Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Tuesday, December 12, 2017

MKUKI KWA NGURUWE-39


‘Nahisi labda rafiki yangu yupo matatani, au hata kama hayupo matatani lakini naweza kukutana naye akaniambia ukweli kuhusu hiyo DNA, Je matokeo yanasemaje..nitamuomba sana..ili nafsi yangu itulia…hata kama…

‘Na ni lazima nifanye lolote,kuonyesha utu, hata kama mtu kakufanyia ubaya, lakini keshaniambia yupo matatani, hayo mawazo yaliuteka ubongo wangu na sikuwa na sababu nyingine ya kuacha kwenda huko uwanja wa ndege....

Endelea na kisa chetu.....

********

Usiku una mitihani yake, japokuwa nilikuwa na nia ya kumsaidia rafiki yangu, lakini moyoni, nilikuwa na mashaka ya usalama wangu, kiukweli mimi sio mtu wa kuogopa ovyo, lakini wakati mwingine unahitajika kuwa na tahadhari, kwani huwezi kujua wenzetu wamejiandaa vipi, ....

Wakati mwingine nikafika kujilaumu, kwanini sikumsikiliza docta, rafiki wa mume wangu pale aliponisihi nisije nikaenda huko uwanja wa ndege, nahisi kuna kitu wameona ambacho sio kizuri, kuna hatari, lakini hatari gani.Japokuwa sikutaka kumwambia naenda wapi, lakini ingelikuwa vyema akajua,...

Nakufahamu sana unataka kwenda huko uwanja wa ndege, ...usije ukafanya hayo makosa, mimi kama mtu ninayekujali, nakukataza kabisa usiende huko....’akasema.

Kawaida yangu na huyu mtu, tunakutana, inakuwa hivyo, huwa hatukubaliani kirahisi, yeye ananifahamu hivyo, na mimi namfahamu sana tabia yake, mimi na yeye ni kama mafahali wawili, ...na sikupenda anione mimi sijui ni nini ninchokifanya hata hivyo, nilishamfahamu kuwa mengine anayafanya ili nimuone kuwa ananijali, au anafanya kuwarizisha wazazi wangu..sikupenda kufanyiwa hivyo.

‘Hivi kwanini rafiki yangu alipofanyiwa hivyo, hakuwapigia simu polis, lakini yeye ni mpiganaji anafahamu lipi jema, siwezi kumlaumu hasa inapofikia kwenye familia yako…’nikasema kimoyo
‘Hao watu sio mchezo, ikibidi kufanya unyama wanafanya, wakijua wana watu wa kuwalinda, kwahiyo uwe makini sana nao…’hiyo ilikuwa moja ya kauli za docta akinitahadharisha.

‘Mimi sijaona uhatari wao…’nikasema na nilisema hivyo, kutokana na kauli ya docta, yeye kaona kuwa watu hao wanafanya hivyo huenda kwa vile wana watu ambao wanaweza kucheza na vifungu vya sheria na kufanya wapendavyo, na pia labda ni kwa vile wana mtu mkubwa wanayemtegemea..’nilijikuta naongea peke yangu kwenye gari.

Safari ya kwenda uwanja wa ndege inaweza ikakufanya hivyo, ukaongea peke yako, ukawaza mengi, na kama huna mtu, utawaza na kuwazua peke yako, na vinginevyo, ukutane na madereva wa daladala, mtukanane,…yaani ukifika sehemu unayokwenda, kama umefika salama ushukuru mungu, ni mtihani kwa kweli.

