumbua familia yake, moyoni, zaidi ya
kutaka kumpata huyo aliyemsababishia binti yake hadi ajiue, hakupendelea hilo jambo liendelee kuwasumbua maana mola keshamchukua mja wake, wanataka nini tena,..
Hata kila hatua, anajikuta tatizo hilo likiendelea kumtafuna, likiendelea kumuathiri, yeye na familia yake, sasa wametokea hawa watu, anahisi wanaweza kumsaidia, lakini pia hataki familia yake isumbuliwe zaidi,.. saa je atafanyaje, …
Akageuka na kumuangalia binti yake, ambaye kwa muda huo alikuwa
akimuangalia huyo dakitari msaidizi, moyoni akahisi labda binti yake
keshampenda huyo dakitari, lakini ule uangaliaji sio wa kupenda ni uangaliaji uliojaa chuki ndani yake, usoni kulionyesha
kila kitu,..akajiuliza ni kwanini binti yake akawa anamuangalia huyo msaidizi
wa docta kwa namna ile,…, lakini hakuweza kusema neno.
‘Nimeuliza ni nani huyo mnamsubiria kwa hamu, nimesikia baadhi ya
mazungumzo yenu, naona yanahusu husu mambo ya waganga wa kienyeji, mimi sitaki
mambo haya kwenye hii nyumba, sitaki tena hayo mambo ya kumtafuta mchawi
yarejee kwenye hii nyumba, kwani hata akipatikana huyo mtu ataweza kumrejesha binti
yetu, ni miaka mingapi imepita, iwe leo…’akasema mama.
‘Lakini mama je akipatikana huyo aliyesababisha dada ajiue,
hutafurahi, ili haki iweze kutendeka..na yeye aadhibiwe?’ akauliza binti yake
na kunifanya nianze kukumbuka ile ndoto,..nilijua tu…ndoto zangu huwa hazisemi
uongo, nikikumbuka,…nikawa sasa naanza kutafuta namna ya kujiokoa hapo!
‘Yupo wapi, kama polisi walihangaika muda wote huo, hawakuweza
kumpata huyo mtu,…ni nani sasa mwenye uwezo zaidi ya polisi kwenye kutafuta
wahalifu, tuyaache hayo mambo jamani, tuyaache kama yalivyo, tumuombe mungu
tu,…yeye anajua ni nini cha kufanya, atamuadhibu kwa jinsi anavyoona yeye mimi
najua duwa ya mwenye kudhulumiwa haipitilizi…’akasema mama, na moyoni nilijihis
vibaya kweli.
Baba mwenye nyumba akatugeukia na kusema;
‘Mke wangu hawa unawafahamu ndio wanaotusaidia kuhakikisha familia
yetu inarejea kwenye msimamo wake tena, na zaidi wamesema wanaweza kutusaidia
hata ile nyumba yetu tuliyoihama ikawa salama tu lakini kwa uwezo wa mungu, sio
kwa madogori..unielewe hapo mke wangu,…hata tukitaka kurejea kule tutaweza au hata
tukitaka kuiuza hewala, itawezekana..’akasema mzee.
‘Mhh, kwa vipi, maana unanitia hamasa tu… ila kiukweli mimi hawa watu nimeshaanza
kuwaamini , kiukweli,…sina shaka na nyie, kwa vile mnafanya mambo kwa utaalamu
na kumtegemea mungu, nimeipenda hiyo…’akasema mama akitukagua mmoja mmoja, na
aliponitupia mimi jicho, akasita, ni kama alitaka kusema neno lakini akasita.
'Mama usimwamini kila mtu, ndio ni madocta,lakini ....'akasema binti akitilia shaka, na baba akamkatiza na kusema;
‘Ndio hivyo,… lakini kwa namna yao wanataka kujua chanzo cha tatizo,
wapi tatizo lilianzia,..unaona kama ni hivyo ina maana wanaturudisha kule
kwenye majonzi,..sizani kama hilo litakufanya ubadili nia, au sio…’akasema na
hapo mkewe akabakia kimia.
