Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Thursday, July 1, 2010

Mwenye shibe hamjui mwenye njaa

‘Hii inashangaza sana hivi kweli kwenye karne hii kuna watoto wanasoma bila viatu, wanatembea pekupeku toka makwao hadi shuleni!’ nilishangaa kumsikia mama mmoja akiwa ndani ya gari lake akiongea na mwenzake ambaye alikuwa amesimama nje ya gari hilo akisubiri daladala.


Kwa jinsi nilivyomuona nilijua kuwa watoto wake wanasoma mashule ya pesa nyingi, kwani watoto wake nyuma walikuwa wameshika simu wakiwapigia rafiki zao. Niliguna na kutafakari kuwa huyu huenda hajawahi kuishi kijiini, au hata kama aliwahi kuishi hajawahi kuishi maisha ya taabu, na kama aliwahi basin ni limbukeni wa mawazo wa kusahau ulipotoka.

‘Hilo sio la kushangaza kwasababu wote hatupo sawa, we huoni mimi nasubiri daladala wewe una gari’ akamjibu mwenzake kwa mzaha.

‘Hapana huweze ukalinganisha tukio lile la watoto karibu wote wanasoma bila viatu na hili la maisha yetu, kwani hivi ni vitu vya kifahari, lakini yapo mambo ya lazima kwa kila mtu hasa mzazi kwa mtoto wake. Hawo wazazi ndio ambao hawawajali watoto wao, hawawalishi vyema na kudai wanapenda kula kwa majirani au kuwa ombaomba…’ wakawa wanaendelea na mazungumzo yao ambayo yalinifanya nikumbuke usemi mmoja unaosema `Aliyeshiba haijui njaa ilivyo.



Haya ndio mazungumzo yetu hasa tukio linapotokea, nan kawaida yetu ni kuwa wepesi kutoa makosa bila kutafiti chanzo cha tukio. Tukumbuke kuwa kila tukio lina chanzo , na hili hatutaki kulifanyia kazi. Kwanini , ni nyepesi kuitamka, na huenda kwasababu gani ikachukuliwa kijuujuu ili kurahisisha mambo. Hili ndio kosa kubwa la kutokujali ukweli halisi. Ukweli halisi ni `umasikini’ . Ndio utasema umesabibishwa na ujinga, ambao umetokana labda na kutokujali elimu. Lakini hebu tuangalie jinsi gani mtu kama Yule atajielimisha haraka na kuuondoa ule umasikini ili mwanae apate ada, apate unadhifu nk. Mwenye kushiba ni rahisi kwake, lakini ndani ya kichwa cha wazai wengi kunawaka moto hasa ipindi hiki wakiwa likizo!

Tumshukuru sana Yule Mkenya, ambaye hakutaka kujadili kwanini, Yule alikimbilia vitendo, hana muda wa maneno mengi kwani hali halisi anaijua, akatoa kile alichojaliwa nacho. Sasa sisi wenye nyumba hatuoni aibu…sidhani kama hulka hiyo tunayo…sidhani kwani inakuhusu nini wakati watoto wako wapo nyumba ndani gari wanapiga simu kwa marafiki zao. Umeshiba, huwezi kuijua njaa ilivyo!

Halihalisi ya vijiji vyetu ndivyo ilivyo, kama hawo waandishi wangeamua kuzunguka sehemu mbalimbali wangegundua mengi zaidi ya hayo, kuna shule hazina madawati, kuna shule hazina walimu, kuna shule mtoto anatoka nyumbani haijui chai au uji wa chumvi…yapo mengi, na yote hayo ni umasikini wetu. Na ili ujue hilo hebu kadiria jinsi gani ya kuishi kwa dola moja kwa siku…


Wakati natafakari hili nilikumbuka bosi mmoja ambaye alikuwa na tabia ya kuwasimanaga wafanyakazi wake kuwa hawavai vizuri…huyu bosi hana tofauti na Yule mzazi anayemsema mwanae kuwa hapendi kula nyumbani kwake, kwasababu kutokuvaa vizuri ni kutokana na kipato. Huyu bosi anahitimisha hisia zake bila kujali hali halisi na kipato anachomlipa mfanyakazi wake, na nini anachomfundisha mfanyakazi wake kama sio kumshawishi aibe, na atamwibia nani kama sio yeye mwenyewe! Ama kweli mwenye shibe hamjui mwenye njaa.

From miram3

3 comments :

Anonymous said...

Duu tumetoka mbali sana, mimi nakumbuka wakati nasoma nilikuwa nikienda shule pekupeku...viatu vilikuwa kwa ajili ya sikukuu au sherehe, au nikienda mjini kumtembelea baba!
Kwa hali ya sasa ni ajabu mtoto kusoma bila viatu, lakini kwa Tanzania mbona bado hiyo imo saana, tatizo nyie mumelamaa mjini, tembeleeni vijijini muone, kuna zaidi ya hilo...mtu anashindia uji wa chumvi...acheni kusema, acheni kabisa kumkufuru mungu. Wewe unakula mlo wa `self-service, hapa kidogo, nyama, paja, mchicha...mmmh, mwishowe unamwaga,masikini anaenda kuokota anakula...mnajua ndio maana laana inatuandama, kwanini usipike kiasi kinakutosha kingine wape wasio na uwezo...
Hongera sana mwenye blog hii, sijui unaitwa nani mwenzetu. Naujua wewe ni mwenzetu kihalihalisia

Anonymous said...

Mimi bwana viatu nimevaa wakati naenda sekondari. Shuleni sana sana nilikuwa nikivaa `makatambuga' unavifahamu vile viatu vya matairi ya gari...basi hivyo, safi kabisa, miba haioani ndani!
Nilikuwa nikisafiri maili nyingi kuipata shule, na bado nilikuwa nikiwahi namba. Siku hizi mtoto bila daladala haendi, nazungumzia sie walalahoi.
Huyo mwandishi amewakilisha sehemu ndogo ya matatizo ya viijini hasa shule,

Anonymous said...

Msilinganishe ya nyuma na ya mbele, tunataka maendeleao na maendeleo ni kutizama mbele, wewe ulikuwa huli kwa kijiko sasa unakula kwa kijiko, wewe ulikuwa hupandi gari sasa...ndio maendeleo, tusitake kuwatesa watoto wetu eti kwasababu wewe ulikuwa hivyo, hiyo ilikuwa karne yako, sasa karne hii ni ya sayansi ta teke linalokujia. Usipoangalia litakubwaga chini, shaurilo