‘Je kama nikutana na hao watu , na wana silaha, nitawezaje kujihami, kama sina silaha..’nikajiuliza, hivi kwanini sikuchukua bastola yangu kwa ajili ya kujihami, ili wakinitishia na silaha na mimi nawaonyesha kuwa nina silaha na pia naweza kuitumia…oh, sasa nifanye nini, nirudi, hapana siwezi kuwahi, …hapana, siwezi kurudi…’ nikawa naongea huku gari linakwenda
.
Niliona kuwa kama nitakwenda nyumbani kuifuata hiyo silaha yangu, nitakuwa nimechelewa sana. Haitakuwa na maana tena, …

‘Hamna shida ngoja niende huko huko, sio lazima nipambane nao kwa silaha, hata hivyo sizani kama kutakuwa na haja ya kutumia silaha, ikibidi, nitatafuta njia nyingine...pale kuna kituo cha jeshi, nitafanya lolote wajue kuwa nipo kwenye hatari, ila tatizo ni usiku…hata sijui, mungu nisaidie tu....’nikasema

Nilipokaribia uwanja wa ndege, nikampiga simu ya rafiki yangu, tena na tena lakini simu yake ilikuwa haipatikani.

 Labda atakuwa keshaingia uwanja wa ndege, au …labda watu hao bado wamemshikilia,..lakini kwanini waendelee kumshikilia, kuna ni nini hajawatimizia,…mmh,  ngoja niwapigie watu wangu kujua kinachoendelea..’nikasema na kuwapigia watu wangu.

‘Hatujampata mpaka sasa hivi, hata uwanja wa ndege hayupo, hajaingia kabisa …’wakasema

‘Muna uhakia, basi Ina maana labda bado wamemshikilia sehemu..?’ nikauliza

‘Yawezekana, maana kwa mara ya mwisho kuna kitu walikuwa hawajaelewana, kukatokea kitu kama vurugu, baada ya hapo mdada akatoweka, na wale watu aliokuwa nao, wakawa wanamtafuta…hadi sasa huyo mdada hajaonekana yeye au mtoto wake, na wale watu bado wanamtafuta…’wakasema

‘Basi yupo kwenye wakati mgumu angalau angelinipigia, nikajua nimsaidie vipi au ndio keshanizarau……sijui nitampataje sasa..’nikasema

‘Madam, tuachie hilo, tutampata tu…’watu wangu wakasema na mimi hadi hapo nilikuwa sijawajulisha kuwa nipo njiani nakuja huko huko, nilitaka hilo lisijulikane mpaka nifike maeneo ya hapo.

 ‘Mtoto wangu aliibiwa…, wakati nipo bafuni naoga, walifika watu nisiowafahamu, wakamchukua mtoto wangu..nilichanganyikiwa…,lakini baadaye wakanipigia simu, kuwa kama namtaka mtoto wangu, akiwa hai basi nifanye wanavyotaka wao, nikawaulize nifanye nini...’

Nilikuwa najaribu kuyakariri maneno yake kuona kama kuna uwalakini wa udanganyifu, lakini niliona huenda ni kweli…..

*********
Nilishafika maeneo ya uwanja wa ndege sasa, nikawa najiuliza niingie ndani moja kwa moja au…nikaona niwapigia watu wangu tena kuhakiki bado wakaendelea kusema kuwa hawajamuona,  hajaonekan ndani ya uwanja wa ndege, na muda wa watu kuingia kwa ajili ya ndege anayoondoka nayo umeshafika..na bado haonekani.

‘Inawezekana kaahirisha safari yake…?’ nikauliza

‘Hapana, tumelichunguza hilo, hajaahirisha bado…’wakasema

Nikawa sasa nimefika sehemu niamua kuingia ndani ya uwanja wa ndege au …kwa mbele nikaliona lile jengo nililoambiwa kuwa Makabrasha ana ofisi zake humo ndani,..kumbe unaweza kuliona bila kupata shida.

 Baada ya kuliona hilo jengo tu, akili yangu ikanituma nifike kwanza kwenye HILO jengo, kwani huko ndani ya uwanja wa ndege wapo watu wangu wanafuatilia, aanglionekana kama alikuwa keshaingia huko, basi bado atakuwa kashikiliwa sehemu na sehemu ninayoishuku mimi ni kwenye hilo jengo.