‘Na wamesema wanahitajia kumuhoji mtu mmoja mmoja, maana tukiongea
kwa pamoja inawezekana kwasababu fulani mtu akaogopa kuzungumza jambo,..anataka
kila mtu awe na uhuru wa kuongea kila kitu, hata kile cha sirini moyoni
mwake,.. sasa walitaka kuongea na wewe peke yako na binti peke yake..mnaonaje…’akasema
baba.
‘Sawa, kama imekuwa ni mambo ya kipolisi tena…, sawa, ila naombeni,
hatutaki kurejesha msiba hapa nyumbani, ulishapita, sasa…kwanini tena, sipendi,
ila kama itasaidia kumpata huyo aliyesababisha binti yetu akajiua hewala,
..itakuwa vyema ili haki iweze kutendeka..’akasema mama.
‘Je akipatikana ulitaka afanyweje..?’ akauliza binti yake.
‘Najua mwenyewe, hata kufungwa afungwe tu, hata kunyongwa, anyongwe
tu, na sizani kama hiyo itatosha, na sijui kama nitaweza kumsamehe…’akasema
mama.
‘Mama jamani, kama atapewa adhabu zote hizo, bado humsamehi,…mwenyewe
umesema tujifunze kusamahe, sasa mbona umesema kinyume chake..?’ akauliza binti
yake.
‘Sijui, kwakweli mimi sijui, kwanza ni apatikane, najua haya ni
maneno tuu, kama ilivyokuwa kwa polisi, ….sasa jamani karibuni, mlitaka muanze kuongea
na nani, na mimi au binti, maana binti alikuwa nahamu sana ya kuongea na nyie,
hususani …msaidizi, sijui kwanini, …’akasema mama akicheka kwa utani.
‘Mamaah…, sijasema hivyo, nilitaka kujua tu, kama ni yeye au la,
nahisi nimeshamuona mahali, …’akasema, na kabla mama hajasema neno, baba
akasimama na kumshika mkewe mkono huku akisema;
‘Sawa, sisi tunakwenda jikoni, leo nataka kumsaidia mke wangu kupika,
sasa sijui mtaongea hapa au mnahitajia sehemu ya faradha zaidi, huko chumbani
kwake, kuna nafsi kubwa tu, mnaweza kwenda kuongea huko…sisi, hatutasikiliza
mazungumo yenu…ila kwa mke wangu, mmh, mtaongea hapa hapa, ….’akasema baba na
kumshika mkono mkewe wakaondoka..
‘Babaaah..’akasema binti yake akiwaangalia kwa makini huku tabasamu
likiwa tel mdomoni lakini alipohisi yupo na wageni, akabadilika, uso ukawa
hauna raha…
*************
‘Mimi nimeshakuona mahali, huwezi kunidanganya tena…’akasema binti
akiniangalia mimi usoni moja kwa moja.
‘Yawezekana maana kama nilivyomuambia mama, kuna kipindi nilipatwa
na matatizo, nikawa kama nimechanganyikiwa, ilianzia kwenye ajali ya gari,
…baada ya hapo kumbukumbu zikawa mbovu, unajua tena,..kiukweli nimapata shida
sana namshukuru huyu dakitari amefanya kazi ya ziada…’nikasema.
‘Kwahiyo mambo ya nyuma huyakumbuki..kama ulikuwa na rafiki,
ukamufanyia mabaya, kama ulikuwa na mke, au mtoto…hukumbuki..?’ akauliza.
‘Baadhi , ni kama akitokea mtu aliyenifahamu akanisimulia, tulikuwa
hivi na vile basi inafikia sehemu nakumbuka kidogo kidogo…, ndio maana ya
safari yetu hadi tukafika huku, sikutegemea kuwa tungefika huku,..sijui, kama
unavyosema uliwahi kuniona, labda unikumbushe…’nikasema.