‘Au watakuwa sehemu gani nyingine…hawa watu wangu kama wamemtafuta kila mahali hajapatikana, basi…hapana ngoja nikahakikishe mwenyewe..’nikasema

Nikawa sasa nimefika eneo la hilo jengo, ni jengo kubwa la ghorofa tatu…na ukiliangalia kwa mbali ni kama halijamalizika kujengwa, lakini nilipofika sehemu yenyewe nilikuta shughuli zinaendelea kama kawaida,

 Sehemu kubwa ya chini imechukuliwa na waendesha biashara za vinywaji, kwahiyo kwa wakati huo watu walikuwa wamekaa kwenye viti vilivyopangwa kwenye miti iliyopandwa kwenye bustani ya eno hilo, wakinywa, na mziki ulikuwa ukipigwa....

Mimi nilipoingia eneo hilo na gari langu, wakaja wapokezi, wakinikaribisha kwa bashasha, huku wakinielekeza sehemu ya kuegesha gari langu, nami nikafanya hivyo, na kutoka nje ya gari, na wale wahudumu, wakaendelea kuonyesha ukarimu wao, inaonekana walisomea hiyo kazi, kwani walijua jinsi gani ya kumkaribisha mgeni, mpaka unavutiwa ..

‘Unakaribishwa mgeni, hapa kuna huduma mbalimbali, kuna vinywaji, kuna chakula, au kama unahitaji kumpumzika kuna sehemu ya kupumzika, vipo vyumba, na huduma nyingine ...’nikashangaa, maana sikujua kuwa jengo hilo lina mambo yote hayo. Kiukweli lilikuwa limekamilia kama jengo la ofisi, burdani na vyumba vya wageni.

‘Kwani hapa kuna vyumba vya ofisi na hata vyumba vya kulala wageni?’ nikauliza

‘Ndio vipo vingi tu, vyumba vya wageni vipo juu na chini, ni wewe tu, unahitaji chumba, kwa muda gani je upo peke yako?’ wakaniuliza.

‘Hapana sihitaji chumba, mimi nataka kumuona mtu fulani…sijui kama ninaweza kumpata humu mmh, sasa ni saa mmh…?’ nikauliza nikijifanya kujibaragua hivyo, kwani sikuwa na uhakika nisemeje, maana nilitakiwa niwe na tahadhari. Hizi kazi za watu, hizi zilimfaa rafiki yangu, sio mimi mtu wa ofisini.

‘Ni mtu gani huyo je ana ofisi hapa, au mteja wa mara kwa mara hapa, tunaweza kukusaidia kumpata…?’ akaniuliza

‘Ndio anaitwa Makabrasha...’nikasema

‘Oh,…kumbe ni muheshimiwa,…mhh, ulikuwa na ahadi naye..?’ akaniuliza

‘Ndio…’nikadanganya hivyo.

‘Basi itabidi uingie sehemu ya ndani, sehemu ya mapokezi, huko ndani watakuelekeza, sisi huku tunashughulika na wateja wan je, na ofisi za chini, karibu sana…’akasema

‘Ahsante,….’nikasema

‘Lakini naona ajabu, muda kama huu, mara nyingi, anakuwa huku chini,  anapenda sana kujichanganya na watu, sasa sijui kwanini hajateremka, na leo siku nzima sijamuona huwa ni rafiki yangu akija hapa lazima tuongee na kutaniana…’akasema

‘Oh kumbe, kwahiyo labda ana wageni, ni mwanamke na mtoto au…?’ nikauliza

‘Yeye kila mara ni mtu wa wageni..ofisini kwake kama huna miadi naye sio rahisi kumpata analindwa utafikiri muheshimiwa gani vile, sikumbuki kumuona huyo mtu mwanamke na mtoto, hata..labda maana sio muda wote ninakuwa hapa, mimi nimeingia jioni hii …’akasema

‘Ok…ngoja nikaonane naye tu nitajua huko mbele kwa mbele…’nikasema

‘Sawa…;lakini sio kawaida yake..kutokuonekana huku chini…, nahisi ana kazi nyingi....ingia ndani watakuelekeza ofisini kwake, karibu sana...’akasema huyo mpokeaji wageni.

‘Nashukuru hamna shida, na gari langu naweza kuacha hapa… , hapa kuna usalama....?’nikauliza

‘Aah , ndio hakuna shaka, ila kama unahitaji ulinzi binafsi inabidi ulipie pale, kwa yule mlinzi, vinginevyo, liache hapo hapo, ..’akaniambia

Na mimi kwa vile sikujua nitakaa huko ndani kwa muda gani, nikaona ni bora nipate hiyo huduma ya ulinzi binafsi, nikaenda kwa yule mlinzi, nikaandikisha, na kulipia. Baada ya hapo nikaingia ndani..

Sikutegemea sehemu ya ndani imejengwa kiofisi kweli, kuna sehemu nzuri za kusubiria wageni, runinga, na vyumba vya huduma za vinywaji…na kulikuwa na wahudumu kutegemeana na ofisi unayokwenda.

Haraka nikaenda kwa muhudumu nikamuelezea shida yangu, na nilipomtaja huyo Makabrasha, akanielekeza kwa askari mmoja…

‘Yule ndiye mtu wake…’akaniambia
 Nikamsogelea huyo askari,  alikuwa kakaa na mbele yake kuna meza, na kitabu kikubwa, alikuwa anasinzia, na aliponiona akasimama na kunikaribisha, nikamuelezea shida yangu.

‘Oh, kwa muda kama huu, mara nyingi huwa hataki wageni, ....lakini mmh, ngoja,  maana alisema hataki usumbufu, …alikuwa na wageni muhimu…mmh, sijawaona wakitoka,…eeh, ok,…unasema una miadi na yeye, jina lako,..maana natakiwa kumpigia simu kuhakiki...’akachukua simu yake na kupiga, ikawa inaita tu, akaniangalia, na kusema;

‘Unaona hataki hata kupokea simu, tafadhali hebu wewe nenda,….si umesema una miadi naye au sio…basi nenda, maana muda umekwenda, ukifika rosheni ya pili, upande wa kushito utaona ofisi yake, na maandishi ya ofisi yake sio sehemu yenye utata,…lakini samahani, natakiwa nikukague kama huna silaha yoyote ni kawaida usijali..’akasema akinipitishia mashine ya kukagua, na aliporizika akasema

‘Ok, sasa unaweza kwenda...’akasema hata bila ya kunipa muda wa kumuuliza nilichotaka kumuuliza, …

na mimi hapo nikawa huru, hata kama nitachukua muda mrefu huko ninapokwenda, kwani yaonyesha kuna utaratibu mnzuri wa usalama, kuanzia nje hadi ndani… 

Nikaelekea kwenye ngazi za kupanda, juu, ..jengo halikuwa na lifti…ni mwendo wa zoezi, sikujali hilo,  maana hata mimi ni mtu wa mazoezi.

Nilipoanza kupanda ngazi ya kwanza simu yangu ikaita, nikaangalia ni nani mpigaji, nikaona ni docta rafiki wa mume wangu, sikutaka kuipokea simu yake kwa muda huo, nikaikata, na kuanza safari ya kwenda juu, huku nikiwa na mawazo mengi mengi kichwani.

‘Hivi haya aliyoniambia docta rafiki wa mume wangu kuwa wakili huyu ni jasusi fulani inaweza kuwa ni kweli..na kwanini mume wangu akamchukua mtu kama huyu, nataka nikikutana naye nimuulize kuhusu huo mkataba na mume wangu, mimi kama mke wa mteja wake nina haki ya kufahamu hilo.

‘Hata hivyo muhimu wangu ni kuhakikisha kama rafiki yangu hayupo naye huko, …’nikasema huku nikiangalia saa, na kwa muda huo kama ni wasafiri wa kuondoka, watakuwa wameshaingia ndani, ..sijui kama huyu rafiki yangu ataweza kusafiri leo..au …yupo matatani.’nikawa naongea kimoyo moyo.