‘Wewe hukuwahi kuwa na mchumba..?’ akaniuliza akiniangalia lakini
alipogundua kuwa docta yupo anatusikiliza,akawa kama katahayari fulani hivi,
mimi nikasema;
‘Mchumba,..hahaha, hapana,… labda wewe ulikuwa mchumba wangu,
unikumbushe, nahisi kama hivyo, lakini sina uhakika, unajua kumbukumbu bado…wewe
ulikuwa mcumba wangu au..?’ nikauliza.
‘Hapana sio mimi, mimi sio mchumba wako, mimi sina mchumba,…na wala
sijawahi kuwa na urafiki na wewe, na sikujui,..lakini nahisi nilishakuona ,
ndio maana ninakuuliza wewe hujawahi kuwa na mchumba ukamuacha, kwani hivi sasa
una mke..?’akauliza maswali hayo kwa pamoja.
‘Sijui labda,…lakini nina uhakika sina mke,… ila la kuwahi kuwa na
mchumba yawezekana, sijui...hebu nifafanulie vyema..labda nina machumba mahali,
unamfahamu nisaidie, nionane naye kama sio wewe…’nikasema na yeye akatulia
kidogo, na hapo docta akaingilia kati na kusema;
‘Binti, uniamini,najua nyote kumbukumbu zenu hazipo sawa, sasa
nataka tupambane na hizo hali, ili wote muweze kukumbuka vyema, hayo tutakuja
kuyaongea baadae…’akasema
‘Docta, lakini mimi nipo ok, kumbukumbu zangu zimesharudi, labda
huyu…’akasema.
‘Sawa kama wewe kumbukumbu zipo safi, basi nataka nikuulize mambo,
kuhusiana na mambo yaliyopita, si utakuwa unayakumbuka yote..?’ akauliza docta.
‘Nazani, ndio nitakuwa nakumbuka, nipo safi docta…’akasema.
‘Safi kabisa,… mimi ni docta wako, kuna mambo nataka kukuuliza,
hasa yanayohusiana na dada yako ni muhimu sana kwako,..na kwa familia yako kwa
ujumla…, kuna kitu nimegundua…nataka usipaniki…dada yako hakujiua mwenyewe,
nataka wewe unisaidie kwa hilo..’akasema.
‘Eti nini, docta,…unapingana na polisi,…kwanini, wakati inaonekana
wazi, unataka kumficha huyo mbaya wetu au sio, nahisi nyie lenu moja….’akasema.
‘Tulia,…una maana huniamini tena,…kuwa mimi ni docta wenu…ina maana
hutaki kujua ukweli wa kifo cha dada yako…sema kama hutaki sawa, au kama hutaki
kuyareesha maisha yenu kama zamani, basi sisi tuondoke zetu…’akasema docta.
‘Haya unataka kuniuliza nini..nimekasirika, maana nahsi huyu mtu
anaweza kuwa ndio yeye, na huenda anajifanya tu…’akasema akinionyeshea kidole,
na mimi nikaonyesha uso wa kushangaa.
‘Kifo cha dada yako, kilipangiliwa, …lakini haikujulikana lini
kitakamilika, lakini yaonekana walivyotaka wao ndivyo ilivyokuwa…maana hata
wewe, familia yenu, wote mumekubaliana na hiyo dhana kuwa dada yenu alijiua…kweli
si kweli?’ akauliza docta.
‘Ni kweli, kwani uwongo…lakini ungelimuuliza baba na mama, kama
huniamini mimi…’akasema sasa kwa hamaki.
‘Siku kabla ya tukio hilo mlikuwa wapi..wewe na dada yako, twende
taratibu usiwe na wasiwasi, nina yetu ni kuwasaidia, hatuna jipya, hatuna jambo
la kukukwanza wewe, au una wasiwasi gani…?’ akaulizwa.