 Wakati natembea sasa kupandisha ngazi ya mwisho ili nifike eneo la ghrofa iliyopo hiyo ofisi …ya makabrasha, mara akatokea mtu akiwa na haraka, karibu anipige kikumbo kwa jinsi alivyokuwa na haraka, ni kama anakimbia, alikuwa kavaa kofia kubwa, kiasi kwamba huwezi kuona sura yake, mpaka, ainue kichwa kidogo.

Yule mtu aliponiona, kwanza aliinua kichwa ili aweze kuniangalia usoni, ni kama kashtuka kuniona na alitaka kuhakiki, akainua kichwa kuniangalia vyema…akataka kuongea jambo… akasita, kama anataka kuniongelesha, lakini akasita, na kunipita kwa haraka na kukimbilia chini, mimi sikumjali nikaendelea na safari yangu ya kwenda juu.

‘Huyu mtu ni nani, mbona anakuwa kama ana mashaka…’ nikajiuliza na hapo nikaanza kuingiwa na mimi na wasiwasi, kiujumla kulikuwa kumetulia maana muda huo ofisi nyingi zilikuwa zimefungwa.

‘Huyu wakili yaonekana sio mtu wa kawaida mpaka anaweka walinzi wa kukagua watu, lakini labda ni mlinzi wa ofisi zote za huku juu..na ofisi nyingi zimefungwa yeye bado yupo kazini…’nikasema

‘Ni lazima nikaongee naye, nitapambana naye uso kwa uso, atashangaaa kuniona muda kama huu..’nikasema kimoyo moyo. Na nilijipa matumaini kuwa hawezi kunifanya lolote, kwa jinsi walivyoweka taratibu zao, mtu anayeingia anajulikana na akitoka  halikadhalika

Hata hivyo kutokana na familia yangu watu wengi wakisikia kuwa mimi ni mtoto wa , basi kuna kuogopwa au kuheshimiwa kwa namna fulani, baba yangu alikuwa na umaarufu fulani hivi…kwahiyo sihitajiki kuwa na mashaka..hata hivyo moyo wa mashaka bado nilikuwa nao..

Sasa kiusalama nikaamua niwapigia watu wangu niwaambia kuwa nipo sehemu hizo wakaribia hapo kama lolote likitokea,..nilishangaa kuona simu yangu haina mawasilinai mtandao haushiki…, hii ni kuashiria kuwa eneo hilo, wameweka vitu vya kuzuia mawasiliano, sasa wao wakitaka kupiga simu nje inakuwaje.

Nikaona haina shaka nisipoteze muda,  nikatembe akwa haraka haraka , maana sasa nilikuwa kwenye korido,.. sehemu ile ya kutembea ili uitafuta ofisi ya huyo muheshimiwa,..hapo nikajiwa na mawazo, nikimuwazia mume wangu, jinsi gani alivyotekwa kimawazo na huyu mtu hadi akukubali kuwa huyu jamaa awe ni wakili wake.

‘Hii inaashiria kuwa mume wangu kafanya makosa, na sasa anajihami, sasa kafanya hivyo ili kujitetea, kwa vile anafahamu fika kosa alilolifanya litamfanya akose kila kitu, na kiukweli mimi sitaweza kukubali, ni lazima sheria ifanye kazi yake.
‘Lakini kafanya kosa gani, ..la uzinzi au….kavunja miiko ya ndoa, hahaha, kama hilo sitaweza kumsamehe kamwe..anafahamu hilo kabisa, sasa kama alifahamu hivyo kwanini akafanya hivyo…na kinachotakiwa ni ushahidi, na ushahidi mnzuri ni huo wa mtoto, kumbe ndio maana,….

‘Na baya zaidi kama wanavyodai watu , kama ni kweli kuwa katembea na rafiki  yangu…mbona nitaumia sana, …hapana..hili sitawasamehe kabisa, ni lazima nifanye jambo, ni lazima nimuonyeshe baba yangu kuwa ninaweza kushika hatamu zake…’nikasema

‘Kwa vyovyote iwavyo, …mume wangu ana makosa, na kama alitembea na rafiki yangu, basi wote wamenisaliti,..na bahati nimkute …kwanza nitamuokoa na hao watu, lakini la pili ni lazima akapambane na adhabu ambayo hataweza kuishau maishani, hataamini kuwa mimi ndio yule rafiki yake..’nikasema

Nilikumbuka kuwa mikataba imebadilishwa, kwahiyo sitaweza kuchuku hatua yoyote kwa sasa, hasa kwa mume wangu maana ndio maana pale kwenye ule mkataba waliandika kuwa:

`....mume ndiye atakuwa na mamlaka ya mali yote, na maamuzi yote.....’ thubutu, mali yangu mwenyewe, mtu aje aniamulie..hilo halikubaliki, tutapambana hadi tone la mwisho, na ikibidi, nitachukua hatua ambayo watu hawataamini kuwa ndio mimi, mtoto wa muheshimiwa baba.

‘Na huyu rafiki yangu nitamfanya nini..maana nsipomfanya kitu kwa hivi sasa hataniheshimu kamwe, ooh, lazima kila nilichopanga na yeye kimkute, haijaslishi yeye ni ni rafiki yangu...’nikasita hapo kidogo nikiwazia adhabu yake.

‘Lakini....’hapo nikatulia kidogo..

‘Ushaidi upo…mtoto anafanana na nani…na mume wangu, kwahiyo…lakini cha muhimu ni hicho kipimo, cha DNA, nikikipata tu, basi…na lazima watakuwa wamempatia huyo wakili kama wameamua kuandikishana kisheria…

Na kuna ushahidi wa DNA, unaonyesha kuwa huyo mtoto sio wa mume wako ni wa mtu mwingine ambaye hajatambulikana…’ nikakumbuka maneno ya docta

 Kwa vyovyote iwavyo, mume wangu kanisaliti,..kawahi kutembea na rafiki yangu vinginevyo asingelikuwa na mashaka hayo, hata kama sio mtoto wake, ..kwanini akawa najihami, hapo hata iwavyo, bado anastahiki adhabu kubwa, …

‘Na huyu rafiki yangu kama kweli hajaondoka, kaahirisha safari, basi…nitamuonyesha kuwa mimi ni nani…kuja kwake atakujutia, ni lazima apambane na kile nilichokiahidi…

Nilipowaza hivyo nikachukua simu yangu ..nikaanza kuipiga huku natembea mwendo wa kawaida, simu hazitoki, basi nikaona niandike ujumbe wa maneno;

‘Mimi ni yule dada niliyekuambia unitafutie wale mabaunsa wa ile kazi, ...nitakuarifu pindi, ..ndio, kuna dada mmoja, kama nikithibitisha kafanya hivyo, nataka tumfunze adabu, ...kabisa kabisa, waweke tayari tayari, nitakuambia yupo wapi, wewe subiria simu yangu.....’nikaandika hivyo na kuutuma huo ujumbe.

Mara nikasikia king’ora cha polisi kikisikika kwa mbali sana…

‘King’ora cha polisi, kuna nini  tena usiku huu, oh na muda umekwenda, huyu rafiki yangu sio muendaji tena, ngoja, nitamuokoa, lakini usiku huu huu atakipata cha moto…’nikasema

King’ora cha polis kikanikumbusha yule mtu niliyekutana naye akikimbia.

‘Nahisi kuna hatari, kwanini nisirudi tu huko nilipotoka..mbona moyo wangu unakuwa na mashaka…’nikajiuliza lakini sikutaka kushindwa, sikurudi nyuma, nikajikakamua, na kuendelea kutembea

Na kwa muda huo king’ora kilikuwa wazi ni cha polisi, nikasimama kidogo kusikilizia, kuhakiki, kama king’ora hicho kilikuwa kikitokea mjini, au njia ya kutokea Gongolamboto, sikuweza kukisia vyema, maana kulikuwa na sauti kubwa ya mziki. Nikajipa moyo kuwa huenda hawo askari watakuwa na safari zao,...