‘Nakumbuka siku ile, tulitoka kidogo,..si ndio unataka kujua hivyo,
au,,,?’ akauliza binti.
‘Mlitoka, mlikwenda wapi wewe na dada yako,…?’ akuliza docta.
‘Sokoni,…na tukapitia dukani, na pia dada alipanga kupitia sehemu,
..’akasema.
‘Alikuambia anataka kupitia wapi, useme ukweli usinifiche, niamini
, usiwe na shaka ,maana ukweli wote utasaidia mambo mengi sana….maana kuna
tatizo limejificha hapo…’akasema.
‘Alisema anakwenda kumpa taarifa mchumba wake, anahisi kapoteza
siku zake, kwahiyo huenda ana mimba, kwahiyo anataka waongozane akapime, wakiwa
pamoja, mimi sikuamini maana dada hakuwa na tabia na wanaume…mmh,
sikuamini..’akasema.
‘Kwahiyo akaenda kuonana na huyo mtu, ..wakati huo wewe ulikuwa
wapi, alikuacha wapi..?’ akauliza.
‘Kwenye duka moja la ..soda, nikawa nakunywa soda pole pole
kupoteza muda nikiwa naangalia runinga iliyokuwemo humo dukani...’akasema.
‘Wakati upo hapo unakunywa soda kuna mtu yoyote alikuja kukuona,
mkaongea, akakuuliza hiki na kile..?’akaulizwa.
‘Mhh..ndio alikuja jamaa mmoja, msumbufu sana yule..anapenda
kutufuatilia fuatilia, sijui alijuaje tupo hapo, aliegesha gari lake,
akanifuata pale nilipokuwa nimekaa akaanza kuniongelesha, sikupenda, spendi
kukaa hivyo na wanaume,…’akasema.
‘Alikuongelesha nini..?’ akaulizwa.
‘Yeye alizidi kunisisitiza kuwa anampenda sana dada yangu na
anataka kumuoa, ananitaka mimi nimsaidie kumshawishi dada,…, lakini kiukweli, dada
alikuwa hampendi,na huyu mtu alishawahi kuleta posa kwa wazazi, lakini dada
kama ajilikanavyo, aliikataa, mimi sikujua kwanini awali, lakini baadae
aliniambia kuwa anye mtu keshampenda, hakutaka kuniambia ni nani, alisema mpaka
siku muafaka..’akasema.
‘Je akaja kukuambia ni nani..?’ akaulizwa.
‘Ndio, ipo siku moja alinitambulisha, lakini ilikuwa haraka haraka,
maana mama alikuwa anakuja kutuchukua, na kweli ..mama alikuja kutufuma
tukiongea na huyo jamaa, na jamaa akaondoka kwa haraka…’akasema.
‘Kwahiyo wewe ukawa umemtambua huyo mtu, kwa sura nk…?’ akaulizwa.
‘Ndio..ndio maana,..n….’akataka kusema kitu na docta akamkatisha
kwa kuuliza swali jingine.
‘Huyo mtu aliyekuja wakati ukinywa soda ni nani,…?’ akaulizwa.
‘Ni lazima nimtaje..?’ akauliza.
‘Ndio ni muhimu sana…’akasema.
‘Ni …aah, anadai kuwa yeye ni ndugu yake na yule mpangaji,..anayelinda
nyumba yetu, lakini simuamini, nahsi alisema hivyo ili awe anapata muda wa
kufika nyumbani, na kuongea na dada, lakini dada hakukubali kabisa kuongea naye….’akasema.
‘Kwahiyo mara kwa mara alikuwa akifika nyumbani..?’ akaulizwa.
‘Ndio hasa wakati wazazi hawapo, sijui alikuwa anajuaje,…’akasema
‘Yeye anaishi wapi…?’ akaulizwa
‘Yeye ana makazi yake huko Mbezi, ana uwezo fulani hivi…’akasema
‘Ok, ana kazi gani, anajishughulisha na kazi gani..?’ akauliza.