Nikawa nimeshafika eneo nililoeleekezwa,na nilipotupa macho kushoto, nikaona kwenye mlango, maandishi, `WAKILI WA KUJITEGEMEA, MH. MAKABRASHA..

‘Mr. Mkabrasha...’nikasema kwa sauti ndogo, huku nikitabasamu.

Nikatulia kidogo, maana sasa huenda naingia kwenye matatizo, na nisipokuwa muangalifu ninaweza kuhatarisha maisha yangu, japokuwa watu wengi walioniona na watakuwa mashahidi wangu, kama likitokea lolote, lakini kama wataniua je, itasaidia nini hapo

Hata hivyo siwezi kujiaminisha sana, kuwa kuna watu wameniona nikipanda juu, kwani watu wote hawo wanaweza kuwa watu wake...wakamtetea yeye.Kwahiyo sasa nifanye nini, na mimi nimeshafika hapo…

Kwanza nikavaa soksi za mikononi, maana ukiwa unakwenda sehemu zenye mashaka, ni vyema ujenga tabia ya kujihami, na mimi tabia hiyo nimekuwa nayo mara nyingi, hasa unapokwenda sehemu unazohisi kuwa zinaweza kuwa na hatari ni vyema pia ukajihami na alama za mikononi, lolote linaweza kutokea.

Kwa haraka, ..nikazitoa soksi za kinga za mikono nilikuwa nazo kwenye mkoba wangu, Mara nayingi nakuwa na hizi soksi kwenye mkoba wangu.
Na nilipohakikisha nimezivaa , ni kitendo cha haraka hapo, japokuwa moyo wangu ulikuwa ukinienda mbio.

Nikauendea huo  mlango, ulioandikwa jina la huyo muheshimiwa, nikajaribu kusikiliza kama kuna sauti yoyote inatokea ndani, lakini kulikuwa kimiya, kimiya kabisa,unachoweza kusikilia kwa mbali ni hizo sauti za ving’ora na mziki toka chini,....nikaona nispoteze muda, nikaugonga huo mlango mara tatu...kimiya, mara nyingine tatu kimiya

Mwili ukaanza kujenga hisia nyingine, nywele zikaanza kunisisimuka, nikawa nahisi uwoga fulani,....nikakumbuka wale watu chini, waliniambia kuwa huyo muheshimiwa yupo juu, kwenye ofisi yake, kwanini nagonga mlango wake mara nyingi, bila ya yeye kutokea au hata mtu mwingine kuja kunifungulia mlango, nikagonga tena na tena kimiya..

Nikaona isiwe taabu nikashika kitasa cha mlango nikakizungusha taratibu, nikaona mlango unafunguka...nikausukuma polepole, ukafunguka kiasi cha mimi kupita, nikaona hapana, nikausukuma, ukafunguka kwa mapana, kiasi cha kuona ndani, nikaona kwe mbele sehemu ya mapokezi, ..kumbe ni ofisi kubwa tu, nikaangalia nje kama kuna mtu anakuja ...hakuna, nikaingia ndani.

Na wakati huo vile ving’ora vya polisi, vilikuwa vimeshafika eneo karibu na hilo jengo ni kama vile wanakuja eneo hili, nikaona afadhali, kama rafiki yangu yupo matatani, nitapata wasaidizi, nikapata nguvu, nikaingia ndani, na kuangalia huku na kule nikaona mlango mmoja umeandikwa:

OFISI YA WAKILI..., nikaangalia saa yangu ilikuwa saa mbili na nusu, nikausogelea ule mlango, nikagonga,...kimya nikagonga tena, kimiya....mara simu yangu ikaita, nikaizima bila kuangalia mpigaji, nikashika kitasa na kufungua mlango, mlango ukafunguka....

Kwanza nilisimama huku nikiangaza macho kukagua hicho chumba na kama kuna usalama,, ilikuwa ni ofisi nzuri tu, ikiwa na kila kitu kinchoweza kupatikana kwenye ofisi za mawakili,na macho yangu yakaenda moja kwa moja kwenye meza, niliona mtu kakaa huku kalala kwenye meza.