‘Yeye …anadai alishawahi kwenda nje na kuishi huko kwa muda, baadae
ndio akarudi hapa nchini, na aliporudi hapa nchini, akawa kaajiriwa hapa na
pale, akaja kufungua studio,…anatengeza matangazo..ni mbunifu wa
matangazo,,anavyodai yey, ila kwa sasa hivi ana duka kubwa sana, kama super
market….kiukweli ana uwezo, ila hajaoa, alitaka kumuoa dada…, sijui kwasasa,
labda kama keshaoa, mimi sijui taarifa zake zaidi…’akasema.
‘Kiukweli unavyoona, je alikuwa akimtaka dada yako au likuwa
akikutaka wewe?’ akaulizwa
‘Yeye alimtaka dada…si ndio mpaka akaleta posa…’akasema.
‘Ndio alimtaka dada, lakini wewe alikuwa hakuoni mara kwa mara ana
alipokuona wewe akawa kama kakupenda wewe zaidi, kweli si kweli..?’ akaulizwa.
‘Hahaha..sina habari na yeye kabisa, wala simpendi, ..sipendagi
wanaume, yeye ananisumbua tu kuwa,…kama dada hamtaki, basi anioe mimi,…nilimkatalai
kabisa nahisi kuna kitu ambacho sio cha kawaida kwake…’akasema.
‘Kwanini…unahisi nini?’ nikamuuliza mimi.
‘Muongeaji sana, halafu, kama ni tapeli fulani hivi, anajua sana
mambo ya nje, wengine wanahisi anauza unga, madawa ya kulevya, wengine…mmh,
wanasema huenda ni…ni..’sema tu.
‘Ni friimasoni, ..kitu kama hicho…’akasema.
‘Nini, ..ni nani alikuambia hayo..?’ nikamuuliza sasa nikihisi
hatari, maana hao watu nimesikia sifa zao, na sitaki kuwafuatilia zaidi.
‘Watu wanasema tu mimi sijui, unajua siku hizi mtu akiibuka na
mali,..akatajirika kwa muda mfupi, basi
watu husema mengi, hukimbilia kusema huyo mtu ni friimason..sasa sijui, ..ila
watu wanasema hivyo..’akasema
‘Kwahiyo baada ya hapo dada yako akarudi, aliporudi ilikuwaje..?’
akauliza
‘Alikuwa analia tu…, hakutaka hata kusema, au kuongea chochote,
mimi namfahamu sana dada yangu akiwa kwenye hali kama hiyo, inatakiwa umpe
muda, basi tukaondoka naye,…tukiwa njiani ndio tukakumbuka kuwa alikuwa na
mpango wa kununua dawa, tangia awali tulikuwa na mpango huo, kwani alikuwa
anajisikia vibaya , ..basi tukapitia duka la dawa akanunua hizo dawa..’akasema
‘Unakumbuka ni dawa gani alinunua,…?’ akauliza docta
‘Ni dawa za maumivu tu, maana alikuwa hajapima kuwa ana tatizo gani,
na hata yeye alihisi ni mauchomvu tu, kichwa kinamuuma, basi, ndio hivyo…?’
akauliza
‘Una uhakika alinunua dawa
hizo..?’ akaulizwa
‘Kwanini unaniuliza hivyo, ndio…wakati ananunua nilikuwepo,
aliagiza dawa za maumivu, na akapewa,….nakumbuka kabisa hilo.., hata leo,
nimeziona kwenye kabati, nilishangaa kuziona, kumbe polisi niliwapa
zingine,..kulikuwa na kipaketi kingine cha dawa za maumivu, sijui kwanini
hatukuziona mapema, tukakimbilia kununua nyingine..’akasema
‘Zipo wapi hizo dawa, , ..’akasema
‘Kwenye kabati lake…’akasema
‘Kwahiyo polisi waliulizia dawa gani, ukasema ni za maumivu,
wakazichukua kwa ajili ya uchunguzi, au sio..?’ akauliza
‘Ndio…lakini nimegundua kuwa sio zenyewe walizochukua, nilikuja
kugundua kuwa nilichowapa sio chenyewe, lakini zote zimeandikiwa jina hilo
hilo..dawa ya maumivu…’akasema.
‘Hebu twende ukanionyeshe..’akasema na docta wakaingia ndani ,
kwenye chumba caha mabinti, maana walikuwa wakichangia chumba, mimi nikabakia
peke yangu hapo kwenye chumba cha maongezi, haikupita muda mara mlango
ukagongwa…nikajiuliza nifanyeje , maana wenyeji hawapo, kabla sijasema kitu
mara mlango ukafunguliwa.
Jamaa alikuwa kasimama mlangoni, akiwa na macho yaliyovimba,
utafikiri hajalala, uso ulikuwa umekunjamana, kama ana hasira fulani, macho
yamemtoka, aliponiona tu akasogea kunijia, lakini akasimama …akageuka huku na
kule kama anahakikisha jambo, halafu akasema;.
‘Oh,… nyie mlifanya nini kule…?’ akauliza
‘Wapi mbona sikuelewi…’nikasema.
‘Nyie....mliingia ndani na kuniharibia mambo yangu, hivi ni tabia
gani hiyo, mnaingie kwenye majumba ya watu, na kuanza kuharibu …na kuiba,…
mnajua nilikuwa nafanya nini pale, mumeharibu kila kitu, mumeni..weka pabaya,…sasa
halafu kwanini mumechukua dhamana yangu..’akatikisa kichwa kama kuhisi kitu,
akahema kwa nguvu, alikuwa hayupo sawa kwa ujumla.
‘Dhamana yako, ndio nini,….na hakuna aliyeingia nyumbani kwako,
kwani wewe unaishi wapi, mbona sikuelewi…’nikasema.
‘Ooh,..nyie watu nyie watu….kwanini… nipeni haraka,
mnanitesa,..hiyo..sio mali yenu kwanza naweza kuwaitia polisi kuwa mumeingia
kwenye nyumba na kuiba, …’akasema sasa akinikodolea macho.
‘Itakuwa vizuri ili polisi wajue unachokifanya..’nikajisemea tu
hivyo na kweli niliona imefanya kazi.
‘Kitu gani nimefanya, nimefanya nini, nipeni ..kwani mwenzako yupo
wapi, halafu, …wewe bwana mdogo usiinichezee unanijua mimi ni nani..?...,
unajua naweza kukuharibu ,…kwanza bahati yako..’akasema.
‘Bahati yangu nini..ulitaka kuniua sio kama ulivyomuua, …’kabla
sijamaliza, mara docta akarudi na yule binti, jamaa huyu alipomuona docta, na
huyo binti, akanywea, akajifanya mpole, akawa anajitahidi kuficha ile hali
aliyo nayo, mara akaanza kutikisika, halafu akasema maneno hayaeleweki, na
kumalizia hivi…
‘Vuuuuuuuh, haya haya…nipeni habari, mnataka nini, sio mimi jamani,
…’akasema akawa anatikisa kichwa, huku anaitikie, ‘Taire..taire..taire…’ halafu
akasema;
‘Sio mimi wahenga, sio mimi, nilitaka kukamilisha kazi, watu
wakaniingilia, wakaharibu, sijui ….nimewaona, …lakini sijakipata….’akatulia,
huku anaitikia ‘taire, taire..taire, ..’ halafu akasema;
‘Hapana wahenga sio mimi, sijaharibu,…nilikuwa mbioni kukamilisha,….na,
niwapeleke wale watu, lakini kabla, ndio,…oh,… nisaidieni,…’akatulia, na mara
akawa kama anahisi maumivu, anajinyonga nyonga, na kulia kama mtu anayeteswa,
baadae akasema…
‘Wahenga jamani nisaidieni jamani, sio mimi sio mimi…nitaongea na
hao watu, nitaambia, hapana msiniue,..’ ghafla akalalala akadondoka, sakafuni…
Sisi pale tukabakia tumetulia tu, baadae akina mama na baba
wakafika, huku wanauliza;
‘Kuna nini mbona tumesikia kelele, za mtu kama ana….omba msaada,
kuna nini, tulijua mambo yameharibika..’akasema baba, na mara wakamuona huyo
jamaa kalala sakafuni, ..