‘Mhh, huyu jamaa kalewa mpaka kalala kwenye meza..ni kawaida yake nini..’nikajisema hivyo.

Alikuwa kalala kichwa kakiweka mezani, lakini ulalaji ule sio wa kawaida, ni kama mtu kalazimishwa, na macho yangu yakatua pembeni yake, nikaona nakala za mikataba, na mmoja kati ya hizo nakala za ni ule mikataba wangu ... nahisi ni ule  waliyotengeneza wao, lakini jamaa anaonekana hajitambui, labda kalewa sana, au ni usingizi gani huo..

Hasira zikanipanda, nilitaka nifike kwa huyu mtu nimuinue nimsuke suke, nikifahamu kuwa kalewa, hatakuwa na ubavu wa kupambana na mimi,...na hapo inaonekana kanywa hadi kapitiliza maana pembeni kwake kulikuwa na chupa kubwa ya kinywaji cha pombe kali, na gilasi mbili,....kuonyesha kuwa hakuwa peke yake, nikaachia mlango, na kusogea kuingia ndani, huku king’ora cha polisi kikisikika kwa nguvu, kuashiria kuwa sasa askari wapo chini ya hili jengo.

Hata hivyo, akilini mwangu nilikuwa na mashaka, nikijiuliza hawo maaskari wamefuata nini hapo...kusije kuwa kuna matatizo.....nikaona nimalizane na kilichonileta, kwanza nikasogea hadi pale kwenye meza, kwa haraka nikauchuku aule mkataba na kuukagua…ni nakala ya mkataba wangu, ..

‘Nahisi walikuwa wakiufanyia kazi…’nikasema kimoyo moyo

‘Sasa walikuwa na nani, …?’ Pale mezani kuna gilasi mbili, na zote zipo nusu… kuashiria hawa watu walikuwa wanaongea, alikuwa na mtu mwingine,.

Nikaone nisipoteze muda, nikaona nimuamushe huyu mtu nimuulize rafiki yangu yupo wapi, na kwanini, kaingilia maswala ya familia yangu kwa kuharibu mkataba wangu na mume wangu,...nilipofikia hapo kimawazo sikujali mambo ya polisi, nikasogea upande ule aliokaa huyo jamaa ili kukabiliana naye....

Ni wakati huo huo, nasogea na mara macho yangu yakatua pale alipolala huyo jamaa, nikaona kitu kilichonishitua, nikaganda, nikarudi kinyume nyume na kugonga ukuta, nikafanya vitu vilivyokuwa nyuma kwenye kimeza kidogo kudondoka,..ule mlio wa kudondoka hivyo vitu ukanishtua

Kwa haraka , nikashika mdomo,...kujizuia,..lakini haikuwezekana, nikajikuta nimepiga yowe, unafahamu yowe, sijawahi kupiga yowe kama hilo....na mara nikasikia mlango wa hiyo ofisi ukifunguliwa, .....

Tuendelee kidogo, mmh, kidole kinauma......wikiendi njema

NB: Kwa leo,..hapa hapa


WAO LA LEO:Kila kazi ina utaalamu na utendaji wake, na pia kuna taratibu zake, ndio maana watu wanakwenda kuzisomea hizo kazi, tusijifanye kuwa tunafahamu kila kitu, eti kwa vile ulipitia pitia shuleni, kuna vitabu umesomasoma , hiyo peke yake haitoshi ...


Ndio maana kuna taaluma tofautitofauti, na kila taaluma, ina mabingwa wake, ina wataalamu wake, ina watu wanapewa madaraja na nyazifa mbalimbali, kuonyesha kuwa hizo ni fani zinazojitegemea, tusipende kujiingiza kwenye kazi za watu ambazo huenda ni za kitaalamu zaidi, na kujifanya tunaufahamu nazo, ilihali hatujazisomea, tujue kuwa  kuongea na kutenda ni vitu viwili tofauti,..tuweni makini na fani za watu jamani.
Ni mimi: emu-three

No comments :