‘Vipi tena huyu mtu karudi mbona kalala hapo, ana nini..?’ akauliza
mzee
‘Hata hatujui kaja,...maana kaingia na kuanza kupandisha , anaomba sijui wahenga wake
wamsaidie….na ghafla huyo kadondoka chini…hatuelewi ana nini…’akasema docta.
‘Mhh…sasa hili si balaa kweli, hivi, akitufia humu ndani itakuwaje..’akasema
mama
‘Atazindukana tu, msiwe na wasiwasi..mimi niliwaambia huyu mtu atakuja,
kuna kitu chake muhimu anakitafuta, ndio mambo yao wanayopewa huko, sasa sijui
ni cha mababu zake au kuna watu wamempa,….’akasema docta.
‘Kitu gani mnacho nyie….?’ Akauliza mzee.
‘Ndio tunacho…tulikichukua, yeye anajua umuhimu wake, sasa ndio huyu keshakuja…atazungumza yote..yaonekana
huyu mtu ana mambo makubwa sana, ambayo yanaweza kuhusiana na matatizo
mnayoyapata,...na huyu ndiye atakuwa njia yetu, …’akasema docta.
Na mara simu ya huyo jamaa ikawa inaita…ilikuwa mkononi mwake..,
docta akasogea pale kwenye hiyo simu na kuichukua, kwanza akawa anasita
kuipokea, baadae, akasema, kuniuliza mimi…
‘Simu yako si inaweza kurekodi,…nataka urekodi sauti ya huyu jamaa
akiongea, sina uhakika ni nani
anampigia, hapa imeandika jina moja tu, ‘mkuu’ haya naiweka hewni weka chambo cha
kurekodia
‘Docta akaiweka hewani, na mara sauti ikasikika ikisema;
‘Sasa umefanya nini..mbona hajaonekana huku, na…umefanya nini mbona
umeharibu, hatukuoni huku,…upo gizani,…na ile kazi imeishia wapi,…unakumbuka…ni
lazima ikamilike kabla ya siku tano , zimebakia siku mbili, vinginevyo, utageukiwa
wewe mwenyewe..unasikia, mbona hujibu kitu…wewe…sema …shhht...’mara akakata simu.
Tukabaki tumeangaliana, na docta akasema,…
‘Mkuu…huyu mtuni nani,…sasa chukua hii namba yake uweke kwako
ufanye kama unamtumia pesa, itataja jina lake…’akasema docta, na mimi nikafanya
hivyo, na mara jina likatokea…
NB: Kuna nini hapa, kumbuka haya yote yalianzia kwenye facebook,
nikampata rafiki, rafiki ndiye kanivuta hadi nimefika hapa, je ni bahati mbaya,
au kuna nini zaidi..tuzidi kuwemo
WAZO LA
LEO: Kutokana
na shida, hali za maisha kuwa ngumu, watu wengine hutegeka na kujiingiza kwenye
mambo wasiyoyafahamu ilimradi tu wapate kipato. Shida na nakama za maisha
sinawafanya watu wanakosa subira, wanaacha maamurisho ya mungu , ya kutenda
mema, na badala yake wanakuwa tayari kutenda maovu, mambo ya kishetani, ..lengo likiwa ni utajiri, hivi ni kweli shetani anaweza
kukupatia utajiri hivi hivi…tuweni makini, tusidanganyike,…Tumuombe mungu
atulinde na kutuongoza kwenye njia sahihi,…Aaamin.
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment